Yehova ‘Ayahimiza’
“Mimi, [Yehova], nitayahimiza hayo wakati wake.”—ISAYA 60:22.
1. Matazamio ya watu wa Yehova yanatofautianaje na yale ya ulimwengu wa Shetani, na kwa sababu gani?
LEO, furaha na shangwe vinapatikana si katika tengenezo la kimbingu la Yehova peke yake, bali pia kote kote katika tengenezo la Mashahidi wa Yehova hapa duniani. Furaha yetu inatofautiana sana na giza ambalo limeufunika ulimwengu wa Shetani. (Zaburi 144:15) Tuna chakula na kinywaji cha kiroho kwa wingi, hata kwamba ‘tunaimba kwa furaha ya moyo.’ (Isaya 5:13-19) Sisi tunajua sababu ya hali ya msiba ya ulimwengu iliyopo. Tumaini letu la uokovu wa mapema kupitia Ufalme wa Mungu linatiwa nguvu tunapoona unabii mbalimbali wa Biblia ukitimizwa katika wakati unaoendelea kupungua ili Har–Magedoni ifike. Tunajua kwamba hiyo “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” itakuja katika “wakati ulioamriwa” barabara, kwa maana njozi hiyo “inafanya haraka ili kuufikilia mwisho wake, wala haitasema uongo.”—Ufunuo 16:14, 16; Habakuki 2:3.
2. Ni hali gani zilizo kwa utele katika tengenezo la Yehova, na hilo linaongoza kwenye swali gani?
2 Hali moja na ilivyo mbinguni, duniani kuna hali ya kudumu ya tengenezo la kitheokrasi la Yehova. Zaidi ya hayo, kwa kuwa Yehova ndiye Chanzo cha nguvu nyingi, ‘huwapa nguvu wao wamtumainio.’ (Isaya 40:29-31) Tengenezo lake liko hai likitenda na daima linasonga mbele. (Linganisha Ezekieli 1:15-21.) Yale makundi 47,869 ya Mashahidi wa Yehova katika nchi 203 duniani pote yamefanywa tengenezo kwa njia nzuri ili yajikaze kwenda mbele kwa bidii katika kazi ya Ufalme. (Mathayo 24:14) Tengenezo hilo lenye nguvu la duniani pote lilitokezwaje?
3. (a) Andiko la Isaya 60:17 limetimizwaje katika nyakati za kisasa? (b) Ni mipango gani kama hiyo iliyoleta fanaka katika nyakati za Biblia?
3 “Tengenezo” ndicho kilichokuwa kichwa cha makala za funzo katika Mnara wa Mlinzi wa Juni 1 na 15, 1938. Makala hizo zilizungumza kirefu Isaya 60:17, ambapo Yehova anazungumza na tengenezo lake la kimbingu, akisema: “Badala ya shaba nitaleta dhahabu, na badala ya chuma nitaleta fedha, na badala ya mti, shaba, na badala ya mawe, chuma; tena nitawafanya wasimamizi wako wawe amani, na [wenye kukugawia kazi] kuwa haki.” Tukiifikiria hali hiyo iliyo bora, tengenezo la Yehova duniani lilitiwa uhai mpya. Kama vile dhahabu ilivyo yenye thamani zaidi ya shaba (na ni hali moja na vitu vinginevyo vilivyotajwa hapo), ndivyo mpango wa kitheokrasi ambao Sosaiti yetu ilieleza makundi ya watu wa Mungu huko nyuma mwaka wa 1938—na ambao makundi yaliukubali kwa moyo wote—ulivyo wa kupendelewa kuliko mipango ya kidemokrasi ya hapo kwanza. Mipango hiyo ni ya Kimaandiko. Inatokeza tengenezo zuri la kuifanyisha kazi ya Mungu, kama ambavyo mipango ya jinsi iyo hiyo ilivyoleta fanaka katika wakati wa Musa na katika siku za kwanza-kwanza za kundi la Kikristo.—Kutoka 18:25; Matendo 6:3-7; Tito 1:5; 1 Petro 5:1-3.
4. (a) Mashahidi wa Yehova walitiwaje nguvu wakabili majaribu ya 1939-45? (b) Ni nini kilichothibitisha kwamba baraka za Yehova zilikuwa juu ya mpango huo wa kitheokrasi?
4 Hivyo, mwaka wa 1938, mwaka mmoja kabla ya kutokea Vita ya Ulimwengu ya Pili, “wasimamizi” na ‘wenye kugawa kazi’ katika makundi yote wakawa “amani” na “haki.” Mpango wenye nguvu na wa umoja wa kitengenezo ulianza kutenda ukiwa na ongezeko lenye mazao. Yehova aliwabariki mashahidi wake wenye umoja. Hesabu zao karibu zilikuwa maradufu, kutoka 71,509 mpaka 141,607 kati ya 1939 na 1945, ijapokuwa mikazo na mateso ya miaka hiyo ya vita.
‘Jeuri Haitakuwapo Tena’
5. Kwa habari ya “amani,” watu wa Yehova wanatofautianaje na ulimwengu?
5 Lakini, namna gani juu ya kipindi kilichofuata Vita ya Ulimwengu ya Pili? Hakujawa na amani kati ya mataifa ya dunia. Kwa kweli inaripotiwa kwamba watu zaidi ya 30,000,000 wameangamia katika vile vita “vidogo-vidogo” ambavyo vimepigwa tangu mwaka wa 1945. Vita kufikia 40 vidogo-vidogo vimekuwa vikiwaka duniani pote wakati mmoja. Basi, sisi tunafurahi sana kutumikia pamoja na tengenezo ambalo limekataa jeuri! (Isaya 2:4; Mithali 20:22) Zaidi ya hayo, tukiwa tengenezo la duniani pote, tunafurahia amani katikati yetu. Kwa kutembea na ‘Mungu wa amani,’ tumepata “amani ya Mungu, ipitayo akili zote.”—Wafilipi 4:7-9.
6, 7. (a) Ni nini kinachofanya watu wa Mungu waonekane wakiwa tofauti? (b) Andiko la Isaya 60:18 limetimizwaje kutuelekea sisi? (c) Tunatofautiana katika njia gani kubwa na wanadini wa uwongo?
6 Kwa kuwa “amani” na “haki” ni tele kati ya watu wa Yehova, tuko tofauti sana na ulimwengu wa Shetani. Kwa kuona hilo, wengine wa majirani wetu wamesema, ‘Ninyi watu mnatuvutia, lakini hatupendi dini yenu.’ Lakini, je, si ni dini yetu imetufanya kuwa tulivyo? Sisi hatupendezwi na siasa zenye kupingana na chuki inayotenganisha mataifa. Bali, mapendezi yetu mawili ni (1) kufundisha wapole katika njia ya uokovu kupitia Ufalme wa Kristo na (2) kusifu Yehova, kuweka jina lake mbele ya watu wote liwe ushuhuda. Sisi ‘si sehemu ya ulimwengu.’—Yohana 17:14, 16, NW.
7 Kwa hiyo, tumeshiriki utimizo wa ahadi ya Yehova: “Jeuri haitasikiwa tena katika nchi yako, ukiwa na uharibifu hazitakuwa mipakani mwako; bali utaziita kuta zako, Wokovu, na malango yako, Sifa.” (Isaya 60:18) Sifa yote imwendee Mungu wetu Yehova! Viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo (na wenzi wao wote walioasi imani) wanalidharau jina hilo—hata kufikia hatua ya kinafiki ya kujaribu kuliondosha kabisa katika tafsiri za Biblia. Lakini “sisi tutakwenda kwa jina la [Yehova], Mungu wetu, milele na milele.”—Mika 4:5.
8. (a) Yehova anawapa watu wake kitia-moyo gani katika Isaya 60:19-21? (b) Gazeti moja lilisema nini baada ya kuona ukamilifu wao?
8 Yehova anatutia moyo tutembee.katika jina lake. Kwenye Isaya 60:19-21, yeye anahakikishia tengenezo lake la kimbingu kwamba atakuwa kwalo “nuru ya milele,” akifunika mng’aro wa jua na mwezi. Kwa njia ya kiroho, anakuwa uzuri walo, na kutimiza pia ahadi yake kwa watu walo: “Watu wako nao watakuwa wenye haki wote, nao watairithi nchi milele; chipukizi nililolipanda mimi mwenyewe, kazi ya mikono yangu mwenyewe, ili mimi nitukuzwe.” Kweli kweli, Yehova ameifanikisha “nchi,” au eneo la utendaji, la mashahidi wake. Kwa kuongezeka, ‘inachipuka’ kwa matunda wakati umati wa wapya unapokusanywa kwenye upande wa Ufalme na kusaidiwa wavae utu wa Kikristo. (Wakolosai 3:10, 12-14) Hilo ‘linamtukuza’ Yehova, kwa kuletea heshima jina lake lenye thamani.
9. Question missing from magazine
9 Mfano wa karibuni ni Meksiko. Katika miaka miwili iliyopita, kilele cha wahubiri katika nchi hiyo kimeongezeka kutoka 113-823 kufikia 151,807—asilimia ya kusifika ya 33! (Mwadhimisho wao wa Ukumbusho wa kifo cha Yesu mwaka wa 1984 ulihudhuriwa na watu 695,369.) Ndugu zetu wa Meksiko walikuwa wenye bidii sana katika utendaji wao wa shambani. Gazeti moja la Monterrey hivi karibuni, liliona pia, ukamilifu wao wa kukabiliana na suala la kutokuwamo, likasema jambo hili kati ya mengine: “Uthabiti na uhodari wao wa usadikisho unatia ndani yetu heshima nyingi kama nini. Hata ingawa watoto wao wanafukuzwa shuleni, wanaonelea ni afadhali waendelee wakiwa washikamanifu kwa imani yao, usadiki wao. Ingekuwaje kama sisi sote Wakristo tungekuwa hivyo, bila tofauti ya kikundi au dini? Meksiko ingekuwa afisi ya tawi ya mbinguni.”
10. (a) Ni nini kinachoonyesha Mashahidi wa Yehova wanazaa matunda hata chini ya marufuku? (b) Ni ulizo gani linalotokezwa hapa?
10 Mashahidi wa Yehova wanaendelea kuzaa tunda hili la sifa, hata katika nchi ambako mateso hayakomi. Ilisisimua kama nini kuona katika Ripoti ya Mwaka wa Utumishi wa 1984 kwamba katika nchi 28 ambako kuna marufuku za kiserikali au vizuizi vingine, jumla ya wahubiri iliongezeka kwa asilimia 3.1, ikawa zaidi ya robo milioni, na mapainia wakaongezeka kwa asilimia 23! Je! unaweza kuwazia ukipainia katika hali kama hizo? Wastani wa ndugu na dada zetu 6,905 katika nchi hizo wamekuwa wakifanya hivyo kila mwezi! Ikiwa mna uhuru, wa kadiri mahali mnapoishi, je, ungeweza kujitahidi kufikia kuwa painia wa kawaida, au angalau upainia msaidizi wa muda?—Luka 17:5, 6.
‘Kuwa Elfu’
11, 12. (a) Ni sehemu gani ya kwanza ya ahadi ambayo Yehova mwenyewe sasa anatoa? (b) Ni nini mingine ya mifano ya ‘mdogo kuwa elfu’? (c) Ni kwa nini kumekuwako ukuzi wa haraka hivyo?
11 Sasa Yehova anatoa ahadi yenye sehemu tatu juu ya jina lake mwenyewe. (Isaya 60:22) Kwanza anatuambia hivi: “Mdogo atakuwa elfu.” Unaposoma kila Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova, je, umeona jinsi mambo yalivyoanzwa na mhubiri wa Ufalme mmoja tu, au wachache, katika nchi fulani ambako sasa kuna maelfu? Kwa mfano, yule ndugu painia aliyekuwa shahidi wa kwanza katika Chile alikodi nyumba na kuwaalika watu waje kwenye mkutano wa Jumapili. Hatimaye mtu mmoja mwenye kupendezwa akaja. Mtu huyo akauliza hivi, ‘Na wengine, watakuja lini?’ Painia huyo akamhakikishia hivi: “Watakuja.” Kwa kweli walikuja. Baada ya miaka 50, mdogo huyo amekuwa 23,985.
12 Katika Italia, Mashahidi wa Yehova waliteswa vikali na utawala wa kifashisti wa Mussolini. Katika mwaka uliofuata vita wa 1946, ni 120 tu waliokuwa wakiripoti utumishi. Lakini kumbuka, ni 120 tu waliokuwako Pentekoste mwaka wa 33. Na lo, makubwa gani yakatoka huko! (Matendo 1:15; 2:1-4, 41) Sasa, kwa njia nyingine, roho ya Yehova imemiminwa katika Italia. Kwa muda wa miaka 38 wahubiri wameongezeka wakafikia kilele cha 119,408, kulingana na ripoti iliyopokewa mwisho. Hiyo ni karibu sana kuwa ongezeko la mara elfu. Kama ilivyo katika nchi nyingi za Katoliki kuizunguka dunia, Mashahidi wa Yehova katika Italia wanapata ongezeko kubwa sana.—Linganisha Zaburi 69:9; Isaya 63:14.
“Taifa Hodari”
13, 14. (a) Sehemu ya pili ya ahadi ya Yehova imetimizwaje? (b) Kwa habari hiyo, maandiko ya 1 Petro 2:9 na Isaya 59:21 yanahusuje? (c) Ni nini ambacho kimekupa kuhubiri kwetu mwendo wa haraka zaidi?
13 Sehemu ya pili ya ahadi ya Yehova yenye sehemu tatu ndiyo hii: “Mnyonge atakuwa taifa hodari.” Kweli ni “mdogo,” mabaki yaliyotawanywa ya wapakwa mafuta, aliyerudishwa kwenye “nchi” ya Yehova ya upendeleo mwaka wa 1919. Lakini alizidika, mpaka Israeli wote wa kiroho wakaingia—hesabu kamili ya warithi wa Ufalme 144,000. (Warumi 11:25, 26) Kwa kweli, mabaki wapakwa mafuta walio duniani, wakiwa sehemu ya “taifa takatifu” la Mungu, wameitwa kutoka gizani kuingia katika nuru ya ajabu. Wamefurahi sana kutangaza kote kote matukufu ya Mungu wao, Yehova. (1 Petro 2:9) Ingawa ni wachache kwa kulinganishwa, wamekuwa hodari kwa roho ya Mungu. “Katika habari zangu, hili ndilo agano langu nao, asema [Yehova]; roho yangu iliyo juu yako, na maneno yangu niliyoyatia kinywani mwako, hayataondoka kinywani mwako, wala kinywani mwa wana wako, wala kinywani mwa wajukuu wako, asema [Yehova], tangu leo na hata milele.”—Isaya 59:21.
14 Kwa usemi huo Yehova anatuhakikishia kwamba kutangaza kwetu “habari njema za mambo mema” ni lazima kufanikiwe bila shaka, na kuhusu hilo tunasali kwa bidii katika hii ‘siku ya Yehova.’ Kuhubiri kwetu kumepata mwendo wa haraka kwa kuwa “wana” wa mabaki wapakwa mafuta, “mkutano mkubwa,” na pia “wana” wao (wapya ambao wao wamewaelekeza kwenye tengenezo la Mungu) wametia vinywani mwao ujumbe huo wa uokovu, kwa kufanya hivyo wakatoa tangazo la hadharani. Kama matokeo, makundi yote yanaendelea kukua kiroho, na pia katika hesabu.—Warumi 10:10, 15, NW; Zaburi 118:24, 25; 1 Wathesalonike 3:12.
15. “Taifa” la mfano la Mungu limekuwa na watu wengi kadiri gani, na ni kwa sababu gani lina furaha?
15 Katika miaka ya karibuni, matunda ya Ufalme yameongezeka sana ajabu kama nini! Kwa kuongezwa kwa hesabu kubwa za “mkutano mkubwa,” taifa la mfano la Mungu sasa lina jumla ya Mashahidi wenye kutenda 2,842,531. Hicho ndicho kilele. “Taifa” hilo lina watu wengi zaidi ya mataifa na nchi 92 hivi za ulimwengu. Tukiwa na furaha tunayarudia maneno ya mwimbaji mzuri: “Shauri lenyewe la Yehova litasimama kwa wakati usiojulikana; mawazo ya moyo wako ni ya kizazi kimoja baada ya kizazi kingine. “Lenye furaha ni taifa ambalo Mungu walo ni Yehova, watu ambao amechagua wawe urithi wake.”—Zaburi 33:11, 12, NW.
‘Kuyahimiza’
16, 17. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba sehemu ya tatu ya ahadi ya Yehova sasa inatimizwa? (b) Upendo kwa ajili ya Mungu na Kristo umeonyeshwaje? (c) Ni utendaji gani wa furaha na ni roho gani ambavyo vimesaidia ‘kuyahimiza’? (d) Andiko la Mathayo 9:35-38 linahusuje leo?
16 Yehova anaongeza sehemu ya tatu kwenye ahadi yake: “Mimi, [Yehova], nitayahimiza hayo wakati wake.” Kwa kuwa tumesimama tukiwa karibu na “dhiki kubwa,” wakati wa jambo hilo ni SASA! (Marko 13:10, 18, 19) Kuharakishwa sana kwa kazi ya Ufalme wakati wa miaka miwili iliyopita kunathibitisha jambo hilo. ‘Kuharakishwa’ huko kunaonekana duniani pote, hata katika nchi ambazo Mashahidi wa Yehova wanalazimika kuonyesha upendo wao kwa Yehova Mungu na Yesu Kristo kwa kuhubiri yajapokuwa mateso au hali nyingine zinazohatirisha maisha zao wenyewe. Hesabu za wahubiri wa wakati wote zikiwa zinaongezeka daima, mapainia ndio wako mbele kabisa. Na tunapata furaha kama nini katika utumishi wa Yehova!—Mithali 10:22.
17 Roho hiyo ya furaha ya upainia imetia moyo makundi kila mahali ‘yaharakishe’ sehemu yao katika kukusanya kwa mwisho. Hata lijapokuwa ongezeko kubwa sana, tunaweza kusema kwamba “mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache.” Katika ulimwengu huu wa leo usio na tumaini, tunaweza kuwaonea watu huruma, kama Yesu alivyofanya alipokuwa duniani, kwa maana kweli kweli walikuwa “wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji.” Kwa hiyo ‘tunamwomba Bwana wa mavuno, apeleke watenda kazi katika mavuno yake,’ na tunafurahi kuona sala zetu zikijibiwa vizuri sana.—Mathayo 9:35-38.
18, 19. Ni ripoti gani nyingine zinazoonyesha shamba la ulimwengu kuwa ni ‘jeupe, tayari kwa mavuno’?
18 Tukichukua mmoja tu wa mifano mingi yenye kusisimua: Katika Aprili wa 1984, Ecuador iliripoti mapainia wasaidizi shambani 1,048, asilimia 10 zaidi ya Aprili uliotangulia. Kufikia Juni nchi hiyo ilikuwa ikiripoti mafunzo ya Biblia ya nyumbani 12,238, likiwa ni ongezeko la asilimia 24 kwa mwaka huo, na wahubiri 8,044, ongezeko la asilimia 17. Hudhurio la Ukumbusho lilivuvumuka likawa 40,728, watu 5 kwa kila mhubiri mmoja. Duniani pote zinatoka ripoti kama hiyo, na hudhurio la ulimwenguni pote la 7,41,974 kwenye mwadhimisho wa Ukumbusho wa Aprili 15, 1984, linaonyesha kwamba mashamba ni ‘meupe, tayari kuvuna’ wale wanaokusanywa kwa ajili ya “uzima wa milele.”—Yohana 4:35, 36.
19 Mara nyingi Yehova ‘anayahimiza’ katika njia zenye kutokeza. Mwangalizi asafiriye anaandika haya kutoka pori za Papua New Guinea ya upande wa kaskazini: “Mtu mmoja aliyefikiwa na painia wa pekee mmoja alirudi kwenye makao yake yaliyo peke yake katika kijiji cha mlimani. Miaka kadha baadaye, alionekana tena kwenye kusanyiko la mzunguko—akiwa na ombi. Mtu huyo ambaye alikuwa hajabatizwa bado alikuwa ametoa ushuhuda kwa njia yenye matokeo sana kwa kijiji chao na sehemu za pori zilizo jirani hata kwamba sasa wazee wa kijiji wakataka Mashahidi wa Yehova waje na kuangalia faida za kiroho za eneo hilo lote.” Mara mbegu ikiisha kupandwa, Mungu ndiye ‘anayekuza.’—1 Wakorintho 3:6.
20. Matawi ya Sosaiti yamepanuliwaje yashughulike na ongezeko hilo?
20 Katika njia nyingi, Yehova amekuwa akiwatayarisha watu wake kwa ajili ya ongezeko kubwa sana linalotokea sasa. Tunafurahi kwamba, katika miaka ya karibuni, Yehova ametunza kwa njia nzuri ajabu vifaa vya matawi ya Sosaiti vyenye kupanuka. Leo, matawi hayo yako tayari kusaidia makundi makubwa sana ya “njiwa.”
21. Tunaweza kuendeleaje kushiriki katika ‘kuyahimiza’?
21 Basi, acheni sote tushiriki kuangaza nuru ya habari njema za Ufalme kwa mamilioni wengi zaidi! Acheni tuwaonyeshe “njiwa” hawa wanaoelekea nyumbani njia ya “wokovu” nyuma ya kuta zenye ulinzi za tengenezo la Yehova na kuongeza “sifa” kwake na malango yalo. Na iwe sala yetu kwamba Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova na kichwa cha kundi la Kikristo, Mfalme wetu mpendwa Yesu Kristo, wataendelea ‘kuyahimiza’ huku utangazaji wa Ufalme ukisonga mbele kuelekea upeo wake!—Kutoka w3/l/85.
Kurudia Funzo Hili:
◻ Ni utimizo gani wenye kutokeza wa Isaya 60:17 uliotokea mwaka wa 1938?
◻ Kupatana na Isaya 60:18, tuna mapendezi gani?
◻ Ripoti kutoka shambani ‘zinamtukuzaje’ Yehova?
◻ Ahadi yenye sehemu tatu ya Isaya 60:22 inasongaje mbele kuelekea kwenye upeo?
[Picha katika ukurasa wa 14]
Majalada ya Mnara wa Mlinzi ya miaka ya 1930 yalionyesha njozi ya Ezekieli ya tengenezo lenye nguvu nyingi la Yehova
[Picha katika ukurasa wa 17]
Roho nzuri ya upainia imesaidia kuelekea ‘kuhimiza’ kazi ya mavuno