Pigano Letu la Kuzuia Wendekevu
“Sisi tunako kushindana mweleka . . . juu ya majeshi ya roho yenye uovu katika mahali pa kimbingu. Kwa sababu hiyo twaeni suti kamili ya silaha kutoka kwa Mungu, ili mpate kuweza kupinga katika ile siku ya uovu na . . . kusimama imara.”—WAEFESO 6:12, 13, NW.
1. Watu wengi kwa ujumla wana maoni gani juu ya ulimwengu wa leo?
KUNA kitu fulani katika hewa ya ulimwengu mbovu huu. Je! wewe unaweza kukigundua? Bila shaka, wengi kati yetu tunakubali kwamba cho chote kinachoienea namna ya kuwaza na mwenendo wa ulimwengu huu kinatoa ushuhuda wenye kuonyesha ni chenye kuharibu afya na kufisha. Tunaweza kuyaona matokeo katika jamii hii ya watu wagonjwa-wagonjwa katika hali ya kiadili na ya kiroho.
2. Ni kiishara gani kimoja kinachoonyesha wazi ugonjwa wa wanadamu?
2 Kiishara kilicho wazi cha ugonjwa huo ni wendekevu (kuruhusu matendo yo yote yafanyike hata kama ni mabaya), nao unaongoza vyepesi kwenye uasi. Watu wengi hawataki kuziepuka zile kanuni za kawaida tu za tabia ya kibinadamu; bali, wao wanajaribu kutupilia mbali karibu vizuizi vyote walivyowekewa. Wanafanya fujo wakidai sana haki yao ya kufanya lo lote liwapendezalo, wakati wo wote wapendao, na kuwa huru wasiwe chini ya mamlaka inayowasimamia, iwe ni wazazi, mawakili wenye kutekeleza sheria au vizuizi vinavyoongoza maadili katika jamii ya watu. Ni nani au ni nini kinachochochea roho hi ya kutokutii? Kwa sababu gani ni lazima Wakristo wafanye pigano la kukaza nia ili wazuie wendekevu huo?
3. (a) Tunaweza kumtambuaje yule anayehusika zaidi katika kufanya wendekevu na uasi uenee sana duniani? (b) Mtu anaonyeshaje kwamba yeye anatokana na Ibilisi?
3 Uhakika wa kwamba kutokutii kulianza na wanadamu katika bustani ya Edeni unajulikana sana. Lakini ni nani kwanza aliyetokeza wendekevu na kuwatega Adamu na Hawa mtego wa kuwafanya wapotoke? Yesu alitambulisha mtu huyo wakati alipoambia Mafarisayo wanafiki kwamba wao ‘walipenda kutenda tamaa za baba yao, Ibilisi,’ ambaye baadaye Yesu alimtambulisha kwa kumwita “mkuu wa ulimwengu huu.” (Yohana 8:44; 14:30) Ibilisi, ambaye “hutenda dhambi tangu mwanzo,” amejaribu kuongoza wanadamu akiwa na makusudi ya kujifaidi mwenyewe. Wale wanaofanya mazoea ya kuwa na uasi wametokana naye.—1 Yohana 3:8.
4. (a) Mavutano ya Shetani yana mweneo gani? (b) Kuna uhusiano gani kati ya wendekevu na uharibifu?
4 Maandiko yanaonyesha wazi kwamba mavutano ya Kishetani yameenea kote kote, kama vile hewa inayoizunguka sayari yetu. Mtume Paulo alimtaja Ibilisi kuwa “mfalme wa uwezo wa anga, roho yule atendaye kazi sasa katika wana wa kuasi.” (Waefeso 2:2) Watu mmoja mmoja wanaojiacha wapofushwe na njia ya kuwaza ya ulimwengu wataelekea zaidi kuongozwa na mavutano yake. Shabaha ya Ibilisi na kundi lake la mashetani ni kupoteza wanadamu kwa njia yo yote wanayoweza kupata ili waharibu mambo yaliyo mema na yenye kufaa. Kwa hiyo, mashetani hao wanachochea vikali roho ya wendekevu mkubwa kabisa. Kwa sababu gani? Kwa sababu watu wanaochagua kufuata nia hiyo ya wendekevu wanajiacha kwa urahisi zaidi wafanywe wagumu na uwezo wenye kudanganya wa dhambi. (Waebrania 3:13) “Wana wa kuasi” wanavuna uharibifu kwa sababu ya kuupandia mwili wakiwa na wendekevu.—Wagalatia 6:7, 8.
