Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 6/1 kur. 15-23
  • Kutoa Ushuhuda Kunaleta Ongezeko la Ufalme

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutoa Ushuhuda Kunaleta Ongezeko la Ufalme
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Mashahidi Wangu”
  • Ni Nani Wanaotoa Ushuhuda?
  • Ushuhuda Mkubwa Mwaka wa 1984
  • Washika-Ukamilifu Wabarikiwa
  • Ongezeko la Ufalme!
  • Walinzi, Inueni Sauti Yenu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Uungaji-Mkono wa Duniani Pote kwa Suala la Ufalme
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Yehova ‘Ayahimiza’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Shangwe ya Yubile Kati ya Watu wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 6/1 kur. 15-23

Kutoa Ushuhuda Kunaleta Ongezeko la Ufalme

“[Yehova] . . . na awafanye kuwa wengi mara elfu kuliko mlivyo, na kuwabarikia, kama alivyowaahidi.”​—KUMBUKUMBU LA TORATI 1:11.

1, 2. (a) Yehova aliahidi Israeli nini? (b) Yeye alitimizaje ahadi zake, lakini kwa kutegemea nini?

ONGEZEKO MARA ELFU MOJA! Musa aliombea hivyo “taifa takatifu” la Yehova la Israeli. Yehova alikuwa ameahidi taifa hilo mambo makubwa. (Kutoka 19:5, 6; ona pia Mwanzo 12:2, 3.) Je! yeye alitimiza ahadi hizo?

2 Miaka 500 hivi baada ya Musa kusema maneno yaliyo juu, iliripotiwa hivi: “Yuda na Israeli walikuwa wengi kama mchanga wa pwani kwa wingi, wakila, na kunywa, na kufurahi.” Malkia wa Sheba, akiwa ametoka mbali ili aone fahari ya ufalme huo, alimwambia Sulemani hivi kwa kustaajabu: “Tazama, sikuambiwa nusu; wewe umezidi kwa hekima na kufanikiwa kuliko habari nilizozisikia. . . . Na ahimidiwe [Yehova], Mungu wako . . . kwa kuwa [Yehova] amewapenda Israeli milele.” (1 Wafalme 4:20; 10:7-9) Maadamu watu hao walitumikia kwa uaminifu wakiwa mashahidi wa Yehova, hakika yeye aliwafanikisha na kuwaongeza.

3. (a) Petro alishuhudia nini kuhusu ‘watu kwa ajili ya jina’ la Mungu? (b) Ni kwa nini jina Mashahidi wa Yehova linawafaa watu hao?

3 Miaka zaidi ya elfu moja baada ya siku za Sulemani, mtume Petro, alipokuwa akitoa ushuhuda mbele ya baraza linaloongoza la Kikristo katika Yerusalemu, ‘alieleza jinsi Mungu hapo kwanza alivyowaangalia Mataifa ili achague watu katika hao kwa ajili ya jina lake.’ (Matendo 15:14) Waisraeli walikuwa wamekuwa watu kwa ajili ya jina la Mungu. Lakini sasa, kwa mara nyingine, Mungu alikuwa akikusanya ‘watu kwa ajili ya jina lake’​—kundi la Kikristo, Israeli wa kiroho​—ambao pia wangetoa ushuhuda kwa ajili ya Yehova, wakijulisha makusudi yake ya Ufalme. (Wagalatia 6:16) Kwa kufaa, watu hao wanatambuliwa leo duniani pote kwa jina ambalo Yehova mwenyewe amelifanya maarufu katika Isaya 43:10-12, ‘Mashahidi wa Yehova.’ Ni jambo gani linalohusika katika wao kuwa watu kwa ajili ya jina la Yehova?

“Mashahidi Wangu”

4. (a) Ni kwa nini ni lazima Mashahidi wa Yehova pia wawe ‘mashahidi wa Yesu’? (b) Kulingana na Maandiko, Yesu alituachia mfano gani katika kutoa ushuhuda juu ya Yehova?

4 Yesu mwenyewe aliwapa mgawo watu hao, akisema: “Nanyi mtakuwa mashahidi wangu . . . hata mwisho wa nchi.” (Matendo 1:8) “Mashahidi wangu”​—je, maneno hayo ya Yesu yanamaanisha kwamba ni kumhusu Yesu tu, wala si Yehova, kwamba ushuhuda unapasa kutolewa? Hata kidogo! Kwenye wakati huo wa badiliko kubwa, wakati kibali ya Yehova ilikuwa ikihamishwa kutoka kwa Israeli wa kimwili mpaka kwa Israeli wa kiroho, ilikuwa lazima kutoa ushuhuda kamili kuhusu Kristo ambaye juu yake mpango mpya huo umefanywa. Hata hivyo, Yesu amebaki akiwa mtiifu kwa Babaye. Yeye alituwekea mfano katika kutoa ushuhuda kuhusu jina la Yehova na Ufalme.​—Yohana 5:30; 6:38; 17:6, 26; 18:37.

5. (a) Ni lazima tutoe ushuhuda kuhusu sehemu gani zinazomhusu Yesu? (b) Katika jambo hilo, tunafuataje hatua za Yesu?

5 Yesu Kristo ndiye Mpatanishi wa agano jipya na Wakristo wapakwa mafuta waliomo wanaitwa waurithi Ufalme. Yeye ndiye “Wakili Mkuu wa uzima” ambaye Yehova anatumia kuwakomboa wanadamu kutoka kifo. Yesu “lazima atawale akiwa mfalme” mpaka maadui wote wa Mungu na wanadamu watiishwe na paradiso tukufu irudishwe kwenye dunia hii. Yeye ndiye “Mwana wa Mungu” anayewaita wafu watoke kwenye makaburi yao katika ufufuo. (Waebrania 9:15; Matendo 3:15, NW; Zaburi 110:1, 2, 5; 1 Wakorintho 15:25-28; Luka 23:42, 43, NW; Yohana 5:25-29) Kwa hiyo, tukiwa Mashahidi wa Yehova, ni lazima tutoe ushuhuda kuhusu sehemu yenye kutokeza ya Mwana katika kulitetea jina la Yehova. Katika jambo hilo, tunafuata hatua za Bwana wetu, ambaye mwenyewe alikuwa shahidi maarufu zaidi wa Yehova​—“shahidi aliye mwaminifu.”​—Ufunuo 1:5; 3:14; Yohana 18:37; 1 Petro 2:21.

Ni Nani Wanaotoa Ushuhuda?

6. (a) Ni nani peke yao leo wanaotoa ushuhuda wa Ufalme? (b) Ni kwa nini inaweza kusemwa kwamba wao wanafanya ‘kazi kubwa zaidi’?

6 Leo, watu wenye umoja wanatoa ushuhuda ‘hata mwisho wa dunia.’ Ni watu wale wanaotajwa na mtume Petro​—‘watu kwa ajili ya jina la Mungu’​—wanaotolea Yehova ushuhuda wa Ufalme wake kupitia Kristo Yesu. Kuhusu hilo, Yesu mwenyewe aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Yeye aniaminiye mimi, kazi nizifanyazo mimi, yeye naye atazifanya; naam, na kubwa kuliko hizo atafanya, kwa kuwa mimi naenda kwa Baba.” (Yohana 14:12) Akiwa kwenye mkono wa kuume wa Babaye mbinguni, Mfalme Yesu Kristo sasa anaelekeza utoaji wa ushuhuda mkubwa zaidi uliopata kufanywa hapa duniani. Kama Yesu alivyotabiri, “habari njema hizi za ufalme” zikiisha kuhubiriwa “katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote . . . ndipo ule mwisho utakapokuja.”​—Mathayo 24:14, NW.

7. (a) Ni kwa nini madhehebu za Jumuiya ya Wakristo zinashindwa kutoa ushuhuda? (b) Tofauti na hizo, ni kwa nini Mashahidi wa Yehova ni wenye bidii sana katika utumishi wao?

7 “Habari njema hizi za ufalme” ndizo habari zenye kusisimua zaidi ambazo zimepata kutangaziwa wanadamu. Ni habari njema tukufu ambazo kuhusu hizo madhehebu za kidini za Jumuiya ya Wakristo zimekaa kimya kabisa bila kuzisema. Hawana tumaini la Ufalme kwa ajili ya wakati ujao. Si ajabu kwamba wanashindwa kutoa ushuhuda! Wameshindwa kuona tukio lenye kusisimua zaidi katika historia yote​—kufika katika utukufu wa Ufalme kwa Mwana wa mtu ili aketi juu ya kiti cha ufalme chake kitukufu na kuhukumu mataifa na watu wa dunia. Hilo ni jambo la kutolea ushuhuda! Kwa hiyo, chini ya uelekezo wa kimalaika, mashahidi wa Yehova na Kristo wake sasa wanatangaza ‘habari njema za milele kwa hao wakaao juu ya dunia, na kila taifa na kabila na lugha na jamaa.’ Je! wewe unashiriki kwa bidii katika utoaji huo wa ushuhuda?​—Ufunuo 14:6, 7; Mathayo 25:31-33.

