Endeleeni Kuwa “Bila Doa Kutokana na Ulimwengu”
“Namna ya ibada iliyo safi na isiyotiwa unajisi kulingana na maoni ya Mungu na Baba yetu ni hii: kutunza yatima na wajane-wake katika dhiki yao, na kujiweka bila doa kutokana na ulimwengu.”—YAKOBO 1:27, NW.
1, 2. Ni nini mengine ya matakwa ya ibada safi?
YEHOVA anataka ibada safi. (Yohana 4:23, 24) Kati ya mambo mengine, dini isiyotiwa unajisi inasukuma watu kufikiria wenye shida kwa njia yenye matendo na upendo. (Wagalatia 2:10) Inatuhitaji pia tujiweke bila kutiwa doa na ulimwengu, yaani, jamii ya kibinadamu isiyo na uadilifu ambayo imetengwa mbali na Mungu na ‘iko katika uwezo wa yule mwovu,’ Shetani Ibilisi. — 1 Yohana 5: 19, NW.
2 “Namna ya ibada iliyo safi na isiyotiwa unajisi kulingana na maoni ya Mungu na Baba yetu ni hii,” akaandika mwanafunzi Yakobo, “kutunza yatima na wajane-wake katika dhiki yao, na kujiweka bila doa kutokana na ulimwengu.” Fasiri nyingine inasema: “Dini yenye kutakata, isiyoharibiwa, machoni pa Mungu Baba yetu ni hii: kuja kuwapa msaada yatima na wajane-wake wanapouhitaji, na kujiweka bila kuchafuliwa na ulimwengu.”—Yakobo 1:27, The Jerusalem Bible.
3. Sasa tutafikiria maulizo gani?
3 Lakini sisi watumishi wa Yehova tunaweza kujiwekaje “bila kuchafuliwa na ulimwengu”? Maoni ya Kimaandiko ni nini juu ya mambo kama shughuli za kilimwengu za jamii ya watu, mipango ya elimu, shughuli za kibiashara na utendaji mbalimbali wa kitafrija?
“Kujiweka Bila Kuchafuliwa na Ulimwengu”
4. Maandiko ya Yohana 17:14 na Isaya 2:2-4 yanaonyesha nini juu ya uhusiano wetu na ulimwengu huu?
4 Kwa kuwa sisi tulio Mashahidi wa Yehova “si sehemu ya ulimwengu,” ni lazima tuwe tofauti na jamii ya kibinadamu isiyo na uadilifu. (Yohana 17:14, NW ) Kwa ufupi, kufanya hivyo kunatutaka tuendelee kutokuwamo katika mambo ya siasa za ulimwengu. Pia lazima tujizuie tusihusike katika jeuri yake na lazima tufuatie amani tukiwa watu ambao ‘wamefua panga zao zikawa majembe.’—Isaya 2:2-4.
5. Ili tuendelee kukaa bila kuchafuliwa na ulimwengu huu, ni hatua gani lazima tuchukue kama inavyoonyeshwa na (a) 1 Wakorintho 6: 9-11? (b) Waefeso 5:3-5?
5 Tukiwa sisi ni watu wanaotaka kuendelea kukaa bila kuchafuliwa na ulimwengu huu, ni lazima tuepuke usemi, mwenendo na nia zinazoonekana sana kati ya watu wa kilimwengu. Kwa mfano, chuki, pupa, mwenendo wa aibu na kufanya mzaha kwa kutumia maneno machafu ni mambo yasiyopasa kuwa katika maisha yetu. (1 Wakorintho 6:9-11; Waefeso 5: 3-5) Si jambo la kushangaza kwamba matendo na nia zetu zinatofautiana na za watu wa kilimwengu, kwa maana wao hawana tumaini la Kikristo tulilo nalo.
Wakati Ni Mfupi kwa Utaratibu Huu wa Ulimwengu
6. Kulingana na 1 Wakorintho 7:29-31, inawapasa Mashahidi wa Yehova wawe na maoni gani juu ya ndoa, mali au vitu vingine vya kidunia?
6 Mtume Paulo aliandika: “Wakati unaendelea kuwa mfupi. Kuanzia sasa acheni wale walio na wake wajiendeshe kama kwamba hawana, na waombolezi kama kwamba hawaombolezi, na wenye nderemo kama kwamba hawateremi; wale wanaonunua kama kwamba si wenye vitu, na wale walioutumia ulimwengu kama kwamba hawakuutumia, kwa sababu utaratibu wa ulimwengu wa sasa unapita.” (1 Wakorintho 7:29-31, Modern Language Bible) Hiyo inaonyesha kwamba ingawa ni lazima waume Wakristo watimize wajibu mbali-mbali wa ndoa, haiwapasi kufanya ndoa iwe ndiyo shughuli ya maisha yote. Wakati wa kufa, Wakristo waliozaliwa kwa roho wataacha nyuma kwa umilele uhusiano wote wa kidunia, mambo yote yanayowafurahisha, yote yanayowahuzunisha na mali zao zote. Hata sasa, huenda Wakristo wakapoteza mke au mali za kimwili, wawe wana tumaini la kimbingu au la kidunia! Zaidi ya hilo, wakati wa “dhiki kubwa” ni uhai, wala si mali za kimwili, utakaohifadhiwa. (Mathayo 24:21; Mhubiri 9:11) Kwa hiyo hakuna ye yote wa Mashahidi wa Yehova leo anayepaswa kuweka ndoa, mali wala vitu vingine vya kidunia kwanza maishani. Bali, Wakristo wote wanapaswa kufanya uhusiano mwema pamoja na Yehova Mungu uwe ndilo jambo la maana kupita yote. Hasa hivyo ndivyo inavyopasa kuwa kwa maana tunaishi katika “siku za mwisho” na “utaratibu wa ulimwengu wa sasa unapita.” —2 Timotheo 3:1.
7. Kulingana na mwanauchumi mmoja, kumekuwa na ukuzi wa nini pamoja na ukuzi wa elimu, mapato, na mambo kama hayo?
7 Watu wengi wanahangaika juu ya wakati ujao wa “utaratibu wa ulimwengu wa sasa.” Kwa mfano, Nancy Brown aliye mwandikaji wa habari za magazetini alimtaja mwanauchumi Ezra Misham kuwa akisema yanayofuata juu ya ukuzi wa elimu na mapato: “[Haukuleta] hali nzuri zaidi katika jamii ya watu. Pamoja na ukuzi wa sayansi, elimu na mali za kimwili, jamii ya watu imeona pia ukuzi wa jeuri, kuharibu mali za watu, uuaji wa binadamu na kujiua kwa watu wenyewe, matumizi ya matusi na misemo michafu.” Maneno ya utangulizi ya makala ya gazeti hilo yalikuwa ya maana: “Ni hatua ya Kimungu tu inayoweza kuokoa ulimwengu usijiangamize.”—Gazeti Times-Colonist, Victoria, British Columbia, Machi 25, 1982.
8. Kwa sababu gani tusijipatie vitu vyote tunavyoweza kutokana na ulimwengu huu?
8 Bila shaka, Yehova aliiumba dunia ikaliwe, si na jamii ya kibinadamu isiyo na uadilifu, bali na wanadamu waadilifu, wenye ukamilifu. (Isaya 45:18; Zaburi 37:29, 38) Kwa hiyo Mungu hataruhusu wanadamu wajiangamize wenyewe. Lakini hakuna shaka kwamba utaratibu huu wa kale wa ulimwengu utapitilia mbali kabisa. Basi, watumishi wa Yehova walio wakfu hawapaswi kuutumia “sana” ulimwengu. Au kama vile tafsiri moja inavyosema: “Mnapoutumia ulimwengu, msijaribu kupata kutokana nao vitu vyote mnavyoweza, kwa kuwa ulimwengu huu kwa namna yake ya sasa unapita.”—1 Wakorintho 7:31, The New Testament in the Language of Today, cha William F. Beck.
Je! Tutumie Ulimwengu Huu Hata Kidogo?
9. (a) Ni kwa kadiri gani watu wa Yehova wanaweza kuutumia ulimwengu huu kwa kufaa? (b) Kulingana na Mathayo 6:31-33 na 1 Timotheo 6:7, 8, inatupasa tuwe na nia gani kuelekea vitu vya kimwili?
9 Basi, je! inafaa sisi mashahidi wa Yehova tulio wakfu tupate kitu kutokana na ulimwengu huu? Ndiyo, Paulo alionyesha kwamba tunaweza kuutumia ulimwengu lakini si sana. Kwa hiyo, tunaweza kutumia vitu vya ulimwengu vilivyo halali ili tutimize wajibu wetu mbalimbali wa Kimaandiko na kuhubiri ujumbe wa Ufalme. (1 Timotheo 5:8; 6:17-19) Lakini, kwa kuwa tunataka tuendelee kuwa “bila doa kutokana na ulimwengu,” haiwezi kufaa tujiingize katika mabishano, maandamano ya kupinga jambo fulani, katika vita vya maneno na vya uhalisi wala katika mambo mengine kama hayo. Hata kwa siri haitupasi kupendelea upande mmoja zaidi ya mwingine. Wala haitupasi kuhangaikia riziki yetu na ufanisi wa kimwili kupita kiasi, kwa maana Yesu alisema: “Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? au Tunywe nini? au Tuvae nini? Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.” Naye Yesu alitenda mambo aliyohubiri, kwa maana ingawa mbweha wana mapango na ndege wana viota, yeye hakuwa na mahali po pote pa kulaza kichwa chake. Basi, sisi na tutosheke na chakula na vitu vya kujifunika huku ‘tukitafuta kwanza ufalme.’—Mathayo 6:31-33; Luka 9:58; 1 Timotheo 6:7, 8.
10. Kwa habari ya elimu, ni maulizo gani yanayostahili kufikiriwa kwa njia ya sala, na wewe ungeyajibuje?
10 Basi, namna gani juu ya kufuatia kazi ya kilimwengu ya maisha yote? Basi, kwa kuwa ulimwengu huu utapita katika siku zetu, je! lingekuwa jambo la akili kupanga kuwa na maisha ya kufuatia maendeleo ya kilimwengu? (Mathayo 24:34) Halingekuwa! Tukiwa na maoni hayo ya kwamba halingekuwa jambo la akili, hakika yatageuza nia yetu kuelekea elimu ya kilimwengu. Ingawa elimu ya msingi inahitajiwa, katika shule za masomo ya juu linakaribia kuwa jambo lisilowezekana kuepuka kuvutwa na wimbi lililoko la mawazo ya kilimwengu. Bila shaka, ni lazima mtu ajifanyie maamuzi yake mwenyewe juu ya elimu. (Wagalatia 6:5) Lakini maulizo kama haya yanastahili kufikiriwa kwa sala: Wakati wa miaka iliyotumiwa katika vyuo vikuu; je! wanafunzi wameweza kuendelea ‘kutafuta kwanza Ufalme na haki ya Yehova’? Je! wanaepuka kabisa kuingiwa na mafundisho ya makisio na falsafa zinazobomoa imani ya kweli? (Wakolosai 2:8) Je! washirika wa kilimwengu wamekuwa na mavutano mema juu yao, au wamepatwa na madhara ya kiroho? (1. Wakorintho 15:33) Na je! watu wengi wenye elimu nyingi wamedumisha unyenyekevu kweli kweli?—Wafilipi 2:2, 3.
11. Hata elimu ya mtu iwe ni ya namna gani, ni msaada gani umetolewa hapa ili achunguze makusudi yake?
11 Kuhusu jambo hilo, wengine wanaoingia shule za mazoezi ya kikazi wanaweza kujiingiza sana katika ufundi fulani hata wasiwe tena na wakati mwingi wa kutumia katika utumishi wa Yehova. Kwa hiyo, hata hali ya elimu yenyewe iwe namna gani, inategemea sana makusudio ya mtu. Je! lengo kubwa ni tamaa ya kujitegemea na kupata mali? Je! elimu hiyo itapunguza sana utumishi wako kwa Yehova au itasaidia kukutegemeza katika utumishi mtakatifu? Ingawa wewe ni Mkristo anayepaswa kuendelea kuwa bila kutiwa doa na ulimwengu, je! badala ya kuwa hivyo unajaribu kujitengenezea jina katika mfumo huu wa mambo au unajishughulisha sana katika kuendeleza faida za Ufalme kwanza maishani?
12. Ni nini kimesukuma watu fulani wenye elimu ya juu wakubali ukweli wa Ufalme?
12 Tunafurahi kwamba watu mmoja mmoja wenye elimu ya juu wamekubali ukweli wa Ufalme. Lakini hawakufanya hivyo kwa sababu ya elimu yao ya juu. Bali, walikuja kutambua kwamba, ijapokuwa wana elimu ya juu, maisha hayakuwa na maana kwa sababu walikuwa hawana Mungu wala tumaini hakika. Sasa wanajua kwamba ‘si wengi wenye hekima, wenye nguvu na wenye cheo’ walio na ukubali wa kimungu. (1 Wakorintho 1:26-31) Hata hivyo, wao wenyewe wanafurahi sana kwamba, mwishowe, wamepata kusudi halisi maishani wakiwa mashahidi wa Yehova.
“Shughuli za Kibiashara za Maisha”
13. Andiko la Timotheo wa Pili 2:3, 4 linapendekeza nini juu ya shughuli za kikazi na Mkristo aliye wakfu?
13 Kwa kuwa tunataka kuendelea kukaa bila kuchafuliwa na ulimwengu huu, inatupasa tuwe na nia gani kuelekea shughuli zake za kikazi? Mtume Paulo alimwambia Timotheo: “Ukiwa askari mwema wa Kristo Yesu chukua fungu lako la kupatwa na uovu. Hakuna mwanamume anayetumikia akiwa askari ajitiaye mwenyewe katika shughuli za kibiashara za maisha, ili kwamba aweze kupata ukubali wa yule aliyemwandika orodhani awe askari.” (2 Timotheo 2:3, 4, NW ) Ni lazima Wakristo wafanye kazi na kujitafutia wao wenyewe na jamaa zao riziki inayopatikana kwa njia ya unyofu. Lakini je! halingekuwa jambo la kushangaza Mkristo aliye wakfu akinenwa hasa kuwa mkuu wa kikazi badala ya mhudumu? Je! kwanza kabisa hapaswi kujulikana kuwa mtangazaji wa Ufalme na “askari mwema wa Kristo Yesu”?
14. Andiko la Waebrania 13:18 linaweza kutumiwaje kuhusu shughuli zetu za kikazi?
14 Basi, katika mambo ya kazi mtu anahitaji kujichunguza kwa njia mbalimbali. Kwanza, jambo la kwamba huenda tukawa tunashughulika na walimwengu wachoyo halitupi kisababu cha kufuata mazoea yao ya ujanja na udanganyifu wala usemi mbaya wao. Bali, ni lazima ‘tujiendeshe wenyewe kwa unyofu katika mambo yote.’ (Waebrania 13:18, NW ) Ni kweli kwamba tukitenda kwa unyofu huenda wafanya biashara wa ulimwengu huu walio wagumu wasitutendee namna iyo hiyo. Lakini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatubariki kwa mwendo wetu wa unyofu, na hiyo ni njia moja ambavyo tunaweza ‘kupamba kufundisha kwa Mwokozi wetu, Mungu.’ —Tito 2:9, 10, NW.
15. Ni shauri gani la Kimaandiko linalotolewa juu ya majaribio ya kazi za kibinafsi?
15 Kwa kuwa sisi ni watu tunaotaka kuendelea kukaa bila kuchafuliwa na ulimwengu huu, inatupasa “tuwatendee watu wote mema; na hasa jamaa ya waaminio.” (Wagalatia 6:10) Lakini hatungekuwa tukifanya hivyo kama tungeendeleza kwa uchoyo jaribio la biashara ya kibinafsi kwa kutumia ufahamiano wetu na watu wa Mungu ili tupate faida kutokana nao. Bila shaka, Wakristo wanapaswa ‘kuenenda kama watu wenye hekima.’ (Waefeso 5:15) Jambo la kwamba mtu anayeitwa ndugu anatujia akiwa na mpango wa kujitajirisha upesi halipasi kutufanya tusadikishwe kwa urahisi kumpa pesa zetu. Tengenezo la Mungu limekuwa na sababu nzuri ya kutoa onyo mara kwa mara juu ya wale wanaosema ni ndugu zetu wa kiroho, lakini wanaojaribu kujifaidi isivyofaa kutokana na “kondoo” za Yehova.
Si wa Kilimwengu kwa Kila Njia
16. Ni nini nyingine za njia za kuonyesha kwamba tunaendelea kuwa “bila doa kutokana na ulimwengu”?
16 Ni wazi kwamba hatuwezi kutaja kila njia ambayo Mashahidi wa Yehova wanaonyesha kwamba wanaendelea kuwa “bila doa kutokana na ulimwengu.” Lakini, kwa uhakika njia za kukaa bila kutiwa doa na ulimwengu huu si kujiingiza kupita kiasi katika vileo, kufurahia sana michezo yenye mashindano makali au jeuri, kutumia saa nyingi kutazama sinema au vipindi vya televisheni vinavyoonyesha majambazi, wauaji, na watu wengine wenye mwenendo mchafu, kusoma vitabu vyenye kujaa mambo ya ngono na kucheza michezo ya video. (1 Wakorintho 6:9, 10; 15:33; Wagalatia 5:19-26; 1 Petro 4:3) Yehova anatazamia mashahidi wake waepuke mambo ya kupita kiasi, uasherati na jeuri ya ulimwengu huu. Kwa hiyo haitupasi kutafuta maarifa ya uovu wa kilimwengu wala kuuonja tuwe tunajua namna ulivyo bali inatupasa tuwe ‘watoto wachanga katika ubaya,’ ambao hawana hatia. — 1 Wakorintho 14:20; linganisha 1 Yohana 3:2, 3.
17. Kutokutiwa kwetu doa na ulimwengu kunapasa kuhusuje uhusiano wetu na wengine?
17 Kukaa bila kutiwa doa na ulimwengu huu kunahusu kila upande wa maisha yetu na pasipo shaka kunatia ndani uhusiano wetu na wengine. Ijapokuwa vitabia kama wivu mkali, magombano, kujigamba na kusema uongo ni mambo yanayoonekana sana katika ulimwengu huu, hayapasi kuwa kati yetu, kwa maana Yakobo aliandika hivi: “N’nani aliye na hekima na ufahamu kwenu? Na aonyeshe kazi zake kwa mwenendo wake mzuri, katika upole wa hekima. Lakini, mkiwa na wivu wenye uchungu na ugomvi mioyoni mwenu, msijisifu, wala msiseme uongo juu ya kweli. Hekima hiyo siyo ile ishukayo kutoka juu, bali ni ya dunia, ya tabia ya kibinadamu na Shetani. Maana hapo palipo wivu na ugomvi, ndipo palipo machafuko, na kila tendo baya.” (Yakobo 3:13-16) Ni jambo la maana kama nini kudhihirisha “upole wa hekima” na ‘kutafuta kwa bidii kuwa na amani na watu wote’! (Waebrania 12:14) Kwa uhakika, sisi mashahidi washikamanifu wa Yehova hatuwezi kuruhusu tofauti za kibinafsi tu ziharibu uhusiano wetu na ndugu na dada zetu katika imani. Badala ya hivyo, ni lazima ‘kuchukuliana, na kusameheana, kama Yehova alivyotusamehe sisi. ‘ (Wakolosai 3:13) Hiyo siyo njia ya kawaida ya kilimwengu ya kushughulika na wengine, lakini ndiyo njia ya kimungu.
18. Kujitenga kwetu na ulimwengu kunaonekana wazi hasa tunapofanya nini?
18 Kufuatia amani na watu ndani na nje ya kundi la Kikristo ni njia ya maana ya kuonyesha kwamba sisi hatukutiwa doa na ulimwengu huu. Lakini kujitenga kwetu na ulimwengu kunaonekana wazi hasa tunapodumisha msimamo wetu tukiwa askari hodari wa Yesu Kristo, tukiwa tumevaa kabisa silaha za kiroho kutoka kwa Mungu na ‘nyayo zetu zimevishwa vifaa vya habari njema za amani.’ (Waefeso 6:11-18, NW) Umati mkubwa wa watu ungali una njaa na kiu ya ujumbe wa Ufalme unaotoa uzima. Basi, bila choyo na tutumie mali zetu, akili na nguvu zetu katika kazi ile kubwa ya kutangaza “habari njema” katika wakati mfupi ambao ungali umebaki mpaka mfumo huu umalizike.—Mathayo 24:14.
19. Tunaweza kutazamia Shetani afanye nini katika hizi siku za mwisho zinazosonga kasi, lakini kwa msaada wa kimungu tutaweza kufanya nini?
19 Katika hizi siku za mwisho zinazosonga mbio, Shetani, mungu wa ulimwengu huu, atafanya mashambulizi zaidi juu yetu sisi tulio mashahidi washikamanifu wa Yehova. Katika jitihada ya kufa au kupona ya kutuondosha kwenye utumishi mtakatifu tunaotolea Mungu wetu, Ibilisi atafanya mali za ulimwengu, vitu vyake vyenye kumetameta, elimu yake ya juu na mambo mengine mengi yaonekane kuwa ya kupendeza sana machoni petu. Lakini kwa msaada wa kimungu usiokwisha tutaweza kuendelea kuwa “bila doa kutokana na ulimwengu” hata tumletee sifa Mungu wetu mtakatifu, Yehova.—Kutoka w 10/1/84.
Wewe Ungejibuje?
◻ Kulingana na Yakobo 1:27, ni nini mengine ya matakwa ya ibada ya kweli?
◻ Ni nini nyingine za njia za kuendelea kukaa bila kuchafuliwa na ulimwengu huu?
◻ Jambo la kwamba ulimwengu huu unapita linaweza kugeuzaje maoni yetu juu ya elimu ya juu?
◻ Kwa habari ya shughuli za kikazi, uchunguzi wa kibinafsi unahitajiwa katika njia gani?
◻ Mashahidi wa Yehova wanaweza kuonyeshaje kwamba ‘hawana doa kutokana na ulimwengu’ kwa habari ya mwenendo na uhusiano wao na wengine?
[Picha katika ukurasa wa 16]
Mashahidi wa Yehova wanaepuka jeuri ya kilimwengu kwa kuwa ni Wakristo wasiokuwamo
[Picha katika ukurasa wa 17]
Si maendeleo ya kimwili yanayoleta ukubali wa Mungu
[Picha katika ukurasa wa 19]
Yehova anatazamia mashahidi wake waendelee kukaa bila kutiwa doa na mambo ya kupita kiasi, uasherati na jeuri ya ulimwengu huu