Waangalizi Wasafirio—Wafanyi-Kazi-Wenzi Katika Ukweli
Katika kundi la Kikristo la karne ya kwanza, kulikuwako waangalizi wenye kusafiri waliozuru makundi ili kuyajenga. Walijitolea wenyewe, bila kutafuta faida ya kibinafsi, ili wasaidie wale waliokuwa katika makundi waendelee kutembea kama inavyofaa kuhusu Mungu.—Matendo 11:23, 24; 14:21, 22; 15:32; 20:2, 31-35; Wafilipi 2:20-22, 29; 1 Wathesalonike 2:5-12.
Leo makundi ya Mashahidi wa Yehova pia yanapokea faida za waangalizi wasafirio. Wanaume hao wana miaka mingi ya ujuzi katika utendaji wa kuhubiri wa Mashahidi wa Yehova na wakiwa waangalizi. Wamejifanya huru wenyewe wasiwe na kazi ya kimwili na madaraka ya jamaa ili waweze kujitoa wenyewe katika huduma ya wakati wote. Kwa wale waliooa, kwa kawaida wake wanashiriki pia huduma ya wakati wote pamoja na waume zao.
Mwangalizi wa mzunguko anapewa mgawo wa kuuangalia mzunguko wenye makundi 18 mpaka 25. Yeye anatembelea kila kundi katika mzunguko karibu mara mbili kwa mwaka na baada ya miaka miwili au mitatu anapewa mgawo kwenye mzunguko mwingine. Kwa njia hiyo makundi yanaweza kufaidika na ujuzi mbalimbali na uwezo wa waangalizi wa mizunguko mbalimbali.
Mwangalizi wa mzunguko anachunguza hali ya kiroho ya kundi na utendaji wake. Anatoa hotuba kadha kwenye kundi na pia anakutana na wazee na watumishi wa huduma ili wafikirie jinsi wanavyoweza kufanya utumishi wao kwa kundi uwe bora.
Wakati wa juma yeye na mkeye, ikiwa ameoa, wanaandamana na Mashahidi wa kundi hilo, wakiwasaidia wafanye huduma yao ya nyumba kwa nyumba iwe bora. Yeye na mkeye watatembelea pia wapya wanaopendezwa ili kuwatia moyo katika imani. Wewe unaweza kuomba utembelewe kwa njia hiyo.
Mwangalizi wa wilaya ana sifa zile zile za kiroho na ujuzi wa miaka mingi. Yeye anasafiri kutoka mzunguko huu kwenda mzunguko mwingine, akitumikia kila juma kuhusiana na makusanyiko ya mizunguko. Yeye na mkeye pia wanafanya kazi katika huduma ya shambani pamoja na Mashahidi katika kundi mojapo la makundi ya mzunguko anaotembelea. Yeye anasimamia matayarisho ya mwisho ya programu ya kusanyiko la mzunguko na anatoa hotuba kadha wakati wa kusanyiko, kutia na hotuba ya watu wote.
Waangalizi wasafirio wanapomaliza ziara yao katika kundi au katika mzunguko, wanaendelea kutembelea mzunguko mwingine, wakifuata ratiba ile ile, mpaka makundi yote au mizunguko yote iwe imetembelewa kwa muda wa karibu miezi sita; kisha wanaanza ziara tena.
Katika nchi nyingi waangalizi wasafirio wanasafiri kwa kutumia gari au basi au gari moshi. Katika nchi nyingine huenda wakatumia baiskeli au hata kutembea kwa miguu. Sosaiti inalipa nauli za mwangalizi asafiriye, na pia kumpatia yeye na mkeye alawansi kidogo ya mahitaji yao ya kibinafsi. Kwa kawaida mwangalizi asafiriye na mkeye wanapatiwa malazi na vyakula na washiriki wa kila kundi.
Utumishi huo unataka roho ya kujidhabihu. Waangalizi wasafirio na wake zao wameazimu kuyatolea makundi utumishi wao bila kuyawekea mzigo wenye gharama. —1 Wathesalonike 2:9.
• Lilikuwa kusudi gani la waangalizi wasafirio katika kundi la Kikristo la karne ya kwanza?
• Waangalizi wasafirio leo wamestahilije na kuwa tayari kwa huduma hiyo?
• Simulia utumishi wa waangalizi wa mizunguko na wilaya na jinsi wanavyoishi.
[Picha katika ukurasa wa 20]
Mwangalizi wa wilaya anahutubia kusanyiko la mzunguko
[Picha katika ukurasa wa 21]
Waangalizi wa mizunguko wanatoa agizo la kuhubiri nyumba kwa nyumba, wanazungumza na wazee wa kundi, wanatembelea mafunzo ya Biblia kwa watu walioanza kupendezwa karibuni, na wanahutubia makundi