Kataa Tamaa za Kilimwengu!
1, 2. (a) Yehova anapasa kuabudiwa namna gani? (b) Jambo hilo linataka nini upande wa Mashahidi wake?
YEHOVA MUNGU anastahili kuabudiwa katika njia safi na ya unyofu na wale wote walio wakf kwake. Nyakati zote na katika kila njia, inawapasa wamheshimu yeye kwa maneno na matendo. Kwa uhakika ni lazima waepuke kuwa na “roho ya ulimwengu huu”—maoni yake makuu au nguvu yenye kutendesha yenye dhambi na ya kichoyo, ambayo mara nyingi inakuwa chafu. (1 Wakorintho 2:12, Today’s English Version) Wakiwa ni kundi la watu waliofanywa tengenezo ili wamsifu Mungu, ni lazima Mashahidi wa Yehova waonekane wazi kuwa tofauti na ulimwengu huu. Ni lazima watumie kwa moyo wote agizo la kimungu la ‘kukataa kabisa hali ya kutomcha Mungu na tamaa za kilimwengu na kuishi kwa utimamu wa akili na kwa uadilifu na utawa katikati ya huu mfumo wa sasa wa mambo.’—Tito 2:11-14, NW.
2 Lakini, jambo la kusikitisha ni kwamba si wote wale wanaodai kuwa wanampenda Yehova wamemheshimu sikuzote na kutoa ushuhuda wa wazi wenye kuonyesha kwamba wamezikataa tamaa au njia za kilimwengu. Habari zinaletwa kusema kwamba wanaume fulani wa Kikristo walio wakf walihudhuria karamu yenye sherehe inayowataka wageni wavae vinyago. Basi wanaume hao walivaa vinyago wakaonekana kama wanawake. Je! tabia ya namna hiyo ingeweza kuonwaje kuwa isiyo ya kilimwengu au ya kumpa Yehova heshima? Kwa uhakika, matendo ya namna hiyo siyo yale tungetazamia yatendwe na wale wasio “sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 15:19, NW ) Ni kwamba, chini ya hali zilizo nyingi, mwanamume akivaa nywele-bandia za mwanamke na mavazi ya kike angeonekana kuwa mwenye hali za kike, na zaidi ya hivyo angefungulia wanaume wale wengine njia ya kuja kumtongoza wafanye ngono isiyo ya asili—Kumbukumbu la Torati 22:5.
3. Kwa habari ya njia na tamaa za kilimwengu, ni maulizo gani yanayostahili kuangaliwa?
3 Kwa kuwa sisi ni Mashahidi wa Yehova, huenda tukakubali kwamba haitupasi ‘kuingia kupita kiasi katika mambo ya kilimwengu,’ kama ilivyoonyeshwa katika makala iliyotangulia. (1 Wakorintho 7:31, The New Testament: A New Translation, iliyotayarishwa na Olaf M. Norlie) Huenda tukawa tunatambua kwamba fadhili zisizostahilika za Mungu “zinatufundisha kusema ‘Hapana’ kwa hali ya kutomwogopa Mungu na kwa nyege za kilimwengu.” (Tito 2:11, 12, New International Version; NW ) Lakini namna gani ikiwa moyo wetu hauitikii kwa njia hiyo? Au namna gani ikiwa tunataka sana kutia nguvu azimio letu la kuzikataa tamaa za kilimwengu? Ni nini kinachoweza kutusaidia?
Ombi kwa “Msikiaji wa Sala”
4, 5. (a) Ni mambo gani yanayofaa yanayoweza kuwa katika sala zetu? (b) Kwa habari ya moyo wetu, huenda nyakati nyingine tukahitaji kusali namna gani?
4 Njia moja ya kufanikiwa katika kukataa tamaa za kilimwengu ni kutoa maombi ya bidii na ya ukawaida ya kutaka msaada kwa “Msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2, NW ) Lakini tunaweza kusali namna gani ikiwa moyo wetu unatamani sana vitu vinavyoelekea kidogo kuwa vya kilimwengu?
5 Kwa kuwa sisi ni Mashahidi wa Yehova, inatupasa ‘katika kila neno haja zetu zijulikane na Mungu.’ Tukifanya hivyo kwa imani, “amani ya Mungu” isiyolingana na jambo lo lote italinda akili na moyo wetu. Bila shaka, Yehova mwenyewe alisema kwamba “mawazo ya moyo wa mwanadamu ni mabaya tangu ujana wake.” (Wafilipi 4:6, 7; Mwanzo 8:21) Kwa hiyo nyakati nyingine tunahitaji kusali tupewe nia tofauti, badiliko la moyo. Kwa mfano, ikiwa vivuta-macho vya ulimwengu vinavuta moyo wetu, tunahitaji kumwomba Baba yetu wa kimbingu atusaidie kuweka tamaa za kiroho zinazofaa mahali pa hiyo tamaa nyingine yenye kushawishi.
6. Ikiwa njia za ulimwengu na vivuta-macho vyake vinaelekea kutuvutia sisi hasa, tunaweza kusali namna gani?
6 Karne nyingi zilizopita, mtunga zaburi Daudi alimwomba Mungu hivi: “Unifanye mimi nijue njia zako mwenyewe, Ee Yehova . . . Unifanye mimi nitembee katika kweli yako na unifundishe mimi.” (Zaburi 25:4, 5, NW ) Yehova alimfanyia Daudi hivyo, na kwa uhakika Yeye anaweza kujibu sala ya namna hiyo asaidie watumishi Wake wa ki-siku-hizi. Kwa kuwa “njia” za Yehova na “kweli” yake si za kilimwengu, mawazo yaliyo katika sala ya kutoka moyoni kama ya Daudi yanaweza kusaidia ikiwa njia za ulimwengu huu zinaelekea kutuvutia sisi hasa.
7. Ni mwendo gani wa hekima tunaopaswa kufuata tukivutwa kwenye vitumbuizo vya kilimwengu visivyofaa?
7 Ulimwengu unashikilia maoni ya ufisadi na kutenda uovu kwa wingi. Mara nyingi jambo hilo linaonekana katika nyimbo za kilimwengu, dansi, vitabu, michezo ya kuigiza, sinema, vipindi vya televisheni, na mambo kama hayo. Ikiwa sisi Wakristo tulio wakf tunavutwa kwenye vitumbuizo vya kilimwengu visivyofaa, sasa iweje? Kwanza, itatufaa tutumie Neno la Mungu tuchunguze tuone vitumbuizo hivyo vina ubora gani. Linaonyesha kwamba inatupasa ‘tulichukie lililo ovu, tuambatane na lililo jema.’ (Warumi 12:9) Halafu inatupasa tuombe msaada wa Yehova ili moyo wetu uache kutamani maovu, ujapokuwa ni usiokamilika. Kwa uhakika, Mungu wetu anaweza ‘kuumba ndani yetu moyo safi’ ikiwa tunamwomba atufanyie hivyo tukiwa na unyofu.—Zaburi 51:10, NW.
Msaada Kupitia Roho Takatifu
8. Kulingana na Zaburi 51:11, ni jambo gani linaloweza kutokea ingawa sasa tuna roho takatifu?
8 Daudi Mfalme wa Israeli alipokwisha kuonyeshwa kwa mkazo mwingi uzito wa dhambi aliyofanya pamoja na Bathsheba, yeye alimsihi sana Yehova akimwambia: “usinitupilie mbali mimi kutoka mbele za uso wako; na roho takatifu yako Ee usiiondoe kwangu mimi.” (Zaburi 51:11, NW ) Mungu alijibu sala hiyo. Lakini angalia hapo kwamba roho takatifu inaweza kupotezwa au kuondolewa kwa mtu.
9. Ni kitu gani kingeweza kutuvuta na kutuingiza katika upotovu wa kilimwengu, na matokeo yanaweza kuwa nini?
9 Sisi Wakristo walio wakf tukiruhusu ulimwengu utuvute na kuturudisha ndani ya “ufisadi ule ule usio na kiasi,” huenda tukazama humo kwa njia ya kiroho. (1 Petro 4:4) Huenda jambo hilo likaanza na hamu ya kutaka sana kujua mambo, labda tukianza kulisha akili na moyo mawazo ya ufisadi ya kilimwengu, yenye kupandwa humo na vitabu na namna za vitumbuizo vinavyotilika mashaka. Neno la Mungu linatuhimiza kwamba ‘katika uovu tugeuzwe watoto wachanga,’ bila kutafuta maarifa ya kuyajua mambo ya ufisadi au uovu. (1 Wakorintho 14:20) Lakini hamu ya kutaka sana kujua mambo ingeweza kutuvuta tuingie katika namna nyingi sana za upotovu, na huenda tukakata shauri lisilo la hekima kwamba tumekomaa au tuna nguvu za kiroho za kuweza kushinda uchafu. Halafu huenda tukawa na shingo ngumu kwa kiasi cha kwamba hatutaki mtu ye yote—hata mwishowe tusimtake Mungu—‘atuambie sisi tunalopaswa kufanya.’ Matokeo yanaweza kuwa yenye msiba, kwa kuwa hakuna mtu anayeweza kumkaidi Mungu kwa kuyakataa mashauri yake akiwa na moyo wa kiburi na aweze ‘kutokeza bila jeraha.’—Ayubu 9:1-4, NW.
10. (a) Kwa habari ya roho takatifu, sisi tunaweza kupatwa na nini ikiwa tamaa za kilimwengu zinaachiliwa bila kuzuiwa? (b) Kwa hiyo ni nini kitakachotusaidia tupinge sana ulimwengu na vishawishi vyake?
10 Bila kuzuiwa, tamaa za kilimwengu zinaweza kutufanya tuhuzunishe roho takatifu ya Mungu kwa kuipuza, tufuate mwendo usiopatana na mwongozo wa roho hiyo na kuweka moyo wetu juu ya malengo yanayotofautiana na yale ambayo roho ingetusukuma tuyatimize. ‘Kuhuzunisha roho takatifu ya Mungu’ kunamaanisha pia kulikataa Neno la Mungu. (Waefeso 4:30; linganisha Matendo 7:51-53.) Kufanya hivyo kunaweza kuongoza mtu afanye uasi wa makusudi juu ya udhihirisho wa waziwazi wa roho ya Yehova na kunaweza kumfanya aikufuru (aitukane) roho hiyo, na hiyo ni dhambi isiyosameheka. (Mathayo 12:31, 32; Marko 3:29; linganisha Waebrania 6:4-6; 10:26-31.) Kwa hiyo tusianze kamwe kutelemka kwenye njia ya kujitegemea wenyewe na kujiingiza katika mazoea ya kilimwengu ambayo hapo kwanza tuliokolewa kwa kuondolewa kwayo kupitia fadhili zisizostahilika za Yehova. Bali, acheni tusali tupewe roho takatifu kisha tukubali kufuata maongozi yake, ambayo yatatusaidia tuupinge sana ulimwengu na vishawishi vyake.—Zaburi 143:10; Luka 11:13.
Neno la Mungu Ni Msaada
11. Sasa tutaangalia nini kinachopasa kutusaidia tupinge sana kishawishi cha ‘kuutumia sana ulimwengu’?
11 Kitu kizuri ajabu kilichotokezwa na roho takatifu ya Mungu ni Neno la Mungu lililoongozwa naye. (2 Samweli 23:2; 2 Timotheo 3:16; 2 Petro 1:20, 21) Ndani ya kurasa zalo yamo mambo ‘yaliyotangulia kuandikwa ili kutufundisha sisi’ na ‘mifano yenye kutuonya sisi ambao miisho ya mifumo ya mambo imefika juu yetu.’ (Warumi 15:4, UV; 1 Wakorintho 10:11, NW ) Basi, je! watu fulani wanaotajwa katika maandishi ya Biblia walikuwa na maoni gani juu ya ulimwengu?
12. Dema alikuwa nani, nasi tunaweza kufaidikaje kwa kufikiria mwendo wake?
12 Hata mfano usiopendeza una faida, kwa maana unaonyesha tunalopaswa kuepuka. Kwa mfano: Mtume Paulo aliachwa na Dema mfanya kazi mwenzake ‘kwa sababu huyo aliupenda mfumo wa sasa wa mambo.’ Njia aliyoitumia na kiasi alichofikia kumwacha Paulo havionyeshwi wazi, lakini huenda ikawa kwamba kupenda anasa za kilimwengu na vitu vya kimwili kulikuwa kumezidi sana kupenda mambo ya kiroho. Lo lote liwalo Dema alishindwa kutumia pendeleo lake lililokuwa bora kabisa amtie nguvu Paulo ndugu yake. (2 Timotheo 4:10, NW ) Jamani! jambo hilo linapasa litusukume tuambatane sana na waamini wenzetu, si kuwaacha kwa sababu ya kuruhusu kupenda mfumo wa sasa wa mambo kuujae moyo wetu!
13. Kuna uthibitisho gani wa kwamba Abrahamu na Sara ‘hawakuwa wameingia kupita kiasi katika mambo ya kilimwengu’?
13 Leo tuna Biblia nzima ikiwa kiongozi chetu. Lakini wale wazee wa ukoo wenye kumcha Mungu, akina Abrahamu, Isaka na Yakobo, na wake zao washikamanifu, ‘hawakuutumia sana ulimwengu, ijapokuwa hawakuwa na hata kitabu kimoja cha Biblia kilicho kamili—Mwanzo. Kwa mfano Abrahamu (Abramu) alifanya kama Yehova Mungu alivyomwelekeza kwa kuuacha mji wa Uru, mji wa Kikaldayo wenye makao mazuri na faida nyingi-nyingi. Ndiyo, vitu ambavyo vimechimbuliwa huko vinaonyesha wazi kwamba yeye na Sara (Sarai) mke wake mpendwa walijinyima vitu vya maana sana vya kimwili ili waende walikoelekezwa na Mungu, wakae katika mahema wakiwa wakaaji wa kigeni katika nchi ya ahadi. Isaka na Yakobo pia walitenda kwa imani wakiwa “warithi pamoja [na Abrahamu] wa ahadi ile ile.” Abrahamu hakuhesabu faida za kilimwengu kuwa zenye maana kubwa, “maana alikuwa akiutazamia mji wenye misingi, ambao mwenye kuubuni na kuujenga ni Mungu.”—Waebrania 11:8-10.
14. (a) Inaweza kuonyeshwaje kwamba Musa ‘hakuutumia sana ulimwengu’? (b) Kwa habari ya maoni yetu juu ya faida za kiroho, tunaweza kufaidikaje na mfano wa Musa?
14 Nabii Musa ni mfano mwema mwingine wa mtu aliyetumaini Yehova na kuzikataa tamaa za kilimwengu. Kwa imani, Musa alichagua kutendwa vibaya pamoja na watu wa Mungu na ‘kukadiria shutumu la Kristo [yaani, la kuwa mtumishi mpakwa-mafuta wa Mungu] kuwa mali zilizo kubwa kuliko hazina za Misri.’ Basi, yeye alikuwa na mapendeleo mazuri sana alipokuwa akitumikia kwa uthabiti ‘kama kwamba alikuwa akimwona Yule asiyeonekana,’ Yehova. (Waebrania 11:24-27, NW ) Ni wazi kwamba Musa angaliweza kupata uamuzi wo wote ulio mzuri kuliko ule wa kutanguliza faida za kiroho maishani vijapokuwako vishawishi vyo vyote vya kilimwengu. Wala sisi hatuna uamuzi ulio mzuri kuliko huo.—Mathayo 6:33.
15. Tutasukumwa tuepuke vishawishi vya kilimwengu vya kufanya uasherati tukiangalia jambo gani lililowapata Waisraeli?
15 Vitu vya ulimwengu vitakavyopitilia mbali karibuni ni kutia ndani “tamaa ya mwili,” inayojidhihirisha kwa njia mbalimbali, nyingine zazo zikiwa ni mbovu. (1 Yohana 2:15-17) Vishawishi vya kilimwengu vinavyoelekeza mtu kwenye uasherati ni vingi sana na nyakati nyingine vimefagia hata watu walio wakf kwa Yehova. Kwa mfano, ingawa Waisraeli walikuwa wamekombolewa kutoka utumwa wa Misri, maelfu yao waliuawa baadaye kwa sababu ya ‘kuzini pamoja na wanawake wa Moabu.’ (Hesabu sura ya 25; 1 Wakorintho 10:8) Hakika jambo hilo linapasa kutusukuma sana tuepuke vishawishi vya kilimwengu vya kufanya uasherati!
16. (a) Wakati Yusufu alipojaribiwa atende uasherati, yeye alifanya nini? (b) Sisi tunaweza kufaidikaje na mfano wa Yusufu?
16 Ufikirie mfano mwema wa Yusufu, mwana wa Yakobo. Mke wa bwana wake wa kazi Mmisri alimwomba-omba afanye ngono naye. Lakini, yeye alikataa kwa uthabiti. Haisemwi kwamba mwanamke huyo alikuwa na sura mbaya sana ya kufukuza mwanamume asimkaribie. Hapana, Yusufu alimkimbia kwa sababu hakutaka kutenda dhambi juu ya Mungu wake mwadilifu, Yehova. (Mwanzo 39:7-20) Je! sisi tunahitaji kufanya marekebisho katika usomaji wetu, tafrija au hali ili tuepuke kutenda dhambi juu ya Mungu? Ikiwa ndivyo, na tuyafanye bila kukawia, kama alivyofanya Yusufu mcha Mungu.—1 Petro 2:11,12.
17. (a) Mara nyingi kufikiri kwa njia ya kilimwengu kunakuza maoni gani? (b) Wanawake fulani wa Yuda wenye moyo wa kiburi walijipambaje, na wao walipatwa na nini pamoja na marembo yao?
17 Mara nyingi kufikiri kwa njia ya kilimwengu kunakuza hali ya kujitegemea na kiburi. Ulimwengu unapotia mkazo juu ya kufuatia mambo ya kimwili ya maisha unafikia kukazia mapambo, hilo likiwa ni jambo linaloonwa kuwa la maana sana na wanawake wanaotaka kuwa na sura nzuri. Katika Yuda ya kale ya siku za Isaya, wanawake wenye moyo wa kiburi walijivika marembo mengi. Wanawake hao wenye kiburi walivaa vinyororo vilivyounganishwa na bangili za miguuni. Vinyororo hivyo vilifanya “mlio kama wa kengele” wakati mwanamke alipotembea, na vilimzuia asichukue hatua ndefu-ndefu hata ikawa kwamba alitembea “kwa hatua fupi za kupiga madaha,” akawa na ule unaoweza kusemwa kuwa mwendo wa kike wa kimaringo. Bila shaka, wakati nchi ya Yuda iliposhindwa na Wababuloni mwaka wa 607 K.W.K., marembo hayo na uhuru waliokuwa nao yalikomeshwa.—Isaya 3:16-24, NW.
18. Maandiko yanaweka kiwango gani kwa habari ya mapambo ya kike?
18 Kwa habari ya mapambo ya kike, kulikuwako tofauti kubwa sana ya nia kati ya Yezebeli mkosa-adabu wa kilimwengu na Esta mcha Mungu aliyekuwa na kiasi, ingawa alivaa mavazi kwa njia nzuri! (2 Wafalme 9:30; Esta 2:7; 5:1) Ni wazi kwamba wanawake Wakristo wanataka kuwa kama Esta. Kwa hiyo, wao wanavaa “mavazi yanayofaa, pamoja na adabu na moyo wa kiasi.” Wanafanya mapambo yao makuu yawe ni “mutu wa moyo, asiyeonekana, katika mapambo yasiyoharibika, ndiyo roho ya upole na utulivu iliyo ya damani kubwa mbele ya Mungu.” —1 Timotheo 2:9; 1 Petro 3:3-5, ZSB.
19. Yesu Kristo alikuwaje mfano ulio bora zaidi wa kutokuwa na uulimwengu?
19 Yesu Kristo ndiye mfano bora zaidi wa kutokuwa na uulimwengu. Ingawa yeye alikuwa mwanadamu mkamilifu aliyekuwa na uwezo wa kupata mafanikio ya kilimwengu kuliko mwanadamu mwingine ye yote, hangaikio lake kuu lilikuwa la kiroho—akalifuatia hilo sana hata akawa “hana pa kulaza kichwa chake.” (Mathayo 8:20) Yesu hakutiwa uchafu kiadili na ulimwengu huu hata kidogo, bali inasemwa juu yake kwamba alikuwa “mshikamanifu, asiye na hila, asiyetiwa unajisi, aliyetenganishwa na watenda dhambi.” (Waebrania 7:26, NW ) Sisi tulio watu wasiokamilika hatuwezi kufuata hatua za Yesu kwa ukamilifu. Lakini tunapaswa kufanya yote tuwezayo, kwa msaada wa Yehova.—1 Petro 2:21, 22.
Endelea Kukataa Tamaa za Kilimwengu
20. Ikiwa wewe ni mwabudu wa Yehova, unaweza kuendeleaje kuwa bila roho ya ulimwengu huu?
20 Ikiwa wewe ni mmoja wa wale walio kati ya msongamano wa waabudu wa Yehova wenye furaha, umebarikiwa kweli kweli. Umepata kitu kinachoshinda kwa mbali vitu vyote ambavyo ulimwengu huu unaoendelea kufa unaweza kutolea watu. Basi, ambatana na ibada ya kweli na uendelee kuwa bila roho ya ulimwengu huu. Ili kufanya hivyo, mwombe mara nyingi yule “Msikiaji wa sala,” utafute msaada wa roho takatifu yake, sikuzote ukubali mashauri ya Neno la Mungu wala usiondoke kamwe katika mlolongo wa mashahidi waaminifu wa Yehova ambao umekuwako muda wa karne nyingi.—Linganisha Waebrania 12:1-3.
21. Kwa habari ya ulimwengu huu, tunapaswa kupiga moyo konde tufanye nini?
21 Piga moyo konde usiutumie sana ulimwengu huu. Bali, kaza akili na moyo wako juu ya kufanya mapenzi ya Mungu. Ukifanya hivyo, utapata tegemezo lisiloshindwa la “mikono ya milele” ya Yehova. (Kumbukumbu la Torati 33:27) Ukiwa na uhakika wa kupata msaada huo wa kimungu, endelea kuishi kwa utimamu wa akili, uadilifu na utawa, huku ukikataa ukosefu wa kumcha Mungu na tamaa za kilimwengu.—Kutoka w10/15/83.
Wewe Ungejibuje?
◻ Ikiwa moyo wetu unatamani kidogo vitu vya kilimwengu, sala inaweza kusaidiaje?
◻ Roho takatifu inaweza kutusaidiaje tupinge sana ulimwengu na vishawishi vyake?
◻ Ni mifano gani ya Kibiblia inayoweza kutusaidia tukatae njia na tamaa za kilimwengu?
◻ Tunaweza kuendeleaje kuwa bila roho ya ulimwengu?
[Picha katika ukurasa wa 21]
Usiruhusu hamu ya kutaka kujua namna mambo yalivyo ikuvute uingie katika upotovu wa kilimwengu
[Picha katika ukurasa wa 23]
Yusufu alikimbia aepuke kutenda dhambi. Hata sisi tunapaswa kuchukua hatua ya haraka tuepuke mwenendo usio wa kumcha Mungu