Sura ya 13
Mpanda Farasi wa Ufalme Aendelea
1, 2. (a) Sasa tunakaza fikira zetu juu ya nani, naye anashika nini katika mkono wake wa kuume? (b) Sababu gani Yohana aliambiwa aache kulia? (c) Ni nani aliye “Simba” wa Yuda, na sababu gani anastahili kuifungua ile mihuri?
NA TUFUNGUE sura ya tano ya Ufunuo. Hapa tunasoma habari za njozi iliyoongozwa na Mungu, aliyopewa mtume Yohana, inayohusiana moja kwa moja na ‘kuja’ kwa ufalme wa Mungu. Inakaza fikira juu ya Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu, “Yeye anayeketi juu ya kiti cha enzi.” Katika mkono wake wa kuume ameshika kitabu cha kukunja cha maandishi, “kimefungwa ndi kwa mihuri saba.” Lakini mtume Yohana anaanza kulia sana. Sababu gani? Kwa sababu, katika ulimwengu mzima wote, hakuna mtu ambaye angeweza kupatikana aliyestahili kukifungua kile kitabu cha kukunja na kujulisha ujumbe uliomo. Lakini, tazama! Kuna mtu fulani anayestahili! Ni “Simba ambaye ni wa kabila la Yuda,” mrithi wa ufalme wa Daudi.—Ufunuo 5:1-5, NW.
2 Anastahili kwa sababu yeye “ameshinda.” Alipokuwa mwanadamu mkamilifu hapa duniani, alionyesha ushikamanifu ulio imara kwa Baba yake, hata kufikia kifo chenye ukatili juu ya mti wa mateso. “Mtawala wa ulimwengu huu,” Shetani, hangeweza kuvunja ukamilifu wake. Yesu aliweza kusema: “Mimi nimeushinda ulimwengu.”—Yohana 14:30, HNWW; 16:33.
3. Sababu gani imetupasa tuushangilie utimizo wa Ufunuo 5:9, 10?
3 Kuna wengine pia, ambao wameushinda ulimwengu, na “Simba” huyo asiyeogopa, yaani, Kristo Yesu, anawahesabu kuwa “ndugu” zake za kiroho. (Mathayo 25:40) Kwa kupata ufufuo wa kimbingu, hao wataungana naye katika utawala wa Ufalme wake wa miaka 1,000, washiriki pamoja naye kuwapa mabilioni ya wanadamu duniani zile faida za dhabihu ya ukombozi wake. Kwa hiyo sauti mbinguni zinaimba wimbo mpya. Zinamwambia Huyo, ambaye wakati mmoja aliongozwa kama mwana-kondoo asiye na hatia akachinjwe:
“Wewe unastahili kukichukua kitabu cha kukunja na kufungua mihuri yake, kwa sababu wewe ulichinjwa na kwa damn yako ukanunua watu kwa ajili ya Mungu kutoka kila kabila na lugha na jamii ya watu na taifa, na ukawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu, nao watatawala wakiwa wafalme juu ya dunia.” (Ufunuo 5:9, 10, “NW”)
Lo! ni baraka kama nini, kwamba Mfalme na wafalme-washirika wake waliojaribiwa na kuthibitishwa wanakaribia kuchukua hatua ya kufaidi wanadamu wenye kudhulumiwa! Lakini kuhusiana na hilo, ni lazima kwanza kuweko vita.
YULE MPANDA FARASI MWEUPE
4. (a) Ni nini vinavyofananishwa na ‘farasi mweupe,’ “upinde” wa mpanda farasi huyo, na kupokea kwake “taji”? (b) Huyo mwenye kupanda farasi ni nani, na alipokea mamlaka ya kifalme wakati gani?
