Mamilioni Wanajitayarisha kwa Uzima Usiokatizwa Hapa Duniani
1. (a) Sasa ndio wakati unaofaa mamilioni ya watu wakumbuke maneno gani ambayo Yesu alimwambia Martha wa Bethania? (b) Ni sehemu gani ya maneno hayo mamilioni ya watu wanasisimukia sasa, na kwa sababu gani?
KWA mamilioni ya watu walio hai sasa huu ungekuwa ndio wakati wenye kufaa zaidi wakumbuke maneno ambayo Yesu Kristo alimwambia Martha wa Bethania: “Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi; naye kila aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele.” (Yohana 11:25, 26) Kwa yale mamilioni ya watu wanaotafuta uzima usio na mwisho katika ulimwengu wenye uadilifu, ni jambo lenye kusisimua sana kufahamu kwamba wakati wa sasa ndipo maneno haya ya Yesu yanapotumika: “Naye kila aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele.”
2. (a) Alipokuwa angali duniani, Yesu Kristo alikuwa “ufufuo” kwa watu gani mmoja mmoja? (b) Katika maneno ambayo Yesu alimwambia Martha, yeye alikuwa akielekeza hasa kwenye wakati gani, na kwa sababu gani angelazimika kuwa “uzima” hata kwa mamilioni ya watu ambao wangekuwa hai wakati huo?
2 Hata Yesu alipokuwa angali duniani, yeye alikuwa “ufufuo” kwa Lazaro na watu wengine aliowafufua. Lakini maneno hayo yake aliyoyanena muda mfupi tu kabla hajamfufua Lazaro yalihusu zaidi wakati wa mbali uliokuwa ukija tangu hapo. Yesu alielekeza kwenye wakati ambao angekuwa ufufuo na uzima si kwa wafuasi wake tu ambao wangekuwa warithi pamoja naye katika Ufalme wa kimbingu bali pia kwa wanadamu-wafu watakaopata uzima wa milele juu ya dunia yetu wakiwa chini ya Ufalme wake. Yesu angehitaji kuwa “uzima” hata kwa wale ambao wangekuwa hai duniani wakati wa Ufalme wake, wale ambao hawangehitaji kufufuliwa kutoka kaburi la kidunia. Kwa sababu gani? Kwa sababu bado wao wangekuwa chini ya laana ya kifo kutokana na udhambi wao waliourithi kwa Adamu asiyekuwa mtiifu. Kwa hiyo wangekuwa bado katika hali ya kufa.—Warumi 5:12.
3. Yesu Kristo anakuwa “uzima” kwa watu walio hai sasa kwa sababu wanajizoeza sifa gani, na sifa hiyo inazoewaje leo?
3 Mfalme Yesu Kristo anayetawala anakuwa “uzima” kwa watu wanaoishi sasa duniani, kwa sababu wao wanamwamini yeye na wanathibitisha imani yao kwa matendo. Wakati wa huu “umalizio wa mfumo wa mambo,” matendo hayo yangetia ndani kushiriki kwa bidii katika utimizo wa unabii wa Yesu ulio kwenye Mathayo 24:14 wa kuzihubiri habari njema za Ufalme wa Mungu kabla “ule mwisho” wa mfumo huu haujaja. (Mathayo 24:3; Marko 13:3, 4, NW) Wenye kujizoeza imani ambao wataokoka mwisho wa mfumo wa sasa wa mambo na wanaotazamia uzima katika Paradiso itakayorudishwa hawatahitaji kamwe kufa hata siku moja. (1 Yohana 2:17) ‘Watazirudia siku za ujana wao,’ ndiyo, warudie ukamilifu wa kibinadamu unaolingana na ule ambao yule mtu wa kwanza, Adamu, alikuwa nao. Sisi tuna msingi wa kuamini kwamba leo kuna mamilioni ya watu walio hai walio na uwezekano wa kuwa na uzima usio na mwisho hapa duniani.
4. (a) Unabii wa Yesu unaonyeshaje msingi ambao watu wanaweza kutumia wapate uzima usio na mwisho hapa duniani? (b) Ni nini “mwili” utakaookolewa uingie katika mfumo mpya wa mambo?
4 Yesu alitoa msingi wa kuwa na tumaini hilo alipotoa unabii wake kuhusu wakati wa taabu isiyo na ulinganifu ambayo ingeukomesha ule “umalizio wa mfumo wa mambo.” Alisema hivi: “Kwa kuwa wakati huo kutakuwapo dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe. Na kama siku hizo zisingalifupizwa, asingeokoka mtu ye yote [hakuna mwili ambao ungeokoka NW]; lakini kwa ajili ya wateule zitafupizwa siku hizo.” (Mathayo 24:21, 22) Kwa hiyo siku za “dhiki kubwa” zitafupishwa na kwa sababu hiyo “mwili” fulani wa kibinadamu utaokolewa uingie katika ule mfumo mpya wa mambo. Hasa mwili huo ungekuwa ni wa watu wengine ambao si wale “wateule” watakaokuwa wangali duniani wakingojea utukuzo wao waingizwe katika Ufalme wa kimbingu wawe pamoja na Yesu Kristo. Baada ya kuiokoka “dhiki kubwa, mwili huo ‘uliookolewa’ utauingia mfumo mpya wa mambo uwe chini ya utawala wa yule atakayekuwa Baba wa Milele wao.—Mathayo 24:31; Marko 13:20, 22, 27; Ufunuo 17:14; Isaya 9:6, 7.
Hatari Inatokezwa na Mnyama-Mwitu
5. Ni kitu gani ambacho Mwana-Kondoo aliyekalia kiti cha enzi alionekana akiwa nacho, na ni majina ya nani yasiyoandikwa katika kumbukumbu hilo?
5 Ni jina la nani litakalopatikana limeandikwa katika “kitabu cha kukunjwa cha uzima” ambacho kinatajwa kwenye Ufunuo 17:8 (NW)? Ni jina lako? Ni langu? Ili kututangazia sisi onyo la wakati wake, mstari huo unasema hivi: “Yule mnyama-mwitu ambaye wewe [Yohana] uliona alikuwako, lakini hayuko, na hata hivyo yu karibu kupanda atoke katika lile shimo refu sana, na yeye ataenda zake akaingie ndani ya uharibifu. Na wakati wao wanapoona namna huyo mnyama-mwitu alivyokuwako, lakini hayuko, na hata hivyo atakuwapo, wale wanaokaa juu ya dunia watashangaa kwa mshangao wa kupendezwa, lakini majina yao hayakuandikwa juu ya kile kitabu cha kukunjwa cha uzima.”
6. (a) Ni wakati gani “mnyama-mwitu” wa mfano aliposhuka akaingia ndani ya lile shimo refu, naye alitokea akiwa namna gani? (b) Ni mwendo gani wa hatari unaohitaji kuepukwa?
6 “Mnyama-mwitu” huyo wa mfano alijulikana hapo kwanza kwa jina Ushirika wa Mataifa. Alishuka akaingia ndani ya shimo refu sana la kutokutenda wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili ya miaka 1939-45 kisha akapanda kwa kutoka humo shimoni akiwa Umoja wa Mataifa baada ya vita hiyo. Kwa hiyo tangu mwaka wa 1945 hali yenye hatari ipo ambayo inaweza kupata mtu anayetafuta kupata uzima wa milele katika dunia-Paradiso. Huenda huyo akadanganywa aingie katika mwendo utakaomwondoa kuwa asiyestahili kuandikwa jina lake katika “kitabu cha kukunjwa cha uzima.” Hivyo, sasa sisi tunahitaji kutumia “akili zenye hekima” katika nia tunayoonyesha kumwelekea “mnyama-mwitu” huyo wa mfano.—Ufunuo 17:9, NW.
7. (a) Mnyama-mwitu wa rangi nyekundu sana wa Ufunuo sura ya 17 anaitwa nini katika Ufunuo sura ya 13? (b) Ni kwa njia gani “sanamu ya yule mnyama-mwitu” ni kifano cha yule mnyama-mwitu wa kwanza, na vichwa saba vyake vinafananisha nini?
7 “Mnyama-mwitu” huyo wa mfano wa Ufunuo sura ya 17, ambaye anaelezwa kuwa mwenye rangi nyekundu sana, kwa kweli ni nakili ya yule “mnyama-mwitu” wa kwanza anayetajwa katika Ufunuo sura ya 13. Mnyama -mwitu huyo wa rangi nyekundu sana anathibitika kuwa kile kinachoitwa “sanamu ya yule mnyama-mwitu.” (Ufunuo 17:3; 13:14-18, NW) Hiyo “sanamu ya yule mnyama-mwitu” ina vichwa saba sawasawa na kifano chake, na vichwa hivyo vina maana ya “wafalme saba.” Wale “wafalme” watano wa mfano waliokuwa wameanguka walifananisha serikali kubwa za ulimwengu za Misri, Ashuru, Babulonia, Mwungano wa Wamedi na Waajemi na Milki ya Ugiriki iliyoanzishwa na Aleksanda Mkuu. “Mfalme” wa sita alikuwa Milki ya Kiroma ya siku za mtume Yohana. “Mfalme” wa saba ambaye angekuja baada ya wakati wa Yohana amethibitishwa kihistoria kuwa ni Serikali Kubwa ya Ulimwengu ya Mwungano wa Waingereza na Waamerika. Halafu “mfalme” wa nane, yule mnyama-mwitu wa rangi nyekundu sana alitokea kwa mara ya kwanza akiwa Ushirika wa Mataifa, akiwa “sanamu” ya mnyama-mwitu yule wa kwanza.—Ufunuo 17:9-14.
8. (a) Zile “pembe kumi” za mnyama zinafananisha nini? (b) Ni kwa muda gani “pembe kumi” zitatawala zikiwa wafalme pamoja na mnyama-mwitu wa mfano, na ni jambo gani litakalowapata wale wanaoshangaa mshangao wa kupendezwa na mnyama huyo?
8 Kwa habari ya “pembe kumi” zilizo juu ya vile vichwa saba vya mnyama-mwitu wa rangi nyekundu sana, hizo zinafasiriwa kuwa “wafalme kumi,” ndiyo kusema, tawala zote za kisiasa zinazowakilishwa na wajumbe katika tengenezo la Umoja wa Mataifa. “Wafalme” hao watafurahia kuwa na fahari au mamlaka ya kilimwengu kwa muda mfupi tu, tunaweza kusema kwa “saa moja.” Hiyo pia inamaanisha kwamba wale wote wanaoshangaa mshangao wa kupendezwa kwa sababu ya kufufuliwa kwa “sanamu ya yule mnyama-mwitu” na kuiunga mkono watakuwa na kipindi kifupi tu cha ziada. Watu hao hawaandikwi majina yao juu ya kile “kitabu cha kukunjwa cha uzima.” Kwa hiyo wale wasiotaka kufa wamalizike katika dunia yetu hawatajiunga na watu hao kuiabudu “sanamu ya yule mnyama-mwitu.”
9. Ni foleni gani za vita zinazotayarishwa sasa, na matokeo ya vita yatakuwa nini?
9 Sasa foleni za vita zimeanza kuwekwa. Zile “pembe kumi” zimejiweka tayari kushambulia. Andiko la Ufunuo 17:14 linasema: “Hawa watafanya vita na Mwana-Kondoo, na Mwana-Kondoo atawashinda, kwa maana Yeye ni Bwana wa Mabwana, na Mfalme wa Wafalme; na hao walio pamoja naye ndio walioitwa, na wateule, na waaminifu.” Hiyo inaonyesha kwamba mabaki ambao wangali hai duniani wa waaminifu hao walioitwa na kuteuliwa (kuchaguliwa) wataelekeana na shambulio la zile “pembe kumi.” Lakini, “pembe kumi” hizo zitashindwa na Mwana-Kondoo, hiyo ikiwa na maana ya kwamba “sanamu ya yule mnyama-mwitu” ‘itaenda zake ikaingie ndani ya uharibifu.’ (Ufunuo 17:8, NW) Wenye kumwendeleza, wenye mshangao wa kupendezwa juu ya mnyama-mwitu huyo na wenye kumwunga mkono pia watapatwa na uharibifu. Majina yao hayapatikani kuwa yameandikwa juu ya “kitabu cha kukunjwa cha uzima.”
10. Bado ni lazima mabaki ya walioitwa na kuchaguliwa wajithibitishe kuwa nini?
10 Ijapokuwa sasa waliosalia kati ya waaminifu walioitwa na kuchaguliwa ni wachache, wao hawana woga. Hata wakiwa wachache hivyo ni lazima wajithibitishe kuwa waaminifu mpaka Kristo atakapomaliza ushindi wake juu ya “sanamu ya yule mnyama-mwitu” na mnyama-mwitu mwenyewe pamoja na wote wenye kumwabudu duniani. Huo ndio utakaokuwa mwisho wa ulimwengu huu! Lakini ingawa ulimwengu utakwisha, jamaa ya kibinadamu itaendelea kuwako!
Kwa Sababu Gani Isemwe “Mamilioni ya Walio Hai Sasa”?
11. Tangazo la kwamba “Mamilioni walio hai sasa hawatakufa kamwe wamalizike katika dunia yetu” halitegemei nini, lakini kuna sababu gani za kutazamia kwamba hawatakufa?
11 Tangazo lenye kushangaza sana la kwamba “Mamilioni ya walio hai sasa hawatakufa kamwe wamalizike katika dunia yetu” halitegemei njia ya kibinadamu tu ya kufanya hesabu, kama ile ya kusema kutakuwa na mwokokaji mmoja kati ya kila watu 1,000 wanaoishi sasa duniani. Yehova Mungu, aliye Chanzo cha uhai haamui mambo ya maana sana kwa kutegemea msingi wa namna hiyo! Yeye hakuamua mambo kwa njia hiyo wakati wa Gharika iliyoukomesha ulimwengu wa siku za Noa. Hata leo haamui mambo kwa njia hiyo! Kuna sababu thabiti za Kimaandiko za kuyatazamia “mamilioni ya walio hai sasa” yaokoke.
12. Ni akina nani katika mwaka wa 1935 waliokuwa wamejitayarisha kusimama upande wa waaminifu walioitwa na kuchaguliwa, nao walionyesha wazi namna gani msimamo wao?
12 Miaka minne kabla ya Vita ya Ulimwengu ya Pili kutokea kwa ghafula na kushuka kwa “sanamu ya yule mnyama-mwitu” ndani ya lile shimo refu sana la hali kama ya kifo, Mwana-Kondoo wa Mungu alikuwa na watu wengine pia duniani ambao walikuwa na mwelekeo wa kuja bila mashaka wajipange upande wake katika foleni moja na mabaki ya waaminifu walioitwa na kuchaguliwa. Mwaka wa 1935, wakati wa lile kusanyiko linalostahili kukumbukwa la Mashahidi wa Yehova katika Washington, D.C., watu hao walionyesha kwa uhakika kabisa kwamba wao walisimama upande wa Mfalme wa wafalme na dhidi ya “sanamu ya yule mnyama-mwitu.” Namna gani? Kwa kubatizwa mahali pa waziwazi, wakiwa 840, kuonyesha kwamba wamejiweka wakf kabisa kabisa kwa Yehova Mungu. Walifanya hivyo baada ya ile siku ambayo wakusanyikaji waliisikiliza hotuba yenye kusema “Umati Mkubwa,” yenye kueleza Ufunuo 7:9-17. (Authorized Version) Hivyo walichukua hatua ya haraka wakatumia nafasi ya kwanza wawe sehemu ya huo “umati mkubwa” unaofua mavazi yao katika damu ya Mwana-Kondoo na unaotoka katika “dhiki kubwa” ambayo Mungu anatumia Kristo kuileta juu ya “sanamu ya yule mnyama-mwitu” na wote waliojipanga nayo na “pembe kumi” zake.
13. (a) Kufupishwa kwa siku za “dhiki kubwa” kuna maana gani kwa mabaki ya wachaguliwa? (b) Kwa hiyo ikiwa mabaki ya wachaguliwa watauokoka mwisho wa ulimwengu huu, hiyo inaonyesha nini pia?
13 Hiyo “dhiki kubwa” ‘itafupishwa’ kwa ajili ya wateule wa Yehova, waitwa na wachaguliwa wake. (Mathayo 24:21, 22) Hiyo inamaanisha kwamba mabaki kati yao wataiokoka dhiki hiyo wakawe mashahidi waliojionea kwa macho yao wenyewe tendo la ajabu la Yehova ambalo atalitumia kuitakasa enzi kuu yake juu ya mbingu na dunia. (Isaya 28:21) Kwa kuwa siku za ile dhiki ‘zitafupishwa’ kwa ajili yao, “mwili” fulani utaokolewa kupitia mwisho wa ulimwengu huu wa kale. Ikiwa mabaki wachaguliwa watapata ulinzi wa Yehova kuwahakikishia kwamba wataokoka, vivyo hivyo “umati mkubwa” wa waaminifu waliojiweka wakf na kubatizwa utaokoka ukiwa chini ya ulinzi wa kimungu. Leo wingi ulio mkubwa wa Mashahidi wa Yehova ni washiriki wa huo “umati mkubwa” utakaookoka “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” kwenye hali ya ulimwengu inayoitwa Har–Magedoni, au Armagedoni.—Ufunuo 16:14-16.
14. Washiriki walio katika “umati mkubwa” wanafikia hesabu kubwa namna gani, na hiyo ikoje inapolinganishwa na hesabu ya watu wa ulimwengu?
14 Kwa sasa hesabu ya watu wa ulimwengu inasema kuwa ni watu bilioni 4.6. Tangu mwaka wa 1935 W.K. wale wa “umati mkubwa” wanapaswa kuwa wamekwisha kuongezeka wakawa mamilioni. Je! wanaongezeka? Ilivyo ni kwamba, mabaki wachaguliwa walio maelfu machache wamekuwa ni kama hawaonekani kwa kuzungukwa na mamia mengi ya maelfu ya mashahidi waliobatizwa wa Yehova ambao ni wenye bidii katika ‘kuzihubiri habari njema hizi za ufalme’ duniani pote “kwa ushuhuda kwa mataifa yote.” (Mathayo 24:14, NW; Marko 13:10) Kulingana na tarakimu zinazohesabiwa kwa uangalifu kila mwaka na makao makuu ya Sosaiti na afisi za matawi yake 95, kuna watu zaidi ya milioni 2.4 wanaotenda kwa ukawaida katika kazi aliyoiagiza Yehova ifanywe wakati wa huu “umalizio wa mfumo wa mambo.” Na mkusanyo wa wale wote watakaojumlika wawe ushirika kamili kabisa wa “umati mkubwa” haujamalizika. Mkusanyo wao unapasa kuongezeka! Lakini kwa sasa kipimo kilichopo ni karibu mshiriki mmoja wa ule “umati mkubwa” kwa kila watu 2,000 walio duniani.
15. (a) Kwa sababu gani ni jambo la akili nzuri kutazamia kwamba watu walio hai sasa watauokoka mwisho wa ulimwengu? (b) Kwa sababu gani Mfalme wa mfumo mpya hatakuwa baba yao wa muda mfupi tu?
15 Kufika hapo tulipo umebaki muda mchache wa ile “saa moja” ambayo zile “pembe kumi” za mfano zinatawala zikiwa wafalme pamoja na mnyama yule wa rangi nyekundu sana, yaani, “sanamu ya yule mnyama-mwitu,” tengenezo la Umoja wa Mataifa. Basi, ni jambo la akili nzuri kutazamia kwamba washiriki wa “umati mkubwa” wanaweza kuuokoka uharibifu unaokaribia wa “mnyama-mwitu” wa mfano na “sanamu” yake. Wao watauokoka mwisho wa mfumo huu mbovu wa mambo wakiwa chini ya ulinzi wa Yehova wakaingie katika mfumo mpya wa mambo ya uadilifu. (Ufunuo 7:16, 17) Wakiwa humo hawataiacha njia ya uzima iliyoonyeshwa na Mungu. Kwa hiyo, Yesu Kristo aliye Mfalme atakuwa Baba wa Milele wao.—Isaya 9:6, 7.
Kujitayarisha kwa Uzima Usiokatizwa
16. Ni maneno gani yanayoweza kusemwa sasa kwa uhakika, na ni maneno gani ya Yesu yanayofaa kukumbukwa kufikia hapo?
16 Basi, maneno yanaweza sasa kunenwa kwa usadiki na maono ya mbele yanayofaa kwamba, “Mamilioni ya walio hai sasa hawatakufa kamwe wamalizike katika dunia yetu.” Hapa tena inafaa sana kuyakumbuka maneno ya Yesu ya kushangaza sana: “Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi; naye kila aishiye na Kuniamini hatakufa kabisa hata milele.”—Yohana 11:25, 26.
17. Wale wa “umati mkubwa” wamekwisha kukubali namna gani kwamba wokovu wao unatoka kwa Yehova Mungu na kwa Mwana-Kondoo, na sasa wao wanatumikia Mungu kwa njia inayokubalika wakiwa wapi?
17 Tayari washiriki walio hai wa “umati mkubwa” wanajizoeza imani katika Yule aliye “ufufuo, na uzima.” Kwa kujiweka wakf kwa Yehova Mungu na kuonyesha wakf huo kwa kubatizwa katika maji, wao wanakubali kwamba wokovu wao wote unatoka kwa ‘Mungu aketiye katika kiti cha enzi, na Mwana-Kondoo.’ Wako katika nyua za hekalu la Yehova, wakiwa wamesimama mbele za kiti cha enzi Chake, nao wanakubaliwa kusimama hivyo kwa sababu wamefua mavazi yao na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo, Yesu Kristo.—Ufunuo 7:9, 10, 14.
18. Ni nini sasa wanachoweza kuhesabiwa “umati mkubwa,” nao wanaweza kuonwa kuwa na uhusiano gani na Mungu?
18 Kwa kuwa “umati mkubwa” unahesabiwa hivyo kuwa umejivika uadilifu, sasa wanaweza kuhesabiwa kuwa wanastahili kuwekewa uzima pia. (Warumi 6:13) Wakiwa kama Abrahamu mzee wa ukoo aliyekuwako kabla ya nyakati za Ukristo, ambaye alihesabiwa uadilifu kwa sababu ya imani yake yenye matendo, wao wanaweza kuhesabiwa kuwa ‘rafiki za Mungu.’ (Warumi 4:6-22; Yakobo 2:23; Zaburi 32:3) Kwa sababu wao wanadumisha msimamo wao wa uadilifu mbele za Yehova Mungu, yeye atawahifadhi wawe hai duniani moja kwa moja kupitia “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” kwenye Har–Magedoni, ambayo italeta mwisho wa mfumo huu wa kale wa mambo.
19. (a) Wao hawatahitaji nini hata waje ‘kuwa wanaishi’? (b) Kwa sababu gani ‘hawatakufa’ kamwe?
19 Kwa hiyo waokokaji wa Har–Magedoni hawatahitaji ufufuo kutoka kwa wafu ili ‘wawe wanaishi’ duniani. Maneno ya Yesu yatatimia kwao kwa maana halisi kabisa: “Kila aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele.” (Yohana 11:26) Wakiendelea kuutimiza wakf wao kwa Yehova Mungu bila kuyumba-yumba na kufanya mapenzi yake wanayojulishwa kupitia Mfalme Yesu Kristo, watafikia uadilifu ulio na ukamilifu mwishoni mwa miaka elfu moja ya utawala wa Kristo. Wakiwa chini ya jaribu la mwisho litakaloletwa juu ya wanadamu wote watakaokuwa wamerudishiwa hali inayofaa wakati huo, wao watathibitisha ukamilifu wao wa nafsi yote kwa Mungu Aliye Juu Zaidi kisha majina yao yakae yakiwa yameandikwa katika “kitabu cha kukunjwa cha uzima.”—Ufunuo 20:7-15, NW.
20. Pendeleo lao na mambo watakayokuwa wamejionea yatakuwa hayana kifani namna gani kati ya wale watakaokaa katika dunia-Paradiso, na ni nani anayestahili kupata shukrani zote kwa jambo hilo?
20 Hakika ni pendeleo lisilo na kifani ambalo “umati mkubwa” wa wale “kondoo wengine” wa Mchungaji Mwema wamewekewa mbele! (Yohana 10:16) Tumaini lililowekwa mbele yao—lile la kuishi katika furaha isiyochafuliwa katika bustani ya Edeni itakayorudishwa duniani na kupanuliwa ifike ulimwenguni pote—linavutia sana. Watakuwa na kitu cha kuishilia kweli kweli. Kati ya wanadamu wote watakaokaa juu ya dunia-Paradiso, mambo ambayo hao wengine watakuwa wamejionea hayatakuwa kamwe na kifani, tena yatakuwa tofauti, kwa kuwa watakuwa wameuokoka mwisho wa mfumo huu mbovu wa mambo na kuwa watu ambao hawatakufa kamwe wamalizike katika dunia yetu. Anayepaswa kupigiwa asante kwa ajili ya tukio hilo ni yule Chanzo cha uzima mkamilifu, Yehova Mungu, kupitia Mwana wake, Yesu Kristo.
—Kutoka w10/1/83.
Maulizo ya Kujikumbusha
◻ Ahadi aliyotoa Yesu juu ya ‘kutokufa milele’ inahusu nani?
◻ Mnyama-mwitu wa Ufunuo sura ya 17 ni nini, na mnyama huyo anahusika namna gani katika kujulikana kama watu watapokea au hawatapokea uzima?
◻ Kwa sababu gani ni jambo la akili nzuri kutazamia kwamba watu walio hai sasa watauokoka mwisho wa ulimwengu?
◻ Mungu ana maoni gani juu ya washiriki wa “umati mkubwa,” nao wanahesabiwa nini?
[Picha katika ukurasa wa 15]
Nia uliyo nayo kuelekea “mnyama-mwitu” huyu ina matokeo gani juu ya kuokoka kwako ufurahie uzima wa milele?
[Picha katika ukurasa wa 17]
Mamilioni ya watu hawatakufa kamwe. Wewe unaweza kuwaje mmoja wao?