Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 11/1 kur. 12-16
  • Sasa Ndio Wakati wa Kufanya Utumishi wa Bidii

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sasa Ndio Wakati wa Kufanya Utumishi wa Bidii
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mifano Yenye Kichocheo
  • Misaada ya Kutupa Uvumilivu
  • Mifano ya Wenye Kufanya Utumishi kwa Bidii
  • Mfumo Wafikia Mwisho
  • Wenye Bidii Katika Imani
  • Wingu Kubwa Sana la Mashahidi!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • “Fanyeni Mioyo Yenu Kuwa Imara”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Yehova Hutimiza Ahadi Zake kwa Waaminifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • ‘Kutembea kwa Imani, Si kwa Kuona’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 11/1 kur. 12-16

Sasa Ndio Wakati wa Kufanya Utumishi wa Bidii

“Atakayevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.”​—MARKO 13:13, Habari Njema kwa Watu Wote.

1, 2. (a) Ni hali gani zinazoonyesha wazi kwamba tunaishi kwenye mwisho wa huu mfumo wa mambo? (b) Ungeweza kuwa na maitikio gani mawili?

WATU wengine wangali wanatia shaka kwamba tunaishi kwenye mwisho wa mfumo uliopo, ingawa ni vigumu kuwazia ni kwa sababu gani wanatia shaka juu ya uhakika huo. Adili zinaharibika. Hali za kiuchumi zinakuwa mbaya zaidi. Jeuri inazidi. Ongezeko kubwa sana la watu linaendelea, uchafuzi wa mazingira unaongezeka, takataka inayotokana na atomu inaongezeka, silaha za atomu zinazidi na wasioamini mara nyingi wanauliza kama uhai utaendelea duniani.

2 Hata hivyo, mwisho wa huu mfumo wa kale haujafika bado. Wakristo fulani walio wakfu huenda wakawa wamechoka kufanya utumishi wa Ufalme. Basi, ikiwa ye yote aliweka wakfu maisha yake si kwa Mungu, bali kwa tarehe fulani, huenda akawa amekwisha kuondolewa. Lakini wale walioweka wakfu maisha zao kwa Yehova Mungu, sikuzote wafanye mapenzi yake na kufuata njia zake, ni wenye nguvu zaidi ya wakati mwingineo wote na hesabu zao zinaendelea kukua.

3. (a) Kwa sababu gani wapenda-uadilifu wanataka kuona sana mfumo huu wa kale ukifikia mwisho? (b) Mpaka utakapofikia mwisho, tunapaswa kuwa tukifanya nini?

3 Watu wanaopenda uadilifu wanataka sana kuona mfumo huu wa kale ukiisha, kwa maana mahali pake patachukuliwa na Paradiso ya kidunia, na Utaratibu Mpya wenye uadilifu ambao Biblia inaahidi. (Isaya 9:6, 7; Mathayo 6:9, 10; 2 Petro 3:13; Ufunuo 21:1-4) Bila shaka, watumishi wa Yehova wanataka badiliko hilo lije mara tu yakiwa mapenzi ya Mungu. Lakini, wakiwa walijiweka wakfu kikweli kwa Mungu, kwa saburi wanangojea wakati wake huku wakisonga mbele kwa bidii katika kazi yenye kusisimua ya kuhubiri Ufalme ambayo amewapa wafanye.​—Mathayo 24:14.

Mifano Yenye Kichocheo

4. Ni mfano gani mzuri uliowekwa na wanaume na wanawake wa imani katika nyakati za kale?

4 Hakuna sababu kwa ye yote kurudi nyuma, kulegea, au kuchoka. Yehova Mungu na Kristo Yesu ni wafanyi kazi. (Yohana 5:17) Zaidi ya hayo, Biblia imejaa masimulizi ya wanaume na wanawake wenye imani ambao walifanya kazi kwa bidii na kwa furaha, nao ni mifano yenye kutuchochea na kututia nguvu. Hata hivyo wengi wa wanaume na wanawake hao waaminifu walijua kwamba ahadi hizo walizongojea hazingetimizwa wakati wa maisha yao. Vizazi vingi, katika visa vingine hata maelfu ya miaka, yangepita kabla mambo waliyongojea hayajatimizwa. Hata hivyo hawakulegea katika utendaji wao. Wengi walitumikia kwa furaha mpaka wakawa wazee sana, wakiwa imara katika imani, wenye bidii katika kumtii Mungu, na kungojea kwa subira utimizo wa makusudi yake. Na zaidi, karne zilipokuwa zikipita, Mungu alitoa ufunuo wake hatua kwa hatua. Kwa hiyo, wanaume hao wa imani wa kale walikuwa na maarifa machache sana ya jinsi Mungu angetimiza mambo aliyokuwa ameahidi, machache zaidi ya unayoweza kuwa nayo leo.

5. Habili aliweka mfano gani?

5 Kwa mfano, fikiria jinsi Habili alivyokuwa na habari chache. Alilojua ni kwamba tu Mungu alikuwa ameahidi “uzao” fulani na kwamba wakati fulani ujao “uzao” huo ungeponda kichwa cha nyoka. (Mwanzo 3:15) Hata hivyo Yesu alimwita Habili “mwenye haki,” naye anatajwa kwanza katika orodha ya Paulo ya watu wa imani wenye kutokeza. (Mathayo 23:35; Waebrania 11:4) Je! wewe ungaliweza kuwa na imani hiyo ukiwa na habari chache tu zilizopatikana wakati wa Habili?

6, 7. Ijapokuwa ahadi fulani zilizotolewa na Mungu hazikutimizwa katika siku za Ibrahimu, yeye alituwekeaje mfano mwema?

6 Nuhu, Ibrahimu, Isaka na Yakobo wote waliishi kabla Yehova hajaonyesha uwezo wake mkubwa ajabu wakati wa Israeli kutoka Misri. Hawakujua lo lote juu ya matukio yenye kutisha ambayo yangekuwako wakati wa kutolewa kwa Torati katika Sinai. Walipokuwa hai, hata kitabu cha kwanza cha Biblia hakikuwa kimeandikwa.

7 Ibrahimu hakuwa na tumaini kwamba Paradiso ingerudishwa duniani wakati wa maisha yake. Badala yake, aliambiwa kwamba uzao wake ungeteswa kwa miaka 400. Ni baada ya wakati mrefu ujao ndipo ahadi ya Mungu ingetimizwa kwamba ‘katika uzao wa Ibrahimu mataifa yote ya dunia watajibarikia.’ (Mwanzo 15:13; 22:18; Wagalatia 3:8) Ibrahimu alikuwa “akitazamia mji wenye msingi, ambao mwenye kuubuni na kuujenga ni Mungu.” (Waebrania 11:10) Uhakika wa kwamba Ibrahimu angeuona si katika siku zake bali katika ufufuo tu haukudhoofisha imani yake, utii na bidii katika kumtumikia Mungu. Huenda tukajiuliza wenyewe hivi: Je! mimi nina imani, utii na bidii aliyokuwa nayo Ibrahimu?

8. Tunajifunza nini kuhusu subira na uvumilivu wa Musa?

8 Musa alifikiri kwamba hangeweza kufanya kazi ambayo Mungu alimgawia. Alisema kwamba yeye hakuwa msemaji mwenye ufasaha na alikuwa na maoni kwamba wala watu wake mwenyewe wala Farao hawangemsikiliza. (Kutoka 4:1, 10; 6:12) Hata hivyo Musa alitii. Alifanya aliyoambiwa na Yehova, na alifanya hivyo kwa muda mrefu sana. Katika jangwa Musa alijua kwamba ingekuwa miaka mingine 40 kabla ya watu wake kuingia katika Nchi ya Ahadi, na kwa sababu ya dhambi yake ya baadaye aliambiwa kwamba hangeingia katika nchi hiyo hata baada ya kipindi hicho. Hata hivyo mwaka baada ya mwaka aliendelea katika njia ya Yehova. (Hesabu 14:33, 34; 20:9-12; Kumbukumbu la Torati 3:23-28; 34:1-6) Je! upendo wako kwa Mungu ungaliweza kutokeza subira na jitihada hiyo katika utumishi wake? Je! wewe ungaliweza kuwaongoza wengine kwa uaminifu kuelekea lengo ambalo ulijua wewe mwenyewe haungelifikia?

9, 10. Isaya na Yeremia walionyeshaje uvumilivu, bila tumaini la kupokea thawabu yenye kutamanika wakati wa maisha yao?

9 Yehova alipouliza ni nani angeweza kwenda aseme kwa ajili yake, Isaya alisema: “Mimi hapa, nitume mimi.” (Isaya 6:8-11) Kwa miaka zaidi ya 40 alitumikia akiwa nabii wa Yehova. Kati ya mambo mengine, Isaya alipokezana ahadi ya Mungu ya “mbingu mpya na nchi mpya,” ingawa hakukuwako tumaini lo lote kwamba kungekuwa mfumo mpya wenye uadilifu katika wakati wa maisha yake. (Isaya 65:17-25) Je! wewe ungaliweza kuwa mwaminifu hivyo kwa sababu tu kudumisha uaminifu lilikuwa jambo la haki na lenye kupatana na upendo wako mwingi kwa Mungu?

10 Yeremia alitumiwa kutangaza maonyo yasiyopendwa na watu wengi. Aliyatangaza kwa watu wasioamini. Hakuna Paradiso yo yote ya kidunia iliyongojewa baada ya kuhubiri kwake. Badala yake, Yerusalemu alioupenda ungekuwa “ukiwa, na kitu cha kushangaza,” uharibiwe kwa ajili ya wakaaji wake kukosa imani. Yeremia alijua kwamba kungalikuwako kurudishwa upya, lakini hakungetokea mpaka baada ya miaka 70—baada ya kipindi kingine ambacho ni karibu maisha ya kawaida ya mtu! (Yeremia 25:8-11; 29:10) Uhakika wa kwamba hangeishi aone kurudishwa huko kulikotabiriwa haukumzuia Yeremia asihubiri. Hata alipojaribu kuacha, neno la Yehova lilikuwa “kama moto uwakao” katika mifupa yake. Akalazimika kusema tu, na Yehova alikuwa pamoja naye “mfano wa shujaa mwenye kutisha.”​—Yeremia 20:7-11.

Misaada ya Kutupa Uvumilivu

11, 12. Biblia inaonyesha nini ambayo mifano ya kale ya imani inapasa kutusukuma tufanye?

11 Mtume Paulo alionyesha matokeo ambayo mifano hiyo yapasa kuleta juu yetu. Aliandika hivi: “Sisi tunalo kundi hili kubwa la mashahidi mbele yetu. Kwa hiyo tuondoe kila kizuizi kinachotuzuia, na dhambi [ukosefu wa imani] ile inayotung’ang’ania. Tupige mbio kwa uvumilivu katika mashindano yaliyowekwa mbele yetu.”​—Waebrania 12:1, HNWW.

12 Pia Paulo aliandika hivi: “Kwa kuwa yote yaliyotangulia kuandikwa yaliandikwa ili kutufundisha sisi; ili kwa saburi na faraja ya maandiko tupate kuwa na tumaini. Na Mungu mwenye saburi na faraja awajalie kunia mamoja ninyi kwa ninyi, kwa mfano wa Kristo Yesu.” (Warumi 15:4-6) Kwa hiyo mifano hiyo ya kale ya imani yapasa kutuchochea tuvumilie, tushikamane na mgawo wetu wa kuhubiri na kufundisha, na hivyo tumtukuze Yehova kwa bidii, aliye Mungu wa Bwana yetu Yesu Kristo.

13. Sisi tunajua nini ambacho watu wa imani wa kale hawakupata kamwe nafasi ya kukijua?

13 Ebu fikiria mambo yenye kutia nguvu imani tunayojua ambayo manabii waaminifu wa kale hawakujua. Walipokuwa hai, hakuna ye yote aliyejua Masihi angekuwa nani. Lakini si kwamba tu sisi tunajua yeye ni nani; bali pia tunajua juu ya kuzaliwa kwake, kufundisha, kifo na kufufuliwa kwa Huyo, Yesu Kristo. Zaidi ya hayo, tunajua juu ya ukombozi, Ufalme na “uzao” ambao watu hao walikuwa wamengojea kwa uaminifu. Zaidi ya hayo, tuna Maandiko yote ya Kigiriki ya Kikristo​—kuanzia Mathayo mpaka Ufunuo. Nasi tuna nafasi ya kuelewa kitabu hicho kizuri ajabu cha Ufunuo, chenye unabii wenye kutia nguvu imani unaotimizwa katika wakati wetu na ambao ungali utatimizwa. Kweli kweli, tunaishi katika wakati wa maana sana wenye kusisimua​—wakati ambao watu hao wa kale walingojea kwa hamu nyingi.

Mifano ya Wenye Kufanya Utumishi kwa Bidii

14, 15. Je! uhakika wa kwamba Ufalme ulikuwa ungali jambo la wakati ujao uliwavunja moyo Wakristo wa karne ya kwanza? Eleza.

14 Wafuasi wa kwanza wa Yesu walikosa subira juu ya kuona Ufalme ulioahidiwa. Walimuuliza Yesu hivi: “Je! Bwana, wakati huu ndipo unapowarudishia Israeli ufalme?” Wakati huo wanafunzi hao hawakutambua kwamba Ufalme huo ungekuwa wa kimbingu. Wangekuja kuelewa hilo baadaye chini ya uongozi wa roho ya Mungu. Lakini Yesu akawajulisha kwamba walikuwa na kazi kubwa ya kufanya. Alisema kwamba wangekuwa “mashahidi [wake] katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa [dunia].” (Matendo 1:6-8) Kazi hiyo haikuonekana kuwa kubwa mno kuweza kufanywa. Katika siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K., wanafunzi 120 hivi, chini ya uongozi wa roho takatifu, walianza kuhubiri habari njema. Watu 3,000 hivi walilishika hilo neno siku hiyo! Na baada ya muda mfupi kuhani mkuu wa Kiyahudi angeweza kusema: “Tazameni, mmeijaza Yerusalemu mafundisho yenu.”​—Matendo 2:41; 5:28.

15 Watu waliokuwapo wakati huo katika Yerusalemu waliotoka sehemu mbalimbali za Ulaya, Esia na Afrika yaelekea walipeleka habari njema katika nchi zao wenyewe. (Matendo 2:5-11) Muda si muda Paulo akawa anahubiri kwa bidii na kusaidia kuanzisha makundi ya Kikristo katika jimbo lote la Roma la Esia na katika Ugiriki. Alisonga mbele mpaka Roma na yawezekana hata mpaka Spania. Petro alienda upande mwingine, mpaka mbali kule Babuloni. Baada ya miaka inayopungua 30 ya utendaji wa Wakristo hao wa kwanza na umati mkubwa wa watu waliofundisha, Paulo angeweza kusema kwamba habari njema zilikuwa ‘zimehubiriwa katika uumbaji wote ulio chini ya mbingu.’ (Wakolosai 1:23, NW) Lo! walifanya kazi kama nini, wakitii kwa bidii amri ya Yesu ya kufundisha wengine!—Mathayo 28:19, 20; Tito 2:13, 14.

Mfumo Wafikia Mwisho

16. Wakristo wa kwanza walikuwa wakitazamia tukio gani?

16 Lakini, kulikuwako kipindi chenye maana ya pekee kwa Wakristo wa karne ya kwanza. Yesu alikuwa amesema: “Hapo mtakapoona mji wa Yerusalemu umezungukwa na majeshi, ndipo jueni ya kwamba uharibifu wake umekaribia. Ndipo walio katika Uyahudi na wakimbilie milimani, na walio katikati yake wakimbilie nje, na walio katika mashamba wasiuingie. Kwa kuwa siku hizo ndizo za mapatilizo, ili yatimizwe yote yaliyoandikwa.”​—Luka 21:20-22.

17, 18. (a) Ni wakati gani na jinsi gani Wakristo walitenda katika kutii maneno ya Yesu yaliyoandikwa katika Luka 21:20-22? (b) Huenda wakawa walikabili jaribu gani jingine?

17 Miaka zaidi ya 30 ilikuwa imepita. Halafu, mwaka wa 66 W.K., majeshi ya Roma yakauzingira Yerusalemu. Yalipokuwa karibu kushinda, yakaondoka. Wakiwa wamesisimuliwa na wazo kwamba walikuwa wameshinda, Wayahudi waliwafuatia Waroma.a Lakini Wakristo wangefanya nini? Eusebio, aliyeishi katika sehemu ya kwanza ya karne ya nne, anaripoti kwamba “wale waliomwamini Kristo walihama kutoka Yerusalemu” mpaka kwenye mji mmoja katika Perea unaoitwa Pella.b

18 Wakati ulisonga mbele. Mwaka wa 66 ukaisha ukafika mwaka wa 67. Halafu mwaka wa 68 ukafika na kupita, hata na mwaka 69. Je! Wakristo hao walikuwa wakijaribiwa na kupita kwa wakati? Je! mambo yalikuwa yamekawia mno kwa wengine? Je! walikuwa wamekosea? Yesu hakuwa amesema wangojee muda mrefu namna gani. Lakini ikiwa wo wote walirudi Yerusalemu ilikuwa huzuni kwao, kwa maana katika mwaka wa 70 Waroma walirudi, wakauteka mji huo na kuua wakaaji wengi wake. Mwanahistoria Yosefo anasema kwamba watu milioni 1.1 walikufa, kwa maana Yerusalemu ulikuwa “umefurishwa na wakaaji,” umati mkubwa ulikuwa umekuja “kutoka nchi yote” mpaka Yerusalemu kwa ajili ya sikukuu ya Kupitwa.c

19. (a) Leo, ni maulizo gani yaliyo ya maana kweli kweli ambayo Wakristo walio wakfu wanapaswa kujibu? (b) Ni nini kinachopasa kutuchochea tushiriki katika utumishi mtakatifu?

19 Je! hayo yanakufanya ufikirie juu ya hali ya leo? Ulizo si: Mfumo huu wa kale utafikia mwisho wakati gani? Mwisho wake utakuja katika wakati wake Mungu. Tunalopaswa kuwa tukifikiria ni tunayofanya sisi. Tunapaswa kujiuliza: Je! nimejifunza Neno la Mungu kwa bidii sana na kuweka wakfu kabisa kabisa maisha yangu kwake? Je! kweli kweli mimi ninaishi kupatana na wakfu huo? Kinachopasa kutuchochea tushiriki katika utumishi mtakatifu si mahali tulipo kwa habari ya wakati. Kama Habili, Ibrahimu, Musa, Isaya na wengine, kumpenda Yehova Mungu kwapasa kutusukuma tufanye hivyo. Ni lazima tumtumikie Yehova kwa moyo wa kupenda, hata mwisho uje wakati gani. Lakini sasa tuna kichocheo cha pekee. Tumefikia sehemu ya kumalizia ya “siku za mwisho” za huu mfumo. (2 Timotheo 3:1) Uhakika huo unapasa kutuchochea tufanye utumishi usio wa kawaida.

20. Matukio ambayo umekwisha kuona yanalinganaje na yale ambayo Wakristo wa karne ya kwanza waliona?

20 Wakristo waliutoroka Yerusalemu kwa sababu walikuwa wameona sehemu mbalimbali za “ishara” ya Yesu zikitimia na wakaona utimizo wa usemi wake juu ya majeshi kuzunguka mji huo. Tangu mwaka wenye matukio mengi wa 1914 tumeona utimizo wa unabii mwingi unaohusu wakati wa mwisho. (Mathayo, sura za 24, 25; Ufunuo 6:1-8; 2 Timotheo 3:1-5) Matukio hayo yaliyotabiriwa yalianza kutokea miaka 70 hivi iliyopita. Hata hivyo Yesu alisema kwamba yangetokea yote wakati wa maisha ya kizazi kimoja. (Mathayo 24:32-34) Kwa wazi, kizazi hicho ki karibu sana kwisha!

Wenye Bidii Katika Imani

21. Kwa sababu gani utumishi wa bidii kwa Mungu ni jambo lenye uharaka?

21 Mara nyingi kazi ya kuokoa uhai inapasa kufanywa kwa haraka. Wakati wetu ni wakati unaotaka utendaji usio wa kawaida, utumishi uliozidishwa na imani na bidii iliyopanuliwa Ni lazima tukumbuke kwamba siku moja itakuwa siku yetu ya mwisho katika mfumo huu wa kale. Ama tutakuwa tumeishi mpaka mwisho wa huu mfumo au maisha yetu wenyewe yatakuwa yamefikia mwisho kwanza. Maisha sasa ni mafupi, yenye kupita kasi. Hakuna anayejua kama atakuwa hai kesho. Tuna wakati mchache tu wa kuthibitisha uaminifu na ukamilifu wetu kwa Mungu. (Zaburi 39:5; Mhubiri 12:1; Luka 12:18-21) Kwa hiyo ingefaa kujiuliza wenyewe hivi: Je! nimeridhika na niliyofanya leo?

22. Maandiko yanasema nini juu ya thawabu?

22 Ni jambo la maana kutosahau thawabu. Weka macho yako kwenye zawadi. Yesu alisema: “Atakayevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.” Paulo aliandika kwamba “kila mtu atapata thawabu yake mwenyewe sawasawa na taabu yake mwenyewe.” Pia alisema: “Mnahitaji saburi, ili kwamba mkiisha kuyafanya mapenzi ya Mungu mpate [utimizo wa] ile ahadi.”​—Marko 13:13, HNWW; 1 Wakorintho 3:8; Waebrania 10:36.

23, 24. Kwa sababu ya mashauri yaliyomo katika maandishi ya Biblia yaliyoandikwa hapa, wewe umeazimia kufanya nini kuhusiana na imani yako na utumishi wa Ufalme?

23 Maandiko yanatuonya hivi: “Kwa kuwa vitu vyote hivyo vitafumuliwa hivyo, ninyi yawapasa kuwa watu wa namna gani katika vitendo vitakatifu vya mwenendo na matendo ya utawa, mkingojea na kukaribisha akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.” Halafu tunaambiwa: “Kwa habari ya nyakati na majira, ndugu, hamhitaji kuandikiwa cho chote. Kwa kuwa ninyi wenyewe mwajua sana kwamba siku ya Yehova inakuja sawasawa kama mwivi usiku. . . . Kwa hiyo, basi, acheni sisi tusilale kama wale wengine wote wafanyavyo, bali acheni sisi tukae tukikesha na kubaki tukiwa na fahamu zetu.”​—2 Petro 3:11, 12, NW; 1 Wathesalonike 5:1-6, NW.

24 Basi, na tudumishe imani thabiti na kubaki wenye bidii katika utumishi wa Ufalme, bila kusita hata kidogo. Tukifanya hivyo, tunaweza kusema hivi pamoja na mtume: “Sisi si aina ya warudio nyuma kwenye uharibifu, bali aina ya walio na imani kuhifadhi hai nafsi.”​—Waebrania 10:39, NW.

[Maelezo ya Chini]

a Kitabu cha Yosefo, Wars of the Jews, II, 19:5-7.

b Kitabu cha Eusebio, Ecclesiastical History, III, 5:3.

c Kitabu cha Yosefo, Wars of the Jews, VI, 9:3, 4

Mambo ya Kufikiria

◻ Mifano ya Habili, Ibrahimu, Musa na Yeremia inatutia moyo sana leo jinsi gani?

◻ Uhakika wa kwamba Ufalme ulikuwa haujaja bado ulikuwa na matokeo gani juu ya Wakristo wa karne ya kwanza?

◻ Huenda Wakristo wa kwanza wakawa walipata jaribu gani baada ya kuutoroka Yerusalemu?

◻ Hangaiko letu kubwa lapasa kuwa nini sasa?

[Picha katika ukurasa wa 14]

Hawakuacha!

Habili

Ibrahimu

Daudi

Yeremia

Paulo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki