Wewe Ni Tofauti na Ulimwengu Jinsi Gani?
“Namna ya ibada iliyo safi na isiyochafuliwa kwa maoni ya Mungu wetu na Baba ni hii: . . . kujitunza bila doa kutoka kwa ulimwengu.”—YAKOBO 1:27, New World Translation.
1, 2. Ni nani aliyesema kwamba Wakristo wangekuwa tofauti na ulimwengu? Ni kwa sababu gani Mashahidi wa Yehova wanapaswa kutazamia kuwa tofauti na ulimwengu?
YESU ndiye aliyesema kwamba Wakristo hawapaswi kuwa sehemu ya ulimwengu. (Yohana 15:19) Na katika sala aliyotoa kwa Babaye usiku ule kabla hajafa, alisikiwa akisema: “Nimewapa neno lako, lakini ulimwengu umewachukia, kwa sababu wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile mimi nisivyo sehemu ya ulimwengu.” Halafu, karibu mara iyo hiyo, akarudia hivi: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile mimi si sehemu ya ulimwengu.”—Yohana 17:14, 16, NW.
2 Dini zilizo nyingi za Jumuiya ya Wakristo hazifanyi jitihada yo yote zitimize maneno hayo. Lakini, Mashahidi wa Yehova wanatambua kwamba Wakristo leo hawana jingine ila kuendelea kujitenga na ulimwengu. Wanajua kwamba Shetani ndiye mtawala wa ulimwengu huu. (Yohana 14:30; 1 Yohana 5:19) Kuwa sehemu ya ulimwengu kunamaanisha kuwa chini ya uvutano wa Shetani. Yakobo alionya hivi: “Kwa hiyo, ye yote anayetaka kuwa rafiki ya ulimwengu anajifanya mwenyewe kuwa adui ya Mungu.” (Yakobo 4:4, NW) Kwa hiyo, twapaswa kutazamia kuwa tofauti.
3. Ni mambo gani ya msingi yanayowafanya Mashahidi wa Yehova wawe tofauti na watu wanaowazunguka?
3 Lakini Mashahidi wa Yehova ni tofauti kwa jinsi gani? Yesu alisema kwamba Wakristo hawangeondolewa kimwili kutoka ulimwenguni. (Yohana 17:15) Na, kwa kweli, Mashahidi wa Yehova wanaishi katika mitaa yake, na wengi wao wanafunga ndoa na kuwa na jamaa, kama watu wengine wote. Wao pia, wanapaswa kutafuta kazi, wakabiliane na kupungua kwa thamani ya pesa, na kulipa kodi zao. Lakini wao ni tofauti. Katika makala inayowahusu, mhariri wa dini wa gazeti moja la United States alieleza ni kwa nini alidhani ndivyo ilivyo. Alisema: “Kinachowatofautisha Mashahidi na wengi wa wachambuzi wao, labda, ni kwamba maisha yao yote—jinsi wanatumia saa zao na wanazitumia wakiwa na nani—yamekazwa kikiki kwenye imani zao.” Barabara! Mashahidi wa Yehova wamejiweka wakfu kabisa kwa Yehova Mungu. Wanaamini kikweli ahadi zake katika Biblia, na wanachukua kwa uzito sana amri zote za Mungu zilizomo. (1 Yohana 5:3) Hilo linawafanya wawe tofauti.
4. Ni mambo gani yanayofanya kujitenga na ulimwengu kuwe kugumu? Kwa hiyo, sisi sote tunapaswa kufanya nini pindi kwa pindi?
4 Lakini, kujitenga hivyo hakupendwi na wengi wala si rahisi. Katika maisha yetu ya kila siku mkazo wa kutenda kama wengine wanavyotenda ni mkubwa. Wengi wetu tuna tamaa ya kisilika ya kutotaka kuwa tofauti sana na watu wengineo. Masuala yanayohusu kutokuwamo yanapotokea, inataka usadikisho wenye nguvu wa kuwa tofauti na kutii amri za Yehova. (Matendo 5:29; 15:28, 29) Kwa hiyo, ni jambo la hekima kila mtu ajichunguze mwenyewe pindi kwa pindi aone msimamo wake ni nini katika habari ya kutokuwa sehemu ya ulimwengu.—2 Wakorintho 13:5.
Wenye Bidii Katika Utumishi wa Shambani
5. (a) Wengine wasio Mashahidi wanasema nini juu ya bidii ya Mashahidi wa Yehova katika kazi ya kuhubiri? (b) Ni kanuni gani nyingine za Biblia zinazowasukuma Mashahidi wawe wenye bidii katika kazi hiyo?
5 Kwa mfano, Mashahidi wa Yehova wanajulikana sana kwa ajili ya bidii yao katika kuhubiri. Kwa kweli hilo linawafanya wawe tofauti. Wengine wanavutiwa nao kwa ajili ya hilo, hali wengine wanakasirishwa. Wamisionari wa tengenezo moja la kievanjeli wanaripoti kwamba po pote wanapoenda ulimwenguni wanakutana na watu wa mahali hapo ambao ni mashahidi wanaotenda, wenye bidii kwa ajili ya Yehova! “Zungumza kwa muda mrefu sana na . . . misionari [ye yote] mahali po pote ulimwenguni juu ya hali za mahali hapo, nawe utasikia Mashahidi wa Yehova wakitajwa,” kikasema kimoja cha vichapo vyao. Ni kwa sababu gani Mashahidi ni wenye bidii sana katika kazi hiyo? Sababu ni kwamba kuhubiri habari njema ni mapenzi ya Mungu na alama ya kutambulisha Mkristo wa kweli. (Mathayo 28:19, 20; Waefeso 6:14, 15; Ufunuo 22:17) Leo, kuhubiri huko kunakofanywa na Mashahidi wa Yehova ni wonyesho wa peupe wa ushikamanifu wao kwa Ufalme wa Mungu na tamaa yao ya kuwasaidia wengine wamwabudu Yehova.—Isaya 2:2-4; Mathayo 24:14.
6. Ni maulizo gani mengine tunayopaswa kujiuliza wenyewe ili tuchunguze maoni yetu kuelekea kazi ya kuhubiri habari njema za Ufalme?
6 Kazi ya kuhubiri ni yenye umaana kadiri gani kwako? Katika ulimwengu, wengi wana maoni kwamba kutafuta riziki, au hata tafrija, ni jambo la maana zaidi ya mazoea ya kidini. (2 Timotheo 3:4; 1 Yohana 2:16) Lakini, Paulo alimwandikia Timotheo hivi: “Jitunze nafsi yako, na mafundisho yako. Dumu katika mambo hayo; maana kwa kufanya hivyo utajiokoa nafsi yako na wale wakusikiao pia.” (1 Timotheo 4:16) Je! wewe una maoni hayo? Je! pia wewe unakumbuka onyo la mtume Petro kwamba unapaswa ‘kukaribisha akilini kuwapo kwa siku ya Yehova’? (2 Petro 3:12, NW) Ikiwa ndivyo, basi unajua kwamba kuhubiri habari njema za Ufalme ni jambo lenye kutaka hatua ya haraka. Huenda hilo likakusukuma utende katika njia ambazo huenda zikaonekana kuwa ngeni kwa wasio Mashahidi.
7. Wengi wamechukua hatua gani kuhusiana na kazi ya kuhubiri? Kwa sababu gani?
7 Kwa mfano, John, mwalimu wa shule katika Ghana, aliyachukua Maandiko kwa uzito. Kwa hiyo akaacha kazi yake ili atumie wakati mwingi zaidi akiwaambia majirani juu ya Ufalme. Brian, mvulana Mwingereza, aliacha nafasi yake ya kwenda kwenye chuo kikuu ili aweze kuwa mhubiri wa wakati wote; na Eva, msichana Mwamerika, aliacha chuo baada ya vipindi vichache vya masomo kwa sababu iyo hiyo. Je! vijana hao walitenda isivyofaa au kwa upumbavu? Kwa kweli, kwa ye yote anayechukua Biblia kwa uzito, walilofanya lilikuwa jambo la kiasi na la akili. Kinyume kabisa cha kuhatirisha wakati ujao wao, walikuwa wakisaidia kuufanya uwe hakika. Kama Paulo alivyosema, kazi waliyochagua inamaanisha wokovu, ‘kwao na kwa wale wanaowasikia.’—1 Timotheo 4:16.
Mwendo wa Aina Tofauti
8. Ni kanuni gani ya Kibiblia katika Waebrania 1:9 ambayo pia inasaidia kuwafanya Mashahidi wa Yehova wawe tofauti?
8 Hii ni kanuni nyingine inayowafanya Wakristo wawe tofauti na ulimwengu: “Umependa haki, umechukia [maovu].” (Waebrania 1:9) Katika kifungu hicho, maneno hayo yameelekezwa kwa Yesu Kristo, lakini Mashahidi wa Yehova wanatambua kwamba yanatoa kiwango kwa Wakristo pia. (1 Petro 2:21) Ni lazima tupende yale ambayo Mungu anasema ni ya uadilifu na kuchukia yale ambayo Mungu anasema ni maovu.
9. (a) Ni nini baadhi ya namna namna za uvunjaji wa sheria? (b) Maoni ya kundi la Kikristo kuelekea uvunjaji wa sheria yanatofautianaje na yale ya ulimwengu?
9 Mtume Paulo alitaja baadhi ya aina za maovu kwa maneno haya: “Waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti, wala wevi, wala watamanio, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi.” (1 Wakorintho 6:9, 10) Leo, ulimwengu unaachilia sana mabaya, hasa mambo ya ukosefu wa adili. Lakini viwango vya Biblia haviwezi kubadilishwa. Biblia inasema kwamba Mkristo ye yote anayehusika katika mazoea ya ukosefu wa adili apaswa kusaidiwa kwa upendo abadili njia yake. (Wagalatia 6:1; Yakobo 5:19, 20) Akikataa kufanya badiliko, basi apaswa kuepukwa na Wakristo.—1 Wakorintho 5:9-13.
10. Ni kwa sababu gani Mashahidi wa Yehova wanapaswa kujiepusha na vitendo vya uvunjaji wa sheria?
10 Wengine wamedai kwamba njia hiyo ya kushughulikia mambo si ya upendo au ni ya kupita kiasi. Wanapendelea njia ya ulimwengu ya kuachilia mabaya. Je! ndivyo maoni yako yalivyo? Au je, unatambua kwamba vitendo hivyo havimaanishi kukosa kumpenda mkosaji bali ni kuchukizwa na matendo yake ya kuvunja sheria. Na je, unafahamu kwamba kundi la Kikristo lapaswa kutenda kwa njia hiyo iwapo litabaki likiwa la Kikristo? Yakobo alisema: “Dini ambayo Mungu Baba yetu anakubali kuwa safi na isiyo na kosa ndiyo hii: . . . mtu kuendelea kuwa asiyechafuliwa na ulimwengu.” (Yakobo 1:27, New International Version) Kikundi kingewezaje kudai kina dini ya kweli kikijiruhusu kichafuliwe na dhambi nzito?
11. Viwango vya Kikristo vina matokeo gani juu ya usemi wa Mkristo?
11 ‘Kuchukizwa kwa Mkristo na ovu’ kunahusu mengi zaidi. Biblia inasema: “Uasherati usitajwe kwenu kamwe, wala uchafu wo wote wala kutamani, kama iwastahilivyo watakatifu; wala aibu wala maneno ya upuzi wala [matusi].” (Waefeso 5:3, 4) Kwa hiyo Wakristo halisi wanajulikana kati ya washiriki wao kuwa wasiotumia lugha chafu-chafu, wasioeleza mizaha ya matusi, au wasiopata furaha isiyofaa kwa kuzungumza mambo machafu. Akili safi na usemi safi ni mambo yanayoendelea kuwa haba leo.
12. Ni jinsi gani Mashahidi wa Yehova ni tofauti na ulimwengu kwa habari ya tafrija?
12 Mashahidi wa Yehova hata wako tofauti kwa habari ya tafrija. Kwa kuwa “ulimwengu mzima uko katika uwezo wa yule mwovu,” wamejifunza kuwa waangalifu kuhusiana na tafrija inayopatikana katika ulimwengu. (1 Yohana 5:19, NW) Wanaepuka kabisa michezo mingi ya karamuni, magazeti, kanda za video, sinema, muziki, na mawonyesho ya televisheni yenye mambo ya kishetani au yenye uchafu wa ngono, au yanayokazia jeuri ya kuchukiza yenye ukosefu wa adili. Wanajihadhari, pia, na inayoitwa tafrija ya jamaa inayotia moyo mawazo ya ngono za ovyoovyo au ya kuachilia ubaya wote ambayo Wakristo hawawezi kukubali. (1 Wakorintho 15:33) Ye yote anayechukua Biblia kwa uzito hangetafuta tafrija katika mambo ambayo hayapasi hata kutajwa kati ya Wakristo.
13. Je! ni jambo la akili ndogo kujiwekea vizuizi kwa habari ya tafrija? Eleza.
13 Je! hayo ndiyo maoni yako? Au je, unahisi kwamba maoni hayo yanawafanya Mashahidi wa Yehova kuwa watu wa akili ndogo na wenye kuweka vizuizi vingi? Ikiwa ndivyo, fikiria hivi: Wakati bidhaa fulani ya kuliwa inapogunduliwa imeharibika na mara moja inaondolewa kwenye duka, wanunuzi hawalalamiki kwamba uhuru wao unawekewa vizuizi kwa sababu hawawezi kununua bidhaa hiyo tena. Badala yake, wanashukuru kwa kulindwa wasile chakula chenye sumu. Hali moja na hiyo, Mashahidi wa Yehova hawalalamiki kwamba uhuru wao unazuiwa kidogo wakati wanapotajiwa uchafu wa tafrija nyingi ya ulimwengu. Badala yake, wanatulia kwa sababu ya kulindwa na hatari inayoletwa na uchafu huo.
Wanapendana
14. Ni sifa gani ambayo Yesu alisema ingefanya jamii ya Kikristo iwe tofauti sana na ulimwengu unaowazunguka?
14 Hiki ni kipimo kingine cha Wakristo kujitenga na ulimwengu. Usiku ule kabla hajafa, Yesu aliwaambia wafuasi wake hivi: “Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” (Yohana 13:35) Ni kwa sababu gani upendo ungekuwa ishara kwa watu wa nje? Kwa sababu, kwa ujumla, hali katika ulimwengu leo ni kama vile Paulo alisema ingekuwa: “Watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, . . . wasiowapenda wa kwao.” (2 Timotheo 3:2, 3) Katika mazingira ya namna hiyo, jumuiya ya watu wa ulimwenguni pote wanaopendana ingekuwa tukio la ajabu. Udugu huo upo kati ya Mashahidi wa Yehova—1 Petro 2:17.
15. Ni nini nyingine za hali ambazo katika hizo Mashahidi wa Yehova wana nafasi ya kuonyeshana upendo?
15 Upendo huo unaonekana wazi sana na mara nyingi unatokeza maelezo ya watu wa nje wakati Mashahidi wanapokusanyika kwenye mikusanyiko yao. Kunapokuwa misiba mikubwa, Mashahidi wanachukua hatua mara moja, na kupelekea ndugu zao msaada. Na ndani ya kundi, Wakristo wa kweli wanaonyeshana upendo na kufikiriana. Hata kunapokuwako tofauti za nyutu, wanajaribu sana ‘kuchukuliana na kusameheana.’—Wakolosai 3:12-14.
Hawakwazani
16. (a) Paulo alizungumza hali gani iliyowapa Wakristo wa karne ya kwanza nafasi nzuri ya kuonyeshana kina cha upendo wao? (b) Alieleza juu ya kanuni gani yenye kutumika katika njia nyingi za kisasa?
16 Upendo huo unawafanya Mashahidi wawe tofauti katika njia nyingine. Leo, wengi wanahangaikia haki zao na kuzilinda kwa wivu. Lakini mtume Paulo aliweka kiwango tofauti: “Na tufuate mambo ya amani na mambo yafaayo kwa kujengana.” (Warumi 14:19) Katika habari hiyo, Paulo alikuwa akizungumza juu ya tatizo lililokuwapo kuhusiana na chakula. Wakristo, tofauti na Wayahudi waliokuwa chini ya Torati ya Musa, walikuwa huru kula cho chote walichotaka maadamu hawakuwa walafi. Hata hivyo, wengine, ambao tangu utoto walikuwa wameona vyakula hivyo kuwa vya kuchukiza, walisumbuliwa mawazo walipoona Wakristo wenzao wakivila. Je! Wakristo hao wengine waling’ang’ania haki yao ya kula cho chote walichotaka? Ikiwa walifuata shauri la Paulo, hawakufanya hivyo. Yeye alisema: “Ni vyema kutokula nyama wala kunywa divai wala kutenda neno lo lote ambalo kwa hilo ndugu yako hukwazwa.” (Warumi 14:21) Hilo ni shauri la upendo kama nini! Je! unaweza kuona jinsi shauri hilo linaweza kutuongoza katika maeneo mengine?
17, 18. (a) Kanuni katika Warumi 14:21 inaweza kutumiwaje kwa habari ya kileo kikali? (b) Inaweza kutumiwaje kwa habari ya mavazi? (c) Unaweza kufikiria sehemu gani nyingine ambazo kanuni iyo hiyo ikitumiwa tutasaidiwa tuonyeshane upendo?
17 Kwa mfano, Biblia inaruhusu Wakristo kunywa vileo kwa kiasi. (1 Timotheo 3:8; 5:23) Lakini wengine wanasumbuliwa mawazo na vileo vikali. Wengine hawajavizoea au hawawezi kuvinywa. Kama ungekuwa kwenye karamu na mtu wa namna hiyo, je, ungejaribu kumkaza au kumwaibisha ajiunge nawe katika kunywa kileo? Au ingekuwa afadhali wewe mwenyewe uepuke kileo ili usimtokezee matatizo?
18 Fikiria mfano mwingine: juu ya mavazi. Biblia haielezi ni mavazi ya aina gani ambayo Mkristo anapaswa kuvaa, ingawa inasema yanapasa kuwa ya kiasi na nadhifu. (1 Timotheo 2:9) Leo, nchi zilizo nyingi zina viwango fulani vya mavazi vinavyoonwa kuwa vyakubalika katika jumuiya ya kawaida. Mara nyingi, kiwango hicho kinakubali mavazi mengi yanayotofautiana, lakini yanapotofautiana sana na kiwango hicho inaonekana ni kujionyesha, jambo la kuamsha nyege, au si jambo la kawaida. Wakristo, wanaume na wanawake, wanapaswa kukumbuka hilo. Je! wewe una nia ya kuwekea uhuru wako wa mavazi vizuizi kwa ajili ya habari njema na ili usiwakwaze ndugu zako?
19-21. (a) Ni kwa sababu gani Mashahidi wa Yehova wanajitahidi kudumisha hali yao ya kujitenga na ulimwengu? (b) Ni katika eneo gani jingine tunamojitahidi kuwa tofauti na ulimwengu?
19 Ndiyo, Yesu alisema kweli aliposema kwamba Wakristo hawangekuwa “sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:16, AW) Katika kuzihubiri habari njema, katika kuepuka lililo ovu, na katika upendo na kufikiriana, Mashahidi wa Yehova ni tofauti kweli kweli. Kujitenga huko kunawaletea Mashahidi baraka, zaidi ya kuwalinda na matatizo mengi yanayoupata ulimwengu leo kwa wingi.
20 Je! wewe unathamini na kusitawisha hali hiyo ya kujitenga maishani mwako mwenyewe? Kumbuka, kama Mashahidi wa Yehova hawangejitenga, wangekuwa wanafanana na ulimwengu, ambao Shetani Ibilisi ndiye Mungu wao. (2 Wakorintho 4:4) Wangepoteza kitambulisho chao cha wazi cha kuwa “watakatifu,” na wangeshindwa kujitunza wakiwa ‘hawajachafuliwa na ulimwengu.’ Kwa hiyo, hawangekuwa tena na “dini safi, ambayo haijaharibiwa, machoni pa Mungu.” (Yakobo 1:27, The Jerusalem Bible, 1 Petro 1:14-16) Ukijikuta unatamani kuwa kama ulimwengu, kumbuka onyo katika Yakobo 4:4.
21 Mtume Paulo alitabiri kwamba kitabia kingine kingekuwako kwa wingi katika ulimwengu leo. Alisema kwamba watu wangekuwa “wenye kupenda fedha.” (2 Timotheo 3:1, 2) Kwa kutimiza maneno yake, kufuatia pesa sasa ni kani yenye nguvu sana hata kwamba kwa wengi hizo ndizo uvutano wenye nguvu zaidi maishani mwao. Je! Wakristo ni tofauti katika hilo pia? Je! inawezekana kuendelea kuishi katika ulimwengu wa leo bila kuwa ‘mpenda fedha’? Tutazungumza hilo katika makala inayofuata. (Itaendelezwa.)
Je! Unaweza Kukumbuka?
◻ Ni kwa sababu gani Mkristo angetazamia kuwa tofauti na ulimwengu?
◻ Ni maandiko gani yanayosaidia Mashahidi wa Yehova wawe na maoni yanayofaa juu ya kazi ya kuhubiri?
◻ Ni katika njia gani tofauti matumizi ya andiko la Waebrania 1:9 yanafanya Mashahidi wa Yehova wawe tofauti na ulimwengu?
◻ Kutumia kanuni inayoelezwa katika Warumi 14:21 kunakuwa na matokeo gani juu ya mwenendo wao?
[Picha katika ukurasa wa 25]
Mashahidi wa Yehova wamejifunza kujihadhari na tafrija inayopatikana katika ulimwengu