Je! Wewe Unathamini Urithi Wako?
“Fuatieni amani . . . , mkilinda kwa uangalifu . . . kwamba kusiwe mwasherati ye yote wala ye yote asiyethamini mambo matakatifu, kama Esau, ambaye kwa kubadilishana ili apate mlo mmoja alitoa haki zake za mzaliwa wa kwanza.”—WAEBRANIA 12:14-16, NW.
1, 2. (a) Urithi ni nini? (b) Ni maswali gani yanayotokea kuhusu urithi ulio bora zaidi?
WATU wameua wengine kwa ajili ya urithi. Wengine wamekufa wasiupate kamwe. Wengi, baada ya kuupata, wameutumia ovyo-ovyo. Huo ni nini? Ni urithi. Na mara nyingi ndivyo mambo yanavyokuwa wakati mali inaporithiwa.
2 Biblia inasema juu ya urithi mara 229, na katika pindi nyingi inazungumza juu ya urithi wa shamba au mali. Lakini, Neno la Mungu linasema pia juu ya urithi ulio bora sana zaidi ya wo wote anaoweza kuachiwa mtu uwe urithi. Na urithi huo bora sana unapatikana kwako wewe usipoudharau. Urithi huo ni nini? Ni nani anayeutoa? Ni kwa sababu gani wengine wanaupoteza? Tunaweza kuonyeshaje kuuthamini?
Urithi Huo Ni Nini?
3. Urithi wa Kikristo ni nini, na mwandalizi ni nani?
3 Wayahudi katika Antiokia walipoukataa ujumbe wa wokovu wa mtume Paulo, aliwageukia wale ambao hawakuwa Wayahudi, “Mataifa.” “Wakafurahi, wakalitukuza neno la [Yehova], nao waliokuwa wamekusudiwa uzima wa milele wakaamini.” (Matendo 13:45-48) Ndiyo, urithi ni uzima wa milele. Kwa wachache inamaanisha “urithi usioharibika na usiochafuliwa na usionyauka . . . katika mbingu.” Mwandalizi ni nani? “Mungu na Baba ya Bwana yetu Yesu Kristo,” akasema Petro.—1 Petro 1:3, 4, NW.
4. Ni urithi gani unaopatikana kwa wengi wa wanadamu?
4 Lakini namna gani kwa wanadamu walio wengi sana ambao hawana tumaini la kimbingu? Urithi wao unaweza kuwa uzima mkamilifu wakiwa sehemu ya “dunia mpya,” jamii mpya ya watu waliokombolewa na dhabihu ya Yesu Kristo. Inatoa uwezekano wa kuwa na uzima wa milele katika sayari itakayobadilishwa, isiyo na uchafuzi. (Ufunuo 11:18; 21:3, 4, NW; Yohana 17:3) Ungependa kutazamia urithi huo? Ikiwa tayari unautazamia, je, unauthamini kweli kweli?
Kudharau na Kuthamini Haki ya Uzaliwa
5, 6. (a) Esau na Yakobo walikuwa nani? (b) Ni jambo gani lililokuwa la pekee kuhusu urithi wao, na kwanza ni nani angefaidika?
5 Ili kufahamu vizuri zaidi jambo hilo la kuthamini urithi, na turudie kwa ufupi mfano wa ndugu wawili. Mmoja alithamini sana viwango vya kiroho, na yule mwingine akapoteza kuthamini kwake mambo hayo na kwa hiyo akapoteza urithi wenye thamani sana. Hao walikuwa ni Yakobo na Esau, wana-mapacha wa mzee wa ukoo Mwebrania, Isaka.
6 Babu yao Abrahamu alikufa walipokuwa na miaka 15. Urithi wa kimwili aliomwachia mwanaye Isaka ulikuwa ni pamoja na mifugo mikubwa na shamba lililokuwa na pango la kuzikia la jamaa. (Mwanzo 25:5-10) Lakini, jambo lenye maana zaidi la urithi huo halikuwa mali wala kitu cho chote chenye kuonekana. Lilikuwa ni ahadi ambayo Yehova alikuwa amempa Abrahamu na kuirudia kwa Isaka baadaye: “Katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia.” (Mwanzo 22:18; 25:24-26; 26:2-5) Hiyo ilifunua kwamba Masihi, akiwa ndiye “uzao” ulioahidiwa wa Mwanzo 3:15, angekuja kupitia nasaba ya Abrahamu katika wakati fulani wa baadaye. Kwa kuwa Esau alikuwa ndiye mzaliwa wa kwanza wa mapacha hao, angekuwa ndiye mwenye haki ya halali kurithi ahadi hiyo, na pia sehemu maradufu ya mali hiyo babaye Isaka akifa. Sasa swali ni hili, Je! yeye alithamini urithi wake?
