Ufalme wa Mungu—Ndio Utatuzi Hakika
“MTU mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.” Usemi huo, ulioandikwa katika Biblia kwenye Mhubiri 8:9, umekuwa wa kweli katika historia yote na hata katika wakati wetu huu. Ni kwa sababu gani iko hivyo? Ni kwa sababu gani wanadamu wameshindwa kufanya nyakati hizi za hatari wanazokabili ziwe afadhali?
“Maarifa madogo ya asili ya mwanadamu yatatusadikisha,” George Washington aliandika katika mwaka 1778, “kwamba, kwa sehemu kubwa zaidi ya wanadamu faida [ya kibinafsi] ndiyo kanuni yenye kuongoza; na karibu kila mtu anaongozwa nayo, kwa kadiri kubwa au ndogo. . . . Ni watu wachache wanaoweza kujinyima maoni yote ya faida ya kibinafsi, au mafaa, kwa ajili ya faida ya wengi. Ni kazi bure kukana ukosefu mkubwa wa adili za asili ya kibinadamu katika jambo hilo; uhakika ni kwamba ndivyo ilivyo, mambo yaliyotokea katika kila kizazi na taifa yamethibitisha hivyo na ni lazima kwa kadiri kubwa, tubadili katiba ya wanadamu, kabla hatujaweza kufanya iwe vingine.”
Kwa kuwa watu wote wanazaliwa wakiwa wasiokamilika na wenye dhambi, imekuwa haiwezekani kwa mtu ye yote kushughulika na mwanadamu mwenzake kwa njia kamilifu kabisa na ya haki. (Warumi 5:12) Faida za kibinafsi za kichoyo ama zinazuia ama zinaongoza maamuzi na matendo yake. Na, hata wanadamu wajaribu namna gani kutunga sheria za kuzuia udhaifu huo uliorithiwa, mambo hayo hayawezi kutupiliwa mbali na serikali yo yote ya kibinadamu. “Hakuna mfumo wo wote wa serikali—iwe ni ya mfalme mmoja, dikteta, mwenye kutawala kwa mabavu, mamlaka ya watu wa cheo cha juu katika jamii, mamlaka ya watu wachache, jamhuri, demokrasia halisi, wala Chama cha Kikomunisti—uliopata kufanywa ambao utahakikisha kwamba viongozi wema na wenye hekima sikuzote wataiongoza merikebu ya serikali,” anaandika Laurence Beilenson katika kitabu The Treaty Trap. “Hiyo ni kwa sababu wale wanaowachagua au kukubali utawala wao wamekuwa ni watu. . . . Wala watu ambao watawala wanasimamia si wema wala wenye hekima. Watu watakapokuja kuwapenda jirani zao kama wanavyojipenda, sheria za kuzuia, polisi wa kuzitekeleza, na jeshi la kulinda halitahitajiwa, wala mapatano [hayatahitajiwa].”
Ingawa Beilenson anahisi, kama wengine, kwamba hiyo “siku ya furaha” ‘haiko karibu,’ maoni hayo hayafikirii kusudi la Mungu kwa ajili ya dunia. Kushindwa kwa wanadamu kutawala kwa hekima na kwa amani, hata iwe ni njia gani yenye kufuatwa, kumeonyesha wazi kwamba wanadamu hawawezi kujitawala. Utatuzi pekee ni Ufalme wa Mungu chini ya utawala wa Mwanaye Yesu Kristo. Ndiyo sababu Yesu, katika kuwapa wanafunzi wake sala iliyo mfano wa kufuatwa, aliwafundisha wasali hivi kwa Mungu: “Ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.”—Mathayo 6:9, 10.
Ni mapenzi ya Mungu kwamba Ufalme wake, ambao tayari umesimamishwa katika mbingu, uwe njia ya kuleta amani kamili duniani. Kuhusu utawala wa Mwanaye, “Mwana-mfalme wa Amani,” masimulizi yaliyoongozwa kwa roho ya Mungu yanasimulia hivi: “Uwezo wake wa kifalme utaendelea kukua; ufalme wake daima utakuwa na amani. Yeye atatawala kama mrithi wa Mfalme Daudi, akitegemeza uwezo wake juu ya haki na hukumu, kuanzia sasa mpaka mwisho wa wakati. Bwana Mwenyezi ameazimia kufanya yote hayo.”—Isaya 9:6, 7, Today’s English Version.
Si kwamba tu Ufalme huo utafanya amani ya kweli ienee katika dunia yote bali pia utatimiza yale ambayo hakuna serikali nyingineyo inaweza: kuondoa kabisa maelekeo ya kichoyo ya wanadamu yanayoletwa na kutokamilika kwao kulikorithiwa. Kwa maana chini ya utawala wa Ufalme, wakiwa wametolewa katika dhambi na laana yake ya kifo, wataweza kufurahia taraja la uzima mkamilifu usio na mwisho juu ya dunia-paradiso. (Warumi 6:23) Ili kutimiza hilo, Mungu “atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.” Na Yehova anaahidi hivi: “Tazama, nayafanya yote kuwa mapya.” (Ufunuo 21:4, 5) Huo utakuwa ndio utatuzi hakika kwa ajili ya nyakati zetu za hatari.