Furaha Ujapokuwa Ulimwengu Wenye Kuvunja Sheria, Usio na Upendo
“Wenye furaha ni wale ambao njia yao haina kosa, wale wanaotembea katika sheria ya Yehova.”—ZABURI 119:1, New World Translation.
1, 2. (a) Furaha ya kweli inatoka kwa nani, na inawezekana kuwa na furaha hiyo kwa muda mrefu kadiri gani? (b) Badala ya kuitwa “Heri,” sehemu ya kwanza ya Mahubiri ya Mlimani iitweje, na kwa sababu gani iitwe hivyo?
FURAHA inatoka kwa Muumba wa mwanadamu. Yeye ndiye “Mungu mwenye furaha,” mwenye habari zilizo njema kwetu. (1 Timotheo 1:11, NW) Ameandalia viumbe vyake vya kibinadamu furaha ya milele hapa duniani. Hata sasa, wanaweza kuingia katika furaha hiyo kwa kujipatanisha na matakwa yake.—Zaburi 119:26, 33.
2 Karne kumi na tisa zilizopita Yesu Kristo, Mwana wa “Mungu mwenye furaha,” alitoa yaliyokuja kuitwa Mahubiri ya Mlimani. Kulingana na Mathayo 5:1-12, mahubiri hayo yanatanguliwa na “Heri.” Lakini, kulingana na lugha ya Kigiriki, ambayo katika hiyo masimulizi ya Mathayo ya maisha ya kidunia ya Yesu Kristo yalitafsiriwa, zapasa kuitwa “Furaha.” Hata masimulizi ya Mathayo katika lugha ya Kiebrania yanatumia neno la Kiebrania linalomaanisha “furaha.”
3. (a) Je! mwandikaji wa Zaburi 119 alistahili kufurahia furaha ya pekee, inayosemwa na Yesu Kristo? Eleza. (b) Simulia maoni ya mtunga-zaburi kuelekea agano la Torati ambalo mpatanishi alikuwa Musa?
3 Mtu mmoja ambaye nyakati za kale alistahili kufurahia hizo furaha kama zilivyotajwa na Masihi Myahudi, Yesu Kristo, alikuwa mwandikaji mwenye kuongozwa na Mungu wa Zaburi 119, zaburi iliyo ndefu zaidi ya Biblia. Kwa kupatana na sababu alizotoa Yesu Kristo za kuwa wenye furaha, mtunga-zaburi alitambua uhitaji wake wa kiroho. Pia alikuwa mwenye kuomboleza, mwenye tabia pole, mwenye njaa na kiu ya uadilifu, mwenye rehema, alisutwa na kuteswa, na kila namna ya jambo baya lilisemwa juu yake kwa njia ya uongo. Aliandika zaburi hiyo mamia ya miaka kabla ya Wakati wa Kawaida wetu, taifa la Israeli lilipokuwa lingali chini ya agano la Torati ambalo nabii Musa alikuwa amepatanisha kati ya Yehova Mungu na taifa hilo mwaka wa 1513 K.W.K. kwenye Mlima Sinai. Kwa kufaa mtunga-zaburi huyo hakuona kosa kwenye Torati ya agano hilo, kwa maana ilikuwa imetolewa na Mungu. Yeye alijua sana kwamba mataifa ya kipagani yenye kuzunguka nchi ya Israeli pande zote hayakuwa na cho chote chenye kulinganika na Torati hiyo ya kimungu. Aliiona kuwa yenye kuangaza sana nuru ya maarifa, akasema katika mistari ya 105 na 130: “Neno lako ni taa ya miguu yangu, na mwanga wa njia yangu. Kufafanusha maneno yako kwatia nuru, na kumfahamisha mjinga.”
4. (a) Zaburi 119 imetungwa kwa utaratibu gani, na jambo hilo linasaidiaje? (b) Kwa kutaja “chuo cha zaburi,” Yesu na wanafunzi wake wanawekea nani kielelezo cha kufuatwa, na kwa kusudi gani?
4 Ili kusaidia kukumbusha, mtunga-zaburi aliifanya iwe zaburi yenye kufuatana kialfabeti, hata kwamba katika beti (vifungu) 22 kila ya mistari 8 ya Kiebrania unaanza kwa herufi ile ile ya Kiebrania, katika utaratibu wa alfabeti. Kwa hiyo kila mstari wa ubeti wa kwanza chini ya herufi ya kwanza ya Kiebrania Aleph ikiwa ndiyo kichwa unaanza kwa herufi hiyo ya kwanza Aleph. Kila mstari wa ubeti wa pili unaanza na herufi ya pili ya Kiebrania Beth. Inafululiza hivyo katika beti zote 22 za zaburi hiyo, kufuatana na herufi 22 za alfabeti ya Kiebrania. Kwa kuwa kila ubeti una mistari minane ya Kiebrania, beti zote 22 za zaburi hiyo zina mistari 176. Katika ufundishaji wake, Yesu Kristo mwenyewe alitaja “chuo cha Zaburi.” (Luka 20:42; 24:44) Aliwekea wanafunzi wake mfano wa kufuatwa katika jambo hilo.—Matendo 1:20; 13:33; 1 Wakorintho 14:26; Waefeso 5:19; Wakolosai 3:16; Waebrania 4:7; Yakobo 5:13.
5. Katika kuianza Zaburi 119, yaelekea mwandikaji alikuwa akifikiria mambo yaliyompata nani?
5 Bila shaka mtunga-zaburi aliandika mambo aliyojionea mwenyewe alipofungua Zaburi 119, kwa kusema: “Wenye furaha ni wale ambao njia yao haina kosa, wale wanaotembea katika sheria ya Yehova. Wenye furaha ni wale wanaoshika makumbusha yake . . . Katika njia zake wametembea. Wewe mwenyewe kwa kuamrisha umetoa maagizo yako yatunzwe kwa uangalifu. O kama njia zangu zingesimamishwa imara ili nitunze matakwa yako! Kwa sababu hiyo sipaswi kuona aibu, ninapoangalia amri zako zote. Nitakusifu kwa unyofu wa moyo, nijuapo maamuzi yako maadilifu ya hukumu. Matakwa yako naendelea kuyatunza. O usiniache kabisa.”—Zaburi 119:1-8, NW.
6. (a) Maneno makuu yanakaziwaje katika zaburi hiyo? (b) Mtunga-zaburi alikuwa mwanafunzi wa nini, na jambo hilo linathibitishwaje?
6 Katika ubeti huo wa kwanza wenye mistari 8 ya Kiebrania tunaona maneno makuu sheria, makumbusha, maagizo, kawaida, amri na maamuzi ya hukumu. Katika mistari yote 176 ya Kiebrania, mtunga-zaburi anakazia maneno hayo. Kwa mfano, anatumia neno “sheria” mara 25, “makumbusha” mara 22, “maagizo” mara 21, “kawaida” mara 21, “amri” mara 20, “maamuzi ya hukumu (uamuzi wa hukumu)” mara 21, na neno “amri” lenye kuhusiana na hilo likiwa limetumiwa mara mbili katika zaburi hiyo. Mtunga-zaburi ajaporudia kutumia maneno hayo ambayo huenda yakasikika kuwa ya kisheria, hakuna ushahidi wo wote kwamba kazi yake ilikuwa wakili wa sheria au hakimu. Kwanza kabisa yeye alikuwa mwanafunzi wa Neno la Yehova lililoandikwa, na uhakika huo unathibitishwa na matumizi yake ya usemi “neno lako” mara 15. Ikiwa yeye alikuwa mfalme wa taifa la Israeli, alikuwa chini ya amri ya kimungu aandike nakala ya kibinafsi ya Torati ya agano la Yehova pamoja na Israeli ili apate kujifunza mwenyewe na kuitumia. (Kumbukumbu la Torati 17:14-18) Mtunga-zaburi hakuona funzo la uangalifu la “neno” la Yehova akiwa anafikiria mambo hayo kuwa lenye kuchosha. Yeye alitamani kile ambacho kingemsaidia atii sheria. (Zaburi 119:40, 131, 174) Je! sisi tuko kama yeye?
7. (a) Kujua na kutembea katika sheria ya Mungu kunatufaidije sisi? (b) “Tora” inahusu nini, lakini Wakristo wako chini ya mpango gani?
7 Tunapolinganisha sheria za kimataifa na za kitaifa za nchi zilizo chini ya uongozi usioonekana wa ‘baba wa uongo,’ Shetani Ibilisi, na sheria ya Yehova, tunaweza kujiunga na mtunga-zaburi kwa kusema: “Sheria yako ni kweli. Ee [Yehova], Wewe u karibu, na maagizo yako yote ni kweli.” (Yohana 8:44; Zaburi 119:142, 151) Kwa hiyo kwa ‘kutembea katika sheria ya Yehova,’ sisi, kama mtunga-zaburi, tutalindwa tusitembee katika njia ya kosa la kilimwengu inayoweza kutuumiza, kimwili na kiroho. Kufanya hivyo kunatuletea furaha. (Zaburi 119:1, NW) Kufanya hivyo kunatuletea baraka na kibali ya kimungu. Jambo hilo ni lenye matokeo mioyoni mwetu, kama Zaburi 119:97, 126, 127 inavyoonyesha. Mtunga-zaburi alikuwa chini ya agano la Torati ya Musa lenye “Tora,” jumla ya sheria ya kimungu iliyotia ndani sheria nyingi zilizo tofauti. Mashahidi wa Yehova waliopakwa mafuta leo wako chini ya agano jipya (ambalo Mpatanishi wake ni Yesu Kristo) kama ilivyo, “sheria” ikiwa ‘imeandikwa katika mioyo yao.’ (Yeremia 31:31-34) Kwa kujifunza Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, wanaifahamu “sheria” ya agano jipya na amri zalo.
8. (a) Je! ulimwengu huu wenye kuvunja sheria una taraja la mambo mema? (b) Mtunga-zaburi alielezaje hangaiko lake lenye kutosha machozi juu ya kushindwa kwa Wayahudi kutunza Sheria ya Mungu? (c) Unabii wa Yesu kuhusu Yerusalemu usio mwaminifu ulitimizwaje, na jambo hilo ni kiishara cha nini kwa Jumuiya ya Wakristo?
8 Wakati unaofaa unakaribia kwa aliye kwa haki Mtoa-sheria, Yehova, kuchukua hatua juu ya ulimwengu huu wenye kuvunja sheria. Taraja lenye kutosha machozi liko mbele. Katika siku zake, mtunga-zaburi, akiwa mpenda-sheria ya Mungu, alilia kwa sababu ya hali hiyo. (Zaburi 119:136) Siku chache kabla ya kupatwa na kifo cha kikatili cha mfia-imani, Yesu Kristo alilia juu ya mji wa Yerusalemu wenye kutunza mapokeo lakini wenye kuvunja sheria. (Luka 19:41) Miaka thelathini na saba baada ya Wayahudi kuleta uvunjaji wao wa sheria kwenye upeo kwa kumfisha Masihi asiye na hatia, Yesu Kristo, mikononi mwa Mataifa, Yehova alichukua hatua. (Zaburi 119:126) Mambo ya maombolezo aliyotangulia kuona Yesu Kristo yaliupata mji huo mwaka wa 70 W.K. Leo kilichofananishwa na Yerusalemu, na Wayahudi ambao uliwatawala, kina hatia kwa kadiri kubwa zaidi. Jumuiya ya Wakristo, ambayo ndiyo mfano wa kisasa wa kuvunja sheria, ni kubwa zaidi sana ya Yerusalemu wa kale na taifa la Israeli. Katika njia yake mwenyewe Yehova atatia katika mioyo ya sehemu za kisiasa za ulimwengu huu zigeukie matengenezo yote ya kidini ya ulimwengu, kutia ndani Jumuiya ya Wakristo, ambao ni Ufalme wa Kristo ulio bandia.—Ufunuo, sura 17.
9. (a) Tofautisha mwendo wa Jumuiya ya Wakristo wa kumwaga damu na nia na mwenendo wa Mashahidi wa Yehova. (b) Mwendo wetu unapatana na kielelezo gani? (c) Kristo anaikataa Jumuiya ya Wakristo leo kwa sababu gani?
9 Je! vita viwili vya ulimwengu havikutokea katika Jumuiya ya Wakristo, na viongozi wake wa kidini wakiunga mkono mapigano kama hayo yenye kumwaga damu? Kwa kutofautiana sana na wavunjaji sheria hao wa agano jipya la Mungu, ambalo linaamuru upendo wa kidugu, mtunga-zaburi alisema hivi, kikiwa ni kielelezo cha kufuatwa na Mashahidi wa Yehova wa leo: “Ninachukia na kuchukizwa sana na uwongo; lakini ninapenda sheria yako.” (Zaburi 119:163, ZSB) Yeye alitamani kutunza sheria kwa moyo wote. Anaeleza kuchukia kwake nia mbili, nia ya uvuguvugu, akisema: “Ninachukia wenye nia mbili; lakini ninapenda sheria yako.” (Zaburi 119:113, ZSB) Hayo ndiyo maoni ya Yesu Kristo kulekea Jumuiya ya Wakristo leo, kwa maana inafanana na kundi la Laodikia wa kale. Kwa haki anaweza kusema hivi kwa Jumuiya ya Wakristo: “Kwa sababu una uvuguvugu, wala hu baridi wala moto, nitakutapika utoke katika kinywa changu.” (Ufunuo 3:16) Hatuwezi kuwa tukiupenda ulimwengu wenye kuvunja sheria, usiopenda na kumpenda Kristo wakati huo huo. Hakuna cha kuwa na nia mbili. Upendo mchangamfu wapasa kuwa nguvu yenye kuchochea utii kwa Mungu. Yehova hangeweza kamwe kumwongoza kwa roho yake, mtumishi wake mwenye kumtumikia kwa moyo wote aseme jambo lenye kichocheo kinachopungua hiki: “Nitajifurahisha sana kwa maagizo yako, ambayo nimeyapenda.”—Zaburi 119:47.
10. (a) Tunapaswa tupende sana nini, kama mtunga-zaburi? (b) Taabu aliyopata mtunga-zaburi ilikusudiwa kufanya nini, lakini yeye alishikilia mwendo gani, na jambo hilo lina matokeo gani kwetu?
10 Kupenda kwetu sana sheria ya Yehova kunaongoza kwenye wokovu. Mtunga-zaburi alikubali hilo aliposema: “Kama sheria yako isingalikuwa furaha yangu, hapo ningalipotea katika taabu zangu.” (Zaburi 119:92) Taabu yake haikuwa ugonjwa fulani wenye kuua. Yeye alikuwa katika taabu ya wenye kujitanguliza (mbele za Mungu), waliokuwa wakimchukia na kumtesa. Akiwa chini ya mkazo angaliweza kushindwa na malengo ya Waisraeli hao na kwenda kinyume cha mapenzi ya Yehova kama hangekuwa anapenda sheria ya Mungu sana. Mtunga-zaburi ni mfano mzuri kama nini kwetu leo tulio chini ya mkazo kama huo kutoka kwa ulimwengu ambao uvunjaji wa sheria ni tele kwa kadiri ambayo upendo wa wengi wa wanadamu umepoa wakati wa huu umalizio wa mfumo wa mambo!—Mathayo 24:3, 12.
11. Wokovu wetu unatokana na nini, na kwa hiyo tunaionaje mipango ya kibinadamu?
11 Ni kwa kutunza sheria ya Mungu tu ndipo tunapokuwa na msingi wa kutazamia kuokolewa milele. Tunataka sana kuokolewa tuingie katika mfumo mpya wa Mungu wa mbingu mpya na dunia mpya. Karibu na mwisho wa Zaburi 119, mstari’ wa 174 unasema hivi kwa niaba yetu: “Ee [Yehova], nimeutamani wokovu wako, na sheria yako ndiyo furaha yangu.” Kwa hiyo, tunakataa mipango iliyokusudiwa ya wanadamu ya wokovu wa ulimwengu huu wenye kuvunja sheria, usio na upendo.
Wenye Kutii Sheria Katika Mateso
12. (a) Kuteswa kwa “mwanamke” na “uzao” wake kunachochewa na kutekelezwa na nani, na kwa sababu gani? (b) Watesi wamekemewaje?
12 Kuteswa kwa Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote kulitabiriwa kungekuwako wakati wa hizi siku za mwisho za huu mfumo wa mambo wa kale unaokufa chini ya utawala wenye kuendelea wa upinzani wa joka wa mfano, Shetani Ibilisi. Ufunuo 12:17 linaonyesha ni wa nani anashambulia, kwa kusema: “Joka akamkasirikia yule mwanamke [tengenezo la Yehova lililo kama mke], akaenda zake afanye vita juu ya wazao wake waliosalia [zaidi ya Ufalme uliotoka kuzaliwa], wazishikao amri za Mungu, na kuwa na ushuhuda wa Yesu.” Kwa sehemu kubwa mateso yanatoka kwa wale wanaoenda njia nyingine mbali na yale ambayo Mungu anaamuru kwa ajili ya hizi siku za mwisho wa mfumo wa mambo uonekanao wa joka ulio duniani. Kupitia ujumbe wa Ufalme unaotangazwa ulimwenguni pote na Mashahidi wa Yehova, Yehova amewakemea hao waliolaaniwa, sawa na Zaburi 119:21 inavyosema: “Umewakemea wenye kiburi, wamelaaniwa waendao mbali na maagizo yako.” Kisa cha waaminifu ambao watesaji hao wenye kujitanguliza wanasuta na kutukana ni tofauti kabisa. Ni kama ilivyokuwa kwa mtunga-zaburi: “Wenye kiburi wamenidharau mno, sikujiepusha na sheria zako.”—Zaburi 119:51.
13. (a) Yajapokuwa makusudi maovu ya watesi, kutunza sheria ya Mungu kunaongoza kwenye matokeo gani? (b) Jambo hilo limeonyeshwaje katika nyakati za kisasa?
13 Kwa kuona kwamba Mashahidi wa Yehova wanasonga kwa upatano na sheria ya Yehova kwa wakati huu, watesi wenye kujitanguliza (wenye kiburi) wanajaribu kuangusha Mashahidi wenye kutii sheria, kama vile tu ilivyoonyeshwa katika kisa cha mtunga-zaburi, aliyesema: “Wenye kiburi wamenichimbia mashimo, ambao hawaifuati sheria yako.” (Zaburi 119:85) Kuaibisha wenye hila wanaojitanguliza hakumaanishi tu kufunua njia zao zenye kupoteza, bali pia hasa, kumtetea Yehova kuwa ndiye Mungu wa kweli. Kwa hiyo bila kutamani kulipiza kisasi mtunga-zaburi angeweza kusali hivi: “Wenye kiburi waaibike, maana wamenidhulumu kwa uongo, mimi nitayatafakari mausia [maagizo] yako.” (Zaburi 119:78) Yehova huhakikisha kwamba hata mateso yanaleta faida na kwamba watesi hawapati faida yo yote kwa hila. Yeye anajibu sala ya Zaburi 119:122 hivi: “Uwe mdhamini wa mtumishi wako, apate mema, wenye kiburi wasinionee.” Kifo chenye kumaliza wengi kilielekea Mashahidi wa Yehova wakati wa tawala za kimabavu za Benito Mussolini na Adolf Hitler, lakini kwa kutosahau sheria na amri za Mungu wao, walisimama imara na wengi waliokoka. Waokokaji wanaweza kusema hivi, kwa maneno ya Zaburi 119:60, 61: “Nalifanya haraka wala sikukawia, kuyatii maagizo yako. Kamba za wasio haki zimenifunga, sikuisahau sheria yako.” Mungu Mweza Yote anaweza kukata au kuvunja-vunja kamba za kizuizi walizofungwa Mashahidi wake na maadui wao na kwa njia hiyo aweke huru watumishi wake katika wakati wake mwenyewe kwa ajili ya kazi ambayo amewaagiza rasmi wafanye wakati wa huu umalizio wa mfumo wa mambo.
14. (a) Kama vile kisa cha mtunga-zaburi, Mashahidi wa Yehova wamepatwa na nini, na matokeo ya jitihada za maadui wao yamekuwa nini? (b) Ni nani wanaoweza kufurahia mateso yao, na kwa sababu gani?
14 Kulingana na maneno yake katika Zaburi 119:84, 86, 161, mtunga-zaburi alipatwa na mateso mengi hata kutoka kwa wananchi wenzake. Mashahidi wa Yehova wamepatwa na mateso ndani na nje ya nchi za Jumuiya ya Wakristo ambamo kwa wakati huu wako chini ya marufuku. Hata hivyo, maadui wameshindwa katika kusudi la mateso yao ya hila, ya dhuluma! Kwa mshangao wa maadui, Mashahidi wa Yehova “wanaotembea katika sheria ya Yehova” na “wanaoshika makumbusha yake” wanachochewa wafurahie mateso yao kwa ajili ya Yehova Mungu na Kristo wake. Wanakumbushwa juu ya yale ambayo Yesu Kristo alisema katika orodha yake ya furaha: “Wenye furaha ni ninyi maskini, kwa sababu ufalme wa Mungu ni wenu. Wenye furaha ni ninyi wakati wo wote watu wanapowachukia, na wakati wo wote wanapowatenga na kuwasuta na kulitupa nje jina lenu kuwa ni ovu kwa ajili ya Mwana wa mtu. Furahini siku hiyo na kuruka, kwa maana, tazama! zawadi yenu ni kubwa mbinguni, kwa maana mambo hayo ni yale yale mababu zao walikuwa wakifanyia manabii [kutia mtunga-zaburi].” (Zaburi 119:1, 2, NW; Luka 6:20, 22, 23, NW) Wakishiriki furaha ya Yehova, Mashahidi wake wenye kuteswa wanaendelea “kuitukuza sheria, na kuiadhimisha.”—Isaya 42:21.
Faida Katika Zaburi 119
◻ Zaburi 119 imepangwaje, na kwa sababu gani?
◻ Mtunga-zaburi alirudia kutumia maneno gani ya pekee?
◻ Sisi, tofauti na Jumuiya ya Wakristo, tuna maoni gani juu ya sheria ya Mungu?
◻ Tunapaswa kupenda nini, yajapokuwa mateso ya Wakristo?
[Picha katika ukurasa wa 14]
Mtunga-zaburi alithamini sana kwamba kujua na kufuata Neno la Mungu kunaweza kuleta furaha
[Picha katika ukurasa wa 16]
Wengi wa Mashahidi wa Yehova walisimama imara na kuokoka mateso ya Nazi. Wangeweza kusema hivi kwa furaha: “Sikuisahau sheria yako”