‘Nyakati Zetu za Hatari’—Jamaa Yako Inahusikaje?
“Hata pawe ni pa hali ya chini, hakuna mahali pazuri kama nyumbani.”
Ndivyo alivyoandika mtungaji mashairi John Howard Payne. Lakini hiyo ni miaka 160 iliyopita. Katika ulimwengu wa leo hali tofauti imetokea. Mara nyingi ingawa nyumbani panapasa kuwa mahali pa kupendeza sana, panakuwa ni uwanja wa mapigano. Upendo na shauku ya asili tunayopasa kutazamia kupata ndani ya jamaa haiko katika nyumba nyingi sana. Lakini kwa sababu gani? Je! kuna jambo lo lote la kutokeza juu ya matata hayo ya jamaa katika wakati wetu?
Jamaa ya Karne ya 20
Katika karne zilizopita jamaa ilikuwa na umoja wa kufanya mambo ya kiuchumi. Yaani, washiriki wote—wazazi na watoto—walishirikiana kujenga nyumba, kutengeneza vifaa vya nyumbani, kama viti na kadhalika, kulima mashamba na kuchunga mifugo. (Mwanzo 37:2; Mithali 31:16) Lakini kilipoanza kile kipindi cha kutokea kwa viwanda vingi, mambo yakabadilika.
Mataifa ya Magharibi, hasa, yalipozidi kuwa na viwanda, jamaa nyingi zilihamia mijini kutafuta kazi ya viwandani. Sasa watu wakalazimika kuondoka nyumbani kwao wakafanye kazi kila siku. Jamaa zikazidi kupungukiwa na wakati wa kuwa pamoja. Vitu kama mavazi na vifaa vya kutumiwa nyumbani kama viti na kadhalika vikanunuliwa badala ya kutengenezwa. Na kama vile kitabu The Family, Society, and the Individual kinavyosema:
“Mabadiliko hayo, kama inavyoweza kutazamiwa, yamegeuza sana . . . maisha ya kinyumbani. Jamaa haina tena umoja wa kushirikiana kufanya mambo ya kiuchumi. Tangu sheria zipitishwe juu ya lazima ya watoto kwenda shuleni na sheria zinazohusu uzazi, watoto wameleta madeni ya kiuchumi badala ya kuwa waleta mali.” Jambo hilo limekuwa na matokeo gani juu ya malezi ya watoto? “Uongozi wa wazee katika jamaa ulibadilika, na nidhamu na heshima kwa mamlaka zikaacha kuwa misingi ya maisha mazuri.”
Mabadiliko hayo yameleta migogoro mikubwa sana, na nyakati nyingine mikubwa hata zaidi, kwenye jamaa ya karne ya 20. Na hilo si tatizo la nchi za Magharibi tu. Ukoloni na viwanda ambavyo vililetwa nao umechafua madaraka yale ya kawaida katika hata zile zinazoitwa nchi zinazoendelea. Katika visa vingine wanawake walioolewa wamechukizwa wasitake kuchukuliwa kuwa wenzi wa ndoa. Hivyo mke mmoja Mwafrika aliomboleza hivi: “Mbona wanaume wanatuacha sisi ndio tubebe mizigo? Mimi naenda shambani nikiwa na jembe begani na mtoto mgongoni. Yeye habebi kitu. Halafu narudi nikiwa na jembe, mtoto, na mtungi mkubwa sana wa maji kichwani. Na bado yeye hashiriki sehemu ya mzigo huo. Pesa zinatumiwa katika unywaji, wala si kwa faida yetu wala ya watoto. Sisi tunaishiriki kazi, au tunafanya sehemu iliyo kubwa zaidi ya kazi hiyo, lakini mwanamume ndiye anayezichukua pesa zote akituambia kwamba ni zake—kwamba yeye ndiye aliyezichuma. Inachekesha.”
Jamaa ya karne ya 20 imejisikia ikipatwa na matokeo mazito ya kitu kingine kisichopata kuonwa tena wakati uliotangulia katika historia—televisheni. Inakadiriwa kwamba wakati kijana anapofikia umri wa miaka 18, atakuwa ametazama televisheni kwa muda wa karibu saa 15,000 zikilinganishwa na saa karibu 11,000 zinazotumiwa darasani. Kufikia umri wa miaka 14, kwa wastani mtoto Mwamerika anakuwa ameona watu kama 18,000 wakiuawa katika televisheni. Matokeo yanakuwa nini? Kinajibu hivi kitabu Childstress!, cha M. S. Miller: “Wataalamu wengi wanaochunguza hali za akili na hata mahakimu wanaihesabu televisheni kuwa ndiyo imesababisha jeuri inayofuatwa na vijana. Wakati mtoto wa miaka tisa aliposimamisha shughuli za banki moja mjini New York akiwa na bunduki ya bandia, kisha akachukua dola mia moja, alisema ni kwa sababu ‘mimi niliona jamaa wakifanya hivyo katika televisheni.’ “Gazeti The Family Coordinator linaongezea hivi: “Ingawa haijathibitishwa kabisa kwamba kuacha vijana waone mambo hayo ndiko kumewaletea matokeo hayo kwa njia ya moja kwa moja, ni wazi kwamba tabia kadha zinaonyeshwa katika vifaa vya utangazaji wa habari ambazo zitageuza sana maisha na mtindo wa maisha ya baadaye ya vijana.”
Bila shaka, jamaa ya karne ya 20 imepatwa na hali za maisha zilizo tofauti kabisa na za nyakati zilizotangulia nazo zimeiletea migogoro na mavutano yasiyopata tena kuonekana katika historia ya kibinadamu. Lakini je! jambo hilo kweli limetokeza matata ya kijamaa ya kiasi cha kutoa ushuhuda unaoonyesha tunaishi katika “siku za mwisho”?
Mtume Paulo alitoa maelezo marefu sana akitabiri kwamba “siku za mwisho” zingekuwa na “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.”a Matokeo ya hizo “nyakati za hatari” yangekuwa nini juu ya maisha ya jamaa? Paulo anajibu hivi: “Watu watakuwa . . . wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na shauku ya upendo wa asili.”—2 Timotheo 3:1-3, NW.
‘Kutokutii Wazazi’
Watoto ni nyama na damu ya wazazi wao na wana deni kwao kwa sababu ya baraka nyingi sana. Unakuwa wonyesho wenye kuogopesha wakati vijana wanapokosa kuonyesha wazazi heshima na utunzaji wanaostahili. Ni kama vile mwanachuo mmoja wa Biblia alivyosema: “Ni ishara ya ustaarabu ulioshuka sana wakati vijana wanapoacha kabisa kuheshimu wazee, na kukosa kutambua deni lile lisilolipika na wajibu mkuu walio nao kwa wale waliowapa uhai.” Je! kweli hivyo ndivyo ilivyo katika jamaa za karne ya 20?
“Mimi naogopa mtoto wangu mwenyewe,” akaomboleza mama mmoja alipokuwa akisema juu ya mambo yenye kuleta fikira nzito zaidi juu ya watoto kuasi wazazi wao—kuwatenda wazazi mabaya. Katika kisa kimoja cha hamaki yenye jeuri, mwana mwenye umri wa miaka 17 wa mwanamke huyo alikuwa ametegua bega lake kwa kumpiga teke kali. Jeuri kama hiyo inatendwa juu ya wazazi kwa kadiri gani? Kinaporipoti juu ya matokeo ya uchunguzi uliofanywa kuhusu jeuri inayofanywa katika jamaa huko United States (Amerika), kitabu Behind Closed Doors kilisema: “Mmoja kati ya watoto watatu walio kati ya umri wa miaka mitatu na kumi na saba anachapa wazazi wake kila mwaka.” Je! kwa kawaida hauwi ni ukosefu mkubwa sana wa heshima wakati mtoto anapoinua mkono apige wazazi wake?—Linganisha Waefeso 6: 1-3.
Watoto wanawaasi wazazi wao kwa njia zisizo za jeuri sana pia. Katika miaka ya 1960 walitumia mavazi ya kihipi na nywele ndefu kuasi. Lakini watu wazima walipofuata maelekeo ya kufanya kama wao, vijana walilazimika kuanzisha njia mpya za kuasi. Kitabu Childstress! kinaeleza hivi: “Kupitia ubuni wote unaofanywa, njia hakika zilizojaribiwa za kuonyesha ukaidi zinaongezeka—dawa za kulevya, kunywa pombe, kutoroka shuleni na nyumbani. Ni kama vile kizazi cha mababu na akina nyanya kinavyosema kwa mshangao, ‘Mimi singependa kuzaa watoto katika kipindi na nyakati hizi.’ “
Si watoto wadogo peke yao wanaokosa kuonyesha wazazi wao upendo na heshima wanayostahili. Kuna kikundi kingine—watu wazima wanaotukana wazee-wazee. Kwa njia gani? Kichapo Psychology Today kinaeleza: “Kutenda wazee-wazee vibaya kunaweza kuwa kuwatesa kimwili, kuwanyang’anya (kwa mfano kuchukua akiba ya pesa zilizowekwa na mzazi), kutokuwajali (kukosa kuwapa chakula au matibabu) au kwa kuwaumiza mawazo (kuwatusi). Wazazi wao wakilalamika, wale wanaowatenda vibaya wanatisha mara nyingi kuwafukuza nyumbani au kuwakabidhi mikononi mwa makao yanayotunza wagonjwa wa akili au mahali pa kutunzia wazee.”
Hasa inasikitisha sana kwamba watoto wengi ambao wamekuwa watu wazima hawajioni wakiwa na daraka la kutunza wazazi wazee. Kwa mfano, F. Ivan Nye, katika gazeti la uchunguzi lililotangazwa katika Journal of Marriage and the Family, alisema: “Wengi wa wale wenye kuhojiwa [katika uchunguzi huu] wanaona wajibu wa kuwa wakiwaona watu wa ukoo wao na kuwasaidia katika shida za pesa zinapotokea kwa dharura, lakini asilimia zaidi ya 30 wanakataa wakisema hakuna wajibu kama huo (wa kusaidia kwa pesa) na wachache kuliko asilimia 40 wa jinsia yo yote wanaonyesha wanachukizwa sana na wengine wanaokosa kutimiza wajibu huo.” Jambo hilo lilimfanya Nye akate shauri kwamba “uhusiano wa kijamaa” ‘unaendelea kutoweka katika ile hali ya kawaida na huenda ukawa’ jambo la kufuatwa katika jamaa wakati tu mtu anapotaka kulifuata. Je! hiyo si “ishara ya ustaarabu ulioshuka sana”? —Linganisha 1 Timotheo 5:3-8.
Si watoto wote wanaotupilia mbali mamlaka ya wazazi. Lakini visa vya vijana wenye kuasi wazazi wao vimeenea vya kutosha kuweza kuthibitisha kabisa kwamba aliyoyatabiri mtume Paulo yanatimia leo: “Watu watakuwa . . . wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu.”
“Wasio na Shauku ya Upendo wa Asili”
Si watoto peke yao wanaopatwa na matokeo ya nyakati hizi “zilizo ngumu kushughulika nazo.” Paulo alitabiri hivi pia: “Watu watakuwa .. . wasio na shauku ya upendo wa asili.”—2 Timotheo 3:2, 3, NW.
Ni jambo la kawaida kutazamia jamaa yako iwe ndiyo yenye kukuunga mkono zaidi kati ya vikundi vya watu. Nyumbani ambapo ni mahali pa kupendeza sana panapasa kuwa na hali ya upendo—kupenda mwenzi wako wa ndoa na watoto wenu. Hata hivyo, mtume Paulo alisema kwamba ukosefu wa “shauku ya upendo wa asili”b ungeonyesha ni “siku za mwisho.” Na kulingana na maneno yake, katika visa vingi mno nyumbani si mahali pa kupendeza sana kama panavyopasa kuwa. Namna gani hivyo?
Katika makala iliyotangulia tuliona kuna mweneo wa kushangaza sana wa ukosefu wa shauku ya asili—kutenda mke vibaya. Kwa uhakika hakuna mke anayestahili kupigwa teke, kupigwa ngumi au kutendwa vibaya kwa njia nyingine. Hiyo ni tofauti sana na vile Maandiko yanavyosihi waume wapende wake zao “kama miili yao wenyewe”! Hilo ni jambo la asili. Kupiga mke si jambo la asili! —Waefeso 5:28-33.
Labda inayoshangaza hata zaidi ni hesabu ya visa vilivyoripotiwa vya kupiga waume. Katika kisa kimoja mume “alikuwa daima na makovu na majeraha” aliyotiwa na mke wake ambaye alikuwa “amemchokoza mume huyo kwa vituko vya kumwogopesha sana, kumpigia-pigia makelele makubwa na kumtenda jeuri mbaya sana ya kimwili.” Wataalamu fulani wanaoshughulika na hali za kijamii wanakadiria kwamba katika United States (Amerika) peke yake, wanaume karibu 282,000 wanapigwa na wake zao kila mwaka. Je! huo pia si mfano wa kushtusha sana juu ya ukosefu wa shauku ya asili iliyo katika jamaa nyingi za karne ya 20?—Linganisha Waefeso 5:22-24, 33.
Ingawa ripoti hizo ni za kuhuzunisha sana, ripoti za visa vinavyoongezeka vya kutenda watoto vibaya vinaumiza moyo hata zaidi. Si ajabu hata kidogo kusoma vichwa vya habari kama vinavyofuata:
“Mtoto aliyetendwa vibaya, anapokuwa mtu mzima, asema juu ya makovu.”
“Mwanamke Akubali Alizamisha Watoto Wake Wanne Wakiwa Usingizini Wakafa Maji.”
“Kuwapa watoto mapigo makali, vifo vyaongezeka sana katika Denver na mkoani.”
“Kutojali Watoto ‘Kwamaliza Sifa ya Uingereza ya Kuwa Wapenda-Watu.’”
Hatutaeleza mambo mengine mengi yaliyo ya kuogopesha sana.
Matendo mabaya hayo yanayofanywa juu ya watoto yameenea kadiri gani? Kikiripoti matokeo ya uchunguzi uliofanywa kuhusu jeuri inayofanywa katika jamaa, kitabu Behind Closed Doors kilikadiria kwamba “kati ya watoto milioni 3.1 na milioni 4 [katika United States] wamepigwa mateke, wakaumwa, au wakapigwa ngumi na mzazi wakati fulani wa maisha zao; . . . kati ya watoto 900,000 na milioni 1.8 walio kati ya umri wa miaka mitatu na kumi na saba wametendwa jambo fulani na mzazi kwa kutumia bunduki au kisu wakati fulani.”
Ingawa ni kweli kwamba watoto, hasa wale wachanga, wanakuwa rahisi kuchapwa na nyakati nyingine wanadai mambo, hakuna mtoto anayestahili kuteswa—kimwili, kimoyoni au kwa njia nyingine yo yote. Ingawaje, kama vile Biblia inavyosema: “Wana ndio urithi wa [Yehova], uzao wa tumbo ni thawabu.”
Hakuna shaka kwamba jamaa ya karne ya 20 imepatwa na mikazo na migogoro isiyopata kuonwa katika historia ya kibinadamu. Kinasema hivi kichapo U.S. News & World Report: “Kwa sababu gani kuna wimbi la matata ya kijamaa? Dakt. Bertrand New, daktari wa akili kwenye Chuo cha Tiba cha Makao ya Westchester Mjini New York, anataja vipingamizi vya kibinafsi na kiuchumi, uzoevu wa kunywa pombe na migogoro mikubwa zaidi ambayo jamii ya watu wa kisasa inaweka juu ya jamaa nyingi.”—Italiki ni zetu.
Wimbi hilo la ugomvi wa kijamaa ni sehemu moja tu ya ile ishara yenye mambo mengi inayotambulisha “siku za mwisho.” Matoleo ya wakati ujao ya Mnara wa Mlinzi yatazungumza kirefu mambo mengine ya maneno ya Paulo kwenye 2 Timotheo 3:1-5. Lakini jambo moja ni hakika: Ripoti zinazohusu uasi wa watoto juu ya mamlaka ya wazazi na upungufu wa shauku ya asili, kama Paulo alivyotabiri, zimeenea kwa kiasi kinachotosha kuwa sehemu ya ushuhuda wa wazi kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” za mfumo huu wa mambo.
Kweli, tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” Lakini, “nyakati za hatari” hizi hazipasi kuharibu furaha ya jamaa yako. Yehova Mungu ameweka miongozo inayofaa katika Biblia, nayo ikifuatwa itafanya maisha ya jamaa yawe ya furaha na mafanikio hata sasa. Zaidi ya hilo, ukifuata sana maagizo hayo, huenda jamaa yako ikahesabiwa kati ya zile zenye furaha zitakazofurahia milele maisha katika utaratibu mpya wenye uadilifu utakaofanyizwa na Mungu, ambao sasa umekaribia sana.—2 Petro 3:13; Mithali 3:13-18.
[Maelezo ya Chini]
a Neno la Kigiriki la kusema “nyakati za hatari” (chalepós) limetafsiriwa ‘kali’ kwenye Mathayo 8:28, ambapo limetumiwa kueleza hali ya wanaume wawili wenye mashetani, waliokuwa wajeuri na hatari kupita kiasi. Hivyo, “siku za mwisho” zingekuwa za kutisha na hatari sana.
b Neno la Kigiriki storgé linahusu upendo wa kijamaa, kupenda watu wa ukoo wa mtu. Lakini neno la kusema “wasio na shauku ya asili” ni namna ya neno ástorgos, linalomaanisha kinyume kabisa cha neno hilo jingine—kuharibika kwa upendo wa asili unaopasa kuwa kati ya washiriki wa jamaa.
[Picha katika ukurasa wa 6]
Yeye anatazama watu wakifyatuliwa risasi, wakipigwa, wakiuawa. Hayo yanakuwa na matokeo gani juu yake?
Kufuata miongozo iliyo katika Biblia kunaweza kufanya maisha ya jamaa yawe ya furaha hata sasa