Kutokutii Wazazi—Ni Ishara ya Siku za Mwisho?
“KUNA kizazi cha watu wamlaanio baba yao; wala hawambariki mama yao.” (Mithali 30:11) Maneno hayo yanakieleza vizuri kizazi cha tangu mwaka wa 1914. Lakini je! tangu wakati huo watoto wameonyesha jambo hilo kwa njia isiyo na kifani? Ikiwa ndivyo, sababu imekuwa nini?
Ulimwengu Wetu Unaobadilika
Zamani zilizopita, jamaa ilikuwa boma lenye upendo na kusaidiana. Hakukuwa na mashaka juu ya ni nani kati ya washiriki wa jamaa alipaswa kutimiza daraka hili au lile. Wanaume ndio waliokuwa watafutaji wa riziki. Hesabu iliyo kubwa ya wanawake walibaki nyumbani na kutunza watoto na kufanya kazi zao za nyumbani. Wanaume na wanawake walishirikiana pamoja kufundisha watoto wao maadili na kanuni za kufuata. Mara nyingi watoto walikuwa na shughuli nyingi mno za kinyumbani wasiweze kupata nafasi ya kufanya utukutu mkubwa.
Matukio ya tangu kutokea kwa ghafula kwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza katika mwaka wa 1914 yameivunja hali hiyo ya kupendeza sana. Sawasawa na alivyotabiri Yesu, yetu imekuwa ni karne ya vita vya kinyama, karne ya kutokutii sheria na ya upungufu wa vyakula. (Mathayo 24:4-14) Matokeo yamekuwa nini? Kumekuwa na badiliko kubwa sana katika njia yetu ya maisha. Kizazi hiki cha usafiri kinatenganisha washiriki wa jamaa kwa umbali mkubwa wakati wengine wao wanapofunga safari zao wenyewe. Kwa sababu ya kuwekwa huru na maendeleo ya mambo ya kiufundi waache kujichosha sana na kazi ya nyumbani, wanawake wengi wanaona afadhali wakaandikwe kazi badala ya kubaki wakifanya kazi za nyumbani. Walimu na mayaya ndio wamekuwa wakitimiza kazi zinazopasa kufanywa na wazazi. Watoto wanapambana na hali ya kujisikia wamechoka kukaa bila jambo la kufanya kwa sababu vifaa vinavyotumia umeme ndivyo vinavyofanya kazi za nyumbani.
Matukio hayo ya hivi majuzi yameongeza sana mikazo ya kijamaa. Hesabu ya talaka imepanda sana. Ndivyo na hali ya kubaki kwa mzazi mmoja tu nyumbani atunze jamaa. Mama mmoja anayekaa peke yake bila mume anasema hivi juu ya ugumu wa kulea mtoto akiwa peke yake: “Kufikia wakati ninapofika nyumbani kutoka afisini, watoto wangu wanakuwa wamekwisha kuondoka shuleni saa tatu kabla ya mimi. Sina njia ya kuchunguza nione wanafanya nini. Nina uhakika binti yangu wa miaka 16 anafanya ngono pamoja na mvulana wa darasa lao na kwamba mwanangu wa miaka 13 ana ukawaida wa kwenda kukaa karibu na jumba la eneo la kwetu la michezo ya kamari baada ya kutoka shuleni.”
Majeruhi wa Kizazi cha Ubinafsi
Labda hakuna kizazi kingine ambacho kimepata kushikilia “haki” za kibinafsi kama hiki cha sasa. Kwa sababu hiyo kulingana na mtaalamu mmoja mashuhuri anayeshughulika na matatizo yanayotokana na fikira za watu akilini, wazazi “wameanza pole kwa pole kuruhusu watoto wao wabishane nao, wadai sana kwamba maoni na mawazo yao wenyewe yafuatwe, hata wawe wasiotii kwa kiasi fulani.” Je! kuruhusu mambo hayo kunakuwa na matokeo mazuri?
Robert Coles, mhariri aliyeshinda zawadi ya mashindano ya uandikaji yaliyoanzwa na Bwana Pulitzer siku za huko nyuma, alisema hivi: “Wazazi wengi wanaogopa kulea watoto kulingana na fikira zao wenyewe—kwa kufuata usadiki wao wenyewe na imani yao wenyewe juu ya maadili. Wanatiwa woga na wastadi wengi wanaoandika vitabu juu ya kulea watoto na kuwaambia mambo wanayopaswa kufanya.” Kwa sababu ya kuongozwa na mawazo ya kulea watoto kwa kuwaendekeza, wazazi wanajikuta wakifanya kama vile watoto wao wanavyotaka—na mwisho wanakuja kuelekeana na kweli ya maneno haya ya Biblia: “Ikiwa mtu anaendekeza mtumishi wake kutokea ujana na kuendelea, katika maisha yake ya baadaye atakuwa mtu asiye na shukrani.”—Mithali 29:21, NW.
Matokeo ya Televisheni
Hivi majuzi Taasisi ya Kitaifa ya Kuchunguza Afya ya Akilini ilitoa ripoti yenye maelezo mengi yenye kichwa kinachosema “Televisheni na Tabia.” Ripoti hiyo ilionyesha kwamba, licha ya televisheni kujaza akili za watu fikira za kutenda jeuri na ufisadi bila kujali inakuwa na mambo mengine yenye kuvuruga maisha ya jamaa. Kwa mfano, “Katika visa vingi ajabu,” uamuzi wa kusema ni kipindi gani kitakachotazamwa unaachiwa watoto, nao “mara nyingi wamekuwa ndio wakataji wa shauri juu ya vipindi vitakavyotazamwa na jamaa; wamekuwa ndio wafanya maamuzi katika jamaa.”
Kitabu Generation of Narcissus kinadai kwamba kuna madhara mengine yasiyoonekana wazi yanayoletwa na televisheni. Kinasema kwamba kwa sababu ya televisheni “watoto wanajionea wenyewe kile kinachoitwa ulimwengu halisi wakiwa mahali panapowafaa kabisa. Wanaona kwamba ulimwengu huo unaanza na wao na kupanuka ukielekea nje.” Ndiyo, huenda ikawa kwamba mtoto aliyezoea sana kutazama televisheni anasitawisha maoni ya maisha ambayo ni ya kujitegemea mwenyewe kabisa.
Mambo hayo yote ndiyo yameondoa usawaziko wa maisha ya jamaa. Lakini je! kweli watoto wanaasi mamlaka ya wazazi?
Kutokutii—Kunakofanywa Waziwazi na Kunakofanywa Faraghani
‘Ongezeko la kutokutii sheria’ kati ya watoto ni moja ya ishara zilizo wazi zaidi za kuonyesha kwamba watoto fulani kwa kweli wanaasi mamlaka ya wazazi. (Mathayo 24:12) Kwa mfano, inaripotiwa kwamba “robo moja ya matendo yote mazito ya uhalifu katika Uingereza yanafanywa na watoto wa shule.” Katika United States “visa vya kukamatwa kwa watoto kwa sababu ya matendo ya uhalifu wa kutumia jeuri . . . viliongezeka kwa asilimia 293% kati ya mwaka wa 1960 na wa 1975; na jumla ya visa vyote vya kukamatwa kwao inaongezeka kwa asilimia 10% kwa mwaka—mara mbili za kiasi cha kukamatwa kwa watu wazima.” Ripoti za kutoka China zinaeleza juu ya “mauaji, kupunja, wivi, kuingilia wanawake kwa nguvu, kufanya biashara ya dawa za kulevya na za haramu” zinazoendeshwa na vijana.
Mengine ya matendo hayo ya jeuri yanayofanywa bila kuona haya yanaelekezwa hata kwa wazazi. Mchunguzi wa mambo ya kijamii, Richard J. Gelles, alisaidia kuendesha uchunguzi uliofunua kwamba “zaidi ya vijana milioni 2 1/2 walio katika umri wa kubalehe [katika United States] waliripotiwa kuwa walichapa mmoja wa wazazi wao angalau mara moja. Karibu wazazi 900,000 wa watoto walio katika umri wa kubalehe... ama walipigwa ngumi, wakaumwa, wakapigwa teke, wakapigwa kwa chombo kigumu, wakapigwa-pigwa, au wakatishwa kwa kisu au bunduki au vitu hivyo vikatumiwa kuwapiga.” Matendo hayo yenye msiba yanakazia utabiri wa Biblia kwamba katika siku za mwisho watu wangekuwa “wasiowapenda wa kwao.” (2 Timotheo 3:3) Lilikuwa jambo la kushusha moyo kweli kweli wakati shauri lilipokatwa kuonyesha kwamba “inaelekea kabisa kuwa kwamba hesabu zinazotolewa kuonyesha kiasi cha watoto wenye umri wa kubalehe wanaotenda wazazi wao jeuri zinatolewa kwa kupunguza kiasi halisi cha matendo hayo.” (Sisi ndisi tumeandika mwandiko wa italiki.)—The Urban & Social Change Review, buku la 15, Namba 1, 1982.
Njia nyingine ambayo watoto wanatumia kutenda kinyume cha vile wazazi wao wanavyotaka ni kufanya ngono za ovyo ovyo. Katika uchunguzi mmoja wa watoto Waamerika 160,000, asilimia 31 walio kati ya umri wa miaka 13 na 15 walikubali kwamba walikuwa wamekwisha kufanya ngono. Asilimia 58 wamekwisha kufanya ngono kati ya walio na umri wa miaka 16 na 18. Vivyo hivyo nchi ya Japani inaripoti kwamba “kisa cha ngono kinachohusu wasichana matineja kimeongezeka kwa njia ya kutokeza katika muda wa miaka saba iliyopita.”
Vijana-matineja wengine wanatumia vileo au dawa za kulevya kwa siri. Karibu asilimia 43 kati yao walikiri kwamba wamekwisha kuvuta bangi. Wachunguzi walikata shauri kwamba kuvuta bangi “ni jambo linalofanywa na matineja wengi wanapopisha wakati.” Nusu kati yao walikubali jambo la kwamba wangewaambia wazazi wao uongo wakiulizwa kama wanavuta bangi.
Vijana wengine wanaasi wakiwa wamenyamaza kwa kutokwenda shuleni kwa makusudi kwa sababu ya kuvurugwa fikira na wazazi wanaowataka sana wafanikiwe katika masomo bila ya wazazi wenyewe kuwasaidia sana. Na bado wengine wanakosa kutiia kwa kukataa kusadikishwa wafuate viwango vya maadili au vya kidini vya wazazi wao. Ni asilimia 53 tu ya vijana waliochunguzwa ambao walisema wangefuata dini ya wazazi wao. Wale wengine ama walisema hawangeifuata au hawakuwa na uhakika wangefanya nini. Hilo ni jambo lenye kukatisha wazazi tamaa kama nini! Asilimia 17 tu walisema wanataka kushauriwa na wazazi wao juu ya ngono; wachache zaidi ya hapo ndio wangeomba maoni ya wazazi wao juu ya kutumia dawa za kulevya. Utofautiano huo wa maoni unafanya nyumba ziwe wanja za mapigano.
Unaloweza Kufanya
Kwa hiyo inaweza kusemwa kwa uhakika kwamba kizazi chetu hakina kifani, ni cha hali zisizo na kifani. Mwelekeo wa kutokutii ulioko ulimwenguni kote, pamoja na ushuhuda mwingine, unatufanya tukate shauri lisiloepukika kwamba tunaishi katika siku za mwisho.
Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova wameona kwamba kujifunza Biblia—si mawazo ya leo yenye utofautiano juu ya namna ya kulea watoto—kunawatayarisha kushughulika na matatizo ya leo. Wao wanaiona amri iliyo kwenye Waefeso 6:1-4 (NW ) kuwa yenye mafaa: “Watoto, mwe watiifu kwa wazazi wenu katika mwungano pamoja na Bwana, kwa maana hilo ni jambo la uadilifu . . . Na ninyi, akina baba, msiwe mkiwaudhi watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” Basi, Mashahidi watafurahi kukusaidia wewe uanze kujifunza Biblia hatua kwa hatua.
Hata kama wewe si mzazi, kujifunza Biblia kutakufaidi sana. Kuendelea kulichungua Neno la Mungu kutakusaidia ufahamiane na Mungu na makusudi yake. Huo ndio mwendo wa hekima, kwa maana Biblia inahimiza hivi: “Itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya [Yehova].”—Sefania 2:3.
[Maelezo ya Chini]
a Neno la Kigiriki la kusema “kutokutii” lina maana halisi ya “hali ya kutoweza kuvutwa kwa usadikisho.”
[Blabu katika ukurasa wa 5]
‘Karibu wazazi 900,000 wenye watoto wa umri wa kubalehe walipigwa ngumi, wakaumwa, wakapigwa teke, wakapigwa-pigwa, au wakatishwa kwa kisu au bunduki au vitu hivyo vikatumiwa kuwapiga’
[Blabu katika ukurasa wa 8]
Mama mmoja anayekaa peke yake bila mume alisema: “Kufikia wakati ninapofika nyumbani kutoka afisini, watoto wangu wanakuwa wamekwisha kuondoka shuleni saa tatu kabla ya mimi. Sina njia ya kuchunguza nione wanafanya nini”
[Picha katika ukurasa wa 6]
Mara nyingi wazazi ambao wamejiacha waongozwe na mawazo ya kulea watoto kwa kuwaendekeza wanajikuta wakiwa na mtoto aliye mjeuri