Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 6/15 kur. 12-17
  • Baraka au Laana—Kuna Chaguo!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Baraka au Laana—Kuna Chaguo!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Baraka Zafanywa Ziwezekane
  • Namna Gani Laana?
  • Tamko la Baraka na Laana
  • Kuchunguza kwa Ukaribu Zaidi
  • Chaguo la Israeli Lilileta Matokeo Tofauti
  • Kumbukumbu la Torati Kinatusihi Tumtumikie Yehova kwa Furaha ya Kutoka Moyoni
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Baraka au Laana—Vielelezo kwa Ajili Yetu Leo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • ‘Chagua Uzima Ili Uendelee Kuwa Hai’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Kitabu Cha Biblia Namba 5—Kumbukumbu La Torati
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 6/15 kur. 12-17

Baraka au Laana—Kuna Chaguo!

“Nimekuwekea mbele yako uzima na mauti, baraka na laana; basi chagua uzima, ili uwe hai.”—KUMBUKUMBU LA TORATI 30:19.

1. Ni uwezo gani waliopewa wanadamu?

YEHOVA MUNGU alikusudia sisi—viumbe vyake vya kibinadamu vyenye akili—tuwe wajumbe wenye hiari ya kuchagua. Sisi hatukuumbwa tuwe mashine tu, au roboti, bali tulipewa pendeleo na daraka la kufanya machaguo. (Zaburi 100:3) Wanadamu wa kwanza—Adamu na Hawa—walikuwa huru kuchagua mwendo wao, nao walipaswa kumtolea Mungu hesabu kwa ajili ya chaguo lao.

2. Adamu alifanya chaguo gani, na tokeo likawa nini?

2 Muumba ameandaa kwa wingi ili uhai wa kibinadamu uwe wenye baraka za daima kwenye dunia iliyo paradiso. Kwa nini kusudi hilo halijatimizwa bado? Kwa sababu Adamu alifanya chaguo baya. Yehova alikuwa amemwamuru huyo mwanadamu hivi: “Matunda ya kila mti wa bustani waweza kula, walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.” (Mwanzo 2:16, 17) Ikiwa Adamu angalichagua kutii, wazazi wetu wa kwanza wangalibarikiwa. Kutokutii kulileta kifo. (Mwanzo 3:6, 18, 19) Kwa hiyo dhambi na kifo zimepitishwa kwa wazao wote wa Adamu.—Warumi 5:12.

Baraka Zafanywa Ziwezekane

3. Mungu aliandaaje uhakikishio kwamba kusudi lake kwa ajili ya wanadamu lingetimizwa?

3 Yehova Mungu alifanyiza njia ambayo kwayo kusudi lake la kubariki wanadamu lingetimizwa hatimaye. Yeye mwenyewe alitabiri kuhusu Mbegu, akitoa unabii hivi katika Edeni: “Nami nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako na uzao wake [“mbegu yako na mbegu yake,” NW]; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino.” (Mwanzo 3:15) Baadaye Mungu aliahidi kwamba baraka zingewajia wanadamu watiifu kupitia Mbegu hiyo, mzao wa Abrahamu.—Mwanzo 22:15-18.

4. Yehova amefanya mpango gani kwa ajili ya kubariki wanadamu?

4 Mbegu hiyo ya baraka iliyoahidiwa ilithibitika kuwa Yesu Kristo. Kuhusu fungu la Yesu katika mpango wa Yehova wa kubariki wanadamu, mtume Mkristo, Paulo, aliandika hivi: “Mungu aonyesha pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi.” (Warumi 5:8) Baraka zitafurahiwa na wale kati ya wanadamu wenye dhambi wanaomtii Mungu na kujinufaisha wenyewe na fadhili za dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo. (Matendo 4:12) Je, utachagua utii na baraka? Kutokutii kutakuwa na matokeo yaliyo tofauti kabisa.

Namna Gani Laana?

5. Maana ya neno “laana” ni nini?

5 Kinyume cha baraka ni laana. Neno “laana” lamaanisha kusema vibaya juu ya mtu fulani au kutamka maovu dhidi yake. Neno la Kiebrania qela·lahʹ linatokana na kitenzi cha msingi qa·lalʹ, linalomaanisha kihalisi “kuwa mwepesi.” Hata hivyo, litumiwapo kwa njia ya kitamathali, lamaanisha ‘kulaani’ au ‘kudharau.’—Mambo ya Walawi 20:9; 2 Samweli 19:43.

6. Ni jambo gani lenye kuhusisha Elisha lililotukia karibu na Betheli la kale?

6 Chunguza kielelezo chenye kusisimua cha hatua ya upesi iliyohusisha laana. Hiyo ilitukia wakati Elisha nabii wa Mungu alipokuwa akitembea kutoka Yeriko hadi Betheli. Simulizi lataarifu hivi: “Alipokuwa akienda njiani, wakatoka vijana katika mji, wakamfanyizia mzaha, wakamwambia, Paa wewe mwenye upaa! Paa wewe mwenye upaa! Akatazama nyuma akawaona, akawalaani kwa jina la BWANA. Wakatoka dubu wawili wa kike mwituni, wakawararua vijana arobaini na wawili miongoni mwao.” (2 Wafalme 2:23, 24) Maneno hasa ambayo Elisha alitumia alipowalaani wale watoto wenye kufanyiza mzaha hayafunuliwi. Hata hivyo, tamko hilo la maneno lilikuwa na matokeo kwa sababu lilisemwa kwa jina la Yehova na nabii wa Mungu aliyekuwa akitenda kupatana na mapenzi ya kimungu.

7. Ni nini kilichowapata wale watoto waliomfanyizia Elisha mzaha, na kwa nini?

7 Jambo linaloonekana kuwa sababu ya huko kufanyiza mzaha ni kwamba Elisha alikuwa amevaa vazi rasmi la Eliya lililojulikana, na hao watoto hawakutaka mwandamizi yeyote wa nabii huyo awe mahali hapo. (2 Wafalme 2:13) Ili kushindana na upinzani wa kuwa kwake mwandamizi wa Eliya na ili kufundisha vijana hao na wazazi wao staha ifaayo kwa nabii wa Yehova, Elisha alilaani kwa jina la Mungu wa Eliya, kundi hilo lenye kufanyiza mzaha. Yehova alidhihirisha kukubali kwake Elisha kuwa nabii wake kwa kusababisha wale dubu wawili wa kike watoke mwituni na kuwararua vipande-vipande vijana 42 wa wale wenye kudhihaki. Yehova alishughulika kwa njia ya mkataa kwa sababu ya ukosefu wao mbaya sana wa staha kuelekea njia ya uwasiliano aliyokuwa akitumia duniani wakati huo.

8. Watu wa Israeli walikubali kufanya nini, na wakawa na mataraja yapi?

8 Miaka kadhaa mapema, Waisraeli walionyesha ukosefu uo huo wa staha kuelekea mipango ya Mungu. Hivi ndivyo ulivyodhihirika: Katika 1513 K.W.K., Yehova alionyesha watu wa Israeli upendeleo kwa kuwakomboa kutoka katika utumwa wa Kimisri kana kwamba “juu ya mbawa za tai.” Muda mfupi baadaye, waliahidi kumtii Mungu. Ona jinsi utii ulivyofungamanishwa sikuzote na kupokea kibali cha Mungu. Yehova alisema hivi kupitia Musa: “Ikiwa mtaitii sauti yangu kweli kweli, na kulishika agano langu, hapo ndipo mtakapokuwa tunu kwangu kuliko makabila yote ya watu; maana dunia yote pia ni mali yangu.” Baadaye, watu wakaitikia kwa kukubali, wakisema: “Hayo yote aliyoyasema BWANA tutayatenda.” (Kutoka 19:4, 5, 8; 24:3) Waisraeli walidai kumpenda Yehova, walijiweka wakfu kwake, wakaapa kutii sauti yake. Kufanya hivyo kungetokeza baraka kubwa.

9, 10. Musa alipokuwa juu ya Mlima Sinai, Waisraeli walifanya nini, na matokeo yakawa nini?

9 Lakini, kabla ya kanuni za msingi za mwafaka huo kuchongwa katika jiwe kwa “chanda cha Mungu,” laana za kimungu zikawa za lazima. (Kutoka 31:18) Kwa nini matokeo hayo yenye kuhuzunisha yalistahili? Je, Waisraeli hawakuwa wameonyesha tamaa ya kufanya yote ambayo Yehova alikuwa amesema? Ndiyo, kwa maneno walitaka baraka, lakini kwa vitendo vyao walichagua mwendo uliostahili laana.

10 Katika kipindi cha siku 40 Musa alipokuwa juu ya Mlima Sinai akipokea zile Amri Kumi, Waisraeli walivunja ahadi yao ya mapema ya uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova. “Hata,” simulizi lasema, “watu walipoona ya kuwa Musa amekawia kushuka katika mlima, wakakusanyana wakamwendea Haruni, wakamwambia, Haya! katufanyizie miungu itakayokwenda mbele yetu, kwa maana Musa huyo aliyetutoa katika nchi ya Misri hatujui yaliyompata.” (Kutoka 32:1) Hiki ni kielelezo kingine cha mtazamo usio wenye staha kuelekea binadamu ambaye Yehova alikuwa akitumia wakati huo ili kuwaongoza na kuwaelekeza watu wake. Waisraeli walivutwa kuiga ibada ya sanamu ya Kimisri wakavuna matokeo mabaya wakati watu wapatao 3,000 kati yao walipouawa kwa upanga katika siku moja.—Kutoka 32:2-6, 25-29.

Tamko la Baraka na Laana

11. Ni maagizo gani kuhusu baraka na laana yaliyotekelezwa na Yoshua?

11 Karibu na mwisho wa safari ya Israeli ya miaka 40 nyikani, Musa alitaja baraka moja-moja ambazo zingevunwa kwa kuchagua mwendo wa utii kwa Mungu. Pia alitaja laana moja-moja ambazo Waisraeli wangejionea ikiwa wangechagua kutomtii Yehova. (Kumbukumbu la Torati 27:11–28:10) Muda mfupi baada ya Israeli kuingia Bara Lililoahidiwa, Yoshua alitekeleza maagizo ya Musa yaliyohusisha baraka na laana hizo. Makabila sita ya Israeli yalisimama chini ya Mlima Ebali, na yale mengine sita yalisimama mbele ya Mlima Gerizimu. Walawi walisimama katika lile bonde katikati. Yaonekana yale makabila yaliyokuwa mbele ya Mlima Ebali yalisema “Amina!” kwa laana, zilizosomwa kuelekea upande huo. Wengine waliziitikia baraka ambazo Walawi walisoma kuelekea upande wao wakiwa chini ya Mlima Gerizimu.—Yoshua 8:30-35.

12. Ni baadhi ya laana gani zilizotamkwa na Walawi?

12 Ebu wazia kwamba unasikia Walawi wakisema: “Na alaaniwe mtu afanyaye sanamu ya kuchonga, au ya kusubu, machukizo kwa BWANA, kazi ya mikono ya fundi, akaisimamisha kwa siri. . . . Na alaaniwe amdharauye baba yake au mama yake. . . . Na alaaniwe aondoaye mpaka wa jirani yake. . . . Na alaaniwe ampotezaye kipofu akakosa njia. . . . Na alaaniwe apotoaye hukumu ya mgeni, na yatima, na mjane aliyefiliwa na mumewe. . . . Na alaaniwe alalaye na mke wa baba yake, kwa kuwa amefunua mavazi ya babaye. . . . Na alaaniwe alalaye na mnyama wa aina yoyote. . . . Na alaaniwe alalaye na umbu lake, binti ya babaye, au binti ya mamaye. . . . Na alaaniwe alalaye na mkwewe, mamaye mkewe. . . . Na alaaniwe ampigaye mwenzake kwa siri. . . . Na alaaniwe atwaaye ujira wa kumwua asiye makosa. . . . Na alaaniwe asiyeyaweka imara maneno ya torati hii kwa kuyafanya.” Baada ya kila laana, makabila yaliyo mbele ya Mlima Ebali yasema, “Amina!”—Kumbukumbu la Torati 27:15-26.

13. Kwa maneno yako mwenyewe, ungeelezaje baraka fulani ambazo Walawi walitamka?

13 Sasa ebu wazia kwamba wasikia wale walio mbele ya Mlima Gerizimu wakiitikia kwa sauti kila baraka huku Walawi wakipaaza sauti hivi: “Utabarikiwa mjini, utabarikiwa na mashambani. Utabarikiwa uzao wa tumbo lako, na uzao wa nchi yako, na uzao wa wanyama wako wa mifugo, maongeo ya ng’ombe wako, na wadogo wa kondoo zako. Litabarikiwa kapu lako, na chombo chako cha kukandia unga. Utabarikiwa uingiapo, utabarikiwa na utokapo.”—Kumbukumbu la Torati 28:3-6.

14. Waisraeli wangepokea baraka kwa msingi upi?

14 Msingi wa kupokea baraka hizi ulikuwa nini? Simulizi lasema hivi: “Itakuwa utakaposikia sauti ya BWANA, Mungu wako, kwa bidii, kutunza kuyafanya maagizo yake yote nikuagizayo leo, ndipo BWANA, Mungu wako, atakapokutukuza juu ya mataifa yote ya duniani; na baraka hizi zote zitakujilia na kukupata usikiapo sauti ya BWANA, Mungu wako.” (Kumbukumbu la Torati 28:1, 2) Ndiyo, ufunguo wa kufurahia baraka za kimungu ulikuwa utii kwa Mungu. Lakini namna gani sisi leo? Je, sisi mmoja-mmoja tutachagua baraka na uhai kwa kuendelea ‘kusikiliza sauti ya Yehova’?—Kumbukumbu la Torati 30:19, 20, NW.

Kuchunguza kwa Ukaribu Zaidi

15. Ni jambo gani lililoonyeshwa katika baraka iliyorekodiwa kwenye Kumbukumbu la Torati 28:3, na twaweza kunufaikaje nalo?

15 Acheni tufikirie baraka fulani ambazo Mwisraeli angeweza kufurahia kwa kumtii Yehova. Kwa kielelezo, Kumbukumbu la Torati 28:3 yasema: “Utabarikiwa mjini, utabarikiwa na mashambani.” Kubarikiwa na Mungu hakutegemei mahali wala mgawo. Huenda watu fulani wakahisi wamezuiwa katika hali zao, labda kwa sababu wanaishi katika eneo lililokumbwa na uharibifu wa mali za kimwili au katika nchi iliyogawanywa na vita. Huenda wengine wakatamani sana kumtumikia Yehova wakiwa kwingineko. Huenda wanaume fulani Wakristo wakavunjika moyo kwa sababu hawajawekwa rasmi kuwa watumishi wa huduma au kuwa wazee kutanikoni. Nyakati nyingine, wanawake Wakristo huhisi kufa moyo kwa sababu hawawezi kushiriki katika huduma ya wakati wote wakiwa mapainia au wamishonari. Hata hivyo, kila mtu ambaye ‘asikiliza sauti ya Yehova na kufanya kwa uangalifu yote anayotaka’ (NW) atabarikiwa sasa na kwa umilele wote.

16. Kanuni ya Kumbukumbu la Torati 28:4 inaonwaje na tengenezo la Yehova leo?

16 Kumbukumbu la Torati 28:4 yasema: “Utabarikiwa uzao wa tumbo lako, na uzao wa nchi yako, na uzao wa wanyama wako wa mifugo, maongeo ya ng’ombe wako, na wadogo wa kondoo zako.” Matumizi ya kiwakilishi cha Kiebrania katika hali ya umoja kinachofasiriwa ‘-ako’ huonyesha kwamba hilo lingekuwa ono la kibinafsi la Mwisraeli mtiifu. Namna gani watumishi watiifu wa Yehova leo? Ongezeko na upanuzi wa ulimwenguni pote unaoendelea katika tengenezo la Mashahidi wa Yehova unatokana na baraka ya Mungu juu ya jitihada zenye bidii za wapiga-mbiu zaidi ya 5,000,000 wa habari njema za Ufalme. (Marko 13:10) Na uwezekano wa kuwa na ongezeko kubwa zaidi ni wazi kwa sababu watu zaidi ya 13,000,000 walihudhuria mwadhimisho wa Mlo wa Jioni wa Bwana wa 1995. Je, wewe unafurahia baraka za Ufalme?

Chaguo la Israeli Lilileta Matokeo Tofauti

17. ‘Kupatwa’ na baraka au laana kulitegemea nini?

17 Kwa kweli, baraka zingemfuatia Mwisraeli mtiifu. Iliahidiwa hivi: “Baraka hizi zote zitakujilia na kukupata.” (Kumbukumbu la Torati 28:2) Vivyo hivyo, ilisemwa hivi juu ya laana: “Ndipo zitakapokujia laana hizi zote na kukupata.” (Kumbukumbu la Torati 28:15) Ikiwa ungalikuwa Mwisraeli wa nyakati za kale, je, ‘ungalipatwa’ na baraka au na laana? Hilo lingalitegemea kama ulimtii Mungu au ulikosa kumtii.

18. Waisraeli wangaliweza kuepukaje laana?

18 Kwenye Kumbukumbu la Torati 28:15-68, matokeo yenye maumivu ya kutokutii yanaonyeshwa yakiwa laana. Baadhi yayo ni kinyume kabisa cha baraka za utii zinazotajwa moja-moja kwenye Kumbukumbu la Torati 28:3-14. Mara nyingi, watu wa Israeli walivuna matokeo mabaya sana ya laana kwa sababu walichagua kushiriki katika ibada isiyo ya kweli. (Ezra 9:7; Yeremia 6:6-8; 44:2-6) Hilo lilihuzunisha kama nini! Matokeo hayo yangaliweza kuepukwa kwa kufanya chaguo lililofaa, la kutii sheria na kanuni za Yehova zenye kufaa, zinazofasili kwa wazi yaliyo mema na yaliyo mabaya. Watu wengi leo hupatwa na maumivu na msiba kwa sababu wamechagua kutenda kinyume cha kanuni za Biblia kwa kuzoea dini isiyo ya kweli, kushiriki katika ukosefu wa adili katika ngono, kwa kutumia madawa haramu, kwa kutumia kupita kiasi vinywaji vya alkoholi, na mambo kama hayo. Kama vile katika Israeli na Yuda ya kale, kufanya machaguo hayo mabaya hutokeza hali ya kutokubaliwa kimungu na maumivu ya moyoni yasiyo ya lazima.—Isaya 65:12-14.

19. Fafanua hali zilizofurahiwa wakati Yuda na Israeli yalipochagua kumtii Yehova.

19 Baraka zilikuwa nyingi na utulivu ulienea wakati tu ambapo Israeli walimtii Yehova. Kwa kielelezo, kuhusu siku za Mfalme Sulemani, twasoma hivi: “Yuda na Israeli walikuwa wengi kama mchanga wa pwani kwa wingi, wakila, na kunywa, na kufurahi. . . . Yuda na Israeli wakakaa salama, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, tokea Dani mpaka Beer-sheba, siku zote za Sulemani.” (1 Wafalme 4:20-25) Hata wakati wa Mfalme Daudi, uliokuwa wenye upinzani mwingi kutoka kwa maadui wa Mungu, taifa lilihisi utegemezo na baraka ya Yehova wakati lilipochagua kumtii Mungu wa ukweli.—2 Samuel 7:28, 29; 8:1-15.

20. Mungu ana uhakika juu ya nini kuhusu wanadamu?

20 Je, utamtii Mungu, au utakosa kumtii? Waisraeli walikuwa na chaguo. Ingawa sisi sote tumerithi mwelekeo wenye dhambi kutoka kwa Adamu, tumepokea pia zawadi ya kuchagua kwa hiari. Ajapokuwa Shetani, ulimwengu huu mwovu, na kutokamilika kwetu, twaweza kufanya chaguo linalofaa. Zaidi ya hayo, Muumba wetu ana uhakika kwamba ingawa kutakuwa na majaribu na vishawishi vingi, kutakuwa na wale wafanyao chaguo linalofaa, si kwa maneno tu bali pia kwa vitendo. (1 Petro 5:8-10) Je, wewe utakuwa miongoni mwao?

21. Ni jambo gani litakalochunguzwa katika makala ifuatayo?

21 Katika makala ifuatayo, tutaweza kuchunguza kwa uangalifu mitazamo na vitendo vyetu kwa kufikiria vielelezo vya wakati uliopita. Kila mmoja wetu na ayaitikie kwa shukrani maneno haya ya Mungu kupitia Musa: “Nimekuwekea mbele yako uzima na mauti, baraka na laana; basi chagua uzima, ili uwe hai.”—Kumbukumbu la Torati 30:19.

Ungejibuje?

◻ Yehova amewezeshaje baraka ziwezekane kwa ajili ya wanadamu wenye dhambi?

◻ Laana ni nini?

◻ Waisraeli wangaliweza kupokeaje baraka badala ya laana?

◻ Israeli lilifurahia baraka zipi kwa sababu ya kumtii Mungu?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Waisraeli walikusanyika mbele ya Mlima Gerizimu na Mlima Ebali

[Hisani]

Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki