“Umoja wa Roho” Katika Kundi Linaloendelea Kukua Upesi Sana
1. (a) Kwenye Waefeso 4:1-6, Paulo aliandika shauri gani linalofaa juu ya umoja? (b) Kwa sababu gani shauri hilo linafaa hata siku zetu?
WAKATI mtume Paulo alipowaandikia Wakristo wa kundi la Efeso alikazia umoja, akawahimiza wawe wanyenyekevu, wachukuliane kwa upendo na kufanya bidii ya ‘kuuhifadhi umoja wa roho katika kifungo cha amani.’ (Waefeso 4:1-6) Paulo alikuwa ametumia miaka zaidi ya miwili katika Efeso na alijua hali za malezi mbalimbali ya ndugu wa huko. Alijua pia kwamba mavutano yenye nguvu za kuleta mwungano ambayo Yehova alikuwa ameanzisha kati ya watu wake yangeweza kuzishinda hali hizo za kutofautiana, naye Paulo aliwahimiza wathamini mavutano hayo na kuyakubali kwa ushirikiano. Ni jambo la maana sana kufanya ivyo hivyo katika siku zetu. Kwa sababu gani? Kwa sababu watu mmoja mmoja wanaotoka kati ya “kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha” wanaendelea kukusanywa kwa wingi sana waingizwe ndani ya tengenezo la Yehova.—Ufunuo 7:9, 10.
2. Yehova analindaje umoja wa tengenezo lake linaloonekana?
2 Kupatana na kusudi lake, Yehova ameunganisha vizuri watumishi wake “kama kundi katika zizi.” (Mika 2:12, NW) Yeye anawatolea mwelekezo wanaohitaji ili kulinda umoja huo. Kwa njia gani? Yeye binafsi aliweka Mwana wake mwenyewe, Yesu Kristo, awe kichwa cha kundi la Kikristo. Katika Biblia, Yehova aliagiza maelezo yanayohusu kusudi lake yaandikwe, na kupitia tengenezo lake linaloonekana anaelekeza jitihada za watumishi wake katika vipitio vinavyopatana na kusudi hilo. Kuangalia ushuhuda unaoonyesha mwelekezo huo wa kimungu katika nyakati za kisasa, tangu mwaka wa 1919, ni jambo lenye kutia imani nguvu.
Wakatayarishwa Kutoa Ushuhuda wa Duniani Pote
3. Ni utendaji gani ambao Biblia ilitabiri ungefanywa katika umalizio wa mfumo wa mambo kwa ajili ya warithi wa Ufalme?
3 Katika kuzungumza umalizio wa mfumo wa mambo, Maandiko yalitabiri kukusanywa upya kwa “wateule” waliotawanyika ili kuwaingiza katika umoja wa tengenezo, na pia yakatabiri kuvunwa kwa washiriki wa mwisho wa jamii ya Ufalme. (Mathayo 24:31; 13:37-43, 47-50) Jambo hilo limetimizwaje?
4. (a) Ni kitu gani chenye kuonekana kilichotumiwa na Kristo na malaika kutimiza tendo hilo la kuwakusanya tena na kuwavuna mabaki? (b) Kwa hiyo hapa Yehova alikuwa akitumia njia gani mbili kuunganisha vizuri watumishi wake?
4 Maandiko yanasema kwamba Kristo angetuma malaika zake wakalitimize. Hakuna mtu aliye duniani anayeweza kuwaona viumbe wa kiroho hao wakifanya kazi, lakini matokeo ya utendaji wao katika tengenezo la Yehova linaloonekana yako wazi kabisa. Baada ya mateso ya ukatili ambayo watumishi wa Yehova walipatwa nayo wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, nguvu mpya zilitiwa ndani yao kupitia makala za Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) zenye kusema “Wabarikiwa Ni Wasioogopa,” zilizochapishwa katika mwaka wa 1919. Yehova alikuwa na kazi nyingi zaidi ya kuwapa. Kwenye kusanyiko lao la mwaka huo katika Cedar Point, Ohio, katika hotuba yenye kusema “Kuutangaza Ufalme,” taarifa ilitolewa juu ya kichapo kipya, The Golden Age (Kizazi cha Ufanisi, ambacho sasa kinaitwa Amkeni!). Kilikuwa cha kuenezwa kote kote ili kuonyesha watu “Kizazi cha Ufanisi cha utawala wa Masihi wenye utukufu.” “Wateule” wote walitiwa moyo washiriki katika utendaji huo. Mwaka wa 1922, kwenye kusanyiko jingine katika Cedar Point, kitia-moyo kilitolewa kwa uthabiti mwingi kikisema “Mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni, Mfalme na ufalme wake.” Mwaka wa 1925; jambo jingine lililoongezea kazi kichocheo cha kusonga mbele ni kufahamu umaana wa utendaji wa baada ya vita wa watumishi wa Yehova kwa msaada wa Ufunuo sura ya 12. Halafu mwaka wa 1931, kupitia azimio lililokubaliwa kwenye kusanyiko katika Columbus, Ohio, na kwenye makusanyiko mengine 50 ya mfano huo yaliyofanywa ulimwenguni pote baadaye, jina Mashahidi wa Yehova lilipokewa kwa furaha, likawatenganisha Wakristo hao na madhehebu zote za Jumuiya ya Wakristo na kukazia kazi yao waliyopewa na Mungu. (Isaya 43:10-12) Hivyo Yehova alikuwa akiwaunganisha vizuri watumishi wake (1) kwa kuwapa ufahamu wa hatua kwa hatua wa Maandiko na (2) kwa kuwachochea wafanye utendaji wa juhudi wakiwa mashahidi wake.
5. Kufikia mwaka wa 1935 ni nini kilichotimizwa hivyo kupitia hatua yenye umoja chini ya mwongozo wa Yehova?
5 Ingawa walikuwa wachache, tendo lao lililounganishwa vizuri chini ya mwongozo wa Yehova lilifanya ujumbe wa Ufalme ukafikia miisho ya dunia. Kuanzia mwaka wa 1921 mpaka wa 1935 waliangusha vitabu na vijitabu 205,217,917 katika lugha nyingi. Mamia ya mamilioni ya trakti yalienezwa pia na radio ikatumiwa kufikia maeneo ya mbali. Basi, maelfu zaidi ya watu walijiweka wakf kwa Yehova, wakabatizwa na kupakwa mafuta kwa roho takatifu wakati mkusanyo wa jamii ya Ufalme ulipokuwa ukikaribia kukoma. Lakini, huduma ya hadharani yao haikumalizika. Yehova alikuwa amekuwa akiwatayarisha kwa ajili ya mambo yaliyokuwako mbele.
Wakatiwa Nguvu Kuelekeana na Upinzani
6. Yehova alikuwa akitayarisha watumishi wake waliopakwa mafuta kwa sababu ya jambo gani jingine?
6 Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, wapakwa mafuta walikuwa wametawanywa na adui. Bado jitihada zaidi zilizo mbovu za kutaka kuimaliza kabisa kazi yao zilikuwa mbele yao. Lakini Yehova aliwaimarisha wasipate tena kuwa kundi lililotawanywa. Jambo hilo lilifanywaje?
7. Wakati wa kujenga upya hekalu, Yehova aliwezeshaje watu wake wasonge mbele kwa umoja kwa kuelekeana na upinzani?
7 Wakati upinzani ulipozuia ujenzi wa hekali la Yehova baada ya wahamishwa kurudi kutoka Babuloni, Yehova aliwatia nguvu watu wake kwa kuinua manabii, wanenaji wenye kuonekana, akawafanya watoe kwa wakati wake ujumbe mbalimbali uliotoka kwake. Zaidi ya hilo, roho ya Yehova mwenyewe ilishinda mapingamizi yaliyokuwa kama milima, akawawezesha watumishi wake watende kazi wakiwa tengenezo lenye umoja.—Hagai 1:1-8; Zekaria 4:1-14.
8. Yehova aliwatia nguvu namna gani akina ndugu katika karne ya kwanza?
8 Wakati waabudu wa kweli waliposumbuliwa sana na adui katika karne ya kwanza, Yehova aliwafanya mitume wakaandika barua zenye kutoa mwelekezo na kitia-moyo. Katika barua hizo mchochezi mkubwa zaidi wa upinzani alionyeshwa waziwazi kuwa ni Shetani Ibilisi, ambaye shabaha yake ni kunyamazisha mahubiri ya habari njema, akifanya hivyo kwa kutumia mateso yenye jeuri au kwa kuvuruga umoja wa makundi kupitia uvutano wa ndugu za uongo. Hivyo wote walisaidiwa kuona wazi masuala yaliyohusika. (Waefeso 6:10-13; 2 Wakorintho 11:12-15; 1 Petro 5:5-8) Walitiwa moyo kwa upendo ‘wasimame imara katika roho moja, kwa moyo mmoja wakiishindania imani ya Injili; bila kuogopa adui zao.’—-Wafilipi 1:27, 28.
9. (a) Katika nyakati za kisasa, Yehova ametoaje msaada huo? (b) Toa mifano ya kuonyesha jambo hilo.
9 Katika nyakati za kisasa, Yehova ameendelea kutolea watumishi wake msaada unaohitajiwa, akifanya hivyo kupitia “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” wale mabaki waliopo duniani leo, ambao Yesu ndiye kichwa kilichowekwa juu yao, na msaada huo unakuja katika wakati unaofaa kabisa. (Mathayo 24:45-47) Hivyo katika mwaka wa 1925 jamii ya “mtumwa” ilitumia Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) kusaidia wasomaji wa gazeti hilo wafahamu kwamba Ufalme wa Mungu ulikuwa umekuwa ukitenda kazi katika mbingu tangu mwaka wa 1914 na kwamba, kwa uhakika, kuna matengenezo mawili tu—-la Yehova na la Shetani. Katika mwaka wa 1929 wajibu wa Kikristo wa kutii sheria ya Mungu sikuzote kuwa yenye nguvu kuliko ya mwanadamu ulikaziwa sana. Marekebisho ya tengenezo yalifanywa hatua kwa hatua mpaka katika mwaka wa 1938 kuwekwa kote kwa waangalizi katika makundi kukafanywa kwa njia ya kitheokrasi, badala ya kutumia njia ya kura za kundi. Yote hayo yaliwaunganisha vizuri na kuwatia nguvu watumishi wa Yehova, tena kwa wakati wake kabisa!
10. (a) Ni kwa njia gani msaada huo ulitolewa kwa wakati wake kabisa? (b) Mateso yalipoendelea kuongezeka, Yehova aliwapa msaada gani zaidi?
10 Wakati wa miaka ya 1930 na moja kwa moja kwenye Vita ya Ulimwengu ya Pili na baada ya hapo, Mashahidi wa Yehova walianza kupata mateso makali sana katika nchi nyingi. Maelfu walipelekwa mahakamani. Katika nchi nyingi kazi yao ikawa chini ya marufuku ya kiserikali. Wengi walitiwa uzuizini muda wa miaka mingi katika kambi za mateso za utawala wa ukatili. Mateso hayo yalipoanza kuongezeka, Yehova alizidi kuimarisha watumishi wake. Katika mafunzo ya Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) mwaka wa 1931, walizungumza juu ya namna Wayahudi katika siku za Malkia Esta walivyojikinga na adui zao licha ya kutetea uhai wao, halafu wakachunguza waone jambo hilo linatumikaje leo katika vita ya kiroho. Makala zilizohusu “Nyungu ya Kuchemshiwa” zilitumia katika mwaka wa 1934 masimulizi ya wale Waebrania watatu waliokuwa katika tanuru ya moto ili kuwafanya Mashahidi wa Yehova wapige moyo konde wasimame imara wakimtumaini Yehova kwa uhakika kamili. (Danieli 3:17, 18, 28) Bado Yehova alikuwa na kazi kubwa ya kufanya, na upinzani wa kishetani usingeruhusiwa uiondoshe kando kazi hiyo.
Kukusanya “Mkutano Mkubwa” kwa Ajili ya Wokovu
11. (a) Yehova alikuwa amekuwa akitayarisha watumishi wake kwa ajili ya kazi gani yenye mweneo mkubwa hata zaidi? (b) Taja nyingine za hatua zilizo katika shughuli ya matayarisho yanayoelekezwa na Mungu.
11 Kukusanywa kwa “kundi dogo” la warithi wa Ufalme kulipokaribia kumalizika, Yehova alielekeza fikira kwenye kazi iliyo kubwa hata zaidi, kuwapa elimu “mkutano mkubwa” ambao wangeiokoka ‘dhiki kubwa’ waishi duniani katika Paradiso itakayorudishwa. Hivyo katika mwaka wa 1918 msimamizi wa Sosaiti alitoa hotuba katika Los Angeles, California, juu ya habari ambayo baadaye ingerudiwa na mamia ya wasemaji wengine. Kichwa chake kilisema “Ulimwengu Umekwisha, Mamilioni Wanaoishi Sasa Huenda Wasife Kamwe.” Halafu katika mwaka wa 1923, Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) ukaonyesha kwamba “kondoo wengine” wa Yohana 10:16 ndio “kondoo” wale wale wa mfano wa Yesu wa kondoo na mbuzi, na kwamba tayari walikuwa wameanza kutokea. Katika mwaka wa 1931 hao walionyeshwa kuwa walitangulia kufananishwa kwenye Ezekieli 9:1-11 kuwa watu waliotiwa alama katika vipaji vya nyuso ili wapate wokovu. Katika mwaka wa 1932 ikafunuliwa kwamba jamii iyo hiyo ilitangulia kufananishwa na Yonadabu, ambaye alitambua kwamba ni jambo la maana sana Yehova ndiye apewe ibada ya pekee. Shughuli hiyo ya kuwatayarisha iliyoongozwa na Mungu ilifikishwa kwenye kilele katika mwaka wa 1935 kwenye kusanyiko la Washington, D.C., wakati “umati mkubwa,” au “mkutano mkubwa,” wa Ufunuo 7:9-17 ulipoonyeshwa pia kuwa ni jamii ile ya kidunia, na mamia ya watu kati ya wasikilizaji wakajitambua wenyewe kuwa wa kikundi hicho. Kukusanywa kwa kikundi hicho sasa kulisonga mbele kwa haraka sana chini ya mwelekezo wa roho ya Yehova.
12. (a) Kwa sababu gani kukusanya watu walio na tumaini la kidunia waingie katika ushirika pamoja na wale wenye tumaini la kimbingu hakukuleta machafuko ya kukosa umoja? (b) Kwa baraka ya Yehova, mpaka sasa jitihada zao za umoja zimekuwa na matokeo gani?
12 Je! mkusanyo huu wa jamii ya kidunia ili kuwaingiza katika ushirika pamoja na wale walio na tumaini la kimbingu umeleta machafuko ya kukosa amani katika tengenezo? Hata kidogo. Kama Yesu alivyotabiri, wao wamekuwa “kundi moja” yeye akiwa ndiye “mchungaji mmoja” wao. (Yohana 10:16) Wao wanatambua kwamba tumaini lo lote walilo nalo kati ya hayo mawili ni ushuhuda wa fadhili zisizostahilika za Yehova, kwamba wote wana pendeleo na daraka la kuwa mashahidi kwa ajili ya jina la Yehova na Ufalme wake, na kwamba kiwango kile kile kimoja cha uaminifu wa Kikristo kinatumika kwa wote kati yao. Wao ni watu walio na umoja kweli kweli. Wamejiunga pamoja wakafanya jitihada ya kutoa ushuhuda wa Ufalme katika dunia yote inayokaliwa na watu, na kwa sababu hiyo kumekuwa na mkusanyo mkubwa. Baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ni maelfu wachache tu walioshiriki katika kutangaza hadharani Ufalme wa Yehova. Mwaka wa 1941 ulipofika ndipo watu zaidi ya 100,000 waliposhiriki katika kazi hii ya ulimwenguni pote. Leo wale walio na umoja wakiwa watangazaji wa hadharani wa ujumbe wa Ufalme wanajumlika kuwa 2,652-323. Imekuwa kama vile Yehova alivyotabiri kupitia nabii Isaya: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa hodari; mimi, [Yehova], nitayahimiza hayo wakati wake.”—Isaya 60:22.
Jitihada za Umoja za Kufanyiza Vifaa vya Kazi Vinavyohitajiwa
13. Ukuzi huo umekuwa na matokeo gani juu ya vifaa vya uchapaji vya Sosaiti, na uhitaji uliopo umetimizwaje?
13 Ongezeko kubwa hilo katika hesabu ya Mashahidi wa Yehova limetokeza uhitaji wa kuwa na vifaa vilivyopanuliwa. Katika miaka ya 1920 sehemu kubwa ya uchapaji wa vitabu vya Biblia vinavyotumiwa na Mashahidi ilifanywa katika Brooklyn, New York. Sasa uchapaji huo unafanywa pia katika nchi nyingine kama 30. Michango ya kujitolea ndiyo inayowezesha pesa zinazohitajiwa zipatikane, na ikiwa katika nchi moja kumekuwa na ukosefu fulani, msaada wa ukarimu kutoka kwa wengine ndio umeondoa ukosefu huo.—Linganisha 2 Wakorintho 8:14.
14. Tangu mwaka wa 1935, Majumba ya Ufalme mapya yenye kuhitajiwa yamejengwaje?
14 Katika mwaka ule ule ambao “mkutano mkubwa” ulijulishwa waziwazi kuwa ni jamii ya kidunia, J. F. Rutherford, aliyekuwa msimamizi wa Sosaiti wakati huo, aliita mahali pamoja pa mikutano ya Mashahidi wa Yehova katika Hawaii Jumba la Ufalme. Kuanzia wakati huo, jina hilo limetumiwa kwa ukawaida na Mashahidi wa Yehova kutaja majumba ya mikutano yao. Kuanzia mwaka wa 1940 mpaka sasa, hesabu ya makundi imeongezeka kutoka 5,118 kufikia zaidi ya 46,000. Maelfu ya Majumba ya Ufalme mapya na vilevile majumba ya makusanyiko yaliyo makubwa zaidi yamejengwa. Jambo hilo limehitaji jitihada ya umoja, kwa habari ya kutoa pesa na pia kwa habari ya kazi yenyewe ya kujenga. Watu wa Yehova wenye umoja wameunga mkono kazi hiyo kwa moyo wote!
15. Kwa sababu gani ni jambo la maana kwetu kuwa na majengo yanayotosha ambamo tutafanyia mikutano?
15 Leo hesabu ya watu wanaomiminika kwenye Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova ni kubwa zaidi ya nyakati zote zilizotangulia na inaongezeka haraka sana. Sisi tunawakaribisha wote wanaotaka kweli kweli kufundishwa njia za Yehova ili waweze kutembea katika vipito vyake. (Isaya 2:2, 3; Waebrania 10:23-25) Pia tunataka kuhakikisha kwamba kuna vifaa vya kutosha vya kadiri inayoweza kuwatunza wale wanaothamini uandaaji huo uliofanywa na Yehova. Jambo hilo linaweza kufanywaje?
16. (a) Ikiwa Jumba la Ufalme jipya linahitajiwa kwa ajili ya kundi letu linaloendelea kukua, imetupasa tuwe na maoni ya namna gani juu ya kazi na gharama zinazohusika, sisi binafsi tuwe tutatumia au tuwe hatutatumia jumba jipya hilo? (b) Wakati kunapokuwa na ongezeko kubwa katika maeneo ambayo bei za viwanja ziko juu sana, Majumba ya Ufalme mapya yanaweza kujengwaje?
16 Ingawa sisi tunakutana katika makundi mengi ya kwetu, bado sisi ni “kundi moja” tu, kundi la watu wenye umoja. Kupendezwa na mpanuko wa ibada safi na kuwapenda ndugu zetu kutatusukuma tusaidie kwa njia yo yote tunayoweza, hata uhitaji wenyewe uwe unahusu mahali gani. Je! ongezeko la hesabu ya makundi yanayotumia Jumba la Ufalme fulani linatokeza uhitaji wa kujenga jingine jipya? Lingekuwa jambo zuri kama nini wale wanaoendelea kutumia majengo ya zamani watoe msaada wo wote wanaoweza ili jumba lijengwe kwa ajili ya kundi linalohitaji kuhamishwa! Katika maeneo mengine, akina ndugu wamejitolea kusaidia ujenzi wa Majumba ya Ufalme mengine wakati wo wote yanapohitajiwa. Kwa kuwa na mipango ya uangalifu na jitihada ya umoja, Majumba ya Ufalme mengi yaliyo mapya na mazuri yamejengwa kwa muda wa siku mbili au kwa muda mchache zaidi. Lakini, katika nchi fulani-fulani bei inayoongezeka sana ya viwanja katika maeneo ya mijini imefanya isiwezekane makundi moja moja yapate pesa za majengo yanayohitajiwa. Lakini jambo lisiloweza kutimizwa na kundi moja linaweza kutimizwa na jitihada ya umoja. Tutakapopashwa habari juu ya nafasi za kusaidia, sisi tutakuwa na itikio la namna gani?
17. Ni kanuni gani za Biblia zinazofaa katika kutimiza uhitaji huo?
17 Wakati Waisraeli walipopewa nafasi ya kuchangia ujenzi wa hema takatifu la Yehova, mioyo yenye nia ya kupenda iliwalazimisha kutoa vitu vilivyozidi kadiri iliyotakwa. (Kutoka 35:5-9; 36:5-7) Michango mikubwa ya kusaidia ibada ya kweli siyo pekee inayothaminiwa. Yesu alisifu ukarimu ulioonyeshwa kwa mchango mdogo sana wa mjane maskini. (Luka 21:1-4) Kwa habari ya misaada ya kusaidia watumishi wenzetu wa Mungu kwa njia za kimwili, mtume Paulo aliandika hivi: “Kama nia ipo, hukubaliwa kwa kadiri ya alivyo navyo mtu, si kwa kadiri ya asivyo navyo. . . . Wakati huu wa sasa wingi wenu uwafae upungufu wao... Kama ilivyoandikwa, Aliyekusanya vingi, hakuzidi, wala yeye aliyekusanya vichache hakupungukiwa.” (2 Wakorintho 8:12-15) Kanuni hiyo inaweza kutuongoza vizuri katika kufanya ushirikiano ili kuwe na Majumba ya Ufalme mapya au yaliyopanuliwa katika mahali po pote yanapoweza kuwa yakihitajiwa, sisi binafsi tuwe tunaishi au tuwe hatuishi katika eneo hilo.
18. (a) Ni nini kilichofanya tutoe Tangazo (Azimio) la Umoja kwenye makusanyiko ya wilaya ya hivi majuzi? (b) Ni nini maana ya lile wazo la kwanza katika Tangazo hilo? (c) ni nini maana ya lile la pili? (d) na maana ya lile la tatu? (e) Tangazo hilo lilimalizia kwa sala gani inayofaa?
18 ‘Umoja wa roho’ ni jambo linaloonekana likiwa katika tengenezo la Yehova, na sisi binafsi tuna pendeleo la kuuonyesha kwa matendo. Kwenye makusanyiko ya duniani pote tuliyofanya hivi majuzi, tulifanya tangazo la wakati wake la kuazimia jambo hilo. Limeonyeshwa kwa mara nyingine katika ukurasa wa 16. Sisi tunakutia moyo urudie kujikumbusha Tangazo hilo sasa, na hivyo ujipe mwenyewe nafasi ya kufikiria tena njia ambazo kwazo wewe binafsi unaweza kulitumia katika siku zitakazokuja.—Kutoka w2/1/84.
Jibu Lako Ni Nini?
◻ Yehova analindaje umoja wa watumishi wake?
◻ Yehova alielekezaje mambo ili Kuvunwa kwa jamii ya Ufalme kumalizwe?
◻ Mashahidi wa Yehova waliimarishwaje kwa ajili ya mateso makali sana kabla na wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili?
◻ Mungu aliwatayarishaje Mashahidi wake kwa ajili ya mkusanyo ulioanza mwaka wa 1935?
◻ Tunaweza kuwa na ushiriki gani katika kuwezesha kuwe na Majumba ya Ufalme yanayohitajiwa kwa haraka?
[Sanduku katika ukurasa wa 16]
TANGAZO (AZIMIO) LA UMOJA
Sisi, Mashahidi wa Yehova, tuliokusanyika kwenye hili letu “Umoja wa Ufalme” Kusanyiko la Wilaya, tungependa kutoa shukrani zetu za kutoka ndani sana moyoni kwa ajili ya mambo yote ambayo Yehova ametufanyia. Sisi tunashukuru kweli kweli kwa dhabihu ya Mwanaye mpendwa na kwa kutuchagua sisi tuwe kundi la watu kwa ajili ya Jina lake.
Basi, SISI TUNATANGAZA kwamba tumeazimia kudumisha umoja wa ajabu ambao katika huo Yehova ametukusanya sisi tukiwa kama kundi katika zizi lake, na tunaamini kabisa mwelekezo na mwongozo wa roho takatifu yake; nyakati zote tutajitahidi kudumisha mwenendo wetu uwe mwema kati ya mataifa huku tukitangaza tumaini la Ufalme kwa juhudi ili wote wenye nia ya kusikiliza wasikilize; tutajihadhari tusiondoke kwa njia yo yote ile katika mwendo wa Yehova hata kama ni nani atakayejaribu kutuvuta tuingie katika njia isiyofaa.
Na SISI TUNASALI tuweze kuendelea kuustahili upendo ambao Yehova ametuonyesha, sikuzote tukilithamini pendeleo tulilo nalo la kuchukua jina lake na la kuzitangaza habari njema za Ufalme wake ulio chini ya Kristo.
[Picha katika ukurasa wa 17]
Kufanya kuwe na Majumba ya Ufalme ya kutosha kunahitaji jitihada ya umoja, kwa habari ya kutoa pesa na pia kusaidia kazi ya kujenga