Wakristo Wana Pigano
5-7. (a) Shetani anatumia njia gani za kushambulia wanadamu? (b) Ni njia gani iliyo ngumu zaidi kushughulika nayo? Toa mfano.
5 Majeshi ya roho waovu yanakusudia hasa kupindua na kutega Mashahidi wa Yehova, wanaojitahidi kushika amri za Mungu. Paulo anaonya kwamba sisi tuna pigano, “si juu ya damu na nyama, bali juu ya . . . majeshi ya roho yenye uovu katika mahali pa kimbingu.” (Waefeso 6:12, NW) Tunapolazimika kushindana na mashambulizi ya uso kwa uso ya dhihaka, mateso na kufungwa gerezani, pigano letu la kiroho linakuwa kama vita ya wazi. Ijapokuwa huenda mashambulizi hayo ya moja kwa moja yakatufanya tuimarishe uzuizi wetu, njia ya ujanja, isiyo ya moja kwa moja huenda ikatunasa bila ya sisi kujua, kwa kuvutia udhaifu mbalimbali wa mwili wetu. Kwa hiyo tunahitaji kuwa macho sikuzote kwa sababu mara nyingi sana ni lazima tuzizuie katika pigano letu njia za ujanja au zisizotazamiwa ambazo zinatumiwa kwa kusudi la kubomoa pole kwa pole jitihada zetu za kufuata kanuni za kimungu na kuharibu uhusiano wetu na Yehova.
6 Kwa mfano, labda wewe umelazimika wakati fulani kuchukua msimamo wa kutetea kisa cha kutokutiwa damu. Labda watu wa ukoo wasioamini au madaktari walikukaza ukubaliane nao. Katika pigano hilo la kuendeleza ukamilifu ulikuwa na nia ya kuvumilia mkazo mwingi. Kwa sababu gani? Kwa sababu suala lenye kuhusika lilionekana waziwazi. Ulikuwa umekaza nia usivunje amri ya Mungu. (Matendo 15:28, 29) Fikiria, pia, ndugu Wakristo waliojitenga na ulimwengu kwa kukataa kununua kadi za chama cha kisiasa ingawa kukataa kwao kuliwaletea taabu. (Yohana 17:16; 1 Petro 3:14; 4:12-14) Wengine wamevumilia kufungwa gerezani kwa sababu ya msimamo wao wa kutokuwamo katikati ya magomvi ya kilimwengu. (Isaya 2:4) Kukataa kuacha kuzihubiri habari njema kumeletea wengine namna nyingine za mateso.—Matendo 5:28, 29, 40.
7 Ndiyo, watu wa Yehova wamesimama imara mara nyingi walipoelekeana na masuala hayo, wakatoa ushuhuda wa kuonyesha wana ukamilifu na ushikamanifu kwa kanuni za Biblia. Lakini nyakati nyingine inakuwaje tunapoelekewa na majaribu yanayohusu kumomonyolewa (kuondolewa) pole kwa pole kwa ushikaji wetu wa viwango vya Kikristo? Wendekevu unafanya wengine wayumbe-yumbe.
8. Ni katika pande gani haitupasi tujiachilie tudanganywe?
8 Tunahitaji kujihadhari tusiruhusu hali zinazoonekana kama kwamba si mbaya zisije zikatutia hangaikio la vitu vilivyo katika mfumo huu, kwa maana kufanya hivyo kungeweza kulinyonga lile neno lililo katika moyo wetu au kutuongoza tuingie ndani ya makosa. (Mathayo 13:22) Kufanya hivyo kunaweza kutupotezea upendeleo wa kimungu na uzima sawasawa na vile kuacha mateso na mashambulizi mengine ya uso kwa uso kunavyoweza kutubomoa au kutushinda nguvu. Tusidanganyike tufikiri kwamba mashirika mabaya, kujifurahisha katika mambo mabaya, kujiingiza mno katika matumizi ya vileo na vitu kama hivyo hakuwezi kututega na kuharibu hali yetu ya kiroho. Mambo hayo yamefagia hesabu fulani ya watu.
Matokeo Yenye Kusikitisha ya Wendekevu
9. Mwenendo wa wendekevu ulitokezeaje Waisraeli fulani matatizo?
9 Israeli wa kale walitaabika sana wakiwa taifa zima wakati nia za wendekevu za watu fulani zilipowatia katika magumu makubwa sana. Kumbuka namna Balaamu na Balaki walivyotia “ukwazo mbele ya Waisraeli, kwamba wavile vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu, na kuzini.” (Ufunuo 2:14) Jambo hilo lilianzaje? Lilianza wakati wengine walipoukubali ukaribishaji wa waabudu-Baali ili wakale na kunywa, kisha kukawa na shangwe za mambo ya kuwatia raha. Kuonyesha kutokuridhishwa na matayarisho ya Yehova kwa kuchagua kushirikiana na watu hao wa nje kulifanya wanaume wa Kiisraeli waamke nyege. Halafu? Walifanya uasherati na wanawake Wamoabi na Wamidiani na kuiinamia miungu yao. Yehova aliwaonyesha hasira kali Waisraeli hao. Watu 24,000 walikufa kuonyesha alitoa hukumu yake. (Hesabu 25:1-9) Looo, hasara gani jamani kwa sababu ya wendekevu!
10. (a) Mwenendo wa Dina wa wendekevu uliongozaje kwenye huzuni nyingi? (b) Mwendo wa wendekevu wa Sulemani uliongoza kwenye nini pole kwa pole?
10 Pia kuna mifano ya watu mmoja mmoja ambao wendekevu wao uliwaingiza matatani. Dina, binti yake Yakobo, alienda kuwatembelea wasichana Wakanaani nchini. Matokeo ya uzembe wa Dina wa kutokujali mashirkia yake yalikuwa nini? Alichafuliwa na mmoja wa wana wa Hamori. Upumbavu huo wenye kuleta aibu nyingi uliwakasirisha wana wa Yakobo, ukawachochea Simeoni na Lawi waue kila mwanamume aliyekuwa huko Shekemu, na huku wana wale wengine wa Yakobo wakajiunga katika ushambulizi huo na kuteka nyara katika mji huo, na hapo Yakobo akawa na kihoro. (Mwanzo 34:I, 2, 7, 25-31) Hata Sulemani, mmoja wa watu wenye hekima zaidi, alijitwalia kwa wendekevu wake walioabudu miungu ya kigeni. ‘Wakaelekeza moyo wake pole kwa pole’ hata miaka ya baadaye yeye akafuata miungu mingine, akitenda yaliyokuwa mabaya machoni pa Yehova.—1 Wafalme 11:1-6, NW; Kumbukumbu la Torati 17:17.
11. Inatupasa tukumbuke nini juu ya wendekevu?
11 Wewe unafahamu nini kutokana na mifano hiyo ya Biblia? Kilicholeta anguko la wengine wa waabudu wa kweli si ushambulizi wa uso kwa uso wa Ibilisi wa papo kwa hapo. Lakini kwa sababu ya wao kuwa na hali ya kuwaza kwa njia ya wendekevu Ibilisi aliweza kugeuza wengine pole kwa pole wakaiacha njia ya unyofu.
Njia za Werevu Zinazotumiwa Leo
12, 13. Ni katika njia gani mbalimbali lazima Mkristo ajihadhari na mbinu zinazotumiwa na Shetani?
12 Shetani, yule “mfalme wa uwezo wa anga,” anatumia njia za werevu zinazofanana na hizo leo. Yeye anajiambia, bomoa-bomoa kwanza, halafu geuza wasiojua neno watoke katika njia ya uadilifu. Basi, Wakristo wanahitaji kujihadhari na mawazo na maelekeo ya ulimwengu huu mbovu. Au sivyo, watawezaje kubaki bila lawama katikati ya “kizazi chenye ukaidi, kilichopotoka”?—Wafilipi 2:15; 2 Timotheo 3:13.
13 Mithali 13:20 inatuambia kwamba “rafiki wa wapumbavu ataumia.” Ni kweli kama nini! Mara nyingi mbegu za wendekevu zinapandwa na kukuzwa baada ya mtu kujichangamanisha na kushirikiana na washiriki wasiofaa, wawe wamo ndani au nje ya kundi la Kikristo. (2 Wathesalonike 3:14; Kutoka 23:2a) Ikiwa washirika wetu wana maelekeo ya kufuata maoni ya kilimwengu, ya kujitafutia anasa, hakika kutatokea matatizo. Ndivyo ilivyo hasa ikiwa tunashawishwa ‘tuzurure-zurure katika mahema ya uovu.’—Zaburi 84:10, NW.
14. Maoni ya watu wengi ni nini juu ya kufurahia anasa?
14 Ulimwengu kwa ujumla unapenda vitu ulivyo navyo, kutia ndani kuona raha ya anasa zisizo na mipaka. (2 Timotheo 3:4) Yale maoni ya kwamba hakuna jambo jingine lililo la maana kuliko kuona raha yanavutia watu wengi. Falsafa hiyo inafundisha kwamba wajibu wa kufuata maadili unatimizwa kwa kutosheleza tamaa za kutafuta anasa ambazo ni asili ya mwanadamu. (1 Wakorintho 15:32) Njia hiyo ya kufikiri inaweza kubomoa njia ya maisha ya Mkristo.
15. (a) Huenda tukadanganywa namna gani na sura za juu-juu? (b) Ni maulizo gani yenye kuamsha mawazo ambayo vijana wanapaswa kuuliza juu ya mashirika?
15 Ikiwa wewe unaenda shuleni, una maoni gani juu ya wanafunzi wale wengine wasioonyesha wanapendezwa kumtumikia Yehova Mungu? Huenda wakaonekana kuwa watu wazuri-wazuri. Hata hivyo, wengi wao wanavuta sigara na kunywa vileo vilivyokatazwa. Hawaoni ubaya wo wote kutumia dawa za kulevya zinazorusha akili. Ushirika pamoja na watu wa namna hiyo utakuwa na matokeo gani kwako? Wewe unaweza kujipatia anasa gani kutokana nao kabla hawajaweza kukushinda au kukukaza kabisa uingie katika maovu yao? Hata kama utakataa, utafanya nini wakikufanyia dhihaka na kukuita-ita majina yasiyofaa? Je! imani yako wewe ina nguvu zisizoweza kwisha hivi kwamba unaweza tu kuendelea kushirikiana nao na bado usipatwe na kasoro? (1 Wakorintho 10:12) Je! wewe utajiacha ushindwe na kishawishi kisha ujitie ndani ili “kuonja,” ili kuona tu mambo yako namna gani? (Mithali 1:10) Je! wewe unafikiri kwamba kwa kuendelea na ushirika wa namna hiyo utabaki mwenye nguvu, imara, mwenye kukaza nia na kuwa mshikamanifu kwa Yehova na Neno lake? Ikiwa una maelekeo ya kufikiri hivyo, jihadhari! Tii wazo la Biblia linalosema “zikimbie tamaa za ujanani,” ndiyo, “ikimbie zinaa [uasherati, NW].” (2 Timotheo 2:22; 1 Wakorintho 6:18) Ili kuzuia wendekevu, “piga vita vile vizuri vya imani” kwa kupinga sana tamaa yo yote au maelekeo ya kuwa na ushirika mbaya.—1 Timotheo 6:12; 1 Wakorintho 15:33, NW.
16. Huenda Mkristo akaelekeana na mitego gani inayohusu ushirika wake na wafanya kazi wenzake?
16 Nyakati nyingine wengine wamekuja kujuta kwa kufanya uhusiano na wafanya kazi wenzao. Mahali pengi pa kazi ya kuajiriwa ni desturi kuwa na chai (karamu) za wafanya kazi au kusherehekea siku za kuzaliwa na sikukuu nyingine. Kwa kawaida katika pindi hizo vileo vinaandaliwa. Huenda kukawa na muziki na kucheza dansi. Mkristo asipofanya pigano azuie wendekevu katika pande hizo, mmomonyoko unaweza kuanza. Kufanya ushirikiano wa kirafiki pamoja na walimwengu kazini kumefanya Wakristo wengine waingie katika matembezi ya wanaume kwa wanawake, wakafanya usherati na makosa mengine.
Kujifurahisha Kubaya
17. Wendekevu juu ya programu za televisheni unaweza kugeuzaje maoni na tamaa za mtu?
17 Nia za wendekevu zinaweza kusitawi pia kuelekea programu za televisheni zinazohusu ufisadi. Televisheni imekuwa ndiyo yaya wa watoto wengi, lakini mara nyingi wazazi hawawekei vizuizi vinavyofaa juu ya mambo watakayotazama na yale wasiyopaswa kutazama. Jambo hilo limeleta matatizo mengi. Kuna watu wazima ambao wamejiachilia wanaswe fikira zao na maonyesho ya televisheni yanayofuatana kwa mfululizo pindi baada ya pindi. Nao wafanya biashara wamewezesha watu waweze kujionea maonyesho fulani ya sinema wakiwa ndani ya nyumba zao bila kulazimika kwenda nje, kwa kutumia kamba za kuzileta katika televisheni au kutumia kaseti za video. Huenda zikawa zina matumizi yanayofaa, hata hivyo watu wengi wanakubali kwamba wanajipatia vitu hivyo ili wajionee katika nyumba zao wenyewe kiasi kikubwa cha kujifurahisha kwa mambo yenye kushusha tabia yanayotamaniwa na kizazi hiki cha uasherati. Ndiyo, mtu anaweza kuchafuliwa akili na moyo akiwa katika chumba chake mwenyewe cha maongezi au cha starehe ikiwa mambo hayo yanapatikana humo. Ingawa “kujifurahisha” kwa namna hiyo kumekuwa malisho ya kila siku ya sehemu kubwa ya watu, ingewapasa Wakristo kukumbuka kitia-moyo cha Paulo wafikirie ‘yo yote yaliyo haki, yaliyo safi na yenye kupendeza.’—Wafilipi 4:8.
Kujichunguza Sisi Wenyewe
18. Kwenye Waefeso 5:3, 4, ni shauri gani zuri ambalo Paulo alitoa?
18 Sisi tulio Wakristo waliojiweka wakf, je! tunawekea jamaa zetu na kundi mfano wa namna gani? Je! tunazoea yaliyo mema safi kiroho na kiadili? (2 Wakorintho 7:1) Kiwango cha hali ya juu tunachopaswa kufuata ni hiki: “Uasherati usitajwe kwenu kamwe, wala uchafu wo wote wala kutamani, kama iwastahilivyo watakatifu; wala [mwenendo wa] aibu wala maneno ya upuzi wala ubishi; hayo hayapendezi; bali afadhali kushukuru.”—Waefeso 5:3, 4.
19. Kwa sababu gani uangalizi wa wenye kukomaa ni wa maana kwenye vikusanyiko vya kiraflki?
19 Ni jambo la maana kuwe na uangalizi unaofaa kwenye vikusanyiko vya kirafiki. Au sivyo, huenda hewa ya wendekevu ikapenya kuharibu pindi hiyo. Ikiwa vileo (pombe) vinaandaliwa, je! watu wanavitumia kwa kiasi? Ikiwa muziki unapigwa, je! ni wa namna ambayo Wakristo waliokomaa hawauoni kuwa wenye kutilika mashaka? Shauri la Maandiko ni ‘kufanya mambo yote kwa utukufu wa Mungu.’ (1 Wakorintho 10:31-33) Kufanya hivyo kunatuongeza nguvu katika pigano la kuzuia wendekevu.
20. Shetani anaweza kujifanya aonekane namna gani ili kudanganya wasiojua neno, lakini Yehova ametoa ulinzi gani?
20 Huu sio wakati wa kusinzia-sinzia katika hali ya kukinai (kutosheka kwamba yote ni sawa tu). (Warumi 13:11-14) Mmomonyoko unaoharibu ushikaji wa kanuni za Biblia unatokea pole kwa pole. Shetani anatumia njia za ujanja kuangamiza imani yetu. Hata anaweza kuonekana kuwa malaika wa nuru. (2 Wakorintho 11:14) Ili tupate ulinzi tunahitaji “suti kamili ya silaha kutoka kwa Mungu” kusudi tusimame imara na kuzuia matendo ya Ibilisi yenye hila. Pigano letu ni “juu ya watawala wa ulimwengu wa giza hili, juu ya majeshi ya roho yenye uovu katika mahali pa kimbingu.” Kwa hiyo tunahitaji silaha zote za kiroho na ulinzi ambao Yehova anatoa, kutia na “upanga wa ile roho, yaani, neno la Mungu,” ili kupinga sana katika hii siku yenye uovu.—Waefeso 6:11-13, 17, NW.
21. Wale wanaopinga sana wendekevu wa ulimwengu wanaweza kutazamia nini?
21 Tunajua kwamba karibuni Yehova atafagilia mbali maovu ya namna zote za wendekevu. Hakutakuwako tena mavutano machafu ya wendekevu huo. Wale watakaouokoka mwisho wa mfumo huu mbovu wataona juu ya dunia pambazuko la Taratibu Mpya ya kupendeza yenye uadilifu, ikiwa chini ya Ufalme wa Mungu ulio mikononi mwa Kristo Yesu. Kaza nia uwe kati ya wale watakaolifurahia pendeleo hilo. Fanya pigano uuzuie wendekevu wa ulimwengu huu kwa kujifahamisha vizuri zaidi kanuni za Neno la Mungu na kuzitumia.—Zaburi 15:1, 2; 19:7-11.—Kutoka w8/15/83.
Wewe Unaweza Kukumbuka?
◻ Majeshi ya Shetani yanaweza kukushambulia kwa njia mbili gani?
◻ Ni mifano gani ya Biblia inayoonyesha hatari ya wendekevu?
◻ Wanafunzi wanaweza kujaribiwaje kuhusiana na nia za wendekevu?
◻ Kwa sababu gani ni lazima sasa tujihadhari juu ya nia yetu?
[Picha katika ukurasa wa 21]
Ni lazima Mkristo aliye shujaa wa vita ajiangalie kuhusu mashambulizi ya moja kwa moja na pia hatari zinazokuja kwa ujanja au bila kutazamiwa
“Naam, tukiujua wakati, kwamba saa ya kuamka katika usingizi imekwisha kuwadia; kwa maana sasa wokovu wetu u karibu nasi kuliko tulipoanza kuamini. Usiku umeendelea sana, mchana umekaribia; basi na tuyavue matendo ya giza, na kuzivaa silaha za nuru. Kama ilivyohusika na mchana na tuenende kwa adabu; si kwa ulafi na ulevi, si kwa ufisadi na uasherati, si kwa ugomvi na wivu.”—WARUMI 13:11-13.