“Ni Nani Amepata Kujua Akili ya Yehova? ”
“Kwa maana ‘ni nani amepata kujua akili ya Yehova, au ni nani amekuwa mshauri wake? ’ ”—WARUMI 11:34, New World Transtation; ISAYA 40:13, Greek Septuagint Version.
1. (a) Ni ulizo gani lenye mwito wa ushindani ambalo Paulo anatumia kutokana na Isaya 40:13? (b) Neno fulani kuu katika mtajo wake wa maneno linatofautianaje na Kiebrania cha kwanza?
MIAKA zaidi ya 2,700 iliyopita ulizo lenye mwito wa ushindani liliwekwa mbele ya taifa la Israeli la kale. Maneno yake yalitajwa hivi na mtu aliyekuwa Mfarisayo Myahudi katika barua yake, kwenye Warumi 11:34 (NW ): “Kwa maana ‘ni nani amepata kujua akili ya Yehova, au ni nani amekuwa mshauri wake? ’ “Maneno ya ulizo hilo yalitumiwa na mtume Paulo kutokana na fasiri iliyofanywa na Biblia ya kale ya Kigiriki ya Septuagint Version juu ya Isaya 40: 13, na tafsiri hiyo inatumia hapo neno “akili” (nous) badala ya neno la kusema “roho” kama linavyopatikana katika maandishi ya kwanza ya Kiebrania.
2. Tunaelewaje wakati “akili” ya kibinadamu inapotajwa? Toa mfano.
2 Sasa, maneno yaliyoongozwa na Mungu yanayosema “akili ya Yehova” yana maana gani? Kwa habari yetu sisi viumbe wa kibinadamu, akili inasimamia njia zetu za kufikiri. Kwa mfano, tunaweza kuamua akilini tuwe na “nia iyo hiyo [ya akili] . . . ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu.” (Wafilipi 2:5; ona pia Mwanzo 11:6.) Nguvu zetu za akili ni za juu kuliko zile za mnyama ye yote.
3-5. (a) Isaya 55:8, 9 inaonyesha nini juu ya “akili” ya Yehova? (b) Kwa sababu gani si ajabu kwamba Paulo alipaaza sauti kwa mshangao wa maneno yaliyoandikwa kwenye Warumi 11:33? (c) Mtume ana maana gani kwa elezo analotoa kwenye Warumi 11:34? (d) Kwa sababu gani waandikaji waliotangulia nyakati za Ukristo hawangeweza kujua “akili” ya Yehova?
3 Jambo ambalo Yehova Mungu, Muumba, anafikiria akilini ni la juu sana kuliko lile ambalo sisi viumbe wa kibinadamu tusio wakamilifu tunaweza kufikiria akilini au kuliko lile ambalo tungeweza kujiwazia. Anavuta fikira kwenye uhakika huo wa maana katika unabii wa Isaya 55:8, 9, ambapo pameandikwa hivi: “Maana mawazo yangu si mawazo yenu, wala njia zenu si njia zangu; asema [Yehova]. Kwa maana kama vile mbingu zilivyo juu sana kuliko nchi, kadhalika njia zangu zi juu sana kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu.” Kwa hiyo, yeye anakusudia jambo bora sana kwa viumbe vyake vya kibinadamu, hasa kwa wale wanaoingia katika uhusiano wa agano pamoja naye, nalo linapita lile ambalo sisi viumbe tulio hapa duniani tungeweza kuwazia. Basi, si ajabu kwamba baada ya kuzungumza sehemu ya kutokeza ya mpango wa Yehova na namna inavyoendelea kutimizwa, yule “mtume wa watu wa Mataifa” alilazimika kupaaza sauti hivi: “Jinsi zilivyo kuu utajiri na hekima na maarifa ya Mungu! hukumu zake hazichunguziki, wala njia zake hazitafutikani! ” (Warumi 11:13, 33) Kwa uhakika hakuna mtu amemtangulia Mungu kwenda kumtafutia njia zake. Kwa hiyo, mtume aliyeongozwa na Mungu anaendelea kutoa elezo hili: “Kwa maana ‘ni nani amepata kujua akili [noun] ya Yehova, au ni nani amekuwa mshauri wake? ’ “(Warumi 11:34, NW ) Hapo The Jerusalem Bible inasema: “Ni nani angeweza kamwe kujua akili ya Bwana? Ni nani angeweza kamwe kuwa mshauri wake? ”
4 Kwa kusema hivyo mtume hamaanishi kwamba, Mungu akiisha kufunua yaliyo katika akili yake, mtu hawezi kujua au kufahamu akili Yake. Hapana! Kwa maana Mungu ametufunulia sisi wanadamu mambo ya akilini mwake katika kurasa za Neno lake aliloliongoza kwa roho, yaani, Maandiko Matakatifu. Maana ya mtume ni kwamba hakuna mwanadamu, kwa kujianzia mwenyewe na kwa kutangulia Mungu katika kupanga akili Yake mwenyewe au kusudi, angaliweza kutimiza au kuendeleza jambo lile lile kwa nguvu zake za kufikiri! Hakuna mwanadamu amefanya hivyo kabla ya ufunuo wa Mungu mwenyewe. Basi, kwa kweli kabla ya ufunuo wa kimungu ulioonyeshwa katika Biblia, hakuna mwanadamu aliyepata kujua “akili ya Yehova.” Hakuna hata mmoja wa waandikaji wa nyakati zilizoutangulia Ukristo wa vile vitabu vya kwanza 39 vya Maandiko Matakatifu aliyefanya hivyo, hata Musa yule mtoa-sheria.
5 Kwa mfano, hakuna mtu angeweza kufahamu Yehova alikuwa akifikiria nini akilini katika kushughulika na Abrahamu na uzao wake, na hakuna mtu angeweza kufahamu yote hayo yalihusianaje na matukio ya karne ya kwanza W.K.
“Akili” ya Yehova Kuhusu “Mzeituni”
6. (a) Paulo alikuwa amekuwa akizungumza ahadi gani katika Warumi sura ya 11? (b) Abrahamu alipendelewaje kwa njia kubwa, na kwa sababu ya nini?
6 Katika Warumi, sura ya 11, mtume alikuwa amezungumza juu ya “uzao wa Abrahamu” uliotabiriwa, kufikia mstari wa 34 (NW ). Kulingana na maandishi ya Musa kwenye Mwanzo 12:3 na 22:17, 18, Yehova Mungu aliahidi kumbariki Abrahamu mzee wa ukoo kupitia mbegu, au “uzao” wake; katika uzao huo, au kwa njia ya huo, Mungu wa Abrahamu angebariki jamaa zote na mataifa ya dunia katika wakati wake. Angekuwa na ahadi nzuri kama nini ya kurithi, tena kwa Abrahamu kuwa mrithi wa ahadi hiyo ilikuwa thawabu kubwa kama nini kwa sababu ya imani na utii!
7. (a) Sehemu mbalimbali za “mzeituni” ulio mfano zilisimamia nini? (b) “Matawi” yalikuwa yakielekea kwenye nini? (c) Kwa habari ya “uzao,” ni jambo gani lililokuwa katika “akili” ya Yehova lingekuja kufunuliwa?
7 Mtume anafananisha yale ambayo Yehova alikusudia akilini na ukuzi wa mzeituni, mti ambao ulipatikana kwa wingi katika nchi ya kuzaliwa kwake, Israeli. Kupatana na mfano huo, mzizi wa mzeituni huo ulio mfano ulikuwa Abrahamu mwenyewe. Kiwiliwili cha mti, au shina, ambacho kilitokea kwa Abrahamu akiwa ndiye mzizi wa mfano kilikuwa ni Isaka mwanaye mpendwa, Yakobo au Israeli mjukuu wake, na wana 12 wa Yakobo, wale mababa wa makabila 12 ya Israeli. Kwa asili wazao wote wa hao wazee wa ukoo 12 walikuwa matawi katika mzeituni huo wa mfano. Wakiwa hivyo, walikuwa wanaelekea moja kwa moja kuwa “uzao wa Abrahamu” ulioahidiwa ambao kupitia kwao jamaa zote na mataifa ya dunia zingebarikiwa kulingana na kusudi lenye upendo la Yehova au “akili” yake. Lakini jambo ambalo hawakujua juu ya “uzao” huo ni kwamba haungekuwa uzao wa kimwili kwa kuwa na asili ya kimwili kutokana na Abrahamu mzee wa ukoo, kwa maana ungekuwa “uzao” wa kiroho. Kwa hiyo baba yao angekuwa mkubwa kuliko Abrahamu, aliye juu kuliko yeye. Angekuwa si mwingine isipokuwa Mpaji-Uzima mkuu, Yehova Mungu mwenyewe. Sasa, ni nani angekuwa ndiye mshiriki mkuu hasa wa “uzao” huo?
8. (a) Yesu alipataje kuwa Yule aliye mkubwa kuliko Isaka? (b) Kwa sababu gani dhabihu ya Yesu na ufufuo wake wa kimbingu ulihitajiwa kabisa ili kubariki jamaa zote za dunia?
8 Huyo alikuwa mkubwa kuliko Isaka, yule mwana wa uzee wa Abrahamu. Alikuwa ndiye ‘mwanadamu Kristo Yesu,’ aliyekuwa mzao wa Isaka lakini akiwa mkubwa kuliko Isaka na mwanaye Yakobo, au Israeli, na wale wana 12 wa Yakobo, ile misingi 12 ya taifa la Israeli. (1 Timotheo 2:5) Mtoto mchanga ambaye angeitwa Yesu alikuwa “Mwana wa Mungu,” kwa maana alifanywa awe katika tumbo la Mariamu mama yake bikira na roho ya Yehova Mungu. Kwa kweli, uhai wake ulihamishwa kutoka makao ya kiroho ukaletwa kwenye tumbo la uzazi la Mariamu, naye Yusufu mume wa Mariamu alikuwa baba-mlezi tu wa kidunia wa Yesu. (Luka, sura za 1-3) Lakini, kama vile mambo yalivyokuja kuwa, Yesu hakuwa mbariki wa jamaa zote na mataifa ya dunia alipokuwa mwanadamu duniani. Ni kweli kwamba kupitia dhabihu yake ya kibinadamu iliyo kamilifu na isiyo na dhambi aliyoitoa huko Kalvari nje ya Yerusalemu mwaka wa 33 W.K., Yesu anaweza kutumika kubariki wanadamu wote. Lakini siku ya tatu ya kifo chake mwaka wa 33 W.K., Yehova Mungu, Baba yake wa kimbingu, alimfufua kutoka wafu na baada ya hapo yeye akarudi mbinguni akiwa Mwana wa Mungu aliye kiumbe wa roho. Akiwa huko ndipo anapobariki jamaa zote na mataifa ya nchi.
9. (a) Sasa ule mzeituni wa mfano unachukua maana gani iliyo kubwa zaidi? (b) Matawi ya kiroho yana hesabu gani, na tunajuaje? (c) Wagalatia 3:28, 29 inatufahamishaje juu ya “matawi” hayo?
9 Kulingana na maoni hayo mfano wa mtume wa mzeituni unachukua maana mpya iliyo kubwa zaidi. “Mzizi” wa mzeituni wa kiroho unathibitika kuwa Yehova Mungu, Mpaji-Uzima Mkuu wa wote, Yule aliye mkubwa kuliko Abrahamu mzee wa ukoo. Mwana mzaliwa pekee wa Abrahamu huyo Mkubwa Zaidi anathibitika kuwa Yesu Kristo, Yule aliye mkubwa kuliko Isaka. Huyo Isaka Mkubwa Zaidi anathibitika kuwa Kichwa cha kundi la Kikristo ambalo limezaliwa na roho ya Abrahamu Mkubwa Zaidi, Yehova Mungu. Washiriki wa kundi la Kikristo ndio matawi ya kiroho yanayotokana na mzeituni huo wa kitheokrasi, na kulingana na Ufunuo 7:1-8 na 14:1-3, mwishowe watakuwa washiriki 144,000. Ndiyo sababu tunasoma hivi katika Wagalatia 3:28, 29: “Hapana Myahudi wala Myunani. Hapana mtumwa wala huru. Hapana mtu mume wala mtu mke. Maana ninyi nyote mmekuwa mmoja katika Kristo Yesu. Na kama ninyi ni wa Kristo, basi, mmekuwa uzao wa [Abrahamu], na warithi sawasawa na ahadi.”
10. (a) Ni nani waliokuwa wa kwanza kuelekea kuwa matawi ya kiroho? (b) Ni nani kati ya hao ‘waliookolewa,’ na Paulo alitumiaje maneno ya unabii kuonyesha hivyo?
10 Wayahudi wa asili wa siku za Yesu, kwa kuwa ndugu zake wa asili, walikuwa ndio wa kwanza kuelekea kuwa “matawi” katika huo mzeituni wa kiroho kwa sababu ya kuwa uzao wa asili uliotokana na Abrahamu mzee wa ukoo. Walikuwa katika agano la Sheria pamoja na Abrahamu Mkubwa Zaidi kupitia mpatanishi Musa. Yesu Kristo hakuja duniani moja kwa moja kwa watu wengine isipokuwa kwa “kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.” (Mathayo 10:6) Kwa hiyo wa kwanza kuwa “matawi” katika huo mzeituni wa kiroho, ambao mzizi wake ni Yehova Mungu, walikuwa ni Wayahudi wa asili, wale mitume 12 waaminifu wa Yesu Kristo na maelfu ya Wayahudi wengine wa asili. Lakini ni “mabaki” madogo tu ya Wayahudi wa asili ‘waliookolewa’ wawe uzao wa Abrahamu Mkubwa Zaidi na kuwa warithi wa “ahadi” yake, sawasawa na ilivyotabiriwa katika Isaya 10:22. Paulo anatumia maneno ya unabii huo katika Warumi 9:27.
11. (a) Ni wakati gani waliotazamiwa kuwa “matawi” walipovunjwa? (b) Sasa “matawi” ya mzeituni-mwitu yalipandikizwaje, na ndani ya mzeituni upi?
11 Kuvunjwa kwa waliotazamiwa kuwa “matawi” ya “uzao wa Abrahamu” kulianza na uongofu wa Wasamaria waliotahiriwa, na kulianza kutenda kazi kwa ukamili miaka mitatu na nusu baada ya kufa na kufufuliwa kwa Yesu Kristo, yule Isaka Mkubwa Zaidi. Wakati huo, waamini wa kwanza wasio Wayahudi na wasiotahiriwa, yaani, Kornelio yule Mroma msimamizi wa askari mia moja, akiwa na jamaa yake na rafiki zake, waliongolewa na mtume Petro na, baada ya kuzaliwa na kupakwa mafuta kwa roho ya Yehova, wakabatizwa. (Matendo, sura ya 10) Hivyo “matawi” kutoka mzeituni-mwitu yalipandikizwa ndani ya mzeituni wa kiroho ambao Yehova Mungu ndiye “mzizi” unaotia uzima.
12. (a) Ni jambo gani lingetukia kama “matawi” yaliyovunjwa yangetubu? Toa mfano. (b) Hiyo ilionyesha nini? (c) Kama Paulo, tunapaswa kutendaje kuhusu ufunuo huo wa “akili” ya Yehova?
12 Lakini, kama wo wote wa Wayahudi wa asili waliovunjwa wangefikiria mambo upya na kutubu, kama Akila na Prisila, wangepandikizwa tena ndani ya pendeleo la kiroho ambalo taifa la Kiyahudi lilikuwa limepoteza kwa kutomwamini Isaka Mkubwa Zaidi, Yesu Kristo. (Matendo 18:1-4, 26; Warumi 16:3; 1 Wakorintho 16:19) Jambo hilo lilionyesha mfano wa fadhili za upendo za Yehova Mungu, yule Abrahamu Mkubwa Zaidi. Hali hiyo ya ukarimu wa kuvutia upande wa Yehova Mungu kuelekea Wayahudi wa asili, ambao bado walikuwa wapendwa kwa Mungu kwa ajili ya babu zao, ndiyo iliyofanya mtume apaaze sauti ya mshangao akisema, “Jinsi zilivyo kuu utajiri na hekima na maarifa ya Mungu! ” Je! ufunuo huo wa “akili” ya Yehova unasisimua hali yetu ya kuthamini moyoni?
Kupenda Mungu kwa Moyo Wote wa Mtu na Akili Yake Yote
13, 14. (a) Mungu aliitoaje Sheria, na kwa kusudi gani? (b) Yesu alisema nini kwa habari ya Sheria hiyo, na hapo anamaanisha “moyo” gani? (c) Ni amri gani mbili ambazo maneno yazo yalitumiwa na Yesu katika mtajo, na kwa sababu gani tuzishike?
13 Yehova Mungu alifanya agano pamoja na uzao wa asili wa Abrahamu mzee wa ukoo, lile taifa la Israeli, nabii Musa akiwa ndiye mpatanishi. Hilo lilitukia huko nyuma sana katika mwaka wa 1513 K.W.K. katika jangwa la Peninsula ya Sinai na kwenye Mlima Sinai. Huko aliwapa Sheria yake. Kuhusu Sheria hiyo mtume Paulo aliandika hivi: “Hivyo torati [sheria] imekuwa kiongozi kutuleta kwa Kristo, ili tuhesabiwe haki kwa imani.” (Wagalatia 3:24) Sasa Kristo Yesu alisema nini juu ya Sheria iliyotolewa kupitia Musa? Alipoulizwa ni ipi iliyokuwa ‘amri kuu’ zaidi katika orodha ya Sheria, Yesu alijibu: “Mpende [Yehova] Mungu wako kwa moyo [Kigiriki: kar·diʹa] wako wote, na kwa [nafsi, psy·kheʹ] yako yote, na kwa akili [di·a·noiʹa] zako zote. Hii ndiyo amri iliyo kuu, tena ni ya kwanza. Na ya pili yafanana nayo, nayo ni hii, Mpende jirani yako kama nafsi yako. Katika amri hizi mbili hutegemea torati yote na manabii.” (Mathayo 22:35-40) Hapo, moyo unatajwa kuhusiana na akili, kuonyesha kwamba bila shaka huo ni “moyo” wa usemi wa mfano.
14 Hapo Yesu alikuwa akitumia maneno ya Kumbukumbu la Torati 6:5: “Nawe mpende [Yehova], Mungu wako, kwa moyo [Kiebrania: le·babʹ] wako wote, na kwa [nafsi, neʹphesh] yako yote, na kwa nguvu zako zote.” Pia, aliyatoa katika Mambo ya Walawi 19:18: “Umpende jirani yako kama nafsi yako; Mimi ndimi [Yehova].” Kwa hiyo Yesu alizipanga hizo kuwa ndizo amri zinazochukua nafasi ya kwanza na ya pili kwa ukubwa kati ya amri za agano la Sheria ya Musa. Sisi leo hatuko chini ya Sheria ya Musa, lakini matakwa hayo ya msingi hayajawa ya kizamani. Inatupasa kuyashika.
15. (a) Ni nini kinachotendesha moyo wa kimwili, nao unafanya kazi namna gani? (b) Moyo wa kimwili una uhusiano gani na ubongo na akili?
15 Tunajua kwamba “roho ya uhai” ndiyo inayoendesha ule moyo halisi. (Ufunuo 11: 11; Mwanzo 7:22) Hiyo kani ya uzima inatendesha moyo wa mwili ulio hai hivi kwamba unapiga-piga damu ya uhai kwenye sehemu zote za mwili wa kibinadamu, kutia ndani ubongo. Yehova Mungu alisema: “Nafsi [neʹphesh] ya kila aina ya mwili ni damu yake kwa nafsi iliyo ndani yake. Kwa hiyo niliwaambia wana wa Israeli hivi: “Haiwapasi ninyi kula damu ya aina yo yote ya mwili, kwa sababu nafsi ya kila aina ya mwili ni damu yake.” (Mambo ya Walawi 17: 14, NW ) Ili mwili mzima uishi, lazima moyo wa kimwili usukume damu inayoendeleza uhai kwenye sehemu zake zote, hata kama uzungukaji wa damu unaendeshwa na moyo wa asili ambao mtu alipewa na Mungu, ama na moyo uliopandikizwa kutoka mwili wa mtu mwingine au na moyo usio na hisi, usio wa nyama, wa aina ya mashine. Hivyo damu inapigwa-pigwa na kufikishwa kwenye ubongo, nguvu zake za kufikiri zinaamshwa kisha akili inafanya kazi. Basi, ni wazi kwamba moyo halisi unalisha ubongo kwa kuupa kani ya utendaji ya uhai, ile “roho ya uhai.” Mtu awe au asiwe ana fahamu, moyo unaendelea kupiga-piga damu kuielekeza kwenye ubongo na sehemu nyingine zote za mwili.
16. (a) Kulingana na Biblia, moyo wa usemi wa mfano ni nini? (b) Tunatakwa tufanye nini katika kumpenda Yehova kwa ‘moyo wetu wote’? (c) Tunampendaje kwa “akili” yetu yote?
16 Lakini acheni tuchukue hatua inayozidi kuutazama ule moyo halisi tu wa chembe zilizo hai. Kama unavyotumiwa katika Biblia, moyo unasimamia makao ya msukumo unaoongoza matendo na pia wa maoni ya ndani. Huo ni moyo wa usemi wa mfano, ambao kwa kweli unamaanisha utu wetu wa ndani kabisa. Kwenye 1 Petro 3:4 unaelezwa kuwa “mtu wa siri wa moyo” (NW ), “mtu aliyefichwa wa moyo” (Revised Standard Version), “utu wako wa ndani” (New International Version). Kwa hiyo tunaamriwa tupende Yehova Mungu kwa “moyo wote.” Pia tunaamriwa tupende Yehova Mungu kwa nafsi yetu yote, kwa utu wetu mzima. Hiyo inatuhitaji tumpende yule Mungu mmoja aliye hai na wa kweli, Mwenye Nguvu Zote, kwa nguvu zetu zote za uhai, tukielekeza nishati zetu zote katika kutenda mapenzi ya Mungu yaliyofunuliwa na kufanya kwa ukamili kazi yake wakati wa huu “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 24:3, NW ) Zaidi ya hilo, lazima tumpende Mungu wa Biblia kwa “akili” yetu yote, nguvu zetu za akilini.—Marko 12:29-31.
17. (a) Tukimpenda Yehova kwa moyo wetu wote na akili yote, tunapata uhakikisho gani? (b) Kulingana na Wafilipi 4:7, mioyo na akili zetu zitakuwaje kwa sababu ya amani ya Mungu?
17 Ni wazi kabisa kwamba tukimwonyesha Yehova Mungu upendo wetu kwa moyo wetu wote na akili yote, yeye atafurahia kujibu sala zetu, na uhakikisho huo utatuondolea hangaiko. Tutafurahia amani ambayo ulimwengu huu wenye msukosuko haufurahii na hauwezi kuifahamu. Kwa sababu gani? Kwa sababu, kama vile mtume Paulo alivyohakikishia Wakristo wapendwa katika Filipi, Ugiriki, “amani ya Mungu, ipitayo wazo [Kigiriki: noun] lote italinda mioyo [kar·diʹas] yenu na nguvu za akili [no·eʹma·ta: “akili nyingi,” Authorized Version; RS] zenu kwa njia ya Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:7, NW ) Hivyo mioyo yetu ya usemi wa mfano haitavurugwa na misukumo yo yote mibaya ya haraka haraka wala na wasiwasi wa kindani, wala nguvu za akili hazitachafuliwa au kupotoshwa. Mkristo ataendelea kufuatia mwendo wake kulingana na Biblia ya Mungu aliyoiongoza kwa roho yake. Atafanya hivyo pia kwa msaada wa yule Kiongozi, Kristo Yesu.
Wewe Unaweza Kujibu?—
◻ Ni nini maana ya “akili” ya Yehova?
◻ Mzeituni wa kitheokrasi ulitumiwaje na Paulo kuonyesha “akili” ya Yehova?
◻ “Moyo” wa usemi wa mfano ni nini?
◻ “Moyo” na “akili” zinahusikaje katika upendo wetu kwa Mungu?
[Picha katika ukurasa wa 11]
Mzeituni wa kitheokrasi: “Matawi” ya Kiyahudi yasiyotii yalikatwa, kisha mahali payo pakawekwa waongofu wa Kisamaria na Mataifa wasiotahiriwa
[Picha katika ukurasa wa 13]
Moyo wa kimwili unasukuma damu inayoendeleza uhai na kuifikisha kwenye ubongo