Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 5/15 kur. 9-14
  • Semeni Neno la Mungu Pasipo Woga Katika Kizazi cha Nyukilia

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Semeni Neno la Mungu Pasipo Woga Katika Kizazi cha Nyukilia
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kula Neno la Mungu na Kwenda Kulisema Ulimwenguni Pote
  • Kueneza Neno la Mungu Kote Kote Katika Ulimwengu Wenye Woga
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • “Roho ya Uhai Itokayo kwa Mungu Ikawaingia”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • “Uyatie Alama Mapaji ya Nyuso”
    Hatimaye Ibada Safi ya Yehova Yarudishwa!
  • Tutakuwa Upande wa Nani Taabu ya Ulimwengu Ifikiapo Upeo?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 5/15 kur. 9-14

Semeni Neno la Mungu Pasipo Woga Katika Kizazi cha Nyukilia

“Kusema Neno la Mungu pasipo woga.”​—WAFILIPI 1:14, ZSB

1. Muumba wa atomi pamoja na kiini chayo cha kati ameagiza nini likasemwa wakati wa miaka 48 iliyopita?

KIZAZI cha nyukilia kimetufikia. Ulimwengu mzima sasa unaelekewa na tisho la kupatwa na vita ya kutumia silaha za nyukilia! Muumba Mwenye Nguvu Zote wa atomi yenye kiini cha kati anajua sana jambo hilo. Neno lake linalohitaji kuhubiriwa ulimwenguni pote linasema nini juu ya siku zetu? Katika wakati wetu yeye ameagiza ‘mtu aliyevalishwa na kitani, aliye na chupa ya wino kando yake’ kwa usemi wa mfano, awe akifanya kazi ya kutia alama.

2. Ni kazi gani ya kutia alama imeendelea, na kwa kusudi gani?

2 ‘Mtu’ huyo amekuwa akitia alama katika vipaji vya nyuso za watu wanaolia na kupiga kite kwa sababu ya machukizo yote yanayoendelea kufanywa, hasa katika makao ya kidini ya Jumuiya ya Wakristo, ambayo inadai kuwa inaabudu Mungu. (Ezekieli, sura ya 9, ZSB) Wanapokumbuka mwenendo uliofuatwa na viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo wakati wa Vita vya Ulimwengu vya Kwanza na Pili, watu hao wanajisikia wakiwa na dhiki kwa kuwa wana sababu ya kuamini viongozi hao wa kidini wangefuata tena mwenendo kama huo wakati wa vita ya kutumia silaha za nyukilia ulimwenguni pote ambayo inaelekea kuwa huenda ikatukia. Kwa sababu ya kutazamia mambo mazuri zaidi yaletwe na wanaoitwa viongozi wa Kikristo ati, wao wanasumbuka sana moyoni kwa sababu ya mambo ambayo sasa viongozi wa kidini wanaruhusu yatendeke katika ulimwengu huu wenye tabia mbovu sana, wenye jeuri na uliogawanyika kidini. Wakiwa katika mfumo wa mambo uliohukumiwa kupatwa na uharibifu wa mapema, watu hao wenye mioyo myema wanaendelea kutiwa alama ya kuhifadhiwa hai waingie katika mfumo mpya wa mambo ya uadilifu.

3. Ni huzuni ya kusikitikia nini iliyo ya maana kuliko huzuni ya kusikitikia maangamizi yanayotazamiwa ya watu wote kwa mpigo mmoja, na kufanywa kwa kazi ya kutia alama kumehitaji nini?

3 Huko mbele hakuna dalili ya kwamba mambo ya kilimwengu yatapata nafuu. Kwa habari ya watu wengi sana wenye mioyo myema ambao wamo ndani ya Jumuiya ya Wakristo na nje yake, ni kitu gani kitakachotuliza woga wao wa kwamba hivi karibuni wataangamizwa kwa njia yenye jeuri, wote kwa mpigo mmoja? Ndiyo, huenda wao wakawa wanahuzunikia hali ya mambo. Lakini, jambo lililo la maana zaidi ni kwamba, je! wao wanahuzunika kwa sababu jina la Mungu wa Biblia Takatifu linahusika na linaendelea kuletewa sifa mbaya kwa sababu ya mwenendo wa wale wanaodai kuwa watu wa Mungu? Hata hivyo, ni nani yule ‘mtu aliyevalishwa na kitani’ kwa usemi wa mfano, anayetia alama wengi zaidi na zaidi kati ya watu hao wanaohuzunika, naye anafanyaje hivyo? Kazi hiyo ya kutia alama haithaminiwi na viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo, nao wanaipinga vikali sana. Basi hali ya kujikaza sana pasipo woga imehitajiwa ili kazi ya kutia alama iweze kufanywa.

4. Yule mtu mwenye kutia alama alitangulia kufananishwa na nani, na kwa hiyo ni sifa gani zinazohitajiwa katika wale wanaotia alama wakati wa sasa?

4 Lakini imesonga mbele kwa mwendo mkubwa zaidi tangu mwaka wa 1935. Imefanywa na jamii ya Wakristo walio wakf kwa Yehova Mungu kupitia Yesu Kristo, ambao walitangulia kufananishwa na nabii Ezekieli, aliyekuwa kuhani wa Israeli wa kale. Yeye ndiye aliyepata njozi ya yule ‘mtu aliyevalishwa na kitani, aliyekuwa na chupa ya wino kando yake.’ Wako wakf kwa Mungu yule yule ambaye Ezekieli alikuwa wakf kwake, kwa hiyo wao ni Mashahidi wa Yehova kama yeye. Ezekieli wa kisasa wa mwaka wa 1984 ni jamii ya kikuhani, ambayo ni ya Israeli wa kiroho, ambao mtume Petro aliwaandikia maneno yale yanayopatikana kwenye 1 Petro 2:9: “Bali ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu.”

5. Kuna makuhani wadogo wangapi watakaokuwa chini ya yule ambaye Yehova anamwapisha aingie katika ukuhani mkuu?

5 Kwa hiyo, sisi tunaitambua jamii ya leo ya Ezekieli kuwa imefanyizwa na wale wanaotumikia kiroho wakiwa makuhani wadogo, chini ya yule Kuhani Mkuu, Yesu Kristo, ambaye Yehova Mungu alimwapisha akamwingiza katika ukuhani “kwa mfano wa Melkizedeki,” aliyekuwa mfalme wa Salemu wa kale na “kuhani wa Mungu Aliye juu sana.” (Zaburi 110:4; Mwanzo 14:18; Waebrania 5:10; 6:20; 7:10, 11, 15-17) Tangu karne ya kwanza, ambayo katika hiyo mtume Petro aliandika barua yake, Yehova Mungu amechagua washiriki wa “ukuhani wa kifalme” huo, ambao mwishowe utakuwa na watu 144,000 wakiwa chini ya Kuhani Mkuu, Yesu Kristo.​—Ufunuo 7:1-8; 14:1-4.

6. Ni wangapi kati ya huo “ukuhani wa kifalme” ambao wangali katika mwili duniani, nao wanatumikia kama mtu gani wa mfano?

6 Leo kuna mabaki madogo tu ya washiriki wa “ukuhani wa kifalme” ambao wangali duniani katika mwili, kulingana na ripoti ya ulimwengu ya utukuzo wa Chakula cha Jioni cha Bwana uliofanywa Machi 29, 1983. Wanatumikia pamoja wakiwa ndio yule mtu aliyevalishwa kitani, anayewatia alama watu wanaostahili katika vipaji vya nyuso zao.

7. Wale ambao walitangulia kufananishwa na yule mtu aliyevaa kitani mwenye chupa ya wino wanapaswa kumtumaini Yehova awafanyie nini?

7 Nabii Ezekieli wa kale alilazimika kuwa na ushujaa mwingi ili asiwaogope wapinzani wa Kiisraeli wa siku zake. Lakini Mungu Mwenye Nguvu Zote alitoa ahadi ya kwamba angeufanya uso wa Ezekieli uwe mgumu sawasawa na nyuso za wahasama (wapinzani) wake, ndiyo, uwe mgumu hata zaidi. Kwa hiyo hakupaswa kuwaogopa wapinzani wake waliokuwa binadamu wa kawaida tu. (Ezekieli 2:4; 3:8; Isaya 51:12) Vivyo hivyo, mabaki ya Wakristo waliopakwa mafuta kwa roho, ambao ndio jamii iliyotangulia kufananishwa na yule mtu aliyevalishwa kitani mwenye chupa ya wino kando yake, wanahitaji kumtumaini Mungu wa Ezekieli ili afanye nyuso zao ziwe ngumu waelekeane bila kusitasita na zile nyuso ngumu za wapinzani walio ndani na nje ya Jumuiya ya Wakristo.

8. Yesu alitoa maagizo gani yanayozifaa siku hizi?

8 Karne kumi na nane zilizopita Mjumbe Mkuu wa Yehova Yesu Kristo, aliwatuma wanafunzi wake katika utume wa kulisema Neno la Mungu pasipo woga katika nchi yao wenyewe. Kabla ya kuwaagiza waondoke, yeye alisema hivi: “Musiwaogope wale wanaoua mwili lakini hawawezi kuua nafsi; lakini zaidi mwogope yeye anayeweza kuharibu nafsi na mwili vilevile katika Gehena.” (Mathayo 10:28, ZSB) Tena, katika kitabu cha mwisho cha Biblia anawaambia mabaki waliopakwa mafuta wa wakati wetu wenyewe hivi: “Usiogope mambo yatakayokupata; tazama, huyo Ibilisi atawatupa baadhi yenu gerezani ili mjaribiwe, nanyi mtakuwa na dhiki siku kumi. Uwe mwaminifu hata kufa, nami nitakupa taji ya uzima.” (Ufunuo 2:10) Maneno hayo ni yenye kutia moyo kama nini!

9. (a) Kufungwa gerezani kwa wengi sana kati ya Mashahidi wa Yehova leo kunaonyesha kwamba wanatii maagizo gani yaliyotolewa hapa juu? (b) Ni matokeo gani tofauti yanayoonyeshwa katika kisa cha Paulo?

9 Wakati tunapokumbuka kwamba leo kuna Mashahidi wa Yehova katika nchi zaidi ya 40 ambako kazi yao imepigwa marufuku au iko chini ya kizuizi cha kisheria​—bila shaka hao sasa wakiwa ni Wakristo wengi kuliko wale waliofungwa gerezani katika karne ya kwanza na ya pili​—Mashahidi wa Yehova wa leo hawaogopi mambo ambayo watalazimika kutaabishwa nayo, kutia ndani kufungwa gerezani. Kufungwa kwa Wakristo kunaweza kuleta matokeo yanayotofautiana na yale ambayo adui walifikiri yangekuwa nayo juu ya Wakristo wenzao. Mtume Paulo aliyekuwa amefungwa aliandika hivi akiwa mahali pake pa uzuizi: “Wengi wa ndugu zetu katika Bwana wakipata matumaini kwa ajili ya vifungo vyangu, wamezidi sana kusubutu kusema Neno la Mungu pasipo woga.”​—Wafilipi 1:14, ZSB.

10. (a) Leo Mashahidi wa Yehova wamewekwa waseme ujumbe wa kutoka chanzo gani? (b) Ni lazima wao wachukue msimamo gani ulio kama wa mitume wa karne 19 zilizopita?

10 Leo, kama ilivyokuwa siku za Paulo, ujumbe unaosemwa na Mashahidi wa Yehova pasipo woga si wa kibinadamu. Ni ule ujumbe unaotolewa katika wakati unaofaa kabisa katika Biblia Takatifu, lile Neno la Mungu Aliye Juu Zaidi, Yehova, ambalo aliliongoza kwa roho yake. Katika Neno hilo anawaambia watu wake walio wakf ambao wamebatizwa ya kwamba ni lazima wawe mashahidi wake, washuhudie juu ya Uungu na Uufalme wake. (Isaya 43:10, 12) Kwa kuwa anawaambia wakaliseme wazi Neno lake lisiloweza kuwa na kosa, ni kiumbe gani, awe ni wa cheo cha juu au cha chini, aliye na haki au mamlaka ya kuwaagiza au kuwalazimisha waache kulisema? Ni lazima wachukue msimamo wa mitume Wakristo wa miaka 1,900 iliyopita, wakati walipoambia maafisa hivi: “Ni lazima sisi tutii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”​—Matendo 5:29, NW.

11. Je! wanadamu wamejifanya miungu kwa kutengeneza kombora la nyukilia, na hali iko namna gani juu ya mamlaka yao ya kupinga kusemwa kwa ujumbe wa Ufalme?

11 Wanadamu hawakujifanya miungu kwa kulitengeneza kombora la nyukilia, na ni lazima wamjibu Mungu Aliye Juu Zaidi juu ya namna wanavyolitumia. (Angalia Zaburi 82:6, 7.) Kwa kulitokeza kombora la nyukilia liwe kama kizuio, serikali zinajaribu kuendeleza milele utawala wao wa dunia, badala ya kuendeleza mbele masilahi ya Ufalme wa Mungu ulio mikononi mwa Yesu Kristo. Wanaona uchungu na kuvuruga utangazaji wa Ufalme huo unaofanywa leo na wafuasi watiifu wa kweli wa Yesu Kristo. Kizazi cha nyukilia hiki hakikuyafanya yawe ya kikale wala yasiyofaa maneno haya ya kiunabii ya Kristo: “[Mambo] hayo ndiyo mwanzo wa utungu. Nanyi jihadharini nafsi zenu; maana watawapeleka ninyi mabarazani; na katika masinagogi mtapigwa nanyi mtachukuliwa mbele ya maliwali na wafalme kwa ajili yangu, kuwa ushuhuda kwao. Na sharti Injili ihubiriwe kwanza katika mataifa yote. Na watakapowachukua ninyi, na kuwasaliti, msitafakari kwanza mtakayosema, lakini lo lote mtakalopewa [kusema] saa ile, lisemeni; kwa maana si ninyi msemao, bali ni [roho takatifu].”​—Marko 13:8-11.

12. Ujapokuwako upinzani wenye jeuri, ni nini kilichopasa kuhubiriwa kwanza, na hiyo ingekuwa ishara yenye kutokeza sana juu ya jambo gani?

12 Utungu wa taabu za ulimwengu ulianza katika mwaka wa 1914. Halafu yakafuata mateso yaliyotabiriwa ya wafuasi waaminifu na watiifu wa Yesu Kristo, nayo yanaendelea mpaka leo hii. Ushuhuda wote unaonyesha kwamba sisi tunaishi katika “umalizio wa mfumo wa mambo,” ndiyo, tunakaribia upeo wake mkubwa katika kizazi hiki cha nyukilia. (Mathayo 24:3, NW; Marko 13:3, 4) Lakini kabla mwisho kamili haujaja, ni lazima “habari njema” ‘zihubiriwe kwanza.’ Kwa hiyo huku “kusema Neno la Mungu pasipo woga” ulimwenguni pote kwa ajili ya Ufalme ni moja la mambo yanayothibitisha kwa njia ya kutokeza kwamba tunaishi katika “umalizio wa mfumo wa mambo.”​—Mathayo 24:14.

Kula Neno la Mungu na Kwenda Kulisema Ulimwenguni Pote

13. Ni tukio gani kama lile linaloelezwa katika Ufunuo sura ya 10 lililopata mabaki wapakwa mafuta baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, na baada ya burudisho kupokewa, ni amri gani iliyotolewa?

13 Yohana, aliyekuwa mwanafunzi wa mwisho kuwa hai ambaye alichaguliwa na Yesu awe mtume, alimaliza maisha yake ya kidunia karibu na mwisho wa karne ya kwanza. Wakati wa huu “umalizio wa mfumo wa mambo” tangu mwaka wa 1914 kumekuwa na mabaki ya Wakristo walio wakf ambao wamebatizwa na kupakwa mafuta kwa roho ya Yehova. Mabaki hao walitangulia kufananishwa na Yohana, yule mwandikaji wa kitabu kilicho cha mwisho kati ya vitabu vinavyokubalika vya Biblia, yaani, Ufunuo. Katika mwaka wa kwanza kufuata vita, yaani mwaka wa 1919, mabaki hao walikuwa na tukio kama lile ambalo Yohana anaeleza juu yake mwenyewe katika Ufunuo sura ya 10. Tukio hilo lingefanyika karibu na wakati ambao “fumbo la Mungu,” au “siri takatifu” yake, ingekuwa karibu kumalizwa. (Ufunuo 10:7, Authorized Version, NW) Kama inavyoweza kusemwa, wakati walipokwisha kupata burudiko la kiroho kwa kula “kitabu cha kukunjwa kidogo” chenye ladha tamu ambacho walipewa wakichukue, wale waliokuwa katika jamii hii ya kisasa iliyotangulia kufananishwa na Yohana ni kama kwamba walikuwa wakiambiwa hivi: “Ni lazima wewe utoe unabii tena kwa habari ya makundi ya watu na mataifa na lugha na wafalme wengi.”​—Ufunuo 10:10, 11, NW.

14. Ni kupitia nani lile agizo alilopewa mtume Yohana akiwa huko Patmo linatimizwa?

14 Sisi hatuna maandishi yaliyoongozwa na Mungu ya kuonyesha kama mtume Yohana akiwa katika kisiwa cha Patmo aliweza kutimiza mgawo wake wa utumishi wenye mweneo mkubwa hivyo katika umri wake wa uzee. Lakini namna gani wale wapakwa mafuta wa leo ambao Yohana alitangulia kuwafananisha? Jamii hiyo ndiyo inayotimiza cheo chake cha kutoa unabii, nayo inahakikisha kwamba agizo alilopewa yeye linatimizwa kwa ukamili. Yale maneno yanayosema, “Ni lazima wewe utoe unabii tena,” yanaonyesha kwamba uendeshaji huru wa kazi yake ya kutoa ushuhuda ulikuwa ukivurugwa na hali yake ya kukaa uhamishoni katika Patmo. Ni wazi kwamba maneno aliyoambiwa alipokuwa huko yalikusudiwa hasa kwa wafananishwa wake wa kisasa katika siku hizi. Kwa kuwa ndivyo ilivyo, tunalazimika kuuliza hivi: Ni katika nchi na lugha ngapi Mashahidi wa Yehova wanasema Neno la Mungu pasipo woga wanapojitahidi kuhubiri “habari njema hizi za ufalme . . . katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda”?​—Mathayo 24:14, NW.

15. Kufikia sasa kazi ya kuhubiri inafanywa kwa kadiri gani?

15 Kitabu 1984 Yearbook of Jehovah’s Witnesses kinaeleza kwamba ni katika nchi 205, na vitabu vinavyohusu Biblia vinachapishwa katika lugha kama 190 hivi. Nchi hizo ni kutia ndani watu wa ngozi nyeusi ya mwili, nyeupe, ya manjano, nyekundu na ya kahawia. Pia ni kutia ndani makabila mbalimbali, mbari mbalimbali za watu na madhehebu pamoja na vilugha mbalimbali. Tangu Vita ya Ulimwengu ya Kwanza hesabu ya “wafalme” ambao wangali wanatawala imepungua sana, lakini kuna namna nyingine nyingi za watawala wa kisiasa ambao wanatawala sasa. Bila kujali wana jina gani la cheo au wana siasa za namna gani, ujumbe wa Mashahidi wa Yehova leo unawatia ndani wote na kuwahusu. Tendo la kuwapiga marufuku Mashahidi wa Yehova katika nchi nyingi sana ni uthibitisho wa uhakika huo.

16. Kwa hiyo ni utangazaji gani umesonga mbele bila kuzuilika, na imekuwa hivyo ijapokuwa viongozi wa ulimwengu wametoa sala za kidini kuomba nini?

16 Kwa hiyo ujapokuwako Ushirika wa Mataifa na Umoja wa Mataifa uliofuata, ambao ulianzishwa uwe njia ya kuendeleza mbele na kudumisha ulimwengu wenye kuungana, kazi ya kutangaza Ufalme wa Mungu ulio mikononi mwa Kristo pasipo woga kwa kuonyesha kwamba huo ndio tumaini la pekee kwa wanadamu imesonga mbele bila kuzuilika. Hizo “habari njema za ufalme” hazikuelekea kuwa “njema” kwa viongozi wa ulimwengu, kwa maana ziko tofauti sana na mambo ambayo wameyawaza kuwa mema, ndiyo, kuwa bora kupita yote, ya kusaidia wanadamu wenye kutaabika sana. Maoni yao ni kwamba wao wenyewe wanaweza kuongoza mambo ya kidunia bila kusumbuliwa na mtu mwingine. Ikiwa wao wanaona uhitaji wa kupata msaada unaopita ule wa kibinadamu, jambo la kweli ni kwamba sala zao za kidini zimefika tu kwa yule “mungu wa ulimwengu huu,” wala hazikupanda juu zaidi ya hapo. Mwanzishi wa kimungu wa “habari njema hizi za ufalme” hapendelei “ulimwengu huu,” ambao mungu wao ni Shetani Ibilisi.​—2 Wakorintho 4:4, AV.

17. (a) Kwa sababu gani Neno la Mungu lililoandikwa limekuwa haliwezi kufutiliwa mbali na wapinzani? (b) Ni kupitia nani Neno hilo limesemwa kwa sauti ya kusikika tangu mwaka wa 1919?

17 Biblia, ambayo ni kitabu cha unabii, inatangaza kwa ujasiri kwamba neno la Mungu litaendelea mpaka wakati usiojulikana na kwamba litadumu kale na kale. (1 Petro 1:23-25) Mpaka leo hii maneno hayo hayajathibitishwa kuwa ya uongo. Biblia, ambayo ni Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho yake, haijafutiliwa mbali, zijapofanywa jitihada zote za kibinadamu kuiangamiza kwa kutumia marufuku na mioto ya kidini. Kulingana na hilo, kuhubiriwa kwa hilo Neno la Mungu lililoandikwa kulihitaji mtu wa kulisema kwa sauti lisikike. Kusemwa kwa hilo Neno la Mungu kumesogezwa mbele kwa uthabiti na Mashahidi wa Yehova tangu mwaka ule ulioifuata vita wa 1919. Limesemwa na vinywa vinavyoendelea kuongezeka, yajapokuwako majaribio ya kufifisha wasemaji wasio na woga yanayofanywa na wapinzani wenye hasira kali.

18. Ni mpaka wakati gani Yehova ataendelea kufanya vipaji vya nyuso zao viwe vigumu?

18 Je! kunaweza kuwa na shaka lo lote la kama Mpaji wa Kimbingu wa Neno hilo ataendelea kuvifanya vipaji vya nyuso vya jamii yake ya kisasa ya Ezekieli na wenzi wao mashujaa viwe vigumu kama almasi ili waelekeane na wapinzani wenye vichwa vigumu mpaka uharibifu utakapogandamiza upinzani wao? Hata shaka moja hakuna! Yeye ameifanikisha njia ya mashahidi wake mpaka sasa. Yeye ataendelea kufanya njia yao iwe na ufanisi mpaka ‘kutoa unabii tena kwa habari ya makundi ya watu na mataifa na lugha na wafalme’ kuwe kumemalizwa pasipo woga. Anaweza kutazamiwa afanye jambo hilo, limletee yeye mwenyewe sifa na kuiondolea malawama enzi kuu yake ya ulimwengu wote.

Wewe Unaweza Kukumbuka?

◻ Ni nini kilichotangulia kufananishwa kwa siku zetu na yule ‘mtu aliyevalishwa kitani, aliyekuwa na chupa ya wino,’ na sasa yeye anafanya kazi gani?

◻ Kwa sababu gani kutokuogopa kunahitajiwa upande wa Mashahidi wa Yehova?

◻ Wakati mtume Yohana alipokula “kitabu cha kukunjwa kidogo,” alipaswa afanye nini baada ya hapo, na ni jambo gani lililo ulinganifu wa hilo katika nyakati za kisasa?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Katika kizazi hiki cha nyukilia mtu wa mfano mwenye kuvaa kitani anaendesha kazi fulani pasipo woga. Je! Wewe unahusika katika kazi hiyo?

[Picha katika ukurasa wa 12]

Kama vile Yohana alivyopokea kitabu cha kukunjwa cha mfano na amri ya ‘kutoa unabii tena,’ ndivyo Wakristo leo wanavyotangaza ujumbe wa Mungu pasipo woga

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki