Wanadamu Wakiwa Wenye Umoja Ingekuwa Hivi
‘KAMA sisi ni Wahindu au Wakatoliki, Wayahudi au Walutheri, Wakweka au Waislamu au wafuasi wa Buddha, tukijaribu kutengeneza Dunia hii hii iwe kama mbinguni kwa juhudi nyingi inayolingana na ile tunayotia kwa ajili ya maisha yetu ya baadaye, ebu fikirieni tungeishi katika ulimwengu ulio mzuri kama nini.’
Mwamerika mmoja, Mel Ellis, aliye mwandikaji wa habari za magazetini alitumia maneno hayo kuonyesha tamaa ambazo watu wengi wanazo leo. Wanataka ulimwengu wenye kupendeza waishi ndani yake. Lakini wakati uo huo wanataka bado kushikilia migawanyiko yao ya kidini na ya kitaifa, na hayo hayo ndiyo mambo ambayo yameleta ugomvi mwingi sana na umwagaji wa damu katika muda wote wa historia.
Hata hivyo, dunia ingeweza kugeuzwa watu wakiwa wenye umoja katika kusudi lao. Tokeo moja la mara hiyo lingekuwa kwamba vita vingekoma. Halafu maneno kama “mashindano ya kuunda silaha” na “silaha za nyukilia zalundamana” hayangesikiwa tena. Miili ya kibinadamu haingelemazwa tena wala akili hazingepata jeraha vitani. Jamaa hazingepatwa tena na sikitiko la kuwapoteza wapendwa katika vita vya kutumia silaha.
Pesa zinazotumiwa kwa silaha na kujitayarisha kijeshi sasa zafikia dola bilioni 800 hivi kwa mwaka mmoja. Kama pesa zote hizo zingetumiwa kushughulikia mambo ya amani, loo! yangetokea mabadiliko ya namna gani hata katika hali za sasa za kutokamilika! Ebu wazia vitu ambavyo vingeandaliwa, nyumba zilizo za lazima, hospitali, shule, vifaa vyenye kuleta afya nzuri, maji safi na vitu vingine. Na yote hayo yangeweza kutokeza kwa urahisi kuajiriwa kazi kwa ukamili kwa wale wanaotengeneza vitu kwa ajili ya faida ya wanadamu. Pia, kama jamaa nzima ya kibinadamu ingefanya kazi pamoja kwa ajili ya faida ya wote, kungekuwa chakula tele kwa ajili ya wote. Mhariri wa gazeti Mfaransa, André Fontaine, alisema: “Kuna utajiri wa kumtosha kila mtu kama tutautumia tu kwa faida ya wanadamu.”
Basi fikiri faida ambazo zingetokana na kuwa na jamaa ya kibinadamu iliyoungana! Kungekuwa na ushirikiano wenye upendo badala ya mashindano yenye ukatili; huruma badala ya chuki ya moyo mkavu; amani yenye kujenga badala ya jeuri ya kishenzi; kuheshimiana kwa njia yenye mwungano badala ya utukuzo wa taifa wenye kugawanya watu.
Lakini mabadiliko hayo yangeweza kutimizwaje? Ni lazima yaanze katika akili za wanadamu. Na ili kubadili akili ni lazima kuwe na badiliko kamili la elimu ya kiadili na ya kiroho ili kuondolea wanadamu mavutano yote yanayowagawanya. Lakini ni wapi leo inakopatikana aina hiyo ya elimu yenye kuunganisha watu? Je! ni katika mifumo ya kisiasa, ya kiuchumi, ya kidini au ya kielimu ya ulimwengu huu?
Biblia inatupa sisi jibu la wazi katika maneno ya nabii Yeremia: “Ee [Yehova], najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.”—Yeremia 10:23.
Kauli hiyo inaungwa mkono na Mark Thee, mkurugenzi Mnorowei wa Taasisi ya Uchunguzi wa Amani ya Kimataifa aliyesema hivi: “Hali ya leo ya kimataifa ni yenye hatari kubwa yenye kupenya karibu sehemu zote za utendaji wa kibinadamu: za kiuchumi na kijamii, za kisiasa na kijeshi, za kiroho na kiadili. Hali zenye kuhitilafiana zinazidi kuongezeka. Jeuri inaongezeka. Kutumia nguvu kumeenea sana katika jitihada za usimamizi wa mambo na za kuleta masikilizano kati ya watu. . . . Kunazidi kuwa na mashaka mengi juu ya uwezekano wa kuleta amani kwa kupunguza vita.”
Basi, je, haiko wazi kwamba wanadamu, wakijitegemea wenyewe, hawana majibu kwa sababu wanakosa hekima ya kuongoza hatua yao wenyewe kuelekea umoja wa dunia yote? Ni kweli, wengine huenda wakawa na maoni kwamba huko ni kutia chumvi na kwamba wanadamu kwa kujitegemea siku fulani wangeweza kuleta umoja. Hata hivyo maandishi yanaonyesha nini? Je! yanatupa msingi wo wote wa kuwa na tumaini kwamba kitu kimoja au zaidi katika ulimwengu huu kingeweza kuwa nguvu ya kuleta umoja wa ulimwengu? Kama sivyo, ungeweza kuletwa na nini?
[Picha katika ukurasa wa 4]
Ebu fikiri ni mambo gani yangeweza kufanywa hata sasa ikiwa pesa zote zinazotumiwa kwa silaha zingetumiwa kutengeneza ulimwengu wenye amani!