Kuonyesha Kupendezwa na “Kundi la Mungu”
“Jiangalieni ninyi wenyewe na kundi lote, ambalo miongoni mwake roho takatifu imeweka ninyi kuwa waangalizi, kuchunga kundi la Mungu, ambalo yeye alinunua kwa damu ya Mwana wake mwenyewe.”—Matendo 20:28, NW.
1. Yesu Kristo alionyeshaje kupendezwa sana na wale aliofananisha na kondoo?
HAKUNA mtu ye yote duniani ambaye amepata kuonyesha kupendezwa kwingi na washiriki wa jamaa ya kibinadamu kuliko alivyofanya Yesu Kristo, aliye Kiolezo Kikuu. Aliwataja wale waliosikiliza sauti yake kama “kondoo.” Naye, akiwa ndiye Mchungaji Mwema, alitoa nafsi yake au uhai wake kwa ajili yao. (Yohana 10:11, 27) Baada ya kufufuliwa kwake kutoka kwa wafu, Yesu alikazia kwa mtume wake Simoni Petro uhitaji wa kuangalia kipekee “kondoo” hao. Yesu alifanyaje jambo hilo? Alilifanya katika njia ambayo ilimchochea Petro katika sehemu nyingine yote ya maisha yake ya kidunia.
2. (a) Kulingana na Yohana 21:15-17, Petro aliitikiaje maulizo aliyoulizwa na Bwana yake? (b) Ni jambo gani Yesu alikazia jambo gani katika habari hiyo? Namna gani?
2 Mara tatu Yesu alimwuliza Petro ulizo lile lile. Mara mbili, yeye aliuliza hivi: ‘Simoni, wanipenda?’ Mwishowe, Yesu aliuliza hivi: “Simoni wa Yohana, wanipenda?” Baada ya kuulizwa ulizo lile lile mara ya tatu, Petro alihuzunika na kwa kukazia akamhakikishia hivi Bwana yake: “Wajua yote: wewe umetambua ya kuwa nakupenda.” Ndiyo, Yesu alitambua kabisa kwamba Petro alikuwa anampenda na kumwonea shauku. Walakini jambo kubwa hapo lilikuwa kwamba mtume huyo angepaswa kuthibitisha jambo hilo kwa kipindi kirefu cha wakati. Namna gani hivyo? Kwa kuonyesha kupendezwa na “kondoo.” Mara zote hizo, baada ya Petro kujibu ndiyo ulilo hilo. Yesu alikazia jambo hilo, kwa kusema hivi: (1) “Lisha wana-kondoo wangu”; (2) “Chunga kondoo zangu”; (3) “Lisha kondoo zangu.” (Yohana 21:15-17) Kwa njia hiyo, Yesu alikazia kwa matokeo zaidi si kupendezwa kwake tu na “kondoo” bali pia daraka kubwa la wakati ujao la Petro la kuwaangalia, kama vile tu Bwana yake alivyokuwa ametaja kwa kukazia.
3. (a) Petro alithibitishaje upendo wake kwa “mchungaji mwema”? (b) Ni jambo gani linaloonyesha kwamba Petro hakuwa peke yake katika kuonyesha kupendezwa na “kundi”? “kundi”?
3 Hilo lilikuwa jambo asiloweza kusahau Petro. Bila shaka, Yesu alikuwa amefikia ndani ndani katika moyo wa mtume huyo. Ili kuthibitisha upendo wake kwa Mchungaji huyo Mwema, Yesu Kristo, Petro hangepuza wakati wo wote kulisha “kondoo” hao. Kwa upendo na kwa unyofu angejitahidi kuchunga “kundi.” Kama miaka 30 baadaye, Petro aliandikia “wakaaji wa muda waliotawanyika hapa na pale,” yaani, wale waliokuwa wamekuwa wanafunzi wa Yesu Kristo. Wakiwa sehemu ya “kundi la Mungu” walikumbushwa juu ya kuokolewa na mwendo wao wa kwanza usiokuwa na matunda. Jambo hilo lilikuwa limetimizwaje? Si kwa kununuliwa kwa vitu vya kawaida kama vile fedha au dhahabu, bali “kwa damu yenye thamani, kama ile ya mwana-kondoo asiye na kasoro na madoa, ndiyo ya Kristo.” (1 Pet. 1:1, 18, 19, NW) Petro alithamini kwamba hiyo ilikuwa bei kubwa ya kulipa. Ilikuwa imemgharimu Yehova Mungu dhabihu ya Mwanawe-pekee, ambaye alimtuma hapa duniani atoe ukombozi kwa wengi. (Mt. 20:28; Yohana 3:16) Kufikia wakati Petro alipoandika barua yake ya kwanza, washiriki walionunuliwa wa “kundi” hilo walikuwa wamefika maelfu mengi. Kwa hiyo wakati huo kulikuwako “kondoo” wengi kuliko ambavyo Petro angeweza kuangalia akiwa peke yake. Hata hivyo, pamoja na Petro, wanaume wengine wenye kustahili walikuwa wametokezwa ambao walionyesha kupendezwa na “kundi” hilo lililokuwa mali ya Yehova. Na katika siku zetu jambo hilo limeonekana kabisa na makumi ya maelfu ya wachungaji wadogo ambao wamepewa daraka la kulichunga “kundi la Mungu” lililo chini ya uangalizi wao.
4. Petro alitoa shauri gani linalofaa kuhusu uchungaji wakati alipokuwa akiandikia wanaume wazee katika kundi la Kikristo?
4 Petro alipoongozwa na Mungu aandike barua yake ya kwanza, bila shaka aliweza kukumbuka jambo lile ambalo Yesu alikuwa amekazia akilini na moyoni mwake kwa habari ya kuchunga “kondoo.” Jambo hilo linaonekana wazi katika maneno ya mtume huyo ya kusihi yaliyoelekezwa si kwa wale wachungaji wadogo wa karne ya kwanza peke yao bali pia kwa wanaume wazee kiroho kati ya watu wa Mungu leo. Petro aliandika hivi: “Kwa hiyo, mimi nawatia moyo wanaume wazee miongoni mwenu hivi, kwa maana mimi pia ni mwanamume mzee pamoja na wao na shahidi wa mateso ya Kristo, mshiriki hata wa utukufu utakaofunuliwa: Lichungeni kundi la Mungu lililo katika uangalizi wenu, si kwa kulazimishwa, bali kwa moyo wa kupenda; wala si kwa kupenda mapato ya udanganyifu, bali kwa bidii; wala si kupiga ubwana juu ya wale ambao ni urithi wa Mungu, hali kuwa mifano kwa kundi. Na wakati aliye mchungaji mkuu atakapofunuliwa, ninyi mtaipokea taji ya utukufu isiyonyauka.”—1 Pet. 5:1-4, NW.
Kuliangalia kwa Upendo “Kundi la Mungu”
5. (a) Ili apate matokeo, mwangalizi Mkristo anapaswa kuwa na nia gani ili atimize daraka lake linalohusu “kundi”? (b) Sababu gani mwangalizi leo anaweza kuyaona mambo kama vile Petro alivyoyaona?
5 Akiwa shahidi aliyeona mateso ya Kristo, Petro alichochewa akazie maana ya kuonyesha kupendezwa na “kundi la Mungu.” Kama vile tu Mchungaji Mkuu, Yesu Kristo, alivyoonyesha kupendezwa huko, ndivyo inavyopaswa kuwa kwa habari ya wale wote wanaolichunga “kundi” hilo. Walakini mwangalizi Mkristo hawezi kufanya jambo hilo iwapo anaona kwamba anatumikia kwa kulazimishwa. Hakuna mzee ye yote leo aliyewekwa anayepaswa kuona kwamba anapaswa kutumikia kwa ajili ya kukazwa. Ingawa kuna kazi nyingi katika kuchukua daraka hilo lenye pendeleo, mchungaji mdogo mwenye upendo ataonyesha tamaa ya kusaidia na kuwa mwenye kutumikia. Walakini ataionyesha roho hiyo iwapo tu ana nia ile ile ya akili kama ile aliyokuwa nayo Kristo Yesu, ambaye alionyesha unyenyekevu na nia ya kuvumilia mateso. (Flp. 2:5-8; 1 Pet. 4:1) Iwapo mzee anajiona kuwa sehemu ya “kundi” hilo lililo chini ya uangalizi wa Mchungaji Mkuu, Yehova Mungu, kuwa atatoa hesabu Kwake na kwa Mchungaji Mwema, Yesu Kristo, wala si kwa mwanadamu fulani, ndipo atakapotumikia kwa kutaka sana, pasipo kunung’unika. (1 Pet. 2:25) Ingawa wao hawajakuwa mashahidi walioona mateso ya Yesu kama vile Petro, waangalizi leo wamependelewa kwa kuwa na masimulizi marefu ya Biblia ya maisha ya Kristo na huduma yake. Kwa hiyo wanaweza kuyaona mambo kama alivyoyaona Petro na hivyo wawe na roho ile ile kama ya mtume huyo wanapolichunga “kundi” hilo.
6. Waangalizi wanapaswa kukumbuka jambo gani wanaposhughulika na “kundi”?
6 Ili awe mfano unaofaa, mchungaji mdogo wa Kikristo hapaswi kuvutiwa apate mapato ya udanganyifu wala mapato ya kichoyo, au kupata umashuhuri asiostahili. ‘Ukubwa’ wo wote uliopo unakuja kwa kujitoa atumiwe na ndugu zake, awe mwenye kuambilika, akitumikia faida zao za kiroho. Wakijua kwamba “kundi” hilo ni mali ya Yehova, ambaye alilinunua kwa damu ya Mwanawe, wanaume wazee walio mfano mzuri ‘hawapigi ubwana juu ya wale ambao ni urithi wa Mungu.’ Mahali pake, wachungaji hao wadogo hulitendea “kundi” kwa upole na kwa kulilinda, hivyo wakifuata shauri na kiolezo kilichotolewa na Mchungaji huyo Mwema.—Mt. 20:25-27; Tito 1:7; tofautisha Ezekieli 34:2-4; Yuda 16.
7. Waangalizi wengi wanaonyesha kupendezwa kweli kweli na “kundi” katika njia zipi?
7 Lazima ikubaliwe kwamba waangalizi wengi walio Wakristo leo wanaonyesha kupendezwa na “kundi” katika njia mbali-mbali. Wakati na jitihada inayotumiwa katika kulisha “kondoo” hao, kwa kuwaangalia kibinafsi watu mmoja mmoja, na katika kusimamia mikutano ya kundi inatoa mifano mizuri kwa waamini wenzao. (1 Tim. 5:17) Fikiria, vilevile, uongozi mzuri ambao wachungaji wadogo waaminifu wanatoa katika utendaji wa shambani,wakitafuta watu wengine wenye mfano wa kondoo na kufanya wanafunzi (Mt. 28:19, 20; 2 Tim. 4:5) Na namna gani juu ya kupendezwa kunakoonyeshwa katika kulilinda “kundi” hilo na mambo ya kilimwengu na wale wanaowinda “kundi” hilo? (Efe. 4:11-14; Kol. 2:8; Yuda 22, 23) Katika njia hizo na katika njia nyinginezo nyingi “kundi la Mungu” linapata faida kutokana na wale wanaowachunga wakiongozwa na upendo wenye kuhangaikia hali njema yao ya kiroho.
Masomo Yenye Thamani Kwetu Leo
8. Ili atoe kitiamoyo cha kiroho, mtume Paulo alitayarisha jambo gani kwa ajili ya wanaume wazee kutoka Efeso?
8 Kwa kusoma masimulizi ya Kibiblia ya yale ambayo waangalizi wa karne ya kwanza walitimiza kwa ajili ya “kundi” hilo, tunavutiwa na mfano mwema wa mtume Paulo. Vilevile alitoa kitia-moyo kwa wanaume wazee, kama vile Petro alivyofanya. Alipokuwa akienda Yerusalemu, Paulo aliitisha mkutano wa wanaume wazee kutoka Efeso. Bila shaka walithamini sana nafasi ya kutumia wakati fulani pamoja na Paulo, kama vile tu waangalizi leo wanavyokutana vipindi fulani kubadilishana mambo yaliyoonwa yenye kusaidia, wapate kujengana katika imani na kupata mashauri ya Kimaandiko.
9. Masimulizi katika Matendo 20:18-21 yanaonyeshaje kwamba Paulo alikuwa mwanamume mwenye kujinyima wa Mungu?
9 Twaweza kujifunza masomo yenye thamani katika mazungumzo ya Paulo pamoja na waangalizi hao waliotoka Efeso. Maandishi katika Matendo 20:17-38 yanatupa ufahamu wa ndani kuhusu namna ya mfano ambao mtume huyo alikuwa amewekea ndugu zake, kutia ndani wanaume hao wazee waliotoka Efeso. Je! Paulo alikuwa mhudumu asiyejitumikisha ambaye alifurahia kusafiri huku na huku katika sehemu mbalimbali za wilaya ya Asia? Sivyo kabisa. Yeye alikuwa mwanamume mwenye kujinyima wa Mungu ambaye alikuwa ‘anamtumikia Bwana kwa unyenyekevu wote, na kwa machozi na majaribu’ wakati wote alipokuwa huko. (Matendo 20:18, 19) Hakujiepusha ‘kufundisha . . . waziwazi na nyumba kwa nyumba,’ naye akafanya hivyo katika hatari zote. Wala yeye hakuogopa namna wakaaji wengine wa ujamii huo walivyomdhania kuwa, wala vitisho vya wapinzani Paulo alitoa ushuhuda mkamilifu katika eneo hilo.—Matendo 20:20-21, NW; linganisha Matendo 19:1–20:1; 2 Wakorintho 1:8-11.
Kuchunga katika Nyakati za Mateso
10. Waangalizi wengi wa kisasa wamemwigaje Paulo katika jitihada zao za kusaidia “kundi” wajapoteseka binafsi?
10 Sasa mtume huyo alikuwa akielekea Yerusalemu, bila kuogopeshwa na taraja la kwamba “vifungo na dhiki” vilikuwa vinamngoja huko. Alikuwa tayari kutoa maisha yake, ikiwa lazima, ili amalize mwendo wake kwa uaminifu na kutimiza huduma aliyopewa na Bwana Yesu. (Matendo 20:22-24.) Huo ulikuwa mfano mwema kama nini kwa waangalizi hao Waefeso! Paulo hakupendezwa tu na wale waliohitaji kusikia “habari njema” bali pia alipendezwa na watu mmoja mmoja waliokuwa wanachukua daraka la kueneza ujumbe huo kwa wengine. Je! Huko si ndiko kupendezwa ambako wazee wote Wakristo waliowekwa wanapaswa kuwa nako leo? Ni jambo la furaha kwamba tuna wanaume ambao wanamwiga Paulo kwa kuwa wana nia ya kuhatirisha maisha zao wenyewe kwa ajili ya “habari njema”na kulinda ndugu zao. Hakika katika nchi ambazo Wakristo wanapatwa na mateso makali, wachungaji wengi wadogo walio waaminifu wameendelea kuwa pamoja na “kundi” hilo kwa ushikamanifu, hata ingawa njia ilijitokeza kwa wanaume hao wenye madaraka wanende kwenye nchi ambazo mateso hayo yangeweza kuepukwa bila shaka. Kuonyesha jambo hilo kwa mfano: Hivi karibuni mzee mmoja ambaye tayari amekwisha kufungwa miaka mingi na kupigwa vibaya sana alitembelea Amerika apate mazoezi wanayopewa waangalizi wa Sosaiti. Nafasi ilikuwapo kwake apate kwenda nchi moja isiyokuwa na mateso yo yote kwa sasa. Walakini alichagua kurudi katika nchi ambayo alikuwa anatumikia hata ingawa kufungwa na mateso makali yalionekana kuwa ni lazima ayapate huko. Kama vile wachungaji wengi wadogo wa Kikristo, anaona kuwa kulitunza “kundi” ni pendeleo lenye thamani zaidi kuliko uhuru wake wa kibinafsi. Kweli kweli, waangalizi kama hao wanapaswa kusifiwa. Ni jambo jema kama nini kwamba waendelee kutoa uangalizi kwa ‘kondoo walio taabani’!—Linganisha Isaya 32:1, 2.
11. (a) Kwa sababu ya Matendo 20:25-27, msimamo wa Paulo kuhusiana na hatia ya damu ulikuwa nini, nao waangalizi leo wanaweza kuendelezaje msimamo kama huo? (b) Kwa wazi, maoni ya waangalizi ni nini juu ya watu ambao waliwasaidia kwa mara ya kwanza wawe wanafunzi?
11 Paulo alikuwa ameenda ‘akihubiri ufalme’ kati ya wale ambao sasa walikuwa waangalizi katika Efeso. Wao wenyewe walikuwa wamesikia ujumbe huo toka kinywani mwake. Alikuwa amewaambia wao na wengine wote yaliyokuwa katika moyo wake katika kutangaza “habari ya kusudi lote la Mungu,” wala si mawazo yake. Kwa hiyo dhamiri yake ilikuwa safi. Hangeweza kutozwa hesabu ya kuwa na hatia ya damu kwa ajili ya kushindwa kutoa ushuhuda. (Matendo 20:25-27) Ndivyo inavyopaswa kuwa kwa waangalizi katika wakati huu wa jaribu, wenye magumu na shida katika kumaliza kazi ya kutoa ushuhuda, wenye kuenea wa Ufalme. Leo waangalizi wanajua kwamba mambo mengi yanategemea mfano wao wa bidii katika kuongoza katika kazi hiyo. Kwa sababu hiyo, wanajitahidi kuwa na sehemu kubwa ya kushiriki kwa kadiri inavyowezekana katika kutangaza “habari njema.” Kwa hiyo wao, pia, wanajiepusha na hatia yo yote ya damu. Wengine katika kundi wanaona kwamba wazee hao wanaongoza katika kuwaonya waovu na kutafuta wenye mioyo minyofu. Vivyo hivyo, waamini wenzao wanatiwa moyo wafuate mfano wao mwema. Kama vile kwa habari ya wale ambao Paulo alisaidia, wengi leo walio washiriki wa “kundi” hilo ni watu ambao kwa mara ya kwanza walifikiwa na waangalizi ambao walikuwa wakitoa ushuhuda katika eneo lao. Sasa kwa kuwa watu hao wamo kundini, waangalizi hao huwaonyesha kupendezwa kwingi hata zaidi.—1 The. 1:5, 6; 2:7, 8.
12. Tueleweje usemi wa Paulo katika Matendo 20:28?
12 Kupendezwa kwingi kwa Paulo na wanaume hao wazee waliotoka Efeso, pamoja na “kundi” lililokuwa chini ya uangalizi wao, kunaonyeshwa na maneno yake: “Jiangalieni ninyi wenyewe na kundi lote, ambalo miongoni mwake roho takatifu imeweka ninyi kuwa waangalizi, kuchunga kundi la Mungu, ambalo yeye alinunua kwa damu ya Mwana wake mwenyewe.” (Matendo 20:28, NW) Hakika kila mmoja wa wanaume hao aliona uhitaji wa kujichunguza mwenyewe kwa sababu ya daraka zito lililohusika katika kulichunga “kundi” hilo. Vilevile, waangalizi hao walihitaji kutumia shauri la Paulo kwao wenyewe kama baraza ya wanaume wazee. Walipaswa kushirikiana na kufanya kazi pamoja katika kulitunza “kundi” hilo. Ili matokeo yapate kuwa bora kabisa, kulipaswa kuwepo umoja wa kuwaza na wa kutenda upande wao. Jambo hilo lenyewe lingeonyesha kwamba walikuwa wanapendezwa sana na “kundi” hilo.
13. Ni jambo gani linaloweza kusemwa juu ya matumizi ya Matendo 20:28 leo?
13 Inafaa kama nini kutumia shauri la Paulo kwa ajili ya faida ya wanaume wazee Wakristo leo! Mara nyingi, kama vile wakati waangalizi wanaposafiri wanapokutana na wazee wa kundi, maneno hayo yaliyoandikwa katika Matendo 20:28 yametumika kama msingi wa shauri linalofaa. Na iangaliwe kwamba yanayosemwa hapo hayamaanishi kujiangalia mwenyewe tu. Mahali pake, baraza yote ya wazee katika kila kundi ina daraka la kuangalia mahitaji ya “kundi.” Ndivyo ilivyo hata ingawa kila mzee anaweza kuwa na mgawo fulani ambao unashiriki sehemu katika kutimiza kusudi hilo moja kubwa. Waangalizi wanapaswa kutimiza madaraka yao ya kuchunga kwa uaminifu kwa kuhangaika kwa upendo, wakitambua kwamba “kundi” hilo ni lenye thamani kwa Yehova kwa sababu ya bei iliyolipwa ili lipate kununuliwa.—Efe 1:7.
Kulinda na “Mbwa-mwitu” Makafiri
14. (a) Ni onyo gani linalopatikana katika Matendo 20:29, 30? (b) Sababu gani ulikuwa wakati wenye kufaa kwa Paulo kuwaonya waangalizi Waefeso?
14 Akijua ambayo yangetokea baada ya kifo chake na cha wale mitume wengine; Paulo alitoa onyo hili: “Najua mimi ya kuwa baada ya kuondoka kwangu mbwa-mwitu wakali wataingia kwenu, wasilihurumie kundi; tena katika ninyi wenyewe watainuka watu wakisema mapotovu, wawavute hao wanafunzi wawaandamie wao.” (Matendo 20:29, 30) Baadaye mtume Petro alionya kwamba kungekuwako watu wenye kutumia nafasi ambazo zingekuwako wakati huo na wenye kuendeleza madhehebu wakiwaharibu wasiojihadhari, wasiofundishwa na wasio imara. (2 Pet. 2:1-3; 3:15, 16) Maadamu mitume walikuwapo, walikuwa kama kizuizi cha maelekeo hayo. Walakini kwa wazi Maandiko yalitabiri ukafiri mkubwa, na kutokea, ulitokea. Ungali unaendelea ukiwa ndiyo Jumuiya ya Wakristo.—2 The. 2:6-10.
15. (a) Sababu gani wale wanaolichunga “kundi” wakati huu wanapaswa kuwa macho? (b) Nyakati nyingine, sababu gani inakuwa lazima wazee wachukue hatua kulingana na uongozi unaotolewa katika Warumi 16:17-19?
15 Katika huu “wakati wa mwisho’ mashahidi Wakristo wa Yehova wanaonywa waziwazi juu ya kufanywa wakufuru au kukengeuka. (Dan. 12:4; Mt. 24:9-13) Kwa hiyo, wachungaji wadogo Wakristo walio waaminifu wanapaswa kupendezwa na “kundi” kwa kuwa waangalifu. Wanapaswa kuwa macho ili walinde washiriki wa “kundi” wasiteleze na kuingia katika mashirika mabaya. (1 Kor. 15:33) Kuendeleza maoni na nia inayofaa ya kiroho si jambo rahisi kwa sababu ya mikazo ya wakati wote kutoka kwa ulimwengu mchafu. Ndiyo sababu kila mtu kundini anapaswa kutii shauri hili: “Wakumbukeni wale wanaoongoza kati yenu, ambao wamewaambia neno la Mungu, nanyi mnapotazama sana namna mwenendo wao utakavyokuwa iigeni imani yao.” (Ebr. 13:7, NW) Nyakati nyingine wanaume wazee wanaona kuwa ni jambo la lazima kutoa shauri la Kimaandiko na kuwaonya waamini wenzao juu ya uvutano wa wale wanaotafuta mapendezi yao wenyewe ya kichoyo na anasa kuliko kutafuta hali njema ya kiroho ya “kundi” lote kwa ujumla. Uongozi thabiti uliotolewa na Paulo; katika Warumi 16:17-19 unapasa katika visa kama hivyo. Yeye, alisema hivi. “Ndugu zangu, nawasihi waangalieni wafanyao fitina na mambo ya kukwaza kinyume cha mafundisho mliyojifunza: mkajiepushe nao. Kwa sababu walio hivyo hawamtumikii Bwana wetu Kristo, bali matumbo yao wenyewe; na kwa maneno laini na ya kujipendekeza waidanganya mioyo ya watu wanyofu. Maana utii wenu umewafikilia watu wote; basi nafurahi kwa ajili yenu, lakini nataka ninyi kuwa wenye hekima katika mambo mema, na wajinga katika mambo mabaya.
Kutumikia “Kundi”
16. (a) Ni nini linaloonyeshwa na uhakika wa kwamba nyakati nyingine Paulo alishauri kwa machozi? (b) Ili kuonyesha kupendezwa, waangalizi leo wanafanya kazi kwa bidii wapate kufanyia “kundi” nini?
16 Kwa sababu Paulo alisafiri sehemu kubwa, alikuwa anajua mambo mengi yaliyokuwa yakitendeka katika makundi ya wakati wake. Alijua kwamba kulikuwako matatizo na hatari mbalimbali. Kwa hiyo inafahamika kwamba anawasihi wanaume wazee wa Efeso wawe macho kiroho. Kwa kipindi cha zaidi ya miaka mitatu Paulo alikuwa ameonyesha upendo wake na kuhangaika kwake kwa kuendelea kuwashauri, hata kwa machozi. (Matendo 20:31) Bila shaka kulikuwako mambo yenye kusikitisha katika uchungaji huo. Ulimpasa Paulo achukue hatua fulani ili atoe uangalizi huo wa upendo na wa kuwa macho. Kwa hiyo, haishangazi kwamba waangalizi leo wanapata mambo kama hayo nyakati nyingine, sana sana kunapokuwako matatizo magumu kutatua. (Linganisha 2 Wakorintho 2:4.) Katika hali kama hizo hangaiko lao la kwanza ni kwa ajili ya “kundi.” Wanatumikia kwa juhudi ili waliweke likiwa safi kiroho na lenye afya pia, pasipo chachu.—1 Kor. 5:6; Gal. 5:7-10; Tito 2:1.
17. (a) .Ni jambo gani la maana tunalopaswa kujifunza katika maneno ya Paulo katika Matendo 20:32? (b) Kukabidhi watu na faida zao mikononi mwa Yehova kunaruhusu matokeo yawe nini?
17 Kwa kuwaweka waangalizi Waefeso “katika mikono ya Mungu, na kwa neno la neema yake,” Paulo angeweza kuwa na hakika kwamba walikuwa katika ulinzi bora zaidi, (Matendo 20:32) Vivyo hivyo leo, baada ya waangalizi kufanya yote wawezayo katika kutoa mashauri na msaada, au katika kuchukua hatua yo yote nyingine ya kutia adabu inayoshauriwa na Maandiko, wanaweza kumwachia Mungu mambo. Ikiwa ndugu na dada zetu wapendwa katika imani wanapatwa na matatizo makubwa, sikuzote inafariji kujua kwamba kwa kuwakabidhi pamoja na faida zao kwa Yehova katika sala na kuruhusu Neno lake, roho na tengenezo vitoe uongozi unaohitajiwa, matokeo yatakuwa kulingana na mapenzi yake. Chini ya hali hizo, lo lote litakalotokea litakuwa ni kwa ruhusa ya Mungu. (Linganisha 1 Petro 2:23.) Kwa mara nyingine, jambo hilo linaonyesha kupendezwa na “kundi,” kwa kuwa linaelekeza fikira kwake Yeye awezaye kufanya yaliyo mema kabisa katika hali yo yote.
18. (a) Maoni ya Paulo yalikuwa nini kuhusu mali zake? (b) Kwa kuiga mifano wa Paulo katika jambo hilo, waangalizi huonyeshaje kupendezwa na “kundi”?
18 Akiwa na dhamiri safi, Paulo aliweza kutaja ushuhuda wa kwamba hakuwa ametafuta kujitajirisha mwenyewe kwa hasara ya nduguze. Alikuwa amefanya kazi kwa mikono yake na kwa hiyo alikuwa na uradhi wa kuyaangalia mambo ya lazima aliyoyahitaji, (Matendo 20:33, 34) Ni kweli kwamba alipokuwa na uhitaji alikubali kitu kutoka kwa Wakristo Wafilipi. Yeye hakutafuta zawadi kama hizo, bali, matunda yanayounganishwa na utoaji wa namna hiyo. (Flp. 4:14-17) Kama vile Paulo alivyokuwa mwenye bidii wala hakutumikia apate mapato ya udanganyifu, ndivyo waangalizi wa siku zetu wanavyoweza kuweka mfano mwema kwa kuonyesha kwamba wao si wavivu, wala kwamba hawajaribu kuepuka kazi ngumu. Kupendezwa kwao na “kundi” kunawazuia wasiwe mzigo kwa kundi.—2 The. 3:6-10.
19. Kutenda kwa kupatana na kanuni ambayo imetajwa katika Matendo 20:35 kunakuwa na matokeo gani kwa waangalizi na kundi lote?
19 Wakiwa wameona yale ambayo Paulo alikuwa ameonyesha katika maisha na utumishi wake, waangalizi hao Waefeso walikuwa na mfano wa kufuata wakati walipokuwa wanajitahidi kusaidia walio dhaifu na kujitoa kulijenga kundi. Wakitenda kwa kupatana na kanuni ya kwamba “kuna furaha nyingi katika kutoa kuliko zilivyo katika kupokea,” waangalizi wa kisasa wanaweka mfano mzuri kwa wengine. (Matendo 20:35, NW) Hakika, si kwamba wanatoa vingi tu bali pia wanatoa bila unyimivu. Kuendelea kwao kufanya hivyo kunatokeza furaha ya wote katika kundi la Mashahidi wa Yehova.
‘Masumbuko ya Kulinda Makundi Yote’
20. Petro na Paulo walipendezwa na “kundi” kwa kadiri gani?
20 Ni wazi kwamba mifano myema inayotolewa na mitume hao waaminifu kama vile Petro na Paulo ilikuwa yenye kutokeza. Walijitumikisha kwa ajili ya Wakristo wenzao nao walionyesha kupendezwa sana si na kundi moja tu bali pia na ushirika mzima wa ndugu zao. (1 Pet. 2:17) Yajapokuwa mambo mengi yasiyowafaa, matatizo na majaribu, mitume walikumbuka kwanza hali njema ya kiroho ya “kundi.”
21. (a) Kulingana na 2 Wakorintho 11:23-28, baadhi ya “maneno yale ya inje” ambayo Paulo alipata yalikuwa mambo gani? (b) Paulo alionyeshaje kupendezwa kwingi na wengine?
21 Akiandikia waamini wenzake katika Korintho, Paulo alitaja mapigo, vifungo, mambo yenye kujaribu na hatari mbali-mbali alizokutana nazo katika kutumikia kama mhudumu. Mtume huyo aliongeza hivi baada ya hayo: “Na pamoja na maneno yale ya inje, kuna maneno yanayonisonga mimi kila siku, ndiyo masumbuko ya kulinda [makundi] yote.” (2 Kor. 11:23-28, ZSB) Twaweza kuwazia tu mikazo ambayo Paulo alikuwa nayo na kuhangaikia ‘makundi yote,’ kwa kuwa alikuwa anaarifiana na hesabu fulani ya rafiki Wakristo. (2 Tim. 4:9-13) Alisafiri sehemu nyingi katika mwendo wa ziara zake za umisionari naye akafanya ziara kadha za kurudia kwa makundi hayo. (Matendo 15:36) Utendaji wake kwa ajili ya wengine ulihitaji mambo mengi kweli kweli. Alitoa hotuba kwa vipindi virefu naye alitoa ushuhuda kwa ukawaida katika masinagogi, sehemu za watu wote na nyumba kwa nyumba. (Matendo 17:2; 19:9, 10; 20:20) Ili ajipatie mahitaji yake ya kimwili na kuepuka kuwa mzito kwa kundi, lilikuwa jambo la lazima kwa Paulo kufanya kazi ya kimwili (Matendo 18:1-3; 2 The. 3:8, 9) Bila shaka, mtume huyo alitumia wakati mwingi pia akijifunza Neno la Mungu, nayo maarifa aliyoyapata kwa hakika yalimfaa alipoongozwa na Mungu aandike vitabu 14 kati ya 27 vinavyofanyiza Maandiko ya Kikristo ya Kigiriki. Kweli, Paulo alikuwa mwanamume mwenye shughuli sana, walakini aliendelea, sikuzote akionyesha kupendezwa na “kundi.”
22, 23. (a) Katika wakati wetu, ni zipi baadhi ya njia ambazo mipango inafanywa kwa ajili ya “kundi la Mungu”? (b) Mipango yote hiyo inatoa ushuhuda wa jambo gani, na hilo lapaswa kuwa na matokeo gani kwetu?
22 Kuna kazi nyingi sana inayofanywa leo kwa ajili ya “kundi la Mungu.” Kukiwapo makundi 42,000 ya watu wa Yehova, ebu wazia utunzaji unaopaswa kutolewa wa mahitaji yao. Chakula cha kiroho cha kawaida kinatolewa na “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” (Mt. 24:45-47) Programu za mikutano ya kundi, makusanyiko ya mzunguko na makusanyiko ya wilaya zinatayarishwa kwa ukawaida ili kuwezesha Wakristo waje pamoja kwenye funzo, ibada na ushirika wenye kujenga kiroho. (Ebr. 10:23-25) Waangalizi wasafirio wanatumwa watembelee na kuangalia mahitaji ya pekee ya makundi yote. (Linganisha Matendo 16:4, 5.) Habari zenye mashauri na vitia-moyo zinapelekwa kwenye makundi na baraza za wazee. (Linganisha Wafilipi 1:1; 1 Petro 5:12; Yuda 3.) Mipango mingine, mingi sana, inafanywa kwa ajili ya kufaidi “kundi la Mungu” kiroho na kwa njia nyinginezo.
23 Kazi hiyo inatia ndani wakati mwingi sana, jitihada nyingi sana na gharama nyingi sana. Walakini inathibitisha jambo gani? Inaonyesha kwamba Yehova huwaangalia watu wake. Kupitia kwa Mwanawe, Mchungaji Mwema, Mungu huonyesha uwezo wa ajabu wa kuchunga. (Isa. 40:10, 11) Makumi ya maelfu ya wachungaji wadogo wamewekwa na roho takatifu nao wanashiriki katika kulichunga “kundi la Mungu.” Yote hayo yanaonyesha kuhangaika kwa kupendezwa na “kundi” lote na watu mmoja mmoja walio washiriki wa “kundi.” Ebu sisi binafsi tuonyeshe kuthamini huko kwa kutoka moyoni kwa ajili ya upendo unaoonyeshwa na Mchungaji Mkuu, Yehova Mungu, na Mwanawe, Yesu Kristo, katika kutuangalia kabisa kwa upole.
[Picha katika ukurasa wa 8]
”Lisha Kondoo Zangu”