Maswali Kutoka kwa Wasomaji
■ Kwa kuwa Biblia inataja wanaume fulani kuwa‘watiwa mafuta’ kwa sababu walikuwa wamechaguliwa kwa njia ya pekee, au wakawekwa, na Mungu, waangalizi wote leo wangeweza kuitwa ‘watiwa mafuta’?
Maneno ya Kiebrania na Kigiriki ya ‘kutia mafuta’ yana wazo la kukandika, au kupaka, kama kwa mafuta. Maneno ‘kutia mafuta’ yangeweza kutumiwa pia wakati roho takatifu ilipomiminwa juu ya mtu, kama vile Yesu na Wakristo ambao Mungu anachagua wawe warithi-washirika wake,—Mwanzo 28:18, 19; 31:13; Zaburi 133:2; 45:7; Isaya 61:1; Luka 4:18; Waebrania 1:9; Waefeso 1:13, 14.
Nyakati nyingine Biblia inatumia maneno ‘kutiwa mafuta’ kuhusu mtu aliyechaguliwa, au akawekwa, kwa daraka au cheo cha pekee. Kwa mfano, Eliya alipaswa ‘kumtia mafuta Hazaeli awe mfalme wa Shamu’ na ‘Elisha awe nabii mahali pako.’ (1 Wafalme 19:15, 16) Hata hivyo, hakuna kumbukumbu la kuonyesha kwamba walitiwa mafuta halisi, kama Yehu. (2 Wafalme 9:1-6) Kwa wazi Koreshi yule Mwajemi hakumiminiwa mafuta halisi wala roho takatifu, lakini aliitwa mtiwa mafuta wa Yehova kwa sababu aliagizwa kwa njia ya pekee kwa ajili ya daraka la waziwazi. (Isaya 45:1) Vivyo hivyo, Musa angeweza kutajwa kuwa “Kristo [mtiwa mafuta]” kwa sababu Mungu ndiye aliyemwagiza, akamweka kwa njia ya pekee,—Waebrania 11:26.
Namna gani wazee, au waangalizi, katika makundi ya mahali? Kwenye Matendo 20:28 mtume Paulo aliambia wazee wa kundi kwamba “roho takatifu imeweka ninyi kuwa waangalizi.” (NW) Hayo yalisemwa katika wakati ambao Wakristo wote waliobatizwa ambao Mungu aliwakubali walikuwa wakitiwa mafuta kwa roho takatifu na kuitwa kwenye uzima wa kimbingu,—2 Wakorintho 1:21,22; 1 Yohana 2:20, 27.
Lakini, katika kusema kwamba “roho takatifu imeweka ninyi kuwa waangalizi,” Paulo hakutumia neno la Kigiriki la kutia mafuta. Alitumia namna ya neno tithemi, linaloweza kumaanisha tia, weka mahali, simamisha mahali, weka kwenye cheo.—Linganisha Marko 4:21; 16:6; 1 Wakorintho 3:10; 9:18; 15:25; 2 Timotheo 1:11; Waebrania 1:2.
Ni kweli kwamba Mungu anatumia roho takatifu yake katika kuweka, kuagiza, au kutia, wazee katika vyeo walivyogawiwa. Lakini haingefaa kutaja waangalizi wa makundi kuwa watiwa mafuta. Kufanya hivyo kungeleta mvurugo, kutokeze wazo lenye makosa kwamba wazee wote wametiwa mafuta kwa roho takatifu na wana mwito wa kimbingu. Kwa kweli, kiasi kikubwa cha waangalizi waaminifu katika makundi leo wana tumaini la kupata uzima wa milele katika Paradiso ya kidunia itakayorudishwa, ingawa wamewekwa kuwa wazee.