Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 3/15 kur. 13-20
  • Mtumaini Yehova Atimize Kusudi Lake

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mtumaini Yehova Atimize Kusudi Lake
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ni Nini Kilichofanya Hali Ziharibike?
  • Kusudi la Mungu Halijabadilika
  • Walimtumaini Yehova
  • Mashahidi Wakristo Humtumaini Mungu
  • Yehova Hutimiza Ahadi Zake kwa Waaminifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Abrahamu Alikuwa Nani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
  • Jaribu la Imani
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
  • Waokokaji Kutoka Mataifa Yote
    Kuokolewa Kuingia Katika Dunia Mpya
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 3/15 kur. 13-20

Mtumaini Yehova Atimize Kusudi Lake

“Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.”—ZABURI 37:29.

1. Kusudi la Yehova kwa wanadamu na kwa dunia hii ni nini?

YEHOVA alipoumba wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, yeye aliwaumba wakiwa wakamilifu. Na aliwaumba ili waweze kuishi milele juu ya dunia hii—ikiwa wangetii sheria zake. (Mwanzo 1:26, 27; 2:17) Zaidi ya hiyo, Mungu aliwaweka katika mazingira ya kiparadiso. (Mwanzo 2:8, 9) Yehova aliwaambia hivi: “Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha.” (Mwanzo 1:28) Hivyo, hatimaye wazao wao wangeenea kotekote duniani, na sayari hii ingekuwa paradiso iliyojaa jamii ya watu wakamilifu, wenye furaha. Familia ya kibinadamu ilikuwa na mwanzo mzuri kama nini! “Mungu akaona kila kitu alichokifanya, na tazama, ni chema sana.”—Mwanzo 1:31.

2. Hali ya mambo ya kibinadamu yazusha maswali gani?

2 Lakini, hali ya mambo ya kibinadamu ambayo imekuwapo kwa maelfu ya miaka haipatani kabisa na kusudi la awali la Mungu. Ainabinadamu haijakamilika na haina furaha kabisa. Hali za ulimwengu zimekuwa zenye kutaabisha, na kama ilivyotabiriwa, zimekuwa mbaya zaidi katika wakati wetu. (2 Timotheo 3:1-5, 13) Kwa hiyo twaweza kuwaje wenye uhakika kwamba kusudi la Mungu kwa wanadamu litatimizwa katika wakati ujao ulio karibu? Je! vipindi virefu zaidi vya wakati vitapita huku hali zenye kutaabisha zikiendelea?

Ni Nini Kilichofanya Hali Ziharibike?

3. Kwa nini Yehova hakukomesha uasi wa ainabinadamu mara hiyo?

3 Wale wenye ujuzi sahihi wa Neno la Mungu lililopuliziwa wajua kwa nini Yehova ameruhusu hali hizo mbaya duniani. Wao wajua pia yale atakayofanya juu ya hali hizo. Kutokana na simulizi la Biblia, wamejifunza kwamba wazazi wetu wa kwanza walitumia vibaya zawadi nzuri ajabu ya hiari ambayo Mungu alikuwa amewapa wanadamu. (Linganisha 1 Petro 2:16.) Walichagua isivyofaa mwendo wa kutomtegemea Mungu. (Mwanzo, sura 2 na 3) Uasi wao ulizusha masuala ya maana sana, kama vile: Je! Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Mzima ana haki ya kutawala wanadamu? Je! utawala wake ndio uwafaao zaidi? Je! utawala wa kibinadamu waweza kufanikiwa bila usimamizi wa Mungu? Njia ya hakika ya kupata majibu ya maswali hayo ilikuwa ni kuacha karne nyingi za utawala wa kibinadamu zipite. Matokeo yangeonyesha pasipo shaka lolote kama wanadamu wangeweza kufanikiwa bila kumtegemea Mfanyi wao.

4, 5. (a) Tokeo limekuwa nini kwa sababu ya wanadamu kukataa utawala wa Mungu? (b) Kupita kwa wakati kumeonyesha nini bila shaka yoyote?

4 Adamu na Hawa walipomwacha Mungu, yeye hakuwaendeleza wakiwa wakamilifu. Bila utegemezo wake, wao walizorota. Matokeo yalikuwa kutokamilika, uzee, na hatimaye kifo. Kupitia sheria za urithi-tabia, wazazi wetu wa kwanza walipitisha tabia hizo zenye madhara kwa wazao wao wote, kutia na sisi. (Warumi 5:12) Na vipi juu ya matokeo ya utawala wa kibinadamu wa maelfu ya miaka? Umekuwa wenye msiba, kama vile Mhubiri 8:9 NW, isemavyo kwa kweli: “Mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa umizo lake.”

5 Kupita kwa wakati kumeonyesha bila shaka yoyote kwamba wanadamu hawana uwezo wa kuelekeza mambo yao kwa mafanikio bila kumtegemea Muumba wao. Mwandikaji wa Biblia aliyepuliziwa Yeremia alijulisha hivi: “Ee BWANA [Yehova, NW], najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.”—Yeremia 10:23; Kumbukumbu la Torati 32:4, 5; Mhubiri 7:29.

Kusudi la Mungu Halijabadilika

6, 7. (a) Je! maelfu ya miaka ya historia imebadili kusudi la Yehova? (b) Ni nini kinachotiwa ndani ya kusudi la Yehova?

6 Je! kupita kwa maelfu ya miaka ya historia ya kibinadamu—iliyojaa sana uovu na kuteseka—kumebadili kusudi la Mungu? Neno lake husema hivi: “Maana BWANA [Yehova, NW], aliyeziumba mbingu, asema hivi; Yeye ni Mungu; ndiye aliyeiumba dunia na kuifanya; ndiye aliyeifanya imara; hakuiumba ukiwa; aliiumba ili ikaliwe na watu.” (Isaya 45:18) Kwa hiyo Mungu aliiumba dunia ili ikaliwe na wanadamu, na hilo bado ni kusudi lake.

7 Yehova hakuumba dunia ikaliwe tu na watu bali pia alikusudia kwamba iwe paradiso ifurahiwe na watu wakamilifu, wenye furaha. Hiyo ndiyo sababu Biblia ilitabiri kwamba kungekuwa na “dunia mpya,” jamii mpya ya kibinadamu, ambamo “uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13, NW) Na kwenye Ufunuo 21:4, Neno la Mungu hutuambia kwamba katika ulimwengu wake mpya, “atafuta kila chozi katika macho yao [ainabinadamu], wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.” Ni kwa sababu hizo kwamba Yesu angeweza kusema juu ya ulimwengu mpya unaokuja duniani kuwa “Paradiso.”—Luka 23:43, NW.

8. Twaweza kuwaje wenye uhakika kwamba Yehova atatimiza kusudi lake?

8 Kwa kuwa Yehova ndiye Muumba wa ulimwengu wote mzima mwenye nguvu zote na mwenye hekima yote, hakuna mtu anayeweza kubatilisha kusudi lake. “BWANA [Yehova, NW] wa majeshi ameapa, akisema, Hakika yangu kama vile nilivyoazimia, ndivyo itakavyokuwa; na kama nilivyokusudia, ndivyo itakavyotokea.” (Isaya 14:24) Hivyo, Mungu anaposema atafanya dunia hii kuwa paradiso inayokaliwa na watu wakamilifu, hilo ndilo litakalotokea. Yesu alisema hivi: “Heri [Wenye furaha ni, NW] wenye upole, maana hao watairithi nchi.” (Mathayo 5:5; linganisha Zaburi 37:29.) Twaweza kuwa na uhakika kwamba ahadi hiyo itatimizwa. Kwa kweli, twaweza kuwa tayari kufa kwa ajili yayo.

Walimtumaini Yehova

9. Abrahamu alifanya nini kilichoonyesha tumaini lake kwa Yehova?

9 Watu wengi wenye kumhofu Mungu katika muda wote wa historia walikuwa tayari kufa kwa ajili ya kusudi la Mungu kwa dunia kwa sababu walisadikishwa kwamba yeye angelitimiza. Ingawa huenda ujuzi wao ulikuwa mdogo, wao walimtumaini Mungu na kushughulikia kufanya mapenzi yake. Mathalani, kulikuwa na Abrahamu, aliyeishi karibu miaka 2,000 kabla ya Yesu kutembea duniani—muda mrefu kabla Biblia haijaanza kuandikwa. Yeye alimtumaini Yehova atimize ahadi Zake. Yaelekea kwamba Abrahamu alijifunza juu ya Muumba kutoka kwa babu wa kale mwaminifu Shemu, aliyefunzwa na Noa. Kwa hiyo Mungu alipomwambia Abrahamu ahame kutoka bara la Uru la Wakaldayo lenye ufanisi, aende kwenye bara la Kanaani asilolijua na lenye hatari, mzee huyo wa ukoo alijua angeweza kumtumaini Yehova, na kwa hiyo alienda. (Waebrania 11:8) Baadaye, Yehova alimwambia hivi: “Nitakufanya wewe kuwa taifa kubwa.”—Mwanzo 12:2.

10, 11. Kwa nini Abrahamu alikuwa tayari kumtoa dhabihu mwanawe mzaliwa wa pekee, Isaka?

10 Ni nini kilichotukia baada ya Isaka kuzaliwa na Abrahamu? Yehova alimwonyesha Abrahamu kwamba ilikuwa kupitia Isaka kwamba wazao wake wangesitawi na kuwa taifa kubwa. (Mwanzo 21:12) Hivyo, ni lazima iwe ilionekana kuwa jambo la kupingana, Yehova alipomwambia Abrahamu amtoe dhabihu mwanawe Isaka, huo ukiwa mtihani wa imani yake. (Mwanzo 22:2) Na bado, hali Abrahamu akimtumaini Yehova kabisa, yeye alichukua hatua ili kutii, akiinua kihalisi kisu chake ili amchinje Isaka. Katika dakika ya mwisho, Mungu alimtuma malaika amzuie Abrahamu.—Mwanzo 22:9-14.

11 Kwa nini Abrahamu alikuwa mtiifu hivyo? Waebrania 11:17-19 lafunua hivi: “Kwa imani Ibrahimu alipojaribiwa, akamtoa Isaka awe dhabihu; na yeye aliyezipokea hizo ahadi alikuwa akimtoa mwanawe, mzaliwa pekee; naam, yeye aliyeambiwa, Katika Isaka uzao wako utaitwa, akihesabu ya kuwa Mungu aweza kumfufua hata kutoka kuzimu; akampata tena toka huko kwa mfano.” Vilevile Warumi 4:20, 21 lasema hivi: “Lakini [Abrahamu] akiiona ahadi ya Mungu hakusita kwa kutokuamini, . . . huku akijua hakika ya kuwa Mungu aweza kufanya yale aliyoahidi.”

12. Abrahamu alithawabishwaje kwa ajili ya imani yake?

12 Abrahamu alithawabishwa kwa sababu ya imani yake si kwa kuhifadhiwa tu kwa Isaka na kwa “taifa kubwa” kutokezwa kupitia yeye, bali kwa njia nyingine pia. Mungu alimwambia Abrahamu hivi: “Katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu.” (Mwanzo 22:18) Jinsi gani? Mfalme wa Ufalme wa Mungu wa kimbingu angekuja kupitia mstari wa uzao wa Abrahamu. Ufalme huo ungevunjilia mbali ulimwengu huu mwovu ulio chini ya Shetani usiwepo. (Danieli 2:44; Warumi 16:20; Ufunuo 19:11-21) Kisha, katika dunia iliyosafishwa chini ya utawala wa Ufalme, Paradiso ingesitawishwa tufeni pote, na kutoka kwa “mataifa yote” watu wanaofanya mapenzi ya Mungu wangefurahia afya kamili na kuishi milele. (1 Yohana 2:15-17) Na ingawa Abrahamu alikuwa na ujuzi mdogo tu juu ya Ufalme, yeye alimtumaini Mungu na kutazamia mbele kwenye kusimamishwa kwa Ufalme huo.—Waebrania 11:10.

13, 14. Kwa nini Ayubu alimtumaini Mungu?

13 Mamia kadhaa ya miaka baadaye, kulikuwa na Ayubu, aliyeishi kati ya karne za 17 na 16 K.W.K. katika ile iitwayo sasa Uarabuni. Yeye pia aliishi kabla ya Biblia kuanza kuandikwa. Ayubu “alikuwa mkamilifu na uelekevu, ni mmoja aliyemcha Mungu, na kuepukana na uovu.” (Ayubu 1:1) Shetani alipompiga Ayubu kwa maradhi mabaya sana yenye uchungu mwingi, mwanamume huyo mwaminifu “hakusema hata neno moja lenye kosa” katika janga lote alilopata. (Ayubu 2:10, The New English Bible) Ayubu alimtumaini Mungu. Na ingawa hakujua mambo madogo-madogo juu ya sababu ya kuteseka sana hivyo, yeye alikuwa tayari kufa kwa ajili ya Mungu na ahadi Zake.

14 Ayubu alijua kwamba hata akifa, siku moja Mungu angemrudisha tena kwenye uhai kupitia ufufuo. Yeye alionyesha tumaini hilo aliposema hivi kwa Yehova Mungu: “Laiti ungenificha kuzimuni [kaburini], . . . na kuniandikia muda ulioamriwa, na kunikumbuka! Mtu akifa, je! atakuwa hai tena? . . . Wewe ungeita, nami ningekujibu.” (Ayubu 14:13-15) Ingawa alikuwa katika uchungu, Ayubu alidhihirisha imani katika enzi kuu ya Yehova, akisema: “Hata nitakapokufa sitajiondolea uelekevu [uaminifu-maadili, NW] wangu.”—Ayubu 27:5.

15. Daudi alionyeshaje uhakika wake katika kusudi la Yehova?

15 Karne sita hivi baada ya Ayubu na karibu miaka elfu moja kabla ya Yesu kuja duniani, Daudi alidhihirisha tumaini lake katika ulimwengu mpya. Yeye alisema hivi katika zaburi: “Wamngojao BWANA [Yehova, NW] ndio watakaoirithi nchi. Maana bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo . . . Bali wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani. Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” Kwa sababu ya tumaini lake lisiloyumbayumba, Daudi alihimiza hivi: “Umtumaini BWANA [Yehova, NW] . . . Nawe utajifurahisha kwa BWANA [Yehova, NW], naye atakupa haja za moyo wako.”—Zaburi 37:3, 4, 9-11, 29.

16. “Wingu kubwa la mashahidi” lilikuwa na tumaini gani?

16 Katika muda wa karne zote, wanaume na wanawake waaminifu wamekuwa na tumaini hilohilo la uhai wa milele duniani. Kwa kweli, walifanyiza “wingu kubwa la mashahidi” ambao walikuwa tayari kufa kihalisi kabisa kwa sababu ya ahadi za Yehova. Wengi wa hao mashahidi wa Yehova wa kale waliteswa na kuuawa kwa sababu ya imani yao, “ili wapate ufufuo ulio bora.” Jinsi gani? Katika ulimwengu mpya, Mungu atawathawabisha kwa ufufuo ulio bora na taraja la uhai wa milele.—Yohana 5:28, 29; Waebrania 11:35; 12:1.

Mashahidi Wakristo Humtumaini Mungu

17. Wakristo wa karne ya kwanza walimtumaini Yehova kwa uthabiti kiasi gani?

17 Katika karne ya kwanza W.K., Yehova alifunulia kutaniko la Kikristo lililotoka tu kuanzishwa, mambo mengi madogo-madogo juu ya Ufalme na utawala wao juu ya dunia. Kwa kielelezo, roho yake ilimpulizia mtume Yohana aandike kwamba idadi ya wale watakaoshirikiana na Yesu Kristo katika Ufalme wa mbinguni ingekuwa 144,000. Hao wangekuwa watumishi wa Mungu walio waaminifu ambao walikuwa “wamenunuliwa katika wanadamu.” (Ufunuo 7:4; 14:1-4) Wao wangetawala juu ya dunia “wakiwa wafalme” pamoja na Kristo mbinguni. (Ufunuo 20:4-6, NW) Wakristo hao wa karne ya kwanza walimtumaini Yehova kabisa atimize ahadi yake kwa ajili ya Ufalme wa kimbingu na milki yayo ya kidunia kiasi cha kwamba walikuwa tayari kufa kwa ajili ya imani yao. Wengi wao walifanya hivyo.

18. Mashahidi wa Yehova leo huwaigaje wenzao wa zamani za kale?

18 Leo, Mashahidi wa Yehova karibu milioni tano wanamtumaini Mungu vivyo hivyo kama vile wenzao walioishi karne nyingi kabla yao walivyofanya. Mashahidi hao wa siku-hizi wako tayari pia kufa kwa ajili ya ahadi za Mungu. Wameweka maisha zao wakfu kwake na wana Biblia nzima ya kuimarisha imani yao. (2 Timotheo 3:14-17) Hao Mashahidi wa Yehova wa kisasa huiga wafuasi wa Yesu wa karne ya kwanza waliojulisha kwamba ‘imewapasa kumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.’ (Matendo 5:29) Katika karne hii wengi wa hao Mashahidi Wakristo wamenyanyaswa kwa ukatili. Baadhi yao hata wameuawa kwa sababu ya imani yao. Wengine wamekufa kutokana na ugonjwa, aksidenti, au uzee. Hata hivyo, kama vile mashahidi waaminifu wa nyakati zilizopita, wamemtumaini Mungu kwa sababu walijua kwamba angewarudisha kwenye uhai katika ulimwengu wake mpya kupitia ufufuo.—Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15; Ufunuo 20:12, 13.

19, 20. Twatambua nini juu ya unabii wa Biblia kwa ajili ya siku yetu?

19 Mashahidi wa Yehova wathamini kwamba kutolewa kwao kutoka mataifa yote kuingia katika udugu wa tufeni pote kulitabiriwa zamani za kale katika unabii wa Biblia. (Isaya 2:2-4; Ufunuo 7:4, 9-17) Na Yehova anawapa kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote ili kukusanya katika upendelevu na ulinzi wake watu wengineo wenye mioyo yenye kufuatia haki. (Mithali 18:10; Mathayo 24:14; Warumi 10:13) Wote hao waweka tumaini lao lote katika Yehova, wakijua kwamba karibuni ataleta ulimwengu wake mpya ulio mzuri ajabu.—Linganisha 1 Wakorintho 15:58; Waebrania 6:10.

20 Unabii mwingi wa Biblia waonyesha kwamba, tangu ule mwaka wa msingi wa 1914, ulimwengu wa Shetani umekuwa katika siku zao za mwisho kwa karibu miaka 80 sasa. Ulimwengu huu unakaribia mwisho wao. (Warumi 16:20; 2 Wakorintho 4:4; 2 Timotheo 3:1-5) Kwa hiyo, Mashahidi wa Yehova wana moyo mkuu kwa sababu wanang’amua kwamba karibuni Ufalme wa Mungu utachukua mamlaka kamili juu ya mambo yote ya dunia. Kwa kukomesha ulimwengu huu mwovu wa sasa na kuleta ulimwengu wake mpya wenye uadilifu, Mungu atafuta kabisa hali mbaya ambazo zimekuwako duniani kwa karne nyingi sana.—Mithali 2:21, 22.

21. Kwa nini twaweza kufurahi kujapokuwa matatizo yetu ya sasa?

21 Kisha, kwa umilele wote, Mungu ataonyesha jinsi anavyotujali sana kwa kumimina baraka zitakazolipia kwa kiasi kikubwa umizo lolote ambalo huenda tulipata zamani. Tutapata mambo mengi mazuri sana katika ulimwengu mpya hivi kwamba tutasahau matatizo yetu ya wakati uliopita. Jinsi inavyofariji kujua kwamba wakati huo Yehova ‘ataufumbua mkono wake, akishibisha kila kilicho hai matakwa yacho.’—Zaburi 145:16; Isaya 65:17, 18.

22. Kwa nini tumtumaini Yehova?

22 Katika ulimwengu mpya, ainabinadamu yenye uaminifu itaona utimizo wa Warumi 8:21: “Viumbe vyenyewe navyo vitawekwa huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu, hata viingie katika uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu.” Wataona utimizo wa sala hii ambayo Yesu alifundisha wafuasi wake: “Ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.” (Mathayo 6:9, 10) Kwa hiyo mtumaini Yehova kabisa kwa sababu ahadi yake isiyobatilika ni hii: “Wenye haki watairithi nchi nao watakaa humo milele.”—Zaburi 37:29.

Wewe Ungejibuje?

◻ Kusudi la Yehova kwa wanadamu na kwa dunia hii ni nini?

◻ Kwa nini Mungu ameruhusu hali mbaya duniani?

◻ Watu waaminifu wa kale walionyeshaje tumaini lao kwa Yehova?

◻ Kwa nini watumishi wa Mungu leo humtumaini Yehova?

[Picha katika ukurasa wa 16]

Mungu aliumba wanadamu waishi milele kwa furaha katika dunia-paradiso

[Picha katika ukurasa wa 18]

Abrahamu alitumaini juu ya uwezo wa Yehova kufufua wafu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki