Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w79 8/15 kur. 8-13
  • Ziara za Wanaume Wazee Huwafaidi Watu wa Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ziara za Wanaume Wazee Huwafaidi Watu wa Mungu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • NAMNA ZIARA ZA WANAUME WAZEE ZILIVYOONWA
  • MSAADA WENYE KUFAA UNAOTOLEWA MAKUNDI
  • MPANGO WENYE UPENDO WA KUTUTUIA NGUVU SISI
  • Waangalizi Wasafirio—Zawadi Zikiwa Wanadamu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Waangalizi—Iweni Mifano Myema kwa “Kundi”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Waangalizi Wasafirio Waleta Faida Leo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Jinsi Ambavyo Waangalizi Wasafirio Hutumikia Wakiwa Wasimamizi-Nyumba Waaminifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
w79 8/15 kur. 8-13

Ziara za Wanaume Wazee Huwafaidi Watu wa Mungu

“Wakarejea mpaka Listra na Ikonio na Antiokia, wakifanya imara roho za wanafunzi na kuwaonya wakae katika ile Imani, na ya kwamba imetupasa kuingia katika ufalme wa Mungu kwa njia ya dhiki nyingi.”​​—⁠Matendo 14:21, 22.

1. Ni kwa sababu gani ziara za waangalizi wasafirio zahitajiwa leo, kama zilivyohitajiwa katika karne ya kwanza?

KATIKA karne ya kwanza, mitume pamoja na wanaume wengine wazee walifanya ziara katika wakati ufaao kwenye makundi ya Kikristo wakiwa kama waangalizi wasafirio. Leo waangalizi wasafirio wanafanya ziara kwa ukawaida kwenye makundi zaidi ya 42,000 ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Je! ziara hizo, za kale na za kisasa zina mengi yanayofanana? Ndiyo, bila shaka! Kwa kuwa mahitaji ya Wakristo leo ni kama yale yale ya nyakati za kimtume. Tunahitaji kutiwa moyo pamoja na msaada wenye kufaidi wa ziara hizi ili tuendelee kufanya mapenzi ya Mungu chini ya hali zenye kujaribu.

2. (a) Wakristo wamekutana na magumu gani, katika karne ya kwanza na katika wakati wa sasa, kukahitaji kazi gani ifanywe? (b) Ni kwa sababu gani ziara za wanaume wazee zimeonwa kuwa msaada?

2 Kwa sababu ya kutokamilika kulikorithiwa, Wakristo wa kwanza walipatwa na magumu kama yale yanayotupata sisi. (Rum. 3:23) Majaribu waliokabili yalifanana na yale tunayolazimika kupinga sasa. (1 Kor. 10:13) Waliishi katikati ya taratibu mbovu ya mambo ambayo ingali ipo leo na ambayo sisi sote tunatamani kukombolewa kutokana nayo. (Gal. 1:4) Adui yao mkubwa, Ibilisi, lazima nasi vilevile tumpinge. (1 Pet. 5:8) Wakikabiliwa na udhaifu wa kimwili, mikazo kutoka katika ulimwengu pamoja na upinzani kutoka kwa jeshi la pepo wabaya wasioonekana, Wakristo hao wa karne ya kwanza walikuwa na kazi ya kufanya. Agizo lao lilikuwa kuhubiri “habari njema” na kufanya wanafunzi. Leo agizo hilo linawapasa Mashahidi wa Yehova vilevile nalo lazima likamilishwe kabla mwisho unaokuja wa ulimwengu huu usiomwogopa Mungu. (Mt. 28:19, 20; Matendo 1:8) Katika wakati huo na wakati wa sasa, ziara za wanaume wa kiroho zimepokelewa na kuonwa kuwa msaada wa kutia nguvu na kuwatia moyo pamoja na kusaidia watu wa Mungu.

3. Tunaweza kupata faida gani kwa kujikumbusha habari za ziara za nyakati za kimtume na kutoa mifano ya kisasa?

3 Ziara hizi za nyakati za kimtume hutoa uongozi unaofaa kwetu sisi leo. (Matendo 14:21-23; 15:36) Tunapochunguza habari za Kimaandiko na kuona mifano inayolingana nayo leo, tunapaswa kuthamini zaidi mpango huo wa “zawadi katika wanaume” wanaotumikia na kutosheleza mahitaji yetu.​—⁠Efe. 4:8, 11, 12, NW.

