Har–Magedoni—Itatoka kwa Mungu wa Upendo?
““HAR-MAGEDONI”—jina hilo la Kibiblia lina maana gani? Mfululizo wa makala zenye habari nyingi zinazohusu kichwa hicho utakuwa katika matoleo manne ya Mnara wa Mlinzi ya Juni na Julai 1985, na kila mara jalada la gazeti litakuwa la hali yenye kupatana na habari. Inatumainiwa kwamba mazungumzo hayo ya Kimaandiko yatakufariji kwa kukujulisha maana yenyewe hasa ya HAR-MAGEDONI.
WEWE unafikiri juu ya nini unapoona neno “Har–Magedoni”? Kwa wengi linamaanisha pambano lenye jeuri kati ya mataifa yenye nguvu zaidi ya ulimwengu. Wengi wanapiga picha akilini na kuona maafa makubwa yatakayoifuata—maangamizi makubwa ya nyukilia yatakayoifanya dunia yetu kuwa kaa lililo ukiwa, lenye miale yenye sumu na kuwapo kwa waokokaji wachache, ikiwa wo wote wataokoka. Lakini, tofauti na maoni hayo yaliyoenea sana, hiyo siyo Har–Magedoni hata kidogo.
Neno “Har–Magedoni” chanzo chake ni Biblia. Na humo linaonekana mara moja tu—katika sura ya 16 ya kitabu cha Ufunuo. Baada ya kueleza jinsi “wafalme wote wa ulimwengu” watakavyokusanywa “kwa ajili ya vita ya Siku Kuu ya Mungu Mwenyezi,” unabii huo unasema: “Wakawaita wafalme waje pamoja mahali paitwapo, katika Kiebrania, Har–Magedoni.”—Mistari 13 hadi 16, The Jerusalem Bible.
“Vita ya Siku Kuu ya Mungu Mwenyezi”! Kwa wazi, Har–Magedoni ni vita ya Mungu. Ni kweli inawatia ndani wafalme, au mataifa, ya ulimwengu. Lakini wanakuja, si kupigana wao kwa wao, bali ili wapigane dhidi ya Mungu na majeshi ya kimbingu yakiongozwa na Mfalme wake aliyewekwa, Yesu Kristo—ambaye anafananishwa akiwa amempanda farasi mweupe. Matokeo yanakuwa nini? Masimulizi ya Biblia yanasema: “Wafalme wa [dunia], na majeshi yao, [wakakusanyika] kufanya vita na yeye aketiye juu ya farasi yule, tena na majeshi yake. . . . [Wakauawa] kwa upanga wake yeye aliyeketi juu ya yule farasi . . . Na ndege wote wakashiba kwa nyama zao.”—Ufunuo 19:19-21.
Vita Yenye Umwagaji Mwingi wa Damu
Har–Magedoni itakuwa yenye kuleta uharibifu mkubwa hivi kwamba mauaji hayo yanatajwa kuwa ni kuvuna “mavuno ya nchi” kwa mundu wenye makali. “Malaika yule akatupa mundu wake hata nchi, akauchuma mzabibu wa nchi, akazitupa zabibu katika shinikizo hilo kubwa la ghadhabu ya Mungu. Shinikizo lile likakanyagwa nje ya mji, damu ikatoka katika shinikizo mpaka kwenye hatamu za farasi, kama mwendo wa maili mia mbili.”—Ufunuo 14:15-20.
Ndiyo, damu nyingi itamwagwa na majeshi ya Mungu yenye kuua. Vile vifo 69 milioni vya vita vya ulimwengu viwili vitakuwa si kitu vikilinganishwa na wale waliouawa katika vita ya Mungu ya Har–Magedoni. Kuwahusu hao nabii Yeremia aliandika hivi: “Na waliouawa na [Yehova] siku ile watakuwapo, toka upande mmoja wa dunia hata upande wa pili; hawataliliwa, wala kukusanywa, wala kuzikwa; watakuwa samadi juu ya uso wa nchi.”—Yeremia 25:30-33.
Makombora yenye kuwaka moto, mvua za moto, na kani nyingine zenye kuleta msiba ambazo zitaambatana na hukumu ya Mungu zitaleta hofu kubwa ndani ya mioyo ya wanadamu duniani pote. Kwa kuvurugika kila mmoja atamgeukia jirani yake, huku majeshi ya kuua ya Mungu yakiwapiga bila kujali wao ni wa umri gani au jinsia gani. Kwa maana Mungu anawaagiza wasionyeshe rehema yo yote: “Mkapige; jicho lenu lisiachilie, wala msione huruma; waueni kabisa, mzee, na kijana, na msichana, na watoto wachanga, na wanawake.”—Ezekieli 9:5, 6; Zekaria 14:12, 13.
Lakini inawezaje kuwa hivyo? Mungu wa upendo anawezaje kutoa agizo kama hilo? Au je, yeye ni Mungu mwenye ubaridi, asiyejali, mwenye kutaka kulipa kisasi, asiye na huruma kwa uumbaji wake wa kibinadamu? Je! kweli kweli Mungu wa upendo angeleta vita ya namna hiyo kama Har–Magedoni?