Mzeituni Wenye Kuzaa
“Kwa njia hiyo Israeli wote wataokolewa.”—Warumi 11:26, NW.
1. Ni jambo gani linaloweza kusemwa juu ya mizeituni?
MIZEITUNI inajulikana kuwa ni miti yenye kukua muda wa mamia mengi ya miaka. Hata wakati linapokufa lile shina lenye miaka mingi, ambalo mara nyingi huwa na shimo ndani, nyakati nyingine vishina vipya vinatokea kwenye mizizi, kisha kwa njia hiyo mizeituni mipya inazaliwa. Hata iwe hivyo, kuna mzeituni mmoja uliopandwa karibu miaka 4,000 iliyopita ambao ungali hai na unazaa matunda leo!
2. Paulo anasema habari za mzeituni kuhusiana na ahadi gani, na mzeituni huo unakuwa mfano wa kuonyesha nini?
2 Katika barua yake kwa Waroma, mtume Paulo anatumia mzeituni kuwa mfano wa njia nzuri ajabu ambayo Yehova anatumia kutimiza sehemu ya ahadi fulani ambayo Yeye alimpa Abrahamu karne nyingi mapema:
“Katika kubariki nitakubariki, na katika kuzidisha nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni, na kama mchanga ulioko pwani; na uzao wako utamiliki mlango wa adui zao; na katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu.”—Mwanzo 22:16-18.
Agano la Kiabrahamu
3, 4. (a) Ni kwa njia gani Abrahamu alikuwa amethibitisha imani yake muda mfupi uliotangulia? (b) Ni nini kilichotangulia kufananishwa na kisa hicho?
3 Ni muda mfupi tu uliokuwa umepita tangu Abrahamu athibitishe kwamba alikuwa na nia ya kupenda kumtoa Isaka awe dhabihu, mwanaye wa pekee aliyempata kupitia Sara, mke wake wa kwanza. (Waebrania 11:17-19; tafadhali soma Mwanzo 22:1-18.) Tangu nyakati za zamani kabisa Wakristo wameona katika kisa hicho ufananishi wa Yehova akimtoa Mwanaye awe dhabihu kisha kumpokea tena kwa kumfufua. Ndiyo, “Mungu aliupenda ulimwengu [wanadamu], hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16.
4 Kwa hiyo katika mfano huo wa kiunabii, Abrahamu alitangulia kufananisha Yehova Mungu, na Isaka—kijana wa kiume ambaye angaliweza kumpinga babaye mwenye umri wa miaka 125 kama angalitaka—alifananisha Yesu Kristo, aliyetoa uhai wake wa kibinadamu kwa nia ya kupenda ukawa dhabihu ya ukombozi.—Waebrania 7:27; 10:12.
5. Kwa habari ya uzao ulioahidiwa wa Mwanzo 3:15, ni nini kilichofunuliwa katika agano ambalo Mungu alifanya na Abrahamu?
5 Kwa sababu ya Abrahamu kuwa na imani kubwa, mapema kidogo Yehova alikuwa amefanya naye agano lililotukia mwaka wa 1943 K.W.K. (Mwanzo 12:4, 7; Wagalatia 3:17) Karibu miaka 50 baadaye, baada ya Yehova kuuona ubora uliojaribiwa wa imani ya Abrahamu, hata kuhusiana na Isaka, yeye aliirudia ahadi hiyo ya agano na kuikuza, kama ilivyoandikwa katika Mwanzo sura ya 22. Hilo agano la Kiabrahamu lililotajwa kwa ukamili lilieleza kirefu namna makusudi mazuri sana ya Mungu yangetimia. Lilionyesha kwamba uzao wenye kuleta ukombozi ambao uliahidiwa katika Edeni ungetokea duniani ukiwa mzao wa Abrahamu, kwamba ungekuwa uzao wenye kuzidika (lakini hesabu ya uzao wenyewe haikufunuliwa wakati huo), na likaonyesha kwamba ungefutilia mbali adui zao na, mwishowe, kupitia uzao huo mataifa yote ya dunia yajipatie baraka nyingi.—Mwanzo 3:15.
Kuutambua Uzao wa Abrahamu
6, 7. (a) Kulingana na Maandiko, ni nani Uzao wa Abrahamu ulio wa kwanza? (b) Tunajuaje kwamba kungekuwako uzao wa Abrahamu ulio wa pili? (c) Hesabu iliyo kamili ilifunuliwa wakati gani, na ilikuwa hesabu gani?
6 Watu walio na imani kama ya Abrahamu na wanaotaka kubarikiwa na Yehova wanapendezwa kujua kila kijambo kidogo cha ahadi hiyo. (Warumi 4:16) Ni nani aliyekuwa uzao wa kwanza wa Abrahamu, ambaye kupitia kwake mataifa yote ya dunia yangejibariki hatimaye? Mtume Paulo anautambulisha huo Uzao wa kwanza kuwa ni Kristo.—Wagalatia 3:16.
7 Zaidi ya hilo, kwa kuwa Yehova alimwahidi Abrahamu kwamba angezidisha uzao wake, ni watu gani wangekuwa ile sehemu ya pili ya uzao wa Abrahamu? Ni nani wangekuwa “warithi sawasawa na ahadi,” “warithi washirika” pamoja na ule Uzao ulio wa kwanza, yaani, Kristo? (Wagalatia 3:29, UV; Warumi 8:17, NW) Kwa muda wa miaka karibu 2,000 hata hesabu yenyewe ya wale ambao wangekuwa huo ‘uzao wa Abrahamu’ ulio wa pili haikujulikana na wanadamu, sawa-sawa na vile isivyojulikana hesabu ya “nyota za mbinguni” au “mchanga ulioko pwani.” Halafu, kuelekea mwisho wa karne ya kwanza W.K., mtume Yohana alisikia “hesabu yao waliotiwa muhuri katika kila kabila ya Waisraeli, watu mia na arobaini na nne elfu.”—Mwanzo 22:17; Ufunuo 7:4.
8. Wayahudi waliotahiriwa walikuwa na nafasi gani ya pekee?
8 Tena, zaidi ya hilo, ni kutoka kwa akina nani hao “Waisraeli” 144,000 wangechaguliwa na kutiwa muhuri? Kama Waisraeli wa kimwili wenye hesabu ya kutosha wangalilifuata agano la Torati likiwa ‘kiongozi mwenye kuwaleta kwa Kristo [yule Uzao wa Abrahamu aliye wa kwanza],’ wangaliweza kutokeza washiriki wote 144,000 wa ule uzao wa Abrahamu ulio wa pili na hivyo wawe “ufalme wa makuhani, na taifa takatifu,” ili wayabariki mataifa yote ya dunia. (Wagalatia 3:24; Kutoka 19:5, 6) Lakini je! watu wa kutosha walijithibitisha kuwa watoto wa kweli wa Abrahamu, yule aliye “baba yao wote waaminio”?—Warumi 4:11.
9. Yohana Mbatizaji alionyeshaje kwamba uzao wa kiroho wa Abrahamu haukuwa ni lazima uwe na Wayahudi peke yao?
9 Hata kabla Yesu hajaanza huduma yake ya kidunia, Yohana Mbatizaji aliwaonya viongozi wa kidini Wayahudi akawaambia: “Wala msiwaze mioyoni mwenu kwamba, Tunaye baba, ndiye [Abrahamu]; kwa maana nawaambia ya kwamba Mungu aweza katika mawe haya kumwinulia [Abrahamu] watoto. Na shoka limekwisha kuwekwa penye [mzizi wa] miti; basi kila mti usiozaa matunda mazuri hukatwa na kutupwa motoni.” (Mathayo 3:9, 10) Kufikia wakati wa Paulo, njia yenye hekima ya ajabu ambayo Yehova angetumia kukusanya hesabu kamili ya ule uzao wa Abrahamu ulio wa pili ilikuwa imefunuliwa. (Warumi 16:25-27) Paulo anaeleza jambo hilo kwa urefu katika barua aliyowaandikia Waroma.
Barua ya Paulo kwa Waroma
10. Wayahudi wa kimwili waliamini nini kwa makosa?
10 Wayahudi walijisikia sana kuwa walikuwa watu wachaguliwa wa Mungu. Kwa habari ya maneno “watu wachaguliwa,” The Concise Jewish Encyclopedia inasema: “Ni jina linaloonyesha imani ya kwamba Wayahudi wana uhusiano wa pekee pamoja na Mungu. Wazo hilo linategemea msingi wa agano lililofanywa pamoja na Abrahamu.” Kwa sababu ya kuwa na kiburi cha kwamba walikuwa wazao wa Abrahamu, Wayahudi walifikiri wao ndio waliokuwa uzao ambao kupitia huo mataifa mengine yote yangebarikiwa, na kwamba wangeweza kujitetea kuwa wenye haki mbele za Mungu kwa kutenda mambo yaliyotimizwa chini ya agano la Torati.—Yohana 8:33, 39; Warumi 9:31, 32; 10:3, 4; 11:7.
11, 12. (a) Wakati Paulo alipowaandikia Waroma, hali ilikuwa nini katika kundi la huko Roma? (b) Kwa sababu gani Paulo aliwaandikia Wakristo Wayahudi na Mataifa katika Roma?
11 Mtume Paulo aliliandikia kundi la Kikristo katika Roma kwa kuifikiria hali hiyo. Wengine wa Wayahudi waliokuwa Roma walikuwa wamekuwa Wakristo, lakini hesabu iliyo kubwa kati yao ilikataa kumwamini Yesu kuwa ndiye Masihi. Kundi la Kikristo katika Roma lilikuwa na Wakristo wengi wasio Wayahudi pia.
12 Kwa sababu zenye kutofautiana Wayahudi na hata watu wa Mataifa walijisikia kuwa wakubwa—Wayahudi kwa sababu walitokana na lile shina kuu la kwanza la Kiabrahamu—Mataifa kwa sababu walikuwa wameruhusiwa kuingia ndani ya mapendeleo ya pekee ya agano la Kiabrahamu kwa sababu ya ukosefu wa imani upande wa Wayahudi wasioamini. Paulo alijaribu kusadikisha Wakristo wenye asili ya Kiyahudi na wale wasio wa asili hiyo kwamba vikundi vyote viwili vilipata msimamo wa uadilifu mbele za Mungu kwa sababu ya kumwamini Kristo wala si kwa sababu ya matendo yao. (Warumi 3:21-27) Katika kuandika barua yake, shabaha ya Paulo ilikuwa kuleta umoja na uzaaji wa Kikristo, ili kumletea utukufu Yehova kwa sababu ya njia nzuri ajabu anayofuata kusonga mbele akitimiza zile ahadi za agano la Kiabrahamu.
Mzeituni wa Mfano
13. Kwa sababu gani Paulo alionyesha kihoro, naye alionyesha nini kwa kutumia mfano wa mzeituni uliokuzwa?
13 Mtume Paulo anaonyesha kihoro kwa kusema kwamba “hawawi wote Waisraeli walio wa uzao wa Israeli,” kisha anataja hivi: “Wala hawawi wote wana [sehemu ya uzao wa kiroho wa Abrahamu] kwa kuwa wazao wa [Abrahamu].” Halafu anaendelea kutoa mfano wa namna Yehova ‘anavyomwinulia Abrahamu watoto.’ (Warumi 9:1, 2, 6, 7) Ili kueleza namna agano la Kiabrahamu linavyozaa hesabu kamili ya washiriki wa uzao wa kiroho wa ahadi, yeye anatumia mfano wa mzeituni uliokuzwa kwa njia ya pekee.—Tafadhali soma Warumi 11:13-26.
14. Ni nani mzizi (chanzo) wa mzeituni wa mfano, na ni maandiko gani yanayoonyesha hivyo?
14 Paulo anataja mzizi (chanzo) kabla hajasema habari za mti wenyewe, kisha anasema “mzizi wenyewe ni mtakatifu.” (Warumi 11:16, NW) Yehova Mungu ndiye “Aliye Mtakatifu Zaidi.” (Hosea 11:12, NW) Yeye anaitwa mara nyingi “Mtakatifu wa Israeli,” hasa katika kitabu cha Isaya. (Isaya 10:20; 29:19; 60:9) Mtume Petro anashauri Wakristo waliotiwa mafuta, akisema: “Kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote.” (1 Petro 1:15, 16) Yehova Mungu, yule Abrahamu Mkubwa Zaidi, ndiye mzizi (chanzo) wa huo mzeituni wa mfano.
15. (a) Ni kwa njia gani mbalimbali Yehova ndiye mzizi (chanzo) wa Israeli wa kiroho? (b) Ni nani shina (kiwiliwili) la mzeituni? Kwa sababu gani?
15 Kama vile Abrahamu mzee wa ukoo alivyokuwa mzizi (chanzo) wa taifa la Israeli, ndivyo Yehova anavyowapa uhai Israeli wa kiroho. Kama vile yale makabila 12 ya Israeli yalivyotokana na Abrahamu kupitia Isaka mwanaye, ndivyo yale makabila 12 ya mfano ya Israeli wa kiroho yanavyotokana na Yehova kupitia yule Isaka Mkubwa Zaidi, Kristo Yesu. Yeye, akiwa ndiye Uzao wa Abrahamu ulio wa kwanza, anafananishwa na shina la mzeituni wenyewe, au kiwiliwili chake. (Wagalatia 3:16) Yehova, aliye mzizi (chanzo), ndiye anayezaa hesabu kamili ya washiriki wa ule uzao ulio wa pili kupitia Mwanaye, Kristo Yesu (Wagalatia 3:29) Lakini ni namna gani au ni kwa njia gani Yehova anazaa hesabu inayotakwa ya matawi ya mfano?
Matawi Fulani Yanakatwa, Mengine Yanapandikizwa
16. Ni nini ile “siri takatifu” iliyotajwa na Paulo katika Warumi 11:25 na Waefeso 3:3-6 (NW)?
16 Paulo anaendelea kuueleza mpango huu ulio mzuri ajabu. Yeye anaandika hivi: “Kwa maana mimi sitaki ninyi, akina ndugu, mwe hamna ufahamu wa siri takatifu hii, ili ninyi msiwe wenye akili katika macho yenu wenyewe: kwamba hali ya kutokuwa na fahamu imetiwa katika Israeli kwa sehemu mpaka hesabu kamili ya watu wa mataifa yote iwe imeingia, na kwa njia hiyo [Kigiriki, kai houʹtosa] Israeli wote wataokolewa.” (Warumi 11:25, 26, NW; linganisha Waefeso 3:3-6.) Yehova ‘angemwinulia Abrahamu watoto’ kwa kuikubali iingie ndani ya ule uzao wa pili wa Abrahamu hesabu ya watu waliotakwa, au “hesabu kamili ya watu wa mataifa [yasiyo ya Kiyahudi].” Kwa kuonyesha ‘imani ya Abrahamu,’ hesabu ndogo hiyo ya watu wasio Wayahudi ingethibitika kuwa Wayahudi wa kiroho, sehemu ya Israeli wa kiroho, yule “Israeli wa Mungu.”—Warumi 4:16; 2:28, 29; Wagalatia 6:15, 16.
17. (a) Paulo alitoa maelezo juu ya utaratibu gani wa kufanya mambo usiofanywa kwa kawaida? (b) Ni nani waliofananishwa na matawi yaliyokatwa na machipukizi yaliyopandikizwa kutokana na mzeituni-mwitu? (c) Mfano huo ulifunua nini juu ya Wayahudi wenye kiburi na majivuno?
17 Paulo alitoa mfano juu ya namna “siri takatifu” hiyo inavyofanya kazi kwa kuilinganisha na ustadi wa kukuza miti. Kawaida inayotumiwa ni kupandikiza machipukizi ya mti uliokuzwa kwenye shina la mti uliojikuza wenyewe mwituni, ili kuufanya uzae. Paulo alilijua sana jambo hilo. Yeye aliwaambia Wakristo Mataifa kwamba ‘walipandikizwa kinyume cha asili katika mzeituni ulio mwema’ (wa bustanini). (Warumi 11:24) Kwa njia hiyo aliwafananisha watu wasio Wayahudi ambao wangeruhusiwa kuingia ndani ya agano la Kiabrahamu na vitoto, au machipukizi, vya kutoka kwenye mzeituni-mwitu ambavyo vingepandikizwa kwenye shina (kiwiliwili) cha “mzeituni ulio mwema” (wa bustanini). Wao wangechukua nafasi ya matawi ya asili yaliyokuwa yamekatwa, nayo yalifananisha Wayahudi wa kimwili waliokuwa wamekataliwa kwa sababu ya ukosefu wao wa imani. (Warumi 11:17, 19, 20, 24) Mfano huu usio wa kawaida ulitumika kuifichua wazi sana hali yenye kiburi na majivuno ya Wayahudi wasioamini, waliowahesabu Mataifa kuwa wafu sawasawa na mawe au kuwa wasioweza kuzaa matunda mema kama matawi ya mzeituni-mwitu. Ulihakikisha jambo la kwamba Yehova ‘angeweza kumwinulia Abrahamu watoto,’ sawasawa na vile Yohana Mbatizaji alivyotangulia kuonya.—Luka 3:8.
18. (a) Ni nini lililotukia mwaka wa 36 W.K., lakini je! matawi yo yote yaliyokatwa yalipandikizwa kwa kurudishwa tena katika ule mti wa agano la Kiabrahamu? (b) Paulo aliendelezaje umoja ndani ya kundi la Kikristo?
18 Hata hivyo, Wakristo wasio Wayahudi waliokuwa ‘wamepandikizwa kinyume cha asili’ wakaingizwa ndani ya mti wa agano la Kiabrahamu wawe sehemu ya ule uzao wa kiroho hawakuwa na sababu ya kujiona kuwa wakubwa kuliko Wayahudi. Paulo alieleza hivi: “Na hao pia [Wayahudi], wasipokaa katika kutokuamini kwao, watapandikizwa; kwa kuwa Mungu aweza kuwapandikiza tena.” (Warumi 11:23) Baki dogo la Wayahudi wa asili liliukubali ule Uzao ulio wa kwanza likawa matawi yenye kudumu katika ule mti wa mfano. (Warumi 9:27; 11:5) Lakini hesabu iliyo kubwa ya Wayahudi ilikuwa imekatwa ikaondolewa katika mti wa agano la Kiabrahamu katika mwaka wa 36 W.K., mwishoni mwa lile juma la 70 la miaka lililotabiriwa na Danieli. (Danieli 9:27)b Lakini, baada ya hapo Wayahudi fulani walikuwa wamepandikizwa wakarudishwa “katika mzeituni wao wenyewe” kwa kumwamini Masihi, Yesu, ule Uzao wa Abrahamu ulio wa kwanza. (Warumi 11:24; Matendo 13:5, 42, 43; 14:1) Kwa kuyaonyesha wazi mambo hayo, Paulo aliendeleza umoja kati ya Wakristo waliotiwa mafuta, kwa maana wote walikuwa wamekuwa ‘washirika katika mzizi wa unono wa mzeituni’ kupitia “fadhili za Mungu.”—Warumi 11:17, 22, NW.
Mzeituni Wenye Kuzaa kwa Ukamili
19. Ni kwa njia gani agano la Kiabrahamu limezaa uzao wa kiroho pole kwa pole, hata “Israeli wote” waokolewe?
19 Muda wa karne zote, na hasa katika sehemu yenye upendeleo ya huu wakati wa mwisho, Wayahudi wengine na watu wasio Wayahudi walipandikizwa katika mzeituni wa mfano. Hivyo agano la Kiabrahamu linazaa “hesabu kamili” ya Wayahudi na Mataifa wanaohitajiwa ili kuukamilisha ule uzao wa kiroho. “Kwa njia hiyo Israeli wote wataokolewa,” si Israeli wa kimwili, bali wale walio ‘Israeli’ kweli kweli,” wale washiriki 144,000 wa Israeli wa kiroho.—Warumi 11:12, 25, 26; 9:6-8, NW; Ufunuo 7:4.
20, 21. (a) Utimizo wa sehemu hiyo iliyo ya maana zaidi ya agano la Kiabrahamu unapasa kutokeza ndani yetu itikio gani? (b) Ni mambo gani yatakayochunguzwa katika makala inayofuata?
20 Njia nzuri ajabu ambayo Yehova ametumia kutimiza sehemu hii iliyo ya maana zaidi ya agano la Kiabrahamu, kwa kuzaa shina (kiwiliwili) na hesabu kamili ya matawi ya mti huu wa mfano inapasa kutustaajabisha sana. Kama Paulo, sisi tunapaza sauti tukisema: “Jinsi zilivyo kuu utajiri na hekima na maarifa ya Mungu! hukumu zake hazichunguziki, wala njia zake hazitafutikani! Maana ni nani aliyeijua nia ya [Yehova]? Au ni nani aliyekuwa mshauri wake? Au ni nani aliyempa yeye kitu kwanza, naye atalipwa tena? Kwa kuwa vitu vyote vyatoka kwake, viko kwa uweza wake, tena vinarejea kwake. Utukufu una yeye milele. Amina.”—Warumi 11:33-36.
21 Lakini ni masomo gani yenye mafaa yanayoweza kupatikana kutokana na mfano wa ule mzeituni uliopandikizwa, masomo ya kufaidi yale matawi ya mfano (Wakristo waliotiwa mafuta) na wengine ambao wanaweza kujibariki sasa kupitia uzao uliozaliwa na mti wa agano la Kiabrahamu? Mambo hayo yatazungumzwa katika makala inayofuata.
[Maelezo ya Chini]
a “καὶ οὕτως = na hivyo; si kumaanisha wakati tu.” (The Expositor’s Greek Testament) Linganisha Today’s English Version (“na hivi ndivyo”), Authorized Version, Revised Standard Version na New International Version (“na kwa hiyo”). Wale walio na imani ya kwamba mwishowe kabisa taifa zima la Kiyahudi litapata uongofu na wokovu wanayafanya maneno kai houʹtos yamaanishe “na ndipo,” wakionyesha yanatumika kuhusiana na wakati. (Ona Warumi 11:26, The Jerusalem Bible.) Vingi vya vitabu vya Jumuiya ya Wakristo vinavyoieleza Biblia vinatoa fasiri hiyo, ingawa inapingana na njia yote ya Paulo ya kueleza mawazo na inapingana na mambo ya uhakika ya historia, ya zamani na ya sasa.—Linganisha Warumi 2:28, 29; 9:1-6, 27; 10:1, 21; 11:5, 7-10, 14; Matendo 13:45, 46.
b Ona sura ya 7 ya kitabu “Let Your Kingdom Come,” kilichopigwa chapa na Sosaiti.
Wewe umeyashika mambo makuu haya?
◻ Ni ahadi gani ambazo zimetiwa ndani ya agano la Kiabrahamu?
◻ Ni nani uzao wa kwanza na uzao wa pili?
◻ Eleza ni nani wanaosimamiwa na sehemu zinazofuata za ule mzeituni wa mfano:
—mzizi (chanzo)
—shina (kiwiliwili)
—matawi ya asili yaliyokatwa
—matawi ya asili yaliyoachwa mtini au yakapandikizwa kwa kurudishwa tena
—matawi ya mzeituni-mwitu yaliyopandikizwa
◻ “Siri takatifu” iliyotajwa na Paulo katika Warumi 11:25 (NW) ni nini?
◻ Kwa sababu gani mzeituni wa mfano unazaa kwa ukamili?
[Picha katika ukurasa wa 10]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
MZEITUNI WA MFANO—Kifananishi na Kifananishwa
MATAWI
Makabila l2 ya Israeli
Waisraeli wa kiroho 144,000 (uzao wa pili)
SHINA (Kiwiliwili)
Isaka, Yakobo na wazee wa ukoo 12
Masihi Yesu (uzao wa kwanza)
MZIZI (CHANZO) :
Abrahamu
Yehova