Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 4/15 kur. 14-19
  • Yehova Hutimiza Ahadi Zake kwa Waaminifu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova Hutimiza Ahadi Zake kwa Waaminifu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Imani ya Kweli Katika Nyakati za Kale
  • Matokeo ya Kukosa Imani
  • Imani Yaonyeshwa Wakati Wetu
  • Waaminifu Wana Wakati Ujao Mzuri Ajabu
  • Wakati Ujao Wenye Furaha Wahakikishiwa
  • Mtumaini Yehova Atimize Kusudi Lake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • ‘Kutembea kwa Imani, Si kwa Kuona’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Wingu Kubwa Sana la Mashahidi!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • “Imani Iliyotenganishwa na Matendo Imekufa Kama Mzoga”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 4/15 kur. 14-19

Yehova Hutimiza Ahadi Zake kwa Waaminifu

“Yeye ni mwaminifu aliyeahidi.”—WAEBRANIA 10:23.

1, 2. Kwa nini twaweza kuwa na uhakika kabisa katika ahadi za Yehova?

YEHOVA huwataka watumishi wake wasitawishe na kudumisha imani thabiti katika yeye na katika ahadi zake. Mtu akiwa na imani kama hiyo aweza kumtumainia Yehova kabisa afanye yale ambayo ameahidi kufanya. Neno lake lililopuliziwa hujulisha hivi: “BWANA wa majeshi ameapa, akisema, Hakika yangu kama vile vilivyoazimia, ndivyo itakavyokuwa; na kama nilivyokusudia, ndivyo itakavyotokea.”—Isaya 14:24.

2 Ile taarifa, “BWANA wa majeshi ameapa,” yaonyesha kwamba yeye hula kiapo rasmi cha kutimiza ahadi zake. Hiyo ndiyo sababu Neno lake laweza kusema hivi: “Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.” (Mithali 3:5, 6) Tumtumainipo Yehova na kujiruhusu tuongozwe na hekima yake, vijia vyetu bila shaka vitaongoza kwenye uhai udumuo milele, kwa kuwa hekima ya Mungu ni “mti wa uzima kwao wamshikao sana.”—Mithali 3:18; Yohana 17:3.

Imani ya Kweli Katika Nyakati za Kale

3. Noa alionyeshaje imani katika Yehova?

3 Rekodi ya matendo ya Yehova kuelekea walio na imani ya kweli hushuhudia kutegemeka kwake. Kwa kielelezo, miaka zaidi ya 4,400 iliyopita, Mungu alimwambia Noa kwamba ulimwengu wa siku yake ungeharibiwa katika Furiko la tufeni pote. Alimwagiza Noa ajenge safina kubwa ya kuokoa uhai wa wanadamu na wanyama. Noa alifanya nini? Andiko la Waebrania 11:7 latuambia hivi: “Kwa imani Noa, baada ya kupewa onyo la kimungu la mambo yasiyoonwa bado, alionyesha hofu ya kimungu akajenga safina kwa ajili ya kuokoa watu wa nyumbani mwake.” Kwa nini Noa alikuwa na imani katika jambo ambalo halikuwa limepata kutokea hapo awali, jambo ambalo “halikuwa limeonwa”? Kwa sababu alijua mambo ya kutosha juu ya shughuli za wakati uliopita za Mungu pamoja na familia ya kibinadamu na alijua kwamba lolote ambalo Mungu husema, hutimia. Kwa hiyo Noa alikuwa na hakika kwamba Furiko pia lingetimia.—Mwanzo 6:9-22.

4, 5. Kwa nini Abrahamu alimtumainia Yehova kabisa?

4 Kielelezo kingine cha imani ya kweli ni Abrahamu. Yapata miaka 3,900 iliyopita, Mungu alimwambia amdhabihu Isaka, mwana wake wa pekee aliyezaliwa na mke wake, Sara. (Mwanzo 22:1-10) Abrahamu aliitikiaje? Waebrania 11:17 hutaarifu hivi: “Kwa imani Abrahamu, alipojaribiwa, ni kana kwamba alimtoa Isaka.” Hata hivyo, ni kana kwamba wakati wa mwisho kabisa, malaika wa Yehova alimzuia Abrahamu. (Mwanzo 22:11, 12) Hata hivyo, kwa nini Abrahamu angeweza hata kufikiria kufanya jambo kama hilo? Kwa sababu, kama andiko la Waebrania 11:19 lisemavyo, “alihesabu kwamba Mungu alikuwa aweza kumfufua [Isaka] hata kutoka kwa wafu.” Lakini Abrahamu angewezaje kuwa na imani katika ufufuo wakati ambapo hakuwa ameona ufufuo wowote na hakukuwa na rekodi ya wakati uliopita ya ufufuo wowote?

5 Kumbuka kwamba, Sara alikuwa na umri wa miaka 89 Mungu alipowaahidi mwana. Sara hangeweza kupata mimba tena. (Mwanzo 18:9-14) Mungu alimwezesha Sara kupata mimba, naye akamzaa Isaka. (Mwanzo 21:1-3) Abrahamu alijua kwamba kwa kuwa Mungu alimwezesha Sara kupata mimba, basi angeweza kumrudisha Isaka kwenye uhai ikiwa ingehitajika. Waroma 4:20, 21 husema hivi juu ya Abrahamu: “Kwa sababu ya ahadi ya Mungu yeye hakusitasita kwa ukosefu wa imani, bali akawa mwenye nguvu nyingi kwa imani yake, akimpa Mungu utukufu na akisadikishwa kikamili kwamba alilokuwa ameahidi alikuwa na uwezo pia wa kufanya.”

6. Yoshua alionyeshaje uhakika katika Yehova?

6 Miaka zaidi ya 3,400 iliyopita, Yoshua alipokuwa na umri wa zaidi ya miaka mia moja, na baada ya maisha ya kujionea jinsi Mungu ni mwenye kutumainika, alitoa sababu hii ya uhakika wake: “Mnajua mioyoni mwenu, na rohoni mwenu, ya kuwa halikuwapungukia ninyi hata neno moja katika mambo hayo mema yote aliyoyanena BWANA, Mungu wenu, katika habari zenu; yote yametimia kwenu hapana neno lo lote mlilopungukiwa.”—Yoshua 23:14.

7, 8. Wakristo waaminifu wa karne ya kwanza walifanya tendo gani lenye kuokoa uhai, na kwa nini?

7 Yapata miaka 1,900 iliyopita, watu wengi wanyenyekevu walionyesha imani ya kweli. Waling’amua kutokana na utimizo wa unabii wa Biblia kwamba Yesu alikuwa ndiye Mesiya nao wakakubali mafundisho yake. Wakiwa na msingi huo imara katika mambo ya hakika na katika Maandiko ya Kiebrania, waliweka imani katika yale ambayo Yesu alifundisha. Hivyo, Yesu alipowaambia kwamba hukumu ya Mungu ilikuwa ikija dhidi ya Yudea na Yerusalemu kwa sababu ya ukosefu wa uaminifu, walimwamini. Naye alipowaambia waliyopaswa kufanya ili kuokoa uhai wao, waliyafanya.

8 Yesu aliwaambia waamini kwamba wakati ambapo Yerusalemu lingezingirwa na majeshi, walipaswa kukimbia. Majeshi ya Roma yalikuja dhidi ya Yerusalemu mwaka wa 66 W.K. Lakini kwa sababu ambayo haikueleweka, Waroma waliondoka. Hiyo ndiyo iliyokuwa ishara kwa Wakristo waliache hilo jiji, kwa kuwa Yesu alikuwa amesema hivi: “Mwonapo Yerusalemu limezingirwa na majeshi yaliyopiga kambi, ndipo jueni kwamba kufanywa ukiwa kwalo kumekaribia. Ndipo waacheni wale walio katika Yudea waanze kukimbia hadi kwenye milima, na waacheni wale walio katikati yalo waondoke, na waacheni wale walio katika sehemu za mashambani wasiingie ndani yalo.” (Luka 21:20, 21) Waliokuwa na imani ya kweli waliliacha Yerusalemu na mazingira yake na kukimbilia usalama.

Matokeo ya Kukosa Imani

9, 10. (a) Viongozi wa kidini walionyeshaje ukosefu wao wa imani katika Yesu? (b) Matokeo ya kukosa imani huko yalikuwa nini?

