Waliosafishwa na Wenye Bidii kwa Ajili ya Kila Kazi Njema
‘Yesu Kristo alijitoa ili asafishe kwa ajili yake watu walio wake hasa, wenye bidii kwa ajili ya kazi njema.’—TITO 2:13, 14, NW.
1. Ni kwa sababu gani mashahidi wa Yehova wanapaswa kuwa safi na wenye bidii?
YEHOVA ni mtakatifu, mwema na asiye na hila. Yeye na Mwanaye pia wanatimiza kazi bora sana kwa bidii. (Mambo ya Walawi 19:2; Zaburi 25:8; Yohana 5:17) Kwa hiyo, mashahidi wa Yehova wote ni lazima wajisafishe na kuwa wenye bidii kwa ajili ya kazi njema.
2. (a) Mtume Paulo alikamatanishaje usafi na bidii? (b) Tutachunguza maswali gani sasa?
2 Mtume Paulo alitaja usafi na bidii alipoandika kwamba kwa fadhili zisizostahilika za Mungu, “alijitoa kwa ajili yetu ili atuokoe na kila aina ya uvunjaji wa sheria na kusafisha kwa ajili yake watu walio wake hasa, wenye bidii kwa ajili ya kazi njema.” (Tito 2:11-14, NW) Kuna matakwa gani kwa wale ambao Yesu amesafisha? Tunapaswa kuwa wenye bidii kwa ajili ya kazi njema gani? Na mashahidi waliosafishwa na wenye bidii wa Yehova wanafurahia baraka gani?
Usafi wa Kiroho Ni wa Lazima
3. (a) Watumishi wa Yehova wanapaswa kudumisha kiwango gani cha usafi? (b) Uhitaji wa usafi ulikaziwaje wakati wahamishwa Wayahudi walipofunguliwa kutoka Babuloni?
3 Ni lazima watumishi wa Yehova wadumishe kiwango cha juu cha usafi wa kimwili, kiadili na kiroho. (Kutoka 30:17-21; Kumbukumbu la Torati 23:12-14; Waefeso 5:25-27; 2 Wakorintho 7:1) Jambo hilo la msingi lilikaziwa katika karne ya sita K.W.K., wakati wahamishwa Wayahudi walipofunguliwa kutoka Babuloni. (Ezra 1:1-4) Upesi baada ya hapo wangefunga safari ya kurudi katika nchi ya kwao, kwa furaha wakiwa wamebeba vyombo vitakatifu ambavyo Mfalme Nebukadreza alikuwa amechukua kutoka hekalu la Mungu katika Yerusalemu. Lilikuwa jambo la lazima kama nini kwamba vyombo hivyo vya patakatifu vichukuliwe na waabudu safi wa Yehova peke yao! Basi, kwa kufaa, waliambiwa hivi: “Jitengeni, jitengeni, tokeni huko, msiguse kitu cho chote kichafu; tokeni katikati yake, endeleeni kuwa safi, ninyi ambao mnachukua vyombo vya Yehova.” (Isaya 52:11, NW) Wachukuaji hao walipaswa kusafishwa uchafu wote wa dini na adili wa Babuloni.
4. Kwa kupatana na 2 Wakorintho 6:14-17, ni nini kinachotakiwa kwa mashahidi wote wa Yehova?
4 Mtume Paulo alihusisha dai hilo la usafi na Wakristo wapakwa mafuta wanaoacha Babuloni Mkuu, milki ya ulimwengu ya dini ya uongo. Aliandika hivi: “Msifungiwe nira pamoja na wasioamini, kwa jinsi isivyo sawasawa; kwa maana pana urafiki gani kati ya haki na uasi? . . . Kwa hiyo, Tokeni kati yao, mkatengwe nao, asema [Yehova], Msiguse kitu kilicho kichafu.” (2 Wakorintho 6:14-17; Ufunuo 18:4, 5; Yeremia 51:45) Kweli kweli, Yehova anataka usafi wa kiroho kwa wafuasi wapakwa mafuta wa Yesu na wenzi wao, “mkutano mkubwa.”—Ufunuo 7:4-9.
‘Kataa Ubaya na Tamaa za Kilimwengu’
5. Kulingana na 2 Wakorintho 4:2, huduma yetu inapasa kuwaje?
5 Kati ya mambo mengine, wale wanaotumikia wakiwa mashahidi wa Yehova walio safi kiroho wamepewa mwito wa “kukataa ubaya na tamaa za [kilimwengu].” (Tito 2:11, 12) Kama alivyosema Paulo mahali pengine: “Tumekataa mambo ya aibu yaliyositirika, wala hatuenendi kwa hila, wala kulichanganya neno la Mungu na uongo; bali kwa kuidhihirisha iliyo kweli twajionyesha kuwa na haki, dhamiri za watu zikitushuhudia mbele za Mungu.” (2 Wakorintho 4:2) Kama mtume, Wakristo wa kisasa ni lazima wajithibitishe kuwa wasio na lawama katika huduma yao, bila shtaka lo lote la kweli la kuwa wamepotoka au ni wenye hila katika matendo yao. (2 Wakorintho 8:20, 21; Zaburi 101:1-8) Ni lazima wasiongozwe na hekima ya ulimwengu na roho yake, au kani yenye kutendesha, yenye dhambi na ya choyo.—1 Wakorintho 1:21; 2:12; 3:19; Waefeso 2:1, 2.
6. Ni jambo gani tunaloweza kufanya ikiwa tunashindana na maelekeo kama vile kupotoka na tamaa za mwili zisizofaa?
6 Ili watimize makusudi yao, watu wenye roho ya kilimwengu mara nyingi wanatumia njia za hila. Lakini ikiwa anayedai kuwa Mkristo anafanya hivyo, yeye ‘hajakataa ubaya’ na hafurahii ukaribu pamoja na Yehova. (Mithali 3:31, 32) Na ikiwa mtu anaongozwa na tamaa chafu za mwili, ‘hajakataa tamaa za kidunia.’ (Wagalatia 5:19-21; 1 Yohana 2:15-17) Lakini tufanyeje ikiwa tunashindana na maelekeo yasiyo ya kiroho kama vile kuwa wenye hila na tamaa za kimwili zisizofaa? Basi ingefaa kusali kama Daudi, aliyesema: “Umba ndani yangu moyo safi, Ee Mungu, na weka ndani yangu roho mpya, iliyo imara. Usinitupilie mbali mimi kutoka mbele za uso wako; na roho takatifu yako Ee usiiondoe kwangu mimi.” (Zaburi 51:10, 11, NW; Yohana 15:19) Tukisali kwa njia hiyo na kutumia kwa faida kamili msaada unaopatikana kupitia Neno la Mungu, roho na tengenezo, tutaweza kunyosha kufikiri kwetu na kuweza kutumikia kwa uaminifu tukiwa waabudu safi wa Yehova.
7. Ni kwa sababu gani wakosaji wasiotubu wanapaswa kutengwa na ushirika?
7 Ikiwa wengine kati yetu bila kutubu wanafuatia mwendo ulio mchafu sana, ni lazima watengwe na ushirika ili jina la Yehova lisitukanwe, tengenezo lake linatunzwa likiwa safi na watumishi wake waaminifu wanalindwa na kukaziwa uzito wa ufanyaji wa kosa zito. (Mambo ya Walawi 22:31-33; Kumbukumbu la Torati 13:6-11) Miaka mingi iliyopita, watu wa Mungu walitambua kwamba mkosaji asiyetubu hakustahili tena ushirika wao. Kwa mfano, mwaka wa 1904 msimamizi wa kwanza wa Sosaiti, Charles Taze Russell, aliandika hivi: “Ni lazima kundi limnyang’anye ushirika walo na ishara zo zote au mawonyesho yo yote ya udugu.” (Kitabu The New Creation, ukurasa 290) Leo, pia, watu wa Yehova wanafuata shauri la Kimaandiko la ‘kumwondoa mbaya’ miongoni mwao.—1 Wakorintho 5:9-13.
8. Maandiko ya Luka 3:8 na Wagalatia 6:1 yanahusuje juu ya jinsi wazee wanavyoshughulika na wakosaji?
8 Kutunza tengenezo la Yehova likiwa safi ni jambo la kuhangaikiwa sana na wazee waliowekwa. Bila shaka, ni lazima wawe wenye rehema wakati ‘matunda yanayoistahili toba’ yanapoonyeshwa, sawa na ambavyo Yehova anatoa rehema inapofaa. (Luka 3:8, NW; Zaburi 86:15; 130:3, 4) Na mwamini mwenzi akichukua hatua ya uwongo kabla hajatambua, wale wenye sifa za kiroho wanapaswa kujaribu kumrekebisha “kwa roho ya upole.”—Wagalatia 6:1.
Jinsi Wazee Wanavyoweza Kusaidia
9. Ni njia gani mbili ambazo wazee wanaweza kuwasaidia Wakristo wengine kiroho?
9 Waangalizi wanaweza kusaidiaje Wakristo wengine waendelee kuwa safi kiroho? Njia moja ni kwa kutoa hotuba zenye kujenga. Njia nyingine ni kupitia mazungumzo ya kibinafsi na ziara za uchungaji. (1 Petro 5:1-4) Nyakati hizo, kwa kufaa wazee wanatumia Biblia kufundisha, kukumbusha, kutia moyo na hata kukaripia waamini wenzi.
10. (a) Wazee wanapaswa kuwa na nia gani kuelekea kusema mbele ya watu wote? (b) Ni kwa sababu gani wachungaji wa kiroho wanapaswa kuwa wanafunzi wa Biblia wenye bidii?
10 Uhitaji wa kufundisha ulikaziwa wakati Paulo alipomsihi mfanyi kazi mwenzi wake Tito “nena mambo yapasayo mafundisho yenye uzima.” (Tito 2:1) Wazee wanyenyekevu Wakristo hawatafuti utukufu wakiwa wasemaji wa watu wote bali wanataka sana kutumia Biblia vizuri wafundishe. (Mithali 25:27) Kwa kupendeza, aliyekuwa rais wa Marekani wakati mmoja John Quincy Adams alisema: “Kwa miaka mingi nimelifanya zoea kusoma Biblia yote mara moja kila mwaka.” Kila mfalme wa Israeli alipaswa kufanyiza nakala ya sheria ya Mungu na kusoma “humo siku zote atakazoishi.” Yoshua alifuata maagizo ayo hayo. (Kumbukumbu la Torati 17:14-20; Yoshua 1:7, 8) Bila maarifa waliyopata kwa njia hiyo, wanaume hao wa Israeli ya kale wangewezaje kutenda kwa hekima au kusaidia wengine kiroho? Kwa hiyo ikiwa wewe ni mzee aliyewekwa, je, umekwisha kuisoma Biblia yote, labda mara nyingi? Bila shaka kufanya hivyo kungeongeza uwezo wako wa kushauri wengine, kutia Wakristo walio wakfu ambao pengine wao wenyewe wamekwisha kusoma Maandiko yote mara nyingi. Wale wanaotumikia wakiwa wachungaji wa kiroho wanapaswa kuwa wanafunzi wenye bidii sana wa Neno la Mungu, lililo msingi wa “mafundisho yenye uzima.”
11. (a) Ni vikumbusho gani vya Kimaandiko vilivyohitajiwa na Wakristo wa karne ya kwanza katika Krete? (b) Kuhusu vikumbusho vya Kibiblia, wazee waliowekwa wanapaswa kuwa wanstahili kufanya nini?
11 Vilevile Paulo alimwambia Tito hivi: “Endelea kuwakumbusha kuwa wenye kunyenyekea na kutii serikali na mamlaka kuwa watawala, kuwa tayari kwa kila kazi nzuri, kutosema yenye kuumiza juu ya ye yote, si kuwa wenye kutaka vita, wepesi kukubali maoni ya wengine, wenye kuonyesha upole wote kwa watu wote.” (Tito 3:1, 2, NW) Vikumbusho hivyo vya waziwazi vilihitajiwa na Wakristo wa karne ya kwanza kwenye kisiwa cha Krete. Vivyo hivyo, tatizo linapotokea leo, wazee wanapaswa kuweza kutaja vikumbusho vya Kimaandiko vinavyofaa. Na sikuzote na tuwe wenye shukrani wakati tunapoonyeshwa vikumbusho vya Yehova.—Zaburi 119:99, 129.
12. (a) Maana yake nini kuonya kwa bidii? (b) Onyo la bidii lapasa litolewe kwa nia gani?
12 Vilevile Tito aliambiwa hivi: “Endelea kuwaonya kwa bidii wanaume vijana wawe timamu katika akili.” (Tito 2:6, NW) Kwa sababu ya upendo wake wa kweli na hangaikio, Paulo hakukosa kuonya kwa bidii ilipohitajiwa. Kwa kweli, angeweza kuwaambia hivi wazee wa Efeso: “Endeleeni kukesha na kukumbuka kwamba kwa miaka mitatu, usiku na mchana, sikuacha kuwaonya kwa bidii kila mmoja kwa machozi.” (Matendo 20:31, NW) Wazee wa siku hizi wanaoonyesha nia iyo hiyo, na wanaotoa kitia moyo cha nguvu au kuonya kwa bidii, ni baraka kweli kweli kwa kundi!
13. (a) Kukaripia ni kufanya nini? (b) Wazee wanapaswa kutoa karipio wakiwa na nia gani?
13 Vilevile Paulo alitaja karipio, akamsihi Tito hivi: “Endelea kuwakaripia kwa ukali, ili wawe wenye afya katika imani, kutosikiliza hadithi zisizo za kweli za Wayahudi na amri za watu wanaojiondoa mbali na ule ukweli.” (Tito 1:13, 14, NW) Kukaripia ni “kujulisha kosa kwa kawaida kukiwa na kusudi la fadhili la kusahihisha au kusaidia,” au “kuonyesha kutokubali” mtu kwa ajili ya maneno au matendo yake. (Kamusi Webster’s New Collegiate Dictionary) Paulo alizungumza juu ya kukaripia, lakini kwa kusudi zuri—“ili wawe wenye afya katika imani.” Vivyo hivyo leo, wazee wanaepuka ukali usio wa Kikristo. Tofauti na waasi wa imani wenye kulalamika, wazee wa kweli walio Wakristo hawajaribu kuwa “mabwana” wa imani na maisha za waamini wengine bali wanatumikia wakiwa mawakili na wafanyi kazi wenzao iwe kwa furaha yao, wakiwasaidia wasimame imara katika imani yao.—2 Wakorintho 1:24, NW; 1 Wakorintho 4:1, 2.
14. Ni nini kitakachotusaidia tubaki tukiwa safi kiroho?
14 Kutii mafundisho, vikumbusho, maonyo ya bidii na makaripio ya Biblia kutatusaidia tubaki tukiwa safi kiroho. Kufanya hivyo kunatufanya tufae kwa ajili ya utumishi mtakatifu wa Mungu. Lakini tunapaswa kufanya utumishi huo kwa roho gani?
Uwe na “Bidii kwa Ajili ya Kazi Njema”
15. (a) Bidii inaweza kufasiriwaje? (b) Ni kazi gani iliyo bora zaidi ambayo Mkristo anaweza kufanya?
15 Wakiwa baraza lililo tengenezo la Wakristo walio wakfu, Mashahidi wa Yehova ni “wenye bidii kwa ajili ya kazi njema.” Bidii maana yake ni “kutaka sana na kupendezwa kwingi kushughulikia jambo fulani.” (Kamusi Webster’s New Collegiate Dictionary) Kulingana na barua ya Paulo aliyomwandikia Tito, Wakristo wote wanapaswa kufuatia “kazi njema” za namna nyingi. Kwa mfano, wanawake vijana wanapaswa kuwa safi, wafanyi kazi nyumbani na wenye kutii waume zao. Tito alipaswa kuwa “mfano wa kazi njema,” aonyeshe kutokupotoka katika mafundisho yake, atumie usemi wenye kujenga, na kadhalika. (Tito 2:1-14, NW) Bila shaka, kazi bora zaidi anayoweza kufanya Mkristo ni ile ya kuwasaidia wengine wajifunze juu ya Mungu na kumtumikia Yeye. Ikiwa wewe ni shahidi wa Yehova, je, kweli kweli wewe ni mwenye bidii katika kufanya “kazi njema”? Wakristo wa karne ya kwanza walionyesha bidii ya kueneza evanjeli, hata ilipomaanisha mateso.—Matendo 11:19-21.
16. (a) Sababu ya msingi ya kuwapo kwa kundi la Kikristo ni nini (b) Ni maulizo gani yamesemwa juu ya kazi ya kueneza evanjeli ya Mashahidi wa Yehova?
16 Kujapokuwa kuteswa kwa Mashahidi wa Yehova leo, roho ya Mungu inawasukuma watekeleze mgawo wa kuhubiri Ufalme—kufanya hivyo ni sababu ya msingi ya kuwapo kwa kundi la Kikristo. (Mathayo 24:14; 28:19, 20; Isaya 61:1, 2) Kama Wakristo wa kwanza, kwa bidii wanafanya kazi njema ya kutangaza “habari njema” nyumba kwa nyumba na kwa njia nyinginezo. (Matendo 5:41, 42; 20:20, 21) Katika kitabu chake Evangelism, inc., G. W. Target anazungumza juu ya njia za kutoa ushuhuda kutia “uenezaji wa evanjeli mlangoni” na kusema kwamba “watu wengine hata wangesema ndiko njia iliyo ya kawaida zaidi—hasa baada ya ziara ya karibuni zaidi ya Mashahidi wa Yehova. . . . Wengine wameanza kufanya hivyo sana, lakini Mashahidi wa Yehova wanaongoza.” Kuhusu matumizi ya vitabu vya Biblia, Target anakubali hivi: “Kwa mara nyingine, Mashahidi wa Yehova wanaongoza. . . . Kwa kulinganisha, . . . kwa kweli ni dini chache sana zinazochapisha vitu vya kueneza evanjeli.” Kweli kweli, vitabu vya Kikristo vinavyotayarishwa kwa msaada wa roho takatifu ya Mungu na vinavyopatikana kwa Mashahidi wa Yehova kwa mchango vinasaidia wenye mfano wa kondoo duniani pote wajifunze na kufanya mapenzi ya kimungu.
17. Inaweza kuthibitishwaje kwamba Mungu amefanikisha kazi ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova?
17 Yehova alifanikisha kazi ya kuhubiri ya Wakristo wa kwanza. Kwa sababu hiyo makundi yalianzishwa mahali pamoja baada ya pengine—Roma, Korintho, Efeso, Filipi, Kolosai, Thesalonike na kwingine. Hali moja na hiyo, Yehova anafanikisha utendaji wa kuhubiri wa watumishi wake wa kisasa, hata kwamba makundi zaidi ya 47,000 ya Mashahidi wa Yehova sasa yapo ulimwenguni pote. Sifa inamwendea Mungu kwa ajili ya ukuzi huo mzuri ajabu.—Isaya 60:22; 1 Wakorintho 3:6, 7.
Baraka Nyingi Zetu
18-20. Ni zipi nyingine kati ya baraka tunazofurahia tukiwa watumishi wa Mungu?
18 Watu wa Yehova leo wanafurahia baraka na faida nyingi kweli kweli za utumishi wa bidii na ulio safi. (Mithali 10:22) Kwa mfano, tukiwa watumishi wa Mungu waliosafishwa, tuna uradhi wa kumpendeza yeye. (1 Petro 1:13-16) Ukweli wa Kimungu umetuweka huru na Babuloni Mkuu, milki ya ulimwengu ya dini ya uongo. (Ufunuo 18:4, 5) Sisi si mateka wa ushirikina, hatuogopi wafu na mambo kama hayo. (Mhubiri 9:5, 10; Yohana 8:32) ‘Amani ya Mungu inalinda mioyo yetu na nguvu za akili.’ (Wafilipi 4:6, 7, 13, NW) Kukusanyika kwa ukawaida na waabudu safi kunafanya tujisikie salama, kama ‘kondoo katika zizi.’ (Mika 2:12) Kuwa na roho takatifu ya Mungu kunatusaidia tuonyeshe matunda ya upendo, furaha, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole na kujiweza. (Wagalatia 5:22, 23) Hayo yote yanapasa kutufanya tufurahi kama nini!
19 Tukiwa watangazaji wa Ufalme wenye bidii, tunamtumikia Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote—ambalo ni pendeleo bora zaidi ambalo mwanadamu ye yote anaweza kuwa nalo. Yetu ni “kazi takatifu ya habari njema.” Hakuna shughuli nyingineyo yote ya kidunia inayoleta furaha kubwa zaidi ya kutangaza ujumbe wa “Mungu wa furaha” na kusaidia wengine wajifunze juu yake!—Warumi 15:16, NW; 1 Timotheo 1:11, NW.
20 Uhusiano wa karibu pamoja na Mungu ni baraka nyingine kati ya baraka nyingi zetu. Tunaweza kusali kwake tukiwa na uhakika kwamba atatusikia. (1 Yohana 5:14, 15) Ni jambo zuri ajabu kuwa na ukaribu huo kwa Yehova! Ni kama mtunga zaburi alivyosema: “Kumkaribia Mungu ni kuzuri kwangu. Katika Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu ndimo nimeweka kimbilio langu, nipate kuzitangaza kazi zako zote.”—Zaburi 73:28, NW.
21. Tukiwa watu wa Yehova waliosafishwa na wenye bidii, azimio letu lapasa kuwa nini?
21 Basi kwa sababu ya baraka zetu nyingi tukiwa watu wa Mungu waliosafishwa na wenye bidii, na tuazimie kubaki tukiwa safi kiroho na wenye kuwaka kwa bidii ya kimungu. Tukibaki hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatutegemeza na kutuelekeza tukiwa mashahidi wake. Zaidi ya hayo, usafi na bidii katika utumishi mtakatifu wa Mungu katika hizi siku za mwisho, kwa fadhili zisizostahilika zake, zitatufungulia njia tutumie umilele tukifanya kazi safi na za bidii iwe kwa sifa ya Yehova.
Wewe Ungejibuje?
◻ Ni nini kinachohitajiwa ili mtu awe sehemu ya watu wa Yehova waliosafishwa?
◻ Wazee waliowekwa wanaweza kusaidiaje wengine waendelee kuwa safi kiroho?
◻ Watu wa Mungu wanapaswa kuwa wenye bidii hasa kwa ajili ya kazi gani njema?
◻ Ni zipi nyingine kati ya baraka wanazofurahia mashahidi wa Yehova waliosafishwa na wenye bidii?
[Picha katika ukurasa wa 15]
Wazee wanapaswa kuwa wanafunzi wenye bidii wa Biblia na wanapaswa kuitumia ili kufundisha, kukumbusha, kuonya kwa bidii na hata kukaripia wengine