Yule “Neno” Alikuwa Mungu?
WATU wanaoamini kwamba Mungu ni Utatu, na kwamba Yesu ni Mungu, wanaonyesha Yohana 1:1 na Yohana 20:28 kuwa uthibitisho wa imani hiyo.
Katika tafsiri nyingi Yohana 1:1 inasema: “Hapo mwanzo kulikuwako Neno, naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye neno alikuwa Mungu.” Lakini, watafsiri wenye uaminifu wameliona kuwa jambo linalohitajiwa kabisa kukiri kwamba pana tofauti kati ya hayo matumizi mawili ya neno “Mungu” katika andiko hilo.
The New English Bible inasema, “Kile Mungu alikuwa, ndicho Neno alikuwa.” Today’s English Version inasema, “Yeye alikuwa sawa kama Mungu.” An American Translation inasema, “Yule Neno alikuwa wa kimungu.”
Kwa sababu gani tafsiri hizo hazisemi vyepesi tu kwamba Neno “alikuwa Mungu”? Ni kwa sababu katika Kigiriki, lugha iliyotumiwa kuandika maneno hayo mara ya kwanza kabisa, matumizi yale ya pili ya neno “Mungu” si sawa na yale ya kwanza. Neno “ho” ambalo ni kionyesho cha kutaja wazi jambo fulani limewekwa kabla ya matumizi ya kwanza ya neno Mungu lakini kabla ya matumizi ya pili neno hilo halikuwekwa. Kwa hiyo The Anchor Bible inasema hivi: “Ili kuhifadhi katika Kiingereza utofautiano mdogo sana unaokuwa katika neno theos [Mungu] wakati linapokuwa na wakati lisipokuwa na lile neno la kutofautisha jambo na mambo mengineyo, watu wengine (Moffatt) wanatafsiri kwamba ‘Yule Neno alikuwa wa kimungu.’ “
Tunaweza kuelewa vizuri zaidi maneno ya Yohana hapa tukichunguza-chunguza kwa makini kabisa vile alivyosema. Angalia tena kwamba yeye aliandika hivi: “Hapo mwanzo kulikuwako Neno.” Bila shaka, maneno hayo hayakuwa yakisema juu ya mwanzo wa Mungu, kwa maana Mungu hakuwa na mwanzo. (Zaburi 90:1, 2) Ulikuwa ni mwanzo wa mambo ambayo Yohana alikuwa akiyazungumza hapo, kutia ndani uumbaji wa vitu vingine vingine vyote kupitia “Neno.” Ndipo Yohana akasema: “Naye Neno alikuwako kwa Mungu [pamoja na Mungu, tafsiri ya New World].” Ni wazi kwamba wakati mtu anapokuwa kwa mtu fulani (au anapokuwa pamoja na huyo mwingine), haiwi kwamba yeye pia ndiye mtu yule mwingine aliye pamoja naye.
Bila shaka, jambo lililo la maana ni vile Yohana alivyomaanisha wakati alipoandika kifungu hicho. Je! hilo linatokeza tatizo? Linatokeza ikiwa wewe unataka kifungu hicho kiseme Yesu ni “MUNGU,” kwa maana ni jambo lililo wazi sana kutokana na maandishi ya Yohana kwamba yeye hakumwelewa Yesu kuwa “Mungu” katika maana ile ambayo Baba ni Mungu. Kwa mfano, katika sura iyo hiyo, Yohana aliandika hivi: “Hakuna mtu amewahi kuona Mungu; ni yule Mwana wa pekee, ambaye yuko karibu na moyo wa Baba zaidi ya wengine wote, ambaye amemfanya yeye ajulikane.” (Yohana 1:18, The Jerusalem Bible) Je! kuna mtu ye yote ambaye amepata kuona Mungu? Hapana. Je! kuna mtu ye yote ambaye amepata kuona Yesu? Ndiyo!
Imani ya Athanasia ya Jumuiya ya Wakristo, ambayo inaeleza maana ya Utatu, inasema “hakuna aliye mkuu zaidi au mdogo zaidi ya mwingine.” Lakini Yohana anarudia-rudia kuandika maneno ya Yesu mwenyewe yenye kuonyesha alimnyenyekea Mungu. Yeye ‘alipelekwa’ na Baba yake, akagawiwa kazi mbalimbali na Baba yake, akaambiwa na Baba yake mambo ya kufanya na ya kusema, kisha akasema hakuja kufanya mapenzi yake mwenyewe “bali mapenzi yake [aliyempeleka].”—Yohana 6:38; 3:17; 5:36; 8:28; 12:49, 50.
Yohana pia aliandika maneno yaliyosemwa na Yesu mwenyewe kwamba Baba ndiye “Mungu wa pekee wa kweli,” na kwamba “Baba ni mkuu kuliko mimi.” (Yohana 17:3; 14:28) Aliandika pindi sita ambazo katika hizo Yesu alimwita Baba “Mungu wangu.” Pindi tano ambazo Yesu anasema “Mungu wangu” ni za muda mrefu baada ya kufufuliwa kwake na kupaa mbinguni. (Yohana 20:17; Ufunuo 3:2,12) Nyakati nyingine zaidi zisizopungua tano, Yohana aliandika kwa uangalifu, si ile tofauti iliyo kati ya Baba na Mwana-Kondoo tu, bali pia tofauti iliyo kati ya Mungu na yule Mwana-Kondoo Yesu Kristo. (Ufunuo 1:1; 7:10; 21:22; 22:1-3) Yohana hasemi aliandika ili aonyeshe kwamba Yesu ni Mungu, wala hata “Mungu Mwana,” bali “ili mpate kuamini ya kwamba Yesu ndiye Kristo, Mwana wa Mungu.”—Yohana 20:31.
Maneno hayo yanaonyesha uhusiano ambao Yohana alijua ulikuwa kati ya Yesu na yule ambaye Yohana anatuambia Yesu alimwita “Mungu.” Andiko la Yohana 1:1 haliyapingi maneno hayo. Tafsiri iliyo sahihi ya andiko hilo ni hii: “Mwanzoni Neno alikuwako, na Neno alikuwa pamoja na Mungu, na Neno alikuwa mungu mdogo.” Uo huo ndio mtungo wa maneno utakaokuta kwenye Matendo 28:6, ambapo watu wa Melita walifikiri Paulo alikuwa “mungu” mdogo.
Basi, namna gani juu ya mshangao uliotamkwa na Tomaso wakati alipomwona Yesu mfufuliwa: “Bwana wangu na Mungu wangu! ” (Yohana 20:24-29) Tomaso alivutwa sana na kutambua kwa njia yenye kutokeza sana kwamba Yesu Kristo alikuwa amefufuliwa kweli kweli, na kwamba alikuwa anaonana naye ana kwa ana. Lakini, hakuna jambo lo lote katika masimulizi linaloonyesha kwamba Tomaso alifikiri Yesu alikuwa sawa na Baba yake. Yohana, ambaye ndiye aliandika maneno ya Tomaso, alikuwa amemtaja Yesu kuwa akisema kwamba hata wanadamu waliitwa “miungu.” Kwa uhakika, Bwana Yesu Kristo aliyefufuliwa ni mkuu kuliko mwanadamu ye yote. (Yohana 10:34, 35) Na katika sura iyo hiyo ambamo tunasoma maneno ya Tomaso, Yohana aliandika maneno ya Yesu kwamba yule Baba ni Mungu wa Yesu.—Yohana 20:17.
Paulo alionyesha namna Wakristo wa karne ya kwanza walivyokuwa na ufahamu sahihi juu ya uhusiano ulio kati ya Yesu na Baba yake wa kimbingu wakati alipoandika kwamba “kwetu sisi Mungu ni mmoja tu, aliye Baba . . . yuko na Bwana mmoja Yesu Kristo.”—1 Wakorintho 8:6.