Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 3/15 kur. 14-19
  • ‘Msiutumie Sana Ulimwengu’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • ‘Msiutumie Sana Ulimwengu’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Ulimwengu . . . Unapitilia Mbali”
  • “Mwepesi Kama Inavyowezekana”
  • ‘Hatukupokea Roho ya Ulimwengu’
  • Endeleeni Kuwa “Bila Doa Kutoka Kwenye Ulimwengu”
  • Endeleeni ‘Kuwa Watakatifu kwa Mungu Wetu’
  • ‘Msiutumie Sana Ulimwengu’
  • Lazima Waokokaji Wawe “Si Sehemu ya Ulimwengu”
    Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
  • Endeleeni Kuwa “Bila Doa Kutokana na Ulimwengu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Sababu kwa Nini Ni Lazima Tusiwe Sehemu ya Ulimwengu Huu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Kataa Tamaa za Kilimwengu!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 3/15 kur. 14-19

‘Msiutumie Sana Ulimwengu’

“Wale wanaolazimika kushughulika na ulimwengu wasiingize fikira zote katika huo. Mimi nasema hilo kwa sababu ulimwengu kama sisi tunavyoujua unapitilia mbali.” — 1 WAKORINTHO 7:31, The Jerusalem Bible.

1, 2. (a) Ni maoni gani juu ya wakati ujao wa ulimwengu waliyo nayo watu wengi leo? (b) Paulo alisema nini juu ya ulimwengu na kuutumia?

“MTU hawezi kutabiri mambo mazuri yasiyotazamiwa wala mambo ya kukatisha tamaa yaliyo katika wakati ujao.. . . Hata hivyo, inaelekea kuwa ulimwengu unapata maendeleo na utapata maendeleo kwa njia iliyo kombo au iliyonyoka.” Ndivyo alivyosema H. G. Wells mwanahistoria anayejulikana sana, makumi machache ya miaka iliyopita. Ijapokuwa kuna hatari nyingi na misiba mingi sana, watu wengine wanaona kwamba wanadamu watatatua matatizo yao kwa njia fulani, kisha ulimwengu, kama tunavyoujua, utaokoka hali ya hatari.

2 Lakini, akiandika chini ya uongozi wa Mungu, Paulo mtume wa Kikristo alionyesha hali tofauti wakati alipowahimiza hivi waamini wenzake: “Waacheni... wale wanaotumia ulimwengu [wawe] kama wale wasioutumia sana; kwa maana tamasha ya ulimwengu huu inabadilika.” Tafsiri nyingine inasema hivi: “Wale wanaolazimika kushughulika na ulimwengu wasiingize fikira zote katika huo. Mimi nasema hilo kwa sababu ulimwengu kama sisi tunavyoujua unapitilia mbali.” (1 Wakorintho 7:29-31, New World Translation; JB) Shauri hilo lina maana gani kwa watumishi wa Yehova Mungu leo?

“Ulimwengu . . . Unapitilia Mbali”

3. Paulo alizungumza habari gani kwenye 1 Wakorintho sura ya 7, na ni nini mengine ya mambo aliyotaja hapo?

3 Kwenye 1 Wakorintho sura ya 7 Paulo alikuwa akizungumza habari ya ndoa kati ya Wakristo. Ingawa alipendekeza useja kuwa ndio mwendo mzuri zaidi, alikubali wazi kwamba wale wanaoingia katika kifungo cha ndoa ‘hawatendi dhambi’ kwa kufanya hivyo. Hata hivyo aliongezea kwamba wangekuwa na “dhiki katika mwili wao,” kwa maana ndoa inafuatana na mahangaiko fulani. Kwa mfano, ugonjwa wa mpendwa unaweza kuleta mkazo. Ingawa hapo Paulo hakutaja mateso, dhiki zaidi inaweza kupata watu waliooana kwa mfano wakati wenzi wanapokuwa wametengana au wazazi wanapotenganishwa na watoto wao.—1 Wakorintho 7:25-28,NW

4. Ni nini maana ya 1 Wakorintho 7:29?

4 Paulo aliendelea kusema hivi: “Zaidi ya hayo, nasema hivi, ndugu, wakati unaobaki umepunguzwa. Tangu sasa na kuendelea waacheni wale walio na wake wawe kana kwamba hawakuwa nao.” (1 Wakorintho 7:29, NW ) Kwa kuwa “wakati unaobaki umepunguzwa,” Wakristo waliooana hawapaswi kutumia wakati mwingi kabisa wakitimiza mapendeleo na wajibu mbalimbali wa ndoa mpaka mambo hayo yawe yanawazuia kufanya mambo mengine ya maisha. Bali, inawapasa waweke kwanza faida za Ufalme maishani, ingawa hawatakosa kutimiza madaraka ya ndoa. (1 Wakorintho 7:3-5, 29-40 NW ) Kwa kuwa tunaishi katika “siku za mwisho,” sababu inaongezeka ya kutufanya tufuate shauri hilo lililoongozwa na Mungu. —2 Timotheo 3:1-5.

5. “Ulimwengu” tusiopaswa kuutumia sana ni nini?

5 Kwa kuwa “wakati unaobaki umepunguzwa,” Paulo alisema, “waacheni . . . wale wanaotumia ulimwengu [wawe] kama wale wasioutumia sana.” (1 Wakorintho 7:29-31 NW ) Katika kifungu hicho cha maneno, neno la Kigiriki lililotafsiriwa “ulimwengu” (kósmos) halitumiki kwa wanadamu kwa njia ya moja kwa moja, kama linavyotumika katika Yohana 3:16, bali linatumika kwa hali ya maisha ya kibinadamu na shughuli zake. Wanadamu wana vikundi-vikundi vya lugha, mataifa, makabila, jamaa, matajiri na maskini, na shughuli za ujumla ambazo zinawazunguka na kugeuza hali yao. (1 Wakorintho 14:10; Yakobo 2:5, 6; Ufunuo 7:9; 14:6) Ndiyo, Paulo alikuwa akimaanisha hali ya maisha ya kibinadamu na mambo yanayotokezwa na hali hiyo wakati aliposema: “Mnapoutumia ulimwengu, msijaribu kupata kutokana nao vitu vyote mwezavyo.”—1 Wakorintho 7:31, The New Testament in the Language of Today, William F. Beck.

6, 7. (a) Ni kwa njia gani “tamasha ya ulimwengu huu unabadilika”? (b) Mtume Yohana alionyesha nini juu ya wakati ujao wa ulimwengu?

6 Paulo alionyesha pia kwamba Wakristo ‘hawapaswi kuutumia ulimwengu sana’ kwa sababu “tamasha ya ulimwengu huu inabadilika.” Ulimwengu huu ni kama tamasha zinazobadilika jukwaani za mchezo wa kuigizwa. Ingawa huenda ulimwengu ukaonekana kuwa wa kuvutia, wenye kuigiza michezo yake wanabadilika, na ndivyo hali zake zinavyobadilika pia. Wanadamu wanakuja ‘jukwaani,’ na wengine wanatenda kwa moyo wa kiburi. Lakini baada ya muda mfupi wanaondoka pamoja na kizazi chao kisha wanasahauliwa. (Mhubiri 1:4) Katika wakati wetu, ulimwengu huu wa kale uko karibu kutokomea! Kwa kweli, “ulimwengu kama sisi tunavyoujua unapitilia mbali.”—1 Wakorintho 7:31, JB.

7 Mtume Yohana alitaja jambo linalofanana na hilo, akasema: “Ulimwengu unapita na ndivyo na tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” (1 Yohana 2:15-17, NW ) Kwa wazi Yohana alimaanisha kwamba jamii ya kibinadamu isiyo na uadilifu ilikuwa karibu kupitilia mbali kwa kupatwa na uharibifu wa kimungu, sawa na vile ulimwengu uliotangulia Gharika ambao haukumcha Mungu ulitoweka. (Waebrania 11:7; 2 Petro 2:5; 3:6) Bila shaka, shughuli za sasa za kibinadamu na vitu vyote vinavyotokana nazo zitakwisha pamoja na watu wasio waadilifu.

8. Ingawa ulimwengu huu unapitilia mbali, Wakristo wana tumaini gani, na tumaini hilo liwe na matokeo gani juu ya matumizi yetu ya ulimwengu?

