Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 8/15 kur. 5-8
  • Je! Umoja Unaweza Kutokana na Ulimwengu Huu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Umoja Unaweza Kutokana na Ulimwengu Huu?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Matendo ya Kisiasa
  • Mvurugo wa Kiuchumi
  • Matatizo ya Jamii ya Watu Yanazidi
  • Ni Wapi Tunapoweza Kuona Umoja Katika Ulimwengu Huu Wenye Ugomvi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Wanadamu Wakiwa Wenye Umoja Ingekuwa Hivi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Je! Wanadamu Wanaweza Kuleta Amani na Usalama Wenye Kudumu?
    Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
  • Umoja wa Ufalme Umeonekana Leo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 8/15 kur. 5-8

Je! Umoja Unaweza Kutokana na Ulimwengu Huu?

JE! NDOTO ya kutaka umoja wa ulimwengu ingeweza kutimizwa na jitihada za ulimwengu huu? Je! inawezekana kwamba mojapo watu wenye kuongoza mambo ya ulimwengu angeweza kuelekeza wanadamu kwenye mradi huo?

Ulimwengu huu umekuwa na maelfu ya miaka ya kujaribia serikali mbalimbali, na pia mifumo ya kiuchumi na kijamii? Je! yo yote kati ya hiyo imepata kuwa nguvu ya kuleta umoja? Je! yo yote kati ya hiyo ingeweza kuondoa hali yenye msiba ya kukosa umoja ambayo jamaa ya kibinadamu imo ndani yake? Ikiwa sivyo, ni nini kinachoweza?

Matendo ya Kisiasa

Nguvu kubwa katika mambo ya kibinadamu ni viongozi wa kisiasa. Lakini, kwa kusikitisha, historia inaonyesha wazi kwamba hawajawa nguvu ya kuwafanya watu wawe wenye umoja. Tofauti yake, baada ya maelfu ya miaka ya kujaribu kila namna ya maongozi ya kisiasa, ulimwengu umegawanyika zaidi ya wakati mwingine. Sasa kuna mataifa mengi zaidi yaliyo huru na aina tofauti za mifumo ya kisiasa kuliko wakati mwingineo wote katika historia.

Ikiwa serikali ya kibinadamu ingekuwa nguvu ya kuleta umoja wa ulimwengu, hakika ingalipaswa kuwa imekwisha kuonyesha hivyo kufikia sasa. Badala yake, kila karne imepakwa doa la damu ya vita moja baada ya nyingine​—maelfu ya vita. Na tofauti kabisa na kuwa na maendeleo ya hatua kwa hatua kuelekea umoja katika nyakati za kisasa, karne yetu ya 20 imekuwa ndiyo ambayo kwa msiba imegawanyika zaidi ya zote. Vita vya ulimwengu viwili vyenye kuogopesha sana vimepiganwa, na uhai milioni 70 hivi ukakatishwa. Isitoshe, kitabu cha majuzi War in Peace kinatangaza kwamba tangu Vita ya Ulimwengu ya Pili mapigano ya kijeshi 130 hivi katika nchi zaidi ya mia moja yameua watu milioni 35 hivi. Fikiria hilo! Na hilo limetokea katika wakati unaoitwa ni wa amani ati!

Sababu kubwa ya hali hii yenye kuhuzunisha sana ni kushikilia kwa wanadamu ushikamanifu wao wa mambo ya kikale ya kisiasa na kitaifa. Mambo hayo yameiweka jamaa ya kibinadamu katika hali ya kugawanyika kabisa kabisa na kupingana-pingana. Ndiyo sababu mwanahistoria Arnold Toynbee alisema kwamba utukuzo wa taifa “umekuwa ndiyo dini kubwa kuliko zote,” kwa kuwa watu wengi wanaabudu kwa utii wao utukuzo wa taifa. Toynbee alisema kwamba ibada hiyo ya serikali zenye enzi kuu zinagombanisha washiriki wazo “kwa sababu dini hiyo ni wonyesho wa ubinafsi.” Na yeye alikuwa na maoni kwamba “ubinafsi ndicho chanzo cha ugomvi wa namna zote.”

Migawanyiko ya kisiasa imekuwa yenye kusikitisha hata zaidi sasa kwa sababu tumekwisha kuingia sana katika kile kizazi chenye makombora ya nyukilia. Vita vya kutumia makombora ya nyukilia inaogopwa katika kila taifa, hasa tunapofikiria maangamizi yanayoweza kuletwa na silaha za nyukilia leo. Katika kichapo The Fate of the Earth, Jonathan Schell anaandika hivi: “Inapolinganishwa na kadiri ulimwengu umejitayarishia sasa silaha za kinyukilia, kilichotukia Hiroshima kilikuwa kidogo sana hata kuliko kisehemu kimoja cha milioni ya maangamizi makubwa.”

Schell aliongeza hivi: “Kwa hiyo, siasa zimebaki zikielekeana daima na upumbavu huu: kwa mkono mmoja zinajenga mambo ya wakati ujao ambayo mkono ule mwingine unajitayarisha kuyabomoa. Kila wakati mwanasiasa ana[po]inua sauti yake anene habari za ulimwengu bora kwa ajili ya watoto wetu na wajukuu wetu . . . ile hatari ya kuangamia inampinga kwa jibu hili la kumvunja moyo sana: Huenda wakati ujao kusiwe na watoto wala wajukuu.”

Yaliyotabiri hali hii hii kwa ajili ya siku zetu ni maneno ya kiunabii ya Yesu Kristo katika Luka 21:25, 26, NW: “Duniani huzuni kuu ya mataifa, wasijue njia ya kutokea kwa sababu ya uvumi wa bahari na msukosuko wake, huku wanadamu wakizimia moyo kwa sababu ya hofu na kwa kutazamia mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa na watu.” Hayo ni masimulizi yanayofaa kama nini juu ya hali ya mgawanyiko ya wakati huu ya wanadamu!

Kwa sababu ya kutazamia mambo hayo yenye kutia hofu, huenda ulizo liulizwe hivi: Kwa kuwa hakuna mfumo wo wote mmoja wa kisiasa unaoweza kufanya jamaa ya kibinadamu iwe na umoja, je, Umoja wa Mataifa unaweza kufanya hivyo? Lazima jibu liwe hapana. Kwa sababu gani? Kwa sababu, kwa kweli, UM ni wonyesho tu kwamba ulimwengu wetu ni wenye ugomvi. Katibu-mkuu wa UM alikubali hivi: “Hakika tumeiacha kabisa Katiba ya U.M.” Yeye alisema kwamba maazimio ya baraza hilo “yanazidi kukaidiwa au kupuuzwa na wale wanaojiona kwamba wao wenyewe wana nguvu za kutosha kufanya hivyo.” Basi, akamalizia: “Sisi tunakaribia kwa njia yenye hatari fujo-fujo mpya za kimataifa za kutokutii utawala.” Hivyo, kulingana na matendo ya huo, kuaminika kwa UM kunatiliwa mashaka hata na maafisa wenyewe.

Kwa hiyo, tukiyakubali mambo kama yalivyo, ni lazima tuseme kwamba matendo ya kihistoria yanaonyesha hakuna mfumo wo wote wa kisiasa duniani unaoweza kufanya wanadamu wawe na umoja, hata viongozi wawe wanyofu namna gani. Kwa kufaa, katika Zaburi 146:3 Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho yake linashauri hivi: “Msiwatumainie wakuu, wala binadamu ambaye hakuna wokovu kwake.”

Mvurugo wa Kiuchumi

Je! tunaweza kutumaini mfumo wo wote wa kiuchumi wa ulimwengu huu kuwa nguvu yenye kuleta umoja, ili jamaa nzima ya kibinadamu iweze kufaidika na uwezo wa dunia wa kuzalisha kwa wingi? Kwa mara nyingine, matendo ya historia yanajibu hapana. Hakuna hata mfumo mmoja wa kiuchumi wa wanadamu umeweza kutoa kielelezo cha kufuatwa kwa umoja ili mambo yaliyo ya faida kabisa kwa wanadamu yatimizwe. Kila mfumo wa kiuchumi umeletea mamilioni wengi hali ya kutoridhika na magumu.

Katika miaka ya karibuni kumekuwako hatari moja baada ya nyingine katika uchumi wa dunia yote. Madeni ya nchi ambazo hazijasitawi yamekuwa makubwa sana, lakini uwezo wazo wa kulipa haukukua. Hata madeni ya mataifa mengi yaliyositawi yamekuwa makubwa sana. Umaskini umeenea sana. Mamilioni hawana kazi ya kuajiriwa. Kila mwaka mamilioni mengine wanaendelea kufa kwa njaa au maradhi yanayoletwa na ukosefu wa chakula kinachofaa. Kwa umati mkubwa wa watu maskini duniani pote, ukweli wa neno la kiunabii la Mungu katika Ufunuo 6:6 umethibitishwa: “Kibaba cha ngano kwa mshahara wa siku nzima.” (The New English Bible) Ndiyo, katika sehemu nyingi mshahara wa siku moja unanunua karibu kipande cha mkate tu.

Zijapokuwa nafuu zinazopatikana baada ya uchumi kupunguka au kushuka, hali ya kiuchumi inaendelea kuwa kama ile inayoripotiwa na gazeti The New York Times: “Ukamatano na fanaka ya uchumi wa ulimwengu unaelekewa na tisho lililo baya zaidi katika kipindi cha baada ya vita vikuu. Infuleshoni, kuharibika kwa hali ya uchumi, ukosefu mkubwa wa kazi ya kuajiriwa, mikazo inayozidi kiasi ya kibiashara na kifedha inalemea sana kanuni za mwenendo na mashirika ya jumuiya ya mataifa yote ya kiuchumi.” Na mhariri wa gazeti Mfaransa, André Fontaine alitangaza hivi: “Mimi sioni Serikali yo yote katika ulimwengu wa leo inayoonekana kuwa inaweza kuyatatua yale matatizo makubwa-makubwa ya kiuchumi ya wakati wetu. Sababu ni kwamba hayo ni matatizo yanayohusu ulimwengu kwa ujumla, na hakuna nchi moja inayoweza kuyatatua ikiwa pekee”

Hapo ndipo penye kiini cha jambo lenyewe. Ili kutatua matatizo ya kiuchumi ya ulimwengu, tendo lenye umoja linatakwa. Lakini kuna mapendezi mengi mno ya kichoyo hivi kwamba hakuwezi kuwako utatuzi wo wote wa daima.

Matatizo ya Jamii ya Watu Yanazidi

Matatizo ya jamii ya watu yanaonyesha pia kwamba wanadamu hawana umoja. Chuki na ubaguzi, uhalifu na jeuri, uharamia na mapigano ya kutumia silaha​—katika kontinenti zote​—ni dalili za ulimwengu mgonjwa. Maisha katika majiji mengi hasa yamekuwa hatari. Kwa hiyo, wakati afisa wa polisi katika Italia alipojaribu kumtia moyo mfungwa mmoja kwa kumwambia kwamba huenda akafunguliwa karibuni, jibu la kushangaza la mfungwa huyo lilikuwa, kama ilivyoripotiwa na kichapo La Nazione: “Sijali kufunguliwa. Hizi ni nyakati za magumu. Mimi napendelea kukaa gerezani. Ni rahisi sana mtu kuuawa akiwa huko nje.”

Pia kuna udhaifu wa kibinadamu unaogawanya jamaa na kuharibu ubora wa maisha katika kila namna ya mfumo wa kisiasa. Talaka zinaongezeka karibu kila mahali; katika sehemu nyingine karibu nusu ya ndoa zote zinaishia katika talaka. Pia uepukaji wa matatizo ya maisha kwa kunywa kupindukia unaharibu nchi za Mashariki na za Magharibi vilevile. Tokeo moja ni kwamba kila siku watu wanaoendesha motokaa wakiwa wamelewa wanaongeza hesabu ya watu wanaouawa ulimwenguni ambayo ni vifo kama 300,000 kila mwaka.

Pigo la kuzoelea dawa za kulevya limeletea mamilioni huzuni. Uendekevu wa kuachilia matendo ya ngono yenye kuenea sana unaletea watu wengi sana magonjwa yenye kuogopesha ya kisonono na kaswende, mengine sasa yanashinda dawa nguvu. Kuongezea hilo ni wimbi kubwa la mimba zisizotakwa na kuharibu mimba.

Hali iko sawa kabisa na ilivyotabiriwa na unabii wa Biblia kuhusu kipindi hiki wakati iliposema: “Siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari.” Unabii huo umepanga hali ambazo zasikika kama kwamba unasoma gazeti lako la kila siku. Ulionyesha kwamba watu wangekuwa ‘wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kiburi, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasiojizuia, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu.’​—2 Timotheo 3:1-5.

Matatizo ya kijamii yanaharibiwa zaidi na jambo la kwamba dola zaidi ya bilioni 800 kwa mwaka zinatumiwa kutengeneza silaha. Hiyo ni zaidi ya dola bilioni mbili kwa siku! Hata hivyo, mamilioni ya watoto wanakufa kila mwaka kwa sababu ya kukosa chakula kinachofaa, na watu wazima pia. Basi, hatuwezi kuepuka ukweli unaohusu jambo hilo: matatizo ya kijamii na kutendewa kwa watu kwa njia zisizolingana yanaongezeka. Mamia ya mamilioni ya watu wanaoonewa wanajikuta wakiwa hawana tumaini lo lote. Na hakuna mfumo wa kijamii wo wote wa ulimwengu huu unaoweza kutatua matatizo hayo kwa kuwa hakuna hatua ya umoja ya kuyaelekea.

Hakika, kufikia sasa ni wazi kwamba hakuna mfumo wo wote wa kisiasa, kiuchumi au kijamii wa ulimwengu huu unaoweza kuwa nguvu ya kuletea wanadamu umoja. Lakini namna gani dini za ulimwengu huu? Je! tunaweza kuzitumainia kuwa kitu chenye kuleta umoja? Kweli kweli, ni nini hasa tunaweza kutumainia kuwa nguvu ya kuletea umoja jamaa ya kibinadamu iliyogawanyika kwa njia ya kusikitisha? Makala mbili zifuatazo zitazungumza juu ya maulizo hayo.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Sasa wanadamu wanao uwezo wa kuharibu uhai wote duniani

[Picha katika ukurasa wa 8]

Mamia ya mamilioni wanakufa njaa

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki