Sababu kwa Nini Ni Lazima Tusiwe Sehemu ya Ulimwengu Huu
“Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile mimi nisivyo sehemu ya ulimwengu.—YOHANA 17:16, NW.
1. Yesu alisema wafuasi wake wangeweza kutazamia kutendwa namna gani?
YESU KRISTO alikataliwa, akachukiwa na hata akateswa na ulimwengu huu. Kwa hiyo wafuasi wake wangeweza kutazamia nini? Yeye aliwaambia: “Ulimwengu ukiwachukia ninyi, mjue kwamba umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi. Kama mngalikuwa sehemu ya ulimwengu, ulimwengu ungalikipenda kilicho chake wenyewe. Sasa kwa sababu ninyi si sehemu ya ulimwengu, bali mimi nimewachagua katika ulimwengu, kwa sababu hii ulimwengu unawachukia ninyi. Kumbukeni neno nililowaambia, Mtumwa si mkubwa kuliko bwana wake. Ikiwa wamenitesa mimi, watawatesa ninyi pia; ikiwa wameshika neno langu, watashika lenu pia.”—Yohana 15:18-20, NW.
2. (a) “Ulimwengu” ambao wafuasi wa Yesu wanatofautiana sana nao ni nini? (b) Badala ya kuondoa wanafunzi wa Kristo ulimwenguni, Yehova anawafanyia nini?
2 Ndiyo, wafuasi wa kweli wa Yesu wanatofautiana sana na ulimwengu huu—jamii ya wanadamu wenye dhambi ambao wametenganishwa na Mungu. Wanafunzi wa Kristo wako tofauti sana hivi kwamba wanachukiwa na kuteswa na ulimwengu huu. Lakini katika kuwa wasio wa kilimwengu, wafuasi wa Yesu wanafuata sana mfano wake ulio mzuri kabisa, naye Yehova Mungu anawalinda kupatana na sala ya Kristo: “Mimi nakuomba, usiwaondoe katika ulimwengu, bali uwalinde kwa sababu ya yule mwovu. Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile mimi si sehemu ya ulimwengu. Watakase kupitia ule ukweli; neno lako ni ukweli.” —Yohana 17:15-17, NW.
3. Kwa habari ya ulimwengu huu, ni maulizo gani yanayotaka majibu?
3 Maana yake nini kuwa “si sehemu ya ulimwengu”? Je! inaonyesha kwamba lazima wafuasi wa Yesu waepuke uhusiano wote pamoja na watu wasio Wakristo?
Wakristo Hawawezi Kuwa Watu wa Kukaa Peke Yao
4. Yesu aligawia wanafunzi wake kazi gani, ikafanya isiwezekane wawe wakaa peke yao?
4 Kwa uhakika, Yesu hakutazamia wafuasi wake wajitenge wawe peke yao katika mitaa ya kidini isiyoingiwa na watu wengine. Bali, yeye aliwapa kazi ya kufanya duniani pote, akisema: “Mtapokea nguvu wakati roho takatifu itakapofika juu yenu ninyi, na ninyi mtakuwa mashahidi wangu mimi katika Yerusalemu na katika Yudea yote na katika Samaria na kwenye sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.” (Matendo 1:8, NW ) Pia aliwaamuru hivi: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi. Na, tazama! mimi nipo pamoja na ninyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 28:19, 20, NW ) Bila shaka, ingawa “watu wa mataifa yote” wangekuwa wanafunzi kwa njia hiyo, haikupasa kutazamiwa kwamba mataifa mazima yenyewe yangekubali mafundisho ya Yesu Kristo.
5. Ni kwa njia gani yenye mamlaka ya Kimaandiko watu wanageuzwa na kuingia katika Ukristo?
5 Lakini huenda wengine wakasema: ‘Je! mataifa mazima hayakugeuzwa yakafuata Ukristo? Na je! hayo siyo yale yanayokuwa kinachoitwa Jumuiya ya Wakristo? ’ Basi, watawala fulani wameamulia raia zao dini watakayofuata kisha wakafanya haraka kufikiliza uamuzi wao kwa njia za ukatili na ushenzi. Zaidi ya hilo, kuogopa kuteswa-teswa katika moto wa mateso ulio wa kihadithi tu kumefanya watu wengi waingie katika ule unaoitwa uongofu wa kufuata Ukristo wa jina. (Linganisha Mhubiri 9:5, 10.) Lakini yote hayo yako mbali sana na njia iliyoamriwa na Maandiko ya kueneza imani ya kweli ya Kikristo! Utendaji huo wenye heshima kubwa unapasa kuendeshwa kwa kutoa ushuhuda wa bidii, kufundisha na kufanya wanafunzi. Wakaa peke yao au watawa wenye kujitenga na watu wengine hawangeweza kamwe kutimiza kazi hiyo wala kufuata amri ya Kristo ‘kuacha nuru yao iangaze mbele ya watu.’ (Mathayo 5:14-16) Nako kulazimisha watu ‘waongoke’ hakuhusiani hata kidogo na kazi ya kutoa ushuhuda, kuhubiri na kufundisha inayosaidia watu wenye mioyo minyofu wa mataifa yote wafanye wakfu wa akili na wa kujisikia moyoni kumwelekea Yehova Mungu.
Sababu kwa Nini “Si Sehemu ya Ulimwengu”
6. Kama ilivyoandikwa kwenye Yohana 13:35, kwa sababu gani inaweza kusemwa kwamba yale maelezo ambayo Yesu alitoa juu ya wafuasi wake yanawafaa Mashahidi wa Yehova?
6 Jina “Mkristo” limekuwa mara nyingi la udanganyifu. Ni matendo mengi kama nini ya pupa, kuteka nchi nyingine, kuua katika vita na kugandamiza umati wa watu yanayoweza kuhesabiwa kuwa yamefanywa na watu hata mataifa ya Kikristo! Lakini wafuasi wa kweli wa Kristo wako tofauti sana! “Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi [ni] wanafunzi wangu,” akasema Yesu, “mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” (Yohana 13:35) Kweli kuna watu wanaolingana na maelezo hayo leo—Mashahidi wa Yehova. Kuwa na upendo kati yao kunamaanisha kutokuwa na mashindano ya ukatili, kutokasirishana, kutotumia wenzao ili mtu ajifaidi kwa njia ya uchoyo. Bali, kunamaanisha kusema mamoja, kutokuwa na migawanyiko, kuungana “katika nia moja na shauri moja.” (1 Wakorintho 1:10; 13:4-8) Mashahidi wa Yehova wamejifunza njia ya kuwaza ya Mungu na Kristo na wanaongozwa nayo. (Warumi 12:1, 2; 1 Wakorintho 2:16) Sehemu ya maana sana ya njia hiyo ya kuwaza ni kwamba lazima Wakristo wawe “si sehemu ya ulimwengu.”—Linganisha Yakobo 1:27.
7. Maneno ya Paulo kwenye Matendo 17:30, 31 yanaonyeshaje kwamba haifai Wakristo kuwa sehemu ya ulimwengu huu?
7 Kuna sababu nzuri za wafuasi wa Yesu kutokuwa ‘sehemu ya ulimwengu huu.’ Kwa muda wa miaka karibu 4,000, walio wengi zaidi kati ya wanadamu ‘wamekuwa bila tumaini na bila Mungu katika ulimwengu.’ (Waefeso 2:12, NW ) Lakini kile kipindi kirefu cha kuwa mbali na Yehova kwa sababu ya dhambi ya kibinadamu hakitaendelea kwa wakati usiojulikana. Karne kumi na tisa zilizopita mtume Paulo alisema kwamba Mungu alikuwa “anawaagiza watu wote wa kila mahali watubu,” kwa maana ‘alikuwa ameweka siku atakayowahukumu walimwengu kwa haki, kwa mtu aliyemchagua,’ Yesu Kristo. Paulo aliongeza kwamba Mungu “amewapa watu wote uthabiti wa mambo haya kwa kumfufua [Yesu] katika wafu.” (Matendo 17:30, 31) “Siku” hiyo ya Utawala wa Mileani yake iko karibu sana. Ni lazima ulimwengu mwovu utokomee. Utahukumiwa, ulaaniwe na kufutiliwa mbali milele. Basi, haifai hata kidogo Wakristo wawe sehemu ya ulimwengu huu!
8. Ni kazi gani inayoonyesha kwamba “mwisho” uko karibu, kisha kwa njia hiyo inatoa sababu nyingine ya kufanya watu wa Yehova wasiwe ‘sehemu ya ulimwengu’?
8 Zaidi ya miaka 1,900 imepita tangu Yesu afufuliwe, na bila shaka kufikilizwa kwa hukumu ya kimungu juu ya Jumuiya ya Wakristo yenye kuasi imani pamoja na sehemu ile nyingine yote ya ulimwengu wa Shetani kumekaribia sana. (2 Petro 3:10; 1 Yohana 5:19) Kwa sasa, Mashahidi wa Yehova wanatangaza ujumbe wa Mungu duniani pote na “nyakati za kuburudishwa” zinafurahiwa na wanadamu wanaotubu na kuthamini mambo. (Matendo 3:19-21) Kupatana na maneno ya unabii ya Yesu kuhusu siku zetu, mashahidi wa Yehova zaidi ya 2,650,000 wanahubiri sasa “habari njema hizi za ufalme” katika nchi 205. Wakati kazi hiyo itakapokuwa imekuwa “ushuhuda kwa mataifa yote” kwa kadiri ambayo Mungu anapenda, ‘ule mwisho utakuja.’ (Mathayo 24:14, NW ) Kwa uhakika, basi, kwa vyo vyote watu wa Yehova hawapaswi kuwa “sehemu ya ulimwengu” kwa maana mwisho wa mfumo mbovu huu uko karibu sana.
9. (a) Kwa kuwa ulimwengu wa Shetani uko karibu kwisha, inatupasa tuwe na maoni ya namna gani juu ya faida na matakwa ya Ufalme? (b) Ni maulizo gani ambayo sasa yanastahili tuyafikirie?
9 Kwa kuwa ulimwengu wa Shetani uko karibu kwisha, ni jambo la maana sana kuhakikisha kwamba tunatafuta kweli kweli Ufalme wa Mungu kwanza! (Mathayo 6:33) Hata tuwe tuna umri gani, elimu au cheo gani katika maisha, “sisi sote tutasimama mbele ya kiti cha hukumu cha Mungu.” (Warumi 14:10) Kwa hiyo je! tumezoea kufuata matakwa ya Ufalme kwa matendo katika maisha yetu? Au bado tunajitahidi kujipatanisha na ulimwengu huu unaochukia Wakristo wa kweli? Je! tuna tamaa za makuu ya ulimwengu na matumaini yake? Je! tunaiga mitindo ya ulimwengu isiyopatana na Maandiko? Na je! tunavutiwa na sanamu zinazoabudiwa nao? Kumbuka kwamba “urafiki pamoja na ulimwengu ni uadui pamoja na Mungu.” (Yakobo 4:4, NW ) Basi, ili tujizuie tusiwe adui za Mungu, tunaweza kuepukaje kuchafuliwa na ulimwengu? Ni mambo gani kati ya yale yaliyo katika ulimwengu ambayo lazima tuyaepuke?
Epuka Kupenda Ulimwengu
10. Andiko la Yohana wa Kwanza 2:15, 16 linataja mambo gani matatu katika ulimwengu huu ambayo lazima watu wa Yehova waepuke kuyapenda?
10 Mtume Yohana aliandika: “Msiwe mkipenda wala ulimwengu wala vitu vilivyomo katika ulimwengu. Mtu ye yote akipenda ulimwengu, upendo wa Baba haumo katika yeye; kwa sababu kila kitu kilichomo katika ulimwengu—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na kujionyesha kwa mtu mali yake— hakitokani na Baba, bali chatokana na ulimwengu.” (1 Yohana 2:15, 16, NW ) Hapo Yohana alitaja mambo matatu makubwa yaliyo katika ulimwengu huu ambayo lazima watu wa Yehova waepuke kuyapenda.
11. Kwa sababu gani ni lazima Wakristo waepuke kujiacha wafuate “tamaa ya mwili”?
11 “Tamaa ya mwili” ingeweza kutuingiza katika mazoea mengi yenye madhara na yanayoleta kifo ambayo yanapatikana sana katika ulimwengu huu mbovu unaoongozwa na Shetani. Kati ya hayo kuna “matendo” ya mwili wenye dhambi—“uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo.” Hatuwezi kuepuka adhabu tukipuuza onyo la mtume Paulo “kwamba watu [wazoeao] mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.” (Wagalatia 5:19-21) Kwa kweli, wale wanaozoea “matendo ya mwili” bila kutubu ni sehemu ya ulimwengu huu nao hawatakuwa na ushiriki katika Ufalme ulioahidiwa utakaoondolea jina la Yehova lawama na kugeuza dunia iwe paradiso. (Luka 23:43, ZSB) Basi, ni wazi kwamba lazima Wakristo waepuke kujiacha wafuate “tamaa ya mwili.”
12. (a) “Tamaa ya macho” ni nini, na inaweza kuwa na matokeo gani juu ya msimamo wa mtu kiroho? (b) Kuhusu “tamaa ya macho,” tunaweza kujiuliza nini?
12 “Tamaa ya macho” ni tabia nyingine ya wale walio sehemu ya ulimwengu huu. Wanapojirundikia utajiri na mali, hawaelekei kutosheka kamwe. Ndiyo, hata wengi ambao wamefuata kwa kadiri fulani ukweli wa Biblia unaoenezwa na Mashahidi wa Yehova wanajiacha mwishowe wafuate “tamaa ya macho” na, kwa hiyo, hawafanyi maendeleo yo yote ya kiroho. Tamaa yao ya mavazi mapya, magari, nyumba, vifaa vipya na vitu vingine vingi vinavyopendeza macho inakuwa yenye nguvu sana hivi kwamba, kama Yesu alivyosema, “udanganyifu wa mali, na tamaa za mambo mengine zikiingia, hulisonga lile neno, likawa halizai.” (Marko 4:18, 19) Jambo linalofaa kuangaliwa ni kwamba, Shetani alishawishi Hawa kwa kumfanya atamani kitu kilichokatazwa ambacho angeweza kuona kwa macho yake. Lakini, alishindwa kabisa katika jitihada zake za kumvuta Yesu atende dhambi kwa kujinyosha apate vitu alivyoona kwa macho. (Mwanzo 3:1-6; Luka 4:5-8) Lakini namna gani wewe? Je! unafuata mfano thabiti wa Yesu? Au kutosheleza “tamaa ya macho” kumechukua sana wakati, fikira na nishati zako hata ukawa unaachilia faida za Ufalme? Ikiwa unaendelea kuweka nyuma mambo ya kiroho yanayopasa kuhangaikiwa, chukua hatua upesi urekebishe hali hiyo!
13. Kama inavyoonyeshwa na Paulo na katika mithali fulani, “tamaa ya macho” yenye pupa inaweza kuongoza kwenye nini?
13 “Tamaa ya macho” yenye pupa inaweza kuongoza mtu kwenye udanganyifu, kijicho, kutamani vitu vya watu na kutenda dhambi nyingine zinasotahili kumfanya akataliwe na Mungu. Kama Paulo alivyosema, “wenye pupa” ni kati ya wale ambao “hawatarithi ufalme wa Mungu.” (1 Wakorintho 6:9, 10, NW ) Pia, kwa kufaa mithali zenye hekima zinaonya hivi: “Mtu mwaminifu atakuwa na baraka tele; lakini afanyaye haraka kuwa tajiri hakosi ataadhibiwa. Mwenye husuda afanya haraka kuwa tajiri; wala haufikiri uhitaji utakaomjilia.” (Mithali 28:20, 22) Hata kama umaskini hautawajilia upesi watu mmoja mmoja wenye pupa na kijicho, ama watakufa wakiwa nje ya upendeleo wa Mungu au watafikia mwisho wenye kusikitisha kwenye umalizio wa mfumo huu wa mambo. — Mathayo 24:3, NW; Luka 12:13-21.
14. (a) “Kujionyesha kwa mtu mali yake” kunaweza kujidhihirishaje? (b) Ni nini shina la “kujionyesha” kwa njia hiyo, kuwa na majisifu na kutafuta cheo? (c) Kwa sababu gani tupinge kishawishi cha kujionyesha kuhusu mali zetu na mambo tunayodhani tumetimiza?
14 “Kujionyesha kwa mtu mali yake” lazima kuepukwe pia na watumishi wa Yehova. Mtu anaweza kupatwa sana na kishawishi cha kutaka kujionyesha kwamba ana vitu vya bei ya juu! Zaidi ya kujaribu kuwa na vitu vinavyolingana na vya wengine, mara nyingi tamaa mbaya hiyo inafanya mtu ajitahidi kuwa na vitu vingi vya kimwili kuwapita. Yanayofanana na jambo hilo ni majisifu juu ya mambo ambayo mtu anafikiri ametimiza. Akitumaini kupata cheo au msimamo fulani, huenda hata akasitawisha urafiki na watu wenye vyeo na kutaka wamwunge mkono. Lakini wale wanaojiruhusu watumiwe kwa njia hiyo ni wapumbavu, naye mtu mwenye kujitakia makuu bila kujizuia huenda mwishowe akawa kama “makafiri” wa siku za Yuda ambao ‘vinywa vyao vilinena maneno makuu mno ya kiburi, wakipendelea watu wenye cheo kwa ajili ya faida.’ (Yuda 4, 16) Shina la kutafuta cheo kwa njia hiyo na kujionyesha ni kiburi chenye dhambi. (Mithali 8:13; 16:18; 21:4) Basi, kwa uhakika ni lazima tupinge kishawishi cha kujionyesha kuhusu vitu vyetu na mambo tunayodhani tumetimiza. Hapa basi mithali hii inafaa: “Haifai kula asali nyingi mno; vile vile mtu kutafuta utukufu wake mwenyewe si utukufu.” (Mithali 25:27) Na kwa kuwa wanadamu walio wengi wanatembea katika njia ile pana inayoongoza kwenye uharibifu, maneno ya Yesu ni ya wakati wake kabisa, “Ole wenu ninyi watu wote watakapowasifu”!
“Ulimwengu Unapita”
15. (a) Mtume Yohana anatoa sababu gani ya msingi ya kutokuwa “sehemu ya ulimwengu”? (b) Inawapasa Wakristo washikamanifu waelekeze jitihada zao kuu kwenye nini?
15 Yohana anatupa sababu ya msingi ya kutokuwa “sehemu ya ulimwengu” anapoongezea hivi: “Tena, ulimwengu unapita na ndivyo na tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” (1 Yohana 2:17, NW ) “Ulimwengu,” ambao ni jamii ya kibinadamu isiyo na uadilifu, umekaribia mwisho wake katika “dhiki kubwa” inayokaribia mbio-mbio. (Mathayo 24:21) Wakati wa kipindi hicho kila kisehemu cha matengenezo ya siasa, biashara na dini za uongo za ulimwengu huu kitaharibiwa. Kwa hiyo mashahidi wo wote wa kweli wa Yehova wangewezaje kutumia wakati wao wote, nishati na mali zao kwenye mategenezo hayo yatakayomalizika karibuni? Badala ya hivyo, Wakristo washikamanifu wataelekeza jitihada zao kuu kwenye uendelezaji wa faida za Ufalme na mambo yanayodumu, ya milele. Zaidi ya hilo, kupitia ushikamanifu huo na imani watu wa Yehova ‘watashinda ulimwengu’ wa jamii ya kibanadamu isiyo na uadilifu, kama vile Yesu Kristo alivyofanya. (Yohana 16:33) Nao wataokoka wakati ulimwengu huu utakapopita kwa kupatwa na uharibifu wa kimungu, sawa na vile Noa na jamaa yake walivyookoka Gharika.—2 Petro 2:5.
16. Ni maulizo gani yanayobaki tuyafikirie?
16 Basi, kwa kuwa ulimwengu huu unapita, inawapasa Wakristo wawe na maoni ya namna gani juu ya kuhusika katika mambo ya jamii ya watu? Inawapasa wawe na nia gani kuelekea shughuli za elimu, biashara na tafrija? Maulizo ya namna hiyo yamebaki ili tuyafikirie kwa uangalifu.
Wewe Ungesema Nini?
◻ Ni ulimwengu gani ambao wafuasi wa kweli wa Yesu si sehemu yake?
◻ Wanafunzi wa Kristo hawawezi kuwa wakaa peke yao kwa sababu ya kazi gani waliyogawiwa?
◻ Ni nini nyingine za sababu zinazofanya Mashahidi wa Yehova wasiwe “sehemu ya ulimwengu”?
◻ Ili kufuata shauri la 1 Yohana 2:15-17, ni mambo gani matatu ya msingi yaliyo ulimwenguni ambayo lazima watu wa Yehova waepuke kuyapenda?
[Picha katika ukurasa wa 11]
Ingawa Mashahidi wa Yehova “si sehemu ya ulimwengu,” wanashughulika wakisaidia watu wa mataifa yote kiroho
[Picha katika ukurasa wa 13]
Ikiwa sisi “si sehemu ya ulimwengu,” hatutajiacha tufuate tamaa za mwili na macho wala hatutajionyesha kuwa tuna mali