4 Wakati yule “Mwana-kondoo” anapokichukua kile kitabu cha kukunja na kufungua muhuri wa kwanza, sauti inanguruma kutoka mbinguni hivi: “Njoo!” Halafu tunaona nini? “Kumbe palikuwa na farasi mmoja mweupe hapo”—akifananisha vita ya uadilifu. Aliyempanda ana “upinde.” Yeye anaweza kuharibu adui zake akiwa mbali—akisafiri kilometa nyingi sana kuliko na makombora yenye kufanyizwa na wanada mu yenye kutupwa kutoka bara moja mpaka bara nyingine. Apewa “taji,” na hilo linaelekeza kwenye mwaka wa kisasa wa 1914, wakati Yehova anapompa mamlaka ya kifalme juu ya mataifa. Kwa kuwa ni mwenye nguvu nyingi sana kuliko mabwana au wafalme wanyonge wa kibinadamu, huyu “Bwana wa mabwana na Mfalme wa wafalme” atashinda maadui wote wa uadilifu, akiwa pamoja na Wakristo wapakwa-mafuta “aliowaita na kuwachagua, ambao ni waaminifu,” wenye kuungana naye katika ufalme wake wa kimbingu.—Ufunuo 6:1, 2; 17:14, HNWW.
5. (a) Ni ushindi gani wa kwanza ambao huyo mwenye kupanda farasi alijipatia? (b) Matokeo yake yamekuwa nini kwa wanadamu, lakini sababu gani imetupasa tutu lile onyo la Marko 13:32-37?
5 Huyo mpanda ‘farasi mweupe’ ni mshindi mwenye nguvu. Basi, anapoanza kupanda kwake, ni jambo gani ambalo lingeweza kuwa lenye kufaa kuliko kumfukuza mbinguni yule “nyoka wa zamani” Shetani na malaika zake wa kishetani! Vurururu chini kwenye dunia hii, anawavurumisha! Si ajabu kwamba sasa yule Ibilisi ana hasira kuu. Kama tulivyokwisha kuona, anaelekeza hasira yake kuu kwenye wanadamu, akifanyiza “ole wa nchi na bahari.” Yule Ibilisi anajua kwamba “ana wakati mchache tu,” lakini ni mwerevu sana. Angependa kutuvuta sisi tufikiri kwamba zile “siku za mwisho” bado zitaendelea tu mpaka kwenye wakati ujao ulio mbali. Ye yote kati yetu asilazwe usingizi kwa fikira hizo!—Ufunuo 12:9-12; Marko 13:32-37.
FARASI MWEKUNDU
6. (a) Kulingana na Ufunuo 6:3, 4, ni kitu gani kinachotokea sasa duniani? (b) Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilikuwaje tofauti na vile vita vyote vilivyotangulia?
6 Yule “Mwana-kondoo” anafungua muhuri wa pili. Anatokea ‘farasi mwekundu’! “Mpanda farasi wake alikabidhiwa jukumu la kuondoa amani duniani, watu wauane; akapewa upanga mkubwa.” (Ufunuo 6:4, HNWW) Loo, ile vita ya ulimwengu iliyo katika historia inatokea duniani kwa mshindo. Amani inaondolewa, si kutoka mataifa machache tu, bali “duniani,” wakati majeshi makubwa mno ya nchi kavu na majeshi ya baharini yanapigana, yakitumia silaha zenye kuogopesha za kuangamiza watu kama mainzi. Ijapokuwa vita vilivyotangulia vimepiganwa na majeshi ambayo hiyo ndiyo kazi yao, kwa kawaida yakiwa ya nchi chache tu, Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ni vita ya kutumia vifaa vyote. Kwa mara ya kwanza katika historia, mali zote za mataifa mengi, kutia na askari wenye kuandikwa kwa lazima, zinatumiwa katika pigano.
7-9. Kwa habari ya ‘kuuana,’ ni takwimu na maneno gani yanayoonyesha kwamba mwaka wa 1914 ulikuwa mwanzo wa kipindi chenye mauaji makubwa zaidi sana katika historia yote?
7 Ule unabii unataja “wauane,” na ‘waliuana’ kweli kweli! Katika lile pigano la Somme, uvumbuzi mpya na wenye kuua sana, yaani bunduki aina ya bombomu (bunduki-mimina-risasi), ilifyeka-fyeka askari-jeshi wa Uingereza na Ufaransa chungu-nzima. Kulingana na makadirio fulani, uvumbuzi huo ulisababisha asilimia 80 ya majeruhi wote. Kwa muda wa miezi tisa katika Verdun, wanaume wengi sana walikufa kuliko wale walioingia Urusi na jeshi la Napoleoni. Ishara fulani iliyoandikwa kwa damu kwenye ukuta wa makaburi katika Verdun ilikuwa na maneno yenye kusema “KILOMETA TANO KUFIKA MACHINJONI.” Kwa jumla, askari-jeshi wapatao 9,000,000 walichinjwa wakati wa miaka minne ya ile Vita Kuu.
8 Je! mwaka wa 1914 ndipo yule mpanda ‘farasi mwekundu’ aliondoa amani duniani? Wanahistoria wengi wanaunga mkono maoni hayo. Kwa mfano, miaka karibu 50 baada ya hapo, mhariri wa gazeti la kihistoria linaloitwa American Heritage aliandika hivi: “Katika kiangazi cha mwaka wa 1914 mataifa yalikuwa na amani na wakati ujao ulionekana kuwa wenye utulivu. Ndipo bunduki zikalia, na mambo hayakuwa namna ile ile tena kamwe. . . . Mwaka wa 1914 ulikuwa mmojawapo miaka yenye kujaa sana misiba katika historia ya kibinadamu . . . Katika mwaka huo kukatokea kimoja cha vile vipindi vya mabadiliko makubwa vinavyotokea mara moja au mbili tu katika muda wa miaka elfu moja. Labda itachukua wakati mrefu kabla hatujaifahamu kabisa hali tulimoingizwa na mwaka wa 1914, lakini angalau tunaweza kuanza kuona kile ambacho ulituondolea.” Kweli kweli, yule mpanda ‘farasi mwekundu’ aliondoa amani katika dunia, na hiyo ni katika mwaka wa 1914.
9 Yule mpanda farasi ameendeleza upandaji wake wenye mauaji mpaka kuingia vita ya ulimwengu ya pili, ambayo katika hiyo askari-jeshi 16,000,000 walikufa katika pigano. Tunaposonga na miaka hii ya 1980 na kitu, profesa wa Hangare anakadiri kwamba katika muda wa miaka 30 baada ya mwisho wa Vita ya Ulimwengu ya Pili, askari-jeshi wengine 25,000,000 walikufa katika pigano. Anaeleza kwamba wakati wa ile miaka 33 iliyofuata kumalizika kwa Vita ya Ulimwengu ya Pili, kulikuwako siku 26 tu ambazo katika hizo hakukuwa na vita mahali fulani katika ulimwengu.
10. Mpanda farasi huyo ametumiaje “upanga mkubwa”?
10 Unabii ule unatuambia kwamba mpanda farasi huyo alipewa “upanga mkubwa.” Na kwa kweli, silaha zenye kufisha zimetimiza sehemu kubwa katika machinjo ya vile vita vya karne hii ya 20. Katika Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, gesi zenye sumu, silaha za kujifyatukia, vifaru vya kijeshi, eropleni na nyambizi (sabmarini) zilitokea mara ya kwanza kwa wingi kabisa. Katika Vita ya Ulimwengu ya Pili, vita vya kupigana hewani vilifagia kabisa majiji, majeruhi wengi wakiwa wanawake, watoto na wazee wasio na hatia. Katika usiku mmoja jiji la Coventry, kule Uingereza, liliharibiwa, na baadaye shambulio la ndege za kivita lililofanywa na Mataifa Rafiki likaua watu 135,000 katika Dresden, Ujeremani. Kisha watu wasiopungua 92,000 wakauawa kama mainzi katika Hiroshima na 40,000 katika Nagasaki, Ujapani, kwa kutumia mabomu ya atoms. Tena wengi wa hao walioangamizwa ni raia wasio askari-jeshi. Kiasi ambacho huo “upanga mkubwa” unaweza kuchinja leo ikitokea vita ya nyukilia hakiwaziki!
TAZAMA! FARASI MMOJA MWEUSI
11, 12. (a) Yule mpanda ‘farasi mweusi’ ameJionyeshaje kuwa mwenzi wa yule mpanda farasi wa pili? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba kupanda kwake kumeendelea mpaka wakati wetu?
11 Yule “Mwana-kondoo” anapoufungua muhuri wa tatu, ‘farasi mmoja mweusi’ atokea kwa kasi. “Mpanda farasi wake alikuwa na vipimo viwili vya kupimia uzito mkononi mwake.” (Ufunuo 6:5, HNWW) A, huyu ni mpanda farasi mwenzi wa yule mpanda farasi wa vita vya kutumia vifaa vyote! Huyu ndiye mpanda farasi anayeleta njaa kuu. Wakati wa vita hivyo viwili vya ulimwengu, hali za njaa kuu zilipata nchi nyingi. Kupimiwa chakula, kama inavyofananishwa na vile “vipimo viwili vya kupimia uzito,” kukawa ndiyo kawaida ya wananchi wa mataifa yenye kupigana. Baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ikaja ile njaa kubwa kuliko zote katika historia yote. Gazeti The Nation la Juni 7, 1919, lilitaarifu kwamba watu 32,000,000 katika India ‘walikaribia kufa njaa.’ Gazeti World’s Work la Machi 1921 lilisema kwamba katika upande wa kaskazini wa China pekee, watu 15,000 walikuwa wakifa kila siku kwa njaa. Kichapo cha New York Times kinachoitwa Current History Magazine cha Oktoba 1921 kilinakili ripoti ya Uingereza ya kwamba katika Urusi “watu wasiopungua 35,000,000 wanapatwa na kituko chenye kuogopesha sana cha njaa kuu na ugonjwa wa kipuku.” Hali za njaa kuu zinazofanana na hizo zilienea baada ya Vita ya Ulimwengu ya Pili, wakati gazeti Look la Juni 11, 1946 lilipotaarifu hivi: “Robo ya ulimwengu inakufa njaa leo.”
12 Hata bila vita ya kutumia vifaa vyote, kuharibika kwa mazao katika ulimwengu wetu wa sasa kunaleta mara nyingi habari za magazetini kama hii iliyotokea mwaka wa 1974: “India inakumbwa na mpanda farasi wa tatu.” Katika mwaka wa 1976: “Ulimwengu Wenye Kuzidi Kupatwa na Njaa Wakabili Upungufu Mkubwa wa Chakula.” Na katika mwaka wa 1979: “Watu milioni 450 wanakufa njaa.” Wakati idadi ya watu ulimwenguni inapoongezeka, ile hali ya chakula katika nchi zenye maendeleo kidogo na zile zenye kupatwa na vita inazidi kuwa mbaya sana. Ule Uchunguzi wa Kimagazeti wa Atlasi Ulimwenguni uliokuwa katika gazeti New Scientist la Mei 1975, ulieleza hivi: “Ulimwengu unakabili jini lenye vichwa viwili. Njaa kuu ni kimoja cha vichwa hivyo: kile kingine ni utapiamlo usioponyeka. FAO [Shirika la Chakula na Kilimo] linakadiri kwamba mataifa 61 kati ya 97 yanayositawi yalitoa au yaliingiza nchini chakula kidogo sana kutoka nchi za kigeni mwaka wa 1970 kuliko kilichohitajiwa kulisha watu wao. Kwa kadirio la kiasi, FAO linakisia kwamba watu milioni 460 wanapatwa na utapiamlo (ugonjwa wa kutopata chakula kinachofaa); kwa ufasili mkubwa zaidi hesabu hiyo inaweza kuwa bilioni moja.” Sasa, katika miaka hii ya 1980 na kitu, hali hiyo ni mbaya zaidi sana.
13. Ni hali na hofu gani za kisasa zinafananishwa kimbele katika Ufunuo 6:6?
13 Wakati yule mpanda farasi wa tatu anapoendelea kupanda, sauti kutoka zile mbingu yapazwa: “Kibaba kimoja cha unga wa ngano kwa kiasi cha fedha dinari moja, na vibaba vitatu vya shayiri kwa dinari moja. Lakini usiharibu mafuta wala divai.” (Ufunuo 6:6, HNWW) Kwa kuwa dinari ilifananisha mshahara wa siku kutwa, mfanya kazi angeona uchungu kweli kweli kwa sababu ya kupanda sana kwa bei. Je! infuleshoni haiendelei kushambulia lile pato la makabwela wa leo? Lakini vipi zile bidhaa kama “mafuta” na “divai”? Watu wenye pupa ya kupata faida na wengine wenye mali wangependa kulinda maisha yao ya utajiri. Lakini, watafaulu? Tutaona, wakati yule ‘farasi mweusi’ anapokimbia kasi uku na huku katika dunia yote.
‘FARASI RANGI KIJIVU, AKIWA NA KIFO’
14. Yule mpanda farasi wa nne na mwenzake wanaunganishaje vya kufaa matuklo ya tangu mwaka wa 1914?
14 Ule muhuri wa nne wafunguliwa, na “farasi mmoja hapo, rangi yake kijivu” ajiunga na wale farasi wenye kuruka-ruka. Mwenye kumpanda ni Kifo. Hadesi aja akifuata karibu-karibu—kwamba amepanda farasi mwingine ama sivyo, maandishi hayasemi. Lakini wana tume yenye kuogofya sana: “Hao walipewa mamlaka juu ya robo moja ya dunia, wawaue watu kwa upanga, njaa, tauni, na kwa wanyama wakali wa dunia.” (Ufunuo 6:7, 8, HNWW) Tangu mwaka ule wa 1914 wenye kujaa msiba, kuwapo kwa Kifo na Hadesi kumeenea kweli kweli kwenye pembe nne za dunia.
15, 16. (a) Unabii huo ulipata utimizo gani mkubwa katika miaka ya 1918-1919? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba farasi huyo amekuwa akiruka-ruka daima tangu mwaka wa 1914?
15 “Tauni” au pigo la kufisha! Waliita tauni hiyo ugonjwa wenye kuua watu wengi wa 1918-1919, au homa ya mafua ya Kispania. Kwa muda wa majuma machache, waliouawa na ugonjwa huo wakawa mara mbili ya hesabu ya wale waliokuwa wamekufa katika wanja za mapigano za Vita ya Ulimwengu ya Kwanza—jumla yenye kustaajabisha ya watu wasiopungua 21,000,000. Katika nchi ya United States tarakimu rasmi ya vifo vilivyotokana na homa ya mafua ilikuwa 548,452. Hiyo ni zaidi ya mara 10 ya ile hesabu ya askari wa Kimarekani waliouawa vitani. Hasa waliouawa na ugonjwa huo ni vijana na makakawana. Katika India, watu zaidi ya 12,000,000 walikufa. Ugonjwa huo haukuacha bara wala kisiwa cho chote—isipokuwa kisiwa kimoja tu cha St. Helena. Vijiji vizima kati ya Waeskimo na katika Afrika ya Kati vilikumbwa na ugonjwa huo. Katika Tahiti, maziko ya kuchoma maiti yalitumiwa kuchoma maiti zile za watu 4,500 waliokufa katika muda wa siku 15 tu, na katika Samoa Magharibi watu 7,500 kati ya wakaaji 38,000 waliangamia kwa tauni hiyo.
16 Walakini, homa ya mafua ya Kispania haikuwa ndiyo ugonjwa pekee wenye kufisha ulioletwa na yule mpanda ‘farasi rangi kijivu.’ Gazeti New York Times lilitoa ripoti kwamba mwaka wa 1915, katika kupigania Gallipoli, ugonjwa wa kuhara damu uliva askari-jeshi wengi kuliko wale waliouawa kwa risasi. Kutoka mwaka wa 1914 kufika 1923 ugonjwa wa kipindupindu uliva watu 3,250,000 katika India. Katika mwaka wa 1915 “vifo vya kuanzia milioni mbili na nusu mpaka milioni tatu” katika Urusi vilihusishwa na ugonjwa wenye kuletwa na chawa. Na wakali yule mpanda farasi anaporuka-ruka kuingia katika nyakati za karibuni zaidi, magonjwa ya moyo na kansa yamekuwa makubwa katika kuua, kaswende ukiwa “ndiye Mwuaji Na. 2 Kati ya Magonjwa Yenye Kuambukia” na ugonjwa wa ini ukawa ni “Mlipuko wa Ulimwenguni Pote wa Ugonjwa.”
FARAJA IKO KARIBU
17, 18. (a) Mwanasiasa mmoja alisema nini, akionyesha uhusiano kati ya mpanda farasi wa pili, wa tatu na wa nne? (b) Lakini ni nani ambaye viongozi wa ulimwengu wanapuza? (c) Sababu gani tunaweza kufurahia yale ambayo yule Mfalme mtukufu atafanya?
17 Sasa kwa miaka zaidi ya 60, yule ‘farasi mwekundu,’ yule ‘farasi mweusi’ na yule ‘farasi rangi kijivu’ wamekuwa wakipandwa wakiwa sambamba, na Hadesi ikiwa inafuata karibu-karibu. Kweli kweli, Hadesi imevuna mavuno mengi ya majeruhi, ambao wamejumlika kuwa mamia ya mamilioni. Inapendeza kujua kwamba rais wa zamani wa United States, Herbert Hoover, aliunganisha pamoja wapanda farasi hao watatu, akasema hivi mwaka wa 1941: “Nyakati zote matokeo ya vita vikubwa ni njaa kuu na ugonjwa wa kipuku . . . Ile Vita ya Ulimwengu ya miaka 25 iliyopita ilileta njaa kwa watu 300,000,000. .. . Baada ya mwaka mmoja na nusu wa vita ya sasa [yaani, Vita ya Ulimwengu ya karibu watu 100,000,000 zaidi wanapungukiwa chakula kuliko baada ya miaka mitatu ya ile vita ya mwisho.” Lo! vita ya ulimwengu ya tatu ingekuwa msiba kama nini kwa wanadamu!
18 Viongozi wa ulimwengu wanaijua sana ile hasara kubwa inayoletwa na mpanda ‘farasi mwekundu’ mpanda ‘farasi mweusi’ na mpanda ‘farasi rangi kijivu.’ Walakini, wanampuza yule Mpanda ‘farasi mweupe.’ Ile siku yenye furaha inakaribia Mfalme huyo mtukufu achukue hatua ya kubadili utaratibu wa mambo! Badala ya vita, ataingiza amani. Badala ya njaa kuu, ataandaa shibe. Badala ya magonjwa, atarudisha wanadamu kwenye afya bora kabisa, na hata Hadesi itatoa nje wale wafu. Kifungu kinachopatana na habari hiyo katika Zaburi kinasimulia juu ya huyo mpanda ‘farasi mweupe’ kwa maneno haya: “Ujifungie upanga wako pajani, Ee wewe mwenye uwezo, utukufu wako na enzi yako. Katika enzi yako panda na kuchukuliwa na baraka, kwa sababu ya kweli na upole na haki; na mkono wako wa kuume utakufundisha maneno ya kuogopesha.” (Zaburi 45:3, 4, “ZSB”) Ule ushindi wa Mpanda Farasi wa Ufalme unakaribia!
19. (a) Kulingana na utimizo wa Ufunuo 6:2-8, je! tufadhaike? (b) Ni mfano gani uliotajwa kututia moyo tuwe wenye nguvu katika imani?
19 Kwa hiyo tusifadhaishwe bure na hali inayozidi kuwa mbaya leo duniani. Badala yake, maoni yetu na yawe kama yale ya mwanamke mmoja wa Mashahidi wa Yehova ambaye, kwa sababu ya imani zake, alikaa gerezani miaka 20 kati ya ile ya kuanzia 1956 mpaka 1978 akiwa katika nchi ya kisoshalisti. Wakati fulani alikuwa katika hukumu ya kifo, na mpaka leo hii ana alama za mateso katika mikono yake. Aliendeleaje kuwa mwenye nguvu katika imani? Ni kwa kuvitafakari vifungu vingi vya Maandiko ambavyo alikumbuka kutokana na kujifunza Biblia kwa bidii hapo kwanza. Anasema kwamba kimoja cha vifungu hivyo ni Ufunuo 6:2. Alikuwa amesadikishwa kwa nguvu kwamba yule Mpanda ‘farasi mweupe,’ yaani, Mfalme Yesu Kristo, alikuwa ametawazwa katika mbingu mwaka wa 1914, naye aliazimia kuvumilia mpaka huyo mpanda farasi mweupe amalize “kushinda” kwake. Wale wengine wote wanaosali ufalme wa Mungu “uje” na waendelee kuwa waaminifu mpaka yule Mfalme ashinde kabisa!
[Box on page 123]
YULE FARASI MWEUSI AENDELEA KURUKA-RUKA
“Benki ya Ulimwengu inakadiri kwamba watu milioni 780 kote kote ulimwenguni wanaishi katika umaskini kabisa, hali ‘ambayo ni mbaya sana kwa wanadamu kuishi ndani yake.’ ”—Detroit “Free Press,” Septemba 1, 1980