Ushuhuda Mkubwa Mwaka wa 1984

8. (a) Ni kwa nini tunapaswa kuwa wenye furaha kuhusu Ripoti ya Mwaka wa Utumishi wa 1984? (b) Ni jambo gani linalovutia wanafunzi wapya?

8 Ripoti ya Mwaka wa Utumishi wa 1984 ya Mashahidi wa Yehova Ulimwenguni Pote, iliyoko kwenye kurasa 16-19 za gazeti hili, inaonyesha jinsi Mungu wetu, Yehova, anavyobariki kwa wingi jitihada za mashahidi wake wanyenyekevu. Kwa ujumla, nchi 203 zinawakilishwa. Kati ya hizo, nchi 172 zinaripoti ongezeko la wahubiri. Na kwa furaha, watangazaji hao wa Ufalme pia wanasema juu ya jinsi ‘Bwana amewafanya waongezeke, ndiyo, akawazidisha katika upendo, wao kwa wao, na kwa watu wote.’ (1 Wathesalonike 3:12) Umoja wa upendo kati ya watu wa Yehova, pamoja na utoaji wa ushuhuda wa Ufalme, unavuta umati wa wanafunzi wapya. Yesu anawaambia hao hivi: “Mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.”​—Yohana 8:31, 32.

9. (a) Huenda ikawa ulipendelewaje kushiriki kufanya ripoti hii? (b) Tarakimu zinaonyesha nini kuhusu Yehova na watu wake?

9 Hii ripoti ya utumishi iliyo nzuri sana imejumlishwa namna gani? Imejumlishwa kutokana na ripoti za utumishi wa shambani ambazo ninyi​—wahubiri mmoja mmoja wa Ufalme​—mmekuwa mkitoa kwa uaminifu kila mwezi. Je! wewe hufurahi kwamba umefanya sehemu ndogo yako mwenyewe katika hii ripoti kubwa nzuri? Tarakimu hizi zinaonyesha jinsi Yehova ‘amemwaga furiko la baraka’ juu ya Mashahidi wake​—hao ‘watu kwa ajili ya jina lake’​—ambao amewafanya wenye umoja katika kifungo cha duniani pote cha utumishi wa upendo.​—Malaki 3:10; Zaburi 56:10, 11; Wakolosai 3:14.

10. (a) Ni jambo gani linalokazia kwamba ni lazima mashahidi wawe wenye kujinyima? (b) Maandiko yanasema nini juu ya washika-ukamilifu na thawabu yao?

10 Sehemu kubwa ya utoaji huo wa ushuhuda imetimizwa chini ya mateso au magumu na kwa kujinyima sana. Hilo ni jambo la kutazamiwa, kwa maana neno “ushuhuda” kama linavyotumiwa hapa ni tafsiri ya neno la Kigiriki martýs au martyr, linalomaanisha mtu anayetoa ushuhuda mpaka kufa. Hilo linakazia kwamba sisi, tukiwa Mashahidi wa Yehova, twapaswa kuwa wenye kujinyima, sikuzote tukiwa tumeazimia kujitumikisha na kushika ukamilifu chini ya hali zote, hata ikiwa lazima mpaka kufa.​—Luka 9:23; linganisha Ayubu 2:3; 27:5; 31:6; Matendo 22:20; Ufunuo 2:10.

Washika-Ukamilifu Wabarikiwa

11, 12. (a) Yehova anatupa mahakikisho gani yenye kutia nguvu? (b) Watu wake wameshindaje maonezi ya mamlaka zenye kutawala kwa mabavu?

11 Katika nyakati za mateso, ‘watu wa jina’ la Yehova wamehitaji “nguvu zinazopita zile za kawaida” ili waweze kushinda mashambulio makali sana ya Shetani na majeshi yake ya kishetani. Yehova anatoa nguvu hizo na kuwaokoa na anawafanikisha mashahidi wake waaminifu. (2 Wakorintho 4:7-9; Isaya 54:17; Yeremia 1:19) Chukua kwa mfano hali katika mamlaka zilizoafikiana za Vita ya Ulimwengu ya Pili, zikiongozwa na Ujeremani, Italia, na Japani. Akitumia serikali zenye ukatili za kidikteta, Ibilisi ‘alitoa katika kinywa chake maji kama mto’ wa mateso, ili kuizamisha kazi ya kutoa ushuhuda yenye kuelekezwa na tengenezo la kimbingu la Mungu lililo kama mwanamke. Lakini je, Shetani alifaulu katika jambo hilo? Hata kidogo! Yehova aliongoza mambo hata kwamba mataifa ya kidemokrasi ya dunia yakameza mafuriko hayo. ‘Watenda mabaya walikatiliwa mbali’ na mashahidi washikamanifu wa Yehova sasa wanafanikiwa sana katika nchi hizo.​—Ufunuo 12:15, 16; Zaburi 37:28, 29.

12 Hivi karibuni, katika nchi tatu hizo, Sosaiti yetu imehitaji kujenga na kuweka vifaa katika viwanda vikubwa ili kutoa namna tofauti ya mafuriko​—mamilioni ya mamilioni ya Biblia na vichapo vya Ufalme vinavyohusiana kwa ajili ya kulisha Mashahidi wa Yehova na watu wengine njaa ya ukweli. Katika Ujeremani, Italia, na Japani, leo wahubiri wa Ufalme zaidi ya 300,000 wanapeleka ushuhuda kwenye nyumba za watu. Na katika shamba la ulimwengu wote Yehova anabariki kwa ongezeko watu wake wenye kutunza ukamilifu!—Linganisha Zaburi 115:12-15.

13. (a) Ni jambo gani katika Ripoti ya Mwaka linaloonyesha kwamba mashahidi waaminifu wameishi kwa kulingana na andiko la mwaka la 1984? (b) Jambo hilo linapasa kutusisimuaje?

13 Hata hivyo, Ibilisi, akijua kwamba wakati wake ni mfupi, anaendelea kufanya vita na wale ‘wazishikao amri za Mungu, na kutoa ushuhuda wa Yesu.’ (Ufunuo 12:12, 17) Upinzani wa Shetani ni mkali hasa katika nchi zilizoorodheshwa katika ripoti iliyoambatanishwa kuwa “Nchi Nyingine 28.” Mashahidi katika maeneo hayo wameishi kwa uaminifu kulingana na andiko la mwaka letu la 1984, ‘wakizidi sana kusubutu kusema Neno la Mungu pasipo woga.’ (Wafilipi 1:14, ZSB) Ongezeko lao la wahubiri la asilimia 3.1 ni la kusifika sana. Kwa kutiwa moto na mfano wao, sisi sote na tuendelee kwa bidii kumpa “Mungu dhabihu ya sifa daima, yaani, tunda la midomo iliungamayo jina lake.”​—Waebrania 13:15.

14. (a) Ni jambo gani ambalo huenda likatugeukia iwe “ushuhuda”? (b) Tunapaswa kuendelea kutoa ushuhuda kwa uhodari zijapokuwa hali gani, na kwa nini?

14 Hali za ulimwengu zinapokuwa mbaya zaidi, wengine wetu, bila shaka, watateswa, wapelekwe mbele mahakamani na kufungwa gerezani. Yesu alisema juu ya mambo kama hayo kuwa kati ya mambo ambayo “hayana budi kutukia” kabla ya mwisho, akaongeza hivi: “Hayo yatakuwa ushuhuda kwenu.” Katika hali zote, basi, Mashahidi wa Yehova ni lazima waendelee kutoa ushuhuda kuhusu Mungu na Kristo. Wengi wanaendelea kufanya hivyo ujapokuwa upinzani mkali wa jamaa, na masuto kumiminwa juu yao katika eneo lao la kuhubiri. Je! wewe unatoa ushuhuda kwa ujasiri zijapokuwa hali zenye kujaribu? Basi wewe ni mmoja wa wale ambao kuwahusu Yesu alisema: “Nanyi kwa subira yenu mtaziponya nafsi zenu.”​—Luka 21:7, 9-19.

Ongezeko la Ufalme!

15. Ni nini baadhi ya mambo yenye kutokeza katika chati iliyo kwenye ukurasa huu?

15 “Ongezeko la Ufalme”​—kilikuwa kichwa chenye kufaa kama nini kwa ajili ya makusanyiko ya wilaya yetu ya mwaka wa 1984! Kwa maana hakika huo umekuwa ndio mwaka wetu bora zaidi wa ongezeko. Ebu angalia tu chati iliyo kwenye ukurasa huu! Imejumlishwa kutokana na ripoti za matawi ya Sosaiti yetu 95 yanayosimamia kazi ya kutoa ushuhuda katika nchi 203.

16. Taja semi halisi za furaha kutoka duniani pote.

16 Nafasi haituruhusu tuchapishe semi zote zilizoandikwa za furaha ambazo zimepokewa kutoka hizo afisi za tawi zikiwa pamoja na ripoti zao za kila mwaka, lakini hapa kuna mionjo fulani kutoka duniani pote:

Alaska: Kijiji chote cha Metlakatla kilikuja kuona Mashahidi wa Yehova 230 wakijenga Jumba la Ufalme lenye kuvutia katika saa 32; liliwekwa wakfu siku ya Jumapili ya mwisho-juma uo huo.

Honduras: Wahubiri 3,663 ndicho kilichokuwa kilele chetu cha juu zaidi tulichopata kuwa nacho; kukiwa na hudhurio la Ukumbusho la 17,005 mengi yangali yamebaki yafanywe.

Brazili: Vilevile vilifikia upeo katika wahubiri 160,927, na watu 474,450 wakahudhuria Ukumbusho.

Thailand: Roho ya upainia iko hai, asilimia 22 ya wahubiri wote wakiwa katika utumishi huo mwezi Aprili.

Papua New Guinea: Kilele cha mapainia wasaidizi kiliongezeka kwa asilimia 91; hudhurio la Ukumbusho lilipanda kwa zaidi ya 1,000—kufikia 7,704.

Austria: Roho ya upainia inaongezeka, na tulikuwa na vilele vya mfululizo vitano katika shamba hilo; tulikuwa na vilele saba vya wahubiri, cha karibuni zaidi kikiwa 15,618.

Zambia: Tulifikia kilele kisichopata kufikiwa tena cha wahubiri 58,925: hudhurio la Ukumbusho lilikuwa 393,431—110,447 zaidi ya mwaka jana.

17. (a) Shamba la painia linapanukaje? (b) Ni miradi gani ya kufaa inayopendekezwa, na inapendekezwa kwa nani? (c) Kilele kipya cha wahubiri ni nini na huenda ikawa ni nini kilichokitokeza?

17 Ripoti zinaonyesha kwamba wamisionari na mapainia waaminifu wanaendelea kuongoza katika kuupeleka ushuhuda kwenye maeneo mapya na ya zamani. Inatia moyo kweli kweli kuona ongezeko katika mapainia. Jumla ya mapainia wasaidizi wenye kuripoti mwezi wa Aprili ilipanda haraka kufikia kilele kisichopata kufikiwa tena cha 323,644 likawa ongezeko la asilimia 49. Wengi wa hao wameona pendeleo lao la kusonga mbele na kuingia katika hesabu ya mapainia wa kawaida. Zaidi ya hayo, wengi wa wahubiri wetu vijana wa Ufalme wanaweka utumishi wa painia kuwa mradi wao na wanafanya matayarisho yenye kufaa wafikie lengo hilo wakati wa miaka yao ya mwisho ya shule ya sekondari. Matokeo ya ujumla yanaonyeshwa na ongezeko zuri ajabu la mapainia. Jambo hilo limesaidia pia kusitawisha roho ya bidii katika makundi yetu, na bila shaka, likatokeza kilele kipya cha ulimwenguni pote cha wahubiri 2,842,531, ongezeko la asilimia 7.2 zaidi ya kilele cha mwaka wa 1983. Je! wewe hufurahi kwamba umeshiriki katika hatua kubwa hiyo ya kusonga mbele?

18. (a) Ni maongezeko gani makubwa ajabu yaliyokuwako mwaka wa 1984? (b) Ripoti ya Ukumbusho inaonyesha uwezekano gani wa kuwapo kwa mpanuko na wasomaji wetu wanaweza kuitikiaje?

18 Ushuhuda wa furaha uliotolewa wakati wa mwaka wa 1984 unaonyeshwa pia na ongezeko la maangusho ya magazeti na vitabu vingine, hesabu iliyo rekodi ya saa za utumishi wa shambani zilizoripotiwa, ongezeko lenye kutokeza sana katika ziara za kurudia watu wenye kupendezwa na katika mafunzo ya Biblia ya nyumbani yaliyoongozwa kwa watu hao. Jinsi tunavyotazamia matunda zaidi katika utumishi huu wa bidii! Na kungali kuna uwezekano mkubwa wa ukusanyaji mkubwa zaidi! Jambo hilo linaonyeshwa na hudhurio la kutokeza kwenye Chakula cha Jioni cha Bwana Aprili 15 uliopita. Katika makundi ya Mashahidi wa Yehova kuzunguka dunia, jumla ya 7,416,974 walihudhuria, ambao kati yao 9,081 walionyesha kwamba walikuwa wa “kundi dogo” la Bwana kwa kushiriki kula mkate na kunywa divai. Wasomaji wetu wote na waendelee kukua kiroho, ili wapate nafasi ya kushiriki katika utoaji mkubwa wa ushuhuda na ukusanyaji ambao ungali mbele.​—Linganisha Waefeso 4:15; Wafilipi 1:9-11.

19. Tunaweza kumshukuru Yehova kwa ajili ya nini, na sala yetu kuhusu wakati ujao ni nini?

19 Kweli kweli, tunaweza kurudia maneno ya Musa katika kusema hivi juu ya Mashahidi wa Yehova, ‘watu kwa ajili ya jina lake’ wa kisasa: “[Yehova], Mungu wenu, amewafanya kuwa wengi, nanyi, angalieni, mmekuwa leo mfano wa nyota za mbinguni kwa wingi.” (Kumbukumbu la Torati 1:10) Ni sala yetu kwamba Bwana Mwenye Enzi Kuu, Yehova, ataendelea kufanikisha utoaji wa ushuhuda wa Ufalme na kuongeza ongezeko!—Kutoka w 1/1/85.

Wewe Ungesemaje?

◻ Ni kwa nini Mashahidi wa Yehova wanapaswa ‘kutoa ushuhuda juu ya Yesu’ pia?

◻ Ni ushuhuda gani mkubwa uliotolewa mwaka wa 1984?

◻ Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova anawabariki mashahidi waaminifu?

◻ Ripoti ya mwaka wa 1984 inapasa kutusisimua katika njia zipi?

[Sanduku katika ukurasa wa 23]

‘‘Wenye Furaha, Shukrani’

Kutoka nchi moja ambako kazi ya Mashahidi wa Yehova imezuiwa kwa miaka zaidi ya 40 ripoti hii inakuja: “Furaha kubwa zaidi ambayo tumekuwa tukipata ni utendaji ulioongezwa wa kuhubiri na kufundisha shambani. Wengi wamekuwa wakitumikia wakiwa mapainia wasaidizi. Mmoja wao alieleza hisi zake kwa maneno haya: ‘Nimejawa na furaha na uradhi mwingi.’ Painia msaidizi mwingine alisema: ‘Ninafurahi sana kwamba ninafanya jambo fulani linalompendeza Yehova. Niliweza kuanzisha mafunzo ya Biblia ya nyumbani mapya matano.’ Mwingine aliongeza hivi: ‘Ninamshukuru Yehova aliyenisaidia nisitawishe upendo unaohitajiwa ili kuwasaidia watu wengine.’ Katika kundi moja la wahubiri 61, 38 walitumikia wakiwa mapainia wasaidizi katika mwezi mmoja. Matokeo yakawa kwamba mafunzo ya Biblia mapya 66 yalianzishwa.”

[Chati katika ukurasa wa 16-19]

RIPOTI YA MWAKA WA UTUMISHI WA 1984 YA MASHAHIDI WA YEHOVA ULIMWENGUNI POTE

(Ona buku lililojalidiwa)

[Chati katika ukurasa wa 19]

Ulinganisho wa Ripoti ya Ulimwengu

1984 1983 Ongezeko

Matawi ya Sosaiti 95 94

Nchi Zinazoripoti 203 205

Kilele cha Wahubiri 2,842,531 2,652,323 7.2%

Wastani wa Wahubiri 2,680,274 2,501,722 7.1%

Wastani wa Mapainia 258,936 206,098 25.6%

Mapainia Wasaidizi (Aprili) 323,644 217,860 48.6%

Jumla ya Saa za Shambani 505,588,037 436,720,991 15.8%

Vitabu Vilivyoangushwa 36,639,925 36,039,400 1.7%

Maandikisho Yaliyoangushwa 1,812,221 1,756,153 3.2%

Magazeti Yaliyoangushwa 287,358,064 258,698,636 11.1%

Ziara za Kurudia 195,819,093 174,687,309 12.1%

Wast. Mafunzo ya Biblia 2,047,113 1,797,112 13.9%

Hudhurio la Ukumbusho 7,416,974 6,767,707 9.6%

Walioshiriki Mifano 9,081 9,292

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki