Mwisho wa Vita Vyote—Je! Unaweza Kufikiwa?
“HAR-MAGEDONI”—jina hilo la Kibiblia lina maana gani? Mfululizo wa makala zenye habari nyingi zinazohusu kichwa hicho umekuwa katika matoleo manne ya Mnara wa Mlinzi ya Juni na Julai 1985, na kila mara jalada la gazeti limekuwa la hali yenye kupatana na habari. Inatumainiwa kwamba mazungumzo hayo ya Kimaandiko yanakufariji kwa kukujulisha maana yenyewe hasa ya HAR-MAGEDONI.
“NJONI, enyi watu, yatazameni matendo ya Yehova, jinsi alivyoweka matukio yenye kustaajabisha duniani. Yeye avikomesha vita hata sehemu ya mwisho ya dunia. Upinde au vunja-vunja naye au kata-kata mkuki; magari ya vita ayateketeza katika moto.”—Zaburi 46:8, 9, NW.
Maneno hayo yaliyo juu ya mtunga zaburi aliyeongozwa na roho ya Mungu yanapatana na tamaa ya moyoni ya watu katika vizazi vyote. Kwa kweli, ni nani ambaye hajatamani kuona siku ile ambapo vita haitakuwapo tena? Hata hivyo, ijapokuwa tumetaka sana kuiona, kufikia sasa, mwisho wa vita umeshindwa kuletwa na jitihada zote za kibinadamu. Si kwamba tu vita viko pamoja nasi kwa wingi bali pia vimekuwa vyenye kuharibu sana na vyenye kuua sana hata kwamba kwa mara ya kwanza katika historia ya kibinadamu kuendelea kuwako kwa ustaarabu, na hata uhai wenyewe, uko hatarini.
Kwa sababu ya hatari kubwa sana iliyoko mbele, hatuna budi kuuliza: Ni kwa sababu gani jitihada za kibinadamu za kuzuia vita zimeshindwa vibaya sana? Je! kweli vita haviwezi kuepukika? Ndiyo, hasa ni kwa sababu gani vita vimepiganwa?
Sababu ya Jitihada za Kibinadamu Kushindwa
“Ikiwa unaishi katika ujirani ambao hakuna polisi na kila mtu ana bunduki na daima anaishi akiogopa kushambuliwa, basi kutakuwako mtupiano mwingi wa risasi,” aandika mwandikaji wa magazeti na mwanahistoria wa mambo ya kijeshi Gwynne Dyer. “Huo ndio ujirani ambao mataifa yote ya ulimwengu yanaishi ndani yake,” aendelea kusema. “Hakuna polisi wa kimataifa, kwa hiyo kila nchi inajipa silaha daima na tayari kutumia jeuri; lakini namna ya jeuri ambayo mataifa yanahusika ndani yake ina jina la pekee. Tunaiita vita.”
Ingawa hayo ni maelezo yaliyorahisishwa, yanaonyesha mambo kadha ya msingi yanayofanyiza vita. Ni lazima kuwepo njia ya kufanya vita na pia maelekeo ya kufanya hivyo. Pamoja na hayo, tunaona pia ukosefu wa kufuata sheria na utaratibu katika “ujirani,” ambao katika habari hii ni ulimwengu.
Wanahistoria wanaojulikana sana Will na Ariel Durant walitaja mambo hayo hayo ya msingi walipoandika hivi katika kitabu chao The Lessons of History. “Katika ukosefu wa sasa wa sheria na maoni ya kimataifa ni lazima taifa liwe tayari dakika yo yote kujikinga; na wakati faida zalo za lazima zinapohusika linapasa liruhusiwe kutumia njia yo yote linaloona kuwa ni ya lazima ili liendelee kuwapo. Amri Kumi lazima ziwe kimya wakati hali ya kujihifadhi inapokuwa hatarini.”
Kwa hiyo, kufanikiwa au kushindwa kwa jitihada yo yote kukomesha vita kungetegemea kwa sehemu kubwa juu ya jinsi linavyoshughulika na mambo hayo ya msingi. Je! mpango wo wote wa kibinadamu, hata uwe ni wazo zuri namna gani, umefanikiwa kufanya hivyo? Ebu tuchunguze mambo ya hakika.
Ukosefu wa Utaratibu wa Mataifa Yote
Majaribio mengi yamefanywa wakati uliopita ili kuunda shirika la ulimwengu la namna fulani lenye uwezo wa kuchunguza mataifa na kudumisha sheria na utaratibu katika mataifa yote. Ushirika wa Mataifa, kwa mfano, uliundwa mwishoni mwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ili uhakikishe kwamba ulimwengu haungetumbukizwa tena kwenye vita. Kama ilivyo ulizama ukapotelea mbali mwishoni mwa Vita ya Ulimwengu ya Pili. Halafu, mwaka wa 1945, tengenezo la Umoja wa Mataifa likatokea, likasifiwa na kuabudiwa na viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo kuwa tumaini la wanadamu la amani. Kumbukumbu yalo imekuwa nini? Kwa mara nyingine historia inatoa jibu. “Watu zaidi ya milioni nne sasa wanashiriki katika vita, maasi na mizozo ya ndani ya nchi tofauti tofauti 42. . . . Kati ya watu milioni moja na milioni tano wameuawa katika mapambano hayo,” likaripoti The New York Times mwaka wa 1984. Leo watu wachache wanaamini kwamba Umoja wa Mataifa unaweza kuzuia vita na mapigano yasitokee. Kuwapo kwao kunatimiza machache katika kuondoa woga wa vita ya ulimwengu ya tatu au maangamizi makubwa ya nyukilia.
Tisho na Wasiwasi Wenye Kuongezeka
Sababu moja ya mashirika kama Umoja wa Mataifa kuwa hoi yasiweze kuzuia vita ni kwamba mataifa kuuzunguka ulimwengu yamejitoa kabisa kwa enzi na haki za kitaifa. Hayajali sana juu ya daraka la kimataifa au amri za mwenendo. Ili kutimiza miradi yao, mataifa mengine yana maoni kwamba yana haki kabisa kutumia njia zo zote yanazoziona kuwa za lazima—kuchinja watu kwa wingi, kuua, kuteka nyara, kulipua makombora, na kadhalika—mara nyingi wasio na hatia wakiuawa. Hata mataifa makubwa ya ulimwengu yanasukumana sana yakisema ati ni kwa kusudi la kujihifadhi na kulinda faida za kitaifa. Ni kwa muda gani mataifa yataendelea kuvumiliana katika mwenendo huo wa upumbavu na usiofaa? Ni visa vingapi zaidi kama vya Falkland, Afghanistan, Grenada, kulipuliwa kwa ndege ya Korea, na kadhalika ambavyo ulimwengu unaweza kuvumilia bila kuwapo pigano kubwa? Si vigumu kuona ni kwa sababu gani utukuzo wa taifa na kushikilia kauli yao yamekuwa vizuizi vikubwa vya kukomesha vita.
Yana Silaha na Yako Tayari
Kufikia sasa inajulikana wazi kwamba silaha za mataifa yenye nguvu zaidi zimerundikwa kukiwa na silaha za nyukilia zinazotosha kuangamiza uhai wote wa kibinadamu duniani mara nyingi. Lakini namna gani mataifa yale mengine? Kulingana na ripoti ya serikali ya United States, mataifa yanayositawi kuuzunguka ulimwengu, ingawa yanakazwa sana kiuchumi, yametumia dola za United States zaidi ya bilioni 230 katika kumi moja la miaka lililopita ili kununua baadhi ya silaha za kiufundi zaidi zinazopatikana: ndege, makombora, na vifaru. Matokeo yamekuwa nini? “Imefikia kiwango ambacho wengi wa wanunuzi hao wana matatizo ya kuweza kutumia silaha mpya zao zote.” Mataifa hayo yana silaha nyingi kama njugu. Uhakika wa kwamba wana silaha zisizo za nyukilia peke yake unayafanya yatake zaidi kuzitumia.
Je! Kuna Sababu Yo Yote ya Kuwa na Tumaini?
Kushindwa tena na tena kwa jitihada za kibinadamu kukomesha vita kunakazia tu ukweli wa Biblia kwamba “kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) Hata wanadamu watake sana kama nini kuona mwisho wa vita, wao wenyewe hawajui hata kidogo jinsi ya kutekeleza hilo. Basi, namna gani ahadi ya kwamba ‘vita vitakomeshwa hata sehemu ya mwisho ya dunia’? Je! imetolewa ili kuamsha tumaini tu au kutudhihaki? Hakika sivyo. Kwa maana Yehova anatuhakikishia hivi kuhusu neno au ahadi yo yote inayotoka kinywani mwake: “Halitanirudia bure.” (Isaya 55:11) Basi, ahadi hiyo itatimizwaje? Kuna msingi gani hakika wa kutusadikisha kwamba Mungu atafaulu kutimiza jambo ambalo wanadamu wameshindwa tena na tena?