Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 8/15 kur. 14-19
  • “Taifa Hodari” la Mungu Lenye Umoja Kujaza Dunia

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Taifa Hodari” la Mungu Lenye Umoja Kujaza Dunia
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kutenganisha “Kondoo” na “Mbuzi”
  • Kuhubiri kwa Umoja
  • Ukuzi wa Haraka-Haraka Kutokana na Hesabu Ndogo
  • “Taifa Hodari” Laijaza Dunia
  • ‘Mdogo Awa Taifa Hodari’
    Kuokolewa Kuingia Katika Dunia Mpya
  • Kugawanywa kwa Watu kwa Kutegemea Suala la Ufalme
    Kuokolewa Kuingia Katika Dunia Mpya
  • Lile Suala la Ufalme Lawekwa Mbele!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Ufalme wa Mungu Ni Nini?
    Mungu Anataka Tufanye Nini?
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 8/15 kur. 14-19

“Taifa Hodari” la Mungu Lenye Umoja Kujaza Dunia

“Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa hodari; mimi, [Yehova], nitayahimiza hayo wakati wake.”​—ISAYA 60:22.

1, 2. (a) Umoja na utaratibu wa ulimwengu umeenda wapi? (b) Katikati ya ulimwengu usio na adili, kunatukia nini kwa watumishi wa Yehova?

WATU wenye maarifa wanakubali kwamba ulimwengu huu unakuwa wenye mgawanyiko na mvurugo zaidi na zaidi. Makala ya mhariri katika kichapo The New York Times ilitangaza hivi: “Jeuri ya kisiasa inaenea duniani pote ambavyo haijaonekana sana hapo mbele. . . . Kuna jeuri nyingi sana sasa hata kwamba ni vigumu kuzikumbuka zote.” Kichapo hicho kilisema: “Uhakika ni kwamba hakuna mtu anayeuendesha ulimwengu tena na kutunza namna fulani ya utaratibu.” Hata hivyo, uharibifu huo ndio Neno la Mungu lilitabiri ungekuwapo siku zetu.​—2 Timotheo 3:1-5, 13; Mathayo 24:3-13.

2 Kwa watumishi wa Yehova wenye umoja, mvurugo unaoenea ni ishara hakika kwamba mfumo wa mambo wa kale unakaribia mwisho wake, na mfumo mpya wa mambo unatokea. (Luka 21:28) Lakini, katikati ya ulimwengu ambao unazidi kumwiga mungu wake asiye na adili, Shetani Ibilisi, Yehova anasafisha watu wake na kuwaongoza kuelekea Utaratibu Mpya mwangavu. Yeye anawakusanya kwenye ibada yake safi, ambayo imeinuliwa juu kama kwamba ni juu ya mlima, juu zaidi ya namna nyingine zote za ibada. Wale wanaogeukia ibada hiyo ya umoja ya Mungu wa kweli halafu wanawaambia wengine hivi: “Njoni, twende juu mlimani kwa [Yehova], nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, naye atatufundisha njia zake; nasi tutakwenda katika mapito yake.” (Isaya 2:2, 3) Wale walioingizwa katika ibada hiyo yenye umoja wanatazamia sana ‘mbingu mpya na dunia mpya ambamo katika hizo uadilifu utakaa.’​—2 Petro 3:13, NW.

Kutenganisha “Kondoo” na “Mbuzi”

3, 4. (a) Ni matukio gani ambayo yamekuwa yakitendeka tangu mwaka 1914? (b) Watu wanatenganishwaje kwa ajili ya wokovu?

3 Kulingana na orodha ya wakati wa mambo ya Mungu ya unabii wa Biblia, “mbingu mpya” (Ufalme wa kimbingu wa Mungu chini ya utawala wa Kristo) zilisimamishwa katika mwaka wa maana wa 1914. Tangu wakati huo uchaguzi wa watawala washirika 144,000 wa “mbingu mpya” kwa ujumla umekamilishwa. (Ufunuo 14:1-4) Sasa Yehova anaita watu wawe raia za kidunia wa Ufalme huo. ‘Watatoka katika dhiki ile iliyo kuu’ wakiwa waokokaji waanze kujenga utaratibu mpya wenye uadilifu chini ya uongozi wa Ufalme.​—Ufunuo 7:9, 14; Mathayo 24:21.

4 Yesu alitabiri kukusanywa huko kwa maneno haya: “Hapo atakapokuja Mwana wa Adamu [Kristo] katika utukufu wake [katika uwezo wa Ufalme wa kimbingu], na malaika watakatifu wote pamoja naye, ndipo atakapoketi katika kiti cha utukufu wake; na mataifa yote watakusanyika mbele zake; naye atawabagua kama vile mchungaji abaguavyo kondoo na mbuzi; atawaweka kondoo mkono wake wa kuume, na mbuzi mkono wake wa kushoto.” Matokeo yawe nini? Yesu alisema: “Kisha mfalme atawaambia wale walioko mkono wake wa kuume [watu wenye mfano wa kondoo], Njoni, mliobarikiwa na Baba yangu, urithini ufalme mliowekewa tayari tangu kuumbwa ulimwengu. . . Kisha atawaambia na wale walioko mkono wake wa kushoto [watu wenye mfano wa mbuzi], Ondokeni kwangu, mliolaaniwa, mwende katika moto wa milele [uharibifu wa milele] aliowekewa tayari Ibilisi na malaika zake. . . . Na hao watakwenda zao kuingia katika adhabu ya milele; bali wenye haki watakwenda katika uzima wa milele.”​—Mathayo 25:31-46.

5. Rehema ya Yehova imedhihirikaje sasa?

5 Lakini, Yehova ni Mungu mwenye upendo na rehema. “Huvumilia kwenu, maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba.” (2 Petro 3:9) Kwa hiyo, kabla Mungu hajakomesha ulimwengu huu wenye mgawanyiko, wenye kupigana, ni mapenzi yake kwamba watumishi wake watangaze ujumbe wa tumaini la uzima wa milele katika Utaratibu Mpya wenye uadilifu. Ndiyo sababu, Mwanaye alitangaza hivi: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”​—Mathayo 24:14, NW.

6. Yehova anatumia nani katika kazi ya kuuhubiri Ufalme?

6 Ni nani wanaopaswa kuuhubiri Ufalme kabla mwisho haujaja? Bila shaka, Yehova hatatumia wale wasiotaka kumtumikia. Wale anaotumia katika kazi ya kuuhubiri Ufalme ni wale wanaomtii yeye kwa moyo wa kupenda. Unabii huu umetimizwa juu ya mabaki ya Israeli wa kiroho: “Nitawaweka pamoja kama kondoo.” (Mika 2:12) “Kondoo wengine” sasa wanaushiriki umoja huo pamoja nao. (Yohana 10:16) Wote hao ni mashahidi wa Yehova wenye umoja katika mataifa yote. Ni kutia ndani wazee na vijana, wa kiume kwa wa kike, kwa maana zaburi zilizoongozwa kwa roho ya Mungu zinasema: “Msifuni [Yehova ninyi] . . . vijana waume, na wanawali, wazee, na watoto; na walisifu jina la [Yehova].” “Wanawake watangazao habari [njema] ni jeshi kubwa.”​—Zaburi 68:11; 148:1, 12, 13.

Kuhubiri kwa Umoja

7. (a) Mashahidi wa Yehova wana umoja gani? (b) Tunawezaje kuwa na uhakika kwamba umoja huo utahifadhiwa?

7 Yehova, Yesu Kristo na malaika watakatifu wanahakikisha kwamba tengenezo la kidunia la wahubiri wa Ufalme linatangaza ujumbe wa Mungu kwa umoja. (Mathayo 28:19, 20; Yohana 14:26; Ufunuo 14:6, 7) Kwa hiyo Mashahidi wa Yehova wanafanya yale ambayo Neno la Mungu aliloliongoza linasema. Wao ni ‘wenye umoja kabisa, wakiwa na wazo moja tu na kusudi moja.’ ‘Kwa nia moja na kwa kinywa kimoja wanamtukuza Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo.’​—1 Wakorintho 1:10, Today’s English Version; Warumi 15:6.

8. Ni jambo gani la maana katika kudumisha umoja wa ibada?

8 Ili wawe na umoja huo wa wazo, kusudi na kuhubiri, Mashahidi wa Yehova wanajifunza Neno la Mungu la kweli kwa ukawaida. Wanafanya hivyo faraghani, kwenye makusanyiko ya kila mwaka na pia kwenye mikutano mitano ya kundi kila juma. Kwa njia hiyo wanapokea chakula cha kiroho chenye kuleta umoja penye meza ya Yehova. (Mathayo 24:45-47; Waebrania 10:24, 25) Elimu hiyo ya Biblia inatambuliwa kuwa ndiyo msingi wa ibada yao yenye umoja. Ni kama vile mwandikaji Mkatoliki William Whalem alivyosema katika gazeti U.S. Catholic: “Jumba la ufalme lo lote [la Mashahidi wa Yehova] linatoa elimu ya watu wazima katika mwezi mmoja zaidi ya ile inayotolewa mwaka mzima na mitaa mingi ya kanisa la Katoliki.” Ndiyo, elimu ya Biblia ndiyo msingi wa kuwa na “wazo moja,” “kusudi moja,” “kinywa kimoja.”

9. Tunawezaje kuwajua wale ambao Yehova anatumia kuuhubiri ujumbe wa Ufalme?

9 Kama una shaka lo lote juu ya ni nani Yehova anatumia kuhubiri “habari njema za ufalme” zake, jiulize mwenyewe: Watu mmoja mmoja wanapozuru kwenye nyumba za watu ili wazungumze juu ya Yehova na Ufalme wake, hao wenye kuzuru ni nani? Inajulikana wazi ni Mashahidi wa Yehova! Ni mara ngapi unapotembelewa na watu wa dini zile nyingine kuongea na wewe habari za Yehova na Ufalme wake? Ni mara ngapi watu hao wanazungumza juu ya mambo hayo, po pote? Wafuasi wa dini za ulimwengu huu zenye mgawanyiko wamenyamaza kimya juu ya Yehova na Ufalme wake. Ni wachache kati yao wanaojua hata Yehova ni nani au ambayo Ufalme wake utafanyia dunia hii. Na bado, Yehova na Ufalme wake ni habari zenye kutikisa ulimwengu, kwa sababu, kama Danieli 2:44 ilivyotabiri, Ufalme wa Yehova karibuni ‘utazivunja vipande vipande na kuzikomesha serikali nyingine zote kisha huo pekee utatawala milele na milele.’

Ukuzi wa Haraka-Haraka Kutokana na Hesabu Ndogo

10. Kabla ya mwaka 1914 watumishi wa Yehova walikuwa wachache kadiri gani, lakini tunapaswa kuwa na maoni gani juu ya yale yaliyotimizwa wakati huo?

10 Utangazaji wa Ufalme wa kisasa ulianza kwa njia ndogo. Tangu miaka ya kuanza na wa 1870 mpaka mwaka wenye kuleta badiliko wa 1914, hesabu za watangazaji wa Ufalme zilikuwa ndogo. Lakini waaminifu hao waliweka msingi wa mambo ambayo yangekuja. Ingawa mwanzo huo ulikuwa mdogo, unatukumbusha juu ya andiko linalosema ‘usidharau siku ya mambo madogo.’ (Zekaria 4:10) Kabla ya mwaka wa 1914, ilikuwa “siku ya mambo madogo” kwa watumishi wa Yehova, lakini mengi zaidi yangekuja karibuni.

11, 12. (a) Kulikuwa na ushuhuda gani kwamba roho takatifu ilikuwa ikitenda baada ya mwaka 1914? (b) Ni maelezo gani yaliyotolewa juu ya kazi ya Ufalme miaka zaidi ya 30 iliyopita, na twaweza kusema nini juu ya hilo sasa?

11 Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilipoanza mwaka wa 1914, mfumo wa mambo ya kale uliingia katika “siku za mwisho” zake. (2 Timotheo 3:1) Utawala wa Ufalme vilevile ulianza mwaka wa 1914. (Ufunuo 12:10-12) Ndipo Kristo alipopewa mamlaka ya kuanza kutenganisha “kondoo” na “mbuzi.” Kwa hiyo, roho takatifu ya Mungu ikaanza kufanya kazi kwa njia kubwa juu ya watumishi waaminifu wake. (Linganisha Matendo 2:16-21.) Hesabu za watangazaji wa Ufalme zilikua kutoka karibu 4,000 mwaka wa 1918 mpaka zaidi ya 260,000 mwaka wa 1948, hicho kikiwa ni kipindi cha miaka 30. Karibu wakati huo, C. S. Braden, profesa wa historia ya dini, aliandika hivi: “Mashahidi wa Yehova wameifunika dunia yote na ushuhuda wao kwa njia halisi. . . . Inaweza kusemwa kikweli kwamba hakuna kikundi kimoja cha kidini ulimwenguni ambacho kimeonyesha juhudi na udumifu mwingi katika jaribio la kuzieneza habari njema za Ufalme kuliko Mashahidi wa Yehova.”

12 Lakini yeye alisema hivyo miaka zaidi ya 30 iliyopita! Leo, kuna watangazaji wa Ufalme walio mara 10 ya vile walivyokuwa mwaka wa 1948! Kwa kuwa, kama Braden alivyosema, Mashahidi wa Yehova walikuwa “wameifunika dunia” kwa utangazaji wa Ufalme huko nyuma, ni jambo gani lingeweza kusemwa juu ya ukubwa wa kazi ya Ufalme sasa? Na sisi twaweza kusema hili kwa uhakika: Mengi zaidi yatakuja katika wakati ujao ulio karibu!

13. Ni matukio gani ulimwenguni pote yanayoonyesha kwamba andiko la Isaya 60:22 linatimizwa?

13 Ripoti kutoka nchi zaidi ya 200 zinaeleza juu ya upanuzi wa hesabu za watangazaji wa Ufalme. Ili kusonga pamoja na upanuzi huo, majengo ya matawi ya Sosaiti mapya yanajengwa au yanapanuliwa. Kuna mashine mpya, njia mpya za kuchapia na za haraka zaidi, kutumia kompyuta kwa kadiri kubwa, na wafanyi kazi wenye moyo wa kupenda katika jamaa zenye kukua za Betheli ulimwenguni pote. Upanuzi wote huo wa haraka unatuambia kwamba tunaona mbele ya macho yetu wenyewe utimizo wa ahadi yenye kutia moyo iliyotolewa zamani sana kuhusu watumishi wa Mungu waaminifu na wenye subira: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa hodari; mimi, [Yehova], nitayahimiza hayo wakati wake.” (Isaya 60:22) Hakuna shaka juu ya uhakika wa kwamba Mashahidi wa Yehova wanatayarishwa kiroho na kitengenezo ili watoe ushuhuda ulio mkubwa zaidi uliopata kutolewa katika historia ya ulimwengu juu ya Yehova na Ufalme wake!

14. Kwa sababu gani tunaweza kusema kwamba watumishi wa Yehova kwa uhakika wamepiga hatua sana wakawe “taifa hodari”?

14 Leo kuna wahudumu Wakristo wa habari njema wenye kutenda zaidi ya milioni mbili na nusu. Wanapatikana katika makundi zaidi ya 46,000 ulimwenguni pote. Mashahidi wa Yehova walipokusanyika Machi 29, 1983, ili kuadhimisha kifo cha Kristo, watu 6,767,707 walikusanyika pamoja, kwa njia hiyo wakaonyesha kupendezwa kwao na Ufalme wa Mungu. Hesabu hiyo inazidi idadi ya watu wa mataifa moja moja ya ulimwengu ambayo yanafanyiza karibu sehemu mbili juu ya tatu za mataifa yote ya ulimwengu! Kwa uhakika, watumishi wa Yehova wenye umoja wamepiga hatua sana wakawe “taifa hodari,” ingawa wao ni wachache wanapolinganishwa na jumla ya idadi ya watu ulimwenguni ya karibu bilioni nne na nusu.​—Mathayo 7:13, 14.

15. Kumetokea nini katika miaka michache iliyopita kuhusu kukusanywa kwa watu wenye mfano wa kondoo?

15 Hivi majuzi, kukusanywa kwa watu wenye mfano wa kondoo kumeanza mwendo wa mbio-mbio. Watu wenye nia ya kupenda uadilifu sasa wanamiminika kwenye tengenezo la Yehova kwa ajili ya ibada. Katika kufanya hivyo, wanashiriki utimizo wenye kusisimua wa ahadi ya Mungu iliyo kwenye Hagai 2:7, ambapo Yehova anasema: “Nami nitatikisa mataifa yote, na vitu vinavyotamaniwa [vya] mataifa yote vitakuja; nami nitaijaza nyumba hii utukufu.” Watu hao wenye kutamanika na wanyenyekevu wanawaambia watumishi wa Yehova: “Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia kwamba Mungu yu pamoja nanyi.”​—Zekaria 8:23.

16, 17. Yehova atawatumiaje watu wake kabla hajakomesha mfumo huu wa mambo usiomcha Mungu?

16 Tengenezo linaloonekana lenye kupanuka la Yehova linakaribia wakati ambapo yeye atalitumia katika njia nyingine kubwa: kutoa ujumbe wake wa mwisho wa hukumu juu ya mfumo huu. Hilo laweza kufananishwa na wakati Waisraeli, ambao tayari walikuwa wamepiga hatua kuzunguka Yeriko mara moja kwa siku katika siku sita, waliagizwa: “Siku ya saba mtauzunguka mji mara saba, nao makuhani watapiga tarumbeta zao. . . . Nanyi mtakaposikia sauti ya tarumbeta, watu wote watapiga kelele kwa sauti kuu; na ukuta wa mji utaanguka chini pale pale.” Kwa hiyo katika siku ya mwisho kazi iliongeza mbio mara saba! Kisha tarumbeta zikatoa sauti, watu wakapiga kelele ya vita na “ule ukuta wa mji ukaanguka nchi kabisa.”​—Yoshua 6:2-5, 20.

17 Leo maji “mororo” ya ukweli yanapelekwa kwa watu ili kuwatia moyo wamgeukie Yehova. Lakini karibuni itakuja siku wakati ujumbe huo utabadilika uwe “mgumu.” Utatangaza mwisho uliokaribia sana wa mfumo mzima huu wa kishetani. Maji mororo ya ukweli yatashikamana yawe mawe magumu ya mvua ya ukweli. Ujumbe huo mbalimbali wa mwisho wa hukumu utakuwa wenye nguvu sana hata unafananishwa na “mvua ya mawe kubwa sana, ya mawe mazito kama talanta,” yaani, makubwa wee! Ndiyo sababu Ufunuo 16:21 unasema: “Pigo lake ni kubwa mno.”

“Taifa Hodari” Laijaza Dunia

18. (a) Ufalme wa Mungu ni halisi jinsi gani? (b) Andiko la Danieli 2:35 linaonyeshaje ambayo Ufalme huo utafanya hatimaye?

18 Ufalme wa Mungu ambao Mashahidi wa Yehova wanatoa utii wao kamili kwanza ni serikali halisi kweli kweli. Kristo na washirika wake 144,000 ni watawala wake wa kimbingu. Ina sheria halisi na “katiba”​—Neno la Mungu. Serikali hiyo halisi vilevile ina raia ambao wanafanyiza taifa hilo lenye kukua, mamilioni yao wakiwa na umoja kama taifa moja. Na Biblia inatabiri kwamba baada ya Ufalme huo wa Kimasihi kuponda-ponda serikali zote za kilimwengu zisiwepo, ‘utaijaza dunia yote.’ (Danieli 2:35) Hiyo itakuwaje?

19, 20. Ni jinsi gani watumishi wa Yehova watakuwa “taifa hodari” kwa maana kamili?

19 Wale watakaookoka Har–Magedoni wataanza kutengeneza Paradiso ambayo Yesu alisema kwenye Luka 23:43 (NW) (Ufunuo 16:14, 16) Halafu, ndipo “kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.” (Matendo 24:15) Wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo katika uwezo wa Ufalme, wote watapewa nafasi ya kuchukua msimamo wao kwa ajili ya utawala wa Ufalme. Wale wasiotaka utawala wa uadilifu wataondolewa. (Ufunuo 20:6, 11-15) Kwa hiyo, mwishoni mwa miaka elfu, kila mtu atakayekuwa akiishi duniani atakuwa mwabudu aliyejitoa wa Yehova! Halafu itaweza kusemwa kwamba Isaya 11:9 ni andiko litakalotimizwa kwa maana kamili: “Dunia itajawa na kumjua [Yehova], kama vile maji yanavyoifunika bahari.”

20 Huo utakuwa wakati mtukufu kama nini! Kila mtu utakayekutana naye atakuwa mwabudu wa Yehova, mwenye “wazo moja,” “kusudi moja,” “kinywa kimoja.” Mabilioni ya waabudu hao wenye umoja, walioinuliwa mpaka kwenye ukamilifu wa kibinadamu, wataijaza dunia-Paradiso. Kisha kweli kweli watafanyiza “taifa hodari,” taifa kubwa zaidi ambalo dunia imepata kuona. Ndiyo, jamaa ya kibinadamu yenye umoja si ndoto tu. Tayari inaendelea kufanyizwa sasa! Je! wewe ni sehemu yake?​—Kutoka w 3/15/84.

Maulizo ya Kurudia Kujikumbusha

◻ Ulimwengu ujapokuwa na mvurugo zaidi, ni jambo gani linalowapata watu wa Yehova?

◻ Ni kazi gani kubwa ya kutenganisha inayofanywa sasa?

◻ Sababu gani tunaweza kuwa na uhakika kwamba umoja wa watumishi wa Yehova utahifadhiwa?

◻ Tengenezo la Yehova lionekanalo linasitawije kuwa “taifa hodari,” na litaendelea mpaka wapi?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kama mchungaji anavyotenganisha kondoo na mbuzi, ndivyo Yesu Kristo katika uwezo wa Ufalme anavyotenganisha watu leo.

[Picha katika ukurasa wa 17]

Makao ya Betheli na viwanda kama hivi vinajengwa au kupanuliwa ili kusogeza kazi ya kuuhubiri Ufalme

Ebina, Japani

Abidjan, Ivory Coast

Ingleburn, N.S.W. Australia

Enebakk, Norowei

Ajalvir (Madrid), Spania

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki