Kumbukumbu la Torati Kinatusihi Tumtumikie Yehova kwa Furaha ya Kutoka Moyoni
WAABUDU wa Yehova lazima wamtumikie kwa uaminifu na kwa furaha ya kutoka moyoni. Kitabu cha Kumbukumbu la Torati kinaonyesha hilo waziwazi. (Kumbukumbu la Torati 28:45-47) Na kusihi kwacho juu ya kufanya utumishi wa uaminifu na wenye furaha, kuna maana kubwa katika maisha ya mashahidi wa Yehova wa karne ya 20.
Kitabu cha Kumbukumbu la Torati kiliandikwa na nabii Mwebrania, Musa, kwenye nyanda za Moabu mwaka wa 1473 K.W.K. na kinazungumza juu ya matukio ya miezi miwili hivi. Inaelekea kwamba sura ya mwisho iliongezwa na Yoshua au Kuhani Mkuu Eleazari. Kitabu cha Kumbukumbu la Torati ni chenye hotuba nne, na pia wimbo mmoja na baraka aliyosema Musa wakati Israeli walipokuwa wanakaribia kuingia Nchi ya Ahadi. (Kumbukumbu la Torati 1:3; Yoshua 1:11; 4:19) Katika Kumbukumbu la Torati Musa alieleza na kufafanua juu ya mambo fulani ya Torati. Kati ya mambo mengine, kitabu hicho kinaonyesha kwamba Yehova anadai ibada kamili. Pia kinaonya juu ya ibada ya uongo na kusihi watu wa Mungu wawe waaminifu katika utumishi wake mtakatifu.
Lakini, maandishi yaliyomo katika Kumbukumbu la Torati yaliwasaidia Waisraeli katika njia zipi hasa? Na kitabu hicho kinaweza kufaidije Mashahidi wa Yehova leo?
Waisraeli wamekuwa jangwani kwa miaka 40 hivi wakati Musa anapowahutubia sasa. Kwa sehemu fulani, anasimulia juu ya kuwekwa rasmi kwa waamuzi ili wamsaidie. Anataja juu ya ile ripoti mbaya ya wapelelezi kumi iliyotokeza uasi na kutanga-tanga jangwani. Pia, ushindi mbalimbali aliowapa Mungu unarudiwa. Musa anaonya juu ya kufanya sanamu na kukazia hilo kwa kusema (NW): “Yehova Mungu wako ni moto ulao, Mungu anayetaka ibada kamili.” Hilo linafuatishwa na kusihi kwamba wamtii Yehova.—Kumbukumbu la Torati 1:1–4:49.
Katika hotuba ya pili, kwanza Musa anarudia kutaja yale Maneno Kumi (Amri Kumi) na kusimulia tena juu ya kutolewa kwa Torati. Mkazo unatiwa juu ya kumpenda Yehova kwa moyo wote, nafsi yote na nguvu zote za uhai. Kuagiza watoto kunakaziwa. Mataifa saba ya Kanaani na mabaki yayo ya ibada ya uongo yakusudiwa uharibifu. Waisraeli waambiwa kwamba walichaguliwa si kwa sababu ya uadilifu wao bali kwa ajili ya uaminifu wa Yehova akiwa mtunza-agano. Wakiisha kuingia Nchi ya Ahadi, lazima wadumu wakiwa watiifu na wasimsahau Mungu. Maelezo ya visa vya kukosa utii yanarudiwa, na upendo wa kutoka moyoni na kumwogopa Mungu zaonyeshwa kuwa za lazima. Baraka na laana zawekwa mbele ya Israeli, na utii kwa Mungu unatiwa moyo.—Kumbukumbu la Torati 5:1–11:32.
Halafu sheria zinazohusu maisha katika Nchi ya Ahadi zinatajwa. Kati yazo kuna maagizo ya kuharibu mabaki ya dini chafu, kula nyama na kushughulika na damu, kushughulika na manabii wa uongo na uasi-imani, vyakula safi na vichafu na kutoa zaka (sehemu ya kumi). Maelezo ya kirefu yanatolewa juu ya kujiondoa katika deni, utumwa na wazaliwa kwanza wa wanyama. Sikukuu tatu za kila mwaka zinazungumzwa, pia mambo fulani ya hukumu na sheria zinazohusu wafalme na Walawi. Baada ya maonyo juu ya kupashana habari na mashetani, nabii wa mfano wa Musa anatabiriwa.—Kumbukumbu la Torati 12:1–18:22.
Kati ya maagizo mengine yanayoendelea kutajwa ni yale yanayohusu miji ya makimbilio, watu ambao si lazima wajiunge na jeshi, kutakasa na hatia ya damu, kuoa wanawake mateka, haki ya mzaliwa wa kwanza, wana waasi, kuheshimu mali ya wengine na kuheshimu uhai, mambo yanayohusu ngono na mtu kutostahili kuwa mshiriki katika kundi. Na bado sheria nyingine zinatia ndani zile zinazohusu watumwa, riba na nadhiri. Maagizo juu ya mambo kama talaka, mikopo, fadhili kwa watoto wasio na baba na wajane, ndoa ya ndugu-mkwe, vipimo vya haki, kutoa sadaka malimbuko (matunda ya kwanza) na zaka (sehemu ya kumi) yanamalizia hotuba hiyo.—Kumbukumbu la Torati 19:1–26:19.
Hotuba ya tatu ya Musa inaanza na maagizo juu ya kuandika Torati juu ya mawe makuu. Baraka zitatajwa kutoka juu ya Mlima Gerizimu na laana kutoka juu ya Mlima Ebali. Kisha baraka za kutii amri za Mungu zinatofautishwa na laana zinazopasa kutazamiwa kwa sababu ya kutokutii.—Kumbukumbu la Torati 27:1–28:68.
Kwa kukamatana na hotuba ya nne ya Musa, agano kati ya Yehova na Waisraeli linafanywa upya. Musa asimulia tena uangalizi wa Mungu jangwani. Onyo latolewa juu ya kutokutii na rehema ya Yehova inakaziwa. Mwishowe, uchaguzi kati ya uzima na kifo unatolewa. Watu wa Israeli wanaweza kuendelea ‘kuishi kwa kumpenda Yehova, kusikiliza sauti yake na kushikamana naye.’—Kumbukumbu la Torati 29:1–30:20.
Musa anawatia moyo Waisraeli wawe hodari wanapoingia Nchi ya Ahadi, kwa maana Yehova anapiga hatua pamoja nao. Kuagizwa kwa Yoshua awe kiongozi kunafuatiwa na unabii unaohusu uasi wa Israeli. Halafu, katika wimbo, Musa anamkuza Yehova, atabiri ole kwa ajili ya kukosa uaminifu kwa Israeli lakini amalizia kwa uhakikisho wa kisasi ya kimungu pamoja na wito, “Furahini, enyi mataifa, pamoja na watu wake.” Musa atoa baraka za mwisho, kisha nabii huyo mwenye miaka 120 aitazama Nchi ya Ahadi, anakufa na kuzikwa na Yehova katika kaburi lisilo na alama.—Kumbukumbu la Torati 31:1–34:12.
Muhtasari unaotangulia huenda ukachochea hamu yako ya kiroho. Lakini unaposoma Kumbukumbu la Torati, huenda maulizo fulani ya maana yakatokea. Ebu tuwazie mengine yayo sasa na kuyajibu.
Hotuba ya Kwanza ya Musa
• 4:15-24—Je! maneno hayo ya kukataza kufanya sanamu yanamaanisha kwamba ni kosa kuonyesha picha za mtu?
Mistari hiyo inakataza kufanya mifano kwa ajili ya ibada ya uongo. Lakini Waisraeli hawakukatazwa wasifanye mifano kwa ajili ya makusudi mengine. Kwa mfano, kulikuwako kwa ruhusa ya Mungu mfano wa makerubi juu ya vitambaa vya hema la ibada na juu ya kifuniko cha sanduku takatifu. Ingekuwa si sawa kushirikisha kawaida ya upigaji na uonyeshaji wa picha na ibada ya sanamu, isipokuwa zitumiwe kwa ajili ya makusudi ya ibada ya uongo. Kwa kawaida, hakuna kipingamizi cha Kimaandiko cha kupiga picha, kuchora na kuchonga vitu ambako kuna kusudi linalofaa au kusudi la sanaa ya kuonyesha jinsi walivyo watu au vitu.
Hotuba ya Pili ya Musa
• 6:6-9—Je! amri hiyo ya ‘kufunga sheria ya Mungu juu ya mkono’ yapasa kueleweka kihalisi?
Mistari hiyo haiungi mkono zoea la kuvaa vifuniko vidogo vyenye maandishi ya Biblia. Badala yake, matumizi ya maneno hayo yana maana ya mfano. (Linganisha Kutoka 13:9; Mithali 7:2, 3.) Haisemwi kwamba amri hizo zingepasa kuandikwa juu ya kitu fulani halafu zivaliwe na mtu au kufungwa juu ya miimo ya milango na malango. Waisraeli walipaswa kufikiria amri za Mungu nyakati zote, wawe walikuwa nyumbani, barabarani au karibu na malango ya mji, ambako wazee walishughulikia kesi zenye kutaka hukumu. Walipaswa kuweka sheria ya Mungu katika moyo, na kuifundisha kwa watoto wao na kuonyesha kwa vitendo (kama inavyofananishwa na mikono) kwamba walishikamana nayo. Watu hao walipaswa kujitambulisha peupe kuwa ni wenye kutegemeza sheria ya Yehova, kama kwamba ilikuwa imeandikwa katikati ya macho yao ili wote waone. Vivyo hivyo, Mashahidi wa Yehova leo wanatafuta kujithibitisha kuwa watumishi watiifu wa Mungu. Mioyo yao inawachochea watii Neno lake, na wanajaza mioyo yao kwa mambo ambayo ni ya kweli, ya kuhangaikiwa kwa uzito, ya uadilifu, yenye kupendeka, ya wema na ya kusifika. Katika kila njia wanajitahidi kuonyesha kwamba amri za Yehova ziko mbele yao nyakati zote.—Wafilipi 4:8, NW; Wakolosai 3:23.
• 8:3, 4—Je! hiyo maana yake ni kwamba tu mavazi ndiyo waliyopewa yalipokwisha?
Uandalizi wa mana ulikuwa muujiza wenye kuendelea. Ndivyo pia ulivyokuwa uhakika wa kwamba mavazi hayakuchakaa wala miguu yao haikuvimba wakati wa miaka 40 jangwani. Ikiwa tu mavazi yaliletwa mengine kwa njia ya kawaida, huo haungekuwa muujiza. Hakungekuwako tatizo lo lote katika kutumia mavazi yale yale kwa miaka hiyo yote, kwa sababu mavazi ya watoto yangeweza kupokezwa kwa watoto wachanga zaidi na mavazi yangeweza kupatikana kwa matumizi ya wengine, watu wazima walipokufa. Kwa kuwa hesabu ya Waisraeli karibu ilikuwa ile ile mwishoni mwa safari yao ya mguu jangwani kama ile iliyokuwako mwanzoni, mavazi yale yale yaliyokuwa mwanzoni yangekuwako wakati wa miaka ile yote 40.—Hesabu 2:32; 26:51.
• 14:21—Kwa kuwa Waisraeli hawangeweza kula “nyamafu yo yote,” sababu gani angeweza kupewa mgeni au kuuziwa mtu wa nje?
Akiwa Mtoa-sheria Mkuu Zaidi, Yehova alikuwa na haki ya kuwekea Waisraeli peke yao vizuizi fulani. Wao walikuwa “taifa takatifu” kwake. Mataifa mengine hawakufuata katazo hilo la kutokula mnyama aliyejifia mwenyewe. Hakukuwa ukosefu wo wote wa haki kumpa mgeni mnyama mfu asiyemwagwa damu wala kumuuzia mtu wa nje, kwa maana Waisraeli hawakupotoa mambo na mpokeaji au mnunuzi alitenda kwa hiari yake mwenyewe. Inaweza kuongezwa kwamba Kumbukumbu la Torati 14:21 inapatana na Mambo ya Walawi 17:10, ambapo palikataza mgeni kula damu. Mgeni aliyekuwa mwongofu alipaswa asile damu, lakini katazo hilo halikuhusu mgeni ambaye hakuwa mwongofu kamili. Mtu kama huyo angeweza kutumia mzoga wa mnyama aliyekuwa hajamwagwa damu katika njia zilizoonwa kuwa najisi na Mwisraeli mwaminifu au mwongofu.
• 17:5-7—Kwa sababu gani lilikuwa takwa kwamba mashahidi ndio waliopaswa kuinua mkono kwanza juu ya mtu aliyekuwa amehukumiwa kifo?
Kila mtu katika Israeli alipaswa kuwa mwenye bidii kwa ajili ya ibada ya kweli na kuhangaikia kuona kwamba tengenezo lilibaki likiwa safi na kwamba hakuna suto lo lote lililoletwa juu ya jina la Yehova. Mashahidi walipaswa kuonyesha bidii hiyo kwa kuongoza katika kutekeleza hukumu hiyo. (Linganisha Hesabu 25:6-9; Kumbukumbu la Torati 13:6-11.) Bila shaka, lilikuwa jambo moja kushuhudia juu ya mtu fulani na lilikuwa jambo jingine kabisa kumuua mtu. Hilo lingemfanya shahidi afikirie kwa uangalifu sana katika kutoa ushahidi, na ni mtu mwovu tu ambaye angeweza kutoa ushuhuda wa uongo akijua kwamba ndiye angekuwa wa kwanza kuchukua hatua ya kumuua mwanamume au mwanamke huyo. Mashahidi wa Yehova wanaweza kutumia kanuni hizo kwa kuwa wenye bidii kwa ajili ya usafi wa kundi na pia kuwa waangalifu sana watoe ushahidi wa kweli. Ingawaje, kila mmoja wetu atapaswa kutoa jibu kwa Hakimu Mkuu Zaidi, Yehova.—Mathayo 12:36, 37.
• 22:5—Kwa sababu ya katazo hilo, je, ni sawa mwanamke akivaa suruali ndefu?
Kwa wazi kusudi la sheria hiyo lilikuwa ni kuzuia kutumia vibaya jinsia tofauti-tofauti na kuzuia mvurugo wa kutojua jinsia ya mtu. Katika sura na mavazi, kwa kawaida mwanamume anataka kuonekana ni wa kiume na mwanamke ni wa kike. Kwa Mwisraeli kutenda kinyume cha maoni hayo ya kindani ya uungwana ingaliweza kusababisha watu wa jinsia moja kulalana. Ingawa wakati huo wanaume na wanawake walikuwa wakivaa kanzu, kulikuwako tofauti kati ya vazi la waume na la wake. Vivyo hivyo, katika sehemu fulani za dunia leo, wanaume na wanawake wanavaa suruali ndefu, ingawa mitindo inatofautiana ikitegemea jinsia yao. Kanuni katika andishi hili haikatazi wanawake kuvaa suruali ndefu nyakati fulani, kama wanapofanya kazi nyumbani au shambani. Na kulingana na desturi ya mahali na kama hali inataka hivyo, suruali ndefu zaweza kuwa ndiyo mavazi yanayofaa katika sehemu zenye baridi sana. Biblia inawashauri wanawake “wajipambe kwa mavazi ya kujisitiri, pamoja na adabu nzuri, na moyo wa kiasi.”—1 Timotheo 2:9, 10.
• 24:6—Kutwaa jiwe la kusagia la juu wala la chini kuwa rehani, kungewezaje kuwa kama kutwaa nafsi (maisha)?
Kwa kawaida, mkate uliokwa kila siku na wakati mwingi ilikuwa lazima kusaga nafaka iwe unga. Kwa hiyo mkate wa kila siku wa jamaa ulitegemea jiwe la kusagia. Basi, kwa rehema, sheria ya Mungu ilikataza kutwaa jiwe la kusagia la mtu la juu wala la chini. Kutwaa lo lote la hayo kungesababisha jamaa ikose mkate wayo wa kila siku na kungekuwa ni kama kutwaa “maisha” au “riziki.”
Hotuba za Mwisho, Wimbo na Baraka
• 32:39—Inawezaje kuwa hakuna miungu pamoja na Yehova na huku Yohana 1:1 ni andiko linalosema kwamba ‘Neno alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa mungu’?
Maandishi hayo yanazungumza juu ya mambo tofauti kabisa. Jambo linalosemwa katika Kumbukumbu la Torati 32:39 ni kwamba miungu ya uongo haina shirika pamoja na Mungu wa kweli, Yehova, katika matendo yake ya kuokoa. Haiwezi kuokoa waabudu wayo kutoka kwa msiba, na miungu hiyo haikuwa na Yehova katika jambo lo lote alilofanya. Ingawa “Neno” ni mungu au mwenye uwezo mkuu, hampingi Yehova wala kuwa mshindani na yeye, kama ilivyokuwa kwa miungu ya uongo.—Kumbukumbu la Torati 32:12, 37, 38.
• 33:1-29—Kwa sababu gani Simeoni hatajwi katika baraka hii?
Simeoni na Lawi walikuwa wameshirikiana katika tendo la ukatili, na ingawa walipewa posho katika Israeli, hazikuwa kama za yale makabila mengine. Walawi walipewa miji 48 katika nchi yote, nayo sehemu ya Simeoni ilikuwa ndani ya eneo la Yuda. (Mwanzo 34:13-31; 49:5-7; Yoshua 19:9; 21:41, 42) Kwa hiyo Musa alipogeuzia Yuda fikira zake, alijua sana kwamba posho la Simeoni lilikuwa sehemu ya lile lake. Zaidi ya hayo, kabila la Simeoni lilitiwa ndani ya baraka ya jumla: “U heri, Israeli. Ni nani aliye kama wewe, taifa lililookolewa na [Yehova]!”—Kumbukumbu la Torati 33:29.
Ni Chenye Msaada wa Kudumu kwa Watumishi Waaminifu
Kitabu cha Kumbukumbu la Torati ni chenye faida ya kudumu kwa watumishi wa Yehova, na tunaweza kupata maagizo yenye thamani katika hicho. Kwa mfano, wakati wa uvamizi wa Kanaani, Yoshua alifuata kikamilifu mashauri ambayo sasa yameandikwa katika kitabu hicho. Vivyo hivyo, twapaswa kukubali kwa utayari uongozi wa kimungu. (Kumbukumbu la Torati 20:15-18; 21:23; Yoshua 8:24-29) Yesu Kristo alitaja maneno kutoka Kumbukumbu la Torati alipompinga Shetani kwa kufanikiwa. Kama Yesu, tunakubali kwamba mtu lazima aishi kwa usemi wa Yehova, kwamba hatupaswi kumjaribu Mungu na kwamba ni lazima tumtolee yeye peke yake ibada takatifu.—Mathayo 4:1-11; Kumbukumbu la Torati 5:9; 6:13, 16; 8:3.
Kitabu hicho kinamtambulisha Yehova kuwa Mungu anayetaka ibada kamili. (Kumbukumbu la Torati 4:24; 6:15) Pia kinatangaza hivi: “Nawe mpende [Yehova], Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa [nafsi] yako yote, na kwa nguvu zako zote.” (Kumbukumbu la Torati 6:5) Basi, kwa kweli kitabu cha Kumbukumbu la Torati kinatusihi tumtumikie Yehova kwa uaminifu. Kwa hiyo, sisi na tumtolee ibada takatifu kwa furaha inayotoka moyoni.