Usalama—Unaweza Kupatikana Wapi?
VIJANA hao wawili walikuwa wenye kuona uchungu, wamehuzunika sana—na bila kazi ya kuajiriwa. Kulingana na gazeti Time, walikuwa “wameunganisha paipu na mtaimbo wa kutolea moshi, wakaingiza [paipu hiyo] ndani ya kijumba cha abiria na kuzuia nafasi kwenye madirisha kwa kutumia matambara.” Barua yao ya kueleza sababu ya kujiua ilikuwa yenye kuogopesha sana: “Sasa tuko hai kwa kusudi gani na hakuna kazi mtu ye yote apate kuajiriwa?”
Ripoti kama hiyo zinaonyesha kadiri kubwa ya watu kujisikia kukatishwa tamaa leo. Sisi sote, katika njia hii au hii, tunaumizwa na kupanda kwa bei za bidhaa, ukosefu wa kazi ya kuajiriwa na mzigo wa kodi yenye kupanda wakati wote. Kwa jamaa nyingine hiyo inataka wake waende kazini, na katika visa vingine hata watoto. Kwa wengine imemaanisha kufanya mabadiliko makubwa ya tabia za kula, tafrija na nyumba za kuishi. Hata fedha katika benki si uhakikisho wa usalama kwa sababu ya matokeo ya bei za bidhaa kupunguza thamani yake. Kwa kufaa Biblia ilitabiri kwamba hizi zingekuwa “nyakati za hatari.”—2 Timotheo 3:1-5.
Hata matajiri wanapatwa na upungufu wenye kuletwa na kupanda kwa bei za bidhaa. (Ufunuo 6:6) Ili kuzuia kupunguka kwa thamani ya fedha, wengine wanaweka raslimali katika hisa, mashamba na majengo, fedha za kigeni au vito vya thamani. Lakini hata walio wajuzi zaidi wa kuweka raslimali wamefumaniwa na mabadiliko ya ghafula yasiyotazamiwa. Kwa mfano, kumbuka jinsi bei ya dhahabu ilivyoshuka mbio-mbio katika siku chache tu, kutoka dola 875 kwa aunzi moja mpaka dola 650, na baadaye chini ya dola 300 (za U.S.). Kwa hiyo wenye kuweka akiba wanalazimishwa kuangalia raslimali zao kwa makini na kwa wasiwasi. Tunakumbushwa juu ya maneno ya Biblia katika Mhubiri 5:12: “Kushiba kwake tajiri hakumwachi kulala usingizi.”
“Wasijue Njia ya Kutokea”
Lakini, je, wanauchumi wanaweza kuongoza kwenye njia ya kutoka kwenye mvurugo huo? Wawezeje na kuna kutokubaliana kwingi sana kati yao? Kwa mfano, mataifa jirani Uingereza na Ufaransa, yamefuata mashauri ya washauri wakubwa wa kwao. Lakini mataifa hayo mawili yanafuata maongozi ya kiuchumi yaliyo tofauti kabisa. Uingereza inajaribu kupunguza kushuka kwa thamani ya fedha kwa kupunguza matumizi ya serikali na kuruhusu raslimali zenye kuleta mapato makubwa. Lakini Ufaransa inajiweka katika hatari ya thamani ya fedha kupunguka kwa ‘kutumia akiba zote za kitaifa’ na kutumia fedha nyingi ili kutokeza nafasi za kazi. Likieleza juu ya tofauti hizo, gazeti Time lilisema, ‘Kwa wengi falsafa hizo zenye kutofautiana sana zina uwezekano ule ule wa kufaulu.’
Kwa usahihi Biblia ilitabiri kwamba kungekuwako “huzuni kuu ya mataifa, wasijue njia ya kutokea.” (Luka 21:25, NW) Kwa hiyo ikiwa hata viongozi wa ulimwengu wenyewe wanavurugwa na taabu za uchumi wa ulimwengu, mtu wa kawaida kama wewe, ana uwezekano gani wa kuokoka? Je! kuna chanzo cho chote chenye kutegemeka cha kushauri? Je! kuna raslimali zisizo na kasoro zinazoweza kutoa uhakikisho wa wakati ujao salama?