Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 6/15 kur. 17-22
  • Baraka au Laana—Vielelezo kwa Ajili Yetu Leo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Baraka au Laana—Vielelezo kwa Ajili Yetu Leo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Onyo Dhidi ya Ibada ya Sanamu
  • Onyo Dhidi ya Uasherati
  • Onyo Dhidi ya Malalamiko Yenye Uasi
  • Onyo Dhidi ya Kunung’unika
  • Jifunze, na Ufurahie Baraka
  • Msiwe Wasikiaji Wasahaulifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Epukeni Manung’uniko
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Kuishi kwa Kupatana na Wakfu Wetu “Kila Siku”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Baraka au Laana—Kuna Chaguo!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 6/15 kur. 17-22

Baraka au Laana—Vielelezo kwa Ajili Yetu Leo

“Mambo hayo yaliyowapata wao ni kielelezo kwa wengine, na yaliandikwa ili kutuonya sisi, ambao mwisho wa nyakati unatukabili.”—1 WAKORINTHO 10:11, HNWW.

1. Sawa na vile mtu akaguavyo chombo cha kazi, sisi tufanye ukaguzi gani?

KUTU isiyoonwa chini ya mpako wa rangi, yaweza kuanza kuharibu chombo cha kazi chenye kufanyizwa kwa chuma. Huenda ikachukua muda fulani kabla ya hiyo kutu kuonekana juu. Vivyo hivyo, mitazamo na tamaa za moyo wa mtu huenda zikaanza kuzorota muda mrefu kabla ya kuzorota huko kuwa na matokeo mazito au hata kuonwa na wengine. Sawa na vile tungekagua kwa hekima chombo cha kazi ili kuona kama kinapata kutu, ndivyo ukaguzi wa karibu wa mioyo yetu na udumishaji wayo kwa wakati unaofaa huenda ukahifadhi uaminifu-maadili wetu wa Kikristo. Yaani, twaweza kupokea baraka za Mungu na twaweza kuepuka laana za kimungu. Huenda watu fulani wakafikiri kwamba baraka na laana zilizotamkwa juu ya Israeli la kale hazina maana sana kwa wale wanaokabili umalizio wa mfumo huu wa mambo. (Yoshua 8:34, 35; Mathayo 13:49, 50; 24:3) Hata hivyo, sivyo ilivyo. Twaweza kunufaika sana na vielelezo vya kuonya vilivyohusisha Israeli, kama vionyeshwavyo katika 1 Wakorintho sura ya 10.

2. Wakorintho wa Kwanza 10:5, 6 lasema nini kuhusu maono ya Israeli jangwani?

2 Mtume Paulo alinganisha Waisraeli waliokuwa chini ya Musa na Wakristo walio chini ya Kristo. (1 Wakorintho 10:1-4) Ingawa watu wa Israeli wangaliweza kuingia Bara Lililoahidiwa, “wengi sana katika wao, Mungu hakupendezwa nao; maana waliangamizwa jangwani.” Kwa hiyo Paulo aliwaambia Wakristo wenzake hivi: “Basi mambo hayo yalikuwa mifano kwetu, kusudi sisi tusiwe watu wa kutamani mabaya, kama wale nao walivyotamani.” (1 Wakorintho 10:5, 6) Tamaa zinasitawishwa moyoni, kwa hiyo twahitaji kutii vielelezo vya kuonya ambavyo Paulo ataja.

Onyo Dhidi ya Ibada ya Sanamu

3. Waisraeli walifanyaje dhambi kuhusiana na yule ndama wa dhahabu?

3 Onyo la Paulo la kwanza ni: “Wala msiwe waabudu sanamu, kama wengine wao walivyokuwa; kama ilivyoandikwa, Watu waliketi kula na kunywa, kisha wakasimama wacheze.” (1 Wakorintho 10:7, italiki ni zetu.) Kielelezo hiki cha kuonya ni cha Waisraeli kurudia njia za Misri na kufanya ndama wa dhahabu wa ibada ya sanamu. (Kutoka, sura ya 32) Mwanafunzi Stefano alionyesha tatizo la msingi aliposema: “Mtu huyo [Musa, mwakilishi wa Mungu] baba zetu hawakutaka kumtii, bali wakamsukumia mbali, na kwa mioyo yao wakarejea Misri, wakamwambia Haruni, Tufanyie miungu, watakaotutangulia; maana huyo Musa, aliyetutoa katika nchi ya Misri, hatujui lililompata. Wakafanya ndama siku zile, wakaleta dhabihu kwa sanamu ile, wakafurahia kazi za mikono yao.” (Matendo 7:39-41) Ona kwamba “kwa mioyo yao” hawa Waisraeli wakaidi walikuwa na tamaa mbaya zilizowaongoza kwenye ibada ya sanamu. “Wakafanya ndama . . . wakaleta dhabihu kwa sanamu ile.” Zaidi ya hayo, “wakafurahia kazi za mikono yao.” Kulikuwa na muziki, kuimba, kucheza dansi, kula, na kunywa. Kwa wazi, ibada ya sanamu ilikuwa yenye kuvutia na yenye kutumbuiza.

4, 5. Ni mazoea gani ya kuabudu sanamu twahitaji kuepuka?

4 Misri ya ufananisho—ulimwengu wa Shetani—kwa kweli huabudu vitumbuizo. (1 Yohana 5:19; Ufunuo 11:8) Unaabudu waigizaji, waimbaji, na wachezaji mashuhuri, na pia kucheza kwao dansi, muziki wao, dhana zao juu ya raha na nyakati za kupendeza. Wengi wameshawishwa kushiriki kikamili katika vitumbuizo huku bado wakidai kumwabudu Yehova. Wakati ambapo ni lazima Mkristo akaripiwe kwa sababu ya kosa, hali yake ya kiroho iliyodhoofika yaweza mara nyingi kufuatishwa kurudi nyuma hadi kwenye kunywa vinywaji vya alkoholi, kucheza dansi, na kuwa na wakati wa kupendeza kwa njia fulani ambayo huenda ikakaribia ibada ya sanamu. (Kutoka 32:5, 6, 17, 18) Vitumbuizo fulani vyafaa na ni vyenye kufurahisha. Hata hivyo, leo muziki, kucheza dansi, sinema, na vidio za kilimwengu zilizo nyingi hutosheleza tamaa za kimwili zilizo zenye ufisadi.

5 Wakristo wa kweli hawashindwi na ibada ya sanamu. (2 Wakorintho 6:16; 1 Yohana 5:21) Kila mmoja wetu na awe mwangalifu vilevile asije akawa mraibu wa vitumbuizo vya kuabudu sanamu na kuwa na hatari ya kupatwa na matokeo yenye kudhuru ya kushughulikia sana kuwa na wakati wenye kupendeza kwa njia ya kilimwengu. Tukijitiisha wenyewe chini ya mavutano ya kilimwengu, tamaa na mitazamo yenye madhara yaweza kukazwa akilini na moyoni kwa hila sana. Isiposahihishwa, hiyo yaweza hatimaye kuwa na tokeo la ‘kuangamizwa jangwani’ mwa mfumo wa Shetani.

6. Ni hatua gani chanya huenda tukahitaji kuchukua kuhusu vitumbuizo?

6 Sawa na Musa wakati wa tukio la yule ndama wa dhahabu, kwa kweli “mtumwa mwaminifu mwenye akili” anasema hivi: “Mtu awaye yote aliye upande wa BWANA, na aje kwangu.” Kuchukua hatua chanya ili kuonyesha kwamba twasimama imara kwa ajili ya ibada ya kweli kwaweza kuokoa uhai. Kabila la Musa la Lawi lilitenda upesi kuondolea mbali mavutano yenye kushusha heshima. (Mathayo 24:45-47; Kutoka 32:26-28) Kwa hiyo basi, chunguza kwa uangalifu chaguo lako la vitumbuizo, muziki, vidio, na mambo kama hayo. Ikiwa ni yenye ufisadi kwa njia fulani, chukua msimamo wako upande wa Yehova. Kwa kumtegemea Mungu kwa sala, fanya mabadiliko katika chaguo lako la vitumbuizo na muziki, na uharibu vitu vyenye kudhuru kiroho, sawa na vile Musa alivyoharibu yule ndama wa dhahabu.—Kutoka 32:20; Kumbukumbu la Torati 9:21.

7. Twaweza kulindaje moyo wa kitamathali?

7 Twaweza kupingaje uharibifu wa moyo? Kwa kujifunza Neno la Mungu kwa bidii, tukiruhusu kweli zalo zipenyeze ndani ya akili zetu na mioyo yetu. (Warumi 12:1, 2) Bila shaka twapaswa kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida. (Waebrania 10:24, 25) Kuhudhuria mikutano kwa kujikalia tu kungeweza kufananishwa na kupaka rangi mahali penye kutu. Hilo huenda likatuchangamsha kwa muda mfupi, lakini halitatui tatizo la msingi. Badala ya hivyo, kwa utayarishaji wa kimbele, kutafakari, na kushiriki kwa bidii katika mikutano, twaweza kwa juhudi nyingi kuondoa mambo yaletayo uharibifu ambayo huenda yakaendelea kukaa ndani ya moyo wetu wa kitamathali. Hilo litatusaidia kushikamana na Neno la Mungu na kutatuimarisha kuvumilia mitihani ya imani na kuwa “watimilifu bila kupungukiwa na neno.”—Yakobo 1:3, 4; Mithali 15:28.

Onyo Dhidi ya Uasherati

8-10. (a) Ni kielelezo gani cha kuonya kinachorejezewa kwenye 1 Wakorintho 10:8? (b) Maneno ya Yesu yanayopatikana kwenye Mathayo 5:27, 28 yaweza kutumiwaje kwa njia ya kunufaisha?

8 Katika kielelezo kifuatacho cha Paulo, tunashauriwa hivi: “Wala msifanye uasherati, kama wengine wao walivyofanya, wakaanguka siku moja watu ishirini na tatu elfu.”a (1 Wakorintho 10:8) Mtume alikuwa akirejezea wakati Waisraeli walipoinamia miungu isiyo ya kweli “wakaanza kuzini pamoja na wanawake wa Moabu.” (Hesabu 25:1-9) Ukosefu wa adili katika ngono unastahili kifo! Kuruhusu mawazo na tamaa zisizo za adili kuendelea bila kuzuiwa ni kama kuruhusu moyo “kuwa na kutu.” Yesu alitaarifu hivi: “Mmesikia kwamba imenenwa, Usizini; lakini mimi nawaambia, Kila mtu atazamaye mwanamke kwa kumtamani, amekwisha kuzini naye moyoni mwake.”—Mathayo 5:27, 28.

9 Jambo linaloshuhudia matokeo ya ‘kutazama mwanamke kwa kumtamani’ ni tokeo la kule kufikiri kwenye kushusha heshima kwa wale malaika waliokosa kutii, kabla ya Furiko la siku ya Noa. (Mwanzo 6:1, 2) Kumbuka pia, kwamba mojawapo mambo ya kuhuzunisha zaidi maishani mwa Mfalme Daudi lilichochewa na kuendelea kwake kumtazama mwanamke kusivyofaa. (2 Samweli 11:1-4) Kinyume cha hilo, yule mwanamume mwadilifu Ayubu aliyekuwa ameoa ‘alifanya agano na macho yake ili asiweze kumwangalia msichana,’ hivyo akiepuka ukosefu wa adili na akithibitika kuwa mwenye kushika uaminifu-maadili. (Ayubu 31:1-3, 6-11) Macho yaweza kufananishwa na madirisha ya moyo. Na mambo mengi maovu hutoka katika moyo wenye ufisadi.—Marko 7:20-23.

10 Tukiyatumia maneno ya Yesu, hatutaruhusu mawazo mabaya yaendelee kwa kutazama habari ya kiponografia au kwa kufikiria mawazo yasiyo ya adili kuhusu Mkristo mwenzetu, mfanyakazi mwenzetu, na mtu mwingine yeyote. Kutu haiondolewi kutoka chuma kwa kupangusa tu mahali palipoharibiwa nayo. Kwa hiyo, usiondoshe kijuujuu tu mawazo na mielekeo isiyo ya adili kana kwamba hiyo si ya maana sana. Chukua hatua zenye nguvu kujiondoshea mielekeo isiyo ya adili. (Linganisha Mathayo 5:29, 30.) Paulo ahimiza waamini wenzake hivi: “Vifisheni viungo vyenu vilivyo katika nchi, uasherati, uchafu, tamaa mbaya, mawazo mabaya, na kutamani, ndiyo ibada ya sanamu; kwa ajili ya mambo hayo huja ghadhabu ya Mungu.” Ndiyo, kwa ajili ya mambo kama ukosefu wa adili katika ngono, “huja ghadhabu ya Mungu” ikiwa wonyesho wa laana yake. Kwa hiyo twahitaji ‘kuvifisha’ viungo vyetu kwa habari ya mambo hayo.—Wakolosai 3:5, 6.

Onyo Dhidi ya Malalamiko Yenye Uasi

11, 12. (a) Ni onyo gani linalotolewa kwenye 1 Wakorintho 10:9, na ni tukio gani lililorejezewa? (b) Onyo la Paulo lituathirije?

11 Paulo afuata na onyo hili: “Wala tusimjaribu Bwana, kama wengine wao walivyomjaribu, wakaharibiwa na nyoka.” (1 Wakorintho 10:9) Walipokuwa wakisafiri karibu na mpaka wa Edomu, Waisraeli “wakamnung’unikia Mungu, na Musa, Mbona mmetupandisha huku kutoka nchi ya Misri, ili tufe jangwani? maana hapana chakula, wala hapana maji, na roho zetu zinakinai chakula hiki dhaifu,” ile mana iliyoandaliwa kimuujiza. (Hesabu 21:4, 5) Ebu fikiria! Wale Waisraeli ‘walimnung’unikia Mungu’ wakiyaita maandalizi yake kuwa yenye kudharaulika!

12 Kwa malalamiko yao, Waisraeli walikuwa wakitahini subira ya Yehova. Adhabu haikukosa kutolewa, kwani Yehova alituma nyoka zenye sumu miongoni mwao, na wengi wakafa kutokana na maumo ya nyoka. Baada ya watu kutubu na Musa kuomba kwa niaba yao, hilo pigo lilikomeshwa. (Hesabu 21:6-9) Kwa hakika tukio hilo lapaswa litumikie likiwa onyo kwetu kutoonyesha roho ya kulalamika, yenye uasi, hasa dhidi ya Mungu na mipango yake ya kitheokrasi.

Onyo Dhidi ya Kunung’unika

13. Wakorintho wa Kwanza 10:10 laonya dhidi ya nini, na Paulo alikuwa akifikiria uasi upi?

13 Akitaja kielelezo chake cha mwisho kilichohusisha Waisraeli jangwani, Paulo aandika hivi: “Wala msinung’unike, kama wengine wao walivyonung’unika, wakaharibiwa na mharabu.” (1 Wakorintho 10:10) Uasi ulitokea wakati Kora, Dathani, Abiramu, na washiriki wao walipotenda kwa njia isiyo ya kitheokrasi wakapinga mamlaka ya Musa na Haruni. (Hesabu 16:1-3) Baada ya uharibifu wa wale waasi, Waisraeli walianza kunung’unika. Hiyo ilikuwa kwa sababu walianza kusababu kwamba uharibifu wa wale waasi haukuwa wenye haki. Hesabu 16:41 lataarifu hizi: “Siku ya pili yake mkutano wote wa wana wa Israeli wakamnung’unikia Musa, na Haruni, wakasema, Ninyi mmewaua watu wa BWANA.” Tokeo la kuchambua kwao njia ambayo haki ilitekelezwa katika pindi hiyo lilikuwa kuangamia kwa Waisraeli 14,700 kutokana na tauni iliyopelekwa kimungu.—Hesabu 16:49.

14, 15. (a) Dhambi moja ya wale “watu wasiomcha Mungu” waliopenyeza ndani ya kutaniko, ilikuwa nini? (b) Ni somo gani liwezalo kupatikana kutokana na tukio lililohusisha Kora?

14 Katika karne ya kwanza W.K., “watu wasiomcha Mungu” waliopenyeza ndani ya kutaniko la Kikristo walithibitika kuwa walimu wasio wa kweli na pia wanung’unikaji. Watu hao walikuwa ‘wakidharau mamlaka ya Mungu na kuvitukana viumbe vitukufu,’ wanaume watiwa-mafuta waliokabidhiwa uangalizi wa kutaniko wakati huo. Kuhusu hao waasi-imani wasiomcha Mungu, mwanafunzi Yuda alisema hivi pia: “Watu hawa wananung’unika daima na kuwalaumu watu wengine [“walalamikaji juu ya fungu lao maishani,” NW]. Hufuata tamaa zao.” (Yuda 3, 4, 8, 16, HNWW) Leo, watu fulani mmoja-mmoja wanakuwa wanung’unikaji kwa sababu wanaruhusu mtazamo ulioharibiwa kiroho ukue moyoni mwao. Mara nyingi wao hukazia hali za kutokamilika za wale wenye wadhifa wa uangalizi kutanikoni na kuanza kunung’unika dhidi yao. Kunung’unika na kulalamika kwao huenda hata kukafikia kadiri ya kuchambua vichapo vya ‘mtumwa mwaminifu.’

15 Inafaa kuuliza maswali ya moyo mweupe kuhusu habari ya Kimaandiko. Lakini namna gani ikiwa tungekuza mtazamo hasi ujionyeshao katika mazungumzo ya uchambuzi miongoni mwa kikundi cha marafiki wa karibu? Ingefaa tujiulize wenyewe, ‘Matokeo ya kunung’unika huku yaelekea kuwa nini? Je, isingefaa zaidi kuacha kunung’unika na kusali kwa unyenyekevu ili kupata hekima?’ (Yakobo 1:5-8; Yuda 17-21) Kora na wale waliomuunga mkono, walioasi dhidi ya mamlaka ya Musa na Haruni, huenda wakawa walisadikishwa sana kwamba maoni yao yalikuwa halali hivi kwamba hawakuchunguza nia zao. Hata hivyo, walikuwa wamekosea kabisa. Ndivyo na wale Waisraeli walionung’unika kuhusu uharibifu wa Kora na wale waasi wengine. Ni jambo la hekima kama nini kuruhusu vielelezo hivyo vitusukume kuchunguza nia zetu, kuondosha hali ya kunung’unika au kulalamika, na kumruhusu Yehova atutakase!—Zaburi 17:1-3.

Jifunze, na Ufurahie Baraka

16. Maana ya himizo kwenye 1 Wakorintho 10:11, 12, ni nini?

16 Chini ya upulizio wa kimungu, Paulo amalizia orodha ya ujumbe mbalimbali wenye onyo kwa himizo hili: “Basi, mambo hayo yaliyowapata wao ni kielelezo kwa wengine, na yaliandikwa ili kutuonya sisi, ambao mwisho wa nyakati unatukabili. Anayedhani amesimama imara ajihadhari asianguke.” (1 Wakorintho 10:11, 12, HNWW) Sisi na tusipuuze msimamo wetu mzuri katika kutaniko la Kikristo.

17. Tukihisi nia isiyofaa moyoni mwetu, tufanye nini?

17 Sawa na vile chuma kilicho na mwelekeo wa kupata kutu, ndivyo sisi wazao wa Adamu mwenye dhambi tumerithi mwelekeo wa kutenda mabaya. (Mwanzo 8:21; Warumi 5:12) Kwa hiyo, hatupaswi kuvunjika moyo tukihisi nia isiyofaa moyoni mwetu. Badala ya hivyo, acheni tuchukue hatua ya mkataa. Chuma kinapowekwa katika hewa yenye unyevu au katika mazingira ya kubabua, kuharibika kwacho kunaongezeka sana. Twahitaji kuepuka kujiweka katika “hewa” ya ulimwengu wa Shetani, yenye vitumbuizo vyao vibaya, ukosefu wao wa adili ulioenea, na mwelekeo wao wa akili ulio hasi.—Waefeso 2:1, 2.

18. Yehova amefanya nini kuhusiana na mielekeo mibaya ya wanadamu?

18 Yehova ameandalia jamii ya kibinadamu njia ya kupingana na mielekeo mibaya ambayo tumerithi. Alimtoa Mwana wake mzaliwa-pekee ili wale wanaodhihirisha imani katika yeye waweze kuwa na uhai udumuo milele. (Yohana 3:16) Tukifuata nyayo za Yesu kwa ukaribu na kudhihirisha utu ulio kama wa Kristo, tutakuwa baraka kwa wengine. (1 Petro 2:21) Pia tutapokea baraka za kimungu, wala si laana.

19. Twaweza kunufaikaje kwa kufikiria vielelezo vya Kimaandiko?

19 Ingawa sisi leo tunaweza kufanya kosa kwa urahisi kama vile Waisraeli wa zamani, tuna Neno kamili la Mungu lililoandikwa ili kutuongoza. Kutoka katika kurasa zalo twajifunza kuhusu shughuli za Yehova pamoja na wanadamu na pia sifa zake kama zilivyoonyeshwa katika Yesu, ‘mng’ao wa utukufu wake [Mungu] na chapa ya nafsi Yake.’ (Waebrania 1:1-3; Yohana 14:9, 10) Kupitia sala na funzo la Maandiko lenye bidii, twaweza kuwa na “nia ya Kristo.” (1 Wakorintho 2:16) Tunapokabiliwa na vishawishi na mitihani mingine ya imani yetu, twaweza kunufaika kwa kufikiria vielelezo vya Kimaandiko vya kale na hasa kile kielelezo bora kuliko vyote cha Yesu Kristo. Tukifanya hivyo, hatutalazimika kujionea wenyewe utimizo wa laana za kimungu. Badala ya hivyo, tutafurahia upendeleo wa Yehova leo na baraka zake milele.

[Maelezo ya Chini]

a Ona Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 1992, ukurasa 4.

Ungejibuje?

◻ Twaweza kutumiaje shauri la Paulo la kutokuwa waabudu sanamu?

◻ Twaweza kufanya nini ili kutii onyo la mtume dhidi ya uasherati?

◻ Kwa nini tuepuke kunung’unika na kulalamika?

◻ Twaweza kupokeaje baraka za kimungu, wala si laana?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Ikiwa twataka baraka za kimungu, ni lazima tuepuke ibada ya sanamu

[Picha katika ukurasa wa 20]

Sawa na vile kutu huhitaji kuondolewa, acheni tuchukue hatua chanya ili kuondoa tamaa zisizofaa katika mioyo yetu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki