Umoja wa Ufalme Umeonekana Leo
“Mwonapo mambo hayo yanaanza kutokea, tambueni ya kwamba ufalme wa Mungu u karibu.”—LUKA 21:31.
1. Yesu alitabiri juu ya nini katika Luka sura ya 21?
MANENO hayo yaliyo juu yalisemwa na nabii aliye mkubwa kupita manabii wote. Naye Yesu alimaanisha mambo gani hapo? Ni mambo yale yale yanayotuzunguka sisi katika ulimwengu wa leo usio na umoja! Ulimwengu huu unabomoka-bomoka. Ni mambo yale ambayo Yesu aliyatabiri kuwa ishara ya “umalizio” (NW) wa mfumo wa ulimwengu, aliposema juu ya “vita na fitina,... na katika nchi dhiki ya mataifa wakishangaa” wasijue njia ya kutokea. (Mathayo 24:3, 7, 8; Luka 21:9, 25) Ni ukosefu wa umoja kila mahali! Lakini je! Mashahidi wa Yehova wahangaike kwa sababu ulimwengu hauna umoja?
2. Tufanyeje kwa ajili ya hali za ulimwengu, na kwa sababu gani?
2 Bwana yetu anatujibia. Yesu alisema: “Basi mambo hayo yaanzapo kutokea, changamkeni, mkaviinue vichwa vyenu, kwa kuwa ukombozi wenu umekaribia.” (Luka 21:28) Ukombozi kutoka kwenye nini? Kutoka kwenye ulimwengu usio na umoja ambao una ugonjwa wa kuua.—1 Yohana 5:19.
Dhiki ya Kisiasa
3. Watu wenye maarifa wanasema nini kwa masikitiko juu ya matukio ya kisiasa?
3 Hata Umoja wa Mataifa si umoja wa mataifa tena. Akiomboleza juu ya kutokuweza kwa Baraza la Usalama kudumisha amani na usalama, katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa alitangaza hivi: “Tuko karibu sana kuingia katika machafuko hatari ya kimataifa.” Ukosefu wa umoja uliopo ni wa kushtua sana. Mwandikaji mmoja wa gazeti Washington Post anaeleza hivi: “Matukio hayazuiliki.” “Tangu miaka ya 1960 serikali kila mahali, Magharibi na Mashariki, zimeanza kuacha kufanya kazi,” ndivyo anavyoandika mmoja aliyekuwa msaidizi wa White House na mshauri wa kisiasa. Na mmoja aliyekuwa balozi wa U.S. katika Umoja wa Mataifa amesema Baraza Kuu “linakuwa Jukwaa la Upumbavu.”
4. Andiko la Luka 21:26 linatimizwa kwa njia gani mbalimbali zenye kutokeza?
4 Lakini mambo mabaya zaidi yanaweza kutokea, kwa maana vita vya maneno vinazidi kuchemka, na tayari zile serikali kubwa-kubwa zenye nguvu za nyukilia zimelundika akibani silaha kubwa za kivita zinazoweza kuleta maangamzi makubwa yanayoyazidi mara 1,600,000 yale yaliyoupata mji wa Hiroshima. Kulingana na maoni ya mmoja aliyekuwa balozi wa United States (Amerika) huko Mosko, serikali hizo mbili kubwa-kubwa ziko “katika mwendo wa kuelekea kugongana dafurao,” naye anatangaza kwamba “pasipo shaka mahali fulani mlipuko utakuja kutokea.” Hayo ndiyo matunda ya ukosefu wa umoja katika ulimwengu wetu leo. Tisho lililopo ni la kweli. Iko sawa na vile Yesu alivyosema ingekuwa wakati wa “umalizio wa mfumo wa mambo”: “Watu wakivunjika mioyo kwa hofu, na kwa kutazamia mambo yatakayoupata ulimwengu. Kwa kuwa nguvu za mbinguni zitatikisika.” (Luka 21:26) Ndiyo, hata mbingu zingekuwa na tisho, wakati mataifa yangejitayarisha kupeleka vyombo vya angani vyenye kuchukua silaha za nyukilia!
