Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 11/15 kur. 406-522
  • Wachungaji wa Kundi Chini ya Bwana Mmoja

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wachungaji wa Kundi Chini ya Bwana Mmoja
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UTUMISHI WENYE KUUNGANISHA
  • Kuonyesha Kupendezwa na “Kundi la Mungu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Wachungaji, Waigeni Wale Wachungaji Wakuu Zaidi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Wazee, Chukueni kwa Uzito Madaraka Yenu ya Uchungaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Ni Nani Anayestahili Kuwa Mzee?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 11/15 kur. 406-522

Wachungaji wa Kundi Chini ya Bwana Mmoja

1. “Mchungaji mwema” ni nani, naye ahusianaje na “kondoo”?

WAKATI Bwana Yesu Kristo alipokuwa duniani, alijijulisha kuwa “Mchungaji mwema.” Waliosikiliza sauti yake wakamfuata walikuwa “kondoo” zake. Alisema alitoa nafsi yake kwa ajili yao. (Yohana 10:1-15) Hivyo Kristo Yesu aliwalinganisha wafuasi wake wanaofanyiza kundi na kondoo. Katika Luka 12:32 Yesu alitaja “kundi dogo” ambao wangepewa Ufalme, na katika Yohana 10:16 Yesu alitaja “kondoo wengine” ambao wangesikiliza pia sauti yake na kuwa sehemu ya kundi moja ambalo Yesu Kristo ndiye mchungaji wao.

2. Kwa sababu gani wachungaji wadogo wapaswa kutendea kundi kama lenye thamani nyingi?

2 Waandikaji Wakristo wa Biblia walitumia baadaye maneno kama hayo walipokuwa wakisema na waangalizi Wakristo waliopewa mgawo wa kutumikia kama wachungaji chini ya Bwana Yesu Kristo. Paulo aliwaambia waangalizi wa Efeso hivi: “Jitunzeni nafsi zenu, na lile kundi lote nalo, ambalo [roho takatifu imewaweka] ninyi kuwa waangalizi ndani yake, mpate kulilisha kanisa lake Mungu, alilolinunua kwa damu yake mwenyewe.” (Matendo 20:28) Hapa Paulo alikazia uhitaji wa wachungaji hawa kutambua kwamba kundi ni mali ya Mungu na kwamba lilinunuliwa kwa damu ya Mwana wake mwenyewe, naye Mungu aiona damu hiyo kuwa yenye thamani nyingi sana. Kwa hiyo, lazima wachungaji hawa watendee kundi kama kitu chenye thamani nyingi sana sana machoni pa Mungu na Kristo, ambao kundi ni mali yao.

3. (a) Katika karne ya kwanza, kila mshiriki wa kundi alitazamiwa kufanya nini? (b) Umoja ulikuzwaje kundini?

3 Wakati Paulo alipotoa shauri hilo, washiriki wa kundi la Kikristo wenye mfano wa kondoo hawakuwa mahali pamoja wala katika mji mmoja, bali walikuwa katika makundi ya miji mingi ya Milki ya Rumi. Walikuwa mahali pengi lakini bado walikuwa kundi moja, likiwa chini ya mchungaji mmoja, Kristo Yesu, na kila mshiriki wa kundi alitazamiwa kuwa na umoja na wengine, kulingana na sala aliyotoa Yesu kabla ya kufa kwake: “Si hao tu ninaowaombea; lakini na wale watakaoniamini kwa sababu ya neno lao. Wote wawe na umoja; kama wewe, Baba, ulivyo ndani yangu, nami ndani yako; hao nao wawe ndani yetu; ili ulimwengu upate kusadiki ya kwamba wewe ndiwe uliyenituma.” (Yohana 17:20, 21) Wale waliopewa mgawo wa kutumikia makundi karne ya kwanza walipaswa kufanya kazi wakuze umoja wao kwa kuelekeza fikira za watu kwa Kichwa kilichowekwa cha kundi, Yesu Kristo, na kutia wote moyo wamwige yeye kwa kushikamana na kweli na kuonyesha upendo wa kweli. Kama ilivyoandikwa katika Waefeso 4:15, 16, NW: “Tukinena kweli, acheni kwa upendo tukue katika mambo yote ndani ya yeye aliye kichwa, Kristo. Kutoka kwake mwili wote, kwa kuunganishwa pamoja kwa mapatano na kufanywa ushirikiane kupitia kwa kila ungo linalotoa kinachohitajiwa, kulingana na kufanya kazi kwa kila kiungo kimoja kimoja kadiri ifaavyo, mwili wakua upate kujijenga wenyewe katika upendo.” Kwa hiyo, ingawa kulikuwa na namna nyingi za kazi ya kufanywa, walioifanya kazi walikuwa mwili mmoja tu wenye viungo vingi, wakiwa chini ya Kichwa kimoja, Yesu Kristo.

4. (a) Yesu alikazia nini kwa Petro? (b) Petro alikumbusha wanaume wazee nini?

4 Petro ni mmoja aliyefanya kazi ya uchungaji chini ya uongozi wa Mchungaji Mkuu, Yesu Kristo. Baada ya ufufuo wake Yesu alimkazia Petro, kama ilivyoandikwa katika Yohana 21:15-17, NW, kwamba kumpenda Kristo kwaonyeshwa kwa kulisha au kuchunga “kondoo wadogo.” Miaka mingi baadaye Petro aliandikia Wakristo wenzake ambao pia waliingia katika cheo cha wanaume wazee katika kundi la Kikristo, akisema katika 1 Petro 5:1-4 hivi: “Nawasihi wazee walio kwenu, mimi niliye mzee, mwenzi wao, na shahidi wa mateso ya Kristo, na mshirika wa utukufu utakaofunuliwa baadaye; lichungeni kundi la Mungu lililo kwenu, na kulisimamia, si kwa kulazimishwa, bali kwa hiari kama Mungu atakavyo; si kwa kutaka fedha ya aibu, bali kwa moyo. Wala si kama wajifanyao mabwana juu ya mitaa yao, bali kwa kujifanya vielelezo kwa lile kundi. Na Mchungaji mkuu atakapodhihirishwa, mtaipokea taji ya utukufu, ile isiyokauka.” Kwa njia hiyo wanaume wazee hawa, wachungaji hawa walio chini ya Kristo Yesu, walikumbushwa kwamba kundi ni mali ya Mungu, kwamba lahitaji uangalizi na kwamba yawapasa wanaume wazee walihangaikie sana.

5. (a) Ni nini maana ya uangalizi wa Kikristo? (b) Yesu alikaziaje hilo?

5 Mchungaji Mkristo ni mwangalizi, lakini maana yake si sawa na maoni ya ulimwengu juu ya mwangalizi wa wajenzi au wafanya kazi wa shamba. Katika kundi la Kikristo hakuna kupiga ubwana juu ya wale walio urithi wa Mungu. Uangalizi si kutukuza wanadamu. Petro alikuwa amejifunza hilo vizuri sana kwa Kristo Yesu miaka mingi mapema wakati wa mwadhimisho wa chakula cha mwisho cha jioni ambacho Yesu alikuwa nacho na mitume wake. Maandishi katika Luka 22:24-27 yasema: “Yakatokea mashindano kati yao, kwamba ni nani anayehesabiwa kuwa mkubwa. Akawaambia, Wafalme wa Mataifa huwatawala, na wenye mamlaka juu yao huitwa Wenye fadhili; lakini kwenu ninyi sivyo; bali aliye mkubwa kwenu na awe kama aliye mdogo; na mwenye kuongoza kama yule atumikaye. Maana aliye mkubwa ni yupi? yeye aketiye chakulani, au yule atumikaye? Siye yule aketiye chakulani? Lakini mimi kati yenu ni kama atumikaye.” Wanafunzi walifanya kosa kubishana vikali hivyo, lakini lo! Yesu alikuwa mwenye fadhili namna gani akiwasahihisha!

6, 7. (a) Yesu alikuwaje mfano bora kwa waliotazamiwa kuwa wachungaji? (b) Petro pia alikazia sifa gani? (c) Sifa hiyo inalifaidije kundi?

6 Mchungaji Mkuu alikuwa mfano bora kwa hao waliotazamiwa kuwa wachungaji. Maandishi ya Yohana juu ya chakula hicho cha jioni cha Yesu na wanafunzi wake yatoa mfano wa hilo, yakisema: “Hata chakula cha jioni kilipokuwa kikiendelea . . . [alisimama] akaweka kando mavazi yake, akatwaa kitambaa, akajifunga kiunoni. Kisha akatia maji katika bakuli, akaanza kuwatawadha wanafunzi miguu, na kuifuta kwa kile kitambaa alichojifunga.” (Yohana 13:2-5) Yesu alikuwa mwalimu mwema, kwa hiyo aliendelea kueleza sababu alisafisha miguu yao, akisema: “Je! mmeelewa na hayo niliyowatendea? Ninyi mwaniita, Mwalimu, na, Bwana; nanyi mwanena vema, maana ndivyo nilivyo. Basi ikiwa mimi, niliye Bwana na Mwalimu, nimewatawadha miguu, imewapasa vivyo kutawadhana miguu ninyi kwa ninyi. Kwa kuwa nimewapa kielelezo; ili kama mimi nilivyowatendea, nanyi mtende vivyo.”​—⁠Yohana 13:12-15.

7 Petro alivutwa sana na mfano wa Kristo Yesu na uhitaji wa mchungaji kutendea kundi kwa unyenyekevu, sikuzote akiwa tayari kuwatumikia. Kwa hiyo Petro aliandika hivi: “Si kama wajifanyao mabwana juu ya mitaa yao, bali kwa kujifanya vielelezo kwa lile kundi.” Unyenyekevu huu ni sifa ambayo Kristo Yesu alitaka kuona ndani ya wale wanaofanya kazi ya uchungaji katika kundi la Mungu. Kwa hiyo, Petro aliendelea kusema hivi: “Vivyo hivyo ninyi vijana, watiini wazee. Naam, ninyi nyote jifungeni unyenyekevu, mpate kuhudumiana; kwa sababu Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu neema. Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake.” (1 Pet. 5:5, 6) Kuna faida ya kuwa wanyenyekevu. Kunafanya iwe vyepesi kufikiwa usaidie kutatua matatizo, na roho hii yavuta kundi zima pamoja katika upendo. Kutumikia kwa upendo na unyenyekevu kwaondolea mbali tendo lo lote la kutumia nguvu bila kujali maoni ya wengine au kupiga ubwana juu ya walio urithi wa Mungu. Mchungaji wa kweli anafikiria sana kuwa mfano kwa kundi.

8. (a) Wazo kuu katika neno la Kigiriki epískopos ni nini (b) Kwa sababu gani neno hilo latumika zaidi kwa waangalizi wa Kikristo kuliko neno la Kigiriki kýrios?

8 Neno “mwangalizi,” lililotafsiriwa kutoka neno la Kigiriki epískopos, lamaanisha mtu aliye mlinzi au anayeangalia kitu fulani. Ulinzi ni wazo kuu katika neno epískopos. Kwa hiyo mwangalizi wa Kikristo ni yule anayehangaikia kundi la Mungu na anayeliangalia kama vile mchungaji angeangalia kondoo halisi. Kama mwangalizi hapaswi kupiga ubwana juu ya kundi la Mungu. Neno “bwana” limetokana na neno la Kigiriki kýrios na lamaanisha mtu mwenye uwezo na mamlaka juu ya wengine kama vile bwana wa nyumba au kichwa cha jamaa. Linatafsiriwa pia kuwa “mwenyeji.” Mwenyeji wa mtumwa yumo pia katika jamii hiyo, lakini wenyeji wa watumwa si wengi siku hizi. Walakini, matajiri au mabwana-wakubwa wangefaa katika masimulizi ya kýrios au “bwana.” Lakini wazee hawapaswi kudhani uhusiano wao na ndugu zao ni kama ule wa tajiri na mfanya kazi wake. Wazee ni wachungaji, na wachungaji huongoza kondoo kwenye malisho mema na sehemu zenye maji, na vilevile huwalinda na kujaribu kuponya vidonda au magonjwa yao. Katika kundi la Kikristo wachungaji wanatia ndugu zao moyo wafanye kazi ya Bwana kwa kuwa wafanya kazi wenzao, wakitambua kwamba sote tuna Bwana mmoja wa kimbinguni ambaye chini yake twatumikia na lazima tumtolee hesabu.

9, 10. (a) Petro alikuwaje mfano wa unyenyekevu? (b) Tofauti na dini ya uongo, ni sifa gani ya wachungaji wa kweli inayoleta umoja, na Yesu aliikaziaje?

9 Petro mwenyewe alikuwa mfano mwema wa jambo hili; hakujitukuza. Alipoandika yaliyoandikwa katika 1 Petro 5:1, akisema na wanaume wazee, alijieleza, akisema hivi: “Mimi niliye mzee, mwenzi wao.” Hiyo yatofautiana kabisa na maoni ya kidini ya ulimwengu juu ya Petro, yanayojaribu kumtukuza Petro kwenye cheo fulani kikubwa zaidi cha papa. Huo sio mfano uliowekwa na Petro.

10 Bila shaka Petro aliyakumbuka wazi-wazi maneno ya Yesu aliponena kwamba waandishi na Mafarisayo walijitukuza wenyewe kisha akasema, kama ilivyoandikwa katika Mathayo 23:8-12: “Bali ninyi msiitwe Rabi, maana mwalimu wenu ni mmoja, nanyi nyote ni ndugu. . . . Wala msiitwe viongozi; maana kiongozi wenu ni mmoja, naye ndiye Kristo. Naye aliye mkubwa wenu atakuwa mtumishi wenu. Na ye yote atakayejikweza, atadhiliwa; na ye yote atakayejidhili, atakwezwa.” Unyenyekevu wa Kikristo upande wa wachungaji wanaotumikia chini ya Kristo Yesu husaidia kuleta umoja wa kundi na kuleta baraka ya Yehova.

11. Paulo na Barnaba waliwekea waangalizi leo mfano gani mwema?

11 Wakati mmoja, Paulo na Barnaba kama waangalizi wenye kusafiri walikabiliwa na tatizo la wanaume fulani wenye kufundisha kwamba kutahiriwa ni kwa lazima ili mtu apate wokovu. Matendo 15:2 yaonyesha kwamba Paulo na Barnaba hawakukubaliana na fundisho hilo bali walilibishia. Hata hivyo, ili kuwe na umoja wa tengenezo zima, walipeleka ulizo hilo kwa baraza inayoongoza ya mitume na wazee Yerusalemu. Shauri hilo lilipofikiriwa sana kisha baraza inayoongoza ikafikia uamuzi, waangalizi wa huko wenye kusafiri, kama Paulo, walikubali uamuzi huo kwa moyo wakayapelekea makundi mafundisho ya maana ya kiroho. Matendo 16:4, 5 yasema: “Basi walipokuwa wakipita kati ya miji ile, wakawapa zile amri zilizoamriwa na mitume na wazee walioko Yerusalemu, ili wazishike. Makanisa yakatiwa nguvu katika ile Imani, hesabu yao ikaongezeka kila siku.” Hiyo iliongeza umoja na mapatano ya mawazo kati ya wote kundini na kwa wazi ilimpendeza Yehova, kwa maana Yehova aliyafanikisha makundi akayaongeza. Kwa kuheshimu mpango wenye kuongoza wa kundi la Kikristo, Paulo na Barnaba waliweka mfano mwema kwa waangalizi leo.

12. (a) Sikuzote Paulo alimpa nani utukufu? (b) Paulo alitendeaje waangalizi kundini?

12 Ingawa Paulo alishiriki kuieneza kweli na kuona mpanuko wa kazi, kwa kuweka mfano mwema alimpa Yehova utukufu, bila kutaka watu wamsifu yeye mwenyewe na watumishi wengine wa Mungu kwa kusema: “Apandaye si kitu, wala atiaye maji, bali Mungu akuzaye.” (1 Kor. 3:7) Barua hii kwa Wakorintho yaonyesha wazi pia kwamba kulikuwa na uhitaji wa kukumbusha waangalizi wa kundi la Korintho matakwa fulani ya sheria ya Mungu ambayo hawakuwa wakifikiliza. Sura ya 5 yaonyesha kwamba uasherati ulitajwa kundini lakini hakuna hatua iliyokuwa imechukuliwa. Maandishi hayasemi kwamba Paulo alitaka kuona waangalizi wote wa huko wakiondolewa katika migawo yao kundini kwa sababu ya ukosefu wao. Bali, Paulo aliwaagiza wasishirikiane na mtu ye yote aliyejidai kuwa ndugu aliyekuwa mvunja sheria ya Mungu na wamwondoe mwovu huyo kati yao wenyewe. Paulo aliwasubiri, akawapa nafasi ya kufanya maendeleo ya uchungaji wao na kujisahihisha. Walakini, hiyo haimaanishi kwamba mwangalizi au mtumishi wa huduma hatapoteza kamwe pendeleo la utumishi. Akiwa asiyeaminika kwa wazi na kuwa na lawama, ataondolewa.

UTUMISHI WENYE KUUNGANISHA

13. Mwangalizi apaswa kuonaje daraka?

13 Mwangalizi ana daraka zito. Lakini ni daraka lenye furaha​—⁠pendeleo kubwa! Kuliona hivyo kwasaidia kufanya furushi hilo liwe jepesi. Kumbuka, “Mchungaji mwema” atuambia hivi: “Nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mt. 11:30) Ndivyo Yesu alivyoliona. Yawapasa wachungaji wadogo wake, waliofungwa nira moja na Yesu katika kufanya mapenzi ya Mungu kulingana na mfano wake, walione ivyo hivyo. Mengi yategemea kuweka ‘mambo ya kwanza kwanza.’​—⁠Mt. 6:33.

14. Kazi kubwa ya Yesu ilikuwa nini, naye alizoeza wanafunzi wake jambo gani?

14 Acheni tuchunguze zaidi mfano wa Yesu. Kazi yake kubwa duniani ilikuwa nini? Wakati Yohana Mbatizaji alipokamatwa akafungwa gerezani, Yesu aliingia Galilaya akaanza utumishi wake huko. “Tokea wakati huo Yesu alianza kuhubiri, na kusema, Tubuni; kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia.” (Mt. 4:17) Kazi kuu ya Yesu ilikuwa kuuhubiri Ufalme. Na, sana sana, hiyo ndiyo kazi aliyozoeza wanafunzi wake. (Luka 8:1; 9:1, 2; 10:1, 8, 9) Kuelekea mwisho wa utumishi wake duniani alimwambia Pilato hivi: “Mimi nimezaliwa kwa ajili ya haya, na kwa ajili ya haya mimi nalikuja ulimwenguni, ili niishuhudie kweli.” (Yohana 18:37) Je! wachungaji wadogo, waliofungwa nira moja na Yesu, hawapaswi nao kufanya hivyo?

15, 16. (a) Yawapasa wote wafahamu matatizo gani ya waangalizi? (b) Kwaweza kuwa na baraka gani waangalizi wakisawazisha madaraka ya kuhubiri injili, kuchunga na kufundisha?

15 Walakini, waangalizi wengi huwa na tatizo la kufanya hivyo, na hiyo yaeleweka. Wanatumia wakati mwingi sana wakiangalia madaraka ya jamaa na kufanya ziara za uchungaji hata inakuwa vigumu kupata nafasi za kuongoza kwa juhudi katika utendaji wa nyumba kwa nyumba na pande nyingine za shamba. Hata hivyo, je! hawawezi kusawazisha kuhubiri injili, uchungaji na kufundisha? (Efe. 4:11) Angalia kazi nyingine zinazoweza kutiwa ndani mwangalizi anapopanga ashiriki kwa kawaida kuhubiri injili na kikundi cha utumishi. Mara nyingi, mwangalizi ataweza kupanga kwenda na jamaa yake mwenyewe katika utumishi huu, akiwapa mazoezi yafaayo pamoja na wengine katika kikundi. Kuna furaha nyingi inayopatikana jamaa ikishiriki kwa kawaida katika utumishi ikiwa pamoja, na hii yaweza kuwekea wengine mfano wa kupata furaha.

16 Namna gani juu ya ziara za uchungaji? Anaporudi kutoka katika utumishi, mwangalizi aweza kufanya iwe kawaida kutembelea mtu fulani au jamaa fulani, na bila shaka akiwasimulia mambo aliyoona wakati uo huo shambani atawasisimua. Wengine wamefanya ziara fupi pia wanaporudi nyumbani kutoka kazi ya kimwili. Ziara zikipangwa vizuri hazitachukua wakati mwingi mno wa kuhubiri injili. Waangalizi leo wanaweza kujieleza wenyewe sawa na mtume Paulo: “Maana, ijapokuwa naihubiri Injili, sina la kujisifia; maana nimewekewa sharti; tena ole wangu nisipoihubiri Injili!” (1 Kor. 9:16) Inaburudisha namna gani Mkristo akiendelea kuwa mwenye bidii kuzitangaza habari njema, na lo! kundi huthaminije mfano mwema huo kwa upande wa mwangalizi!

17. Yesu alifanyaje utumishi wake?

17 Wote wanaotumikia kama ‘wahubiri wa injili, wachungaji na waalimu’ wanaweza kujifunza mengi kutokana na njia ya Yesu ya kufanya utumishi wake. Aliutangaza Ufalme ko kote alikoweza kupata watu. Leo twafanya hivyo hasa mlango kwa mlango. Lakini angalia vile Yesu alivyounganisha kuhubiri kwake hadharani na kufundisha wanafunzi wake faraghani. Wakati mmoja Yesu alipanda mashua akasema na makutano makubwa ya watu waliokusanyika pwani. “Akawaambia mambo mengi kwa mifano.” Baada ya kusimulia mfano wa mpanzi, wanafunzi wake walimwuliza sababu yake ya kusema kwa mifano. Kwa hiyo, kwa faragha, aliwajibu ulizo lao. Kisha aliyaambia “makutano kwa mifano” mambo mengine mengi. Baadaye, ‘alipoingia nyumbani,’ wanafunzi walimjia tena naye akawasaidia ‘kuelewa’ fundisho lake.​—⁠Mt. 13:1-3, 10, 11, 34-36, 51.

18. Kwaweza kuwa na faida gani waangalizi wakifanya utumishi wa shambani?

18 Kwa hiyo, Yesu alifanya utumishi wake shambani. Waangalizi wengi leo wamepaswa waweze kufuata kielelezo kama hicho. Wanapofanya kazi na kikundi katika utumishi wa shambani, wanaweza kwenda na watu mbalimbali wanapozungumza na watu milangoni. Hiyo yaweza sana kutia kikundi moyo. Wanapofanya kazi na watu mbalimbali wanaweza kutaka kueleza sababu na njia za kutatua hali wanazopaswa kutatua milangoni, na kuwaonyesha jinsi ya kushinda matatizo ya mahali. Huenda kukawa na nafasi za kuzungumza maulizo ambayo watu mmoja mmoja waweza kuwa nayo, hasa wanapomaliza utumishi wao. Hivyo, wanapokuza shauku ya kikundi ya kufanya kazi ya kuhubiri injili, waangalizi wanaweza kufanya wakati uo huo kazi ya kuchunga na kufundisha.

19. Ni mfano gani bora zaidi alioweka Yesu kama “Mchungaji mwema”?

19 Katika Yohana 10:3, 4, twasoma kuhusu “Mchungaji mwema” hivi: “Huwaita kondoo wake kwa majina yao, na kuwapeleka nje. . . . Huwatangulia; na wale kondoo humfuata, kwa maana waijua sauti yake.” Vivyo hivyo, wachungaji wadogo leo wanaweza kutia moyo kwa njia yenye kufaidi sana wanapopeleka kundi nje katika utumishi wa Ufalme, wakifikiria kwa upendo mahitaji yao mmoja mmoja katika kikundi cha utumishi na kutaka kwa fadhili kujenga kila mmoja ili wote waendeleze uwezo wao wa kuzihubiri na kuzifundisha habari njema. Yesu mwenyewe ndiye aliyeweka mfano bora zaidi wa kutumikia kundi hivyo.​—⁠Zab. 40:9.

20. (a) Kwa sababu gani kundi halipaswi kulaumu waangalizi? (b) Washiriki wa kundi wanawezaje kuunga mkono kwa uthabiti kazi ngumu za upendo za waangalizi?

20 Pindi kwa pindi, huenda matatizo yakamaliza wakati mwingi wa waangalizi, nayo ni matatizo yasiyopaswa kuachiliwa. Mtu ye yote asilaumu waangalizi ikiwa nyakati nyingine matatizo hayo yanawazuia wasiongoze wengine katika utumishi wa Ufalme. Kundi lote lathamini kazi ngumu zao za upendo. Wanathamini kwamba waangalizi wanajaribu kusawazisha sana kazi ya kuhubiri injili, kuchunga na kufundisha. Hali ziruhusupo, wanafurahi sana wakati waangalizi wanapokuwa nao sikuzote katika kazi ya kuhubiri injili. Mara nyingi, watumishi wa huduma na wengine kundini wanaweza kufanya furushi la waangalizi liwe jepesi kwa kuangalia kazi zile ndogo ndogo au madaraka mengine yasiyohitaji sana kuangaliwa na mwangalizi. Watumishi wa huduma na wasaidizi wengine wanaotumikia kwa uthabiti pamoja na waangalizi, na wanaosaidia ko kote iwezekanako, ni baraka kuu kundini.​—⁠Zab. 149:1.

21. Kutakuwa na matokeo gani ya ‘kunena kweli’?

21 Waangalizi, watumishi wa huduma na wengine wote kundini waunganapo katika “kuinena kweli” kwa juhudi katika utumishi wa Ufalme na wao kwa wao, na kundi zima lishirikianapo katika kila jambo kwa kusudi la kuendeleza kazi ya kuuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi, wote kweli ‘watakua kwa upendo katika mambo yote ndani ya yeye aliye kichwa, Kristo.’​—⁠Efe. 4:15, NW.​—⁠Kutoka The Watchtower, July 1, 1976.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki