Wazaaji wa Matunda Wenye Umoja
“Endeleeni kuzaa matunda mengi na mjithibitishe kuwa wanafunzi wangu.”—YOHANA 15:8, NW.
1. Biblia inaonyeshaje kwamba Yehova anathamini sana miti ya matunda?
“[YEHOVA] Mungu akachipusha katika ardhi kila mti unaotamanika kwa macho na kufaa kwa kuliwa.” (Mwanzo 2:9) Katika Israeli miti ya matunda iliyopandwa juzi-juzi ilipasa kuachwa ikue muda wa miaka mitatu bila ya mwenyewe kutumia matunda ya miti hiyo kwa kusudi liwalo lote. Hata matunda yo yote yaliyozaliwa wakati wa mwaka wa nne yalipasa ‘kuwa ni matakatifu, kwa ajili ya kumpa [Yehova] shukrani.’ Katika mwaka wa tano, mwenyewe angeweza kutumia mazao ya mti kama alivyotaka, baada ya kumtolea Yehova malimbuko (matunda ya kwanza). (Mambo ya Walawi 19:23-25; Kumbukumbu la Torati 26:1-10; Nehemia 10:35-37) Kama vita ingetokea, miti ya matunda ililindwa kwa njia ya pekee chini ya Torati ya Musa.—Kumbukumbu la Torati 20:19, 20.
Miti Isiyozaa Yakatwa na Kuangushwa
2, 3. Yesu alisema nini katika mfano wa ule mtini usiozaa?
2 Katika makala iliyotangulia tumeona kwamba matawi mengi ya asili katika ule mzeituni wa mfano (Warumi, sura ya 11) yalivunjwa na mahali payo pakawekwa matawi yaliyotokana na mzeituni-mwitu. Katika mfano huo matawi yaliyokatwa yanafananisha Wayahudi waaminifu waliokataa kulikubali shina (kiwiliwili) la mzeituni au Uzao ulio wa kwanza, yule Masihi, Yesu. Katika mfano tofauti Yesu alilifananisha taifa la Kiyahudi na mti wote—si mzeituni bali mtini.
3 Katika vuli ya mwaka wa 32 W.K. Yesu alisema hivi: “Mtu mmoja alikuwa na mtini umepandwa katika shamba lake la mizabibu; akaenda akitafuta matunda juu yake, asipate. Akamwambia mtunzaji wa shamba la mizabibu, Tazama, miaka mitatu hii naja nikitafuta matunda juu ya mtini huu, nisipate kitu; uukate, mbona hata nchi unaiharibu? Akajibu akamwambia, Bwana, uuache mwaka huu nao, hata niupalilie, niutilie samadi; nao ukizaa matunda baadaye, vema! la usipozaa, ndipo uukate.”—Luka 13:6-9.
4. Yesu alikuwa amejithibitishaje kuwa “mtunzaji wa shamba la mizabibu” aliye mwaminifu?
4 Katika wakati ambao Yesu alinena habari za mtini huo, yeye akiwa ndiye “mtunzaji wa shamba la mizabibu,” alikuwa ametumia miaka mitatu akijaribu kusitawisha imani kati ya Wayahudi. Lakini ijapokuwa wao walikuwa wakijipatia faida nyingi kwa sababu ya kuwa chini ya agano la Kiabrahamu na la Torati, ni baki dogo tu la taifa la Kiyahudi lililomkubali Masihi. (Warumi 9:4, 5, 27) Wakati wa mwaka wa nne wa huduma yake, Yesu alizidisha sana jitihada zake za kusaidia Wayahudi, kwa njia ya mfano akalima na kutia samadi (mbolea) kuuzunguka “mtini” wa Kiyahudi kwa kuhubiri akiwa na juhudi na kufundisha katika Yudea, Perea na mwishowe katika Yerusalemu na maeneo yaliyouzunguka.—Luka, sura 10 mpaka 19.
