Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 6/1 kur. 10-21
  • Uungaji-Mkono wa Duniani Pote kwa Suala la Ufalme

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Uungaji-Mkono wa Duniani Pote kwa Suala la Ufalme
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Yehova Akaliongezea Taifa Lile Mwaka wa 1982
  • “Kupainia” Habari Njema
  • ‘Kushinda’
  • “Kweli ya Ufalme” Makusanyiko ya Wilaya Yaanzisha Kitu cha Maana!
  • Kutoa Ushuhuda Kunaleta Ongezeko la Ufalme
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • 1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Taifa Linaloshika Uaminifu wa Maadili
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Kushangilia Katika Muumba Wetu Mtukufu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 6/1 kur. 10-21

Uungaji-Mkono wa Duniani Pote kwa Suala la Ufalme

“Ee Yehova, wewe umeongezea lile taifa; wewe umejitukuza mwenyewe. Umepanua kwa mbali mipaka yote ya ile nchi.”​—ISAYA 26:15, NW.

1. (a) “Taifa” fulani la kisasa limetimizaje Isaya 26:2? (b) “Taifa” hilo linatofautianaje na mataifa ya kilimwengu?

NI TAIFA jipi ambalo Yehova analibariki hivyo kwa mpanuko? Ni “lile taifa lenye uadilifu ambalo linashika mwenendo wa uaminifu.” (Isaya 26:2, NW) Ni taifa la kiroho la Wakristo wa kweli ambalo mwenzi wa ndoa wa kimbingu wa Yehova, yaani “Yerusalemu wa juu,” alilizaa “mara” (kwa safari moja), katika mwaka wa kisasa wa 1919. “Taifa” la Yehova liko tofauti na mataifa ya dunia na viongozi wao wa kidini waliopiga Vita ya Ulimwengu ya Kwanza waking’ang’ania utawala wa ulimwengu wote, nalo linaunga mkono bila kuwaya-waya Ufalme wake wa Kimasihi uliosimamishwa katika mbingu mwaka wa 1914. (Wagalatia 4:26; Isaya 66:8; Ufunuo 11:15-18) Yehova ameliingiza hilo “taifa lenye uadilifu” katika paradiso ya kiroho ya utendaji wa Ufalme na akalitayarisha kufanya kazi ya kutolea mataifa na mbari za watu wa dunia ushuhuda wa mwisho.​—Mathayo 24:14; 25:31-33.

2. Ni sababu gani zinazolifanya “taifa” hili lifurahi sana?

2 Kwa kutimiza wimbo wa unabii wa Isaya 26:1-6, washiriki wa taifa lililozaliwa karibuni wamepita katika malango yaliyofunguliwa wazi kabisa wakiukaribia “mlima Sayuni, na mji wa Mungu aliye hai, Yerusalemu wa mbinguni.” (Waebrania 12:22) Warithi hao wa Ufalme wanayatii kwa furaha maneno haya ya wimbo huo: “Mtumainini Yehova, enyi watu, kwa nyakati zote, kwa maana Yah Yehova ndiye Mwamba wa nyakati zisizojulikana.” Yehova ‘ameongezea lile taifa,’ washiriki walo wakafikia hesabu kamili, na raia hao wa lile taifa takatifu wanamshangilia Yehova kuwa “Mwamba” wao na “Bwana Mwenye Enzi Kuu,” wakiwa na uhakika wa kwamba yuko karibu kulitimiza kusudi lake lote la ajabu.​—Isaya 26:15; 25:8, NW.

3. Ni kwa njia gani nyingine Yehova ametukuzwa?

3 Katika miaka ya majuzi Yehova ‘amepanua mipaka’ ya nchi yake ya kitheokrasi kwa umbali zaidi. Amefanya hivyo ili awatafutie nafasi wale walio “vitu vya kutamanika” kutoka mataifa yote ya kilimwengu​—“mkutano mkubwa” unaokuwa sehemu ya watu wake waliojiweka wakf. Hao ‘wanajaza nyumba yake utukufu’ wakati wao pia wanapotolea ushuhuda jina lake na Ufalme wake.​—Hagai 2:7, NW; Ufunuo 7:9, 15.

Yehova Akaliongezea Taifa Lile Mwaka wa 1982

4. (a) Ezekieli 9:1-11 inawekaje mfano mwema kwa ajili ya wale wanaohusika katika kazi ya ‘kuwatia watu alama’ leo? (b) Ni uradhi gani tunaoweza kupata kwa sababu ya kuripoti utumishi wetu kwa uaminifu?

4 Mashahidi wa Yehova wanatoa ripoti za maandishi za utumishi wao wa mwezi baada ya mwezi, wanapoendelea kuliunga mkono kwa moyo wote lile suala la Ufalme. Katika kufanya hivyo, wao wako kama yule mtu mwenye kidau cha wino cha mwandishi, ambaye amesimuliwa kwenye Ezekieli 9:1-11, anayepewa agizo atie watu alama ya wokovu kisha anamrudia Yehova kwa uaminifu ampe ripoti, akisema, “Nimefanya kama ulivyoniamuru.” Linaweza kuwa jambo la kuridhisha sana kusikia kwenye Mikutano ya Utumishi maelezo marefu ya ripoti nzuri ya ujumla ya mambo yaliyofanywa na kundi, na kujua kwamba ingawa ripoti yako huenda ikawa ilikuwa ya kiasi kidogo kama ‘kile kidonge cha mjane,’ ilisaidia kuleta matokeo hayo! Pia, wakati kila moja wetu anapochunguza jumla kuu ya utendaji katika ripoti ya ulimwenguni pote ya kila mwaka ya Mashahidi wa Yehova, linaweza kuwa jambo la kusisimua kuufikiria uhakika wa kwamba ripoti zetu wenyewe, hata ziwe zilikuwa ndogo namna gani, zingali zimesaidia kufanyiza hiyo kazi nzuri ajabu ya duniani pote!​—Marko 12:42, Authorized Version.

5. (a) Yehova amejitukuzaje mwenyewe kuhusiana na Ripoti ya Mwaka wa Utumishi wa 1982? (b) Kazi ya ‘kufanya wanafunzi’ imezaaje matunda?

5 Katika kurasa 12-15 utaikuta “RIPOTI YA MWAKA WA UTUMISHI WA 1982 WA MASHAHIDI WA YEHOVA ULIMWENGUNI POTE.” Hakika jina lenye ubora mkubwa sana la Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu linatukuzwa na utumishi huo ulio mzuri ajabu! Tunapotazama tarakimu za ujumla kwenye sehemu ya chini ya ukurasa wa 15, tunaona ongezeko lenye kutia sana moyo la asilimia 4.2 katika hesabu ya wale walioshiriki kila mwezi katika utumishi wa Ufalme kwa kuitii amri hii ya Yesu: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.” Pia, kuna kile kilele kipya cha kupendeza sana, cha Mashahidi 2,477,608 walioshiriki wakati fulani mwakani kuzihubiri habari njema “waziwazi na nyumba kwa nyumba.”​—Mathayo 28:19; Matendo 20:20, NW.

6. Ni tumaini gani la moyo wenye bidii walilo nalo Mashahidi wa Yehova kuhusiana na agizo walilopewa?

6 Walakini, Mashahidi wa Yehova hawatazamii kwamba wataugeuza ulimwengu mzima ufuate imani. Bali, agizo lao la kimungu ni “kutangaza mwaka wa nia njema upande wa Yehova na siku ya kisasi upande wa Mungu wetu.” Tunatumaini na kusali kwa moyo wenye bidii kwamba mamilioni mengine zaidi ya mabilioni ya wakaaji wa dunia walio wengi sana watauitikia ujumbe wa Ufalme kabla “dhiki kubwa” haijaondoa watu wote na mambo yenye kuleta madhara na uharibifu. Ndipo “dunia itajawa na kumjua [Yehova], kama vile maji yanavyoifunika bahari.”​—Isaya 61:2, NW; Mathayo 24:14, 21, 22; Isaya 11:9.

7. Tengenezo la Yehova limejitayarishaje kwa ajili ya mpanuko zaidi?

7 Wakiwa wenye matazamio ya mpanuko wenye kwenda kasi wa kazi ya Ufalme, Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wamekuwa na shughuli nyingi miaka kadha iliyopita wakipanua majengo yao ya kitengenezo. Makao makuu yaliyoko Brooklyn, New York, yametengeneza upya na kupanua majengo ya afisi huko 25 Columbia Heights, na kazi za viwandani za huko Brooklyn na hata kwenye Mashamba ya Sosaiti zikaanza kufanywa kwa kutumia kompyuta na kurekebishwa zilingane na hali ya sasa ya uchapaji wa kutumia mashine za ofseti. Katika sehemu zote za dunia, matawi ya Sosaiti zaidi ya 30 yamekuwa yakijenga majengo mapya yenye nafasi kubwa zaidi, na mengine ya hayo yameonyeshwa katika ukurasa huu mwingine. Tengenezo la Yehova limekaza mwendo likapate ongezeko na mpanuko mkubwa zaidi!

8. Ni mambo gani ya kupendeza umeyaona kwa kuchunguza orodha iliyo katika kurasa 12-15 kuhusiana na ongezeko la wahubiri wa Ufalme?

8 Kwa ujumla, nchi 95 kati ya zilizopangwa katika Ripoti ya Mwaka wa Utumishi zilifikia kilele kinachopita vilele vya nyakati zote zilizotangulia katika hesabu ya wahubiri wa Ufalme mwaka wa 1982, na nyingine kati ya nchi hizo ziliinuka sana. Kwa mfano, mji mkuu wa Hong Kong ulitumikiwa kwa mara ya kwanza na wahudumu (maminista) 1,000 wa Ufalme. (Isaya 60:22) Brazili ilisonga mbele, ikiwa na wahubiri 133,377 shambani. Hicho ni kilele kipya, na sasa hilo ndilo “kundi la kondoo” lililo la pili kwa wingi wa Mashahidi katika nchi zote, nchi ya United States ikiwa ndiyo imetangulia. (Mika 2:12) Wakiwa ndio kundi la kidini lililo la pili kwa ukubwa katika Italia ya Ukatoliki, Mashahidi wa Yehova walifurahia ongezeko la asilimia 8 wakawa na wahubiri wa Ufalme 98,172. (Marko 4:8, 20) Visiwa vya bahari, vikubwa kwa vidogo, tangu Australia mpaka vile vya Karibea, vilipata vilele vipya vya wahubiri. (Isaya 42:10) Kuna furaha ya kuona maendeleo mazuri katika nchi zenye matatizo ya pekee, kama Argentina, El Salvador, Pakistani na Uganda. (Zaburi 91:9, 10) Hata nchi ambako tengenezo la Yehova limekuwa na mizizi imara kwa muda mrefu zilisonga mbele​—Uingereza, Kanada, Jamhuri ya Mwungano ya Ujeremani​—na pia United States (Amerika), ambayo katika mwezi Agosti ilifikia kilele cha watangazaji wa Ufalme 613,007 katika shamba, hilo likiwa ni ongezeko la asilimia 8.8.​—Matendo 16:5.

“Kupainia” Habari Njema

9. (a) Ripoti inaonyesha ongezeko gani la mapainia? (b) Kwa sababu gani inapendekezwa wote wanaoweza kujitafutia nafasi ya upainia wafanye hivyo?

9 Kati ya watangazaji hao wa Ufalme wa ulimwenguni pote, wastani ya 172,859 waliripoti kila mwezi wakiwa wahudumu (maminista) ‘mapainia,’ wenye kutumia wakati mwingi kila siku wakieleza wengine habari njema. Kwa kulinganishwa na mwaka uliotangulia huo, idadi ya wafanya kazi hao wa wakati wote iliongezeka kwa asilimia 14! Wengine wengi, pia, wanapanga kuuingia utumishi huo wenye kujaa furaha. Je! wewe ni mmoja wao? Kusema kweli, utumishi huo ungekuwezesha ‘utoe ushuhuda kamili kabisa,’ kwa kufuata mfano wa mitume, kuhusu baraka tukufu zilizo hapa mbele tu zitakazopatwa na wote wanaomjia Yehova, wakijizoeza “imani katika Bwana wetu Yesu.”​—Matendo 2:40, NW; 8:25; 10:42; 20:21, 24 NW; 23:11; 28:23.

10. (a) Leo ni kwa njia gani kupainia kunaweza kulinganishwa na utumishi wa Wanaziri katika Israeli? (b) Ni kwa njia gani Mashahidi wa Yehova wametia bidii kweli kweli wafanye kazi katika nchi mbalimbali?

10 Ingawa mapainia hao washikamanifu hawaweki nadhiri za kuwa wahubiri wa wakati wote, wao pamoja na “mapainia-wasaidizi” wengi (ambao huenda wakatumikia wakiwa hivyo kwa mwezi mmoja au miwili tu), wako kama wale Wanaziri waliokuwa katika Israeli ya kale, kwa maana mara nyingi wanamhudumia Mungu kwa kujinyima mambo makubwa. Katika nchi fulani-fulani watumishi wa Yehova wametia bidii kweli kweli katika ‘kumpa Mungu dhabihu ya sifa daima,’ Kwa mfano, mwezi Aprili, nchi ya Venezuela iliripoti mapainia-wasaidizi 2,464, hilo likiwa ni ongezeko la asilimia 136 kupita kilele cha mwaka uliotangulia huo. Katika Trinidad asilimia 51 za jumla ya wahubiri wote walifanya utendaji wakiwa mapainia. Mwezi Juni, katika majira yenye mvua nyingi zaidi katika Japan, 25,140 walikuwa wakishiriki katika huduma ya painia, hizo zikiwa ni asilimia 36 za wahubiri wote wa Ufalme walio katika nchi hiyo. Hakika kuna furaha kubwa na uradhi mwingi sana katika kujikana mwenyewe ili kumsifu Yehova kwa kiasi kikubwa zaidi.​—Waebrania 13:15; Hesabu 6:8; Luka 9:23-25.

11. (a) Kwa sababu gani wale wasioweza kupainia hawapaswi kuvunjwa moyo? (b) Ni maandishi gani mazuri sana ya utumishi na ya mahudhurio yanayoonyesha kwamba Mashahidi wa Yehova wamekuwa watendaji sana kila mahali?

11 Walakini, waliofanya jitihada inayostahili sifa katika kuuhubiri Ufalme mwaka wa 1982 si mapainia wenye kujitoa kwa bidii peke yao, bali ni “taifa” zima la Israeli wa kiroho, pamoja na mamilioni ya wenzi wao wa “mkutano mkubwa.” Wote wameshiriki fungu lao la kuongezea kilele kipya kinachopita vilele vyote vilivyotangulia cha saa 384,856,662 zilizotumiwa katika utumishi wa shambani wakati wa mwaka huo, na wengi wameshiriki katika kuongoza mafunzo ya Biblia 1,586,293 kila juma katika nyumba za watu wanaopendezwa. Katika ile pindi ya Ukumbusho wa kifo cha Yesu, iliyoadhimishwa Aprili 8, 1982, hudhurio la ulimwenguni pote, katika makundi 44,953, lilikuwa la watu 6,252,787—umati mkubwa kama nini! Tena acheni tuwe wenye bidii katika kuendelea kuwalisha kiroho hao wote walio “kondoo wadogo”!​—Yohana 21:15-17.

12. Ni baraka gani imetamkwa kwenye Hesabu 6:24-26, na sasa inaweza kutumiwa kuhusu nani?

12 Mara tu baada ya kuitaja sheria yenye kuwahusu Wanaziri, Yehova alimwagiza Musa atangaze baraka juu ya taifa zima, akisema: “[Yehova] akubarikie, na kukulinda; [Yehova] akuangazie nuru za uso wake, na kukufadhili; [Yehova] akuinulie uso wake, na kukupa amani.” Kwa uzuri sana maneno hayo yanatumika leo kulihusu taifa takatifu la Yehova la Israeli wa kiroho​—na pia “kundi kubwa la watu waliochangamana nao” waliotoka katika mataifa yote na kuja kushiriki pamoja nao kumtumikia Yehova! Inasisimua kweli kweli kujua kwamba mashahidi wapya wa Yehova 138,540 walibatizwa katika sehemu zote za dunia wakati wa mwaka uliopita, hilo likiwa ni ongezeko la asilimia 15.6 juu ya hesabu ya waliobatizwa mwaka ule mwingine. Jina la Yehova limewekwa juu ya hao wote, na vilevile juu ya wale wote walio katika kundi, mpaka ikawa kwamba Yehova mwenyewe ‘amewabarikia.’​—Hesabu 6:24-27; Kutoka 12:38.

‘Kushinda’

13, 14. (a) Hali ikoje kuhusu ndugu zetu waliopangwa orodhani chini ya zile “Nchi Nyingine 28’’? (b) Tunaweza kupata kitia-moyo gani kutokana na mfano wao?

13 Katika nchi kadha Mashahidi wa Yehova wanalazimika kufanya vita vikali kwa ajili ya imani wakiwa chini ya hali zenye magumu makubwa sana. Kwa sababu ya adui kuwa wakali sana, na kwa kusudi la kuwalinda ndugu zetu, baadhi ya sehemu hizo hazikupangwa katika orodha ya ripoti, lakini jumla za utumishi wa nchi hizo zimeonyeshwa katika mstari uliotangulia jumla kuu, ambapo Pameandikwa; “Nchi Nyingine 28.”

14 Mashahidi wanaowakilishwa na ripoti hizo ‘wanaendelea kushinda kweli kweli kwa yeye aliyetupenda.’ (Warumi 8:37 39) Tunapofikiria utumishi wao wa uaminifu, sisi pia na tupige moyo konde tuvishinde vipingamizi vyote ili tuendelee kumtumikia Yehova kwa ‘moyo wote, nafsi yote, akili zote na nguvu zote,’ tunapoendelea kusaidia jirani yetu kwa upendo afanye vivyo hivyo. Kwa njia hiyo tunaweza kuonyesha kwamba sisi ‘hatuko mbali na ufalme wa Mungu.’​—Marko 12:29-31, 34, NW.

15-17. (a) Ni ripoti gani zenye kutia moyo tulizo nazo kutoka sehemu za dunia zenye kujawa na ugomvi? (b) Ni ripoti gani nyingine zinazofanana na hizo ambazo umesoma mwaka uliopita? (c) Mashahidi wa Yehova wanatoa sala gani kuhusiana na watawala?

15 Mke wa mwangalizi mwenye kusafiri katika Lebanoni aliandika hivi: “Tunapokuwa katika utumishi, wakati wo wote tusikiapo ufyatuaji wa risasi wenye kushambulia ndege, tunasimama chini ya miingilio ya majengo ili tupate ulinzi, kwa sababu watu watano wameuawa na vizinga vyenye marisau nyingi ndani yavyo katika eneo tulilokuwa tukilifanya kazi nyumba kwa nyumba wakati wa juma iyo hiyo. Daima tulimpelekea Yehova sala za kubariki kusanyiko lililokuwa likija na zenye kuwahusu ndugu zetu katika Beirut ya Magharibi. Kusanyiko la mzunguko lilipangwa liwe Juni 13. Tulifurahi kusikia katika radio tangazo la amri ya kuacha ufyatuaji wa risasi siku iliyoitangulia hiyo, tarehe 12, na basi kusanyiko likamalizika vizuri.” Na baadaye ripoti zilionyesha kwamba hakuna wo wote wa Mashahidi wa Yehova walioumizwa katika Magharibi ya Beirut wakati huo.

16 Katika nchi moja ya Amerika ya Kati ambako huduma yenye amani ya Mashahidi wa Yehova imefahamika vibaya sana na serikali ile mpya, wamisionari wote walifukuzwa nchini. Misionari mmoja na mkewe walikamatwa na kuzuiwa mafichoni muda wa juma mbili, mpaka Mashahidi wenyeji walio washikamanifu walipowapata na kuyafichulia Makao ya Ubalozi ya Uingereza habari za mahali walipozuiwa, halafu mipango ikafanywa ya kuwaondoa nchini. Kutoka eneo hilo iliripotiwa kwamba wenye mamlaka walikuwa wakimsaka (kumtafuta-tafuta) “mtumwa mwaminifu mwenye akili” waliyeambiwa ndiye kiongozi wa kazi ya Mashahidi wa Yehova.​—Mathayo 24:45-47.

17 Katika nchi ya Zimbabwe iliyo katika Afrika, afisa mkubwa wa serikali aliambia mkutano mkubwa wa kisiasa hivi: “Maadamu wao ni Mashahidi wa Yehova hatuna tatizo. Lakini wakiacha kuwa Mashahidi wa Yehova hapo ndipo wasiwasi utakapotuingia.” Watu wa kweli wa Mungu wanasali kwamba maafisa wote wa serikali wawe na maoni hayo yenye mwangaza, ili Mashahidi wa Yehova wote waendelee ‘kuishi maisha ya utulivu na amani, katika utauwa wote na ustahivu.’​—l Timotheo 2:1, 2.

“Kweli ya Ufalme” Makusanyiko ya Wilaya Yaanzisha Kitu cha Maana!

18. Ni kitabu gani cha kutokeza kilichotolewa kwenye “Kweli ya Ufalme” Makusanyiko ya Wilaya, na kusudi lacho ni nini?

18 Wakati wa mwezi wa Juni 1982, mfululizo wa kimataifa wa “Kweli ya Ufalme” Makusanyiko ya Wilaya ya Mashahidi wa Yehova ulianzishwa. Katika United States (Amerika) pekee kulikuwako kilele kipya cha hudhurio la watu 1,108,022.a Kwenye makusanyiko hayo ya 1982 katika United States, na vilevile katika mahali fulani-fulani pengine, kitabu kipya cha kusaidia watu wajifunze Biblia kilitolewa. Hicho ndicho kile kitabu chenye picha za kupendeza sana chenye kurasa 256, kinachoitwa Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani. Lakini hicho si kitabu cha picha tupu tu. Wala si kitabu kilichokusudiwa hasa kwa watoto. Picha za kitabu hicho zilizo nzuri sana zimekusudiwa kufundisha watu wa umri wa namna zote, ili wasaidiwe kusitawisha ile sifa yenye kuokoa uhai, yaani IMANI. Mashahidi washikamanifu wa nyakati za kale waliweza kushinda vipingamizi vilivyoelekea kuwa visivyoshindika kwa sababu IMANI yao ilikuwa na msingi thabiti katika maarifa sahihi ya kumjua Yehova, kujua Neno lake na makusudi yake. Ni kupitia IMANI kwamba “mkutano mkubwa” wa watu wenye maelekeo ya kufuata uadilifu leo wanafanikiwa kukabili utatizi wa hizi “siku za mwisho” na hiyo ndiyo itawafanya wapate wokovu kuipita ile ‘dhiki kubwa’ na kuingia katika Taratibu Mpya ya Yehova.​—Ufunuo 7:9, 14; 2 Timotheo 3:1; Waebrania 10:38, 39; 11:32-38.

19. Wewe mwenyewe ungetoa maelezo gani kuhusu kitabu hicho?

19 Kichwa kimoja cha jamaa, aliyekipokea kitabu hicho kwa furaha, alieleza hivi: “Hakika hii ni zawadi kutoka kwa Yehova, zawadi isiyo na kifani katika muda wangu wa miaka 25 wa kushirikiana na ile kweli. Mtindo uliotumiwa kukiandika unaweza kuvutia mtu ye yote. Picha zenyewe zinavuta sana moyo hivi kwamba unaweza kuhisi kila oni la moyoni lililokusudiwa kuonyeshwa nazo. Makusudi ya Ufalme wa Mungu yanaelezwa hatua-hatua kwa njia yenye kusadikisha mtu.” Tayari kitabu hicho chenye ubora mkubwa kimekwisha kuchapishwa katika lugha 21, na lugha nyingine nyingi zitafuata.

20. (a) Kwa sababu gani ni jambo la kutamanika kwamba mamilioni zaidi ya watu wajifunze kweli kupitia chombo hicho? (b) Wale wanaosikiliza maneno ya Isaya 26:2, 4 wana nafasi ya kuweza kusonga mbele wakapate utimizo gani?

20 Inatumainiwa kwamba mamilioni ya watu wanaoishi katika sehemu zote za dunia yetu watakuwa wangali wanaweza kujifunza ile kweli kupitia kurasa za kitabu kipya hicho, Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, na kwamba watasimama imara kulitetea lile suala la Ufalme wakati ambao, hivi karibuni, yale maneno ya kumalizia “wimbo” wa Isaya sura ya 26 yatatimizwa: “Njoni, watu wangu, ingia wewe ndani ya vyumba vyako, ukafunge mlango nyuma yako ujifiche kitambo kidogo, mpaka ghadhabu hii itakapopita. Kwa maana, tazama, [Yehova] anakuja kutoka mahali pake, ili kuwaadhibu wakaao duniani, kwa sababu ya uovu wao.” Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu atakapokwisha kuliondolea lawama jina lake kuu kwa njia hiyo katika Har–Magedoni, “lile taifa lenye uadilifu ambalo linashika mwenendo wa uaminifu (NW),” pamoja na “mkutano mkubwa” wa waabudu wenzi walo, litatokea bila jeraha (umizo), lipate kusonga mbele litimiziwe ahadi zote zile za ajabu ambazo “Yah Yehova” ameziandika kwa uaminifu sana katika Neno lake.​—Isaya 26:2, 4, 20, 21; Ufunuo 7:9, 14; 16:13-16.​—Kutoka The Watchtower, January 1, 1983.

[Maelezo ya Chini]

a Ulimwenguni kote, kwenye “Ushikamanifu kwa Ufalme’’ Makusanyiko ya Wilaya ya 1981, kulikuwako hudhurio la watu 4,147,256, na Mashahidi wapya 44,357 walibatizwa.

Kuzungumza juu ya utimizo wa kisasa wa “wimbo” wa kiunabii wa Isaya 26:

□ Mstari wa 2: Ni nani waliokuwa wa kwanza kuunga mkono ulimwenguni pote lile suala la Ufalme, kwa njia gani, na matokeo yalikuwa nini?

◻ Mstari wa 4: Maneno haya yanapasa kutia tumaini gani hakika katika kila mtumishi wa Yah?

◻ Mstari wa 15: Vilele vya Ripoti ya Mwaka wa Utumishi wa 1982 vinaonyesha utimizo gani?

◻ Mstari wa 20: Yehova ni kimbilio la namna gani, na kwa muda gani?

◻ Mstari wa 21: Maneno haya yanatia mkazo gani juu ya sababu inayofanya Yehova afikilize hukumu?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 20]

Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote walifurahia sana kutolewa kwa kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani chenye kurasa 256 zenye picha, wakati wa “Kweli ya Ufalme” Makusanyiko ya Wilaya. Kitabu hiki chenye kuonyesha waziwazi mafundisho ya msingi ya Biblia kinavutia watu, wazee na vijana pia, wanaotafuta mambo ya kuletea dunia yetu hali zilizo bora. Kinatazamiwa kusaidia sana katika kuharakisha kazi ya duniani pote ya Mashahidi ya kutia watu moyo wajifunze Biblia nyumbani.

[Chati katika ukurasa wa 12-15]

RIPOTI YA MWAKA WA UTUMISHI WA 1982 WA MASHAHIDI WA YEHOVA ULIMWENGUNI POTE

(Ona Mnara mliochapwa kama kitabu)

[Picha katika ukurasa wa 17]

Mengine kati ya matawi mapya ya Sosaiti yaliyokuwa yakiendelea kujengwa Ulaya mwaka wa 1982

ENEBAKK, NORWAY

HOLBÆK, DENMARK

AJALVIR (MADRID), SPANIA

SELTERS, UJEREMANI

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki