Unga Mkono Ziara ya Mwangalizi wa Mzunguko
1 Kuanzia Oktoba 15, 1946, na kuendelea, makundi yamepangwa katika mizunguko ambayo inatumikiwa na waangalizi wasafirio wa wakati wote. Kwa miaka karibu 43 sasa, watu mmoja mmoja na makundi wamenufaika na uandalizi huu wa kitheokrasi. (Isa. 1:26) Kuendelea kwetu kuunga mkono mpango huu kutatuletea baraka nyingi zaidi.—Efe. 4:7, 8, 11.
KUJITAYARISHIA ZIARA
2 Ziara ya mwangalizi wa mzunguko ikiisha kutangazwa, tunaweza kuanza kujitayarisha kwa ajili yayo. Tunaweza kufanya mipango kurekebisha ratiba yetu ya kawaida ili kuunga mkono kikamili juma la utendaji wa pekee. Wahubiri fulani wanapanga kutumia wakati zaidi katika huduma ya shambani wakifanya upainia msaidizi. Wengine wanaweza kuomba ruhusa ya siku moja au mbili kutoka kazi yao ya kimwili na kushiriki katika huduma. Wahubiri wengi hufanya miadi ya pekee ya kufanya kazi pamoja na mwangalizi asafiriye katika sehemu fulani ya huduma. Kuunga mkono huduma ya shambani kwa moyo mzima katika pindi hii kunaleta thawabu nyingi.
3 Ripoti zinazopokewa kutoka kwa waangalizi wasafirio zinaonyesha kwamba kunaweza kuwa na uungaji mkono vizuri zaidi kwa ziara za kurudia alasiri na utendaji wa funzo la Biblia. Je! unaweza kuratibu uwe na ziara za kurudia au funzo la Biblia alasiri moja wakati wa juma hili? Mwangalizi asafiriye ataambatana nawe kwa nderemo, na ukipenda, angefurahia kuongoza funzo lako.
MSAADA WA KIBINAFSI
4 Lililo juu katika orodha ya mambo ya kutangulizwa ya mwangalizi asafiriye ni uhitaji wa kuandaa mazoezi zaidi kwa yeyote ambaye huenda akawa anafikia pendeleo kubwa zaidi la utumishi. (1 Tim. 3:1) Je! wewe una maswali kuhusu mgawo au madaraka yako hususa? Je! ungependa kufanyia maendeleo uwezo wako na mpango wa kibinafsi? Je! unapendezwa na utumishi wa Betheli, Gileadi, au Shule ya Mazoezi ya Huduma? Je! ungependa kutumikia mahali ambapo uhitaji ni mkubwa zaidi, katika mzunguko wako au mahali pengine katika eneo letu? Hata miradi yako ya kiroho iwe nini, mwangalizi wa mzunguko ataizungumza pamoja nawe kwa nderemo.
5 Ikiwa mwangalizi wa mzunguko wenu ameoa, mke wake vilevile ni mtumishi wa Yehova aliyejitoa. Yaelekea sana sana kwamba yeye ni painia na atakuwa na nafasi ya kuunga mkono kikamili mipango ya utumishi wa shambani. Kwa sababu ya ujuzi wake na kushiriki huduma kwa ukawaida katika maeneo mbalimbali, anakuwa stadi katika kazi ya kuhubiri. Anajifanya apatikane kufanya kazi hasa na akina dada katika utumishi wa nyumba kwa nyumba na kujiunga nao katika ziara za kurudia na mafunzo ya Biblia. Anastahili kusifiwa kwa uchangamfu kama Paulo alivyosifu Fibi.—Rum. 16:1, 2.
6 Jambo lisilopaswa kusahaulika ni pendeleo tulilo nalo kumwonyesha ukaribishaji wageni mwangalizi asafiriye na mke wake, ikiwa ameoa. Ndugu wengi wamekumbuka kwa uthamini sana kitia-moyo ambacho wamepokea kwa sababu ya kufungua makao yao au kushiriki mlo pamoja na wahudumu hawa wasafirio na kushangilia ushirika wa kiroho wenye kupendeza pamoja nao.—3 Yoh. 5-8.
7 Ziara za ukawaida zinazofanywa na waangalizi wasafirio waliokomaa kiroho zinaendelea kuwasaidia watu wa Yehova. Kiwango ambacho kufikia hicho tunaweza kunufaika kama watu mmoja mmoja kwa sababu ya mpango huu kinategemea kadiri ambayo tunajitayarisha na kuunga mkono ziara ya mwangalizi wa mzunguko. Sisi sote na tupige moyo konde kuunga mkono kwa ukamili ziara itakayofuata ya mwangalizi wa mzunguko.