Maswali Kutoka kwa Wasomaji
■ kwa kuwa ndugu anayeendelea kuwa katika kazi ya kuajiriwa ya kubeba silaha hangeonwa kuwa mfano mzuri, je, lingekuwa kosa kwa mmoja wa mashahidi wa Yehova kutafuta ulinzi wa maafisa wa kutunza sheria wenye silaha?
Yesu alisema: “Wote waushikao upanga, wataangamia kwa upanga.” (Mathayo 26:52) Kwa kupatana na kanuni hiyo, Wakristo waliokomaa wanaonywa kwa upole waepuke kazi ya kuajiriwa inayowataka wachukue bunduki (ambayo wakati wa kisasa inafanana na “upanga”). Lakini, hiyo haimaanishi kwamba hawangeweza kutafuta na kukubali ulinzi wa maafisa wa polisi wenye silaha. Kwa sababu gani tunasema hivyo?
Warumi 13:1-4, katika kutaja “mamlaka” ya kiserikali za kibinadamu inayotenda kwa ruhusa ya Mungu wakati wa huu mfumo, inasema: “Kwa kuwa yeye ni mtumishi wa Mungu kwako kwa ajili ya mema. Lakini ufanyapo mabaya ogopa; kwa maana hauchukui upanga bure; kwa kuwa ni mtumishi wa Mungu, amlipizaye kisasi mtenda mabaya kwa ajili ya ghadhabu.” Kwa hiyo Mungu anakubali “mamlaka iliyo kuu” kuwa na silaha, ili kadiri fulani ya sheria na utaratibu ihifadhiwe kati ya wanadamu. Lakini, Kristo akiwa “Mfalme wa amani” atakapoleta wingi wa ‘amani isiyo na mwisho,’ matumizi ya silaha zote za jeuri yatakuwa mambo ya wakati uliopita. Kwa kupatana na Maandiko, basi, Wakristo leo wanaweza kukubali ulinzi wa “mamlaka,” ingawa wao wenyewe wamekwisha ‘kufua panga zao zikawa majembe’ katika kutazamia Ufalme wa Mungu unaokuja.—Isaya 2:4; 9:6, 7.
Tunaweza kuilinganisha hali ya leo na ile ya huko nyuma wakati wa Yeremia. Ni wakati huo Yehova alitumia jeshi la “Nebukadreza, mfalme wa Babeli, mtumishi wangu” kutekeleza hukumu juu ya ufalme wenye kuasi imani wa Yuda. Je! Yeremia na Baruku walijitwalia silaha za kujilinda katika hali hiyo ya hatari? Hapana, kwa maana Yehova alimfanya Yeremia kuwa “mji wenye boma, na nguzo ya chuma, na kuta za shaba, juu ya nchi yote.” Na ingawa hawakujiunga na jeshi la kuchinja la “mtumishi” wa Yehova, walikubali ukombozi kupitia “mtumishi” huyo Yerusalemu ulipoharibiwa.—Yeremia 1:17-19; 25:9; 39:11-14.
Vivyo hivyo leo, Mashahidi wa Yehova wanafuatia amani wanapotangaza ujumbe wa Ufalme katika ulimwengu wenye jeuri. Hata hivyo, maadamu Yehova anaruhusu mamlaka za kiserikali zichukue “upanga” au kinachofanana nao wakati huu ili kuhifadhi utaratibu, wanaweza kwa kufaa kukubali ulinzi wa “upanga.”