Biashara Kubwa-Kubwa Zinatikisika
5. Ni woga na huzuni gani ambazo zimefurikia ulimwengu wa kibiashara?
5 Ukosefu wa umoja na kuwako kwa woga ni mambo yaliyoujaa ulimwengu wa uchumi pia. Msimamizi wa Banki ya Ulimwengu anatangaza kwamba, “Mimi sifikiri kuna usalama wo wote kwa muda wa miaka kumi inayokuja.” Kwenye mkutano uliofanywa mwaka jana, nchi 24 zenye maendeleo makubwa ya viwandani zilitoa utabiri wa kutazamia mabaya kwa kusema kwamba zingekuwa na watu milioni 30 wasioajiriwa kazi mwaka wa 1983. Unabii huo ulitimia kabisa.
6. Neno la Mungu linasema nini juu ya hali mbaya ya kiuchumi ya dini na matokeo yake?
6 Mshindi wa Zawadi ya Nobeli katika mambo ya kiuchumi anaijumlisha hali yote ya kifedha ya ulimwengu kwa kusema, “Mambo yote yameharibika kabisa.” Katika jambo hilo, dini ya ulimwengu inahusika kabisa kabisa. Yale “maji mengi” ya Ufunuo 17:1, 15—“jamaa na makutano na mataifa na lugha” ya ulimwengu huu usio na Mungu—yamekuwa yakiondoa tegemezo lao kwa dini ya uongo hata kwamba tengenezo la kifedha kwa dini ya uongo limekuwa likikauka pia. (Linganisha Ufunuo 16:12.) Lakini hali mbaya sana ya kiuchumi ya wakati huu inayopata makanisa si kitu ikilinganishwa na dhiki watakayopata wakati Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova atakapotekeleza hukumu kwa utimizo wa maneno yake: “Jambo baya, jambo baya la namna ya peke yake; angalia linakuja. Watatupa fedha yao katika njia kuu za mji, na dhahabu yao itakuwa kama kitu cha unajisi; fedha yao na dhahabu yao hazitaweza kuwaokoa siku ya ghadhabu ya [Yehova].” (Ezekieli 7:5, 19) Na watu wenye pupa wenye kuongoza biashara kubwa-kubwa watapatwa pia na huzuni kuu ya dini ya ulimwengu!—Ufunuo 18:2, 3, 16.
Ukosefu Mbaya Sana wa Umoja Katika Dini
7. Ukatoliki umeshindwaje kuleta umoja?
7 Ukosefu wa umoja ni tukio la kweli lenye kuchukiza sana pia katika ulimwengu wa kidini. Dini ya ulimwengu iko katika hali mbaya sana leo! Katika Ukatoliki, kuna mapadri wenye kuhusika katika upigaji wa vita haramu na kwa upande mwingine kuna maaskofu wenye kujishughulisha sana kufanya silaha za nyukilia ziache kuundwa. Papa aliuita mwaka wa 1983 Mwaka Mtakatifu. Je! kufanya hivyo kunasaidia? Vita vya maneno vilichemka zaidi. Mwaka wa 1933 pia ulikuwa Mwaka Mtakatifu kwa kutangazwa na papa kuwa hivyo, lakini ulitimiza jambo gani-i? Hitler alipata mamlaka, akaanza mfululizo wa matukio yaliyotokeza Vita ya Ulimwengu ya Pili.
8. Ni hali gani zenye ukosefu wa umoja zinazoonekana katika Uprotestanti?
8 Baraza la Ulimwengu la Makanisa, limeungwa mkono na matengenezo 301 ya kikanisa ya Uprotestanti na Orthodoksi. Likiwa na washiriki wanaokadiriwa kuwa milioni 400, lilichanga mamia ya maelfu ya dola za kusaidia wanasiasa wenye kutaka mapinduzi. Katika United States pekee kuna madhehebu za kidini zaidi ya 1,200. He! he-he-he! zinapiga tarumbeta yenye sauti nyingi zisizopatana kama nini! Ukosefu wazo wa umoja umeshiriki sana kuleta “fitina” na “maasi” ambayo Yesu alisema yangekuwa hivyo hivyo wakati wa “umalizio wa mfumo wa mambo” (NW).—Luka 21:9; Mathayo 24:3, 12.
9. Kundi la Kikristo la kweli linaweza kutambuliwaje?
9 Ukosefu mkubwa sana wa umoja ambao unaonekana leo katika dini za Jumuiya ya Wakristo unatofautiana kabisa na maelezo ya mtume Paulo juu ya kundi la kweli la Kikristo yanayosema kundi ‘linajitahidi kuuhifadhi umoja wa roho katika kifungo cha amani.’ Paulo alisema: “Mwili mmoja, na [roho moja], . . . Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja. Mungu mmoja, naye ni Baba wa wote, aliye juu ya yote na katika yote na ndani ya yote.”—Efe. 4:3-6.
Mahali Ambapo Umoja ni Tele
10. “Kifungo cha amani” sasa kinapatikana wapi, na kwa sababu gani ni hapo peke yake kinapatikana?
10 Basi, ni wapi tunapoweza kukipata hiki “kifungo cha amani”? Si katika ulimwengu, kwa maana ukombozi tunaopewa ni wa kuondolewa katika ulimwengu wa Shetani na katika ukosefu wao wa umoja wa kisiasa, wa kiuchumi na wa kidini. Kwa kuwa sisi ni Wakristo wenye kuitegemea Biblia, sisi si sehemu ya ulimwengu huu wenye ukosefu wa umoja. Ndiyo sababu Yesu alisema hivi, wakati alipokuwa akisali kwa ajili ya wafuasi wake wapakwa-mafuta: “Wao si sehemu ya ulimwengu, sawa na vile mimi nisivyo sehemu ya ulimwengu.” Kisha aliongezea hivi: “Mimi natoa ombi, si kuhusu hawa tu, bali pia kuhusu wale wanaoniamini mimi kupitia neno lao; ili kwamba wao wote waweze kuwa mmoja, sawa na vile wewe, Baba, ulivyo katika mwungano pamoja na mimi na mimi nilivyo katika mwungano pamoja na wewe ili wao pia waweze kuwa katika mwungano pamoja na sisi, ili kwamba ulimwengu uweze kuamini kwamba wewe ulinituma mimi.”—Yohana 17:16-21, NW.
11. Wakristo wa kweli wamekuwaje “kundi moja”?
11 Tunauona umoja huo wa ajabu leo katika jamii ya mataifa yote ya Mashahidi wa Yehova. Jambo la kufurahisha ni kwamba mamilioni ya watu kutoka ulimwenguni yameuona umoja huo, na wengi wa hao wanaojifunza Neno la Mungu wanakusanyika sasa wakiwa “kondoo wengine” wa Bwana. Hao wanapofanya umoja na “kundi dogo” la Wakristo wapakwa-mafuta, wote wanakuwa “kundi moja” chini ya Mchungaji Mwema. (Yohana 10:16; Luka 12:32) Wote wanafurahi kuitwa Mashahidi wa Yehova, wakiwa wamekusanywa katika umoja wa Ufalme wenye kuonekana kabisa!
Mbona Umoja wa “Ufalme”?
12. (a) Kwa sababu gani Ufalme wa Mungu unapasa kuwa kichwa chenye kuleta umoja maishani mwetu? (b) Kwa sababu gani twapaswa kufurahi ujapokuwa ukosefu wa umoja wa ulimwengu wenye kuongezeka?
12 Mbona tunasema, umoja wa Ufalme? Je! si wazi kwamba Ufalme wa Mungu ndio unaotajwa kuwa kichwa cha Biblia nzima? Basi je! Ufalme haupasi kuwa habari yenye kuleta umoja katika maisha yetu? Limekuwa jambo la kusisimua kuona utimizo wa ishara ya Yesu inayoonyesha kwamba Ufalme wake ulisimamishwa katika mbingu mwaka ule wenye matukio makubwa wa 1914. Naye Yesu ametuambia tushangilie kwa kuona mawingu meusi yaliyo mazito ya Har–Magedoni yakizidi kukusanyika pamoja tangu wakati huo. Yeye amekwisha kutuambia kwamba kile “kizazi” cha mwaka wa 1914—mwaka ambao ishara ilianza kutimizwa—“hakitapita, hata hayo yote yatakapotimia.” (Mathayo 24:34) Wengine wa “kizazi” hicho wangeweza kuendelea kuwa hai mpaka mwisho wa karne hii. Lakini kuna viishara. vingi vinavyoonyesha kwamba “mwisho” uko karibu kutukia kabla ya kumalizika kwa karne hii!
13. Kwa sababu gani sisi hatuna woga wa ulimwengu usio na umoja?
13 Nabii wa Yehova anazungumza juu ya msiba unaokaribia akisema: ‘Ungojee hautakawia.’ (Habakuki 2:3) Kwa sasa sisi hatuna ule woga wa ulimwengu usio na umoja, kwa maana sisi tumekwisha kufanywa wenye umoja duniani pote chini ya ule Ufalme. Ufalme wa Mungu, ambao tunasali, umeonekana. (Mathayo 6:9, 10) Na umoja wetu mtukufu umeonekana. Yote hayo yamekuwa kama yalivyotabiriwa na manabii wa Yehova wazamani.—Isaya 9:6, 7; Danieli 2:44; 7:13, 14,27.
“Mifupa Mikavu” Yarudishwa Kwenye Utendaji
14. Ni tamasha gani yenye kutokeza inayosimuliwa katika Ezekieli 37:1-4?
14 Kukamatana na hilo, ebu tuchunguze Ezekieli sura ya 37. Unabii huo unasema nini?
“Mkono wa [Yehova] ulikuwa juu yangu, naye akanichukua nje katika roho ya [Yehova], akaniweka chini, katikati ya bonde; nalo limejaa mifupa; akanipitisha karibu nayo pande zote; na tazama, palikuwa na mifupa mingi katika ule uwanda! nayo, tazama, ilikuwa mikavu sana. Akaniambia, Mwanadamu, je! mifupa hii yaweza kuishi? Nami nikajibu, Ee Bwana [Yehova], wajua wewe. Akaniambia tena, Toa unabii juu ya mifupa hii, uiambie, Enyi mifupa mikavu, lisikieni neno la [Yehova].”—Ezekieli 37:1-4.
15. Ni hali gani ya kisasa inayoonyeshwa hapa?
15 Ebu wazia hilo. Bonde zima likiwa limelundikana mifupa mikavu! Lakini, hiyo si tamasha ya jambo litakalotukia baada ya Har–Magedoni. Inafananisha jambo lililotukia mapema katika karne yetu. Hiyo ni kwa sababu mifupa hiyo inafananisha hali ya kukosa uhai, ya kukosa utendaji, ya watumishi wapakwa mafuta wa Mungu waliokuwa duniani wakati huo.
16, 17. Yehova aliahidi kufanya nini, na hilo lingekuwaje mwujiza?
16 Lakini Yehova alichukua hatua ya kurekebisha hali hiyo. Sikiliza maneno yake mwenyewe:
“Bwana [Yehova] aiambia mifupa hii maneno haya; Tazama, nitatia pumzi ndani yenu, nanyi mtaishi. Nami nitatia mishipa juu yenu, nami nitaleta nyama iwe juu yenu, na kuwafunika ngozi, na kutia pumzi ndani yenu, nanyi mtaishi; nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi [Yehova].”
Kwa hiyo inakuwa hai, “jeshi kubwa mno.”—Ezekieli 37:5-10.
17 Hapo Yehova alitimiza jambo ambalo hakuna mwanasayansi anayeweza kulinakili. Wanasayansi hawashindwi hata kidogo kunakili umbo la magofu ya miili ya kibinadamu kama yale tunayoona leo katika nyumba za kuhifadhia vitu vya kihistoria. Lakini ni mwanasayansi gani ameweza wakati wo wote kuongezea gofu la mwili wa mtu mishipa, nyama za kulifunika na kuliingiza pumzi ya uhai?
18. (a) Kwa sababu gani matazamio ya watu wa Mungu yalionekana kuwa yasiyo na matumaini mwaka 1918 na mapema mwaka 1919? (b) Kwa kupatana na unabii huo, Yehova aliwakumbukaje waaminifu hao?
18 Lakini mwujiza huo ulifanywa na Yehova Mungu katika historia ya kisasa ya Mashahidi wa Yehova. Wao walikuwa kama hiyo mifupa mikavu, wakawa wametawanywa wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Makao makuu yao huko Brooklyn yalikuwa yamefungwa, maafisa wa sosaiti yao ya uchapishaji wakawa wametiwa gerezani kwa vifungo vya miaka 20 na utendaji wao wa shambani ukasimamishwa. Huko nyuma mwaka wa 1918 na mapema mwaka wa 1919, hali yao ilionekana kuwa isiyo na matumaini. Lakini Yehova aliwakumbuka mabalozi hao waaminifu wa Ufalme. Mwaka wa 1919 yeye aliwafufua, sawasawa na alivyokuwa ametabiri kwenye Ezekieli 37:14:
“Nami nitatia roho yangu ndani yenu, nanyi mtaishi, nami nitawawekeni katika nchi yenu, nanyi mtajua ya kuwa mimi, [Yehova] nimesema hayo, na kuyatimiza, asema [Yehova].”
19. (a) Yehova amewarudisha watu wake jinsi gani na kwa kusudi gani? (b) Kwa sababu gani imekuwa lazima kupanua vifaa vya Sosaiti ulimwenguni pote?
19 Hivyo Yehova aliwarudisha watu wateswa kwenye nchi yenye ufanisi wa kiroho na kuwatayarisha wafanye kazi ya kutoa ushuhuda wa Ufalme ambao umeenea katika sehemu zote za dunia. Sasa, kila siku saa zaidi ya milioni moja zinatumiwa katika kuzitangaza habari njema. Ushuhuda mkubwa sana huo umeleta uhitaji wa lazima wa kupanua sana makao makuu ya Sosaiti katika Brooklyn na Wallkill, katika New York. Makao hayo yanafanya kazi kwa kushirikiana na viwanda vya matawi na afisi nyingi katika sehemu zote za ulimwengu katika kutoa Biblia, vitabu na magazeti, na vilevile msukumo wenye kuchochea, ili ‘habari njema hizi za ufalme . . . zihubiriwe katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.’—Mathayo 24:14, NW.
20. Ni jambo gani ambalo sasa limeonekana, na ni nani anayechukua sifa yote?
20 Ni nani anayechukua sifa yote kwa ajili ya umoja huo wa ajabu wa kufanya kazi pamoja? ‘Mimi nimeyatimiza, asema [Yehova].’ Hivyo umoja huo wa Ufalme umeonekana!
Ushahidi Wenye Kupanuka
21. (a) Mashahidi wa Yehova wamejithibitishaje kuwa kama Wakristo wa karne ya kwanza? (b) Ni mwaliko gani unaotolewa, na matokeo yamekuwa nini?
21 Ushahidi ule mkubwa unaendelea kupanuka katika sehemu zote za dunia, na mamilioni ya wamisionari waaminifu, mapainia na wafanya kazi wa makundi wanashiriki ushahidi huo. Kama Wakristo wa karne ya kwanza, mashahidi wa Yehova wa kisasa wamekuwa wakihubiri tumaini la habari njema “katika uumbaji wote ulio chini ya mbingu.” (Wakolosai 1:23, NW) Kwa kuthamini kwamba “[Yehova] ni Mungu mkuu, na Mfalme mkuu juu ya miungu yote,” sisi tunatolea watu wote wenye mioyo myeupe ukaribishaji huu: “Njoni, tuabudu, tusujudu, tupige magoti mbele za [Yehova] aliyetuumba.” Ni furaha namna gani kujua kwamba kila juma, kwa wastani, wapya zaidi ya 3,000 wanabatizwa na kuingizwa katika umoja wa kundi la yule Mchungaji Mwema! Sasa hao ‘wanamwabudu Baba katika roho na kweli.’—Zaburi 95:3-6; Yohana 4:23, 24.
22, 23. (a) Kwa sababu gani ni jambo la maana wenye mfano wa kondoo wawe na umoja? (b) Maandiko yanaelezaje umoja wetu na sababu ya umoja huo?
22 Katika hii siku ya hukumu ya Yehova juu ya ulimwengu wa Shetani uliogawanyika, ni jambo la maana sana sana watu wote hao walio mfano wa kondoo waliotoka katika mataifa yote wawe na umoja katika kutii ujumbe wa malaika aliye na “habari njema za milele za kutangaza,” akisema hivi kwa sauti kubwa: “Mwogopeni Mungu na kumpa utukufu, kwa sababu saa ya hukumu yenye kuletwa naye imefika, na kwa hiyo mwabuduni Yule aliyefanya mbingu na dunia na bahari na chemchemi za maji.” Je! wewe ni mmoja wa wale ambao wameingizwa katika huo umoja wa Ufalme?—Ufunuo 14:6, 7, NW.
23 Wale watangazaji wa Ufalme 2,500,000 wanaotumikia sasa katika nchi 205 ni kikundi chenye umoja kweli kweli! Roho takatifu ya Mungu inafanya kazi juu yao, nao wanazaa matunda ya roho hiyo. (1 Wakorintho 2:12; Wagalatia 5:22, 23) Ingawa wametolewa katika mataifa mengi mbalimbali, wao wanasema ile lugha moja safi ya kweli. (Sefania 3:9) Wanatumikia bega kwa bega—kwa umoja wa Ufalme!
24. Mistari ya 17 na 22 ya Isaya sura ya 60 imetimizwaje?
24 Wameondoa kati yao ukosefu wo wote wa umoja ambao huenda ulikuwako zamani na hasa tangu Yehova alipoingiza watu wake chini ya mpango wa kitheokrasi tangu mwaka wa 1938. Hilo lilikuwa kwa utimizo wa ahadi yake ya kiunabii iliyo kwenye Isaya 60:17 (NW): “Mimi nitaweka amani iwe kama waangalizi wako na uadilifu kama wenye kukugawia kazi.” Hata kujapokuwako uharibifu mwingi ulioletwa na Vita ya Ulimwengu ya Pili, pamoja na mateso ya ukatili yaliyotendwa juu ya Mashahidi wa Yehova wakati wa vita hiyo, kazi ya Ufalme ya watu wa Mungu wenye umoja imeendelea kukua na kupanuka, hivi kwamba katika nchi baada ya nchi kuzunguka ulimwengu imekuwa kweli kama ilivyotajwa kwenye Isaya 60:22: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa hodari; mimi, [Yehova], nitayahimiza hayo wakati wake.”
25. Ni nini kinachoshuhudia umoja wa Ufalme kwa njia ya ajabu?
25 Ni nani angewaza siku zile zenye magumu za vita ya ulimwengu ya pili, wakati kulipokuwa na Mashahidi wanaopungua 100,000 ulimwenguni pote, kwamba miaka ya mwanzo-mwanzo ya 1980 ingefika kukiwa na Mashahidi watendaji 70,000 katika Kanada na Ufaransa, 80,000 katika Japani, 90,000 katika Uingereza na zaidi ya 100,000 katika Italia, katika Mwungano wa Jamhuri ya Ujeremani, katika Nigeria, zaidi ya 130,000 katika Meksiko na zaidi ya 140,000 katika Brazili, na pia Mashahidi washikamanifu zaidi ya 250,000 katika nchi ambako kazi yetu iko chini ya marufuku kamili au ya kadiri fulani? Na majuzi United States (Amerika) iliripoti kuwa na Mashahidi watendaji 643,170. Huo ni ushuhuda mzuri ajabu wa kwamba kweli umoja wa Ufalme umeonekana!
Wewe Ungejibuje?
Ni ukosefu gani wa umoja unaoonekana katika sehemu kubwa tatu za tengenezo la ulimwengu la Shetani?
Umoja wa kweli uko tele wapi, na kwa sababu gani?
Unabii was Ezekieli 37:1-14 umetimizwaje?
Umoja wa Ufalme umetokeza ushahiid gani?
[Picha katika ukurasa wa 9]
Ukosefu mbaya sana wa umoja katika siasa za karne ya 20, biashara kubwa-kubwa na dini unatangulia kutekelezwa kwa hukumu ya kimungu
[Picha katika ukurasa wa 11]
Njozi ya Ezekieli ya “mifupa mikavu” iliyohuishwa inafananisha kurudishwa kwa watu wa Mungu kwenye fanaka ya kiroho