5. Ni kwa njia gani na kwa sababu gani “mtini” wa Kiyahudi ulikatwa ukaangushwa, na ni wakati gani ‘ulipotupwa motoni’?
5 Lakini, wakati wa nusu moja ya mwaka huo wa nne, siku chache kabla ya kufa kwake, Yesu aliulilia Yerusalemu akauambia mji mkuu huo wa taifa la Kiyahudi kwamba nyumba yao ilikuwa imeachwa pekee. (Mathayo 23:37-39) Yehova, yule mwenye “mtini” wa Kiyahudi, alikuwa amerudia kuukagua katika majira hayo ya nne ya kuutunza sana sana. Alipoukuta mti huo wa taifa zima ukiwa bila matunda, aliagiza ukatwe na kuangushwa kupatana na kanuni iliyotajwa na Yesu kwenye Mathayo 7:19. Kwa njia hiyo Ufalme wa Mungu uliondolewa katika taifa la Kiyahudi likapewa taifa lenye kuzaa matunda, yaani, Israeli wa kiroho. (Mathayo 21:43) Badiliko hilo lilitukia katika Pentekoste ya mwaka ule ule, yaani, 33 W.K. Miaka 37 baadaye, katika mwaka wa 70 W.K., ule “mtini” uliokatwa ‘ulitupwa motoni’ wakati Yerusalemu na taifa la Kiyahudi vilipoharibiwa.—Mathayo 3:9, 10; Luka 19:41-44.
“Mradi Unabaki Katika Fadhili Zake”
6. Mifano ya mtini usiozaa na ule mzeituni uliopandikizwa inakaziaje fadhili za Mungu na ukali mwingi wake?
6 Kama vile mfano wa mtini huo unavyoonyesha kuna mipaka ya mahali subira ya Yehova inaweza kufika, mfano wa Paulo wa mzeituni unaonyesha pia ukali wake ingawa unakazia fadhili za Yehova. Kwa fadhili zake, Yehova alikuwa ametuma Yohana Mbatizaji ayaendee “matawi ya asili” ya Kiyahudi akayaambie ‘yazae matunda yapasayo toba’ na kumwamini Yesu. (Mathayo 3:8; Matendo 19:4) ‘Yalikatwa’ kwa sababu ya ukosefu wa imani. Mpunguo huo katika hesabu ya “matawi ya asili” ya Kiyahudi ukawa ‘utajiri kwa Mataifa,’ kwa kuwa ‘matawi ya mzeituni-mwitu’ ya Mataifa yalipandikizwa kwenye mti wa agano la Kiabrahamu yawe sehemu ya uzao wa kiroho wa Abrahamu.—Warumi 11:12, 17, 20, 21, NW.
7. Paulo aliongeza onyo gani?
7 Lakini Paulo anaongeza onyo. Akiwaambia Wakristo waliotiwa mafuta wasio Wayahudi, yeye anasema: “Kwa maana ikiwa Mungu hakuyaachilia matawi ya asili, wala yeye hatakuachilia wewe. Basi, ona fadhili na ukali mwingi wa Mungu. Kuelekea wale [Wayahudi] ambao walianguka kuna ukali mwingi, lakini kuelekea wewe [Mataifa] kuna fadhili za Mungu, mradi unabaki katika fadhili zake; au sivyo, wewe pia utakatwa.” (Warumi 11:21, 22, NW) Ili wabaki katika fadhili za Yehova, Wakristo Mataifa waliopandikizwa katika mti wa agano la Kiabrahamu walipaswa kuonyesha imani yenye nguvu katika ule Uzao wa Abrahamu ulio wa kwanza. Walikuwa ‘wakisimama kwa imani,’ na walipaswa kuthibitisha walikuwa na imani hiyo kwa kuwa na matunda ya Kikristo, ‘kutoa miili yao iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu.’—Warumi : 11:20; 12:1, NW.
8. Ni somo gani jingine lenye mafaa ambalo Paulo alitokeza kutokana na mfano wake wa mzeituni?
8 Paulo alionyesha somo jingine lenye mafaa kutokana na njia nzuri ajabu ambayo Yehova anatumia kuwezesha mti wa agano la Kiabrahamu uzae hesabu kamili ya “matawi” 144,000 ya Wayahudi na Mataifa. Anaendelea kusema hivi akiambia namna zote mbili za “matawi” hayo: “Mimi naambia kila mmoja aliye huko kati ya ninyi asifikiri mengi zaidi juu yake mwenyewe kuliko inavyohitajiwa kufikiri; bali afikiri ili aweze kuwa na akili timamu, kila mmoja kama vile Mungu amemgawia yeye kipimo cha imani. Kwa maana sawa na vile sisi katika mwili mmoja tulivyo na washiriki wengi, lakini si washiriki hao wote walio na utendaji ule ule mmoja, ndivyo sisi, ingawa wengi, tulivyo mwili mmoja katika mwungano pamoja na Kristo.” (Warumi 12:3-5, NW) Wakristo Wayahudi na hata wasio Wayahudi walikuwa wameingizwa katika uzao wa kiroho wa Abrahamu kwa “fadhili za Mungu.” Paulo aliwakumbusha hivi: “Si ninyi mnaoushikilia mzizi [Yehova], bali mzizi unashikilia ninyi.” (Warumi 11:18, NW) Ili waepuke ‘kukatwa’ ingewalazimu kubaki katika fadhili za Mungu kwa kuendeleza umoja wao wakiwa “mwili mmoja katika mwungano pamoja na Kristo.”—Warumi 11:22, NW.
9. Hapo pana somo gani kwa ‘‘kondoo wengine,” kwa hiyo ni lazima wajiangalie wafanye nini?
9 Je! onyo hilo walilopewa Wakristo waliotiwa mafuta lina somo fulani kwa Wakristo wa leo wasio Waisraeli wa kiroho? Hakika linalo. Ingawa wao si sehemu ya uzao wa kiroho uliozaliwa na agano la Kiabrahamu na hivyo wao “si wa zizi hili,” hao “kondoo wengine” hakika ni sehemu ya ‘mataifa ya dunia’ yanayoweza kujibariki kupitia ule uzao. (Yohana 10:16a; Mwanzo 22:18) Basi ni lazima wawe na imani kama Abrahamu, ambaye pia ana mataraja ya kupata uzima wa kidunia, kisha ‘wazifuate hatua za imani yake.’ (Warumi 4:11, 12, 16) Ni lazima waonyeshe wanajitiisha kwa Mchungaji Mwema, Kristo, yule aliye Uzao wa Abrahamu ulio wa kwanza. Ni lazima pia wafanye ushirikiano pamoja na mabaki ya uzao wa Abrahamu ulio wa pili, wawe “kundi moja” pamoja nao wakiwa chini ya “mchungaji mmoja.” (Yohana 10:14, 16b) Ikiwa Wakristo waliotiwa mafuta wanaweza kuwa katika hatari ya ‘kukatwa’ watoke katika mti wa agano la Kiabrahamu wasipobaki katika fadhili za Mungu, je! haiwapasi pia “kondoo wengine” wajiangalie wasifanye jambo lo lote linaloweza kuwafanya wapoteze nia njema ya Yehova?—Warumi 11:22.
“Wasipobaki” Wakiwa na Ukosefu wa Imani
10. Ni jambo gani lingeweza kutokea kama Myahudi hakubaki katika ukosefu wake wa imani, na hiyo ingemaanisha nini kwake?
10 Mfano wa mzeituni una somo jingine la ujumla linaloweza kuwahusu Wakristo waliotiwa mafuta na “kondoo wengine.” Tunalipata katika andiko la Warumi 11:23, ambalo linasema hivi: “Wao pia [Wayahudi wasio na imani], wasipobaki katika ukosefu wao wa imani, watapandikizwa; kwa maana Mungu anaweza kuwapandikiza tena.” Hapo tunaona upande mwingine wa fadhili za Mungu. Wakati Paulo alipoiandika barua hii (karibu na mwaka wa 56 W.K.), taifa la Kiyahudi lilikuwa limekwisha kukatwa zamani likiwa “mtini” usiozaa matunda. Au, tukiurudia mfano wa mzeituni, hesabu iliyo kubwa ya “matawi ya asili” ilikuwa ‘imekatwa’ kwa sababu ya ukosefu wao wa imani katika Yesu, yule Masihi. Lakini kama mtu ye yote mmoja mmoja kati ya Wayahudi hakubaki katika ukosefu wake wa imani, Yehova Mungu alikuwa na nia ya kumpandikiza arudi katika ule mzeituni wa mfano na kumfanya awe mshiriki wa uzao wa kiroho wa Abrahamu. Hatua ya Yehova ya kumpokea tena Myahudi huyo mwenye kutubu ingemaanisha amepata “uhai baada ya kufa.”—Warumi 11:14, 15.
11. Ni jambo gani limepata wengine wa “kondoo wengine,” lakini inawapasa wafanye nini?
11 Leo, wengine wa “kondoo wengine” wamekuwa na kinaya (hali ya kuona yote ni sawa tu) na, kupitia ukosefu wa imani, wakaacha kumtumikia Yehova. Wamejitenga mbali na ushirika wa bidii pamoja na watu wake. Wengine wao wameingia katika mashaka (magumu makubwa), na maonyo yaliyo katika Neno la Mungu ‘yamewapata.’ Je! wajisikie kwamba wamekwisha kupotea ikawa haiwezekani kwao kurudi? Neno la Mungu linasema: “Lakini huko [nje ya “nchi” ya watu wa Mungu], kama [ukimtafuta Yehova], Mungu wako, utampata, ukimtafuta kwa moyo wako wote, na [nafsi] yako yote. Na wakati uwapo katika mashaka, ukiisha kupatwa na mambo haya yote [ya maonyo], siku za mwisho, utamrudia [Yehova], Mungu wako, na kuisikiza sauti yake; kwa kuwa [Yehova], Mungu wako, ni Mungu wa rehema.”—Kumbukumbu la Torati 4:29-31.
12. (a) “Mtumwa mwaminifu” ameonyeshaje hangaiko kwa “kondoo wengine” hao waliopotea njia? (b) Wewe unaweza kusimulia mifano gani kuonyesha kwamba wengine wamelirudia kundi wakiwa na shukrani?
12 Akiwa kikundi chenye umoja cha matawi yenye kuzaa matunda ndani ya ule mti wa agano la Kiabrahamu, “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” yaani, wale mabaki wa watiwa mafuta wa Kristo walio duniani, wanaona sana kwamba wengine wa wale “kondoo wengine” wanahitaji kuamka watoke katika kinaya na kuwa tena Wakristo wenye kuzaa matunda. (Mathayo 24:45-47) Kwa kusudi hilo, “mtumwa” huyo anapanga zichapwe makala kama ile inayosema “‘Mrudieni Mchungaji wa Nafsi Zenu,’ “iliyo katika toleo hili la Mnara wa Mlinzi. Kuanzia Januari 1982, Huduma ya Ufalme Yetu ilichapisha mfululizo wa makala zenye kichwa icho hicho. Je! uongozi thabiti huo kutoka kwa “mtumwa” wa Bwana umezaa matunda yo yote? Je! wengine wamemrudia Yehova Mungu wao? Wengi wamemrudia. Angalia mifano halisi katika ukurasa huu.
‘Mzae Sana’
13. Wo wote ambao wamekuwa na kinaya wanapaswa kufanya nini sasa, kama inavyoonyeshwa na maneno gani ya Yesu?
13 Ndiyo, Wakristo wo wote waliotiwa mafuta au wenzi wao wa “kondoo wengine” ambao wamekuwa na kinaya na kuwa wasiozaa matunda wanapaswa kukubali msaada ili wawe tena Wakristo wenye kuzaa matunda. Katika mfano unaotofautiana katika mambo kadha na ile ya mzeituni na mtini usiozaa, Yesu alijifananisha na shina la mzabibu na akawalinganisha wanafunzi wake waliotiwa mafuta na matawi ya mzabibu. Alisema hivi: “Mimi ndimi mzabibu wa kweli, na Baba yangu ndiye mkulima. Kila tawi ndani yangu lisilozaa huliondoa; na kila tawi lizaalo hulisafisha, ili lizidi kuzaa. . . . Hivyo hutukuzwa Baba yangu, kwa vile mzaavyo sana; nanyi mtakuwa wanafunzi wangu.”—Yohana 15:1-8.
14. (a) Ni kwa njia gani mbili lazima Wakristo wote waendelee ‘kuzaa sana’? (b) Ni takwa gani kwa Wakristo waliotiwa mafuta limeonyeshwa katika mfano wa ule “mzabibu wa kweli”?
14 Ingawa “kondoo wengine” si matawi ya ule “mzeituni” wa agano la Kiabrahamu wala si matawi ya ule “mzabibu wa kweli,” yaani, Kristo Yesu, ni lazima wajithibitishe kuwa wanafunzi wa Kristo. Ni lazima wao waendelee ‘kuzaa sana’ kama yale “matawi” yote ya Wakristo waliotiwa mafuta. Wanafanya hivyo kwa kuzaa sifa za mfano wa Kristo za utu mpya, kutia ndani ‘tunda la roho.’ (Wagalatia 5:22, 23; Mathayo 28:19, 20; Wakolosai 3:5-14) Lakini ili wazae sana matunda wanaonyesha kwa matendo kwamba wana sifa hizo kwa kushiriki katika kazi ya kuzihubiri “habari njema hizi.” (Mathayo 24:14, NW) Sawa na vile ilivyo lazima “matawi” yaliyotiwa mafuta ya ule “mzabibu wa kweli” yabaki katika mwungano pamoja na Kristo, ni lazima pia “kondoo wengine” wabaki katika mwungano wa karibu pamoja na “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” yaani, “ndugu” za Kristo waliotiwa mafuta. Hivyo tu ndivyo wao wanavyoweza kutumainia ‘kurithi ufalme waliowekewa tayari tangu kuumbwa ulimwengu.’—Mathayo 25:31-40.
‘Mataifa ya Dunia’ Tayari Yanajibariki
15. Wakati lile agano la Kiabrahamu linapomaliza kuzaa “uzao” ulioahidiwa, andiko la Warumi 11:12 linachukua umaana gani zaidi?
15 Wakati mzeituni wa agano la Kiabrahamu unapoendelea kumaliza kuzaa hesabu kamili ya “matawi” ya Mataifa na Wayahudi ukiwa pamoja na ‘mzizi wake wa unono’ (Yehova) na shina lake lililo imara (Kristo), tayari baraka nyingi zinawaendea “watu wa mataifa” wasio Waisraeli wa kiroho. Paulo alitangulia kuona jambo hilo na akaandika hivi: “Sasa ikiwa hatua ya uongo waliyochukua [Wayahudi wa asili] inamaanisha utajiri kwa ulimwengu, na upungufu wao unamaanisha utajiri kwa watu wa mataifa, ni kwa kadiri kubwa inayozidi kama nini ile hesabu kamili yao [Wakristo Wayahudi waliotiwa mafuta] itamaanisha utajiri!—Warumi 11:12, NW.
16. (a) “Hatua ya uongo” iliyochukuliwa na Wayahudi ilimaanishaje “utajiri kwa watu wa mataifa”? (b) Ile kazi ya kupandikiza imefikia hatua gani?
16 Tumekwisha kuona kwamba “hatua ya uongo” iliyochukuliwa na taifa la Kiyahudi kwa ujumla ilifanya Mataifa yapate utajiri mkubwa wa kiroho. Lakini kuwa hivyo kwa matawi ya mzeituni-mwitu washiriki wa uzao wa kiroho wa Abrahamu hakukuyaondoa katika mzeituni wa mfano yale matawi ya asili, yaani, Wakristo waaminifu wa Kiyahudi, ambayo ama yaliachwa yakiwa kwenye mti au ‘yakarudishwa kwa kupandikizwa’ baada ya mwaka wa 36 W.K. Kwa hiyo yale matawi 144,000 yanatia ndani “hesabu kamili” ya Wayahudi na “hesabu kamili” ya watu wasio Wayahudi. (Warumi 11:12, 15, NW) Mambo ya uhakika yanaonyesha kwamba mpandikizo huo uliendelea mpaka miaka ya katikati-katikati ya 1930. Leo, wakati huu ambao siku zimesonga sana, kuna sababu nzuri ya kuamini kwamba “hesabu kamili” ya matawi ya Wayahudi na hata Mataifa imekwisha kupandikizwa. Matawi yo yote yaliyopandikizwa baada ya mwaka wa 1935 yangefikiriwa kwa sababu nzuri kuwa yanachukua sehemu zilizoachwa wazi za matawi ya Kiyahudi au yasiyo ya Kiyahudi yanayokatwa kwa sababu ya kukosa kuzaa matunda.
17. Ni kwa njia gani kukamilishwa kwa ushiriki wa kuwa katika uzao kunamaanisha utajiri mkubwa hata zaidi kwa “watu wa mataifa”?
17 Sasa, Paulo anasema kwamba kukamilishwa hivyo kwa ushiriki wa kuwa katika uzao wa Abrahamu ‘kunamaanisha utajiri kwa watu wa mataifa.’ Ndivyo ilivyo hata zaidi kwa sababu utajiri huo mwingi na baraka za kiroho hazihusu makumi machache tu ya maelfu ya Wakristo waliotiwa mafuta wasio Wayahudi (kama katika utimizo wa sehemu ya kwanza ya Warumi 11:12) bali zinahusu mamilioni ya “watu wa mataifa” wasio wa mzeituni wa mfano.
18. Ni nini linaloweza kusemwa juu ya zile ahadi za agano la Kiabrahamu, kwa hiyo ni sehemu gani ya agano hilo lazima iwe imekwisha kuanza kutimizwa?
18 Jambo hilo linaturudisha kwenye agano la Kiabrahamu. Ule Uzao ulio wa kwanza, yaani Kristo Yesu, sasa amekwisha kuwekwa katika kiti cha ufalme katika mbingu. Yeye amewakusanya washiriki wa uzao ulio wa pili akawaingiza katika jamaa ya agano la Kiabrahamu. Yuko karibu ‘kumiliki mlango wa adui zake,’ kwa kuleta uharibifu wa milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, Babuloni Mkuu, na wa sehemu ile nyingine yote ya tengenezo lionekanalo la Shetani. (Mwanzo 22:17, 18) Basi, si jambo la kushangaza kwamba sehemu ya kumalizia ya ahadi aliyopewa Abrahamu imeanza tayari kutimizwa: “Katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia.”
19. (a) Watu wa kutoka “mataifa yote ya dunia” wameanzaje kujibariki? (b) Tumaini lao ni nini?
19 Ndiyo, “kundi kubwa . . . kutoka mataifa yote,” linalotia ndani Wayahudi wa asili wasio wachache, tayari linajibariki. Watu hao wamejiunga na mabaki ya Israeli wa kiroho wakiwa na imani kamili katika yule Abrahamu Mkubwa Zaidi, Yehova Mungu, nao “wanamtolea yeye utumishi mtakatifu mchana na usiku katika hekalu lake,” wakiwa na tazamio la kupata uzima wa milele duniani. (Ufunuo 7:4, 9-17, NW) Na waendelee kujiletea baraka nyingi kupitia ule uzao, moja kwa moja mpaka ndani ya mfumo mpya wa mambo.
Je! wewe umeelewa?
◻ Ule mtini usiozaa ulifananisha nini, ulikatwa ukaangushwa wakati gani, na ulichomwa wakati gani?
◻ Ni kwa njia gani pekee Wakristo Wayahudi na Mataifa wangeweza kuepuka kukatwa waondolewe kwenye “mzeituni,” na tunaweza kujifunza somo gani hapo?
◻ Kwa sababu gani kurudishwa kwa Wayahudi wenye kutubu kwa njia ya kupandikizwa kunaweza kuwa chanzo cha faraja kwa wo wote ambao wamepotea njia?
◻ Ni kwa njia gani mbalimbali lazima Wakristo wote waendelee kuzaa matunda?
◻ Ni kwa njia gani ‘watu wengi wa mataifa’ tayari wanajibariki?
[Sanduku/Picture katika ukurasa wa 16]
Hawa ‘Wamemrudia Mchungaji na Mwangalizi wa Nafsi Zao’—1 Petro 2:25, NW
Mwanamke mmoja katika Normandy, Ufaransa, anaandika hivi: “Baada ya miaka kumi ya kutokutenda na jitihada kadha zisizo na matokeo za kujaribu kurudia kundi [la Mashahidi wa Yehova], bado mimi nilisitasita kuchukua hatua. Kwa sababu ya mwenendo wangu usiopatana na Maandiko nilioufuata tangu niliache kundi, niliogopa kutiwa adabu na Yehova na nikaogopa kutazamwa kwa njia yenye aibu na wazee na wengine wote kundini. Nilipokuwa katika likizo pamoja na baba mkwe na mama-mkwe nilichukua nakala ya Mnara wa Mlinzi nikasoma kisa cha ndugu asiyetenda ambaye hali yake ilikuwa imekuwa sawasawa na yangu. Niliposoma namna Yehova alivyokuwa amemfadhili, namna wazee walivyokuwa wamempa msaada wenye upendo, na namna washiriki wa kundi walivyokuwa wamemkaribisha tena, nikapata nguvu za kurudia tengenezo la Yehova.”
Suzanne, Shahidi mmoja katika kundi la huko mashariki ya kaskazini ya Ufaransa, anaandika hivi: “Mimi nampigia Yehova, Mwanaye Yesu Kristo na ‘mtumwa mwaminifu mwenye akili’ asante ya unyofu wa moyo kwa msaada unaotolewa kwa wasiotenda. Mimi mwenyewe nilikuwa nisiyetenda wakati wazee waliponitembelea wakajitolea kunipangia mtu wa kujifunza nami Biblia. Mimi nilikubali toleo lao na sasa ninafurahi sana kwa sababu ninahudhuria mikutano tena na kushiriki kwa ukawaida katika kazi ya kuhubiri. Sasa naweza kuwaonyesha upendo wa kidada wengine wanaohitaji kitia-moyo.”
Yolande, Shahidi mwingine wa kike Mfaransa, alikuwa amekosa mikutano yote kabisa muda wa miaka mingi na akaacha kusali kwa sababu alijisikia kuwa mwenye hatia ya kuiacha meza ya Yehova. Aliposaidiwa kurudia utendaji wa Kikristo wenye kuzaa matunda, yeye anaandika hivi: “Mimi namtolea Yehova shukrani zangu zenye kina kirefu kwa kunisaidia mimi na kunipa nafasi nyingine. Kwa moyo wangu wote mimi nawatia moyo wote ambao wamelegeza mwendo kwa sababu fulani wamrudie Yehova.”
[Picture]
Kwa kupewa kitia-moyo chenye upendo, watu wengi waliokuwa wasiotenda wamekuwa tena ‘wazaaji wa matunda’
[Mchorokatika ukurasa wa 13]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Mfano wa Paulo wa mzeituni unaonyesha namna agano la Kiabrahamu linavyozaa “uzao” kamili wa kiroho
AGANO LA KIABRAHAMU (Mwanzo 22:16-18)
UZAO ULIO WA KWANZA UZAO ULIO WA PILI
KRISTO (Wagalatia 3:16) (Wagalatia 3:27-29)
“Hesabu kamili” ya “Hesabu kamili” ya
“matawi ya asili” “matawi mzeituni-mwitu”
(Baki la Kiyahudi (Wakristo waliotiwa mafuta
na Wayahudi waliotubu wasio Wayahudi—
baadaye—Warumi 11:5,12, Waroma 11:25)
Ro 11:21 , 23) “Israeli wote,”
Waisraeli wa kiroho 144,000
Washiriki 144,001 wa “uzao” wa kiroho
wa Abrahamu, wa kubariki “mataifa yote
ya dunia”