8 Lakini kama vile wanadamu wenye maelekeo ya kufuata uadilifu walivyoiokoka Gharika, Yesu alionyesha kwamba ndivyo wengine watakavyoiokoka “dhiki kubwa” inayokaribia mbio-mbio. (Mathayo 24:21, 22, 36-39; linganisha Ufunuo 7:9-17.) Tayari “dunia mpya” inaendelea kufanyika, yaani, jamii ya watu watakaoishi katika dunia hii wakiwa chini ya utawala wa Ufalme. (2 Petro 3:13, NW; Ufunuo 21:1; linganisha Zaburi 96:1.) Kwa hiyo ikiwa sisi binafsi tuna tumaini la kuokoka na la kupata uzima wa milele katika Taratibu Mpya, kwa sababu gani tutumie sehemu iliyo kubwa zaidi ya wakati na nishati zetu katika mambo ya ulimwengu wa kale unaopita?

“Mwepesi Kama Inavyowezekana”

9. Ni kwa njia gani mbalimbali Mashahidi wa Yehova wanaweza kuutumia ulimwengu kwa kufaa?

9 Sisi Mashahidi wa Yehova tunaoishi katika huu mfumo wa mambo hatuwezi kikweli ‘kutoka katika ulimwengu.’ (1 Wakorintho 5:9, 10) Kwa hiyo kwa kufaa tunaweza kuutumia ulimwengu kwa njia zenye usawaziko, zinazofaa na za kiasi. Kwa mfano, kwa kuwa sisi tunalipa kodi mbalimbali, tuna haki ya kupata utumishi fulani-fulani unaotolewa na “mamlaka zilizo kuu.” (Warumi 13:1-7, NW ) Kwa kufaa tunatumia utumishi tunaofanyiwa na wafanya kazi wa posta, polisi na wengine wenye kufanya shughuli zilizo halali, kama vile mifumo ya usafirishaji. Kwa kusudi gani? Ili tuwe na maisha yanayofaa na kuiendesha kazi tuliyopewa na Mungu ya kuutolea Ufalme ushuhuda. Lakini kwa kuwa haitupasi kuutumia ulimwengu “sana,” mambo yote hayo yanatumiwa kufikia kadiri ile tu yanayotimiza faida za Kikristo.

10. (a) Inatupasa tufanye maisha yetu yategemee nini? (b) Yesu alifananishaje thamani kubwa ya Ufalme? (c) Ikiwa sisi tunachukua faida za Ufalme na uhusiano wa kindani pamoja na Yehova kuwa mambo ya maana sana, jambo hilo litakuwa na matokeo gani juu ya matumizi yetu ya ulimwengu?

10 Hatupaswi kuacha faida za kilimwengu zitutawale. Bali, tunahitaji kufanya maisha yetu yategemee uhusiano wetu pamoja na Yehova, yategemee ibada tunayomtolea na yategemee utumishi tunaompa. Je! Matendo yetu yanafunua wazi kwamba tunauchukua, “uhusiano wa kindani pamoja na Mungu” kuwa wa maana sana? (Ayubu 29:4, NW ) Na je! tunautambua ubora mkubwa kabisa wa mambo ya kiroho? Yesu Kristo alifananisha thamani kubwa ya Ufalme na “lulu moja” iliyokuwa ya thamani kubwa sana hata mfanya-biashara “akauza kwa haraka vitu vyote alivyokuwa navyo kisha akainunua.” (Mathayo 13:45, 46, NW ) Hivyo Yesu alionyesha kwamba mtu anayethamini ubora halisi wa kuupata Ufalme angekuwa na nia ya kuachilia kando hazina yo yote ya kidunia ili aupate. Ikiwa sisi tutauhesabu Ufalme na faida zake, na hasa uhusiano wa kindani pamoja na Yehova, kuwa wa maana hivyo kwetu, tutaufanya “kila uhusiano pamoja na ulimwengu . . . mwepesi kama inavyowezekana.”—1 Wakorintho 7:31, Phillips.

‘Hatukupokea Roho ya Ulimwengu’

11, 12. (a) “Roho ya ulimwengu ni nini”? (b) Wakristo wamepokea roho gani, nayo inatofautianaje na roho ya ulimwengu huu?

11 Sababu nyingine ya kutokuutumia ulimwengu sana ni kwamba haiwezekani kufurahia uhusiano wa kindani pamoja na Yehova na huku tukiwa na ile “roho ya ulimwengu.” (1 Wakorintho 2:12, NW ) Roho au nguvu inayotia nishati za kuuongoza ulimwengu wa jamii ya kibinadamu isiyo na uadilifu ni ya kishetani na iko mbali na Mungu kwa njia ya kutenganishwa. Ukiwa chini ya uongozi wa Ibilisi, ulimwengu unachochea choyo na tamaa za mwili wenye dhambi, na matokeo yanakuwa ni kumwonyesha Yehova Mungu uadui.—Yohana 14:30; Waefeso 2:1-3; 1 Yohana 5:19.

12 Mtume Paulo alitofautisha roho ya ulimwengu na roho ya Mungu na akasema hivi juu ya Wakristo: “Tulipokea, si roho ya ulimwengu, bali roho inayotoka kwa Mungu,” (1 Wakorintho 2:12, NW ) Kwa kuwa kiolezo cha ulimwengu cha mawazo na mwenendo kinapingana na mavutano ya roho takatifu ya Mungu na maagizo yanayopatikana katika Neno lake, ni lazima watu wanaomcha Mungu waepuke roho ya ulimwengu. Badala ya kuwa nayo, wenye kumpenda Yehova wanasitawisha na kuonyesha kwa kufaa yale matunda ya roho takatifu ya upendo, furaha, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole na kujiweza.—Wagalatia 5:22, 23,

13. Yohana aliandika nini kwenye 1 Yohana 4:1-6, na je! jambo hilo linahusika vyo vyote juu ya matumizi yetu ya ulimwengu?

13 Jambo la kupendeza ni kwamba mtume Yohana aliyekuwa amezeeka alionyesha kamba “semi zenye kuongozwa na Mungu” kikweli zilikuja kupitia kundi la Kikristo la kweli, si kupitia vyanzo vya kilimwengu visivyo vya Kikristo. Halafu akasema: “Yule anayepata maarifa ya kumjua Mungu anatusikiliza sisi; yule ambaye hatokani na Mungu hatusikilizi sisi.” Ni kweli kwamba habari iliyokuwa ikitajwa na Yohana ni juu ya “semi zenye kuongozwa na Mungu.” Lakini yeye alionyesha kwamba Wakristo ‘hawasemi lile linalotoka kwenye ulimwengu.’ (1 Yohana 4:1-6, NW ) Kwa hiyo kwa sababu gani tuutumie sana ulimwengu?

Endeleeni Kuwa “Bila Doa Kutoka Kwenye Ulimwengu”

14. Wakristo wapakwa-mafuta na washirika wenzao walio wakf wanaonekanaje wazi kuwa “si sehemu ya ulimwengu”?

14 Kazi ya kuajiriwa na utendaji mwingine-mwingine inafanya iwe lazima Mashahidi wa Yehova ‘washughulike na ulimwengu’ kwa njia fulani-fulani. Lakini ‘haitupasi kuingiza fikira zote katika huo’ kwa sababu nyingine bado. (JB) Yesu alisema kwamba wafuasi wake si “sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:14, NW ) Kupitia Kristo, Yehova ametutolea wokovu tujiepushe na ulimwengu huu unaoongozwa na Shetani. (Wakolosai 1:13, 14) Kwa kuitii kweli ya Neno la Yehova iliyofunuliwa wazi, Wakristo wapakwa-mafuta wametakaswa, au wakafanywa watakatifu, wakawekwa kando kwa matumizi ya Mungu katika utumishi wake. Hivyo wao, na pia washirika wenzao wa ule “mkutano mkubwa,’ wanaonekana waziwazi kuwa si “sehemu ya ulimwengu” usioifuata sana kweli ya Yehova. (Ufunuo 7:9; Yohana 17:16,17, NW; Yakobo 1:18; 1 Petro 1:22) Lingekuwa jambo lisilofaa kweli kweli watu wa namna hiyo wakiutumia sana ulimwengu!

15. Kulingana na Yakobo 1:27, ibada safi isiyo na unajisi inahitaji nini?

15 Kutokuwa “sehemu ya ulimwengu” kunahitaji hali ya kutokuwamo katika mizozo na siasa za ulimwengu. (Mathayo 22:21; Yohana 18:36, 37, NW) Wafuasi wapakwa-mafuta wa Kristo na washirika wenzo walio wakf ni lazima waepuke pia kufanya uasherati wa kiroho kwa kuwa na urafiki pamoja na ulimwengu. Wao wanatakwa wawe na usafi wa kiadili na wa kiroho. (Waefeso 4:25-32; Yakobo 4:4) Basi, ili sisi tumtolee Yehova ibada safi isiyotiwa unajisi ni lazima ‘tuendelee kujiweka katika hali ya kuwa bila doa kutoka kwenye ulimwengu’ kwa kutokufuata maoni, usemi na mwenendo ulio kawaida ya wanadamu wenye dhambi waliotengwa mbali na Mungu. (Yakobo 1:27, NW ) Ni lazima tuendelee kuwa bila uchafu wa ulimwengu, jeuri yake, mipango yake ya udhalimu, na mambo kama hayo. Ndiyo, uhitaji wa ‘kuendelea kujiweka katika hali ya kuwa bila doa kutoka kwenye ulimwengu’ ni sababu nyingine ya maana sana ya ‘kutokuutumia ulimwengu tupate kutokana nao vitu vyote tuwezavyo.’—Beck.

Endeleeni ‘Kuwa Watakatifu kwa Mungu Wetu’

16. Kwa sababu gani Waisraeli walipaswa kufanyiza “kingo zenye matamvua” katika mavazi yao ya mfano wa kanzu?

16 Watu wa Yehova wanatofautiana na ulimwengu katika matumaini yao, katika mambo wanayotaka sana kutimiza na katika kujipatanisha na mapenzi ya Mungu wao mtakatifu. (Kutoka 39:30) Wanapaswa kuwa watakatifu kwa Mungu. Kwa hiyo, watu wa Israeli ya kale walipaswa kufanyiza “kingo zenye matamvua juu ya marinda ya mavazi yao [yaliyokuwa mfano wa kanzu],” halafu ulikuwako uzi wa rangi ya samawati juu ya matamvua (nyuzi zilizoning’inia). Walipaswa kufanya hivyo ili wasiwe wanafanana na Wamoabi, Wamisri au watu wengine, kisha jambo hilo liliwakumbusha kwamba walipaswa kuwa tofauti wakiwa watu wa Yehova na kumtii yeye, ‘kujithibitisha kuwa watakatifu kwa Mungu wao.’ (Hesabu 15:37-41, NW ) Tamaa ya kuwa ‘watakatifu kwa Mungu wetu’ inapasa kutufanya tuwe na busara katika kuutumia ulimwengu.

17. Lengo la kilimwengu la kujipatia utajiri linaweza kuutia hatarini namna gani uhusiano wetu na Yehova?

17 Malengo ya kilimwengu yanahusu kuwa na utajiri, sifa na kufanya mambo yasiyoleta hali njema ya kiroho ambayo yanaweza kubomoa imani ya Kikristo. Kwa mfano, tukiruhusu ufuatiaji wa vitu vya kimwili na utajiri uwe ndilo jambo kuu maishani mwetu, huenda ukatushawishi hata tufanye makosa kwa ajili ya faida ya kichoyo, na kwa njia hiyo tutie uhusiano wetu na Yehova hatarini. (Mithali 28:20; linganisha Yeremia 5:26-28; 17:9-11.) Kwa kweli, wale wanaoutumia ulimwengu kwa kiasi cha kwamba wanafanya ufuatiaji wa vitu vya kimwili uwe ndilo hangaikio lao kubwa wamo katika hatari ya kuingia katika mazoea ya udanganyifu na ya kupoteza imani kwa sababu ya kutokujali mambo ya kiroho. Huenda mtu anayepata mafanikio katika biashara au anayekuwa tajiri akawa ‘mwenye kujivuna,’ akifanya kiburi kwa kuyahesabu maoni yake mwenyewe kuwa bora kushinda mashauri yanayotoka kwenye kundi la Mungu. (1 Timotheo 6:9,10, 17) Kwa uhakika hiyo siyo njia ya kuendelea ‘kuwa watakatifu kwa Mungu wetu.’

18. Kwa sababu gani haitupasi kuwa na mradi wa kilimwengu wa kujipatia vitu vya kimwili kwa wingi?

18 Yesu alisema hivi kwa kufaa: “Jifanyieni rafiki kwa mali ya udhalimu, ili itakapokosekana [Rafiki zenu wa kimbingu, Yehova Mungu na Yesu Kristo] wawakaribishe katika makao ya milele.” (Luka 16:9) Kwa hiyo, ingawa tunahitaji vitu fulani vya kimwili na tunaweza kutumia mali hizo kuendeleza faida za Ufalme na kujifanyia Rafiki wa kimbingu, mradi wa kilimwengu wa kujipatia vitu hivyo kwa wingi haupasi kuruhusiwa uchafue moyo wetu.—Luka 12:34.

19. Inatupasa tuwe na maoni ya namna gani juu ya mradi wa kilimwengu wa kujipatia utukufu?

19 Mradi mwingine wa kilimwengu ni ule wa kujipatia cheo, sifa na utukufu. Mara nyingi mtu anatakwa atumie miaka mingi ya kujipatia elimu ya juu zaidi, apate heshima nyingi zaidi kati ya watu na mambo kama hayo ndipo aweze kufikia mradi huo. Lakini Maandiko yanafananisha watu wanaotafuta utukufu wao wenyewe na wale wanaokula asali nyingi mno, inayoweza kufanya watapike. Hivyo tunasoma: “Kula asali kwa wingi si kwema, wala kutafuta heshima [utukufu] yao wenyewe si jambo la kuheshimika.” (Mithali 25:16, 27, Rotherham; NW ) Vivyo hivyo, kutukuza sana majogoo na wachezaji wenye kusifiwa sana wa ulimwengu hakupatani na Maandiko, na basi huenda wazazi Wakristo wakaona nyakati nyingine ni lazima wawaonyeshe vijana wao jambo hilo kwa fadhili. (Linganisha Matendo 12:21-23.) Kwa uhakika, kuwa na maoni yanayofaa juu ya mambo kama hayo kunahitajiwa sana pia ikiwa tunataka tuendelee ‘kuwa watakatifu kwa Mungu wetu’ na kuepuka kuutumia sana ulimwengu.

‘Msiutumie Sana Ulimwengu’

20, 21. Kwa sababu gani haitupasi kuutumia sana ulimwengu?

20 Basi, haitupasi sisi Mashahidi wa Yehova kuutumia sana ulimwengu. ‘Haitupasi kuingiza fikira zote katika huo’ kwa sababu (1) “wakati unaobaki umepunguzwa”; (2) “ulimwengu kama sisi tunavyoujua unapitilia mbali”; (3) maisha yetu yanapasa kutegemea uhusiano wetu wenye thamani kubwa pamoja na Yehova; (4) inatupasa kuonyesha wazi tuna roho ya Mungu, si ya ulimwengu; (5) tunahitaji kuwa “bila doa kutoka kwenye ulimwengu”; na (6) ni lazima sisi tuendelee kuwa “watakatifu kwa Mungu wetu.’

21 Tunaweza kufanya yote hayo kwa msaada wa Yehova tu. (Linganisha Zekaria 4:6.) Kwa kuwa sisi tuna lile tumaini zuri ajabu la Ufalme, haitupasi tutake kuutumia sana ulimwengu, kama kwamba vitu unavyotolea watu ndivyo tu tunavyoweza kupata. Lakini ni nini kinachoweza kutusaidia kweli kweli tuzikatae njia na tamaa za kilimwengu?

Wewe Unakumbuka?

◻ Ni “ulimwengu” gani unaomaanishwa kwenye 1 Wakorintho 7:31?

◻ Kwa kuwa “tamasha ya ulimwengu huu inabadilika,” inawapasa Wakristo wawe na maoni gani juu ya kuutumia ulimwengu?

◻ Ni kwa kadiri gani Wakristo kwa kufaa wanaweza kuutumia ulimwengu?

◻ “Roho ya ulimwengu” ni nini, lakini wenye kumpenda Yehova wanaonyesha wazi roho gani?

◻ Watu wa Yehova wanatofautianaje na ulimwengu kwa habari ya malengo yao?

[Picha katika ukurasa wa 17]

Mfanya-biashara aliuza vitu vyote ili anunue “lulu moja ya thamani kubwa”

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kingo zenye matamvua katika mavazi ya Waisraeli ziliwakumbusha kwamba walipaswa kujithibitisha kuwa watakatifu kwa Yehova. Tamaa ya kuwa ‘watakatifu kwa Mungu wetu’ inapasa kutufanya tuwe na busara katika kuutumia ulimwengu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki