Waangalizi—Iweni Mifano Myema kwa “Kundi”
“Uwe kielelezo kwao waaminio, katika usemi na mwenendo, na katika upendo na imani na usafi.”—1 Tim. 4:12.
1. Sababu gani tutazamie waangalizi Wakristo waweke mfano mwema?
MENGI yanatiwa ndani katika kutumikia kama mwangalizi katika kundi la Kikristo. Jambo hilo la hakika linakubaliwa na maelfu ya wanaume walio wakf, walio wa kiroho ambao wamekabidhiwa pendeleo hilo leo. Kwa kuwa watu wote katika kundi ni ndugu na dada za Kikristo, wazee waliowekwa wanajua kwamba daraka lao haliwafanyi wawe bora zaidi kuliko waabudu wengineo wa Yehova. (Mt. 23:8-12) Hata hivyo, kwa sababu ya madaraka yao na matakwa ya Kimaandiko wanayopaswa kutimiza, mengi yanatazamiwa kutoka kwao. Ni kama vile Yesu alivyosema: “Na kila aliyepewa vingi, kwake huyo vitatakwa vingi; naye waliyemwekea amana [uangalizi] vitu vingi, kwake huyo watataka na zaidi.” (Luka 12:48) “Kundi” linapasishwa sana na yale ambayo wachungaji hao wadogo wanasema na kutenda. Kwa hiyo, inatazamiwa kwamba wanaume hao watawekea. wengine mfano mzuri.
2. Paulo alimtia moyo Timotheo awe mfano mwema katika njia zipi?
2 Jambo hilo la kuwa mfano mzuri lazima likaziwe. Jambo hilo ni mojawapo la mambo ya kushauri ya moja kwa moja yanayopatikana katika barua ya kwanza ya Paulo aliyomwandikia mwangalizi Timotheo. Paulo hakuliona jambo lo lote vivi hivi tu, naye hakutaka Timotheo aone mambo vivi hivi tu. Kwa sababu Timotheo alikuwa angali kijana, huenda wengine wangemdharau. Bila shaka Paulo alijua jambo hilo alipoandika hivi: “Mtu awaye yote asiudharau ujana wako, bali uwe kielelezo kwa waaminio, katika usemi na mwenendo, na katika upendo na imani na usafi. Hata nitakapokuja, ufanye bidii katika kusoma [mbele ya watu wote] na kuonya na kufundisha. Usiache kuitumia karama ile iliyomo ndani yako, uliyopewa kwa unabii na kwa kuwekewa mikono ya [baraza ya] wazee.” (1 Tim. 4:12-14) Hakungekuwako sababu halali kwa wengine kumdharau Timotheo iwapo angeendelea kufuata mwendo wa maisha ya Kikristo ulio mfano mwema.
3. Waangalizi wanapaswa kuchunguza nini, na sababu gani?
3 Kama vile Timotheo, waangalizi kati ya watu wa Yehova leo wanapaswa kuchunguza kielelezo chao cha maisha. Ingawa mazungumzo yetu sana sana yanahusu waangalizi, watumishi wa huduma na wanaume wanaojitahidi kufikia madaraka makubwa zaidi ya kundi, Wakristo wote wanapaswa kufikiria kwa uangalifu yanayohusika katika kutumikia kama mfano kwa “kundi.” (2 Kor. 13:5) Walakini sasa twauliza hivi: “Enyi wazee, je! kweli kweli mnaweka mfano mwema?” Waamini wenzenu wanawaangalia wakiwa wanakumbuka maneno haya yaliyoandikwa katika Waebrania 13:7, NW: “Wakumbukeni wale wanaoongoza kati yenu, ambao wamewaambia neno la Mungu, nanyi mnapotazama sana namna mwenendo wao utakavyokuwa iigeni imani yao.” Ndiyo, wazee, rafiki zenu Wakristo wanataka kujionyesha kuwa waaminifu kwa Yehova. Ili wafanye hivyo wanahitaji si mashauri ambayo msingi wake ni Maandiko na maneno ya kufariji tu bali pia wanahitaji mfano wenu wenye kutia moyo. Wataiiga imani yenu wanapoona mwenendo wenu unaofaa na matokeo yake.
4. (a) 1 Timotheo 3:1 na Mathayo 20:26, 27 yanakaziaje yanayohusika katika kutumika kama waangalizi Wakristo? (b) Ili mzee atimize madaraka yake inampasa afanye mambo gani? (c) Kulingana na 1 Wathesalonike 5:12, 13, akina ndugu wanapaswa kuheshimu nani, nao wanapaswa kuonyesha jambo hilo kwa njia gani?
4 Hiyo haimaanishi kwamba ukiwa mzee aliyewekwa ni wewe tu uwezaye kazi hiyo. Sivyo kabisa. Walakini una “kazi njema” ya kutumikia ndugu na dada zako za kiroho. (1 Tim. 3:1) Cheo chako si ‘ukubwa’ fulani unaotokana na jitihada zako. (Mt. 20:26, 27) Ndiyo, una mapendeleo na madaraka ya ziada. Lakini ili utimize mambo hayo inavyofaa utahitaji kutumikia Yehova kwa unyenyekevu, Yesu Kristo na waamini wenzako. (Rum. 12:11; Gal. 5:13; Kol. 3:23, 24) Hakika, unapaswa kufanya kazi kwa bidii, usimamie, ushauri na kufanya mambo mengine kwa ajili ya ndugu na dada zako walio katika imani. Wanakubali kwamba umepewa mgawo; walakini ni kazi ya bidii unayofanya pamoja na mfano wako, inayowachochea waitikie kutegemeza jitihada zako. Heshima hiyo inastahili nayo yapatana na maneno ya mtume Paulo: “Lakini, ndugu, tunataka mwatambue wale wanaojitaabisha kwa ajili yenu, na kuwasimamia ninyi katika Bwana, na kuwaonyeni; mkawastahi sana katika upendo, kwa ajili ya kazi zao.”—1 The. 5:12, 13.
Mfano Mwema “katika Kusema”
5. Waangalizi wanapaswa kuwa mfano mwema “katika kusema” katika njia zipi mbalimbali, nalo jambo hilo ni la lazima kwa sababu gani?
5 Hakuna shaka kwamba waangalizi wanapaswa kuwa mfano mwema “katika kusema.” Bila shaka, hilo ni jambo linalopaswa kuwa hivyo nyumbani mwao. Vile-vile, linapaswa kuwa wazi wanapozungumza na washiriki mmoja mmoja wa kundi au wakiwa katika jukwaa la kuzungumza na watu wote, pamoja na wanapotoa ushuhuda nyumba kwa nyumba katika ujamii wao. Maelezo ya mwangalizi yanaweza kuongoza wengine kuliko anavyojua. Kwa hiyo anayosema yanapaswa sikuzote kuwa na msingi au kuongozwa na kanuni za Neno la Mungu.
6. Sababu gani wazee wanapaswa kujihadhari na mawazo mabaya ila ‘waseme mema’?
6 Ili usemi uwe wenye kujenga, moyo unapaswa kujazwa na mambo mema kutoka katika Neno la Mungu. Kisha kinywa ‘kitanena mema,’ kikisema mambo ambayo yanafaa na yenye kujenga kiroho. (Mt. 12:34) Mwangalizi anapaswa kujihadhari asiruhusu mawazo mabaya yasitawi akilini au moyoni mwake, kwa kuwa mwishowe jambo hilo lingejionyesha katika usemi wake nalo lingekuwa lenye kuharibu wengine. Ikionyesha mambo yanayopaswa kuepukwa na namna ya misemo inayopaswa kusikiwa, Biblia inashauri hivi: “Usemi mbaya usipitie kinywani mwako, ila tu yaliyo mema na yenye kusaidia wakati huo, ili kwamba yalete baraka kwa wale wanaosikia.”—Efe. 4:29, The New English Bible.
7. Sababu gani waangalizi Wakristo wanapaswa kuepuka kueneza maoni au mawazo yao ya kibinafsi?
7 Ili kuwa mfano mzuri katika kusema, wachungaji wadogo wa Kikristo hawapaswi ‘kupita yale yaliyoandikwa.’ (1 Kor. 4:6) Iwe ni katika mambo yanayohusu mafundisho, adili au utaratibu wa Kikristo, mwangalizi anapaswa ‘kulihubiri neno.’ (2 Tim. 4:2) Kama angeanzisha maoni yake ya kibinafsi au kueneza mawazo yanayopingana na mafundisho yanayopokewa kupitia kwa “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” jambo hilo lingetokeza mvurugo. Mahali pa kujitanguliza kwa kunia makuu katika mwendo ambao unaweza kutokeza kuvunjiwa heshima kwa kufanya hivyo, sababu gani usimngojee Yehova na tengenezo lake? (Mit. 11:2) Pengine jambo hilo litaelezwa zaidi au kufanywa wazi zaidi baadaye. Au, kupitia kwa sala na kujifunza kwa bidii Neno la Mungu kwa msaada wa vitabu vya Sosaiti, mzee huyo anaweza kuona kwamba alikuwa amekosea naye atakuwa na furaha kwamba hakueneza maoni yenye makosa.
8. (a) Sababu gani waepuke kupigana kwa maneno na kujiingiza katika mabishano? (2 Tim. 2:14-19) (b) Mtu akiuliza ulizo naye anataka msaada wa kiroho, msaada unapaswa kutolewaje?
8 Paulo alimwambia Timotheo awaagize wengine “wasiwe na mashindano ya maneno, ambayo hayana faida, bali huwaharibu wasikiao.” Kisha mtume huyo alitaja matokeo mabaya ya misemo ya wanaume ambao walikuwa wamekengeuka na kuiacha kweli. Hakuna jambo la kufaidi ila mengi ya kiroho yanapotezwa kwa kupigana kwa maneno au kujiingiza katika mabishano pamoja na wale wanaokataa mafundisho yanayofaa. (2 Tim. 2:14-19; Tito 1:7-9) Hiyo haimaanishi kwamba mtu hawezi kutokeza ulizo kwa unyofu juu ya jambo fulani asilofahamu. Hata hivyo, kusisitiza maoni fulani kwaweza kutokeza mchafuko usiofaa. Bila shaka, watu fulani wakihitaji msaada wa kiroho, kuna njia inayofaa ya kufundisha, nayo njia hiyo ni kwa ‘uanana’ (upole).—2 Tim. 2:23-26.
9. Ili wafundishe ifaavyo, waangalizi wanatakiwa wafanye nini?
9 Waangalizi wanapaswa ‘kufanya kazi kwa bidii katika kusema na kufundisha,’ si kwa kufikia watu wa nje tu kwa ile kweli bali katika kujenga kundi kiroho. (1 Tim. 5:17, NW) Inahitaji wakati na jitihada kutayarisha hotuba za Biblia na sehemu katika mikutano ambazo ni zenye kuburudisha kiroho, zenye kuagiza na zenye kufaa maishani. Kwa kujifunza Maandiko kwa ukawaida na kwa kutumia vitabu vya Sosaiti, muhtasari wa hotuba na habari nyingine kutoka kwa “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” wasemaji na waalimu wanaweza kusitawisha mambo mengi mazuri ambayo yatawawezesha kutoa mafundisho yanayofaa. Na kwa kuwa mfano katika kusema, waangalizi wanaonyesha kwamba wanajitumikisha katika njia inayofaa.
Sikuzote Kuendeleza ‘Mwenendo Mzuri’
10, 11. (a) Ni uhusiano gani uliopo kati ya mwenendo na hekima ya kimbinguni? (b) Ni jambo gani linalotokea wakati hekima kutoka juu inapoonyeshwa tofauti na hali ambazo katika hizo tabia zisizo za kimungu zinaonekana?
10 Waangalizi wa makundi wanapaswa pia kuwa mfano mzuri “kwa mwenendo.” Ili kufaulu katika kuendeleza mwenendo mzuri, wanahitaji hekima na ufahamu wa kimbinguni. Mwanafunzi Yakobo anakazia jambo hilo, akisema hivi: “N’nani aliye na hekima na ufahamu kwenu? Na aonyeshe kazi zake kwa mwenendo wake mzuri, katika upole wa hekima. Lakini, mkiwa na wivu wenye uchungu na ugomvi mioyoni mwenu, msijisifu, wala msiseme uongo juu ya kweli. Hekima hiyo siyo ile ishukayo kutoka juu, bali ni ya dunia, ya tabia ya kibinadamu, na Shetani. Maana hapo palipo wivu na ugomvi, ndipo palipo machafuko, na kila tendo baya.”—Yak. 3:13-16; 1 Pet. 2:12.
11 Uhusiano kati ya wazee kwa wazee pamoja na washiriki wengine wa kundi unatiwa nguvu kwa mwenendo mzuri unaoonyesha hekima ya kimbinguni. (Yak. 3:17, 18) Kwa upande mwingine, ugomvi, wivu, kujisifu na matendo na tabia nyinginezo za kilimwengu, za kinyama na kishetani zinaharibu uhusiano. Tabia hizo mbaya hazina mahali pake kati ya watu wa Mungu. Kutenda kwa kujifikiria hatupatani na upendo kama wa Kristo. Kwa hiyo, mwenendo mzuri unahitaji ‘kutotenda lo lote kwa kushindana wala kwa majivuno; bali kwa unyenyekevu, kila mtu na amhesabu mwenziwe kuwa bora kuliko nafsi yake.’ (Flp. 2:3) Mwenendo kama huo ni mfano mzuri kweli kweli kwa kuwa unaonyesha nia ya akili kama ile iliyoonyeshwa na Kristo Yesu. Flp. 2:5-8.
12. (a) Washiriki wanawake wa kundi wanapaswa kuonwaje na kutendewaje? (b) Waangalizi wanatakiwa wafanye nini kwa habari ya kuvunjwa kwa kanuni za adili za Mungu? (c) Kwa habari ya mambo yanayohusu kutoa hukumu, kuweka siri kunawapa wazee daraka gani?
12 Ili kuweka mfano mzuri, waangalizi na ndugu wengine wenye madaraka sikuzote wanapaswa kujiendesha kwa uangalifu kuwaelekea wanawake. Wanapaswa kusihi “wanawake wazee kama mama; wanawake vijana kama ndugu wa kike; katika usafi wote.” (1 Tim. 5:1, 2) Kukesha kwa wakati wote kunahitajiwa ili kujihadhari usiachilie kushikamana na kanuni bora za adili za Mungu. Iwapo kuna ushuhuda wa hakika kwamba wengine wanajaribu kupotoa wengine kiadili, waangalizi wanapaswa kuchukua hatua ya haraka kuliweka tengenezo safi, wakijua kwamba Yehova ‘hulipiza kisasi cha mambo haya.’ (1 The. 4:3-8) Wakati uo huo, wachungaji wadogo waliowekwa wanapaswa kuepuka kuzungumza mbele ya wengine mambo ya hukumu yanayohusu wale waliovunja kanuni za haki za Mungu. Siri lazima ziendelee kuwekwa. Kundi laweza kutazamiwa kuwa na uhakika tu katika wazee wanaosimamia vizuri na ambao mwenendo wao wa kibinafsi sikuzote ni ule usiolaumika.
Mfano Mzuri “katika Upendo”
13. Ni roho gani inayohitajiwa iwapo waangalizi watafaulu kuweka mfano mwema, na sababu gani ndivyo?
13 Waangalizi hawawezi kufaulu kweli kweli kuwa “kielelezo kwa waaminio” wasipoonyesha roho ya upendo. Baada ya kumkumbusha Timotheo ‘achochee karama ya Mungu, iliyo ndani yake,’ Paulo alisema hivi: “Maana Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi.” (2 Tim. 1:6, 7) Twayajua matokeo yanayofaa yaliyotokezwa maishani mwetu kwa sababu ya Mungu kutuonyesha sifa hii ya upendo. Waangalizi wanapokuwa mifano mizuri katika kuonyesha tunda la roho, upendo, jambo hilo, zaidi ya jambo jingine lo lote, linaonyesha namna wanavyowaona waabudu wenzao wa Yehova. Upendo una uwezo wa kuvuta, ukitusukuma tutafute shauri na msaada wa wachungaji wadogo wenye upendo. Twathamini kupendezwa kwao kwa uchangamfu na tamaa yao nyingi ya kutusaidia tufanye maendeleo ya kiroho.
14. Waangalizi waliooa wana nafasi gani za kuonyesha kwamba ‘wanapenda wake zao kama miili yao,’ nalo hilo linawezesha wake kufanya nini?
14 Ili waendelee kama wanaume wa kiroho waangalizi hujitahidi kuacha ‘mambo yote yatendeke kwa upendo.’ (1 Kor. 16:13, 14) Iwapo wameoa, wanaume hao wanapaswa “kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe,” ambayo wanailisha na kuitunza. (Efe. 5:28, 29) Waangalizi wanathamini kadiri ile ambayo miili yao inahitaji kuangaliwa kila siku. Hivyo, pia wake zao wanahitaji kuangaliwa na uangalizi wa kawaida wa kiroho ambao utawawezesha kutimiza sehemu zao za kike za kuunga mkono katika njia ‘ipendezayo katika Bwana.’ (Kol. 3:18, 19) Kuzungumza andiko la kila siku’ kutoka Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova, kujikumbusha habari katika vitabu vya Sosaiti, kutayarisha mikutano ya Kikristo na kuangalia nafasi za kusali pamoja—yote hayo ni wonyesho wa upendo huo. Vilevile, kwa kadiri nafasi inavyoruhusu, wazee wanapaswa kusaidia wake zao katika njia nyinginezo. Jambo hilo pamoja na kulea vizuri watoto wo wote walio nao litatoa ushuhuda kwamba mwanamume huyo anasimamia vizuri nyumba yake mwenyewe na hivyo anatimiza moja la matakwa ya Kimaandiko ya kutimizwa na waangalizi.—1 Tim. 3:4, 5; 5:8.
15. Mwaangalizi anaweza kuonyeshaje kwamba anaweza ‘kulitunza kundi la Mungu’ na kwamba yeye ana upendo?
15 Hakika, mwangalizi anayeendeleza mpango mzuri wa jamaa anaonyesha kwamba anaweza ‘kulitunza kundi la Mungu.’ (1 Tim. 3:5, NW) Katika kutimiza madaraka ya kundi, mzee anapendezwa sana kibinafsi na wale walio na imani kama yake. (Gal. 6:9, 10) Waangalizi hutayarisha na kuongoza mikutano ya kundi, hutembelea wagonjwa na wengine wanaohitaji msaada, nao hushiriki kwa ukawaida katika kutangaza waziwazi “habari njema.” Yote hayo ni mfano wa kumpenda Mungu, kupenda “kondoo” walio chini ya uangalizi wao na wale ambao wazee hao wanahubiria ujumbe wa Ufalme.
16. Ni nini kilichomchochea Paulo atende kwa faida bora za kundi la Korintho, nayo nia iyo hiyo inapatikana kati ya waangalizi Wakristo leo?
16 Kuna nyakati ambazo waangalizi huliona kuwa jambo la lazima kutoa mashauri ya moja kwa moja au kuchukua tendo la kutia adabu. Tamaa yao ni kusaidia watu mmoja mmoja na kulinda kundi. Katika jambo hilo, wazee wanaiga mtume Paulo. Akichochewa na upendo, mtume huyo alitenda kwa ajili ya faida bora za kundi katika Korintho, ingawa jambo hilo lilimtia wasiwasi mwingi. Yeye aliandika hivi: “Maana katika dhiki nyingi na taabu ya moyo niliwaandikia na machozi mengi; si kwamba mhuzunishwe, bali mpate kujua upendo wangu nilio nao kwenu jinsi ulivyo mwingi.” (2 Kor. 2:4) Ingawa watu wengine katika kundi hilo hawakuthamini kabisa jitihada za Paulo zenye kuendelea na zisizo na choyo, yeye alikuwa na nia ya kujitoa hata zaidi kwa ajili yao, kwa kuwa yeye alisema hivi: “Nami kwa furaha nyingi nitatapanya, tena nitatapanywa kwa ajili ya [nafsi] zenu. Je! kadiri nizidivyo kuwapenda sana, ninapungukiwa kupendwa?” (2 Kor. 12:15) Kama vile Paulo, waangalizi wengi wanajitumikisha sana kwa moyo wote. Wanafanya hivyo kwa ajili ya kupenda ndugu zao, hivyo wakiweka mfano wenye kusifika.
17. Mifano myema ya waangalizi wengi imekuwa na matokeo gani juu ya tengenezo la watu wa Mungu, nalo jambo hilo likatoa msingi kwa maono gani ya moyoni upande wa wachungaji wadogo waaminifu?
17 Inawezekana kuonyesha waangalizi wengi ambao kwa miaka mingi wamejitumikisha kwa halisi katika kutumikia Yehova na kuangalia mahitaji ya ndugu na dada zao za kiroho. Mfano mzuri ambao umetolewa na wanaume hao umeendeleza roho ya upendo katika tengenezo lote la watu wa Mungu. Uhakika wetu umetiwa nguvu na mifano kama hiyo katika kulichunga “kundi” wakati wa siku hizi zenye kujaribu. Kwa sababu ya kuwa na upendo na kuhangaikia kikweli “kundi,” wachungaji hao wadogo wana sababu ya kusema kama alivyosema Paulo, ambaye aliandika hivi: “Bwana na awaongeze na kuwazidisha katika upendo, ninyi kwa ninyi, na kwa watu wote, kama vile sisi nasi tulivyo kwenu; apate kuifanya imara mioyo yenu iwe bila lawama katika utakatifu mbele za Mungu, Baba yetu, wakati wa kuja kwake Bwana wetu Yesu pamoja na watakatifu wake wote.”—1 The. 3:12, 13.
Kuonyesha Imani Hutia Nguvu Waamini Wenzetu
18. Waangalizi wanapaswa kuweza kuonyesha kazi gani kuwa ushuhuda kwamba wana imani ya kweli?
18 Wengi wajapodai waziwazi kuwa ni wanadini leo, “si wote walio na imani.” (2 The. 3:2) Hata hivyo, iwapo tutampendeza Mungu, ni lazima tuwe nayo. (Ebr. 11:6) Hapa, pia, waangalizi Wakristo wanapaswa kuwa mfano mzuri kwa wote—“kwa imani.” Pamoja na hayo, wanapaswa kuwa na vitendo au kazi za kuthibitisha wana imani ya kweli. (Yak. 2:14-26) Kati ya mambo mengine, kazi hizo zinatia ndani vitendo kama vile kufariji waamini wagonjwa, kuwapa wenye mahitaji kati yao na kushiriki kwa ukawaida katika kutangaza “habari njema za ufalme.”—Mt. 24:14, NW; linganisha Mathayo 25:34-40.
19. Sababu gani imani ni ya lazima, nayo inawezesha wengi kufanya nini?
19 Ni jambo lenye maana fulani kwamba Paulo kwa kurudia-rudia alikazia jambo hili kwamba ‘mwenye haki ataishi kwa Imani.’ (Kum. 1:17; Gal. 3:11; Ebr. 10:38) Si kwamba imani inatupa maono ya yaliyoko mbele tu bali pia inatuchochea tufanye mambo. Kwa mfano, inahitaji imani kujiandikisha kama painia msaidizi au wa kawaida na kisha kutumikia kama wahubiri wa wakati wote wa “habari njema.” (Marko 13:10, ZSB) Yajapokuwa madaraka ya jamaa na kazi nyingine, waangalizi wengi pamoja na watumishi wa huduma wanapanga kushiriki katika utendaji huo. Wengi wanafanya marekebisho katika kazi zao za kimwili na mambo mengine ili waangalie zaidi madaraka ya kundi. Nayo imani ya kweli inahitajiwa wakati wa kuwa na sehemu ya moja kwa moja katika kuhubiri “habari njema,” kutimiza migawo kwenye makusanyiko ya Kikristo, kujenga Majumba ya Ufalme au kushiriki katika utendaji mbalimbali wa kitheokrasi kila siku. Hakika, inahitaji imani kwa waangalizi na watu wote wa Yehova kuamini, kuishi kufanya kazi na kuabudu kulingana na Neno la Mungu.
20. (a) Imani inafanya sehemu gani katika kuchukua msimamo imara katika kumpinga Ibilisi? (b) Waangalizi wanaweza kusaidiaje sana sana waamini wenzao wapate kushinda majaribu ya imani yao?
20 Vilevile imani inahitajiwa ili kuvumilia magumu na kushinda majaribu ya imani. Baada ya Petro kusihi wanaume wazee wawe mifano kwa “kundi,” alionya hivi: “Zitunzeni akili zenu, iweni wenye kukesha. Adui yenu, Ibilisi, anatembea-tembea uku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta kunyafua mtu fulani. Bali chukueni hatua ya kumpinga yeye mkithibitika katika imani, mkijua kwamba mambo ayo hayo kwa namna ya mateso yanatimizwa katika ushirika mzima wa ndugu zenu ulimwenguni.” (1 Pet. 5:8, 9, NW) Wakati wote waangalizi wanapaswa kuwa macho kuona njia za Ibilisi na vyombo anavyotumia kukengeusha, kunasa au kunyafua (kumeza) watumishi wa Mungu. Wakristo hawapaswi kujiruhusu watiwe kwenye ubaridi kuhusu hali wanayoelekeana nayo, nao wachungaji wadogo waliowekwa wa “kundi” wanapaswa sana sana kukesha. Katika nchi nyingi mambo yaliyoonwa yanaonyesha kwamba matatizo na majaribu yanapopata Mashahidi wa Yehova, waangalizi wanakuwa mbele kabisa katika vita hiyo. Wakitegemea Mungu, wazee hao wanaendelea kusaidia waamini wenzao katika njia mbalimbali, wakimpinga Adui, wakisali sana na kutumia ngao kubwa ya imani na silaha nyingine za kiroho.—Efe. 6:10-18
21. Kwa kuwa mifano katika imani waangalizi husaidia “kundi” lifanye nini kwa habari ya imani na tumaini?
21 Waangalizi wanapaswa kusaidia “kundi” litembee kwa imani na kufurahi katika tumaini lililo mbele. Kwa sababu ya kuwa wasioweza kuonekana, hatuwezi kumwona Yehova Mungu wala Mwanawe katika makao ya kimbinguni. Hata hivyo, mambo wanayotutendea yanaonekana. (Ebr. 11:27) Yanayotokea kwa sababu ya uongozi wao yanatimiza yale ambayo Biblia ilitabiri. Waangalizi wanapaswa kusaidia sana ndugu na dada zao za kiroho wathamini jambo hilo la hakika na kuona kwamba washiriki wa “mkutano mkubwa” wanakusanywa kwa hesabu kubwa. Baraka ya Yehova i juu ya kazi inayofanywa. (Isa. 60:22, Ufu. 7:9) Tunapata usalama wa kiroho alioahidi. (Zab. 91:1, 2) Matunda ya roho takatifu ya Yehova kutia ndani imani, yamejaa sana kati ya watu wa Mungu leo. (Gal. 5:22, 23, NW; linganisha Warumi 1:8) Macho yetu ya imani yanaona kutekelezwa kunakokuja kwa hukumu za Yehova. (Ufu. 11:16-18; 16:14, 16) Baada ya ile “dhiki kubwa” taratibu mpya itaanza, nayo Dunia italetwa kwenye hali ya Paradiso. (Mt. 24:21; Luka 23:43; 2 Pet. 3:11-13) Kutakuwako ufufuo. (Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15) Jamii ya kibinadamu itarudishwa kwenye uhusiano wa amani pamoja na Mungu, nao uzima wa milele utakuwa sehemu ya wale watakaoionyesha kuwa watiifu wakati wa jaribu la mwisho. (Ufu. 20:7-10) Walakini tunapotazamia wakati ujao, twathamini makumi ya maelfu ya waangalizi ambao sasa wanatumikia kama mifano katika imani, wachungaji wadogo washikamanifu wanaofanya mengi sana ili kusaidia “kundi” lifurahi katika tumaini lililo mbele.—Rum. 12:12.
‘Kwa Usafi’—Mifano Inayostahili
22. (a) Kufikiria Wafilipi 4:8 na Yakobo 3:17 kunaweza kusaidiaje waangalizi wawe mifano myema katika usafi? (b) Katika kupendekeza ndugu wapate madaraka ndani ya kundi, waangalizi wanapaswa kujitahidi waendelee kuwa safi kwa njia gani?
22 Mwishowe, waangalizi wanasihiwa ‘wawe kielelezo kwao waaminio . . . katika usafi.’ Jambo hilo lamaanisha zaidi ya kuwa safi katika akili na mwenendo wa adili. Bila shaka, wanapaswa kuwa waangalifu kwamba yale ambayo akili zao zinafikiria ni safi. (Flp. 4:8; Yak. 3:17) Walakini, ili waendelee kuwa safi, waangalizi wanapaswa kufanya maamuzi mazuri wanapofikiria kuwapa ndugu madaraka ndani ya kundi. Sifa zao zapaswa kuchunguzwa kwa uangalifu kwa msaada wa matakwa ya Kimaandiko. Upendeleo haupaswi kuonyeshwa kamwe kwa rafiki wa mtu binafsi wala watu wa ukoo. Iwapo kuna mashaka juu ya mwenendo wa adili wa mtu, acheni wakati na mambo ya hakika yaondoe mashaka hayo. Jambo hilo litapatana na shauri zuri linalopatikana katika 1 Timotheo 5:22: “Usimwekee mtu mikono kwa haraka, wala usizishiriki dhambi za watu wengine. Ujilinde nafsi yako uwe safi.”
23. Ni jambo gani litakalosaidia waangalizi waendelee kuwa safi katika kuendesha mambo yanayohusu kutoa hukumu?
23 Vilevile, waangalizi huepuka kushiriki katika dhambi za wengine kwa kuendesha mambo ya kutoa hukumu kwa njia inayofaa. Wanaposhughulika na kesi za kufanya makosa, wazee wanapaswa kuwa wenye rehema wakati hali zinapotaka rehema ionyeshwe, lakini hawapaswi kuachilia wala kuona dhambi vivi hivi. (Mit. 28:13; Yak. 2:13; linganisha Yuda 3:15, 22, 23.) Wazee waliowekwa wanapaswa kuwa waangalifu ili wasivutwe upande na upendeleo, wala maono ya moyoni wanaposikiliza yale yanayosemwa na wakosaji au ushuhuda wa wengine. Kwa kuruhusu kanuni za Biblia ziongoze maamuzi yo yote wanayofanya katika kesi hizo, wachungaji wadogo waaminifu wataendelea kuwa safi.
24. Ni jambo gani litawezesha waangalizi waseme kama alivyosema Paulo katika 1 Wakorintho 11:1?
24 Kwa kuwa mifano katika njia zilizotangulia kutajwa, waangalizi Wakristo walio waaminifu wanaweza kusema kwa dhamiri safi kama alivyosema Paulo: “Niigeni mimi kama nami ninavyomwiga Kristo.” (1 Kor. 11:1, HNWW) Ingawa alikuwa anatambua udhaifu wake wa kibinafsi, mtume huyo angeweza kusema kwa uhakika kwamba alikuwa anamfuata Kristo. Ndivyo ilivyo kwa waangalizi leo wanaojitahidi kutenda kulingana na matakwa ya Mungu.
Kundi Latiwa Moyo Linene Neno Hilo Kwa Ujasiri
25. Kwa kuiga mfano mwema uliowekwa na waangalizi Wakristo matokeo kundini yanaweza kuwa nini kwa ajili ya baraka za Mungu?
25 Twaweza kutazamia matokeo gani kwa kufuata mfano unaotolewa na wachungaji wadogo waaminifu wa “kundi la Mungu”? Wote kundini watatiwa moyo waendelee kunena neno la Mungu kwa ujasiri huku wakiendeleza mwenendo mzuri! (Matendo 4:29-31; 1 Pet. 2:12) Tunda la upendo litatambulisha kundi pasipo shaka kuwa washiriki wake ni wanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo, nalo jambo hilo litavuta wengine washirikiane na watu wa Mungu. (Zek. 8:23; Yohana 13:34, 35) Imani yenye kutenda itaonyeshwa kwa kufanya kazi njema kama vile kuhubiri “habari njema,” kufanya wanafunzi na kufuatia njia za kimungu. (Mt. 24:14, NW; 28:19, 20) Usafi ukiwa jambo kuu maishani mwa wote wanaotafuta kibali ya Mungu, kundi lote litawekwa safi. Basi na tuendelee kumtumikia Yehova pamoja kwa uaminifu, tukithamini baraka tunazofurahia tukiwa watu wa Mungu. Na Baba yetu wa kimbingu ni mwenye upendo aendelee kubariki jitihada zetu za umoja tunapofanya kazi pamoja na waangalizi Wakristo walio mifano mizuri kwa “kundi.”
—Kutoka The Watchtower Sept. 1, 1981