Kueneza Neno la Mungu Kote Kote Katika Ulimwengu Wenye Woga
1. Ni hali gani ya woga wa ulimwengu isiyopata kuwa na ulinganifu ambayo nabii aliye mkubwa kupita wote katika historia ya kibinadamu alitabiri?
NABII aliye mkubwa kupita wote katika historia yote ya kibinadamu, Yesu Kristo, alitabiri kuhusu kipindi chenye kubadili ulimwengu kilichoingia wakati Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilipotokea mwaka wa 1914 akasema hali ya akilini ya mataifa yote ingekuwa hivi: “Watu wakizimia kwa woga, na kwa kutazamia maneno yanayokuja katika dunia; kwani nguvu za mbingu zitatetemeshwa.”—Luka 21:26, 27, ZSB.
2. Ni nani wasiojiacha waingiwe na woga, na kwa sababu gani?
2 Lakini, hata lionekane kuwa jambo la kushangaza, kuna watu ambao hawawi wenye woga wala hawazimii kwa kutokujua la kufanya. Hao ni Mashahidi wa Yehova ambao sasa wanapatikana katika nchi 205. Wao wanafanya vile Yesu alivyohimiza: “Wakati maneno haya yanapoanza kuja, tazameni juu, munyanyue vichwa vyenu kwa sababu ukombozi wenu umekaribia.”—Luka 21:28, ZSB.
3. Kwa sababu gani Ufalme wa Kimasihi haukuwekwa Yerusalemu katika Israeli, na kwa sababu gani Ushirika wa Mataifa na lile shiriki lililoufuata haukuzuia mbali kizazi cha nyukilia?
3 Leo uhakika unazidi kuthibitika ya kwamba “nyakati zilizowekwa za mataifa,” “majira ya Mataifa,” ziliisha katika nusu ya pili ya mwaka wa 1914 na kwamba wakati huo ule Ufalme wa Yehova Mungu ulioahidiwa kuwa mikononi mwa Yesu Kristo ulisimamishwa katika mbingu utawale katikati ya adui zake. (Luka 21:24, NW, Union Version) Kwa hiyo, mpaka leo hii huo Ufalme wa Kimasihi haujawekwa kwenye Yerusalemu wa kidunia. Pia, kulingana na vile ingetazamiwa kwa akili nzuri, Ushirika wa Mataifa ulishindwa kuwa “wonyesho wa kisiasa wa Ufalme wa Mungu duniani.” Umoja wa Mataifa, ulioufuata Ushirika wa Mataifa, umeshindwa kutimiza sala za Jumuiya ya Wakristo baada ya kuwapo kwa miaka zaidi ya 35; haukusukumia mbali kizazi cha nyukilia.
4. Ushirika wa Mataifa kwa kweli ulikuwa hila yenye madhara juu ya nini?
4 Tangu wakati ule ule ambao wazo lilitokezwa ili ushirika fulani wa mataifa ufanyizwe kuelekea mwishoni mwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, Mashahidi wa Yehova wametoa taarifa ya kwamba mashirika ya kibinadamu yanayowekwa kwa njia hiyo yawe badala ya kitu kile halisi kinachofaa, yaani serikali ya kifalme ya Yehova ikiwa mikononi mwa Kristo, yangeshindwa kutimiza kusudi layo. Mashirika hayo yameongoza mwendo wayo kulingana na unabii wa Isaya 8:12: “Ninyi msiseme, Umoja wa shauri, kwa wote hao ambao kundi hili la watu litasema, Umoja wa shauri; wala ninyi msihofu hofu yao, wala msiogope.” (AV) Mpango huo wa kibinadamu ni “hila yenye madhara,” ndiyo, hila yenye madhara juu ya masilahi zenye thamani kubwa za Ufalme wa Mungu ulio mikononi mwa Kristo. (NW, Revised Standard Version) Basi mpango huo ungewezaje kupata baraka na tegemezo la Mfalme wa wafalme, Yehova Mungu?
5. (a) Wakati Ezekieli alipokula “gombo la chuo,” lilikuwa na ladha gani bila kujali yale yaliyokuwamo? (b) Kuingizwa kwa Neno la Mungu katika vinywa vyetu ili tutumikie tukiwa mashahidi wake ni jambo la namna gani?
5 Ujumbe wa Ufalme ambao Mashahidi wa Yehova wangali wakiendelea kutangaza una mwito wa kushindana kweli kweli katika ulimwengu wenye maelekeo yanayotofautiana nao. Wao wamepatwa na tukio kama lile lililompata nabii Ezekieli, wakati alipokuwa mateka katika nchi ya Babuloni, miaka kadha kabla ya Yerusalemu kuharibiwa na Wababuloni katika mwaka wa 607 K.W.K. Sawa na vile ilivyokuwa baadaye kwa mtume aliyekuwa katika kisiwa cha Patmo, Ezekieli alipewa “gombo la chuo.” Nabii anatuambia hivi: “Nalo lilikuwa limeandikwa ndani na nje; ndani yake yalikuwa yameandikwa maombolezo, na vilio, na ole!” (Ezekieli 2:9, 10) Baada ya kutii maagizo ya Mungu ale hilo “gombo la chuo,” Ezekieli anaeleza hivi: “Nalo kinywani mwangu lilikuwa tamu, kama utamu wa asali.” (Ezekieli 3:1-3) Leo, kuingizwa kwa Neno la Mungu katika kinywa cha ye yote kati yetu ili kutumikia tukiwa wachukuaji wa ujumbe wake ni pendeleo tamu, bila kujali mambo yote yaliyo katika Neno hilo, hata maombolezo, kilio na ole (yowe, NW). (Linganisha Zaburi 19:7-10.) Mashahidi wa Yehova wanalithamini sana Neno la Mungu lililofunuliwa baada ya kulila kuanzia mwaka ule ulioifuata vita wa 1919 na kuendelea. Neno hilo liliwatia nguvu, sawa na vile asali ya halisi ilivyomtia Yonathani nguvu.—1 Samweli 14:26, 27.
6. Wakati siku ya kisasi cha Mungu inapoendelea kukaribia, kwa sababu gani ushujaa unahitajiwa, lakini Mashahidi wa Yehova wanaweza kuwa na uhakika wa jambo gani?
6 Wakati “siku ya kisasi cha Mungu wetu” inapoendelea kuja mbio-mbio, ushujaa unahitajiwa upande wa Mashahidi wa Yehova ili waonyeshe watu “maombolezo, na vilio, na ole” utakaoipata jamii yote ya kibinadamu hivi karibuni. (Isaya 61:1, 2) Watu wanaotafuta kitulizo wa ulimwengu huu unaoelekewa na tisho hawana nia ya kusikiliza habari ya namna hiyo inayotoka vinywani mwa Mashahidi wa Yehova. Lakini kwa kuwa Mungu ndiye anayewapeleka wakaeneze Neno lake, wao wanaweza kuwa na uhakika wa kwamba atawasaidia moja kwa moja mpaka siku ile ya kisasi.
7. Yehova angewezeshaje Ezekieli kutimiza mgawo wake?
7 Si jambo la kupendeza kuona watu wakikataa kusikiliza, lakini acheni tutii maneno ambayo Mungu alimwambia Ezekieli: “Nyumba ya Israeli hawatakusikiliza wewe; kwa kuwa hawanisikilizi mimi; maana nyumba yote ya Israeli wana vipaji vigumu, na mioyo yenye ukaidi. Tazama, nimeufanya uso wako kuwa mgumu juu ya nyuso zao, na kipaji cha uso chako kuwa kigumu juu ya vipaji vya nyuso vyao. Kama almasi ilivyo ngumu kuliko gumegume, ndivyo nilivyokifanya kipaji chako; usiwaogope, wala usifadhaike kwa sababu ya nyuso zao, wajapokuwa ni nyumba ya kuasi. . . . Haya! enenda uwafikilie watu hao waliohamishwa, kwa wana wa watu wako, ukaseme nao, na kuwaambia, Bwana [Yehova] asema hivi; kwamba watasikia, au kwamba hawataki kusikia.”—Ezekieli 3:7-11.
8. Jamii ya Ezekieli ilielekeanaje na hali ile ya kuogopesha baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, na ingalikuwaje kama viongozi wa kidini wangalisikiliza?
8 Hali ya kuogopesha kama hiyo ilikabiliwa na mabaki ya Wakristo wale waliokuwa wamezaliwa kwa roho ya Mungu wawe wana wake wa kiroho na wakawa wamepakwa mafuta kwa roho yake ili wawe mashahidi waliowekwa naye. Wao ndio wanaokuwa jamii ya Ezekieli ya karne ya 20. Kwa hiyo, kama Ezekieli, wao hawakurudi nyuma wakijikunja kwa woga kwa sababu ya nyuso za kuogopesha za viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo waliosomea kazi yao na wenye mavazi ya kuvutia, ambao huenda wakadai kwamba ni Waisraeli wa kiroho. Kama viongozi hao wa kidini wangalifanya nyuso zao ziwe nyororo na kuusikia ujumbe wa Ufalme kwa kutii unaotangazwa na mabaki wapakwa mafuta tangu mwaka wa 1919, Jumuiya ya Wakristo isingalijitupa ndani ya vita ya ulimwengu ya pili iliyokuwa kubwa zaidi na yenye madhara mengi zaidi ulimwenguni pote kuliko ile ya kwanza.
9. Mabaki na wenzi wao walio wakf wamewezeshwaje kutimiza mgawo wao?
9 Leo, viongozi wa kidini hawajabadili hali ya uso wao kuelekea watangazaji wa Ufalme hata ijapokuwa kwamba tisho la kuwaza kutokea kwa vita ya nyukilia linaongezeka na kuna tengenezo la Umoja wa Mataifa. Kwa hiyo mabaki wapakwa mafuta wakiwa ni mabalozi wa Ufalme na washirika wao walio wakf na waliobatizwa kutoka mataifa yote wamelazimika kufanya nyuso zao ziwe ngumu kama almasi kwa sababu ya upinzani wa kidini uliofanywa imara. Wao wanazidi tu kulisema Neno la Mungu pasipo woga.
10. Mashahidi wa Yehova wangalipaswa kusikilizwa na viongozi wa kidini na watu wa mitaa yao kwa sababu gani, na bado kuna uhakika gani ambao wanadini hao watakuja kuukubali?
10 Viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo na wafuasi wa mitaa yao ndio wangalipaswa hasa kuwa wameelewa ujumbe na mashauri ya Mashahidi wa Yehova. Mashahidi wanatoa maneno wanayosema katika Biblia ile ile ambayo wanadini wa ule unaoitwa ulimwengu wa Kikristo ati unadai kuikubali na ambayo sosaiti zao za Biblia zinaeneza kote kote katika lugha nyingi. Mambo yamekuwa sawa na vile Yehova Mungu alivyomwambia Ezekieli, kulingana na Biblia ya New World Translation: “Na wana walio wakavu wa uso na wagumu wa moyo—mimi ninakutuma wewe kwao, na lazima wewe ukawaambie wao ‘Hivi ndivyo Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu amesema.’ Na kwa habari ya wao, kama watasikia au wataepuka—kwa maana wao ni nyumba yenye uasi—wao kwa uhakika watajua pia kwamba nabii mwenyewe alipata kuwa katikati yao.”—Ezekieli 2:4, 5, NW.
11. Ni sifa gani ambazo Jumuiya ya Wakristo imeonyesha kuelekea mabaki walioagizwa na Yehova, naye amewawezeshaje mabaki kutimiza agizo hilo lenye mwito wa ushindani?
11 Yule mwenye kujiita Israeli wa kiroho, Jumuiya ya Wakristo, ameonyesha ukavu wa uso na ugumu wa moyo kuwaelekea mabaki wapakwa mafuta ambao Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu amewaagiza watolee watu ujumbe wake wa mwisho wakati wa huu “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 24:3,14, NW) Mungu Mwenye Nguvu Zote alijua kwamba angeweza kutia ndani ya mfananishwa wa kisasa wa Ezekieli hali ya kutokuogopa ambayo ingewapa moyo mabaki hao wapakwa mafuta wakubali na kutimiza agizo hilo lenye mwito wa kushindana.
12. Kwa njia hiyo ni shtaka gani la uongo ambalo Yehova anakanusha, na ni tukio gani linalohusiana na hilo litakalomwacha akiwa na kumbukumbu safi?
12 Yule Mungu asiyeweza kuletewa sifa mbaya amekusudia kukanusha uwezekano wote wa kulaumiwa kuwa asiyejali, mwenye kushindwa kuwatolea watu walio hatarini onyo linalowapasa. Hali zinazidi kutusonga mpaka zitakapofikia hatua ya kutufunua tuonekane wazi kabisa namna tulivyo. Ndipo wale wasiotii watakapolazimika kuukubali uhakika wa kwamba nabii kutoka kwa Yehova amekuwa kati yao. Huo ni wakati Babuloni Mkuu, ile milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, itakaposhuka katika uharibifu wa milele utakaoletwa na serikali za kisiasa ambazo milki hiyo ilikuwa ikifanya umalaya wa kiroho nazo bila kuona aibu. Jambo hilo litamwacha Mungu wa ibada safi akiwa na kumbukumbu safi.
13. Umekuwa ni mfano mwema kwa “kondoo wengine” wakati Yehova alipowatimizia mabaki wapakwa mafuta ahadi gani, na kwa njia gani?
13 Hali ya kutokuogopa kusema ambayo imeonyeshwa na mabaki wapakwa mafuta mpaka sasa imekuwako kwa sababu Yehova ametimiza ahadi yake: “Tazama, nimeufanya uso wako kuwa mgumu juu ya nyuso zao, na kipaji cha uso chako kuwa kigumu juu ya vipaji vya nyuso vyao. Kama almasi ilivyo ngumu kuliko gumegume, ndivyo nilivyokifanya kipaji chako; usiwaogope, wala usifadhaike kwa sababu ya nyuso zao, wajapokuwa ni nyumba ya kuasi.” (Ezekieli 3:8, 9) Wakiwa wameimarishwa hivyo, mabaki wamekuwa mfano wenye kutia moyo kundi linaloongezeka la “kondoo wengine” ambao Yesu Kristo, yule Mchungaji Mwema, aliahidi kuwakusanya upande wa mabaki wapakwa mafuta wake. (Yohana 10:16; Ufunuo 7:9-17) Wakiwa ni Mashahidi wa Yehova, “kondoo wengine” hao wamekuwa wajasiri kama simba.
14, 15. (a) Ni kwa sababu ya tofauti gani mashahidi wengi wa Yehova walio ndani na nje ya nchi za Jumuiya ya Wakristo wanataabika kwa kufungwa magerezani? (b) Matokeo ya vifungo hivyo juu ya Mashahidi walio huru yanakuwaje tofauti na vile ingaliweza kutazamiwa?
14 Mashahidi wa Yehova hawaigi Babuloni Mkuu. Kwa hiyo pande zote, ndani na nje ya nchi za Jumuiya ya Wakristo, wao wana ndugu zao katika imani ya Kikristo ambao wanataabika magerezani kwa sababu ya kushikilia kabisa hali yao ya kutokuwamo. Jambo hilo halikuingiza woga ndani ya Mashahidi wale ambao wangali huru na wasio katika magereza, na ivyo hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa ndugu za Kikristo za mtume Paulo katika Roma. Katika kesi moja ya mahakamani Paulo alikuwa ameomba rufani kwa Kaisari wa Roma ili afanyiwe haki, na hakimu alikuwa ametoa amri akasema: “Umetaka rufani kwa Kaisari! basi, utakwenda kwa Kaisari.” (Matendo 25:10-12) Kwa hiyo Paulo alisafirishwa mpaka Roma akiwa amefungwa minyororo kisha akafungwa huko, akingojea hukumu. Ni chini ya hali hizo aliposema hivi alipokuwa akiandikia Wakristo wenzake wapendwa sana wa mji wa Filipi, Ugiriki:
15 “Na wengi wa ndugu zetu katika Bwana wakipata matumaini kwa ajili ya vifungo vyangu, wamezidi sana kusubutu kusema Neno la Mungu pasipo woga.”—Wafilipi 1:14, ZSB.
16. Ijapokuwa ndugu zao za Kikristo walifungwa gerezani, ni sifa gani iliyoonyeshwa na mashahidi huru wa Yehova mara tu baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, na kwa sababu gani sifa iyo hiyo inahitajiwa leo?
16 Kwa njia inayofanana na hiyo kidogo, wakati Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilipokwisha mwaka wa 1918, maafisa na washiriki wa wafanya kazi wa makao makuu ya Sosaiti walijikuta gerezani kwa kushtakiwa mambo ya uongo. Kwa kuwa sasa amani ilikuwa imeingia, hatua za ushujaa zilichukuliwa haraka na ndugu waliokuwa nje ili kutafuta njia ya kufanya wafunguliwe. Katika mwaka wa 1919 walifunguliwa gerezani na kesi yao ikatupwa na mahakama. Hivyo walitangazwa kutokuwa na hatia ya mashtaka yote ya uongo. Kazi ya kuzihubiri habari njema za Ufalme wa Mungu uliosimamishwa ukiwa mikononi mwa Kristo ilianzwa kwa ushujaa mkubwa kuliko wa wakati mwingine wo wote, na hivyo Babuloni Mkuu na hawara zake wakaonyeshwa wazi kwa ujasiri kwamba hawakuweza kitu. Leo, kwa kuwa mashahidi wa Yehova walio gerezani ni wengi sana kuliko wale wa huko nyuma wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, ni juu ya ndugu zao walio huru huko nje ‘kulisema neno la Mungu pasipo woga.’
Wale Walioaibisha Jumuiya ya Wakristo kwa Kusikiliza
17. (a) Kwa habari ya wale ambao wangekuwa na mwelekeo mkubwa zaidi wa kusikiliza, Yehova alimwambia Ezekieli nini? (b) Ni baada ya kukaza jitihada juu ya nani fikira ziligeuzwa kuwaelekea wale wenye nia kubwa zaidi ya kusikiliza, na kwa njia gani?
17 Ulizo la kupendeza lilikuwa, Ni nani wangekuwa na mwelekeo wa kuwa wasikilizaji? Juu ya jambo hilo Yehova alimwambia Ezekieli hivi: “Maana wewe hukutumwa kwa watu wa maneno mageni, ama wa lugha ngumu . . . ambao huwezi kufahamu maneno yao. Bila shaka, kama ningekutuma kwa watu hao, wangekusikiliza.” (Ezekieli 3:5, 6) Nabii huyo alikuwa na wajibu wa kuendelea kusema neno la Mungu kwa watu wa taifa lake mwenyewe, kwa ile sehemu iliyojigawa ya makabila kumi ya Israeli wakiwa katika hali yao ya kutekwa katika nchi ya Babuloni. Vivyo hivyo, kufikia katikati ya kumi la nne la karne yetu ya 20, mabaki wapakwa mafuta wa Israeli wa kiroho walielekeza sana jitihada zao juu ya kukusanya washiriki wa mwisho wa Israeli wa kiroho waingie ndani ya “zizi” la “kundi dogo,” ambao Baba wa kimbingu amekubali kuwapa Ufalme, watawale pamoja na Mwanaye ili kubariki wanadamu waliokombolewa. (Luka 12:32) Ndipo wakati huo unaofaa maneno ya Mwanaye yaliyo kwenye Yohana 10:16 na uhusiano wayo na Ufunuo 7:9-17 yalipofikiriwa kwa mara nyingine.
18, 19. Kwa sababu gani hali ya kutokuwa na woga ilihitajiwa katika mwaka wa 1935 ili kuonyesha kwamba “umati mkubwa” ulihusiana na wale “kondoo” ambao wangefanywa “kundi moja” pamoja na mabaki wapakwa mafuta?
18 Kwenye Yohana 10:16, Yesu, Mwana wa Mungu, alikuwa amesema hivi: “Na kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja.”
19 Ili wale ambao wangepangwa wawe jamii ya “kondoo wengine” wasikilize sauti ya yule“mchungaji mmoja” katika wakati huo, walihitaji hali ya kutokuogopa. Mashahidi wa Yehova walikuwa wakiendelea kupatwa na mateso makali kama moto mikononi mwa vikosi vyenye kutukuza taifa vikiwa chini ya Adolf Hitler, kwa kuungwa mkono na viongozi wa kidini wa Kanisa la Katoliki ya Roma ambalo ndilo lililokuwa kanisa la Hitler wa Nazi. Kwa hiyo kwa kukabiliwa na hali za ulimwengu za namna hiyo, imani kuu, usadikisho na hali ya kutokuogopa ilihitajiwa upande wa msimamizi wa Sosaiti ili aweze kuonyesha wazi katika mwaka wa 1935 kwamba ule “umati mkubwa” wa Ufunuo 7:9-17 (AV) ungekuwa wa wale “kondoo wengine” waliotabiriwa, na kwamba hao wangefanywa wawe “kundi moja” pamoja na mabaki wapakwa mafuta waliokuwa wakiteswa ambao walikuwa katika “zizi hili.” Hata hivyo, ilikuwa lazima kwake ‘aseme neno la Mungu pasipo woga.’ Alifanya hivyo bara-bara.
20. Itikio la wale wenye kuwa “kondoo wengine” limekuwa nini, mpaka “kundi” likaongezeka kufikia kadiri gani leo?
20 Tangu mwanzoni kabisa, mamia kwa mamia ya watu waliitikia, wakajiweka wakf wao wenyewe kwa Yehova Mungu bila masharti, kupitia “mchungaji mmoja” wake na kuonyesha wakf huo kwa kuzamishwa katika maji mbele ya watu wengi. Na kufikia sasa, hao kondoo wengine” wameongezeka wakawa “kundi” la washiriki milioni mbili na nusu au zaidi katika nchi 205, ijapokuwa Vita ya Ulimwengu ya Pili iliwakatiza. Nyingi za nchi hizo ziko nje ya eneo linaloitwa Jumuiya ya Wakristo, kama vile Japani, ambako kunakuwa na wastani ya kila mwaka ya watangazaji wa ujumbe wa Ufalme walio wakf zaidi ya 70,000. Korea ina zaidi ya 30,000 na Nigeria zaidi ya 100,000.
21. Jumuiya ya Wakristo inaaibishwa na itikio la nani kwa mwito wa yule “mchungaji mmoja”?
21 Ni jambo la wazi kwamba Jumuiya ya Wakristo yenye uso mgumu na moyo mgumu inaendelea kuaibishwa na itikio hilo kwa mwito wa yule “mchungaji mmoja” katika nchi hizo ambako huenda lugha inayosemwa ikawa ni ngumu na kidogo isiyofahamika vizuri kwa wale walio katika Jumuiya ya Wakristo, hasa lugha ya kidini ya mifumo yao ya dini. Wale wanaokuwa “kondoo wengine” wa Kristo wanaonyesha ushujaa unaostahili sifa kwa kuwa wanapuuza fikira ambazo ulimwengu unaweza kuwa nazo juu yao na kumwendea kwa wingi yule “mchungaji mmoja” aliye Kiongozi na Mwokozi wao waliyepewa na Mungu. Kama Mchungaji wao, wao wanasema Neno la Mungu pasipo woga.
22. Kwa kuelekeana na ulimwengu, Mashahidi wa Yehova wanapaswa kusema Neno la Mungu wakiwa na nia gani ya akilini?
22 Maoni ya kuwa na woga ya ulimwengu yanazidi kuwa mabaya. Yakiwa chini ya mavutano ya kishetani, mataifa yanapigishwa miguu yakielekezwa kwenye uwanja wa pigano wa Har–Magedoni wakafanye pigano la mwisho la kukata maneno. Mashahidi wa Yehova watasimama kandokando ya uwanja wa pigano kwa usalama na kutazama Mungu wao akipata ushindi. Kwa kuliokoka hilo Pigano la mapigano yote, watajiunga na makundi ya uwinguni yenye shangwe nyingi katika kuvumisha sifa za yule Mungu asiyeshindika, Yehova, na Amiri Jeshi Mkuu wake, Yesu Kristo. (Ufunuo 16:13-16) Huu si wakati wa kukimbia kwa kurudi nyuma! Basi songeni mbele enyi kundi lililounganishwa kwa umoja la Mashahidi wa Yehova, katika ‘kusema neno la Mungu pasipo woga’ mpaka dunia itakapojawa na maarifa ya kuujua utukufu wa Yehova kama vile maji yanavyoifunika bahari.—Isaya 11:9; Ezekieli 47:1-5.—Kutoka w12/15/83.
Umeona?
◻ Ezekieli alipatwa na tukio gani katika Babuloni, nalo lina ulinganifu wa kisasa kwa njia gani?
◻ Kwa sababu ya nia zinazoonyeshwa na viongozi wa kidini, kwa sababu gani watu wa Mungu wanahitaji kutokuwa na woga katika kueneza Neno lake?
◻ Watu wa Yehova walio wakf wametangazaje ujumbe wao kwa ‘watu ambao hawakuweza kuifahamu vizuri lugha yao’?
◻ Wewe unahitaji kuonyesha nia gani sasa na katika wakati ujao?
[Picha katika ukurasa wa 17]
Mashahidi wa Yehova hawana woga wajapokataliwa na viongozi wa kidini na kuonyeshwa ugumu nao