7. Esau na Yakobo walikuwa tofauti namna gani katika kuthamini na utu? (Mwanzo 26:34, 35;28:6-9)
7 Mapacha hao walipokuwa wakubwa zaidi, nyutu zao tofauti-tofauti zikawa wazi. Esau alikuwa mwindaji asiyetulia, “mtu wa nyikani,” naye Yakobo alikuwa “mtu asiye na lawama” (NW), aliyekuwa “mtulivu.” (Mwanzo 25:27) Siku moja Yakobo alipokuwa akipika mchuzi wa dengu, Esau alifika kutoka kondeni amechoka sana na mwenye njaa. “Esau akamwambia Yakobo, [Haraka,] tafadhali, unipe hicho chakula chekundu nile, kwa kuwa ninazimia mimi.”—Mwanzo 25:30.
8. Yakobo alitoa pendekezo gani lenye kushangaza kwa ndugu yake, na Esau aliitikiaje?
8 Hapo Yakobo akatoa kwa ndugu-pacha wake pendekezo lenye kutokeza, akasema: “Kwanza niuzie leo haki yako ya mzaliwa wa kwanza.” (Mwanzo 25:31) Alikuwa akiomba urithi wa Esau wabadilishane na bakuli la mchuzi! Je! unafikiri kwamba Yakobo angetumainia sana kufaulu katika mpango huo wa kubadilishana? Kwa wazi yeye alifikiri angefaulu. Kwa sababu gani? Kwa sababu alijua maelekeo ya ndugu yake na maoni yake kuelekea viwango. Je! alikosea? Esau, bila shaka akiongeza chumvi kuhusu hali yake ya kimwili, akajibu: “Niko mahututi; haki ya uzaliwa yangu yanifaa nini mimi?”—Mwanzo 25:32, The New English Bible.
9. Esau anatofautianaje na nduguye kwa habari ya urithi?
9 Masikilizano hayo yalithibitishwa kwa kiapo, na Yakobo akampakulia nduguye mkate na mchuzi wa dengu. Esau akala na kwenda zake “bila matata zaidi.” Halafu maandishi yaliyoongozwa kwa roho ya Mungu yanataja waziwazi hivi: “Hivyo Esau akaonyesha jinsi alivyoona haki ya uzaliwa yake kuwa yenye thamani kidogo.” (Mwanzo 25:33, 34, NE) Tofauti na hilo, Yakobo alithamini sana kama nini haki ya uzaliwa! Yeye hakutamani mali—shamba la kuzikia na wanyama fulani. Alitaka uzao wa Kimasihi ulioahidiwa uje kupitia nasaba yake. Alitaka urithi wa kiroho.—Linganisha Mathayo 6:31-33.
Je! Wewe Ungebadilishana Urithi Wako Upate Kitu Fulani
10. (a) Paulo alitoa elezo gani lenye kupendeza kuhusiana na Esau? (b) Kuna uhusiano gani kati ya uasherati na kubadilishana kwa Esau haki yake ya uzaliwa?
10 Karne 19 hivi baadaye, mtume Paulo alitumia mfano wa Esau kuwaonya Wakristo wa kwanza, kwa kusema: “Fuatieni amani na watu wote, . . . mkilinda kwa uangalifu kwamba ye yote asinyang’anywe fadhili zisizostahilika za Mungu; . . . kwamba kusiwe mwasherati ye yote wala ye yote asiyethamini mambo matakatifu, kama Esau, ambaye kwa kubadilishana ili apate mlo mmoja alitoa haki zake za mzaliwa wa kwanza.” Ni kwa sababu gani Paulo hapa anahusisha mwasherati na vitendo vya Esau? Kwa sababu kuwa na akili kama ya Esau kunaweza kuongoza kwenye kushindwa kuthamini mambo matakatifu halafu kwenye dhambi nzito zaidi, kama uasherati.—Waebrania 12:14-16, NW.
11. Imekuwaje kwa Wakristo fulani katika nyakati za kisasa?
11 Je! nyakati nyingine wewe unashawishwa ubadilishane urithi wako wa Kikristo, uzima wa milele, upate kitu cha muda tu kama ‘bakuli la mchuzi wa dengu’? Je! wewe, labda bila kujua, unadharau “mambo matakatifu”? Kwa mfano, katika nyakati za karibuni Wakristo fulani wamenaswa na ukosefu wa adili wa kisasa. Inaelekea wana tamaa ya Esau isiyo na subira ya kutosheleza tamaa mbaya ya kimwili. Kama tu alivyomwambia Yakobo: ‘Haraka, tafadhali, unipe hicho chakula chekundu nile,’ si ndivyo watu hao wamesema: ‘Haraka! Sababu gani ningojee ndoa yenye heshima?—Mwanzo 25:30; linganisha Mwanzo 34:1-4.
12. (a) Ni kwa jinsi gani wengine hawakuonyesha kuthamini mambo matakatifu? (b) Lakini, wengine wamechukua hatua gani?
12 Kwa sababu hiyo imetokea nini? Tamaa ya kutosheleza nyege kwa vyo vyote imekuwa ‘bakuli lao la mchuzi wa dengu.’ Matokeo yake yamekuwa kwamba wamedharau mambo matakatifu, kutia uhusiano wao na Yehova Mungu na Yesu Kristo. Wamedharau ukamilifu, uaminifu na usafi. Wamehatirisha urithi wao. Lakini, wengine wao baadaye wamechochewa watubu kikweli na kwa wazi wakaupata tena msimamo wao pamoja na Mungu.—Linganisha Zaburi 51.
Sababu Gani Wengine Wanaanguka?
13. Ni mambo gani yanayoweza kuharibu viwango vyetu vya kiroho?
13 Ni nini kinachosababisha maelekeo hayo ya ukosefu wa adili? Je! yaweza kuwa watu hao wameruhusu viwango vyao vya adili vishambuliwe? Mambo mengi yanaweza kuwa na matokeo yenye kuharibu njia yetu ya kufikiri—marafiki na watu wa ukoo ambao hawana kanuni zinazofanana na zetu, hata watu walio dhaifu kiroho kundini, mazingira yasiyo ya adili kazini, vitumbuizo na usomaji usiofaa, kutafuta mahali pasipofaa upendo na shauku kutoka kwa wasioamini. Yote hayo yanaweza kuongoza kwenye mwenendo usio wa adili. Je! ingeweza kuwa kwamba lo lote la mambo hayo linaharibu maoni yako juu ya viwango sasa hivi?—2 Wakorintho 6:14; 2 Wathesalonike 3:6.
14. Kuna hatari gani katika vitumbuizo vya kisasa?
14 Kwa mfano, je, unajikuta ukitazama televisheni au sinema zinazoendekeza na hata kutia moyo mwenendo usio wa adili? Ni lazima ikubaliwe kwamba sinema hizo zaweza kusisimua mwili wenye dhambi—kama chamchela ya maji yenye kuwafyonza mpaka ndani wasiojihadhari. Hilo linaonekana wazi katika uvutano wenye nguvu sana ambao watu wa jinsia moja wenye kulalana wanao katika ulimwengu wa vitumbuizo. Wamedhamini sinema na michezo inayotetea kulalana kwa watu wa jinsia moja. Matokeo yamekuwa kwamba zilizoonwa hapo kwanza kuwa ngono zilizopotoka sasa zinasemwa kwa usemi usiochukiza kuwa ni “mtindo mwingine wa maisha”! Hali imefikiwa ambayo mtume Paulo alieleza hivi: “Wakiisha kufa ganzi wanajitia katika mambo ya ufisadi wapate kufanyiza kila namna ya uchafu kwa kutamani.”—Waefeso 4:19; 1 Wakorintho 6:9-11.
15. Tunaweza kuepukaje vishawishi vya mwenendo usio wa adili?
15 Utatuzi ni nini? Jiepushe na “upujufu”! Biblia inashauri: “Tafuteni mema, wala si mabaya . . . Yachukieni mabaya; yapendeni mema.” Ndiyo, jaribu lenyewe ndilo hilo—kuchukia kwa bidii yaliyo mabaya.—1 Petro 4:4, NW; Amosi 5:14, 15.
16. Paulo aliwekea Wakristo kiwango gani?
16 Tukiwa na akili ya Kristo, je, dhamiri haipasi kutuzuia kutazama jeuri inayoonyeshwa, ukatili wa ngono wenye kuchukiza na ukosefu mkubwa sana wa adili unaoonyeshwa katika tafrija nyingi leo? Kweli kweli, kiwango chetu chapasa kuwa nini? Paulo anajibu: “Mambo yo yote yaliyo ya kweli, mambo yo yote yanayohusu kwa uzito, mambo yo yote yaliyo ya uadilifu, mambo yo yote yaliyo safi, mambo yo yote ambayo ni yenye kupendeka, mambo yo yote yenye kusemewa vizuri, ukiwapo wema wo wote na likiwapo jambo lo lote linalostahili sifa, endeleeni kufikiria mambo hayo.—Wafilipi 4:8, NW.
17. (a) Wengine wamechafuaje akili zao? (b) Mwendo wa hekima ni nini?
17 Hakika ni afadhali na salama zaidi kutii agizo la mtume huyo. Kwa kusikitisha wengine ‘wameendelea kufikiria’ ngono zisizo za adili katika televisheni, sinema na vitabu. Matokeo yamekuwa kwamba wamechafua akili na mioyo yao na matendo ya kukosa adili na ngono zilizopotoka. Ingelikuwa afadhali kama nini kufuata shauri la mtume huyo: “Ndugu zangu, msiwe watoto katika akili [mambo ya kiroho] zenu; lakini katika uovu mgeuzwe watoto wachanga.”—1 Wakorintho 14:20.
Tunaweza Kuongezaje Kuthamini Kwetu?
18. Ni nini kinachoweza kuwa ulinzi na kinachoweza kutusaidia tuthamini mambo matakatifu?
18 Uhusiano wa karibu pamoja na wazazi wa mtu unaweza kumfanya atambue sana upendo na kanuni zao, na kwa hiyo iwe haielekei sana hataihuzunisha jamaa. Ni hali moja na uhusiano wetu na Yehova. Lakini tunaweza kutiaje nguvu uhusiano huo? Kwa kumjua Mungu kwa undani. Funzo la kibinafsi lenye kina letu la Neno la Mungu litatusaidia tumjue na kumpenda sana hata kwamba tutapinga kishawishi cho chote. Kama alivyosema Daudi katika Zaburi 23, sikuzote tutahisi kwamba Mchungaji wetu, Yehova, yuko pamoja na sisi. Lingekuwa jambo la upumbavu kama nini kufanya kosa zito Mchungaji huyo akiwa karibu sana!—Waebrania 4:13.
19, 20. (a) Ni matatizo gani mawili yaliyopo kuhusiana na funzo la kibinafsi? (b) Ni kwa sababu gani inaonekana kuna wakati mchache sasa kwa ajili ya funzo la kibinafsi?
19 Lakini, kuna matatizo mawili ya msingi. Kwanza, kwa wengine, funzo la kibinafsi ni mzigo. Kwa sababu ya mifumo ya elimu yenye kasoro, watu wengi leo wana tatizo kubwa sana katika kusoma. Kwao, kujifunza ni jitihada. Lakini kitu cho chote maishani chenye thamani ya kudumu kinataka jitihada. Je! haistahili kutia jitihada ili kumjua Yehova, Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote, Baba yetu na Mungu wa fadhili zisizostahilika?—Mathayo 6:9; Yakobo 4:8.
20 Tatizo la pili ni unaonekana kuwa upungufu wa wakati wa funzo la kibinafsi. Na hali miaka 30 au 40 iliyopita ilionekana kuna wakati—wakati wa kuzungumza, kusoma, kuandika barua, kutembea kama jamaa, kutafakari. Ni kwa sababu gani mambo yamebadilika? Namna fulani ya ongezeko la mambo imeupata wakati wetu. Kwa kweli mara nyingi mambo yanayofanywa katika siku moja si ya kadiri ambayo ingestahili katika saa 24. Kwa sababu gani? Kwa sababu “mwivi” ameingia katika nyumba nyingi akachukua wakati mwingi wenye thamani. Je! unamtambua “mwivi” huyo? Ndiyo, ni televisheni, pamoja na uvutano wake wenye kulemaza. Uchunguzi mmoja unaonyesha kwamba “jamaa ya kawaida ya Kiamerika inatazama televisheni kiasi cha saa 7 na dakika 22 kwa siku moja.” Hiyo ni karibu theluthi moja (1/3) ya siku! Kwa wastani, wewe unatumia wakati mrefu kadiri gani ukitazama televisheni kila siku? Kila siku, ulimwenguni pote, mabilioni ya saa za maisha zenye thamani zinapotezwa watu wanapokuwa wakitazama televisheni. Ni kweli kwamba programu fulani ni safi, zenye kutumbuiza au zenye kuelimisha. Lakini hata hizo zinaweza kuwa zenye kumaliza wakati. Chambo cha televisheni ni chenye kushawishi sana.
21. (a) Ni tatizo gani ambalo huenda wengine wakawa nalo? (b) Unafikiri utatuzi ni nini
21 Wakristo wanaweza kuepukaje wasiibiwe na “mwivi” huyo? Ni kwa kusimamia sana tu wakati. Wekeeni vipimo wakati wenu wa kutazama televisheni. Wekeni mambo yaliyo ya maana zaidi—watu na uhusiano ni wa maana zaidi ya televisheni. Kwa mfano, unachukizwa kidogo na wageni wanaotembea wakati wa wonyesho uupendao zaidi katika televisheni? Na je, unaona ugumu kuzima televisheni, hata wakati programu inakuwa yenye kuchosha au mbaya? Basi una tatizo.—1 Wakorintho 9:24-27.
22. Tunaweza kununuaje wakati wa kutazama televisheni tuutumie kwa ajili ya mambo mengine?
22 Ni hatua gani zinazofaa ambazo ungeweza kuchukua ili ununue saa hizo zenye thamani kwa ajili ya funzo la kibinafsi na kwa ajili ya uhusiano na wengine? Andika programu zinazostahili kutazamwa na Mkristo na uzitazame tu ikiwa hakuna jambo jingine la maana linalotaka kufanywa. Wengine hata wamechukua hatua kali zaidi—kutokuwa kabisa na televisheni nyumbani! Hilo ni jambo la kibinafsi. Lakini kwa hakika hawawi maskini wa kiroho kwa sababu ya kutokuwa na televisheni.—Waefeso 5:15,16.
23, 24. Tunaweza kufanya nini ili kuonyesha kuthamini kwa kweli urithi wetu? (Waebrania 11:26)
23 Basi, tunaweza kufanya nini ikiwa tunataka kuhifadhi urithi wetu wenye thamani na kutouuza kwa ajili ya ‘bakuli moja la mchuzi wa dengu’? Hakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi katika maisha ya Mkristo. Jiwekee mambo yaliyo ya maana zaidi na kushikamana nayo. Dhamiria kutii ili upate zawadi ya uzima wa milele, sawa na mtume Paulo ‘alivyofuatia mradi wa thawabu ya wito wa juu.’ Kama Yakobo, onyesha kuthamini sana urithi huo. Kama Musa, ‘tazamia kwa makini kulipwa zawadi.’—Wafilipi 1:9, 10; 3:13, 14, NW; Waebrania 11:24-26, NW.
24 Tunaweza kujisukumaje tufanye yote hayo? Kupitia funzo la Biblia la kujitahidi sana. Fuata hilo kila siku maishani mwako. Hudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida na kusikiliza sana unapokuwa huko. Penda yaliyo ya uadilifu na kuchukia yaliyo mabaya. Usiudharau urithi wako hata kwa kusudi la kutosheleza tamaa fulani ya haraka ya kimwili. Urithi wako, uzima wa milele, unastahili zaidi sana kuliko ‘bakuli lo lote la mchuzi wa dengu,’ uwao wote katika siku za kisasa!—Waebrania 10:24, 25; 12:12-16.
Unakumbuka?
◻ Urithi wa Kikristo ni nini?
◻ Esau alidharauje haki ya uzaliwa yake?
◻ Kuna hatari gani kwa Wakristo leo kuhusiana na urithi wao?
◻ Tunaweza kuongeza kuthamini kwetu katika njia zipi tofauti-tofauti?
[Picha katika ukurasa wa 9]
Je! wewe ungeweza kubadilishana urithi wako na ‘bakuli la mchuzi wa dengu’?