9 Wale ambao hawakuwa na imani ya kweli walifanya nini? Hawakukimbia walipokuwa na fursa ya kufanya hivyo. Walifikiri kwamba viongozi wao wangeweza kuwaokoa. Lakini, viongozi hao na wafuasi wao pia walikuwa na uthibitisho wa Umesiya wa Yesu. Kwa hiyo kwa nini hawakukubali aliyokuwa amesema? Kwa sababu ya hali yao mbaya ya moyoni. Hilo lilifichuliwa mapema walipoona wengi wa watu wa kawaida wakimmiminikia Yesu na kuweka imani katika yeye baada ya kumfufua Lazaro. Andiko la Yohana 11:47 na 48 lasimulia hivi: “Makuhani wakuu na Mafarisayo wakaikusanya pamoja Sanhedrini [mahakama kuu ya Kiyahudi] na kuanza kusema: ‘Twapaswa kufanya nini, kwa sababu mtu huyu [Yesu] hufanya ishara nyingi? Tukimwacha hivyo, wao wote wataweka imani katika yeye, na Waroma watakuja na kuondolea mbali mahali petu na taifa letu pia.’” Mstari wa 53 wasema hivi: “Kwa hiyo tangu siku hiyo na kuendelea walifanya shauri kumuua.”

10 Yesu alikuwa amefanya muujiza wa ajabu sana kama nini—kumfufua Lazaro kutoka kwa wafu! Lakini viongozi wa kidini walitaka Yesu auawe kwa kufanya hivyo. Uovu wao mzito ulifichuliwa zaidi wakati ambapo “makuhani wakuu wa[li]fanya shauri kumuua Lazaro pia, kwa sababu kwa ajili yake wengi wa Wayahudi walikuwa wakienda huko na kuweka imani katika Yesu.” (Yohana 12:10, 11) Lazaro alikuwa ametoka tu kufufuliwa kutoka kwa wafu, nao walitaka kumwona akiwa mfu tena! Hawakuhangaikia mapenzi ya Mungu au hali njema ya watu. Walikuwa na ubinafsi, wakihangaikia nyadhifa zao tu na faida zao tu. “Walipenda utukufu wa wanadamu zaidi ya hata utukufu wa Mungu.” (Yohana 12:43) Lakini waliadhibiwa kwa sababu ya ukosefu wao wa imani. Mwaka wa 70 W.K., majeshi ya Roma yalirudi na kuharibu mahali pao na taifa lao, na wengi wao pia.

Imani Yaonyeshwa Wakati Wetu

11. Mapema katika karne hii, imani ya kweli ilionyeshwaje?

11 Katika karne hii kumekuwa pia na wanaume na wanawake wengi wa imani. Mathalani, nyuma huko mapema miaka ya 1900, watu kwa ujumla walikuwa wakitarajia wakati ujao wenye amani, wenye ufanisi. Wakati huohuo, walioweka imani katika Yehova walikuwa wakitangaza kwamba wanadamu walikuwa wakikaribia kuingia katika wakati ulio na taabu zaidi. Hilo ndilo lililokuwa limetabiriwa na Neno la Mungu katika Mathayo sura ya 24, 2 Timotheo sura ya 3, na kwingineko. Mambo ambayo watu hao wa imani walisema kwa kweli yalitukia, kuanzia na Vita ya Ulimwengu ya Kwanza mwaka wa 1914. Kwa kweli ulimwengu uliingia katika “siku za mwisho” zilizotabiriwa zenye “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Kwa nini watumishi wa Yehova walijua kweli juu ya hali za ulimwengu nyuma huko wakati ambapo wengine hawakujua? Kwa sababu, sawa na Yoshua, walikuwa na imani kwamba hakuna neno hata moja la Yehova ambalo lingekosa kutimia.

12. Leo, ni ahadi gani ya Yehova ambayo watumishi wake watumainia kabisa?

12 Leo, watumishi wa Yehova, ambao huweka imani katika yeye, wajumlika kuwa wapatao milioni sita ulimwenguni pote. Wanajua kutokana na uthibitisho katika utimizo wa neno la Mungu la kiunabii kwamba karibuni Mungu atakomesha mfumo huu wa mambo ulio mfisadi, usio na adili. Kwa hiyo wana uhakika kwamba wakati wakaribia watakapoona utimizo wa andiko la 1 Yohana 2:17, lisemalo hivi: “Ulimwengu unapitilia mbali na ndivyo na tamaa yao, lakini yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hudumu milele.” Watumishi wake watumainia kabisa kwamba Yehova atatimiza ahadi hiyo.

13. Waweza kumtumainia Yehova kadiri gani?

13 Waweza kumtumainia Yehova kwa kadiri gani? Waweza kumtumainia kabisa-kabisa! Hata ukipoteza uhai wako kwa kumtumikia, atakurudishia uhai ulio bora zaidi sana katika ufufuo! Yesu atuhakikishia hivi: “Saa inakuja ambayo katika hiyo wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho [yaani, katika kumbukumbu la Mungu] watasikia sauti yake na kutoka.” (Yohana 5:28, 29) Je, wajua daktari, kiongozi wa kisiasa, mwanasayansi, mfanyabiashara, au binadamu mwingine yeyote awezaye kufanya hivyo? Rekodi zao za wakati uliopita zaonyesha kwamba hawawezi. Yehova aweza, naye atafanya hivyo!

Waaminifu Wana Wakati Ujao Mzuri Ajabu

14. Neno la Mungu lawaahidi waaminifu wakati ujao gani ulio mzuri ajabu?

14 Yesu alionyesha uhakika wa ulimwengu mpya chini ya Ufalme wa kimbingu wa Mungu, akisema hivi: “Wenye furaha ni wenye tabia-pole, kwa kuwa wao watairithi dunia.” (Mathayo 5:5) Hilo lilitia nguvu ahadi ya Mungu ipatikanayo kwenye Zaburi 37:29: “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” Na kabla tu ya kifo cha Yesu, mtenda-maovu alipoonyesha imani katika yeye, Yesu alimwambia mtu huyo hivi: “Utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso.” (Luka 23:43) Ndiyo, akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu, Yesu atahakikisha kwamba mtu huyo atafufuliwa apate uhai duniani akiwa na fursa ya kuishi katika Paradiso hiyo. Leo, wale wawekao imani katika Ufalme wa Yehova waweza pia kutazamia kuishi katika Paradiso wakati ambapo “[Mungu] atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe.”—Ufunuo 21:4.

15, 16. Kwa nini maisha yatakuwa yenye amani sana katika ulimwengu mpya?

15 Acheni tukaze akili zetu mbele kwenye ulimwengu huo mpya. Wazia kwamba tayari tunaishi ndani yake. Mara moja, twaona watu wenye furaha wakikaa pamoja katika amani kamili. Wanaonea shangwe hali zifananazo na zile zifafanuliwazo kwenye Isaya 14:7, Biblia Habari Njema: “Dunia yote ina utulivu na amani, kila mtu anaimba kwa furaha.” Kwa sababu gani wako hivyo? Kwanza, ona kwamba milango ya nyumba haina makufuli. Hayahitajiki kwa kuwa hakuna uhalifu, wala ujeuri. Ni kama tu vile Neno la Mungu lilivyosema hali itakuwa: “Wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu.”—Mika 4:4.

16 Wala hakuna vita tena kamwe, kwa kuwa huu ni ulimwengu mpya, vita imepigwa marufuku. Silaha zote zimegeuzwa kuwa vifaa vya amani. Katika maana kamili, andiko la Isaya 2:4 limetimizwa: “Watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.” Lakini basi, hilo ndilo tulilotarajia! Kwa nini? Kwa sababu wakazi wengi wa huo ulimwengu mpya walijifunza kufanya hivyo walipokuwa wakimtumikia Mungu katika ulimwengu wa kale.

17. Ni hali zipi za kuishi zitakazokuwapo chini ya Ufalme wa Mungu?

17 Jambo jingine uonalo ni kwamba hakuna umaskini. Hakuna mtu aishiye katika kibanda hafifu kichafu au avaaye matambara au asiye na makao. Kila mtu ana nyumba yenye kustarehesha na mali ambazo zimetunzwa vizuri pamoja na miti na maua yenye kupendeza. (Isaya 35:1, 2; 65:21, 22; Ezekieli 34:27) Na hakuna njaa kwa sababu Mungu ametimiza ahadi yake ya kwamba kungekuwa na chakula kingi kwa wote: “Na uwepo wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima.” (Zaburi 72:16) Kwa kweli, chini ya uongozi wa Ufalme wa Mungu, paradiso tukufu yapanuka duniani kote, kama vile tu Mungu alivyokusudia nyuma huko katika Edeni.—Mwanzo 2:8.

18. Katika ulimwengu mpya, ni mambo gani ambayo hayatawahatarisha watu tena?

18 Pia, wastaajabia nguvu zenye sulubu alizo nazo kila mtu. Hiyo ni kwa sababu sasa wana miili mikamilifu na akili kamilifu. Hakuna ugonjwa, maumivu, au kifo tena kamwe. Hakuna mtu aliye katika kiti cha magurudumu au aliyelazwa hospitalini. Yote hayo yametoweka milele. (Isaya 33:24; 35:5, 6) Kwani, hakuna mnyama yeyote aliye tisho; kwa kuwa wamefanywa kuwa wenye amani kwa nguvu za Mungu!—Isaya 11:6-8; 65:25; Ezekieli 34:25.

19. Kwa nini kila siku katika ulimwengu mpya itakuwa siku ya “wingi wa amani”?

19 Ni ustaarabu wa ajabu kama nini unaofanyizwa na hao wakazi waaminifu wa ulimwengu huo mpya! Nguvu zao na stadi zao, na mali za dunia, zimetolewa kwa ajili ya ufuatiaji wenye mafaa, wala si kwa ufuatiaji wenye kudhuru; ili kushirikiana na wengine, si kushindana nao. Na kila mtu unayekutana naye ni mtu uwezaye kumtumaini, kwa sababu, kama Mungu alivyoahidi, wote ni watu ‘wanaofundishwa na BWANA.’ (Isaya 54:13) Kwa kuwa kila mtu aongozwa na sheria na kanuni za Mungu, dunia ‘imejawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.’ (Isaya 11:9) Kwa kweli, kila siku katika ulimwengu mpya huo iko vile Zaburi 37:11 ilivyosema ingekuwa, siku ya “wingi wa amani.”

Wakati Ujao Wenye Furaha Wahakikishiwa

20. Twapaswa kufanya nini ili tuonee shangwe wakati ujao wenye amani?

20 Ni lazima tufanye nini ili tuwe sehemu ya wakati ujao huo wenye furaha? Andiko la Isaya 55:6 latuambia hivi: “Mtafuteni BWANA, maadamu anapatikana, mwiteni, maadamu yu karibu.” Na tutafutapo, mtazamo wetu wapaswa kuwa kama ule ufafanuliwao kwenye Zaburi 143:10: “Unifundishe kuyatenda mapenzi yako, kwa maana ndiwe Mungu wangu.” Wafanyao hilo waweza kutembea bila lawama mbele ya Yehova katika siku hizi za mwisho na waweza kutazamia wakati ujao ulio bora. “Umwangalie sana mtu mkamilifu, umtazame mtu mnyofu, maana mwisho wake mtu huyo ni amani. Wakosaji wataangamizwa pamoja, wasio haki mwisho wao wataharibiwa.”—Zaburi 37:37, 38.

21, 22. Mungu anafanya nini leo, na hayo mazoezi yanatimizwaje?

21 Sasa hivi Yehova anawaita kutoka kila taifa wale watakao kufanya mapenzi yake. Anawafanya watu wawe msingi wa jamii yake mpya ya kidunia, kama vile unabii wa Biblia ulivyotabiri: “Katika siku za mwisho [wakati tunaoishi sasa] . . . , mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa BWANA [ibada yake ya kweli], . . . naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake.”—Isaya 2:2, 3.

22 Ufunuo 7:9 huwafafanua kuwa “umati mkubwa . . . kutoka katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha.” Mstari wa 14 wataarifu hivi: “Hawa ndio wale watokao katika dhiki kubwa,” wakiokoka mwisho wa mfumo uliopo. Msingi huo wa ulimwengu mpya sasa ni watu wapatao milioni sita, wengi wapya wakipata kuwa sehemu yake kila mwaka. Watumishi wa Yehova wote hao waaminifu wanazoezwa kwa ajili ya uhai katika ulimwengu wake mpya. Wanajifunza stadi za kiroho na nyinginezo zihitajiwazo ili kugeuza umbo la dunia liwe paradiso. Nao wanatumainia kabisa kwamba Paradiso hiyo itakuwa uhalisi kwa sababu “yeye ni mwaminifu aliyeahidi.”—Waebrania 10:23.

Hoja za Kupitia

◻ Kukosa imani kulikuwa na matokeo gani katika karne ya kwanza?

◻ Watumishi wa Mungu waweza kumtumainia kadiri gani?

◻ Waaminifu wana wakati ujao wa aina gani?

◻ Twapaswa kufanya nini ili kuhakikisha kwamba tutakuwa na wakati ujao wenye furaha katika ulimwengu mpya wa Mungu?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Hivi sasa Yehova anafanyiza msingi wa jamii mpya ya kidunia

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki