Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 5/15 kur. 4-7
  • Kutenda Watu Unyama—Mwisho Wake Ni Karibu!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutenda Watu Unyama—Mwisho Wake Ni Karibu!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Tendo la “Mtu Kutenda Mwenzake Kinyama” Lilianzaje?
  • Utakomaje?
  • Paradiso Yarudishwa
  • Mungu Ana Kusudi Gani kwa Dunia
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • “Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya”
    “Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya”
  • Kusudi la Mungu kwa Wanadamu Ni Nini?
    Biblia Inatufundisha Nini?
  • Watawala Katika Makao ya Roho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 5/15 kur. 4-7

Kutenda Watu Unyama​—Mwisho Wake Ni Karibu!

“KITU cha umaridadi ni furaha ya milele,” ndivyo akaandika mshairi Keats. Vitu vingi vya umaridadi​—michoro, sanaa na hasa vitabu vilivyoandikwa kwa ustadi mwingi​—vinafunua jambo fulani juu ya mwenye kuvifanyiza. Dunia, ambayo ni “kitu cha umaridadi,” ikiwa na maajabu yake ya uhai, ukuzi, rangi, ladha na maelfu ya vitu vingine vyenye kupendeza, inamfunua Mfanyizaji mwenye hekima yote, uwezo wote na upendo wote.

Kitabu kilichoandikwa kwa ustadi mwingi zaidi ya vyote, yaani Biblia, kimekuwa pia “kitu cha umaridadi” na “furaha” kwa mamilioni ya watu katika muda wa mamia ya miaka. Kinatuambia kwamba “Mungu ni upendo,” kwamba yeye ni ‘mwenye rehema na fadhili’ na kwamba mtu alifanywa “kwa mfano wake.” (1 Yohana 4:8; Kutoka 34:6; Mwanzo 1:27) Wengi wa wanadamu wanaonyesha wazi sifa za Mfanyi wao na kuonyesha huruma na fadhili halisi. Wanakirihi ukatili na mwenendo wa kinyama. Kwa hiyo​—

Tendo la “Mtu Kutenda Mwenzake Kinyama” Lilianzaje?

Kwa uhakika halikuanzwa na Mungu. Kabla ya kuumba watu wawili wa kwanza, aliwatayarishia kwa upendo makao maridadi. Kisehemu cha dunia kilipambwa kwa miti, maua, matunda, vijito na wanyama kwa wingi, hiyo ikiwa ni Paradiso! Ili wafurahie milele umaridadi huo, iliwapasa kutii Mungu, kufanya mambo kwa njia yake. Lakini wao hawakuwa sanamu tu zenye kuendeshwa na nguvu za umeme ili zitii amri; walikuwa na uhuru wa nia na hiari. Mungu aliwataka viumbe wake wa kibinadamu, ambao ndio waliokuwa utukufu wenye kurembesha zaidi uumbaji wake unaoonekana, wamtumikie kwa sababu walimpenda na walifurahia kufanya mapenzi yake.

Bila shaka bustani ya Edeni na wakaaji wake wenye furaha na upatani ilipendeza sana machoni pa Mungu na uumbaji wake usioonekana wa malaika. Kusudi la Mungu lilikuwa kwamba, kutokana na mwanzo huo mtukufu, dunia nzima iwe Paradiso kila mahali ikiwa na watu wenye furaha, wenye kumletea utukuzo na sifa.

Lakini malaika walikuwa pia viumbe vyenye uhuru wa hiari. Mmoja wao aliruhusu tamaa na nia ya makuu imshike sana. Alianza kujiona kuwa mungu wa wanadamu. (2 Wakorintho 4:4) Kwa hiyo alipanga hila awavute watu wawili wa kwanza kwenye upande wake. Ili kushawishi Hawa ajiunge na uasi wake, alimwahidi kwamba, “Mtakuwa kama Mungu,” na, zaidi ya hilo,“hakika hamtakufa”​—uongo wa kwanza kabisa kusemwa. (Mwanzo 3:4, 5) Hawa aliangukia chambo hicho, na baadaye Adamu akajiunga naye kujiachilia wachochewe na mshauri wao mwasi aliyekuwa malaika. Hivyo huyo aliyekuwa malaika hapo kwanza akawa adui wa Mungu, au “Shetani” katika Kiebrania.

“Utakufa hakika.” Mungu alikuwa ameonya Adamu kwamba hilo ndilo lingekuwa tokeo la uasi. (Mwanzo 2:17) Kwa kuwa ahadi ya Shetani ya kutokufa wakiwa katika mwili ilikuwa ya uongo na onyo la Mungu lilikuwa la kweli, Adamu na Hawa walikufa, hivyo ikawa kwamba Shetani “alikuwa mwuaji tangu mwanzo.” (Yohana 8:44) Kwa sababu ya mavutano yake ya kiibilisi, amani na upatani katika jamaa ya kibinadamu iliharibiwa pia. Baadaye, Kaini, mwana mkubwa zaidi ya Adamu, akawa mwenye wivu kwa sababu toleo la Abeli kwa Yehova lilikubaliwa, lakini lake likakataliwa. Kwa ‘kughadhibika sana,’ Kaini alimwua Abeli ndugu yake bila huruma. Hapo likaanza tendo la “mtu kutenda mwenzake unyama.”​—Mwanzo 4:2-8.

Tendo hilo la uuaji lilivuta fikira pia kwenye suala la pambano kati ya ibada safi na ibada ya uongo. Abeli alikuwa wa kwanza wa mstari mrefu wa mashahidi wa Yehova ambao wangeuawa kwa sababu ya imani yao.

Muda fulani baada ya kuuawa kwa Abeli, malaika wengine walivutwa kwa chambo cha Shetani wavae miili ya kibinadamu ili wafanye ngono na wanawake warembo duniani, na hivyo wakaanguka chini ya mavutano ya Shetani. Kutokana na miungano hiyo haramu wakatokea “Wanefili,” au “watu wenye nguvu nyingi”​—wachokozi wakatili. Baada ya muda mfupi, “dunia ikajaa dhuluma”​—“unyama” wa mtu ukazidika. (Mwanzo 6:1-11) Kwa haki na rehema kabisa, Yehova hangeweza kuruhusu hali hizo za msukosuko ziendelee. Aliufagilia mbali huo mfumo wa mambo ya kale katika siku za Noa kwa kutumia Gharika.​—2 Petro 2:5.

Lakini jambo hilo halikuondoa kabisa mavutano mabovu ya Shetani. Gharika ililazimisha malaika wasiotii wavue miili ya kibinadamu. Sasa kwa kuwa walikuwa wametenganishwa na tengenezo takatifu la Yehova, wakawa tengenezo lisiloonekana la kishetani wakiwa chini ya utawala wa Shetani. (Waefeso 6:12) Ili kusimamia wanadamu, wanatumia upashanaji habari na ulimwengu wa roho, upashanaji habari na wafu, unajimu na njia nyingine za kujua mafumbo kwa kutumia uchawi. Ingawa hawawezi kuvaa tena namna ya kibinadamu, mara nyingi wanapagaa wanadamu, wanyama na vitu visivyo na uhai kama hirizi. Wakiwa chini ya mavutano ya nguvu za kishetani na ushupavu wenye upofu wa dini ya uongo, utaifa na ukabila, watu wanafanya mambo ya kinyama ambayo hawangefanya kwa kawaida.

Basi, si ajabu kwamba mateso ya kidini yanaendelea mpaka leo hii. Katika fungu letu la utangulizi katika ukurasa wa 3 kimetajwa kikundi cha Wakristo waliokaribia kuuawa kwa kupigwa rungu. Waliteswa kwa sababu walikuwa ni Mashahidi wa Yehova. Katika pindi hiyo waliendelea kuwa hai baada ya kupigwa. Wakati mwenye kuongoza kikundi hicho alipoendelea kumiminiwa mapigo mengi, alimwomba Yehova “atunze maisha za hawa, ‘kondoo’ Zake.” Polisi walishangaa kuona kwamba hakuna hata mmoja wao aliyekufa. Yehova anaweza kuwalinda walio wake yakiwa ni mapenzi yake.​—2 Mambo ya Nyakati 16:9.

Katika United States (Amerika), matendo ya ukatili wa kikabila yametokeza ghasia za kinyama zenye kufanywa na watu wengi, na hata wakaamua wenyewe kuua watu bila kutegemea sheria. Inajulikana sana pia kuwa weupe wengine wanaokaa Afrika wanatenda weusi kwa nia kali ya majivuno. Mara nyingi dini imeshirikiana na siasa katika kurefusha kumbukumbu lile refu la matendo ya kinyama ya umwagaji wa damu ambayo yamejaa katika vitabu vya historia. Maneno yanayofuata yaliandikwa na E. Bolaji Idowu, profesa wa uchunguzi wa kidini kwenye Chuo Kikuu cha Ibadan, Nigeria: “Tamaa ya makuu ya makuhani wa kidini ikiwa pamoja na sehemu zote zake za . . . namna za unyama wa kuchukiza sana uliotendwa kwa kusingizia Uungu​—mambo hayo yametia aibu daima katika dini . . . Watu wanawezaje kusahau kwamba historia imekuwa na vile Vita Vitakatifu vya Wakristo, vita vya Waislamu vinavyoitwa Jihad, Baraza la Kanisa la Rumi la kugandamiza wenye kulipinga, pia matendo ya kuchoma watu kwa moto na kuwakata viungo vya mwili na kufanya uharibifu kwa uteketezaji?”

Utakomaje?

Kwa uhakika si kupitia jitihada za kibinadamu. Matengenezo fulani yenye huruma ya kibinadamu yanajaribu kufanya hali ya mwanadamu iwe nafuu, lakini ulimwengu umezama mno katika utope wa ufisadi na jeuri hata jitihada za mwanadamu zisiweze kufanikiwa.

Lakini, Yesu alisema: “Yasiyowezekana kwa wanadamu yawezekana kwa Mungu.” (Luka 18:27) Pia aliwaambia wanafunzi wake: “Jipeni moyo; mimi nimeushinda ulimwengu.” (Yohana 16:33) Akiwa ndiye adui mkubwa zaidi wa Mungu, Shetani alichukua Yesu akatumia viongozi wa kisiasa na kidini wamshambulie​—tangu Mfalme Herode aliyejaribu kumwua akiwa kitoto kichanga mpaka makuhani waliotumia nguvu za Rumi kumwua juu ya mti. Pia Shetani alijaribu kumshawishi Yesu kwa chambo chenye fahari nyingi​—“milki zote za ulimwengu, na fahari yake”​—kama tu Yesu angemwabudu. (Mathayo 4:8) Lakini Yesu alishinda jitihada za Shetani kumtawala; aliendeleza ukamilifu kupita mateso mabaya sana ya kupigwa mijeledi na kuwekwa mtini.

Kwa njia ya maana sana, kwenye dakika hiyo ya giza ilipoelekea kama kwamba Yesu angeshindwa, yeye alionyesha kwamba kwa kweli ushindi wa kukata maneno ulikuwa umepatikana juu ya Shetani. Mmoja wa wenzi wake katika kuteswa, mnyang’anyi, alisihi hivi: “Bwana, unikumbuke wakati unapokuja katika ufalme wako.” Kupitia Yesu, hata mhalifu huyo wa cheo cha kikawaida tu alikuja kupata utahamini fulani wa Ufalme wa Mungu kuwa ndilo tumaini la pekee kwa mwanadamu. Yesu alijibu hivi kwa ushindi: “Kweli ninakuambia [leo, Utakuwa] pamoja nami katika Paradiso.”​—Luka 23:42, 43.

Hapo Yesu alikamatanisha wazi Ufalme wake na Paradiso, akaonyesha kwamba hiyo ingechukua daraka kubwa katika kutimiza kusudi la Yehova la hapo kwanza kwa ajili ya dunia hii. Lakini wakati gani? Namna gani? Ni wazi ulimwengu mwovu wa Shetani lazima uondolewe kwanza. Dalili zinaonyesha kwamba jambo hilo litatukia karibuni sana.

Alipoulizwa na wanafunzi wake hilo lingetukia wakati gani, Yesu alitaja vita, upungufu wa chakula, matetemeko ya ardhi, magonjwa ya kipuku, ongezeko la uhalifu, matukio ya ajabu na ya kuogopesha katika mbingu, hangaiko kuu kwa wakati ujao, na mambo mengine, kuwa yangefanyiza ishara yenye mambo mengi kuonesha kwamba “mwisho” ni karibu. (Mathayo 24:3-14; Luka 21:10, 11, 25, 26) Mambo hayo yamekuwa yakitukia kwa kadiri isiyotangulia kuwa na kifani tangu mwaka wa 1914. Kwa hiyo, kama Yesu alivyosema: “Basi mambo hayo yaanzapo kutokea, changamkeni . . . kwa kuwa ukombozi wenu umekaribia . . . Tambueni ya kwamba ufalme wa Mungu u karibu.” (Luka 21:28, 31) Sasa kumbe wakati umekaribia tendo la “mtu kutenda mwenzake unyama” likome!

Hiyo ndiyo sababu Mashahidi wa Yehova tayari wanafanya mabadiliko makubwa katika maisha zao kwa kujifunza Biblia wakiwa na bidii na kutenda inayoyasema. Wao hawahusiki katika mapigano ya kisiasa wala ‘hawajifunzi vita tena kamwe.’ Wanajitahidi kuwa wenye tabia pole na wenye kupenda jirani zao. Yesu alisema: “Wenye furaha ni wenye kuamanika” na “wenye furaha ni wale wenye tabia pole, kwa kuwa watairithi dunia.”​—Isaya 2:4, UV; Mathayo 5:5, 9, NW.

Paradiso Yarudishwa

Katika wakati uliowekwa wa Mungu, Kristo Yesu atapigana na ‘wafalme wa dunia, na majeshi yao’ na kusafisha kabisa dunia hii iondokwe na kila kisehemu cha ulimwengu wa Shetani. Ushindi huo mkubwa sana utakuwa upeo wa “dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu.” Baadaye Shetani na mashetani wake ‘watafungwa,’ au wazuiwe wasitumie mavutano yao mabovu juu ya wanadamu, kwa miaka elfu moja.​—Mathayo 24:21; Ufunuo 16:14-16; 19:11-20; 20:1-3.

Halafu? ‘Mbingu mpya na dunia mpya’ ambamo “haki yakaa”​—Ufalme wa Mungu ukiwa ndio umesimamia mambo yote kabisa huku ‘mapenzi yake yakitimizwa, duniani kama mbinguni.’ (2 Petro 3:13; Mathayo 6:10) Chini ya mwelekezo wa Ufalme, pole kwa pole dunia itarudishwa iwe Paradiso. Na ni katika Paradiso hiyo kwamba mnyang’anyi aliyekufa pamoja na Yesu atainuliwa kwa wafu akiwa mmoja wa mamilioni walio katika “makaburi ya ukumbusho” watakaosikia sauti ya Yesu “na kutoka.”​—Yohana 5:28, 29, NW.

Mtu huyo aliyekuwa mhalifu atakuta nini? Kwamba ule ufisadi na ukatili wa Rumi na milki na serikali nyingine zote zimetokomea milele! Badala ya roho ya kishetani ya pupa, tamaa chafu, chuki na woga kuzaliana duniani, kutakuwa na hali nzuri ajabu ya amani, furaha, umoja na upendo. Paradiso ya kiroho ambayo tayari inafurahiwa na mamilioni ya watu wa Yehova itaenea duniani pote. “Matendo ya mwili,” kama “uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo,” yataondolewa kabisa, kwa sababu “watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.”​—Wagalatia 5:19-21.

Bila shaka mnyang’anyi yule alizoea mengine ya mambo hayo, lakini baada ya kufufuliwa atakuwa na mwanzo mpya kwa sababu “yeye aliyekufa amehesabiwa haki mbali na dhambi.” Mnyang’anyi huyo ameisha kupokea “mshahara wa dhambi . . . mauti” naye atakuwa katika hali ya kuelekea kupokea “karama ya Mungu,” yaani, “uzima wa milele katika Kristo Yesu Bwana wetu.”​—Warumi 6:7, 23.

Lo, kitakuwa kitulizo na taraja zuri kama nini kwa mnyang’anyi huyo na mamilioni zaidi ya watu! Ufalme wa Mungu ukiwa ndio unaosimamia dunia yote kwa uadilifu na hekima, hiyo itazaa matunda yake na kupambwa kwa uzuri. Viumbe vitakavyokuwa hai duniani, vya namna nyingi sana za kusisimua, vitakuwa vimetiishwa tena chini ya mtu kama hapo kwanza. (Mwanzo 1:28; Isaya 11:6-9) Paradiso hiyo ya kidunia, iliyo “kitu cha umaridadi,” itakuwa “furaha ya milele.”

Jambo la maana zaidi ni kwamba, kwa kuwa roho takatifu ya Yehova itamiminika kwa uhuru, tunda la roho hiyo litasitawi​—“upendo, furaha, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujiweza.” (Wagalatia 5:22, 23, AW) Makabila na mataifa yote yatakuwa udugu mmoja mkubwa. Namna gani? Kwa ‘kujivika upendo​—kile kifungo kikamilifu cha muungano.’ Tendo la “mtu kutenda mwenzake unyama“litatoweka milele.​—Wakolosai 3:14.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki