“Bwana Mmoja, Imani Moja, Ubatizo Mmoja”
“[Kuna] Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja. Mungu mmoja, naye ni Baba wa wote, aliye juu ya yote.”—WAEFESO 4:4-6.
1, 2. (a) Kwa habari ya Yeye mwenyewe, Yehova alieleza nini waziwazi sana kupitia Musa? (b) Kwa hiyo je! maoni ya kidini yenye kutofautiana yaliruhusiwa katika Israeli?
“[YEHOVA], Mungu wetu, [Yehova] ndiye mmoja. Msifuate miungu mingine katika miungu ya mataifa wawazungukao; kwani [Yehova] Mungu wako, aliye katikati yako ni Mungu mwenye wivu [anayetaka ibada ya pekee, NW].” Musa alieleza mambo waziwazi kabisa alipokuwa akisema na Waisraeli waliokusanyika kwenye nyanda za Moabi, muda mfupi kabla ya wao kuingia katika Nchi ya Ahadi. Alitaja wazi kwamba Mungu wao, Yehova, ni Mungu mmoja, na kwamba Yehova anatazamia kupewa ibada isiyochanganywa na mambo mengine. Katika hotuba ya wakati uliotangulia, Musa alikuwa amesema hivi: “[Yehova] ndiye Mungu [wa kweli] katika mbingu juu, na katika nchi chini; hapana mwingine. Basi, zishike sheria zake, na amri zake, ninazokuamuru leo, upate kufanikiwa.”—Kumbukumbu la Torati 6:4, 14, 15; 4:39, 40.
2 Maneno hayo hayaweki nafasi ya kuwa na maoni yanayotofautiana ya kidini! Israeli walikuwa na Mungu mmoja. Naye Yehova aliionyesha wazi ile njia moja inayokubalika inayopasa kufuatwa katika kumwabudu yeye.
Madhehebu za Kiyahudi Zinatokea
3. Kwa sababu Wayahudi walio wengi hawakuendelea kuwa waaminifu kwa Yehova, ni jambo gani lililotukia mwishowe?
3 Lakini, Waisraeli walio wengi walikuja kuwa waasi-imani na waabudu wa miungu-sanamu badala ya kuizoea ile ibada safi ya Mungu mmoja tu wa kweli, Yehova. (Yeremia 17:13; 19:5) Kwa sababu hiyo, wao ‘hawakufanikiwa.’ Katika mwaka wa 607 K.W.K. Yerusalemu uliharibiwa na Wababuloni, na Wayahudi wengi wakahamishwa na kupelekwa Babulonia. Baki la waaminifu lilirudi Yerusalemu miaka 70 baadaye na kuanza kujenga hekalu la pili la kumwabudia Yehova. Lakini wakati ulipoendelea kupita, hesabu kubwa ya Wayahudi wakawa waasi-imani na mwishowe wakagawanyika katika madhehebu mbalimbali.
4, 5. (a) Eleza juu ya nyingine za madhehebu ya Kiyahudi yaliyositawi baada ya utumwa wa Kibabuloni. (b) Je! madhehebu hizo zenye kuleta migawanyiko ziliwafaidi Wayahudi kwa njia yo yote? Eleza.
4 Katika karne ya nne au ya tatu K.W.K. madhehebu ya Hasidimu (“wenye kuonyesha woga wa mambo ya kimungu”) ilisitawi. Wao walikuwa wakifuata Torati ya Kiyahudi kwa njia ya kupita kiasi na kwa ujumla wanachukuliwa kuwa ndio watangulizi wa madhehebu nyingine mbili zilizoanza katika karne ya pili K.W.K., yaani, Waessene na Wafarisayo. Waessene na hata Wafarisayo walifuata fundisho la Kigiriki la kwamba nafsi haiwezi kufa. Walikuwako watu wenye kuitwa Masadukayo ambao hawakuamini kama makundi hayo mengine kwamba kunakuwa na uhai mwingine baada ya kufa. Biblia inaitaja mitengano iliyokuwako kati ya Wasadukayo na Wafarisayo wakati wa mitume. (Matendo 23:7-10) Kitabu The Concise Jewish Encyclopedia kinasema hivi: “Mkazo uliokuwa kati ya makundi hayo mawili hata ulitokeza mauaji ya watu wengi sana na ukatokeza vita ya wenyewe kwa wenyewe.”
5 Wazelote walikuwa madhehebu nyingine ya Kiyahudi iliyokuwako katika karne ya kwanza W.K. Wao walikuwa watukuzaji taifa wa kijeshi waliochochea sana maasi ya Kiyahudi yaliyofanikiwa dhidi ya Waroma katika mwaka wa 66 W.K. Baada ya hapo wakajaribu kuzitawala madhehebu zile nyingine zilizokuwa na silaha katika Yerusalemu, na hivyo wakasababisha vita ya wenyewe kwa wenyewe na taabu nyingi. Magombano hayo ya kutumia silaha kati ya madhehebu za Kiyahudi zenye uadui yaliendelea moja kwa moja mpaka Waroma walipofanya mazingiwa ya mwisho kuuzunguka Yerusalemu. Na hata wakati wa mazingiwa hayo, yale magombano ya Kiyahudi yaliendelea mpaka Yerusalemu ukaja kuharibiwa na Waroma hao mwaka wa 70 W.K. Ni wazi kwamba Wayahudi hawakupata faida yo yote kwa sababu ya kuwa na migawanyiko ya madhehebu na kukosa uaminifu kwa ibada safi yenye umoja ya yule Mungu mmoja tu, Yehova.
Wakristo wa Kwanza Hawakuwa Madhehebu
6. Kwa sababu gani Wakristo wa kwanza walijiepusha na madhehebu za Kiyahudi?
6 Ni wazi kabisa kwamba Wakristo wa kwanza walijiepusha na magombano ya Kiyahudi kati ya madhehebu zao mbali-mbali. Wao walijua kwamba Wafarisayo na Wasadukayo walikuwa kati ya adui waliomwonea Yesu uchungu mwingi sana. Wafuasi wa Kristo hawangeweza kushiriki wala imani ya Waessene ya kwamba nafsi haiwezi kufa wala kushiriki katika upendezi wao wa maisha ya kukaa kama watawa waliojitenga na watu, wanaojinyima vitu kupita kiasi. Na kwa sababu wao walikuwa watu wasiokuwamo, kwa uhakika hawakufanya ushirika na Wazelote wenye kutukuza taifa lao. (Yohana 17:16; 18:36) Bali, Wakristo waliifuata kwa mazoea ile ibada safi yenye umoja ya yule Mungu mmoja tu wa kweli, kupatana na maneno ambayo Yesu alimwambia mwanamke asiyekuwa Myahudi: “Saa inakuja, nayo saa ipo, ambayo, waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli.”—Yohana 4:23.
7. Yesu na Paulo walisema nini, na maneno yao yanaonyesha nini juu ya ibada ya kweli ya Kikristo?
7 Akinena kwa ajili ya Wakristo wa kweli, mtume Paulo alisema hivi: “Lakini kwetu sisi Mungu ni mmoja tu, aliye Baba, ambaye vitu vyote vimetoka kwake, nasi tunaishi kwake; yuko na Bwana mmoja Yesu Kristo, ambaye kwake vitu vyote vimekuwapo, na sisi kwa yeye huyo.” (1 Wakorintho 8:6) Ukristo wa kweli una maana ya kumwabudu kwa umoja yule Mungu mmoja tu, aliye Baba, yaani, Yehova, kupitia yule Bwana mmoja, Yesu Kristo. Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Kiongozi wenu ni mmoja, naye ndiye Kristo.”—Mathayo 23:10.
8. Kwa sababu gani Wakristo wa kwanza hawangeweza kuitwa madhehebu kwa kufaa?
8 Ni kweli kwamba washiriki wa madhehebu za Kiyahudi zilizokuwa zimeanzishwa zamani waliwaita Wakristo wa kwanza madhehebu (Kigiriki: hai’resis, maana yake “kundi la watu wenye kujitenga na watu wale wengine na kufuata imani zao wenyewe”). (Matendo 24:5; 28:22) Lakini wakati mtume Paulo alipokuwa akijitetea mbele ya Gavana Feliki, yeye alilikataa jina baya hilo, akisema: “Kulingana na ile njia ambayo wao [adui zake wa kidini] wanaiita ‘madhehebu,’ katika njia hii mimi ninatoa utumishi mtakatifu kwa Mungu wa babu zangu.” (Matendo 24:14, NW) Kwa vyo vyote Wakristo hawangeweza kuitwa madhehebu, kwa maana walikuwa wakimfuata Yesu Kristo, si mwanadamu ye yote. Tena, wao kwa uhakika hawakuwa chipukizi lililotokana na moja ya madhehebu za dini ya Wayahudi zilizokuwako katika karne ya kwanza W.K.
Hakuna Migawanyiko ya Madhehebu
9, 10. (a) Kwa sababu gani Ukristo haukukusudiwa uvunjike-vunjike uwe makanisa na madhehebu zilizotengana? (b) Ni mafundisho gani juu ya mianzo ya Ukristo yaliyo ya uongo kabisa?
9 Ukristo wa kwanza haukuwa madhehebu. Wala haukukusudiwa uvunjike-vunjike uwe madhehebu zilizo mbali mbali. Alipokuwa akimpelekea Baba yake sala, Kristo aliomba kwamba wanafunzi wake “wote wawe na umoja.” (Yohana 17:21) Wanafunzi wake walipaswa ‘kupendana.’ (Yohana 13:35) Jambo hilo liliondoa nje hatua yo yote ya kuanzisha madhehebu zenye kugawanya watu.
10 Uhakika huo unaonyesha uongo wa mafundisho yanayokaziwa na wanahistoria na wanadini wengi kuhusu namna mbalimbali za Ukristo. Wanataja “Ukristo wa Kiyahudi” (unaosemwa kwa kudhaniwa kwamba ulitetewa na Yakobo, Petro na Yohana) ukiwa tofauti na “Ukristo wa Mataifa” (unaosemwa kuwa ulitetewa na Paulo). Wanataja “mafundisho ya kidini ya Yohanine [Yohana] na “mafundisho ya kidini ya Pauline [Paulo],” wakidai kwamba Ukristo usingalienea kamwe ulimwenguni pote kama Paulo asingaliubadili kabisa. Mafundisho hayo yanatokezwa na watu ambao ama hawana imani yo yote katika Ukristo ama ambao wanauona kuwa jambo sawa tu ule mgawanyiko wa Jumuiya ya Wakristo wa kuwa na mamia ya makanisa na madhehebu,
11. (a) Ni maandiko gani yanayothibitisha kwamba si Paulo aliyeanzisha wazo la kueneza Ukristo kwa watu wasiokuwa Wayahudi? (b) Je! Paulo alikubali kuwe na madhehebu zenye migawanyiko? (c) Ni kisa gani kinachoonyesha Paulo alikuwa na umoja na wafanya kazi wenzake?
11 Mambo ya uhakika yanaonyesha habari tofauti. Kabla Paulo hajawa Mkristo, Yesu Kristo aliagiza wanafunzi Wake wawe mashahidi Wake katika mataifa yote, (Mathayo 28:19, 20; Matendo 1:8) Paulo mwenyewe alipigana na elekeo lo lote la kufuata wanadamu, naye akasema: “Pasiwe kwenu faraka [migawanyiko, NW].” (1 Wakorintho 1:10-15; 3:3-5) Kwa hiyo ni kazi bure kabisa kudai kwamba Paulo alikuwa na wazo tofauti juu ya Ukristo, lenye kutofautiana na la Yakobo, Petro na Yohana. Wote walikuwa wameungana kwa umoja katika ile kazi ya kuzieneza habari njema. Pindi moja, labda wakati ule kulipokuwa na baraza la kuzungumza juu ya tohara katika Yerusalemu mwaka wa 49 W.K., watu hao wanne walifanya ushirikiano wa kukubaliana kabisa juu ya kuligawa-gawa shamba la mahubiri.—Wagalatia 2:7-9.
Maonyo ya Kupinga Ukosefu wa Umoja
12. Je! uadui wo wote ulibaki kati ya Paulo na Petro?
12 Ni jambo la kutazamiwa kwamba, kwa kuwa Wakristo wa kwanza walikuwa wanadamu wasiokamilika—wengine wao hata wakiwa na madaraka mazito ya kikundi—walikuwa na hali zenye kutofautiana. Katika Antiokia ya Shamu, Paulo alimnyosha Petro juu ya jambo fulani. (Wagalatia 2:11-14) Lakini je! Petro alienda zake akaanzisha madhehebu iliyojitenga, kama kwamba hakukubaliana na ule uitwao Ukristo wa Paulo? Hakufanya hivyo hata kidogo, kwa maana miaka mingi baadaye, karibu na mwaka wa 64 W.K., yeye alimtaja Paulo kwa kutumia maneno ya upendo.—2 Petro 3:15, 16.
13, 14. (a) Paulo aliipanga “migawanyiko” na “madhehebu” kati ya mambo gani? (b) Kulingana na Paulo, wenye kuleta madhehebu kati ya watu wanapaswa kufanywa nini?
13 Kwa kuongozwa na Mungu Paulo alipanga “migawanyiko” na “madhehebu” kati ya “kazi za mwili.” Yeye aliandika hivi: “Sasa kazi za mwili ziko wazi, na hizo ni uasherati, uchafu, mwenendo mpotovu, ibada ya sanamu, kuzoea kupashana habari na mashetani, tabia za uadui, ugomvi, wivu, hamaki, magombano, migawanyiko, madhehebu . . . Wale wanaozoea mambo ya namna hiyo hawatarithi ufalme wa Mungu.”—Wagalatia 5:19-21, NW.
14 Kwa kuwa wale wanaosababisha “migawanyiko” na “madhehebu” “hawatarithi ufalme wa Mungu,” hawawezi kuachiliwa ndani ya kundi la kweli la Kikristo. Basi, Paulo alimwandikia Tito hivi: “Lakini maswali ya upuzi ujiepushe nayo, na nasaba, na magomvi, na mashindano ya sheria. Kwa kuwa hayana faida, tena hayana maana. Mtu [anayeendeleza madhehebu], baada ya kumwonya mara ya kwanza na mara ya pili, mkatae; ukijua ya kuwa mtu kama huyo amepotoka, tena atenda dhambi, maana amejihukumu hatia yeye mwenyewe.”—Tito 3:9-11.
Umoja wa Kuamini
15, 16. (a) Kwa sababu gani migawanyiko ya mawazo hairuhusiwi ndani ya kundi la Kikristo, naye Paulo anasema nini juu ya jambo hilo? (b) Je! maana yake ni kwamba Mkristo hapaswi kutumia uwezo wake wa kufikiri? (c) Petro, Yuda na Paulo wanasema nini juu ya hatari ya mtu kutia mashaka na kupotoshwa aiache njia ya kweli?
15 Kutokana na mambo yote yaliyotangulia kutajwa, ni wazi kwamba Ukristo wa kweli hauwezi kugawanywa uwe dini mbalimbali wala madhehebu mbalimbali. Hata hakuwezi kuwako maelekeo wala migawanyiko ya mawazo ndani ya kundi la Kikristo wakati ule ule mmoja. Paulo aliwaandikia Wakorintho hivi: “Basi ndugu, nawasihi, kwa jina la Bwana wetu Yesu Kristo, kwamba nyote mnene mamoja; wala pasiwe kwenu faraka, bali mhitimu katika nia moja na shauri moja.”—1 Wakorintho 1:10.
16 Hiyo haimaanishi kwamba shahidi wa Yehova aliye Mkristo wa kweli hawezi kutumia majaliwa aliyo nayo ya kufikiri. Mtume Petro alihimiza kuwe na matumizi ya “uwezo wa kufikiri waziwazi” katika kuwakanusha “wadhihaki” ambao wangetokea “katika siku za mwisho” wakane “kuwapo” kwa Kristo. (2 Petro 3:1-4, NW) Katika barua yake, Yuda anataja “wengine walio na shaka.” (Yuda 22) Lakini wala Petro wala Yuda hasemi kwamba Mkristo anaweza kubaki akiwa mdhihaki au mtia mashaka. Petro anatuambia ‘tujihadhari’ na watu “wasio imara” ambao ‘wanapotoa Maandiko.’ (2 Petro 3:16 ,17, NW) Na Yuda anasema kwamba watiaji wa mashaka wamo katika hatari na wanahitaji ‘kunyakuliwa katika moto.’ (Yuda 23) Wale ambao wamepotezwa wakaacha njia ya kweli wanahitaji kusaidiwa “kwa upole,” kwa tumaini la kwamba ‘watapata tena fahamu zao, na kutoka katika mtego wa Ibilisi.’—2 Timotheo 2:23-26.
17. Mkristo wa kweli atatumia uwezo wake wa kufikiri kwa njia gani, naye atajitahidi kwa bidii nyingi afanye nini?
17 Mkristo wa kweli anatumia ‘uwezo wake wa kufikiri waziwazi’ kwa njia ya unyenyekevu. Paulo anaandika hivi: “Nawasihi . . . mwenende kama inavyoustahili wito wenu mlioitiwa; kwa unyenyekevu wote na upole, kwa uvumilivu, mkichukuliana katika upendo; na kujitahidi kuuhifadhi umoja wa [roho] katika kifungo cha amani. Mwili mmoja na [roho moja], kama na mlivyoitwa katika tumaini moja la wito wenu. Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja. Mungu mmoja, naye ni Baba wa wote, aliye juu ya yote na katika yote na ndani ya yote.”—Waefeso 4:1-6.
Namna Umoja Unavyopatikana na Kudumishwa
18. Ni nini maana ya maneno haya (a) “Mungu mmoja”? (b) “Bwana mmoja”? (c) ‘roho moja’? (d) Ni nini kiongozi kimoja tu cha Ukristo kilichoandikwa?
18 Paulo alimtaja “Mungu mmoja . . . aliye juu ya yote.” Au, ni kama vile Musa alivyoeleza: “[Yehova], Mungu wetu, [Yehova] ndiye mmoja.” (Kumbukumbu la Torati 6:4) Kweli hiyo ya msingi haijabadilika hata kidogo. Hilo ndilo jambo kuu linaloleta umoja wa Kikristo. Kuna Mungu mmoja na njia moja inayokubalika ya kumwabudu yeye, “katika roho na kweli.” (Yohana 4:23, 24) Yule “Bwana mmoja ni Yesu Kristo, aliye “kichwa cha mwili, yaani, cha kanisa.” (Wakolosai 1:18) Ile ‘roho moja’ ni kani (nguvu) ya utendaji ya Yehova ambayo inaleta mwungano wa umoja. Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Yule msaidizi, ile roho takatifu, ambayo Baba atapeleka katika jina langu, hiyo itawafundisha ninyi mambo yote na kuwakumbusha mambo yote niliyowaambia. Mimi nawaachia ninyi amani, mimi nawapa ninyi amani yangu.” (Yohana 14:26, 27, NW) ‘Mambo waliyokumbushwa yaliandikwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Maandiko hayo, pamoja na Maandiko ya Kiebrania, yanakuwa ndiyo Biblia, ambayo ndiyo kiongozi kimoja tu kilichoandikwa cha Ukristo wa kweli.
19. Ule “mwili mmoja’’ ni nini, na ni nani amewekwa awape washiriki wote wa mwili huo chakula kile kile kimoja cha kiroho?
19 “Mwili mmoja” ndilo kundi la Kikristo, ambalo Yesu ndiye “kichwa.” (Waefeso 1:22, 23) Washiriki mmoja mmoja waliopakwa mafuta wa kundi hilo lenye umoja wangepokea wote chakula kile kile cha kiroho. Kwa kusudi hilo, “bwana” wao aliweka jamii ya “wakili mwaminifu” yenye jumla ya watu wengi, yaani, kundi la Wakristo waliopakwa mafuta waliopo duniani tangu Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. Kwa kuwa “bwana” aliwakuta waliobaki wa kundi hilo wakitoa “posho” kwa uaminifu na kwa akili wakati alipofika kuwakagua mwaka wa 1919, yeye aliwaweka “juu ya vitu vyake vyote.” (Luka 12:42-44) Mambo ya uhakika yanaonyesha kwamba tangu mwaka wa 1919 “wakili” huyo ametunza kwa uaminifu “vitu” hivyo.
20. (a) Kwenye Isaya 65:11, 13, ni tofauti gani inayotajwa kati ya watu wa Mungu na waasi-imani wa kidini? (b) Ni nini kilichouongeza sana umoja wa watu wa Yehova?
20 Viongozi wa kidini wa makanisa na madhehebu zilizo nyingi sana za Jumuiya ya Wakristo hawakupatikana wakigawa “posho” (chakula) ya kiroho inayofaa kwa kundi la watumishi. Basi, mapadri hao na makundi yao wana “njaa” ya kiroho. (Isaya 65:11, 13) Kwa upande mwingine, yule “wakili mwaminifu” ameendelea kutayarisha wingi wa “posho kwa wakati wake” kwa ajili ya Wakristo mmoja mmoja waliopakwa mafuta, na tangu mwaka wa 1935 ameufanyia hivyo “mkutano mkubwa” unaoendelea kuongezeka wa “kondoo wengine.” (Ufunuo 7:9, 10; Yohana 10:16) Bila kujali ni wa lugha gani au wanakaa wapi, mashahidi hao wote wa Yehova wanafuata ulimwenguni pote mpango ule ule mmoja wa kujifunza Neno la Mungu. Kufanya hivyo kumeuendeleza sana umoja ulio kati yao na kumeudumisha.
Umoja Mzuri Ajabu wa Watu wa Yehova
21. Umoja unadumishwa namna gani kati ya Mashahidi wa Yehova leo, na jambo hilo linalinganaje na mpango wa kitengenezo katika siku za mitume?
21 Ule umoja wa makundi karibu 45,000 ya Mashahidi wa Yehova yaliyo katika nchi zaidi ya 200 unadumishwa pia kupitia njia zao za Kimaandiko na kitengenezo. “Mitume na wanaume wazee katika Yerusalemu” ndio waliokuwa baraza lenye kuongoza kwa ajili ya kundi la Kikristo la karne ya kwanza. (Matendo 15:2, NW) Wazee hao na wawakilishi wao waliweka “waangalizi” na watumishi wa huduma” katika makundi na wakafanya maamuzi mengine ya usimamizi. (Wafilipi 1:1; Tito 1:5; Matendo 14:23; 16:4, NW) Vivyo hivyo leo, kikundi cha wazee wa Kikristo waliopakwa mafuta ndio walio Baraza Lenye Kuongoza la Mashahidi wa Yehova. Na sawasawa na vile makundi yalivyopashwa habari za maamuzi ya baraza lenye kuongoza katika karne ya kwanza, ndivyo leo makundi ya Mashahidi wa Yehova yanavyopokea maagizo kutoka Baraza Lenye Kuongoza na kupata ziara za waangalizi wanaosafiri. (Matendo 15:22, 23, 30) Kama ilivyokuwa wakati huo, sasa ‘makundi yanaendelea kutiwa nguvu katika ile imani, na hesabu yao inaongezeka kila siku.’—Matendo 16:5.
22. Mashahidi wa Yehova wanathamini nini hasa, nao wataendelea kufanya nini wakiwa wameungana kwa umoja?
22 Mashahidi wa Yehova wamekombolewa kutoka ile migawanyiko ya madhehebu ya Jumuiya ya Wakristo. Wakiwa chini ya mwelekezo wa “Bwana mmoja” wao, Yesu Kristo, na “wakili” wake, wao wanasonga mbele kwa umoja wakizitangaza “habari njema hizi za ufalme.” (Mathayo 24:14, NW) Wao wataendelea “kwa bidii nyingi kujitahidi kuushika umoja wa roho katika kifungo chenye kuunganisha cha amani.” Kwa kweli, wao ‘wanasimama imara katika roho moja, kwa moyo mmoja wakiishindania imani ya Injili.’—Waefeso 4:3, NW; Wafilipi 1:27.—Kutoka w9/15/83.
Wewe Unakumbuka Mambo Haya?
◻ Ni ibada ya namna gani iliyokuwa kwanza katika Israeli wa kale?
◻ Kuanzia karne ya nne K.W.K. na kuendelea, ni jambo gani lililotukia kati ya Wayahudi waasi-imani?
◻ Ni maandiko gani yanayoonyesha kwamba Ukristo haukukusudiwa kamwe kuwa wa madhehebu yaliyogawanyika?
◻ Biblia inaonyeshaje kwamba migawanyiko mbalimbali ya mawazo hairuhusiwi ndani ya kundi la Kikristo?
◻ Ni mambo gani yanayoshiriki kuleta umoja wa ufahamu na utendaji wa kazi kati ya Mahahidi wa Yehova?
[Picha katika ukurasa wa 17]
Mashahidi wa Yehova wameungana kwa umoja katika ibada yao ulimwenguni pote