NAMNA ZIARA ZA WANAUME WAZEE ZILIVYOONWA

4. Ziara katika kundi la Antiokia iliwafaidije ndugu?

4 Ilikuwa baada ya Baraza ya Yerusalemu ya 49 W.K. kwamba Yuda na Sila walipotumwa Antiokia pamoja na Paulo na Barnaba. Ikiwa ungalikuwapo, Ungalionaje? Kulingana na Matendo 15:32 “manabii” hawa wawili Yuda na Sila “walizungumza na hao ndugu kwa muda mrefu wakiwatia moyo na kuwapa nguvu.” (HNWW) Wakati uliotangulia, kulikuwako kutopatana katika Antiokia juu ya ulizo la kutahiri. Walakini sasa kundi la Antiokia lilipopokea barua iliyoongozwa na roho, pamoja na ziara hii ya hawa “manabii” wawili, jambo hilo lilimalizwa. Kundi hilo lilikuwa na sababu nzuri ya kufurahi.​—⁠Matendo 15:2, 22-31.

5. Wafilipi 2:20-22 latuambia nini juu ya kustahili kwa Timotheo?

5 Roho ya unyenyekevu na ya kujinyima ndiyo iliyowafanya hawa “wanaume wazee” wawe kitia-moyo cha namna hiyo kwa ndugu zao. Kwa mfano, kulikuwako Timotheo, mmisionari mwenzi wa Paulo, ambaye kwa habari yake Paulo aliandika hivi: “Maana sina mtu mwingine mwenye nia moja nami, atakayeiangalia hali yenu kweli kweli. Maana wote wanatafuta vyao wenyewe, sivyo vya Kristo Yesu.” Paulo, mwenzi mfanya kazi wa Timotheo hakusita kumtuma katika kundi la Wafilipi, kwa kuwa angetumika kati yao kwa “ajili ya Injili.”​—⁠Flp. 2:20-22.

6. (a) Ndugu katika Kirete wangefaidikaje ikiwa Tito angefuata maagizo ya Paulo? (b) Shauri la Tito lingekuwa na matokeo gani juu ya vijana na wazee, wanaume kwa wanawake?

6 Kwa kawaida, wanaume wazee waliotumwa katika eneo fulani walikaa huko kwa kipindi kirefu ili wawatie ndugu nguvu. Kulikuwako uhitaji mkubwa wa Tito asaidie kutatua matatizo katika Kirete. Aliambiwa “[a] yatengeneze yaliyopunguka, na kuweka wazee katika kila mji.” Vilevile, kwa sababu ya kutotii, pamoja na maneno yasiyo na maana na mafundisho ya udanganyifu ya wengine, Tito alipaswa aendelee kuwakaripia vikali wasio na utaratibu, ili wapate kuwa “wazima katika imani.” (Tito 1:5-14) Alipaswa kuwashauri na kuwasihi wanaume na wanawake wenye umri mkubwa, pamoja na vijana wanaume na wanawake, pamoja na watumwa, ili kwamba njia yao ya maisha ipate ‘kuyapamba mafundisho ya Mwokozi wetu Mungu katika mambo yote.’​—⁠Tito 2:1-10.

7. (a) Huko nyuma waangalizi wenye kuzuru walikuwa wamestahili kwa kutimiza matakwa gani? (b) Kulingana na 1 Wakorintho 11:1, wanaume wazee kama Paulo walipaswa kuonwaje?

7 Ni wazi kwamba waangalizi wasafirio waliostahili walitoa mafundisho yaliyohitajiwa sana kwenye makundi katika karne ya kwanza. Wote walikuwa na ujuzi wa miaka mingi katika kazi ya kuhubiri, na katika kushughulikia madaraka kama wazee na katika kuvumilia magumu. Baada ya kusimulia juu ya mateso na hatari zilizompata, Paulo alionyesha namna yeye alivyoyaona madaraka yake kwa uzito, akisema: “Na pamoja na maneno yale ya inje, kuna maneno yanayonisonga mimi kila siku, ndiyo masumbuko ya kulinda makanisa yote.” (2 Kor. 11:23-28, HNWW) Tito, Timotheo na wengine walishirikiana sana naye katika hayo yaliyompata. (2 Kor. 8:23; 2 Tim. 3:10, 11) Mfano wao mzuri wa imani uliwafanya wastahili kuigwa.​—⁠1 Kor. 11:1.

8. Wazee kutoka Efeso walipokea onyo gani la upole, nao walimwonaje Paulo?

8 Si kwamba tu ndugu waliwaheshimu sana “wazee” hawa wasafirio wenye mfano mzuri kwa sababu ya kazi yao njema bali pia walionyesha upendo wao mwingi sana kwao. Mfano mmoja wenye kutokeza sana unahusu wakati Paulo alipokutana na wazee kutoka Efeso. Aliwapa onyo hili la upole: “Jiangalieni ninyi wenyewe na kundi lote, ambalo miongoni mwake roho takatifu imeweka ninyi kuwa waangalizi, kuchunga kundi la Mungu, ambalo yeye alinunua kwa damu ya Mwana wake mwenyewe.” (Matendo 20:28, NW) Kisha alionya juu ya uasi wa imani uliokuwa ukija, akawasihi wawe macho na kuwasaidia wenye udhaifu. Baada ya kusali pamoja, wazee hao walilia walipokuwa wakimwaga Paulo, wakihuzunika sana sana sana kwa kujua kwamba hawataona uso wake tena.​—⁠Matendo 20:29-38.

MSAADA WENYE KUFAA UNAOTOLEWA MAKUNDI

9. Waangalizi wenye kuzuru waliyasifuje na kuyatia moyo makundi?

9 Mara nyingi waangalizi wasafirio waliwasifu waamini hao wa kwanza kwa sababu ya sifa njema walizozionyesha. Ndivyo ilivyokuwa kwa habari ya “watakatifu” katika Kolosai. Epafra alikuwa amesema juu ya matendo yao mema pamoja na upendo wao katika njia ya kiroho, na kwa sababu hiyo Paulo alishukuru Mungu. (Kol. 1:2-8) Ziara ya Paulo katika Thesalonike ilileta matokeo yenye kutokeza sana. Baadaye aliwaandikia waamini huko akionyesha matendo yao ya imani, kujitaabisha kwao pamoja na uvumilivu. Walikuwa wamelipokea neno kwa taabu nao walikuwa wamekuwa waigaji wazuri wa wanaume kama vile Paulo, Sila na Timotheo. (1 The. 1:1-7) Kwa maneno na kwa mfano, wanaume hao wazee waliwafundisha wanafunzi wa kwanza na kuwaonyesha namna matunda ya roho ya Mungu yangeweza kuonyeshwa katika maisha ya kila siku. Walitiwa moyo wamtumaini Yehova kabisa kabisa na kumtegemea daima katika sala. Makundi yalifurahia ziara hizo, yakikubali kwamba yalitiwa nguvu na kutiwa moyo “wakae katika imani.”​—⁠Matendo 14:22.

10. (a) Kwa sababu gani haikuwezi kuwa kuridhiana kwa habari ya usafi wa kiroho na wa adili? (b) Wanaume hao wazee waliwatiaje moyo wachungaji wa mahali waliowekwa?

10 Bila shaka, mitume pamoja na wanaume wazee walichukua hatua kuona kwamba makundi katika wakati huo yalifanya kazi kwa utaratibu na kwa kupatana, chini ya ukichwa wa Kristo. (Efe. 4:15, 16) Walijua kuwa ilikuwa lazima kudumisha usafi wa kiroho na wa adili. Hakungekuwa kuridhiana katika jambo hilo. Ama sivyo, kundi la Kikristo lingewezaje kujitenganisha na ulimwengu na kutumiwa kama chombo chenye heshima katika kutimiza kazi ya Yehova? (2 Kor. 6:14-17; 1 The. 4:3-8; 2 Tim. 2:20-22) Ili kukazia maana ya kutii matakwa ya kimungu, wanaume hao wazee walifanya ziara na kuandika barua za kuwasaidia waangalizi wa mahali waliowekwa pamoja na kundi lililokuwa katika uangalizi wao.​—⁠1 Pet. 5:1-5.

11. Kupatana na shauri la Paulo kwa Timotheo, ni kitia-moyo gani ambacho waangalizi wenye kuzuru wa-naweza kutoa kwa waangalizi wote wa makundi leo?

11 Paulo alimwonya hivi kwa upole mwangalizi kijana Timotheo: “Uwe kielelezo kwao waaminio, . . . ufanye bidii katika kusoma na kuonya na kufundisha . . . ili kuendelea kwako kuwe dhahiri kwa watu wote.” (1 Tim. 4:12-15) Katika ziara zao leo, waangalizi wasafirio wanatoa mashauri yanayofanana na hayo. Na kama vile Paulo alivyomwagiza Timotheo, wanawatia moyo waangalizi wote wa makundi ‘walihubiri neno, wawe tayari, wakati uwafaao na wakati usiowafaa, wakaripie, na kukemea, na kuonya kwa uvumilivu wote na mafundisho,’ na ‘kufanya kazi ya mhubiri wa Injili,’ kuikamilisha kabisa huduma hii.​—⁠2 Tim. 4:1-5.

12. Ni shauri gani juu ya kutoa hukumu lililopewa kundi la Korintho?

12 Mitume hawakusita kuonyesha linalopaswa kufanywa kwa habari ya kutoa hukumu. Paulo alipokutana na hali iliyohusiana na kufanya makosa ambayo ilikua haijasahihishwa, alitoa shauri kwa barua vile yeye angefanya kama angalikuwapo, akiwaagiza kwa uthabiti wenye madaraka katika Korintho ‘wamwondoe yule mbaya miongoni mwao.’ (1 Kor. 5:3, .13) Vilevile yeye aliwatia moyo kwamba kutopatana kwa kibinafsi kati ya ndugu kunapaswa kumalizwa na wanaume wanaostahili kuhukumu. (1 Kor. 6:1-6) Shauri la namna hiyo liliwasaidia ndugu wenye madaraka watengeneze upya kufikiri kwao.

MPANGO WENYE UPENDO WA KUTUTUIA NGUVU SISI

13. (a) Kwa sababu gani tunaweza kumshukuru Yehova kwa mpango wa waangalizi waaminifu, kutia na wale wanaozuru makundi kwa ukawaida? (b) Wengi wa waangalizi wasafirio wamekuwa na ujuzi gani?

13 Kwa sababu leo roho ya Yehova inafanya kazi katikati ya watu wake, wanaume wenye juhudi wanaostahili wenye ujuzi wa miaka mingi wa kuzuru makundi wanapatikana. (Linganisha Waefeso 4:11, 12.) Wajapokuwa wao ni wanaume wasikamilika (wenye makosa), wanaonyesha nyingi za sifa zilizoonyeshwa na Paulo, Sila, Barnaba, Timotheo na wengine. Kwa wakati huu kuna waangalizi wengi wasafirio walio na ujuzi wa zaidi ya miaka 30 katika utumishi wa wakati wote. Mmoja ambaye anatumikia sasa kama mwangalizi wa mzunguko alichuka utumishi wa wakati wote miaka 55 iliyopita alipokuwa na umri wa miaka 18. (Mhu, 12:1) Aliendelea kutumikia tangu wakati huo, akitumia miaka 30 iliyopita katika kuyatembelea makundi. Karibu wanaume hawa wote wametumikia kama waangalizi na kama mapainia katika makundi ya mahali pao. Wengine wametumia miaka mingi katika utumishi wa misionari au katika afisi ya tawi ya Sosaiti. Kuwako kwa wanaume kama hao katika kundi ni baraka, kukisaidia wote wajipatie nguvu kutokana na mambo ya kiroho ambayo wanashiriki pamoja nao. Ziara zao zaweza kutusaidia katika utumishi pamoja na ibada yetu na katika kusitawisha utu wa Kikristo.

14. Ni jambo gani linaloonyesha kwamba wanaume hawa wazee wanastahili, nao wanajitahidi kusitawisha nini katika wengine?

14 Wajumbe wanaotumwa kwenye makundi sikuzote wanakuwa wanaume wanaoongoza katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. Wao wamelifahamu neno nao wanazaa matunda mengi mema. (Mt. 13:23) Wakiona haraka nyingi kwa sababu ya kuthamini maana ya ufalme wa Mungu, na kutambua hatari ya hizi siku za mwisho, hawatanga-tangi katika kazi yao. (Rum. 12:11) Wakiwa na maoni hayo, wanajitahidi kujenga katika wengine roho ile ile ya kuwa mhubiri wa injili iliyotambulisha kundi la kwanza la Kikristo.​—⁠Matendo 5:42; 8:1-4.

15. (a) Waangalizi wasafirio wanazionaje amri za Yesu katika Mathayo 24:14 na 28:19, 20? (b) Kupatana na yaliyotukia baada ya Pentekoste ya mwaka 33 W.K., wanatoa msaada na mfano gani kwa makundi leo?

15 Kuheshimu sana amri ya Yesu ya kuhubiri “habari njema” na kufanya wanafunzi kunawasukuma waangalizi wasafirio wakazie amri hii yenye sehemu mbili ambayo ni amana takatifu, takwa la kimungu. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Wanakumbuka lililotukia baada ya siku ya Pentekoste katika mwaka 33 W.K., na vilevile baada ya hapo, baada ya Kornelio na nyumba yake kugeuka, yaani, kwamba waamini waliongezeka kwa haraka sana nao wakafunzwa kabisa, ili wapate kuishi kulingana na “habari njema” na kuitangaza kwa wengine kwa matokeo. (Matendo 2:46, 47; 5:14; 6:7; 10:44-48; 20:20) Leo, ili kuongeza waamini wengine, waangalizi wasafirio wanawakaribisha wengi iwezekanavyo washiriki pamoja nao katika kutoa ushuhuda. Wanawasaidia wale wasio na ujuzi. Bidii na uongozi mzuri wa wazee wanaozuru unaongeza sana mpanuko wa kazi ya kutoa ushuhuda. Wanasema pamoja na Paulo hivi: “Ole wangu nisipoihubiri Injili!”​—⁠1 Kor. 9:16.

16, 17. (a) Kwa habari ya kulinda makundi yasiingiliwe na ulimwengu, waangalizi wasafirio wanaweza kutoa kitia-moyo gani? (b) Ni katika njia gani wanaweza kuwasaidia ndugu katika kuyapinga maongozi ya werevu ya mambo ya kimwili?

16 Zaidi ya hayo, kuna kazi nyingi ya kufanywa katika kuwasaidia wale wanaoshirikiana na makundi wafanye maendeleo katika maisha ya Kikristo. (2 Pet. 1:5-10) Wengine ambao bado hawajaacha tabia za kilimwengu huenda wakajaribu kuingiza ndani ya kundi mazoea yanayoweza kupunguza kanuni za juu za mwenendo zilizowekwa katika Neno la Mungu. Ili kulinda uulimwengu usipenye polepole, waangalizi wasafirio wanahitaji kuonyesha ufahamu katika kuyaona maelekeo ya werevu. Watataka kuwatia watu wa Mungu moyo washikamane kabisa na kanuni za Maandiko kwa habari ya mazoea yao ya maisha, adili na katika kushughulika na wengine, ama katika mambo ya watu mmoja mmoja au ya kijamii (1 Kor. 10:31-33; 1 Pet. 1:14-16; Ebr. 13:18) Huenda wakahitaji kuwakumbusha wazee watende kwa uthabiti katika kudumisha usafi wa adili, wa mafundisho na wa kiroho katika makundi.

17 Kupatana na shauri alilopokea Timotheo, waangalizi wasafirio wanahimizwa wawaonye Wakristo juu ya maongozi yenye kuwaingilia ya mambo ya kimwili. (1 Tim. 6:9, 10, 17-19) Kwa mfano wao wenyewe kwa kutanguliza mambo ya kiroho wanawatia wengine moyo ‘watafute kwanza ufalme wa Mungu.’​—⁠Mt. 6:33.

18. Ni kwa sababu gani kuwa imara na kukomaa kiroho ni jambo la maana sana, nao ndugu wanaweza kutiwaje moyo katika hilo?

18 Katika ulimwengu ambamo watu wanapeperushwa huku na huku na pepo zenye kuvuruga akili za mafundisho ya kidini, watu wa Yehova wanahitaji kuwa imara, Wakristo waliokomaa. (Efe. 4:13, 14) Msimamo wao unapaswa kuwa imara, wala si ule wa kugeukageuka kwa haraka kwa sababu ya mawazo ya kujitegemea au mikazo ya moyoni. (Kol. 1:23; 2:6, 7) Kwa kufaa, basi, waangalizi wasafirio wanahitaji kukazia uhitaji wa Wakristo wote kuendelea kukua katika maarifa yaliyo sahihi ya Mungu. (Flp. 1:9, 10; Kol. 1:9-11) Wanatia moyo kuwe na funzo la pekee, la jamaa na la kundi ili Wakristo wasitumie ‘maziwa ya neno’ tu, bali pia watumie “chakula kigumu,” ili walithamini kabisa lile “neno la haki,” na kuwa na “akili zao, kwa kutumiwa, zimezoezwa kupambanua mema na mabaya.” (Ebr. 5:12-14) Wanapoichunguza hali ya kiroho ya kundi, waangalizi wasafirio watatoa mashauri juu ya mambo hayo kwa kutumia Maandiko.

19. Waangalizi wasafirio wanawasaidiaje watu mbali-mbali kulingana na mahitaji ya kila mmoja wao? (Yakobo 5:19, 20)

19 Wanaume hawa wazee wanaweza kutembela wagonjwa, wale wenye umri mkubwa pamoja na wengine, kulingana na unavyoruhusu wakati. (Mit. 16:31; Mt. 18:12-14; tofautisha Ezekieli 34:4.) Wanapokaribiwa na watu ambao wamekosa mapatanao katika mambo ya kipekee, kwa upendo, wanaweza kutoa onyo la upole lakini kwa uthabiti kutoka katika Maandiko, kwa kusudi la kurudisha amani. (1 The. 5:14, 15) Katika njia ambazo mara nyingi hazionwi, wanaweza kuwajenga kiroho wale walio na mashaka juu ya mwenendo wa Kikristo au wanaohitaji kwa vyo vyote ‘kunyakuliwa kutoka katika moto.’​—⁠Yuda 22, 23.

20. Waangalizi wasafirio na wake zao wamekuwa wenye kujinyima namna gani?

20 Kama vile ilivyokuwa katika karne ya kwanza, waangalizi hawa wasafirio pamoja na wake zao wanatumikia chini ya hali mbalimbali. Katika sehemu nyingi za dunia wanakwenda kutoka mahali pamoja kwenda mahali pengine kila juma. Ili wafikie maeneo yaliyo peke yake katika sehemu zenye misitu, wengine wanapanda farasi au mashua, au wanatembea kwa miguu umbali mrefu katika vijia au mapito yanayopitia milimani. Ili wayafaidi makundi wanavumilia magumu mengi. Wengi wao wamekubali migawo mbali sana na jamaa zao na rafiki wakubwa. Walakini bila kujali hali yao, wao wana nia ya kujitoa, na kuwa tayari kuwa wenye kubadilikana kwa ajili ya “habari njema.”​—⁠1 Kor. 9:23.

21. (a) Kujikumbusha juu ya huduma ya wanaume hawa wazee kunapaswa kutusaidie tuthamini jambo gani? (b) Kwa hiyo tunaongozwa tuulize ulizo gani?

21 Kujikumbusha njia ambazo katika hizo ziara za wanaume wazee waaminifu zimeyatia makundi nguvu, katika nyakati za kimtume na za kisasa, kunatufanya tuthamini sana jitihada zao. Kweli kweli wanaume wazee kama hao wenye kujitaabisha sana wamo miongoni mwa wale ambao kwa habari yao mtume Paulo aliandika hivi: “Ndugu, tunataka mwatambue wale wanaojitaabisha kwa ajili yenu, na kuwasimamia ninyi katika Bwana, na kuwaonyeni; mkawastahi sana katika upendo, kwa ajili ya kazi zao.” (1 The. 5:12, 13) Ijapokuwa tunawaheshimu hivyo hawa waangalizi wasafirio, tunawezaje sisi binafsi kupata faida kubwa zaidi kutokana na ziara zao katika siku zijazo? Ebu na tuone sasa.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki