Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 11/15 kur. 10-15
  • Waangalizi Wasafirio—Zawadi Zikiwa Wanadamu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Waangalizi Wasafirio—Zawadi Zikiwa Wanadamu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Roho Yao ya Kujidhabihu
  • Wanathaminiwa
  • “Msisahau Ukaribishaji-Wageni”
  • Kuyaimarisha Makutaniko
  • Waangalizi Wasafirio—Wafanyi-Kazi-Wenzi Katika Ukweli
    Mashahidi wa Yehova—Wanafanya Mapenzi ya Mungu kwa Umoja Ulimwenguni Pote
  • Jinsi Ambavyo Waangalizi Wasafirio Hutumikia Wakiwa Wasimamizi-Nyumba Waaminifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Waangalizi wa Mzunguko Wanatusaidiaje?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
  • Waangalizi Wasafirio Waleta Faida Leo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 11/15 kur. 10-15

Waangalizi Wasafirio—Zawadi Zikiwa Wanadamu

“Alipopaa juu alichukua mateka; alitoa zawadi [zikiwa] wanadamu.”—WAEFESO 4:8, NW.

1. Ni kazi gani mpya iliyotangazwa katika jarida hili mwaka wa 1894?

ZAIDI ya karne moja iliyopita, gazeti Watch Tower lilitangaza jambo jipya. Hilo lilifafanuliwa kuwa “Sehemu Nyingine ya Kazi ya Kuhubiri.” Utendaji huo mpya ulitia ndani nini? Huo ulikuwa mwanzo wa kisasa wa kazi ya waangalizi wasafirio. Toleo la Septemba 1, 1894, la jarida hili lilieleza kwamba kuanzia wakati huo na kuendelea ndugu wanaostahili wangekuwa wakizuru vikundi vya Wanafunzi wa Biblia ‘kwa kusudi la kuvijenga katika kweli.’

2. Waangalizi wa mzunguko na wa wilaya wana wajibu gani mbalimbali?

2 Katika karne ya kwanza W.K., makutaniko ya Kikristo yalitembelewa na waangalizi hao kama Paulo na Barnaba. Wanaume hao waaminifu walikuwa na lengo la ‘kuyajenga’ makutaniko. (2 Wakorintho 10:8) Leo, tumebarikiwa kuwa na maelfu ya wanaume wanaofanya hivyo kwa njia yenye utaratibu. Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova limewaweka rasmi kuwa waangalizi wa mzunguko na wa wilaya. Mwangalizi wa mzunguko hutumikia makutaniko yapatayo 20, kila moja yayo kwa juma moja karibu mara mbili kwa mwaka, akichunguza rekodi za kutaniko, akitoa hotuba, na kushiriki katika huduma ya shambani pamoja na watangazaji wa Ufalme wa mahali hapo. Mwangalizi wa wilaya ni mwenyekiti wa kila moja ya makusanyiko ya mzunguko ya kila mwaka kwa mizunguko kadhaa, yeye hushiriki katika huduma ya shambani pamoja na makutaniko yaliyo wakaribishaji kwenye kusanyiko, na hutoa kitia-moyo katika hotuba zinazotegemea Biblia.

Roho Yao ya Kujidhabihu

3. Kwa nini waangalizi wasafirio huhitaji kuwa na roho ya kujidhabihu?

3 Waangalizi wasafirio husafiri sikuzote. Hilo lenyewe hutaka roho ya kujidhabihu. Mara nyingi kusafiri kutoka kutaniko moja hadi jingine kwaweza kuwa jambo gumu, lakini wanaume hao pamoja na wake zao hufanya hivyo wakiwa na mtazamo wenye shangwe. Mwangalizi wa mzunguko mmoja alisema hivi: “Mke wangu ni mwenye kuunga mkono kabisa na halalamiki . . . Anastahili kusifiwa sana kwa sababu ya roho yake ya kujidhabihu.” Waangalizi fulani wa mzunguko husafiri kilometa zaidi ya 1,000 kati ya makutaniko. Wengi huendesha magari, lakini wengine husafiri mahali-mahali kwa kutumia usafiri wa umma, baiskeli, farasi, au miguu. Mwangalizi wa mzunguko mmoja wa Afrika huhitaji hata kupitia mtoni akiwa amembeba mkewe mabegani pake ili kufikia kutaniko moja. Katika safari zake za umishonari, mtume Paulo alilazimika kukabiliana na joto na baridi, njaa na kiu, usiku kadhaa bila usingizi, hatari mbalimbali, na mnyanyaso wenye jeuri. Alikuwa pia na hali ya “kuhangaikia makutaniko yote”—jambo lililo la kawaida kwa waangalizi wasafirio leo.—2 Wakorintho 11:23-29.

4. Matatizo ya afya yaweza kuwa na matokeo gani katika maisha za waangalizi wasafirio na wake zao?

4 Sawa na Timotheo, mwandamani wa Paulo, nyakati nyingine waangalizi wasafirio na wake zao huwa na matatizo ya kiafya. (1 Timotheo 5:23) Hayo huwawekea mkazo wa ziada. Mke wa mwangalizi wa mzunguko mmoja aeleza hivi: “Kuwa pamoja na akina ndugu sikuzote ni mkazo ninapokuwa mgonjwa. Nikiwa nimefikia mwanzo wa komahedhi, nimeona hilo kuwa jambo gumu hasa. Kuhitaji kufunga tu vitu vyetu vyote kila juma na kuhamia kwingineko ni jambo gumu kwelikweli. Mara nyingi, inanibidi nitue na kusali kwa Yehova anipe nguvu za kuendelea.”

5. Yajapokuwa majaribu mbalimbali, ni roho gani ambayo imeonyeshwa na waangalizi wasafirio na wake zao?

5 Yajapokuwa matatizo ya afya na majaribu mengine, waangalizi wasafirio pamoja na wake zao hupata shangwe katika utumishi wao nao huonyesha upendo wenye kujidhabihu. Waangalizi fulani wamehatarisha uhai wao ili kutoa msaada wa kiroho katika nyakati za mnyanyaso au vita. Wazurupo makutaniko, wamedhihirisha roho inayofanana na ile ya Paulo, aliyewaambia Wakristo Wathesalonike hivi: “Tulikuwa wapole katikati yenu, kama vile mlezi awatunzavyo watoto wake mwenyewe. Vivyo hivyo nasi tukiwatumaini kwa upendo mwingi, tuliona furaha kuwapa, si Injili ya Mungu tu, bali na roho zetu pia, kwa sababu mmekuwa wapendwa wetu.”—1 Wathesalonike 2:7, 8.

6, 7. Waangalizi wasafirio wenye bidii waweza kuwa na uvutano gani mzuri?

6 Sawa na wazee wengine katika kutaniko la Kikristo, waangalizi wasafirio ‘hujitaabisha kwa kuhutubu na kufundisha.’ Wazee wote hao wapasa “wahesabiwe kustahili heshima maradufu.” (1 Timotheo 5:17) Kielelezo chao chaweza kuthibitika kuwa chenye kunufaisha ikiwa, baada ya ‘kuuchunguza sana mwisho wa mwenendo wao, twaiga imani yao.’—Waebrania 13:7.

7 Wazee fulani wasafirio wamekuwa na uvutano gani juu ya wengine? “Ndugu P—— alikuwa na uvutano wa ajabu kama nini maishani mwangu!” akaandika Shahidi mmoja wa Yehova. “Alikuwa mwangalizi asafiriye katika Mexico tangu mwaka wa 1960 na kuendelea. Nikiwa mtoto, nilingoja ziara zake nikiwa na hamu na shangwe. Nilipokuwa na umri wa miaka kumi, aliniambia, ‘Wewe pia utakuwa mwangalizi wa mzunguko.’ Katika ile miaka migumu ya utineja, mara nyingi nilimtafuta kwa sababu sikuzote alikuwa na maneno yenye hekima ya kutoa. Hangaiko lake kuu maishani lilikuwa kulichunga kundi! Sasa kwa sababu mimi ni mwangalizi wa mzunguko, sikuzote mimi hujaribu kutumia wakati pamoja na vijana na kuwatia moyo wafuatie miradi ya kitheokrasi sawa na vile alivyonifanyia. Hata katika miaka ya mwisho-mwisho ya maisha yake, ajapokuwa na matatizo ya moyo, sikuzote Ndugu P—— alijaribu kutoa kitia-moyo. Siku moja tu kabla ya kifo chake katika Februari 1995, aliandamana nami kwenye siku ya kusanyiko la pekee akamtia moyo ndugu fulani ambaye ni msanifuujenzi afuatie miradi ifaayo. Papo hapo ndugu huyo akatoa ombi la kutumikia Betheli.”

Wanathaminiwa

8. Ni nani walio “zawadi zikiwa wanadamu” wafafanuliwao katika Waefeso sura ya 4, nao hunufaishaje kutaniko?

8 Waangalizi wasafirio na wazee wengine ambao wamependelewa kwa kupewa migawo ya utumishi kwa fadhili isiyostahiliwa ya Mungu wanaitwa “zawadi zikiwa wanadamu.” Akiwa mwakilishi wa Yehova na Kichwa cha kutaniko, Yesu ameandaa wanaume hao wa kiroho ili kila mmoja wetu aweze kujengwa na kufikia ukomavu. (Waefeso 4:8-15) Zawadi yoyote ile hustahili kuonyeshwa uthamini. Ndivyo ilivyo hasa kwa habari ya zawadi inayotutia nguvu tuendelee kumtumikia Yehova. Kwa hiyo basi, twaweza kuonyeshaje kuthamini kwetu kazi ya waangalizi wasafirio? Twaweza kuonyesha katika njia zipi kwamba ‘twahesabu watu kama hao kuwa watu wa kuheshimiwa’?—Wafilipi 2:29.

9. Twaweza kuonyesha katika njia zipi kuthamini kwetu waangalizi wasafirio?

9 Ziara ya mwangalizi wa mzunguko inapotangazwa, twaweza kuanza kufanya mipango ya kushiriki kikamili katika utendaji wa kutaniko kwa juma hilo. Labda twaweza kuweka kando wakati wa ziada ili kuunga mkono mipango ya utumishi wa shambani wakati wa hiyo ziara. Huenda tukaweza kutumikia tukiwa mapainia-wasaidizi mwezi huo. Kwa hakika tutataka kutumia madokezo ya mwangalizi wa mzunguko ili kuboresha huduma yetu. Roho hiyo ya kuitikia upesi itatunufaisha na itamhakikishia kwamba ziara yake ni yenye mafaa. Ndiyo, waangalizi wasafirio huzuru kutaniko ili kutujenga, lakini wao pia huhitaji kujengwa kiroho. Kulikuwa na nyakati ambazo Paulo alihitaji kitia-moyo, na mara nyingi aliwaomba Wakristo wenzake wasali kwa ajili yake. (Matendo 28:15; Warumi 15:30-32; 2 Wakorintho 1:11; Wakolosai 4:2, 3; 1 Wathesalonike 5:25) Waangalizi wasafirio wa sasa vilevile huhitaji sala zetu na kitia-moyo chetu.

10. Twaweza kusaidiaje kufanya kazi ya mwangalizi asafiriye iwe yenye shangwe?

10 Je, tumepata kumwambia mwangalizi wa mzunguko na mkewe jinsi tuthaminivyo ziara zao? Je, sisi humshukuru kwa sababu ya shauri lenye msaada analotutolea? Je, sisi humjulisha wakati madokezo yake ya utumishi wa shambani yaongezapo shangwe yetu katika huduma? Ikiwa sisi hufanya hivyo, hilo litasaidia kufanya kazi yake iwe yenye shangwe. (Waebrania 13:17) Mwangalizi wa mzunguko mmoja katika Hispania alieleza hasa kadiri yeye na mkewe wathaminivyo barua za shukrani ambazo wamepokea baada ya kuyazuru makutaniko. “Sisi huweka kadi hizo na kuzisoma tuhisipo tumevunjika moyo,” yeye asema. “Hizo ni chanzo cha kitia-moyo halisi.”

11. Kwa nini tuwajulishe wake wa waangalizi wa mzunguko na wa wilaya kwamba wanapendwa na kuthaminiwa?

11 Mke wa mwangalizi asafiriye kwa hakika hunufaika kutokana na maneno ya pongezi. Yeye ametoa dhabihu kubwa ili kumsaidia mumewe katika sehemu hii ya utumishi. Dada hawa waaminifu hujinyima tamaa ya asili ya kuwa na nyumba yao wenyewe, na pia katika visa vingi, ya kuwa na watoto. Binti Yeftha alikuwa mmoja wa watumishi wa Yehova aliyeacha kwa utayari fursa yake ya kuwa na mume na familia kwa sababu ya nadhiri aliyoweka babaye. (Waamuzi 11:30-39) Dhabihu yake ilionwaje? Waamuzi 11:40 lataarifu hivi: ‘Binti za Israeli walienda mwaka baada ya mwaka ili kumkumbuka huyo mwana wa Yeftha, Mgileadi, siku nne katika mwaka.’ Ni jambo zuri kama nini tujitahidipo kuwaambia wake wa waangalizi wa mzunguko na wa wilaya kwamba wanapendwa na kuthaminiwa!

“Msisahau Ukaribishaji-Wageni”

12, 13. (a) Kuna msingi gani wa Kimaandiko wa kuwa wenye ukaribishaji-wageni kwa waangalizi wasafirio na wake zao? (b) Toa kielezi cha jinsi ukaribishaji-wageni huo uwezavyo kuwa wenye kunufaisha kwa wote.

12 Kuonyesha ukaribishaji-wageni ni njia nyingine ya kudhihirisha upendo na uthamini kwa wale walio katika kazi ya kusafiri ya Kikristo. (Waebrania 13:2) Mtume Yohana alimpongeza Gayo kwa sababu ya kuonyesha ukaribishaji-wageni kwa wale waliozuru kutaniko wakiwa wamishonari wasafirio. Yohana aliandika hivi: “Mpenzi, kazi ile ni ya uaminifu uwatendeayo hao ndugu na hao wageni nao, waliokushuhudia upendo wako mbele ya kanisa; utafanya vizuri ukiwasafirisha kama ipasavyo kwa Mungu. Kwa maana, kwa ajili ya Jina hilo, walitoka, wasipokee kitu kwa Mataifa. Basi imetupasa sisi kuwakaribisha watu kama hao [“kuwapokea watu wa namna hiyo kwa ukaribishaji-wageni,” NW], ili tuwe watenda kazi pamoja na kweli.” (3 Yohana 5-8) Leo, twaweza kuendeleza utendaji wa kuhubiri Ufalme kwa kuwaonyesha waangalizi wasafirio na wake zao ukaribishaji-wageni uo huo. Bila shaka, wazee wa mahali fulani wapaswa kuhakikisha kwamba makao ni yenye kufaa, lakini mwangalizi wa wilaya mmoja alisema hivi: “Kushirikiana kwetu na ndugu hakuwezi kutegemea ni nani awezaye kutufanyia jambo fulani. Hata tusingetaka kudokeza hivyo. Ni lazima tuwe tayari kukubali ukaribishaji-wageni wa yeyote kati ya ndugu zetu, awe ni tajiri au maskini.”

13 Ukaribishaji-wageni waweza kuwa wenye kunufaisha kwa wote. “Katika familia yetu, tulikuwa na desturi ya kualika waangalizi wasafirio kukaa nasi,” akumbuka Jorge, aliyekuwa mwangalizi wa mzunguko hapo awali anayetumikia Betheli sasa. “Nahisi kwamba ziara hizo zilinisaidia zaidi ya vile nilivyong’amua wakati huo. Wakati wa ubalehe wangu, nilikuwa na matatizo ya kiroho. Mamangu alihangaikia jambo hilo lakini hakujua njia barabara ya kusaidia na basi akamwomba mwangalizi wa mzunguko azungumze nami. Mwanzoni nilimwepa, kwa kuwa niliogopa kuchambuliwa. Lakini njia yake yenye urafiki ilinishawishi nimfunulie yote. Alinialika kula mlo pamoja naye Jumatatu moja, nami nikamwambia yote yaliyokuwa moyoni mwangu kwa sababu nilihisi uhakika kwamba alikuwa akinielewa. Yeye alisikiliza kwa uangalifu. Madokezo yake yenye kutumika yalifanya kazi kwelikweli, nami nikaanza kufanya maendeleo kiroho.”

14. Kwa nini tuwe wenye uthamini badala ya kuwachambua wazee wasafirio?

14 Mwangalizi asafiriye hujaribu kusaidia kiroho vijana na wazee vilevile. Basi, kwa hakika twapaswa kuonyesha uthamini wetu kwa jitihada zake. Hata hivyo, namna gani ikiwa tungemchambua kwa sababu ya udhaifu wake mbalimbali au kumlinganisha isivyofaa na wengine ambao wamelizuru kutaniko? Yamkini, hilo lingevunja moyo sana. Halikuwa jambo la kumtia moyo Paulo kusikia kazi yake ikichambuliwa. Yaonekana, baadhi ya Wakristo Wakorintho walikuwa wakichambua sura yake na uwezo wake wa kusema. Yeye mwenyewe aliwanukuu wachambuzi hao kuwa wakisema: “Nyaraka zake ni nzito, hodari; bali akiwapo mwenyewe mwilini ni dhaifu, na maneno yake si kitu.” (2 Wakorintho 10:10) Lakini kwa furaha, waangalizi wasafirio kwa kawaida husikia maneno ya uthamini wenye upendo.

15, 16. Waangalizi wasafirio na wake zao huathiriwaje na upendo na bidii zionyeshwazo na waamini wenzao?

15 Mwangalizi wa mzunguko mmoja katika Amerika ya Latini hutembea kwa taabu katika vijia vyenye matope ili kuzuru ndugu na dada zake wa kiroho wanaoishi katika kanda inayodhibitiwa na wapiganaji wa kuvizia. “Inagusa moyo kuona jinsi ambavyo akina ndugu huonyesha uthamini wao kwa ziara,” yeye aandika. “Hata ingawa ni lazima nijitahidi sana kufika huko, nikikabili hatari na magumu mengi, yote hayo yanathawabishwa kwa ule upendo na bidii ambayo hao ndugu huonyesha.”

16 Mwangalizi wa mzunguko katika Afrika aandika hivi: “Kwa sababu ya upendo tulioonyeshwa na akina ndugu, tulilipenda eneo la Tanzania sana! Akina ndugu walikuwa tayari kujifunza kutoka kwetu, nao walifurahi kuwa nasi nyumbani mwao.” Kulikuwa na uhusiano wenye upendo na furaha kati ya mtume Paulo na wale wenzi wa ndoa Akila na Priska Wakristo wa karne ya kwanza. Kwa kweli, Paulo alisema hivi juu yao: “Nisalimieni Priska na Akila, watenda kazi pamoja nami katika Kristo Yesu; waliokuwa tayari hata kukatwa kichwa kwa ajili ya maisha yangu; ambao ninawashukuru, wala si mimi tu, ila na makanisa ya Mataifa yote pia.” (Warumi 16:3, 4) Waangalizi wasafirio na wake zao ni wenye shukrani kuwa na marafiki walio kama Akila na Priska wa siku ya kisasa ambao hufanya jitihada ya pekee kuonyesha ukaribishaji-wageni na kutoa uandamani.

Kuyaimarisha Makutaniko

17. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba kuna hekima katika mpango wa kuwa na waangalizi wasafirio, nao hupata wapi maagizo yao?

17 Yesu alisema hivi: “Hekima imejulikana kuwa ina haki kwa kazi zake.” (Mathayo 11:19) Ni wazi kwamba kuna hekima katika mpango wa kuwa na waangalizi wasafirio kwa sababu huo husaidia kuyaimarisha makutaniko ya watu wa Mungu. Wakati wa safari ya umishonari ya pili ya Paulo, yeye na Sila ‘walipitia Siria na Kilikia wakiyaimarisha makanisa,’ kwa mafanikio. Kitabu cha Matendo chatuambia hivi: “Walipokuwa wakipita kati ya miji ile, wakawapa zile amri zilizoamriwa na mitume na wazee walioko Yerusalemu, ili wazishike. Makanisa yakatiwa nguvu katika ile Imani, hesabu yao ikaongezeka kila siku.” (Matendo 15:40, 41; 16:4, 5, linganisha Habari Njema kwa Watu Wote.) Waangalizi wasafirio wa sasa hupokea maagizo kupitia Maandiko na vichapo vya “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” sawa na Wakristo wengine wote.—Mathayo 24:45.

18. Waangalizi wasafirio huyaimarishaje makutaniko?

18 Ndiyo, lazima wazee wasafirio waendelee kujilisha kwenye meza ya kiroho ya Yehova. Lazima wafahamu vizuri njia na miongozo inayofuatwa na tengenezo la Mungu. Ndipo wanaume hao wawezapo kuwa baraka halisi kwa wengine. Kupitia kielelezo chao chema cha bidii katika utumishi wa shambani, wao waweza kusaidia waamini wenzao waboreke katika huduma ya Kikristo. Zile hotuba zinazotegemea Biblia ambazo hutolewa na wazee hao wanaozuru hujenga wasikilizaji kiroho. Kwa kusaidia wengine watumie shauri la Neno la Mungu, watumikie kwa upatano na watu wa Yehova duniani pote, na watumie maandalizi ya kiroho yatolewayo na Mungu kupitia ‘mtumwa mwaminifu,’ waangalizi wasafirio huyaimarisha makutaniko wanayopendelewa kuzuru.

19. Ni maswali gani yanayosalia kufikiriwa?

19 Tengenezo la Yehova lilipoanzisha kazi ya wazee wasafirio miongoni mwa Wanafunzi wa Biblia karibu miaka mia moja iliyopita, jarida hili lilitaarifu hivi: “Tutachunguza ili kuona matokeo na kuona mwongozo zaidi wa Bwana.” Mwongozo wa Yehova umeonekana wazi. Kwa sababu ya baraka yake na usimamizi wa Baraza Linaloongoza, kazi hii imepanuliwa na kuboreshwa katika ile miaka ambayo imepita. Likiwa tokeo, makutaniko ya Mashahidi wa Yehova kotekote duniani yanafanywa imara katika imani na yanaongezeka kila siku. Kwa wazi, Yehova anabariki roho ya kujidhabihu ya zawadi hizo zilizo wanadamu. Lakini waangalizi wasafirio waweza kutimizaje kazi yao kwa mafanikio? Malengo yao ni nini? Wao waweza kuyanufaishaje makutaniko kikamili zaidi?

Ungeitikiaje?

◻ Ni upi baadhi ya wajibu mbalimbali wa waangalizi wa mzunguko na wa wilaya?

◻ Kwa nini waangalizi wasafirio huhitaji kuwa na roho ya kujidhabihu?

◻ Uthamini waweza kuonyeshwaje kwa kazi ya wazee wasafirio na wake zao?

◻ Waangalizi wasafirio waweza kufanya nini ili kuyafanya makutaniko yawe imara katika imani?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kusafiri sikuzote hutaka roho ya kujidhabihu

[Picha katika ukurasa wa 13]

Je, umewaonyesha waangalizi wasafirio na wake zao ukaribishaji-wageni?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki