‘Chagua Wanaume Hodari Katika Kazi, Wanaoogopa Mungu’
“Lakini lazima wewe mwenyewe utafute wanaume hodari katika kazi, wanaoogopa Mungu kati ya watu wote, wanaume wanyofu na wasioweza kutiwa ufisadi, kisha waweke wasimamie hao watu.”—KUTOKA 18:21, The New English Bible.
1. Kwa sababu gani maneno “mwangalizi” na “mwanamume mzee” yanawapendeza Mashahidi wa Yehova kwa njia ya pekee?
“KUTOKA wakati wa Homeri [karibu karne ya 9 ya K.W.K.] mpaka siku zetu maneno mengi yamefifia yakamalizika; mengine mengi yameanzishwa. Maneno epískopos [mwangalizi] na presbýteros [mwanamume mzee] yameendelea kutumika.” Maelezo hayo ya msomi wa kisasa wa Kigiriki yanakazia nguvu nyingi zilizo katika maneno hayo ya Kigiriki ya kusema “mwangalizi” na “mwanamume mzee.” Kwa maelfu ya miaka maneno hayo yameshirikishwa na sehemu iliyo ya maana sana katika mpango wa kitengenezo ambao Yehova amepangia watu wake. Ikiwa wewe unashirikiana na Mashahidi wa Yehova, basi mazungumzo yanayofuata juu ya namna maneno hayo yalivyoingia katika kundi la Kikristo yatakufaa sana wewe.
2, 3. Musa alipaswa kusadikisha nani ili atumikie akiwa kiongozi wa Waisraeli aliyewekwa na Mungu?
2 Bila shaka, historia ya Biblia inaturudisha nyuma sana kuliko yule Homeri mshairi wa Kigiriki. Katika karne ya 16 K.W.K. Musa alipokea kwa Yehova agizo la kurudi Misri akawaongoze Waisraeli watoke utumwani. Kwa kuwa yeye alikuwa amekuwa mbali na watu wake mwenyewe muda wa miaka karibu 40, yeye angewaonyesha nani sifa zake za ustahili? “Wewe nenda,” Mungu akasema, “na lazima ukusanye wanaume wazee [Kigiriki, gerousía, “baraza la wazee”; ona Septuagint Version] wa Israeli . . . Na hao kwa uhakika watasikiliza sauti yako, na wewe lazima uje, wewe na wanaume wazee wa Israeli, kwa mfalme wa Misri.”—Kutoka 3:16, 18, NW.
3 Inaelekea kuwa wazi kwamba kuanzia wakati wa wazee wa ukoo, wanaume wazee walikuwa wakiheshimiwa sana kwa sababu ya ujuzi wao maishani, kwa sababu ya maarifa, hekima na uamuzi unaofaa. Wao ndio ambao Musa alipaswa kuwasadikisha ili wamkubali kuwa kiongozi wao wa kuwakomboa aliyewekwa na Mungu.
Sifa Zilizohitajiwa kwa Wanaume Wazee Katika Israeli.
4. Yethro alimtolea Musa wazo gani, na wazo hilo lilileta matokeo gani?
4 Waisraeli walipokwisha kuwa huko nje jangwani, wakiwa huru bila kuzuiwa na watekaji wao wa Kimisri, daraka la Musa la kufanyia taifa hilo maamuzi likawa mzigo mzito. Yethro, baba-mkwe wake mwenye kumtembelea, aliona wazi sana kwamba Musa alikuwa akilemewa mpaka akampa wazo linalofaa ambalo kwa wazi lilikubaliwa na Yehova. Yeye alisema hivi: “Si vema vile wewe unafanya. Kwa uhakika wewe utachoka kabisa, wewe na kundi hili la watu walio pamoja na wewe, kwa sababu shughuli hii ni furushi kubwa mno kwako wewe. Wewe huwezi kuifanya ukiwa peke yako. Sasa sikiliza sauti yangu. Mimi nitakupa maoni, na Mungu atathibitika kuwa pamoja na wewe. Wewe mwenyewe tumikia ukiwa mwakilishi kwa ajili ya watu hawa mbele za Mungu wa kweli . . . Lakini wewe mwenyewe unapaswa kuchagua kutoka kati ya watu wote wanaume hodari katika kazi, wanaomwogopa Mungu, wanaume wanaostahili kutumainiwa, wanaochukia faida ya udhalimu . . . na lazima wao walichukue furushi pamoja na wewe.” (Kutoka 18:17-23, NW) Mpango huo mpya wa hukumu katika Israeli ulisaidia kuligawanya furushi kwa wanaume wengine waliokuwa hodari katika kazi. Sasa kundi la Israeli lilikuwa na baraza la wazee waliopangwa kitengenezo wakistahili kushughulikia mambo ya hukumu na magomvi.
5. Je! Musa alipaswa kuchagua wanaume wazee wo wote tu waliopatikana?
5 Hiyo ni tofauti kubwa sana na mfumo wa sasa wa ulimwengu ambapo ni watu wachache sana wanaothamini ubora wa kanuni za hali ya juu—ambapo rushwa na ufisadi vinaharibu sifa ya watawala na watawalwa! Huko nyuma katika Israeli wa kale wanaume waliopaswa kutumikia pamoja na Musa katika kufikiliza hukumu kwa taifa walipaswa kutafutwa kwa uangalifu. Ni kama vile Yethro alivyosema: “Lazima wewe mwenyewe utafute wanaume hodari katika kazi, wanaoogopa Mungu kati ya watu wote, wanaume wanyofu na wasioweza kutiwa ufisadi, kisha waweke wasimamie hao watu.” (Kutoka 18:21, The New English Bible) Halikuwa shauri la kuchagua tu wanaume waliokuwa na umri mkubwa zaidi katika miaka. Musa alipaswa ‘kutafuta’ wanaume hodari katika kazi, wenye kustahili, wasioweza kutiwa ufisadi. Hakika hicho ni kiwango kizuri sana kwa wale walio na lazima ya kutunza faida za watu wa Yehova leo!
Wanaume Wazee Wenye Kupewa Uwezo na Yehova
6, 7. Yehova alichukua hatua gani ili kuweka wanaume wazee katika Israeli?
6 Muda fulani baadaye Waisraeli walilalamika juu ya hali za jangwani. Kwa sababu ya Musa kujisikia akilemewa sana na mzigo wa kulisimamia taifa, sasa alikiri tatizo hilo kwa Yehova. Mungu alitoa utatuzi gani? Tunasoma hivi: “Naye Yehova akamwambia Musa: ‘Nikusanyie mimi wanaume sabini kati ya wanaume wazee [Kigiriki, presbytéron, Septuagint Version] wa Israeli, ambao wewe unajua kwamba ni wanaume wazee [presbyteroi] wa hao watu na maafisa wao, . . . na mimi nitapaswa kuondoa kiasi fulani cha roho ambayo iko juu yako wewe na kuiweka juu yao, nao watapaswa kukusaidia wewe katika kulichukua furushi.’ “—Hesabu 11:16, 17, NW.
7 Musa alifanya kama alivyoamriwa, nasi tunaambiwa hivi: “Ndipo Yehova akaja chini katika wingu na kunena naye na kuondoa kiasi fulani cha roho ambayo ilikuwa juu yake na akaiweka juu ya kila mmoja wa wale wanaume wazee [presbytérous] sabini. Halafu ikaja kuwa kwamba mara tu ile roho ilipotua juu yao, ndipo wao wakaanza kutenda kama manabii.” (Hesabu 11:24, 25, NW) Huo ulikuwa ushuhuda wa wazi wa kuonyesha kwamba hao “wanaume wazee” waliwekwa kwa njia ya kitheokrasi. Yehova alikuwa amewapanga watu wake kitengenezo akawakomboa katika utumwa na sasa alikuwa akitumia ‘wanaume hodari katika kazi, wenye kutumainiwa na wenye kumwogopa Mungu’ ili washiriki daraka la uongozi na usimamizi pamoja na Musa.
8. Wakati Waisraeli walipokwisha kutulia katika makao ya Nchi ya Ahadi, wanaume wazee walitimiza daraka gani?
8 Baadaye, hao Waisraeli wenye kutanga-tanga waliiteka Nchi ya Ahadi wakarudia kukaa katika makao yasiyohamwa-hamwa katika miji na majiji, kama walivyokuwa wameishi huko Misri. Hiyo ilimaanisha kwamba wanaume wazee sasa walikuwa wamepata daraka la kuwaangalia watu katika mitaa-mitaa. Walitenda kazi wakiwa baraza la waangalizi katika mitaa yao mbalimbali, wakawa wakitolea watu waamuzi na maafisa wa kufikiliza hukumu na kudumisha amani, utaratibu mzuri na afya ya kiroho.—Kumbukumbu la Torati 16:18-20; 25:7-9; Ruthu 4:1-12.
Je! Kuwa na Kichwa Chenye Mvi Kunatosha?
9, 10. Pamoja na ukomavu wa kimwili, ni matakwa gani mengine yanayotakwa kwa “mwanamume mzee”? Toa uthibitisho wa Kimaandiko.
9 Je! yaliyotangulia yanamaanisha kwamba mwanamume ye yote aliyekuwa na umri mkubwa katika Israeli angekuwa moja kwa moja “mwanamume mzee” katika cheo cha hukumu au cha usimamizi? Je! kiwango fulani cha umri uliowekwa kingegeuza Mwisraeli awe “mwanamume mzee” katika maana hiyo? Hapana, halingekuwa jambo la akili nzuri kukata shauri hivyo. Elihu alieleza mambo kwa uwazi, akasema: “Si wale walio na wingi wa siku tu wanaothibitika kuwa wenye hekima, wala si wale walio wazee wa umri tu wanaoelewa hukumu.” Naye mkusanyaji mwenye hekima aliandika hivi: “Kuwa na kichwa chenye mvi ni taji ya uzuri wa sura wakati kunapopatikana katika njia ya uadilifu.” (Ayubu 32:6, 9; Mithali 16:31, NW; Mhubiri 12:9, 10) Maandiko ya Kiebrania yanaonyesha wazi kwamba umri wa uzee na ujuzi wa maisha katika “mwanamume mzee” mwenye kustahili ulipasa kuambatana na hekima na mwenendo wa uadilifu.
10 Lakini, umri na ujuzi wa maisha ni mambo yenye ubora mkubwa. Ili wastahili mapendeleo ya utumishi, ni lazima wanaume wazee wakubali uongozi wa roho ya Mungu na kujipatia ufahamu wa Neno lake. Haitoshi kuweza kutaja maneno ya maandiko hata bila kuyaangalia. Kujua namna ya kuyatumia kwa hekima ndilo jambo linalohitajiwa sana kwa “mwanamume mzee.”—Mithali 4:7-9; Tito 1:9.
Wanaume Wazee Katika Kundi la Kikristo
11, 12. (a) Je! bado mitaa ya Kiyahudi ilikuwa na wanaume wazee wakati Yesu Kristo alipokuwa duniani? (b) Wazee waliwekwa katika kundi la Kikristo kwa kufuata mpango wa namna gani?
11 “Kutokana na mambo ambayo tumeangalia, ni wazi kwamba tangu nyakati za kale “wanaume wazee” wenye kustahili ndio wametumiwa kuchukua uongozi katika mambo ya watu wa Yehova. Lakini kufikia wakati ambao Yesu Kristo alikuwa duniani Wayahudi walikuwa wameanzisha katika Yerusalemu baraza kuu la makuhani na wazee waliojulikana kuwa Sanhedrini. Baraza hilo lilitumika kama mahakama kuu ya Kiyahudi. (Mathayo 26:57-68) Hata hivyo, ushuhuda unaonyesha kwamba vikundi-vikundi vya wanaume wazee vilikuwa vingali vikifanya kazi katika mambo ya mitaa ya watu majijini, wala si katika mambo ya taifa lote kwa ujumla tu.—Luka 7:3-5.
12 Kwa kufikiria hali hizo za msingi za huko nyuma, ni vyepesi kuona namna kundi la Kikristo la kwanza lingeendelea kutumia mpango wa kitheokrasi unaofanana na ule uliokubaliwa na Yehova wakati wa Musa. Wakiwa chini ya uongozi wa roho takatifu ya Mungu, hao “wanaume wazee” waliowekwa katika kundi la Kikristo wangekuwa ‘hodari katika kazi, wanyofu, wasioweza kutiwa ufisadi na wenye kumwogopa Mungu.’
13. Kwa sababu gani wanaume wenye bidii na hodari katika kazi walihitajiwa katika kundi la Kikristo?
13 Tangu Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. kundi la waamini liliendelea kukua kwa haraka sana. (Matendo 2:41; 4:4) Wao hawakujitenga katika vikundi-vikundi vya kujifunza Biblia faraghani kama kwamba walikuwa watawa wenye kujiepusha na watu wa ile madhehebu ya Wayahudi iliyoitwa Esene. Ukristo haukuwa jambo la kufichwa faraghani. Ulipasa kujulishwa waziwazi, kutangazwa kwa mataifa. (Mathayo 5:14-16; 28:19, 20) Kwa sababu hiyo, wanaume wenye bidii na hodari katika kazi walihitaji kuchukua uongozi katika tengenezo la Kikristo. Ni jambo la akili nzuri kusema kwamba hao wangekuwa ndio “wanaume wazee.”
Sifa za Kustahilisha “Wanaume Wazee”
14. Petro alikazia matakwa gani ya kutimizwa na wazee?
14 Kwa uhakika, kufikia kumi la saba la miaka ya Wakati wa Kawaida sifa za kiroho zilikuwa zimekwisha kuwekwa zitimizwe na hao wanaume wazee ambao wangechukua uongozi katika kundi la Kikristo. Hivyo tunapata mitajo tele ya sifa hizo katika maandishi ya mitume Petro na Paulo. Kwa mfano, Petro aliandika hivi:
“Kwa hiyo, mimi nawatia moyo wanaume wazee miongoni mwenu hivi...: Lichungeni kundi la Mungu lililo katika uangalizi wenu, si kwa kulazimishwa, bali kwa moyo wa kupenda; wala si kwa kupenda mapato ya udanganyifu, bali kwa bidii; wala si kupiga ubwana juu ya wale ambao ni urithi wa Mungu, bali kuwa mifano kwa kundi.” (1 Petro 5:1-3, NW)
Inaweza kusemwa kwa kufaa kwamba wakati Petro alipokazia kwamba “wanaume wazee” hawakupaswa kutumikia “kwa kupenda mapato ya udanganyifu, bali kwa bidii,” alikuwa akilirudia shauri alilopewa Musa, kwamba achague “wanaume hodari katika kazi, wanaomwogopa Mungu, wanaume wanaostahili kutumainiwa, wanaochukia faida ya udhalimu.”—Kutoka 18:21, NW.
15. Ni matakwa gani ambayo Paulo alionyesha yanapasa kutimizwa na “mwanamume mzee”?
15 Katika barua ambayo Paulo alimwandikia Tito mfanya kazi mwenzake aliyemtumaini ambaye alikuwa akitumikia katika kisiwa cha Bahari ya Kati cha Krete, alimwagiza ‘asahihishe mambo ambayo yalikuwa na upungufu’ katika makundi kisha ‘aweke wanaume wazee [presbytérous] katika mji baada ya mji.’ Jambo la kupendeza ni kwamba neno la Kigiriki lililotafsiriwa “wanaume wazee” linatoa wazo la kuwa “mwanamume aliyekomaa, anayefaa kutawala jamaa yake au watu kwa sababu ya ujuzi wake na kwa sababu ya kuwa mwenye makini.” (Episcopos ya Presbyteros, kilichotayarishwa na Profesa Manuel Guerra y Gómez) Ufahamu wa kwamba hivyo ndivyo ilivyo unakaziwa pia katika matakwa ambayo Paulo alimweleza Tito kwamba yalipasa kutimizwa na Wakristo ambao wangestahili kutumikia wakiwa waangalizi. Yeye aliandika hivi:
“Ikiwa kuna mwanamume ye yote asiye na shtaka, mume wa mke mmoja, mwenye watoto wanaoamini ambao hawakushtakiwa kuwa na ufisadi wala utundu. Kwa maana yampasa mwangalizi [Kigiriki, epískopon] awe bila shtaka kama mtumishi wa nyumba ya Mungu, si mwenye kutaka yake, si mwenye kuhamaki, si mpiga kelele ya ulevi, si mpigaji, si mwenye pupa ya mapato ya udanganyifu, bali mkaribishaji wa wageni, mpenda mema, timamu katika akili, mwenye uadilifu, mshikamanifu, mwenye kujiweza, mwenye kushikamana kwa imara na neno la uaminifu kwa habari ya ustadi wake wa kufundisha, apate kuweza kutia moyo kwa fundisho ambalo ni lenye afya na kukaripia pia wale wanaopinganisha.” (Tito 1:5-9, NW)
Kurudia kuyaangalia kwa makini matakwa hayo kunatusaidia tufahamu kwamba ilikuwa lazima “mwanamume mzee” katika kundi la Kikristo afikie kiwango cha juu cha mwenendo na hali ya kiroho.
16. Tunajuaje kwamba wazee walikuwa waangalizi pia katika karne ya kwanza W.K.?
16 Pia inapendeza kuangalia namna Paulo anavyoyatumia maneno ya Kigiriki presbýteros na epískopos, “mwanamume mzee” na “mwangalizi.” Kutokana na hilo tunaweza kukata shauri la kwamba wanaume wazee wenye kustahili walitimiza wajibu mbalimbali wa waangalizi katika makundi. Maandiko mengine yanaonyesha kungeweza kuwa na hesabu kubwa ya waangalizi-wanaume wa namna hiyo katika kundi lile lile moja.—Matendo 14:23; 20:28; Wafilipi 1:1.
17. (a) Paulo alimpelekea Timotheo matakwa gani ya kutimizwa na mwangalizi? (b) Ni kwa sababu gani lazima mzee awe mwenye bidii katika utendaji wa kuhubiri pia?
17 Alipokuwa akimwandikia Timotheo pia, Paulo alionyesha matakwa yanayopasa kutimizwa na mwangalizi, lakini akatumia maneno tofauti kidogo, labda kwa kuzifikiria hali tofauti zilizohusika. (1 Timotheo 3:1-7) Kwa kuwa kundi la kwanza la Kikristo kwa asili lilikuwa tengenezo lenye kueneza evanjeli, lilionwa kuwa jambo la kawaida kwamba hao wanaume wazee wangekuwa pia wenye bidii katika kuzitangaza habari njema. Hawakuruhusiwa nafasi ya kufanya ugoigoi.—Luka 24:46-48; 1 Wakorintho 9:16; linganisha Mathayo 25:24-27.
Uasi-Imani Unajipenyeza-penyeza
18. Uasi-imani uligeuzaje cheo cha waangalizi?
18 Kundi lilipozidi kusonga mbele na kuingia katika karne ya pili na ya tatu, mambo yalianza kubadilika. Uasi-imani uliokuwa umetabiriwa ulitia mizizi. (Matendo 20:29, 30; 2 Petro 2:1) Watu wenye kujitakia makuu waliinuka kati ya wazee wale wale waliokuwa katika makundi. Wakiwa wamegeuza makusudi yao wakaanza kukiona cheo chao cha mwangalizi kuwa cha uwezo na cha kujipatia heshima kubwa. Hata waangalizi fulani wa makundi wakawa “maaskofu” wenye kutawala wilaya fulani au kikundi cha makanisa. Baadaye maaskofu hao wakapigiwa kura na watu walio wa kawaida tu kidini ili waingie katika cheo, wengine wao wakiwa ni watawala wenye ushawishi mkubwa. Basi, ni kama vile mwanahistoria mmoja Mkatoliki alivyoandika: “Jambo hilo lilileta hatari kubwa sana, hasa kuanzia wakati heshima kuu ya askofu ilipozidi kuongezeka na wenye vyeo hivyo wakapewa mapato makubwa na faida za kimwili . . . [na hivyo] wanasiasa wakapandishwa kwenye vyeo vya kusimamia maeneo yaliyo na maongozi makubwa zaidi ya kiaskofu.”
19. Matokeo ya mwisho ya uasi-imani yalikuwa nini?
19 Ndiyo, kila askofu aliinuliwa cheo kama mtawala mwenye uwezo mwingi. Halafu jambo hilo nalo likatokeza migawanyiko na vikundi-vikundi vilivyo katika Jumuiya ya Wakristo, ambayo ilikuwa imekwisha kuacha Ukristo wa kweli muda mrefu uliopita. Mpango wa kitheokrasi wa kuwa na waangalizi-wazee walio hodari katika kazi, wanyofu na wenye kujali mambo ya kiroho ukazorota na kuwa utawala wa serikali ya mapadri. Ule utumishi ambao kundi lilikuwa likipewa kwa njia ya kujitolea ukageuzwa ukawa kazi yenye malipo yenye kuhitaji mtu awe na elimu ya juu katika mambo ya kidini, falsafa na sheria za kanisa.
20. Ni maulizo gani ambayo sasa yanahitaji majibu?
20 Je! hiyo ilimaanisha kwamba Ukristo wa kweli, pamoja na mpango wa kitheokrasi uliokuwa nao hapo kwanza kwa ajili ya kila kundi, usingerudishwa tena? Au ilimaanisha kwamba ule utumishi wenye kufaa usiotia ndani mambo mengi-mengi ambao ulifanywa na “wanaume wazee,” au “waangalizi,” ulikuwa umepotea milele? Namna gani ule unabii wa Isaya wenye kuelekeza kwamba tengenezo la kitheokrasi lingeinuliwa liwe na hali ya juu? Unabii huo unasema: “Badala ya shaba nitaleta dhahabu, na badala ya chuma nitaleta fedha, na badala ya mti, shaba, na badala ya mawe, chuma; tena nitawafanya wasimamizi wako wawe amani, na hao wakutozao fedha [wanaokugawia kazi, NW] kuwa haki.” (Isaya 60:17) Makala inayofuata itajibu maulizo hayo ya maana.
Wewe Unaweza Kujibu?
◻ Ni wanaume wa namna gani waliochaguliwa kugawana na Musa daraka la hukumu katika Israeli wa kale?
◻“Wanaume wazee” walitumikia wakiwa katika cheo gani wakati Waisraeli walipokuwa wamekwisha kutulia katika Nchi ya Ahadi?
◻ Ni nini nyingine za sifa zenye kutokeza ambazo wazee au waangalizi Wakristo walitazamiwa kuwa nazo?
◻ Ule uasi-imani uliotabiriwa ulikuwa na matokeo gani juu ya mpango wa wazee?
[Picha katika ukurasa wa 11]
Wanaume wazee wa Israeli walitumikia wakiwa waamuzi kwenye malango ya mji