Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 2/15 kur. 8-13
  • “Israeli Wote Wataokolewa”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Israeli Wote Wataokolewa”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ni Nani Wanaokuwa “Israeli Wote”?
  • Sasa Kazi ya Kupandikiza Imekwisha Kufanywa
  • “Israeli Wote” Wanaokolewa Wabariki Wanadamu Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Mzeituni Wenye Kuzaa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Wayahudi
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • ‘Lo! Jinsi Kilivyo Kina cha Hekima ya Mungu!’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 2/15 kur. 8-13

“Israeli Wote Wataokolewa”

“Kwa njia hiyo Israeli wote wataokolewa. Sawasawa na ilivyoandikwa: ‘Mkombozi atatoka Sayuni na kugeuza mazoea yasiyo ya kumwogopa Mungu yatoke kwa Yakobo.’”​—WARUMI 11:26. NW.

1. (a) Kwa habari ya Warumi 11:26, ni maulizo gani yanayotokezwa? (b) Kwa sababu gani Jamhuri ya Israeli siyo Israeli ambayo ‘ingeokolewa’?

NI TAIFA gani linalomaanishwa hapa? Linaokolewaje? Na mataifa mengine yote yanakuwaje linapookolewa? Wakati amri ya Uingereza ya kusimamia Palestina ilipokwisha mwaka wa 1948, Wayahudi walichukua sehemu ya eneo hilo kisha wakaanzisha Jamhuri ya Israeli. Waisraeli walipanua mipaka ya jamhuri yao kwa kushinda vikosi vya Waarabu katika ile vita ya siku sita ya 1967. Lakini tangu Jamhuri ya Israeli ilipoanzishwa, imelazimika kuendeleza kuwako kwayo kwa kutumia silaha. Israeli ya kisasa iwe au isiwe ina makombora mengi ya nyukilia yaliyokusanywa ili kulinda taifa lao, ni wazi kabisa kwamba haitegemei ‘mkombozi ye yote kutoka Sayuni.’ Kwani, taifa hilo la kisiasa lililo changa kwa kulinganishwa na mengine ni sehemu ya Umoja wa Mataifa likiwa pamoja na Mataifa yasiyo ya Kiyahudi! Kwa wazi, jamhuri hiyo si theokrasi, kama vile taifa la Israeli lilivyokuja kuwa katika siku za Musa, huko nyuma mwaka wa 1513 K.W.K.

2. Kuanzishwa kwa Jamhuri ya Israeli kulitofautianaje na kurudishwa kwa Wayahudi kwenye nchi ya kwao mwaka wa 537 K.W.K.?

2 Theodor Herzl aliye Mwisraeli wa Australia, ambaye ndiye aliyeanzisha Tengenezo la Wasayuni Ulimwenguni mwaka wa 1897, alitangaza kwamba Wayahudi walikuwa taifa kisha akadai eneo liwekwe kando ili kusimamisha serikali ya Kiyahudi. Lakini hakuna hata moja kati ya matukio yote yanayohusu Jamhuri ya Israeli yanalingana kwa vyo vyote na kurudishwa kwa Wayahudi kwenye nchi yao mwaka wa 537 K.W.K., ule mwaka wa kwanza wa mfalme Mwajemi Koreshi Mkuu. Kurudishwa kwao wakati wa kale kulitimiza kusudi lililotangazwa la Mungu wa Israeli, Yehova, kama lilivyotabiriwa kwenye Isaya 45:1-5. (2 Mambo ya Nyakati 36:22, 23; Ezra 1:1-4) Lakini Jamhuri ya Israeli ilipoanzishwa hatukuona mwendo wa amani ukifuatwa kwa kumwamini kabisa Mungu wa Israeli wa kale. Kwa hiyo hatua hiyo haiwezi kufasiriwa kuwa utimizo wa unabii mbalimbali wa Maandiko ya Kiebrania; wala huo si ushuhuda wa kwamba kuja kwa Masihi yule anayetazamiwa na Wayahudi kumekaribia.

3. Wakati mmoja Wanafunzi wa Biblia wa Mataifa Yote walikuwa na maoni gani juu ya “Israeli wote,” lakini ni jambo gani lililotukia kuhusiana na jambo hilo mwaka wa 1932?

3 Hata kufikia mwaka wa 1929 washiriki wa Shirika la Wanafunzi wa Biblia wa Mataifa Yote walifikiri kwamba Wayahudi wa asili wangali walikuwa watu wachaguliwa wa Mungu, kwamba wangekusanywa warudi Palestina katika hali ya kutokuamini, kwamba wangeongolewa wamwelekee Yesu Kristo kuwa ndiye Uzao wa Abrahamu ulioahidiwa na kwamba hapo ndipo wangekuwa taifa kuu la dunia la kubarikia wanadamu wote. Lakini, mwaka wa 1932 huo ulithibitishwa kuwa ufahamu usiofaa wa unabii wa Biblia, kutia ndani maneno ya Warumi 11:26 juu ya kuokoa “Israeli wote.”​—Ona Funzo la 8 la kitabu Thy Kingdom Come, chenye haki ya kunakili ya 1891, kilichotolewa na Sosaiti.

Ni Nani Wanaokuwa “Israeli Wote”?

4. Ni hali gani leo zinazoonyesha kwamba Jamhuri ya Israeli siyo “Israeli wa Mungu”?

4 Kwenye Wagalatia 6:16 mwandikaji Myahudi alikiita “Israeli wa Mungu” kile alichokiita “Israeli wote” kwenye Warumi 11:26. Lakini ikiwa Wayahudi wa asili katika Jamhuri ya Israeli na katika sehemu zote za dunia sio “Israeli wote,” washiriki wa kundi hilo ni nani? Hilo ni ulizo la maana sana, kwa kuwa Wayahudi wa asili leo hawajui kati ya yale makabila 12 ya Israeli ni jipi lililo lao. Wana walimu wa kidini lakini hawana ukuhani, hawana kuhani mkuu duniani, hawana hekalu Yerusalemu wala hawana madhabahu huko ya kuwekea dhabihu ili wazitoe kulingana na Sheria ambayo Mungu aliwapa kupitia Musa. Vitu vyote hivyo vimekuwa haviko tangu Warumi walipoharibu Yerusalemu mwaka wa 70 W.K. Pia hakuna ushuhuda wa kwamba Mungu ambaye jina lake wanakataa kutamka bado yuko pamoja nao wakiwa taifa zima. Hata hivyo, duniani pana Israeli fulani wa Yehova Mungu, katika karne ii hii ya 20. Kwa hiyo washiriki wake ni nani?

5, 6. Paulo alionyeshaje kwamba kuwa “Israeli wa Mungu” hakutegemei hali za kiasili, za kimwili?

5 Sauli wa Tarso yule Myahudi wa asili, aliyepewa pendeleo la kuwa Paulo mtume wa Kikristo, anatoa jibu la kutosheleza. Karibu na mwaka wa 56 W.K. aliwaandikia barua ndefu “wote walioko Rumi, wapendwao na Mungu, walioitwa kuwa watakatifu.” (Warumi 1:1, 7) Katika barua hiyo, Paulo anawatambulisha wale wanaohesabiwa na Mungu kuwa Waisraeli wa kweli​—si Waisraeli upande wa mwili bali kulingana na roho. Paulo aliandika hivi:

6 “Si wote wanaotokana na Israeli walio ‘Israeli’ kweli kweli. Wala si wote walio watoto kwa sababu ya wao kuwa ni mbegu ya Abrahamu, lakini: ‘Kitakachoitwa “mbegu yako” kitakuwa kupitia Isaka.’ Yaani, watoto walio katika mwili si watoto wa Mungu kweli kweli, lakini watoto kwa njia ya ile ahadi wanahesabiwa kuwa ndio mbegu. . . . Zaidi ya hilo, Isaya anapaaza sauti kuhusu Israeli: ‘Ingawa huenda hesabu ya wana wa Israeli ikawa kama mchanga wa bahari, mabaki ndiyo yatakayookolewa. Kwa maana Yehova atafanya hesabu duniani, aimalizie na kuifupisha.’ Pia, sawa na vile Isaya alivyokuwa amesema hapo kwanza: ‘Kama Yehova hangalituachia sisi mbegu, tungalikuwa sawa na Sodoma, nasi tungalifanywa tuwe sawa na Gomora.’”​—Warumi 9:6-9, 27-29, NW.

7, 8. Kwa sababu gani Waisraeli wa asili walishindwa kujaza nafasi zote wakiwa matawi ya mzeituni wa mfano ulioelezwa katika Warumi sura ya 11?

7 Baadaye, katika Warumi sura ya 11, Paulo alifananisha taifa la Israeli na mzeituni unaokamatana na “rafiki ya Yehova,” yule mzee wa ukoo Abrahamu. (Yakobo 2:23, NW) Baada ya “rafiki” huyo kuonyesha utii wake, Mungu alimwambia: “Katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu.” (Mwanzo 22:18) Kwa sababu walio wengi kati ya Wayahudi wa asili hawakuonyesha imani ya Abrahamu babu yao na kumtii Mungu, Waisraeli hao wasioamini walikatwa kwenye mzeituni wa mfano ambao mzizi wake ulikuwa yule Abrahamu Mkubwa Zaidi, Yehova Mungu. Nafasi zao zilichukuliwa na Mataifa wasioamini, au watu wasio Wayahudi, ili ule mti wa mfano uweze kuwa na hesabu kamili ya matawi. Wenye kuchukua nafasi za Waisraeli wa asili wakawa “mbegu ya Abrahamu” wakiwa waongofu, au Waisraeli kwa kuchaguliwa wawe wana wa kulelewa na Mungu, Yule aliye mkubwa kuliko Abrahamu. (Wagalatia 3:26-29) Wakawa Waisraeli katika maana ya kiroho, yaani, Waisraeli wa kiroho. Ndiyo sababu Paulo aliendelea kusema:

8 “Kwa maana sitaki, ndugu, musijue siri hii, ili musijione wenyewe kuwa wenye akili, ya kwamba kwa sehemu ugumu umepata Israeli, mupaka utimilifu wa Mataifa umefika; na hivi Israeli wote wataokolewa; kama ilivyoandikwa: Mwokozi atakuja kutoka Sayuni, na ataondolea kutokuogopa Mungu katika Yakobo: Na hili ni agano langu nao, wakati nitakapowaondolea zambi zao.”​—Warumi 11:25-27, ZSB.

9. Ingawa “nyakati zilizowekwa za mataifa” zilimalizika mwaka wa 1914, Jamhuri ya Israeli ina maoni gani kuelekea Mpatanishi wa agano jipya?

9 Tunaona kwamba Paulo hasemi, ‘mpaka nyakati za Mataifa zitimizwe.’ Bali, anasema, “mupaka utimilifu wa Mataifa umefika,” au, “mpaka hesabu kamili ya watu wa mataifa iwe imeingia.” (NW) Majira ya Mataifa, au “nyakati zilizowekwa za mataifa,” zilikwisha mwaka wa 1914, mwaka ambao Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilitokea. (Luka 21:24,NW) Hata hivyo, leo, miaka 70 baadaye, Jamhuri ya Israeli na Wayahudi wa asili katika sehemu zote za dunia hawadai kuwa katika agano jipya ambalo Yehova alisema angeanzisha pamoja na nyumba ya Israeli. (Yeremia 31:31-34) Karne zaidi ya 19 zilizopita, siku ya Nisani 14, 33 W.K., usiku wa Kupitwa kwa Kiyahudi, aliyetazamiwa kuwa Mpatanishi wa agano hilo alipokeza mitume wake waaminifu kikombe cha divai kisha akaeleza hivi: “Kikombe hiki kinamaanisha lile agano jipya kwa uwezo wa damu yangu, ambayo itamwagwa chini kwa ajili yenu.” (Luka 22:20, NW) Lakini baada ya muda wote huo Jamhuri ya Israeli haitambui Yesu Kristo kuwa Mpatanishi wa agano lililotabiriwa katika unabii wa Yeremia.

10. Wayahudi wa asili wenye kuamini walifanyiza kiasi gani cha “uzao” wa Abrahamu wa kubarikia wanadamu wote, na matokeo yalikuwa nini?

10 Kulingana na Waisraeli, “mwokozi” hajaja bado kutoka Sayuni. (Isaya 59:20; Warumi 11:26) Lakini siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., mabaki ya Israeli wa kale walimkubali Yesu kuwa ndiye Masihi. Ndipo mabaki hao walipoanza kupokea roho takatifu iliyoahidiwa na kuingizwa katika agano jipya lililotabiriwa. Hata hivyo, mabaki hawakutosha kujaza hesabu kamili ya washiriki wa “bibi arusi” wa Kristo aliye wa kiroho, hesabu yao ikiwa ni 144,000. (Ufunuo 7:1-8; 14:1-3; 21:9) Hivyo si hesabu ya kutosha ya Waisraeli iliyokuwa sehemu ya mzeituni wa mfano ambao mzizi wake ni Abrahamu Mkubwa Zaidi, aliyeahidi kwamba “mbegu” ya yule mzee wa ukoo wa kale ingeziletea baraka jamaa zote za dunia, za Kiyahudi na zisizo za Kiyahudi.

11, 12. Maneno “Israeli wote” yanamaanisha Israeli gani, na hilo linaweza kuthibitishwaje Kimaandiko?

11 Basi, “Israeli wote” wangekuja ‘kuokolewa’ namna gani kupitia “mwokozi” aliyeahidiwa? Tafadhali angalia kwamba Paulo aliwaandikia Warumi barua yake karibu na mwaka wa 56 W.K., baada ya yeye kuwa amewaandikia Wagalatia (karibu na 50-52 W.K.). Kwa hiyo, Warumi 11:25-27 iliandikwa baada ya maneno yake kwenye Wagalatia 6:16 yanayosema juu ya “Israeli wa Mungu.” Israeli huyo ndiye yule ambaye agano jipya lilifanywa pamoja naye kupitia Yesu Kristo, si nabii Musa. Yesu alikuwa Mpatanishi kwa ajili ya Israeli wa Kikristo, Israeli wa kiroho, waliozaliwa kuwa taifa siku ya Pentekoste, mwaka wa 33 W.K., wakati roho takatifu ilipomiminwa juu ya Wayahudi waliomkubali Yesu Kristo kuwa Mpatanishi wa agano jipya.

12 Aliyekuwapo wakati huo ni mtume Myahudi Petro. Baadaye, aliwaandikia “wale waliochaguliwa kulingana na maarifa ambayo Mungu alitangulia kuwa nayo” kisha akasema: “Ninyi ni ‘jamii iliyochaguliwa, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu kwa ajili ya milki ya pekee’ . . . wakati mmoja ninyi hamkuwa watu, lakini sasa mu watu wa Mungu.” (1 Petro 1:1, 2; 2:9, 10, NW) Hilo linahakikisha kwamba Israeli “wote” ambao ‘wataokolewa’ si jamhuri ya kisasa ya Waisraeli wala si Waisraeli wa asili waliotawanyika kila mahali duniani. “Israeli wote” ambao ‘wangeokolewa’ ni Israeli wa kiroho waliozaliwa wakati wa Pentekoste ya 33 W.K. na pindi hiyo walizaliwa kwa roho ya Mungu yenye kuzaa. Hao ndio “Israeli wa Mungu” ambao Mwokozi aliyeahidiwa angewajia.

13. (a) Mwokozi aliyeahidiwa alitoka Sayuni namna gani na wakati gani? (b) Baadaye, ni nani waliopata kuwa washiriki wa “Israeli wa Mungu”?

13 Mwokozi huyo alikuja siku ya Pentekoste ya 33 W.K. Namna gani? Kwa kumimina roho takatifu ya Yehova juu ya wanafunzi karibu 120 katika chumba cha ghorofani kwenye mji mkuu wa kitaifa, Yerusalemu. Hivyo wanafunzi hao wakawa kisehemu cha kwanza cha “Israeli wa Mungu” waliozaliwa kwenye uzima wa kiroho na wenye tumaini la kupata uzima wa milele katika makao ya roho huko juu. Kati ya Israeli wa kiroho hao kukaja mwishowe kuwa na watu wasio Wayahudi waliomwamini Mwokozi aliyeahidiwa. Hilo lilitukia wakati gani? Ni wakati wa kuongolewa kwa Wasamaria​—na baadaye kwa Mataifa wasio Wayahudi hata kidogo wakati wa kuongolewa kwa Kornelio yule Mroma aliyekuwa mkuu wa askari mia moja, pamoja na jamaa na rafiki zake mwaka wa 36 W.K.​—Yehova, Abrahamu Mkubwa Zaidi, alichagua waamini wote hao wasio Wayahudi wawe watoto wa kulelewa katika Mwanaye mzaliwa pekee, Yesu Kristo, lile shina la mfano la mzeituni wa usemi wa mfano. Hivyo watu hao wasio Wayahudi wangeweza kuchukua nafasi za Wayahudi wasio na imani waliovunjwa wakaondolewa katika mzeituni huo wenye “matawi” 144,000.​—Matendo, sura ya 10; 15:14-21.

Sasa Kazi ya Kupandikiza Imekwisha Kufanywa

14. Kufikia sasa kuna ushuhuda wa kutosha kuonyesha nini juu ya “Israeli wote”?

14 Miaka 1,948 imepita tangu wakati wa tukio hilo kuu la mwaka wa 36 W.K. Basi, kulingana na kuwaza kuzuri, kufikia sasa kazi ya Mungu Mwenye Nguvu Zote ya kuokoa “Israeli wote” imekwisha kufanywa kwa njia ya kutosha. Hicho kilikuwa kipindi kirefu kuliko ule muda wa Wayahudi kupewa wakiwa peke yao upendeleo wa kimungu tangu mwaka wa 1513 K.W.K., siku za Musa, kufikia mwaka wa 36 W.K., wakati wa uongofu wa kwanza wa watu wasiotahiriwa ambao si Waisraeli, au Mataifa. Bila shaka, kipindi hicho kirefu kilitoa muda wa kutosha kuokoa “Israeli wote,” kwa habari ya kutokeza washiriki wa kutosha. Sasa kuna ushuhuda mwingi wa kuonyesha imekuwa hivyo.

15. Katika unabii wa Yesu juu ya “ishara” ya “umalizio wa mfumo wa mambo,” alisema “wachaguliwa” wangekusanywa namna gani?

15 Yesu Kristo alielekeza kwenye kipindi hicho alipotoa unabii juu ya “kuwapo” kwake kwa kiroho kusikoonekana na juu ya “umalizio wa mfumo wa mambo,” akasema: “Ishara ya Mwana wa mtu itatokea mbinguni, halafu makabila yote ya dunia yatajipiga kwa maombolezo, nao wataona Mwana wa mtu akija juu ya mawingu ya mbingu kwa uwezo na utukufu mkubwa. Naye atatuma malaika zake kwa sauti kubwa ya tarumbeta, nao watakusanya wachaguliwa pamoja kutoka zile pepo nne, kutoka mwisho mmoja wa mbingu mpaka mwisho mwingine wazo.” (Mathayo 24:3, 30, 31, NW) “Kuwapo” huko kwa Yesu Kristo kulianza wakati gani?

16, 17. “Kuwapo” kwa Yesu Kristo kulianza wakati gani, na ni matukio gani makubwa yaliyofuata kuwahusu “wachaguliwa” waliokusanywa?

16 “Kuwapo” kwa Yesu kulianza zilipokoma “nyakati saba” za Mataifa katika vuli ya mwaka wa 1914. (Danieli 4:23-36) Wakati huo Yesu Kristo aliyetukuzwa aligeuza fikira zake kwenye matumizi ya uwezo wake kuelekea dunia hii iliyokuwa na vita. Mambo ya historia yanathibitisha kwamba katika mwaka ule ulioifuata vita wa 1919 Mfalme Yesu Kristo mwenye kutawala alituma malaika zake za kimbingu wakakusanye pamoja “wachaguliwa” kutoka sehemu zote za dunia. Wakiwa chini ya usimamizi wa Sosaiti, waliletwa pamoja katika umoja wa ulimwenguni pote, waunganishe jitihada zao kuanzia wakati huo ili kutimiza mwelekezo wa kiunabii wa Yesu ulioandikwa kwenye Mathayo 24:14 (NW): “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”

17 Kwenye kusanyiko kuu la watu wa Mungu mwaka wa 1931, walichagua kwa nia moja lile jina jipya, ili wajulikane kuwa Mashahidi wa Yehova. Baadaye ukafuata uchapishaji wa kitabu cha Sosaiti kinachoitwa Jehovah, chenye kueleza jina la Mungu walilofurahia sana kujulikana kwalo. Mashahidi wa Yehova walikipokea kwa shukrani kitabu kipya hicho mwaka wa 1934, wakati Kiongozi wa Nazi, Adolf Hitler, alipokuwa akijiondokea akamalize kabisa Mashahidi katika Ulaya ya kati.

18. Katika wakati wake, ni tukio gani lililoonyesha kwamba hesabu kamili ya “wachaguliwa” ilikuwa imekusanywa?

18 Yaliyofuata yalionyesha kwamba mkusanyo wa “wachaguliwa” waliojiweka wakf na kubatizwa kwa ajili ya Ufalme wa kimbingu ulikuwa umefanywa. Namna gani hivyo? Kwa sababu katika mwaka wa 1935 fikira na jitihada za “wachaguliwa” hao zilielekezwa kwenye “umati mkubwa” uliotangulia kuonyeshwa katika njozi ya Ufunuo 7:9-17, (AV) Huo “umati mkubwa,” au “mkutano mkubwa,” ungekuwa na nani ndani yake? Ungekuwa na watu ambao wangemhesabia Yehova Mungu na Yesu Kristo utukufu na heshima, na wangethawabishwa uzima wa milele katika dunia-paradiso ambamo wangeingia bila kufa kujapokuwako “dhiki” iliyo kubwa kupita zote katika historia ya kibinadamu. Wapendelewa hao walitambulishwa kuwa “kondoo wengine” wa Mchungaji Mwema, Yesu Kristo. Kwa furaha, wangefanywa “kundi moja” pamoja na mabaki ya “Israeli wote” waliokuwa wangali duniani.​—Yohana 10:16.

Jibu Lako Ni Nini?

◻ Kwa sababu gani Jamhuri ya Israeli siyo Israeli inayotajwa kwenye Warumi 11:26?

◻ Kwa sababu gani Waisraeli wa asili walishindwa kujaza nafasi zote wakiwa matawi ya mzeituni wa mfano?

◻ Ni nani Mwokozi aliyeahidiwa, na ni wakati gani na namna gani alitoka Sayuni?

◻ Ni nani wanaohusika katika “Israeli wote,” na ni kufikia wakati gani hesabu yao kamili ilipokusanywa?

[Blabu katika ukurasa wa 12]

Mwaka wa 1935 “kondoo wengine” wenye kushirikiana na mabaki ya “Israeli wote” walitambulishwa kuwa “mkutano mkubwa”

[Picha katika ukurasa wa 10]

Yesu alipoanzisha Chakula cha Jioni cha Bwana, “kikombe” kilimaanisha nini?

[Picha katika ukurasa wa 12]

Wasikilizaji waliojaa mno kwenye kusanyiko la 1935 katika Washington, D.C.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki